Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Jinsi Hali ya Hewa Inavyoweza Kubadili Historia
    Amkeni!—2011 | Juni
    • Dhoruba Ilipopiga

      Mnamo 1588, Mfalme Philip wa Hispania alituma msafara wa meli, zilizojulikana kama Manowari za Hispania, kushambulia Uingereza. Lakini mambo yalimwendea mrama kwani hali ya hewa ilivuruga kabisa mipango yake.

      Msafara wa meli hizo za Hispania uliingia kwenye Mlango-Bahari wa Uingereza na kukutana na meli za Uingereza. Meli hizo za Uingereza zinazoweza kuendeshwa kwa urahisi zilishambulia zile za Hispania lakini zikaharibu chache tu. Kisha, Manowari za Hispania zikatia nanga katika bandari ya Calais ili kuchukua wanajeshi wa kuvamia Uingereza.

      Ilipokuwa usiku, majeshi ya Uingereza yaliwasha moto meli zake kadhaa, na kuziacha zielee zikisukumwa na upepo bila kuongozwa na mtu yeyote na kuelekea meli za Hispania zilizokuwa zimetia nanga. Wanajeshi wa meli za Hispania walikata nanga nyingi ili kukwepa meli hizo za Uingereza zilizokuwa zikiwaka moto. Hatua hiyo ya Wahispania iliwaletea matatizo baadaye.

      Baada ya kisa hicho kilichotokea huko Calais, meli zote zilielekea kwenye Bahari ya Kaskazini, huku upepo ukizisukuma kutoka upande wa nyuma. Kufikia sasa, majeshi ya Uingereza yalikuwa yameishiwa na silaha, hivyo yakatia nanga kwenye pwani ya Uingereza. Kwa kuwa Waingereza walizuia Manowari za Hispania zisiweze kurudi Hispania na upepo ulikuwa ukipiga dhidi ya meli hizo, Wahispania walilazimika kusafiri kuelekea upande wa kaskazini kuzunguka Scotland, halafu waelekee kusini kupita Ireland, kisha warudi Hispania.

      Kufikia wakati huu, meli za Hispania zilikuwa zimeishiwa kabisa maji na chakula, na zile zilizokuwa zimeharibiwa zilikuwa zikiwasafirisha wanajeshi wengi waliokuwa wamejeruhiwa vibaya pamoja na wengine waliokuwa wakiugua kiseyeye. Kwa hiyo, wasafiri wote walipimiwa sana chakula na hivyo wakazidi kuwa hoi.

      Baada ya meli hizo kuzunguka Scotland, dhoruba kali sana kutoka Bahari ya Atlantiki ilipiga meli hizo na kuzisukuma kuelekea ufuo wa Ireland. Kwa kawaida, chini ya hali hizo wangetia nanga na kusubiri dhoruba hiyo ipite. Hata hivyo, kwa sababu nyingi ya nanga zilikuwa zimekatwa wakati wa mashambulizi ya hapo awali, meli 26 za Hispania zilivunjika kwenye pwani ya Ireland, na kusababisha vifo vya wanaume kati ya 5,000 na 6,000.

      Kufikia wakati Manowari hizo ziliporudi Hispania, karibu watu 20,000 walikuwa wamekufa. Kwa kweli hali mbaya ya hewa ndiyo hasa iliyosababisha vifo vya watu hao wote na kuharibu meli hizo. Inaonekana kwamba Waholanzi waliamini hivyo. Baadaye, walipotengeneza medali ya kukumbuka kushindwa kwa Manowari za Hispania, walitangaza wazi imani iliyokuwa imeenea sana kwamba Mungu husababisha misiba ya asili na hivyo wakaandika hivi kwenye medali hiyo: “Yehova alipuliza nao wakatawanyika.”

  • Jinsi Hali ya Hewa Inavyoweza Kubadili Historia
    Amkeni!—2011 | Juni
    • [Picha katika ukurasa wa 24]

      Manowari za Hispania

      [Hisani]

      © 19th era/Alamy

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki