Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Unabii wa Maana Sana
    Mnara wa Mlinzi—2011 | Machi 1
    • Unabii wa Maana Sana

      “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.”—MATHAYO 24:14.

      WASOMI mbalimbali wa Biblia wanakubali kwamba unabii huo ni wa maana sana. Ni wa maana sana kwa sababu, kazi ambayo unabii huo unazungumzia inapaswa kufanywa duniani pote. Pia, ni wa maana kwa sababu unaonyesha kazi ambayo Wakristo wanapaswa kuwa wakifanya—kazi ya kuhubiri ambayo ingefanywa kabla ya tukio muhimu na kubwa ambalo Yesu aliliita “mwisho.”

      Unabii huo unatimizwa leo. Wewe unahusika kwa sababu habari njema inatoa mwaliko na onyo pia. Inakupa nafasi ya kuamua kati ya mambo mawili: Ukubali Ufalme wa Mungu au uukatae. Uamuzi utakaofanya utaathiri maisha yako.

      Fikiria mistari mingine inayozunguka mstari huo. Siku kadhaa kabla ya Yesu kuuawa, wanafunzi wake walimwendea na kumuuliza kuhusu wakati ujao. Walitaka kujua kuhusu kuanzishwa kwa Ufalme wa Mungu, ambao Yesu alikuwa ameuzungumzia mara nyingi. Pia, walitaka kujua kuhusu “umalizio wa mfumo wa mambo,” au “mwisho wa dunia” kama vile tafsiri nyingine zinavyosema.—Mathayo 24:3, Union Version.

      Katika jibu lake, Yesu alitabiri kwamba kungekuwa na vita vikubwa, njaa, magonjwa ya kuambukiza, na matetemeko makubwa ya ardhi. Pia, alisema kwamba uvunjaji wa sheria ungeongezeka, walimu wa dini wa uwongo wangewapotosha wengi, na Wakristo wa kweli wangechukiwa na kuteswa. Hizo zote zilikuwa habari mbaya.—Mathayo 24:4-13; Luka 21:11.

      Lakini pia kulikuwa na habari njema. Yesu alitaja maneno yaliyonukuliwa hapo juu, maneno ambayo yamewasisimua na kuwachochea watu kwa miaka mingi. Ingawa watu wanakubaliana kuhusu umuhimu wa maneno ya Yesu, wana maoni tofauti kuhusu maana ya maneno hayo. Habari njema ni nini hasa? Ufalme ni nini? Unabii huo utatimizwa na nani na wakati gani? Na “mwisho” ni nini? Acheni tuone.

  • Ufalme wa Mungu Ni Nini?
    Mnara wa Mlinzi—2011 | Machi 1
    • Ufalme wa Mungu Ni Nini?

      “Hii habari njema ya ufalme . . .”—MATHAYO 24:14.

      KATIKA Mahubiri yake ya Mlimani yanayojulikana sana, Yesu alifundisha sala ya kielelezo, ambayo inatia ndani ombi hili linalotolewa kwa Mungu: “Ufalme wako na uje.” Watu wengi wameikariri sala hiyo na wameirudia-rudia mara nyingi. Kitabu kimoja cha marejeo kinasema kuwa “hiyo ndiyo sala kuu inayotumiwa na Wakristo wote katika ibada yao ya kawaida.” Hata hivyo, wengi wanaorudia-rudia maneno ya sala hiyo hawajui Ufalme ni nini wala hawajui utafanya nini utakapokuja.—Mathayo 6:9, 10.

      Hilo si jambo linaloshangaza. Kwa kuwa viongozi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo husema mambo yenye kupingana, kuchanganya, na magumu kueleweka wanapoufafanua Ufalme. Mwandishi mmoja anasema kwamba Ufalme wa Mungu ni “kitu kisicho cha kawaida, . . . uhusiano wa ndani kati yetu na Mungu aliye hai . . . , mambo tunayojionea kumhusu Mungu ambayo katika hayo wanaume na wanawake wanapata ukombozi.” Mwingine anaelezea injili kuhusu Ufalme kuwa “miongozo kuhusu kanisa.” Na kitabu kimoja cha Kanisa Katoliki (Catechism of the Catholic Church) kinasema: “Ufalme wa Mungu [ni] uadilifu na amani na shangwe katika Roho Mtakatifu.”

      Utapata ufafanuzi ulio wazi zaidi katika ukurasa wa 2 wa gazeti hili. Ufafanuzi huo unasema: “Hivi karibuni Ufalme wa Mungu, ambao ni serikali halisi iliyo mbinguni, utakomesha uovu wote na kuigeuza dunia kuwa paradiso.” Acheni tuone jinsi Biblia inavyounga mkono maoni hayo.

      Watakaoitawala Dunia Yote Wakati Ujao

      Ufalme ni serikali inayoongozwa na mfalme. Mfalme wa Ufalme wa Mungu ni Yesu Kristo aliyefufuliwa. Kuwekwa kwake kuwa mfalme mbinguni kulifafanuliwa katika maono aliyopewa nabii Danieli, ambaye aliandika: “Nikaendelea kuona katika maono ya usiku, na, tazama! mtu fulani kama mwana wa binadamu [Yesu] alikuwa anakuja na mawingu ya mbingu; naye akaja kwa Mzee wa Siku, [Yehova Mungu] nao wakamleta karibu mbele zake Yule. Naye akapewa utawala na heshima na ufalme, ili vikundi vyote vya watu, vya mataifa na lugha vimtumikie yeye. Utawala wake ni utawala unaodumu mpaka wakati usio na kipimo ambao hautapitilia mbali, na ufalme wake ni ufalme ambao hautaharibiwa.”—Danieli 7:13, 14.

      Kitabu cha Danieli pia kinaonyesha kwamba Mungu atauimarisha kabisa Ufalme huo ambao utazikomesha falme zote za kibinadamu, nao hautapinduliwa kamwe. Sura ya 2 inafafanua kuhusu ndoto iliyoongozwa na roho ambayo mfalme wa Babiloni aliota. Katika ndoto hiyo, aliona sanamu kubwa iliyowakilisha mfuatano wa serikali kuu za ulimwengu. Nabii Danieli aliifasiri ndoto hiyo. Nabii huyo aliandika, “Katika siku za mwisho . . . Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaharibiwa kamwe. Na ufalme huo hautapewa watu wengine wowote. Utazivunja na kuzikomesha falme hizi zote, nao utasimama mpaka wakati usio na kipimo.”—Danieli 2:28, 44.

      Mfalme wa Ufalme wa Mungu hatatawala peke yake. Wakati wa huduma yake hapa duniani, Yesu aliwahakikishia mitume wake waaminifu kwamba wao, pamoja na watu wengine, wangefufuliwa na kuketi katika viti vya ufalme mbinguni. (Luka 22:28-30) Yesu hakumaanisha viti halisi vya ufalme, kwa kuwa kama alivyoonyesha, Ufalme huo ungekuwa mbinguni. Biblia inaeleza kuwa hao watawala wenzake wanatoka katika “kila kabila na lugha na watu na taifa.” Wangekuwa ‘ufalme na makuhani kwa Mungu wetu, nao wangetawala wakiwa wafalme juu ya dunia.’—Ufunuo 5:9, 10.

      Kwa Nini Habari Kuhusu Ufalme Huo Ni Njema?

      Ona kwamba Kristo Yesu amepewa utawala juu ya “vikundi vyote vya watu, vya mataifa na lugha” na wale watakaoshirikiana naye “watatawala wakiwa wafalme juu ya dunia.” Ni nani watakaokuwa raia wa Ufalme huo? Wale wanaokubali habari njema inayohubiriwa leo. Raia hao wanatia ndani wale watakaofufuliwa hapa duniani wakiwa na tumaini la kuishi milele.

      Biblia inaeleza waziwazi baraka ambazo watu watazifurahia chini ya Ufalme huo. Ona baadhi ya baraka hizo:

      “Anakomesha vita mpaka kwenye mwisho wa dunia. Upinde anauvunja na kuukata mkuki vipande-vipande; magari ya kukokotwa anayateketeza motoni.”—Zaburi 46:9.

