Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Babu na Nyanya Walio “Tofauti”
    Amkeni!—1999 | Machi 22
    • Babu na Nyanya Walio “Tofauti”

      “Karibu nyumbani kwa Babu na Nyanya—Watoto Waendekezwa Unapongoja.” Ndivyo isemavyo ishara kwenye mwingilio wa makao ya Gene na Jane.

      HATA hivyo, unapoingia ndani, hutawapata wenzi wazee-wazee wakiketi kwenye viti vya kubembea. Badala yake, utaona wenzi wa ndoa wenye nguvu wakiwa na umri wa miaka 40 hivi. Pasipo kuepuka madaraka yao wakiwa ‘viongozi wazee,’ Gene na Jane wamekubali kwa furaha kuwa nyanya na babu. “Kweli, hali ya kuwa babu na nyanya ni mojawapo ya ishara ndogo maishani inayoonyesha kwamba unazidi kuzeeka,” asema Gene, “lakini hii ni mojawapo ya thawabu, za kulea watoto wako—wajukuu.”

      Mithali moja ya kale yasema: “Wana wa wana ndio taji ya wazee.” (Mithali 17:6) Mara nyingi babu na nyanya na wajukuu hufurahia kifungo cha kipekee cha upendo na uhusiano wa karibu. Na kulingana na jarida Generations, “watu wengi sana katika jamii ya Kimarekani ni babu na nyanya.” Sababu ni nini? “Watu wanaishi maisha marefu zaidi na kutokea kwa mitindo mipya katika maisha ya watu,” yaeleza makala hiyo. “Mabadiliko katika hali ya kufa na uwezo wa kuzaa yanamaanisha kwamba idadi inayokaribia robo tatu ya watu wazima wataishi kufikia kuwa babu na nyanya . . . Watu wengi wa umri wa makamu huwa babu na nyanya wanapokuwa na umri wa miaka 45 hivi.”

      Kizazi cha babu na nyanya walio tofauti kimeibuka katika nchi fulani. Ingawa hivyo, wengi wanazidi kujipata wakihusika katika kuwatunza wajukuu wao. Kwa kielelezo, mwana wa Gene na Jane na mkwe wao wa zamani wametalikiana na wanashirikiana katika kumlea mtoto. “Tunajaribu kusaidia kutunza mjukuu wetu wa kiume huku mwana wetu akifanya kazi,” aeleza Jane. Kulingana na uchunguzi mmoja, babu na nyanya huko Marekani wanaowatunza wajukuu wao hutumia kwa wastani muda wa saa 14 kwa juma katika kazi hiyo. Muda huu unakuwa sawa na kufanya kazi yenye malipo ya dola bilioni 29 kwa mwaka!

      Babu na nyanya wa siku hizi hupata shangwe zipi? Wanakabili magumu gani? Makala zinazofuata zinachunguza maswali haya.

  • Babu na Nyanya—Shangwe na Magumu Yao
    Amkeni!—1999 | Machi 22
    • Babu na Nyanya—Shangwe na Magumu Yao

      “Ninapenda kuwa babu au nyanya! Unafurahia wajukuu wako bila kuhisi ukiwa na daraka kuwaelekea. Unatambua kwamba unaathiri maisha yao lakini hatimaye huchangii uamuzi wa mwisho. Wazazi wao watafanya hivyo.”—Gene, ambaye ni babu.

      NI KITU gani kinachoweza kuchochea shauku hiyo unapokuwa babu au nyanya? Watafiti wanasema kwamba mambo ambayo kwa kawaida wazazi hudai kiasili kutoka kwa watoto wao yaweza kutokeza mkazo mkubwa sana. Kwa sababu kwa kawaida si lazima babu na nyanya wadai mambo hayo, wanaweza kufurahia uhusiano usio na mkazo pamoja na wajukuu wao. Kama asemavyo, Arthur Kornhaber, M.D., wako huru kuwapenda wajukuu wao “kwa sababu tu ni wajukuu wao.” Nyanya mmoja anayeitwa Esther asema hivi: “Nilipokuwa na watoto wangu, nilijihusisha sana na kila kitu walichofanya. Nikiwa nyanya, nahisi nikiwa huru kufurahia na kuwapenda wajukuu wangu tu.”

      Kisha mtu anapokuwa na umri mkubwa anapata hekima na ufahamu zaidi. (Ayubu 12:12) Babu na nyanya wamepata uzoefu wa miaka mingi katika kulea watoto, kwa kuwa wao si wachanga tena. Wakiwa wamejifunza kutokana na makosa yao, wanaweza kuwa na ufahamu zaidi wa kushughulikia watoto kuliko waliokuwa nao walipokuwa na umri mdogo zaidi.

      Hivyo Dakt. Kornhaber amalizia kwa kusema: “Kifungo kinachofaa na chenye upendo kati ya babu na nyanya na wajukuu ni cha lazima ili vizazi vyote vitatu vipate afya ya kihisia-moyo na furaha. Kifungo hiki ni haki ya kuzaliwa ya kiasili kwa watoto, . . . urithi walioachiwa na wazee wao ambao hunufaisha kila mmoja katika familia.” Vivyo hivyo jarida Family Relations lasema: “Babu na nyanya wanaoshiriki na kuelewa daraka lao husitawisha hali njema na imani zaidi.”

      Daraka la Babu na Nyanya

      Babu na nyanya wanaweza kutimiza madaraka mengi yenye thamani. “Wanaweza kuwategemeza watoto wao waliofunga ndoa,” asema Gene. “Nafikiri kwa kufanya hivyo, wanaweza kukomesha baadhi ya hali ngumu ambazo huwapata wazazi wachanga.” Babu na nyanya pia wanaweza kufanya mengi zaidi kuwategemeza wajukuu wao wenyewe. Mara nyingi babu na nyanya ndio husimulia matukio fulani ambayo humfahamisha mtoto historia ya familia. Mara nyingi, pia babu na nyanya hutimiza daraka la maana katika kupitisha urithi wa kidini wa familia.

      Katika familia nyingi, babu na nyanya hutumikia wakiwa washauri wanaoaminiwa. “Huenda kukawa na mambo ambayo watoto watakuambia ambayo hawajihisi huru kuyazungumzia pamoja na wazazi wao,” asema Jane, aliyetajwa katika makala ya kwanza. Kwa kawaida wazazi hufurahia msaada huo wa ziada. Kulingana na uchunguzi mmoja, “zaidi ya asilimia 80 ya vijana waliwaona babu na nyanya yao kuwa marafiki wao wa karibu. . . . Idadi kubwa ya wajukuu waliokomaa hudumisha mawasiliano kwa ukawaida pamoja na babu na nyanya yao wa karibu.”

      Babu au nyanya mwenye upendo aweza kuwa mtu wa maana sana hasa kwa mtoto ambaye amekosa malezi yanayofaa nyumbani. “Nyanya yangu ndiye aliyekuwa mtu wa maana zaidi maishani mwangu nilipokuwa mchanga,” aandika Selma Wassermann. “Nyanya yangu ndiye aliyenilea. Nyanya yangu alikuwa mwenye kufikika na tayari daima kunibeba kwenye paja lake ili kunifariji na kunipa uhakikishio zaidi. . . . Nilijifunza mambo ya maana zaidi kunihusu kutoka kwa nyanya yangu—kwamba nilipendwa na kwa hiyo napendeka.”—The Long Distance Grandmother.

      Mikazo ya Familia

      Ingawa hivyo, hali ya kuwa babu au nyanya haikosi kuwa na mikazo na matatizo. Kwa kielelezo, mzazi mmoja, akumbuka akibishana vikali na mama yake kuhusu njia inayofaa ya kumfanya mtoto apige mbweu. “Jambo hilo lilisababisha kuvunjika kwa uhusiano wetu kwenye pindi ambayo ningeweza kudhurika kwa urahisi.” Kwa kueleweka, wazazi wachanga wanataka wazazi wao wakubali njia wanayolea watoto wao. Hivyo madokezo kutoka kwa wazazi wao wenye nia njema yaweza kusikika kuwa uchambuzi unaoharibu mambo.

      Katika kitabu chake Between Parents and Grandparents, Dakt. Kornhaber asema juu ya wazazi wawili wenye tatizo jingine la kawaida. Mzazi mmoja asema hivi: “Mimi huingiliwa kila siku na wazazi wangu, nao hukasirika wanapokuja nyumbani na kunikosa. . . . Hawanifikirii—hisia zangu na haki yangu ya kuwa na faragha.” Mwingine alalamika akisema: “Wazazi wangu wanataka kumtawala msichana wangu mdogo. Wanataka kujihusisha katika kila jambo linalohusu maisha ya Susie. . . . Tunafikiria kuhama.”

      Nyakati nyingine babu na nyanya pia hulaumiwa kwa kuwaendekeza wajukuu wao kwa kuwapa zawadi nyingi sana. Bila shaka, ukarimu ni jambo la kiasili kwa babu na nyanya kama ilivyo kupumua, lakini wengine huvuka mipaka katika jambo hili. Hata hivyo, nyakati fulani, malalamiko ya wazazi yaweza kutokana na wivu. (Mithali 14:30) “Wazazi wangu walikuwa wakali sana kunielekea,” akiri Mildred. “Inapohusu watoto wangu wao huwaonyesha ukarimu na [kuwaendekeza]. Nina wivu kwa sababu hawajabadili hata kidogo namna wanavyonitendea.” Hata nia au sababu iwe nini, inaweza kusababisha matatizo ikiwa babu au nyanya haheshimu mapendezi ya wazazi kuhusu kuwapa wajukuu zawadi.

      Hivyo babu na nyanya watakuwa wenye hekima kutumia busara wanapoonyesha ukarimu. Biblia inaonyesha kwamba hata kitu kizuri kinapokuwa kingi sana chaweza kuwa kibaya. (Mithali 25:27) Ikiwa huna hakika ni zawadi za aina gani zinazofaa, shauriana na wazazi. Kwa njia hii ‘utajua jinsi ya kuwapa zawadi zilizo njema.’—Luka 11:13.

      Upendo na Staha—Ndizo Funguo!

      Kwa kusikitisha, babu na nyanya fulani hulalamika kwamba kazi yao ya kutunza na kulea watoto haithaminiwi. Wengine huhisi kwamba hawapewi muda wa kutosha kuwa na wajukuu wao. Lakini babu na nyanya fulani husema kwamba watoto wao wakubwa wamewaepuka kabisa bila hata kuwaeleza sababu. Mara nyingi matatizo hayo yanayoleta uchungu yanaweza kuepukwa ikiwa washiriki wa familia wataonyeshana upendo na staha. Biblia husema: “Upendo ni wenye ustahimilivu na wenye fadhili. Upendo hauna wivu, . . . hautafuti masilahi yao wenyewe, haupati kuwa wenye kuchokozeka. . . . Huhimili mambo yote, huamini mambo yote, hutumaini mambo yote, huvumilia mambo yote.”—1 Wakorintho 13:4, 5, 7.

      Labda wewe ni mzazi mchanga na Nyanya atoa dokezo au maoni yenye kuudhi, ijapokuwa ana nia njema. Je, kweli una sababu nzuri ya “kuwa mwenye kuchokozeka”? Kwa vyovyote, Biblia huonyesha kwamba daraka la mwanamke Mkristo mwenye umri mkubwa ni kufundisha “wanawake vijana . . . kuwapenda waume zao, kuwapenda watoto wao, kuwa timamu katika akili, safi kiadili, wafanyakazi nyumbani.” (Tito 2:3-5) Na je, si ni kusudi lako, la babu na la nyanya kutimiza lengo lile lile—la kuwapa watoto wenu vitu vilivyo bora zaidi? Kwa kuwa upendo “hautafuti masilahi yao wenyewe,” labda itakuwa bora kufikiria mahitaji ya mtoto—si kufikiria hisia zako tu. Kufanya hivyo kwaweza kuwasaidia mwepuke “kuchochea shindano juu ya mtu na mwenzake” kuhusu mambo madogo yenye kuudhi.—Wagalatia 5:26, kielezi-chini New World Translation of the Holy Scriptures—With References.

      Ni kweli, unaweza kuhofia ukarimu mwingi sana utamharibu mtoto wako. Lakini kwa kawaida babu au nyanya hawi na nia mbaya anapokuwa akionyesha ukarimu. Wataalamu wengi wa utunzaji-watoto wanakubali kwamba jinsi unavyomzoeza na kumtia nidhamu mtoto wako kutakuwa na matokeo makubwa zaidi kuliko kuingiliwa kati pindi kwa pindi na babu au nyanya. Daktari mmoja ashauri kwamba: “Inasaidia kuwa na ucheshi.”

      Ukiwa na hangaiko halali kuhusu suala fulani la utunzaji wa mtoto, usiwazuie kabisa wazazi au wakwe zako kuwasiliana na watoto wako. Biblia husema: “Pasipo mashauri makusudi hubatilika.” (Mithali 15:22) Katika ‘wakati unaofaa,’ uwe na mazungumzo mazito na ufunue mahangaiko yako. (Mithali 15:23) Mara nyingi, masuluhisho yanaweza kupatikana.

      Je, wewe ni babu au nyanya? Basi ni muhimu kuwastahi wazazi wa mjukuu wako. Bila shaka, ungehisi kuwa na daraka la kusema ikiwa ungeona kwamba mjukuu wako yuko hatarini. Lakini ijapokuwa ni jambo la kiasili kwako kumpenda na kumtunza mjukuu wako, wazazi—wala si babu na nyanya—ndio wenye daraka la kulea watoto wao. (Waefeso 6:4) Biblia huwaamuru wajukuu wenu wawastahi na kuwatii wazazi wao. (Waefeso 6:1, 2; Waebrania 12:9) Hivyo, jiepushe kuwapatia wazazi wao mashauri mengi kupita kiasi na ambayo hawajaomba au kuhujumu mamlaka ya wazazi.—Linganisha 1 Wathesalonike 4:11.

      Kweli, kutojihusisha, kunyamaza—na pengine kungojea ukiwa na wasiwasi jambo fulani litokee—na kuacha watoto wako wafanye kazi yao wakiwa wazazi haliwi jambo rahisi sikuzote. Lakini kama asemavyo Gene, “isipokuwa waombe shauri, utahitaji kukubaliana na kile ambacho wazazi wanahisi kuwa bora kwa watoto wao.” Jane asema: “Ninakuwa mwangalifu kutosema, ‘Hivi ndivyo inavyopasa kufanywa!’ Kuna njia nyingi tofauti-tofauti za kufanya mambo, na ikiwa unashikilia sana maoni yako, inaweza kusababisha matatizo.”

      Kile Ambacho Babu na Nyanya Wanaweza Kutoa

      Biblia inaonyesha kwamba kuwa na wajukuu ni baraka kutoka kwa Mungu. (Zaburi 128:3-6) Kwa kupendezwa na wajukuu wako, unaweza kuathiri sana maisha yao, ukiwasaidia wasitawishe kanuni za kimungu. (Linganisha Kumbukumbu la Torati 32:7.) Katika nyakati za Biblia mwanamke mmoja aliyeitwa Loisi alitimiza fungu la maana katika kusaidia mjukuu wake wa kiume, Timotheo, akue na kuwa mtu wa Mungu mwenye kutokeza. (2 Timotheo 1:5) Vivyo hivyo, unaweza kupata shangwe wajukuu wako wanapokubali kuzoezwa kimungu.

      Pia unaweza kuwa chanzo cha upendo na shauku inayohitajiwa sana. Kweli, huenda usiwe mtu mwenye kuzungumza sana kwa shauku. Hata hivyo, upendo wa kimungu waweza kuonyeshwa pia kwa kupendezwa kwa moyo mweupe na bila ubinafsi na wajukuu wako. Mwandishi Selma Wassermann asema hivi: “Kupendezwa na mambo ambayo mtoto anakuambia . . . kwa hakika kutaonyesha kwamba unajali. Kuwa msikilizaji mzuri, bila kuingilia kati, kutokuwa mchambuzi—yote haya huonyesha staha, shauku, uthamini mkubwa.” Kwa mjukuu, uangalifu huo wenye upendo waweza kuwa mojawapo ya zawadi bora kabisa ambazo babu na nyanya waweza kutoa.

      Kufikia hapa mazungumzo yetu yamekazia madaraka ya kidesturi ya kuwa babu au nyanya. Hata hivyo, babu na nyanya wengi wa kisasa, hubeba mzigo mzito zaidi.

      [Blabu katika ukurasa wa 6]

      “Nilijifunza mambo ya maana zaidi kunihusu kutoka kwa nyanya yangu—kwamba nilipendwa na kwa hiyo napendeka”

      [Sanduku katika ukurasa wa 6]

      Madokezo kwa Babu na Nyanya Wanaoishi Mbali

      • Waombe wazazi wakupelekee kanda za vidio au picha za wajukuu.

      • Wapelekee wajukuu wako “barua” zilizorekodiwa katika kaseti. Kwa watoto wadogo, jirekodi mwenyewe ukisoma hadithi za Biblia au ukiimba nyimbo za kubembeleza mtoto.

      • Wapelekee wajukuu postikadi na barua. Ikiwezekana, uwe unawaandikia barua kwa ukawaida.

      • Ikiwa unaweza kulipia gharama, wasiliana na wajukuu wako walio mbali kwa kuwapigia simu. Unapoongea na watoto wadogo, anzisha mazungumzo kwa kuuliza maswali sahili, kama vile, “Ulikula nini asubuhi?”

      • Ikiwezekana, fanya ziara za kawaida, na fupi.

      • Fanya mipango na wazazi wa wajukuu wako wakutembelee. Panga shughuli za kujifurahisha, kama vile kwenda kuwatazama wanyama, kwenye majumba ya ukumbusho, na kwenye bustani.

  • Babu na Nyanya Wanapokuwa Wazazi
    Amkeni!—1999 | Machi 22
    • Babu na Nyanya Wanapokuwa Wazazi

      “Nilikuwa nimefika tu nyumbani kutoka mkutanoni kwenye Jumba la Ufalme. Mlango ulibishwa kwa nguvu, na huko nje walisimama polisi wawili pamoja na watoto wawili wachafu ambao nywele zao zilikuwa zimesokotwa na ambao walionekana kana kwamba hawakuwa wameoshwa kwa miezi kadhaa. Hungeweza kutambua kamwe kwamba walikuwa watoto! Walikuwa wajukuu wangu, na mama yao—mraibu wa dawa za kulevya—alikuwa amewatupa. Nilikuwa mjane, na tayari nilikuwa na watoto sita. Lakini singeweza kukataa kuwachukua.”—Sally.a

      “Binti yangu aliniuliza ikiwa ningewachukua watoto wake hadi arekebishe maisha yake. Sikujua kwamba alikuwa mraibu wa dawa za kulevya. Niliishia kuwalea watoto wake wawili. Miaka kadhaa baadaye, binti yangu alipata mtoto mwingine. Sikutaka kumchukua, lakini mjukuu wangu wa kiume alinisihi, akisema, ‘Nyanya, je, hatuwezi kukubali mmoja zaidi?’”—Willie Mae.

      HALI ya kuwa babu na nyanya ilikuwa ikifafanuliwa kuwa “raha bila madaraka.” Lakini haifafanuliwi hivyo tena kamwe. Wengine wanakadiria kwamba katika Marekani peke yake, watoto zaidi ya milioni tatu huishi na babu na nyanya yao. Na idadi hiyo inazidi kuongezeka.

      Ni nini kinachochangia mwelekeo huu wenye kuhuzunisha? Watoto ambao wazazi wao wanatalikiana waweza kuishia kuishi pamoja na babu na nyanya yao. Vivyo hivyo, jambo hili laweza kuwapata watoto ambao wametupwa au waliotendwa vibaya na wazazi wao. Jarida Child Welfare lasema kwamba kwa sababu uraibu huwafanya wazazi washindwe kutekeleza wajibu wao, ‘kokeini yenye nguvu inatokeza kizazi kilichopotoka.’ Pia kuna mamilioni ya watoto “wasio na wazazi” kwa sababu ya kutupwa, kifo cha wazazi, na maradhi ya akili. Watoto ambao mama zao wanauawa na UKIMWI waweza pia kuishia kutunzwa na babu na nyanya yao.

      Kutwaa madaraka ya kulea watoto wakati wa “siku zilizo mbaya” za uzeeni kwaweza kulemea. (Mhubiri 12:1-7) Kwa wazi watu wengi hawana nguvu za kukazia uangalifu wa kutosha watoto wadogo. Babu na nyanya wengine pia wanawatunza wazazi wao wanaozeeka. Na bado wengine ni wajane au wametalikiana na wanalazimika kuishi bila utegemezo wa mwenzi. Na wengine wanapata kwamba hawako tayari kifedha kutwaa mzigo huo. Katika uchunguzi mmoja, babu na nyanya watunzaji 4 kati ya 10 walikuwa na mapato yanayokaribia kufikia kiwango cha ufukara. “Watoto walikuwa wagonjwa,” akumbuka Sally. “Nililazimika kulipa pesa nyingi sana kwa dawa. Sikupata msaada wowote kutoka kwa serikali.” Mwanamke mmoja mzee-mzee akumbuka hivi: “Nililazimika kutumia malipo yangu ya uzeeni kuwatunza wajukuu wangu.”

      Mikazo na Shida

      Haishangazi kwamba, uchunguzi mmoja ulifunua kwamba “kutunza wajukuu kulisababisha mkazo mkubwa kwa babu na nyanya, huku asilimia 86 ya babu na nyanya 60 waliofanyiwa uchunguzi wakiripoti kuwa ‘wameshuka moyo au kuhangaika wakati mwingi.’” Kwa kweli, wengi huripoti kuwa na matatizo ya afya. “Kuliniathiri kimwili, kiakili, na kiroho,” asema Elizabeth, mwanamke aliyemtunza mjukuu wake wa kike. Willie Mae, anayesumbuliwa na matatizo ya moyo na msukumo mkubwa wa damu, asema: “Daktari wangu anaamini kwamba unahusiana na mkazo wa kulea watoto.”

      Wengi hawako tayari kubadilika ili kufaana na mtindo-maisha wa kulea watoto. “Kunakuwa na pindi ambapo siwezi kwenda mahali,” asema babu mmoja. “Ningehisi kuwa na hatia . . . kuwaacha na mtu mwingine, hivyo badala ya kwenda mahali fulani au kufanya jambo fulani, siendi au silifanyi.” Mwingine alifafanua wakati wa kufanya mambo yake ya kibinafsi kuwa “haupo.” Kujitenga na wengine na upweke ni mambo ya kawaida. Nyanya mmoja alisema: “Katika rika letu wengi wa marafiki zetu hawana watoto [wachanga] na kama tokeo mara nyingi hatukubali mialiko ya kwenda kwa sababu watoto wetu [wajukuu] hawajaalikwa.”

      Mikazo ya kihisia-moyo husababisha maumivu pia. Yasema makala moja katika U.S.News & World Report: “Wengi wao [babu na nyanya] wanasumbuliwa na aibu na hatia ya kwamba watoto wao wameshindwa kufanikiwa wakiwa wazazi—na wengi hujilaumu, wakishangaa ni wapi walipokosea wakiwa wazazi. Ili waweze kuandaa makao salama na yenye upendo kwa wajukuu wao, babu na nyanya fulani wanalazimika kuwaondoa akilini watoto wao wenye kutenda vibaya au waraibu wa dawa za kulevya.”

      Uchunguzi mmoja waripoti kwamba: “Zaidi ya sehemu moja kwa nne . . . walisema kwamba uradhi wao katika uhusiano wa ndoa ulipungua likiwa tokeo la kuandaa utunzaji.” Mara nyingi waume hasa, huhisi kuwa wametupwa huku wake zao wakibeba fungu kubwa katika kuwatunza watoto. Waume fulani huhisi kwamba hawawezi kung’ang’ana na mkazo huo. Mwanamke mmoja asema hivi kuhusu mume wake: “Alitutupa. . . . Nafikiri alihisi tu akiwa katika hali ambayo hangeweza kujiepusha nayo.”

      Watoto Wenye Hasira

      Lasema U.S.News & World Report: “Mikazo hiyo inaongezwa na uhakika wa kwamba baadhi ya watoto ambao [babu na nyanya] hurithi ni miongoni mwa watoto wanaohitaji sana utegemezo wenye upendo, waliovurugika zaidi kihisia-moyo na wenye hasira zaidi katika nchi.”

      Mfikirie mjukuu wa kike wa Elizabeth. Baba ya mtoto huyo alimtupa kihalisi kwenye pembe moja ya barabarani ambapo Elizabeth alikuwa akifanya kazi ya kusaidia kuvusha watoto. “Yeye ni mtoto mwenye hasira,” asema Elizabeth. “Ameumizwa.” Wajukuu wa Sally wamepatwa na madhara kama hayo. “Mjukuu wangu wa kiume amefungia kinyongo. Anahisi kwamba hakuna mtu yeyote anayemtaka.” Kuwa na baba na mama mwenye upendo ni haki ya kuzaliwa ya mtoto. Ebu wazia jinsi mtoto anavyohisi anapotupwa, anapoachiliwa, au anapokataliwa nao! Kuelewa hisia hizi kwaweza kuwa ufunguo wa kushughulika kwa njia ya saburi na watoto wanaositawisha matatizo ya kitabia. Mithali 19:11 yasema: “Busara ya mtu huiahirisha hasira yake.”

      Kwa kielelezo, mtoto aliyetupwa aweza kukinza jitihada zako za kumtunza. Kuelewa hofu za mtoto na mahangaiko yake kwaweza kukusaidia umtendee kwa huruma. Labda kukiri hofu zake na kumhakikishia kwamba utafanya yote uwezayo kumtunza kutasaidia sana kupunguza hofu yake.

      Kukabiliana na Mikazo

      ‘Nimekuwa nikihisi nimeumizwa sana na kujisikitikia. Hatustahili kupatwa na mambo haya.’ Ndivyo alivyosema nyanya mmoja mlezi. Ikiwa uko katika hali hiyo, waweza kuwa na hisia za namna hiyo. Lakini jambo hilo si lenye kukatisha tumaini. Sababu moja ni kwamba, huenda umri ukapunguza nguvu zako za kimwili, lakini umri ni kitu chenye manufaa, hekima, saburi, na ujuzi vinapohusika. Haishangazi kwamba, uchunguzi ulifunua kwamba “watoto waliolelewa na babu na nyanya peke yao walifanikiwa zaidi walipolinganishwa na watoto katika familia zenye mzazi mmoja wa asili.”

      Biblia hutuhimiza ‘tutupe hangaiko letu lote juu ya Yehova, kwa sababu yeye hutujali sisi.’ (1 Petro 5:7) Hivyo, sali daima akupe nguvu na mwongozo, kama alivyofanya mtunga-zaburi. (Linganisha Zaburi 71:18.) Kazia uangalifu mahitaji yako ya kiroho. (Mathayo 5:3) “Mikutano ya Kikristo pamoja na kuhubiria wengine ni mambo yaliyonisaidia niendelee,” asema mwanamke mmoja Mkristo. Inapowezekana, jaribu kufundisha wajukuu wako njia za Mungu. (Kumbukumbu la Torati 4:9) Kwa hakika Mungu atategemeza jitihada zako za kulea wajukuu “katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.”—Waefeso 6:4.b

      Usiogope kutafuta msaada. Mara nyingi marafiki wanaweza kusaidia, hasa ndani ya kutaniko la Kikristo. Sally akumbuka hivi: “Ndugu na dada kutanikoni waliandaa utegemezo kwelikweli. Niliposhuka moyo walikuwapo ili kunitegemeza. Wengine hata walinipa msaada wa kifedha.”

      Usiachilie msaada unaoweza kupatikana kutoka kwa serikali. (Waroma 13:6) Kwa kupendeza, kulingana na uchunguzi mmoja uliofanyiwa babu na nyanya, “wengi hawajui ni msaada gani unaopatikana au mahali pa kutafuta msaada.” (Child Welfare) Wafanyakazi wa huduma za jamii na mashirika ya mahali penu yanayosaidia wazee-wazee yaweza kukuelekeza upate huduma zinazosaidia.

      Katika visa vingi, babu na nyanya walezi ni miongoni mwa watu wanaopatikana katika “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1-5) Kwa uzuri, nyakati hizi ngumu ni ishara kwamba karibuni Mungu ataingilia kati na kuumba “dunia mpya” ambayo hali zenye msiba zinazopata familia nyingi leo zitapitilia mbali. (2 Petro 3:13; Ufunuo 21:3, 4) Kwa wakati uliopo, babu na nyanya walezi watalazimika kufanya yote wawezayo ili kufanikiwa katika hali yao. Wengi wanafanikiwa sana katika jitihada zao! Sikuzote kumbuka kwamba kujapokuwa kukatishwa tamaa, shangwe yaweza kupatikana. Kwani, huenda ukapata shangwe ya kuwaona wajukuu wako wakiwa wapenda-Mungu walio wanyofu! Je, hustahili kufanya kazi ngumu ili kufanikiwa?

      [Maelezo ya Chini]

      a Baadhi ya majina yamebadilishwa.

      b Kitabu Siri ya Kupata Furaha ya Familia (kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.) kina kanuni nyingi za Biblia zenye kusaidia ambazo babu na nyanya walezi wanaweza kutumia kuwalea wajukuu wao.

      [Sanduku katika ukurasa wa 10]

      Masuala ya Kisheria

      Kama utachukua hatua za kisheria kuwa mlezi wa mjukuu wako ama la, ni swali linalohitaji kushughulikiwa kwa uangalifu sana na lililo tata. Mtaalamu wa habari hii, Mary Fron aeleza hivi: “Kwa upande mmoja, una haki chache za kisheria bila kuwa mlezi wa mtoto. Katika visa vingi, wazazi wa asili wanaweza kurudi na kumchukua mtoto au watoto wakati wowote. Kwa upande mwingine, babu na nyanya wengi wanasitasita kutafuta kuwa walezi wa mtoto, kwa sababu hiyo inamaanisha kutoa ushahidi mahakamani ya kwamba mtoto wako ni mzazi asiyefaa.”—Good Housekeeping.

      Bila haki ya kisheria ya kuwa mlezi mara nyingi babu na nyanya wanapata ugumu wa kuandikisha watoto wao shuleni au hata kuwapatia matibabu. Hata hivyo, kupata malezi, kwaweza kuwa masaibu yenye gharama kubwa, yanayochukua wakati, na yenye kuchosha kihisia-moyo. Na hata yanapopatikana, huenda babu na nyanya wakanyimwa msaada wa kifedha kutoka kwa serikali. Hivyo jarida Child Welfare lawashauri babu na nyanya “watafute mashauri kuhusu mambo ya kisheria kutoka kwa wakili aliye na uzoefu katika sheria ya familia ya nchi, kesi za malezi, na hali njema ya mtoto.”

      [Sanduku katika ukurasa wa 11]

      Kuhesabu Gharama

      Kumwona mtoto akiwa katika uhitaji—hasa aliye wa jamaa yako—ni jambo la kuhuzunisha sana. Na Biblia huwaamuru Wakristo wawatunze ‘walio wao wenyewe.’ (1 Timotheo 5:8) Hata hivyo, katika hali nyingi nyanya au babu atakuwa mwenye hekima kufikiria jambo hili kwa uzito kabla hajachukua daraka hili. (Mithali 14:15; 21:5) Lazima mtu ahesabu gharama.—Linganisha Luka 14:28.

      Fikiria mambo haya kwa sala: Je, uko tayari kimwili, kihisia-moyo, kiroho, na kifedha kutimiza mahitaji ya mtoto huyu? Mwenzi wako anahisije kuhusu hali hiyo? Je, kuna njia yoyote ya kutia moyo au kusaidia wazazi wa mtoto ili waweze kumtunza mtoto wao wenyewe? Kwa kusikitisha, wazazi fulani wasiowajibika wanafuatia tu mtindo-maisha usio na adili. Nyanya mmoja akumbuka hivi kwa uchungu: “Nilichukua baadhi ya watoto wake. Lakini aliendelea kutumia dawa za kulevya na kuzaa watoto zaidi. Nilifikia mahali ambapo nililazimika kukataa!”

      Kwa upande mwingine, usipowajali wajukuu wako, ni nini kitakachowapata? Je, unaweza kukabiliana na mkazo wa kujua kwamba wanatunzwa na wengine, labda na watu usiowajua? Vipi juu ya mahitaji ya kiroho ya watoto? Je, wengine wataweza kuwalea kulingana na viwango vya Mungu? Huenda wengine wakafikia mkataa kwamba kujapokuwa magumu yanayohusika, hawana jingine ila kutwaa daraka hilo.

      Haya ni mahangaiko yanayohuzunisha sana, na lazima kila mtu ajiamulie mwenyewe.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki