-
“Ninyi Ni Mashahidi Wangu”!Unabii wa Isaya II—Nuru kwa Wanadamu Wote
-
-
Miungu Yafanyiwa Kesi
10. Ni mwito gani wa ushindani ambao Yehova anaweka mbele ya mataifa na miungu yao?
10 Sasa Yehova anafanya ile ahadi yake ya kuwaweka huru Israeli iwe msingi wa kuifanyia miungu ya mataifa kesi katika mahakama ya ulimwengu mzima. Tunasoma hivi: “Na wakusanyike mataifa yote, kabila zote wakutanike; ni nani miongoni [mwa miungu wao] awezaye kuhubiri neno hili, na kutuonyesha mambo ya zamani? [Hao miungu wao] na walete mashahidi wao, wapate kuhesabiwa kuwa na haki; au na wasikie, wakaseme, Ni kweli.” (Isaya 43:9) Yehova anaweka mwito wa ushindani wa kuogopesha mbele ya mataifa ya ulimwengu. Ni kama anasema hivi: ‘Miungu yenu na ithibitishe kuwa ni miungu kwa kutabiri wakati ujao kwa usahihi.’ Kwa kuwa ni Mungu wa kweli tu anayeweza kutoa unabii bila kukosea, jaribu hili litafichua walaghai wote. (Isaya 48:5) Lakini Mweza Yote anaongeza takwa jingine la kisheria: Wote wanaodai kuwa miungu ya kweli lazima walete mashahidi wa kutetea matabiri yao na pia utimizo wake. Ni wazi kuwa Yehova hajiondoi katika takwa hilo la kisheria.
11. Ni agizo gani ambalo Yehova anampa mtumishi wake, na Yehova anafunua nini juu ya Uungu wake?
11 Miungu ya uwongo haiwezi kutokeza mashahidi maana haiwezi kitu. Basi aibu ndiyo hiyo, kizimba cha ushahidi kinabaki tupu. Lakini sasa ni wakati wa Yehova kuthibitisha Uungu wake. Akiwatazama watu wake, anasema hivi: “Ninyi ni mashahidi wangu, . . . na mtumishi niliyemchagua; mpate kujua, na kuniamini, na kufahamu ya kuwa mimi ndiye; kabla yangu hakuumbwa Mungu awaye yote, wala baada yangu mimi hatakuwapo mwingine. Mimi, naam, mimi, ni BWANA [“Yehova,” “NW”], zaidi yangu mimi hapana mwokozi. Nimetangaza habari, nimeokoa, nimeonyesha, na hapakuwa mungu wa kigeni kati yenu; kwa sababu hiyo ninyi ni mashahidi wangu, . . . nami ni Mungu. Naam, tangu siku ya leo, mimi ndiye; wala hapana awezaye kuokoa katika mkono wangu; mimi nitatenda kazi, naye ni nani awezaye [kuuzuia mkono wangu]?”—Isaya 43:10-13.
12, 13. (a) Watu wa Yehova wana ushuhuda gani mwingi wa kutoa? (b) Jina la Yehova limetokeaje waziwazi nyakati za kisasa?
12 Kwa kuyaitikia maneno ya Yehova, umati wa mashahidi wenye shangwe unajaa upesi kizimbani. Ushuhuda wao ni wazi na hauwezi kukanushwa. Wao, kama vile Yoshua, wanashuhudia kwamba ‘yote aliyonena Yehova yametimia. Hapana neno lo lote limepungua.’ (Yoshua 23:14) Bado watu wa Yehova wanayakumbuka maneno ya Isaya, Yeremia, Ezekieli, na manabii wengine waliotabiri, kana kwamba ni kwa sauti moja, kuhamishwa kwa Yuda kisha kukombolewa kwao kimwujiza. (Yeremia 25:11, 12) Koreshi, mkombozi wa Yuda, alitajwa jina mapema sana hata kabla hajazaliwa!—Isaya 44:26–45:1.
13 Ushuhuda chungu nzima umetolewa, basi nani atakataa kwamba Yehova ndiye Mungu wa pekee wa kweli? Ni Yehova tu asiyeumbwa, tofauti na miungu ya kipagani; ni yeye tu Mungu wa kweli.a Basi, watu wanaoitwa kwa jina la Yehova wana pendeleo la kipekee, tena la kusisimua, kusimulia maajabu yake kwa vizazi vya wakati ujao, na kwa wengine wanaoulizia habari zake. (Zaburi 78:5-7) Vivyo hivyo, Mashahidi wa Yehova wa kisasa wana pendeleo la kutangaza jina la Yehova duniani pote. Miaka ya 1920, Wanafunzi wa Biblia walizidi kufahamu umaana mkubwa wa jina la Mungu, Yehova. Kisha, Julai 26, 1931, kwenye mkusanyiko kule Columbus, Ohio, msimamizi wa Sosaiti, Joseph F. Rutherford, akatokeza azimio lenye kichwa “Jina Jipya.” Yale maneno, “Nasi twataka tujulikane na kuitwa kwa jina hili, yaani, mashahidi wa Yehova,” yalisisimua wahudhuriaji, sauti zao zikavuma “Ndiyo!” kwa kukubali azimio hilo. Tangu hapo, jina la Yehova limesifika ulimwenguni pote.—Zaburi 83:18.
14. Yehova anawakumbusha nini Waisraeli, na kwa nini kikumbusha hicho ni cha wakati unaofaa?
14 Yehova anawajali wale wanaoitwa kwa jina lake huku wakililetea heshima, na anawaona “kama mboni ya jicho” lake. Anawakumbusha Waisraeli hivyo kwa kuwaeleza jinsi alivyowakomboa kutoka Misri, akawaongoza salama kuvuka jangwa. (Kumbukumbu la Torati 32:10, 12) Wakati huo hakukuwa na mungu wa kigeni kati yao, maana walijionea miungu ya Misri ikiaibishwa kabisa. Ndiyo, miungu yote ya Misri haikuweza kulinda Misri wala kuzuia Israeli wasiondoke. (Kutoka 12:12) Vivyo hivyo, Babiloni hodari, ambayo ina mji wenye angalau mahekalu 50 ya miungu ya uwongo, haitaweza kuzuia mkono wa Mweza Yote anapowaweka huru watu wake. Ni wazi “hapana mwokozi” zaidi ya Yehova.
-
-
“Ninyi Ni Mashahidi Wangu”!Unabii wa Isaya II—Nuru kwa Wanadamu Wote
-
-
[Picha katika ukurasa wa 52]
Yehova hutolea mataifa mwito wa ushindani watokeze mashahidi wa kutetea miungu yao
1. Sanamu ya Baali ya shaba nyeusi 2. Visanamu vya udongo vya Ashtorethi 3. Utatu wa Kimisri wa Horusi, Osirisi, na Isisi 4. Miungu ya Kigiriki Athena (kushoto) na Afrodaiti
-