      “Hakika wao watajenga nyumba na kukaa ndani yake; na hakika wao watapanda mashamba ya mizabibu na kula matunda yake. Hawatajenga na mtu mwingine akae ndani yake; hawatapanda na mtu mwingine ale.”—Isaya 65:21, 22.

      “[Mungu] atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”—Ufunuo 21:3, 4.

      “Wakati huo macho ya vipofu yatafunguliwa, na masikio ya viziwi yatazibuliwa. Wakati huo kilema atapanda juu kama vile paa anavyofanya, na ulimi wa bubu utapaaza sauti kwa furaha.”—Isaya 35:5, 6.

      “Saa inakuja ambayo wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti [ya Yesu] na kutoka, wale waliotenda mambo mema kwenye ufufuo wa uzima.”—Yohana 5:28, 29.

      “Wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.”—Zaburi 37:11.

      Bila shaka, hiyo ni habari njema! Zaidi ya hayo, unabii mbalimbali wa Biblia uliotimizwa unaonyesha kuwa wakati umekaribia kwa Ufalme kuanza kuitawala dunia yote kwa uadilifu.

  • Habari Njema Ni Nini?
    Mnara wa Mlinzi—2011 | Machi 1
    • Habari Njema Ni Nini?

      “Hii habari njema . . .”—MATHAYO 24:14.

      WAKRISTO wanapaswa kuhubiri “habari njema ya ufalme” kwa kuwaeleza wengine kuuhusu, wakifafanua kwamba Ufalme huo ni serikali ya wakati ujao itakayoitawala dunia kwa uadilifu. Hata hivyo, maneno “habari njema” yametumiwa kwa njia nyinginezo katika Biblia. Kwa mfano, tunasoma kuhusu “habari njema za wokovu” (Zaburi 96:2); “habari njema ya Mungu” (Waroma 15:16); na “habari njema juu ya Yesu Kristo.”—Marko 1:1.

      Kwa ufupi, habari njema inatia ndani kweli zote zilizofundishwa na Yesu na kuandikwa na wanafunzi wake. Kabla hajapanda mbinguni, Yesu aliwaambia hivi wafuasi wake: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.” (Mathayo 28:19, 20) Hivyo, kazi ya Wakristo wa kweli si kuwaeleza tu wengine kuhusu Ufalme; wanapaswa pia kujitahidi kufanya wanafunzi.

      Je, makanisa yanatii agizo hilo? Watu wengi hawafahamu Ufalme ni nini, hivyo hawawezi kuwafundisha wengine kwa usahihi kuuhusu. Badala yake, wanahubiri mambo yanayokusudiwa kuwafurahisha watu, kama vile msamaha wa dhambi na kumwamini Yesu. Pia, wanajitahidi kupata waumini kwa kujaribu kuboresha maisha ya watu au kwa kujenga hospitali, shule, na kuwajengea maskini nyumba. Ingawa shughuli hizo zinaweza kuongeza idadi ya waumini wa kanisa, hazitokezi Wakristo wa kweli wanaojitahidi kwa unyofu kuishi kulingana na mambo ambayo Yesu alifundisha.

      Mwanatheolojia mmoja aliandika hivi: “Ni wasomi au viongozi wachache miongoni mwa Wakristo wanaopinga kwamba tunapaswa kuwafanya watu kuwa wanafunzi wa Yesu na kuwafundisha kufanya mambo yote ambayo Yesu alisema. . . . Maagizo ya Yesu kuhusu jambo hilo ni wazi kabisa. Lakini hatufanyi wala hatujaribu hata kidogo kufanya yale aliyotuagiza tufanye. Na inaonekana hata hatujui jinsi ya kuyafanya.”

      Vivyo hivyo, uchunguzi uliohusisha Wakatoliki nchini Marekani ulionyesha kwamba asilimia 95 ya watu walikubali kwamba kuhubiri habari njema ni takwa la imani yao. Hata hivyo, wote walihisi kuwa njia bora ya kuhubiri habari njema si kuwaeleza wengine kuihusu, bali ni kuishi kwa njia itakayokuwa mfano kwa wengine. Mmoja wa wale waliohojiwa alisema: “Kuhubiri hakumaanishi kuzungumza tu na watu. Tunapaswa kuishi kulingana na Habari Njema.” Gazeti lililofanya uchunguzi huo (U.S. Catholic), lilisema kwamba wengi husita kuwaeleza wengine kuhusu imani yao kwa sababu ya “sifa mbaya ya kanisa inayotokana na visa vya hivi karibuni vya unyanyasaji wa kingono na mafundisho ya kanisa yenye utata.”

      Kwingineko, askofu wa Kanisa la Methodisti alisikitika kwamba kanisa lake limegawanyika na kuchanganyikiwa na linakosa ujasiri wa kutimiza utume wake, na kuwa waumini wake wengi wanaishi tu kama watu wa ulimwengu. Akionekana kuwa amekata tamaa, aliuliza: “Ni nani walio na jukumu la kuhubiri habari njema ya Ufalme?”

      Askofu huyo hakujibu swali lake. Lakini kuna jibu. Utalipata katika makala inayofuata.

      [Blabu katika ukurasa wa 6]

      Habari njema inahusu Ufalme wa Mungu na ukombozi unaopatikana kwa kumwamini Yesu Kristo

  • Ni Nani Wanaohubiri Habari Njema?
    Mnara wa Mlinzi—2011 | Machi 1
    • Ni Nani Wanaohubiri Habari Njema?

      “ . . . itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa.”—MATHAYO 24:14.

      HABARI njema inahubiriwa ulimwenguni pote na Mashahidi wa Yehova. Wanafanya hivyo katika njia tofauti-tofauti. Njia moja ni kwa . . .

      Kuzungumza na Watu. Kama Yesu na wanafunzi wake, Mashahidi wa Yehova wanawatembelea watu ili kuwahubiria habari njema. (Luka 8:1; 10:1) Mashahidi hawangoji watu wawatafute. Kuwahubiria watu kuhusu Ufalme wa Mungu ni kazi inayofanywa na Mashahidi wote, ambao ni zaidi ya milioni saba. Wanahubiri nyumba kwa nyumba, barabarani, kwa simu, na kwa njia nyingine. Mwaka uliopita, Mashahidi walitumia zaidi ya saa bilioni moja na nusu katika kazi hiyo.

      Wanawafundisha wengine kuhusu Ufalme wa Mungu na pia kuhusu ‘mambo yote ambayo Yesu aliwaamuru.’ (Mathayo 28:20) Wanaongoza mafunzo ya Biblia zaidi ya milioni nane bila malipo.

      Mashahidi wanahubiri ulimwenguni pote—katika nchi 236. Wanawahubiria watu wa aina zote. Wanahubiri vijijini na hata mijini, katika misitu ya Amazoni, misitu mikubwa ya Siberia, majangwa ya Afrika, na katika Milima ya Himalaya. Hawalipwi kwa kufanya kazi hiyo, bali wanaifanya kwa kutumia wakati na gharama zao wenyewe. Wanachochewa na upendo wao kwa Mungu na jirani. Pia, wanahubiri habari njema kupitia . . .

      Machapisho. Gazeti hili, ambalo jina lake kamili ni Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova, sasa linachapishwa katika lugha 185 likiwa na jumla ya nakala zaidi ya milioni 42 kwa kila toleo. Gazeti la Amkeni!, ambalo pia linatangaza kuhusu Ufalme, linachapishwa katika lugha 83 likiwa na jumla ya nakala milioni 40 hivi kwa kila toleo.

      Vitabu, broshua, trakti, CD/MP3, na DVD ambazo zinafafanua mafundisho ya Biblia zinapatikana katika lugha 540 hivi. Katika kipindi cha miaka kumi tu iliyopita, Mashahidi wametayarisha na kugawanya vifaa zaidi ya bilioni 20. Hiyo ni sawa na vifaa vitatu hivi kwa kila mtu anayeishi duniani!

      Mashahidi wa Yehova pia wamechapa au kuagiza uchapaji wa tafsiri mbalimbali za Biblia. Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ambayo imetafsiriwa, kuchapwa, na kusambazwa na Mashahidi, sasa inapatikana ikiwa nzima au kwa sehemu katika lugha 96. Zaidi ya nakala milioni 166 zimesambazwa. Mashahidi pia wanahubiri habari njema ya Ufalme . . .

      Kwenye Mikutano ya Kikristo. Mikutano inayofanywa kila juma katika Majumba ya Ufalme si utaratibu tu wa ibada za kidini; inakusudiwa kuelimisha watu. Hotuba hutolewa kulingana na kichwa fulani cha Biblia, na watu hujifunza Biblia wakitumia gazeti la Mnara wa Mlinzi na machapisho mengine. Katika mikutano hiyo, pia Mashahidi hujifunza jinsi ya kuwa na matokeo zaidi wakiwa watangazaji wa habari njema.

      Mashahidi hujifunza habari ileile katika makutaniko zaidi ya 107,000 ulimwenguni pote. Jambo hilo linachangia umoja wao. Watu wote wanakaribishwa kwenye mikutano hiyo. Hakuna sadaka zinazokusanywa. Bila shaka, yote hayo hayangekuwa na maana yoyote ikiwa Mashahidi wangeshindwa kuishi kulingana na yale wanayohubiri. Hivyo basi, wanajaribu kupendekeza habari njema . . .

      Kwa Mfano Wao Mzuri. Wanajitahidi kuweka mfano mzuri kuhusiana na mwenendo wao wakiwa Wakristo, wakifanya kadiri wanavyoweza kuwatendea wengine kwa njia ambayo wao wenyewe wangependa watendewe. (Mathayo 7:12) Ingawa hawajakamilika na nyakati nyingine wanakosea, bado wao wanatamani kwa unyofu kuwatendea watu wote kwa upendo, si kwa kuwahubiria habari njema tu, bali pia kwa kuwasaidia katika njia nyingine inapowezekana.

      Mashahidi wa Yehova hawajaribu kuugeuza ulimwengu kupitia kazi yao ya kuhubiri. Yehova atakaporidhika kuwa kazi hiyo imefanywa vya kutosha, ndipo mwisho utakapokuja kama Yesu alivyotabiri. Hilo litamaanisha nini kwa dunia na watu?

      [Picha katika ukurasa wa 7]

      Habari njema inahubiriwa na Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote

  • “Mwisho” Ni Nini?
    Mnara wa Mlinzi—2011 | Machi 1
    • “Mwisho” Ni Nini?

      “. . . na ndipo ule mwisho utakapokuja.”—MATHAYO 24:14.

      HIVI karibuni kumekuwa na mazungumzo mengi kuhusu mwisho wa dunia. Katika vitabu, sinema, na magazeti kuna habari zenye kuchekesha na hata za kisayansi zinazoonyesha kwa njia mbalimbali misiba itakayotokea katika siku ya maangamizi. Misiba hiyo inatia ndani uharibifu utakaotokana na vita vya nyuklia, kugongana kwa sayari ndogo, virusi hatari, mabadiliko makubwa ya hali ya hewa, au wavamizi kutoka sayari nyingine.

      Maoni ya dini pia yanatofautiana. Dini nyingi zinafundisha kwamba “mwisho” utakomesha uhai wote duniani. Akizungumzia kuhusu Mathayo 24:14, mwanatheolojia mmoja aliandika maneno haya yenye kuogopesha: “Huu ni mmoja kati ya mistari muhimu zaidi katika Neno la Mungu . . . Kizazi chetu kinakabili maangamizi ya kiwango kikubwa sana hivi kwamba ni wachache kati yetu wanaojaribu kuwazia jinsi hali itakavyokuwa.”

      Kwa kawaida, wenye maoni hayo hupuuza jambo hili muhimu: Yehova Mungu ‘aliifanya dunia ikiwa imara,’ yeye “hakuiumba tu bila sababu, [bali] aliiumba ili ikaliwe na watu.” (Isaya 45:18) Hivyo, Yesu alipozungumza kuhusu “mwisho,” hakumaanisha kwamba dunia itaharibiwa; wala hakumaanisha kuwa wanadamu wote wataangamizwa. Alimaanisha kwamba waovu—wale ambao kwa kiburi wanakataa kuishi kulingana na mwongozo wenye upendo wa Yehova—wataharibiwa.

      Fikiria mfano huu: Tuseme unamiliki nyumba nzuri na unawaruhusu watu waishi humo bila malipo. Baadhi yao wanaishi na wengine kwa amani na wanaitunza nyumba yako vizuri. Hata hivyo, wengine wanasababisha vurugu, wanapigana, na kuwaonea wale wakaaji wazuri. Wanaharibu nyumba yako na kwa kiburi wanakataa kukusikiliza unapojaribu kuwazuia wasifanye hivyo.

      Ungefanya nini ili kurekebisha mambo? Je, ungeibomoa nyumba yako? Yaelekea hungefanya hivyo. Labda ungewaondoa wale wakaaji wabaya na kurekebisha uharibifu ambao umefanywa.

      Yehova atafanya vivyo hivyo. Alimwongoza mtunga-zaburi kuandika: “Watenda-maovu watakatiliwa mbali, bali wale wanaomtumaini Yehova ndio watakaoimiliki dunia. Na bado muda kidogo tu, na mtu mwovu hatakuwako tena; nawe hakika utapaangalia mahali pake, naye hatakuwapo. Bali wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.”—Zaburi 37:9-11.

      Mtume Petro alizungumza kuhusu jambo hilohilo. Aliongozwa na roho ya Mungu kuandika hivi: “Mbingu zilikuwapo tangu zamani za kale na dunia ikisimama imara kutoka katika maji na katikati ya maji kwa neno la Mungu; na kwa njia hizo ulimwengu wa wakati huo uliangamia kwa gharika ya maji.” (2 Petro 3:5, 6) Hapa mtume alikuwa akirejelea Gharika ya siku za Noa. Ulimwengu wa watu wasiomwogopa Mungu uliharibiwa, lakini dunia yenyewe haikuharibiwa. Gharika hiyo iliyoikumba dunia nzima ‘iliweka kielelezo kwa watu wasiomwogopa Mungu juu ya mambo yatakayokuja.’—2 Petro 2:6.

      Kisha Petro akaongeza: “Mbingu na dunia za sasa zimewekwa akiba kwa ajili ya moto.” Ikiwa tungesoma sehemu hiyo tu, huenda tungekosa maana ya mstari mzima. Hata hivyo, ona kwamba mstari huo unaendelea kusema: “Na ya kuangamizwa kwa watu wasiomwogopa Mungu.” Huo si uharibifu wa dunia, bali wa watu wasiomwogopa Mungu. Ni nini kinachofuata? Petro aliandika: “Kulingana na ahadi yake tunangojea mbingu mpya [Ufalme wa Kimasihi wa Mungu] na dunia mpya [jamii ya wanadamu waadilifu], na humo uadilifu utakaa.”—2 Petro 3:7, 13.

      Unabii wa Biblia pia unaonyesha kwamba “mwisho” utafika hivi karibuni. Soma Mathayo 24:3-14 na 2 Timotheo 3:1-5 ili uone mambo yanayothibitisha kwamba maneno hayo ni ya kweli.a

      Je, inashangaza kuwa watu wengi wamechanganyikiwa kuhusu Mathayo 24:14, andiko ambalo hata mtoto mdogo anaweza kulielewa? Kuna sababu za kuchanganyikiwa. Shetani amepofusha watu wasielewe kweli zenye thamani zinazopatikana katika Neno la Mungu. (2 Wakorintho 4:4) Pia, Mungu ameficha makusudi yake yasijulikane na watu wenye kiburi lakini ameyafunua kwa watu wanyenyekevu. Kuhusiana na hilo, Yesu alisema: “Ninakusifu wewe hadharani, Baba, Bwana wa mbingu na dunia, kwa sababu umewaficha mambo haya wenye hekima na wenye akili na umeyafunua kwa watoto.” (Mathayo 11:25) Ni pendeleo kubwa kama nini kuwa miongoni mwa watu wanyenyekevu wanaoelewa vizuri Ufalme wa Mungu ni nini, na wanaoweza kuwa na tazamio la kupata baraka ambazo wale wanaounga mkono Ufalme huo watapata!

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki