Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Mahakama ya Ulaya Yasahihisha Ukiukwaji wa Sheria
    Amkeni!—1998 | Januari 8
    • Kufungwa Gerezani Kinyume cha Sheria

      Kulingana na sheria hii, mwishoni mwa mwaka wa 1989 na mwanzoni mwa mwaka wa 1990, Dimitrios Tsirlis na Timotheos Kouloumpas, ambao ni wahudumu waliowekwa rasmi wa Kutaniko la Kikristo la Central la Mashahidi wa Yehova katika Ugiriki, waliwasilisha maombi yao katika ofisi zilizowahusu za uandikishaji wa askari ili waruhusiwe wasijiandikishe katika utumishi wa kijeshi. Pamoja na fomu zao za maombi, waliwasilisha hati zinazothibitisha kwamba wao walikuwa wahudumu wa kidini. Kama ilivyotarajiwa, maombi hayo yalikataliwa kwa sababu zisizo na ukweli kwamba Mashahidi wa Yehova si “dini inayojulikana.”

      Ndugu Tsirlis na Kouloumpas waliripoti katika vituo walivyotakiwa vya mafunzo ya kijeshi na kukamatwa, wakashtakiwa kwa kukosa utii, na kuwekwa kizuizini. Wakati huohuo, Makao Makuu ya Jeshi yalikataa rufani zao dhidi ya uamuzi wa ofisi za uandikishaji wa askari. Wenye mamlaka wa kijeshi walisema kwamba Sinodi Takatifu ya Kanisa Othodoksi la Kigiriki ilikuwa imewaarifu kwamba Mashahidi wa Yehova si dini inayotambuliwa! Hili lilipingana na maamuzi mengi ya mahakama za kiraia ambazo zilikuwa zimesema kwamba kwa kweli Mashahidi wa Yehova ni dini inayojulikana.

      Mahakama za kijeshi nazo zikawapata Tsirlis na Kouloumpas kuwa na hatia ya kukosa utii na kuwahukumu kifungo cha miaka minne gerezani. Ndugu hao wawili walikata rufani ya maamuzi haya kwa Mahakama ya Kijeshi ya Rufani, ambayo iliahirisha kusikiliza kwa rufani mara tatu kwa sababu mbalimbali. Hata hivyo, ilikataa kila mara kutoa amri ya kuruhusu wakata-rufani kutolewa gerezani, ingawa sheria za Ugiriki zinatoa ruhusa ya jambo hili.

      Wakati huohuo, katika kesi nyinginezo, Mahakama Kuu Zaidi ya Usimamizi ilibatilisha maamuzi ya Makao Makuu ya Jeshi, kwa msingi wa kwamba Mashahidi wa Yehova kwelikweli ni dini yenye kujulikana!

      Katika kipindi cha miezi 15 ambacho Tsirlis na Kouloumpas walilazimika kukaa katika Gereza la Kijeshi la Avlona, walikabili matendo yasiyo ya kibinadamu kabisa na ya kushusha sana pamoja na Mashahidi wengine waliotiwa gerezani. Ripoti moja ya wakati huo ilisema kuhusu “hali mbaya sana za gereza ambazo [wafungwa Mashahidi wa Yehova] wanakaa, ikitaja nyama zilizooza na mikia ya panya, ambayo mara nyingi huandaliwa pamoja na chakula, kukatizwa kwa saa za kutembelewa kulingana na maoni ya Usimamizi, ukosefu wa nafasi kwa sababu ya kujaa kupita kiasi kwa wafungwa na kutendwa kubaya kwingi zaidi kulikotolewa kwa wafungwa kama hao walio wakataaji wa kudhamiria.”

      Hatimaye, Mahakama ya Rufani ya Kijeshi iliwaondolea hatia Ndugu Tsirlis na Kouloumpas lakini wakati huohuo iliamua kwamba Serikali haikuwa na wajibu wa kuwalipa fidia kwa kuwekwa kwao kizuizini kwa sababu “kuwekwa kwao kizuizini kulitokana na uzembe mzito kwa upande wa wakata-rufani.” Hili lilitokeza maswali halali miongoni mwa wanasheria: Ni nani aliyekuwa na uzembe mzito? Mashahidi hao au mahakama za kijeshi?

      Mara moja ndugu hao waliachiliwa kutoka gerezani na hatimaye waliondolewa jeshini kwa msingi wa kwamba wao walikuwa wahudumu wa kidini. Walipoachiliwa, shirika la Amnesty International lilitangaza kwamba lilifurahia kuachiliwa kwa Dimitrios Tsirlis na Timotheos Kouloumpas na lilieleza matumaini ya kwamba kwa wakati ujao, wahudumu wa Mashahidi wa Yehova wangeruhusiwa wasishiriki katika utumishi wa kijeshi kulingana na ruhusa itolewayo na sheria ya Kigiriki. Lakini, baada ya muda mfupi, matumaini haya yangetupiliwa mbali.

  • Mahakama ya Ulaya Yasahihisha Ukiukwaji wa Sheria
    Amkeni!—1998 | Januari 8
    • Kukata Rufani kwa Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu

      Baada ya kuondolewa hatia na kufunguliwa kutoka gerezani, wahasiriwa wote watatu wa ubaguzi huu wa kidini walihisi kimaadili kukata rufani kwa Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu. Msingi wa rufani hii ulikuwa kuwekwa kizuizini kwao kulikokuwa kinyume cha sheria, ambako kwenyewe hakukuwa halali, na mateso ya kiakili na ya kimwili waliyopata, hali kadhalika matokeo ya kiadili na ya kijamii yaliyohusika kutokana na kunyimwa-nyimwa uhuru wao kwa kipindi kirefu sana cha wakati. Kwa sababu hizi walifuatilia kiasi cha haki na kinachostahili cha fidia.

      Tume ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu ilifikia mkataa kwa pamoja kwamba katika kesi za Tsirlis na Kouloumpas, walivunjiwa haki zao za uhuru na usalama wakiwa watu, kwamba kuwekwa kwao kizuizini hakukuwa halali, kwamba walikuwa na haki ya kupata fidia, na kwamba hawakupata haki ya kusikilizwa vizuri na mahakama katika kesi yao. Mkataa kama huo ulifikiwa na Tume hiyo katika kesi ya Georgiadis.

      Udhalimu Wasahihishwa

      Kesi ilipangwa kusikilizwa Januari 21, 1997. Wengi walikuwapo mahakamani, kutia ndani wanafunzi kutoka chuo kikuu cha mahali hapo, waandishi wa habari, na Mashahidi wa Yehova kadhaa kutoka Ugiriki, Ujerumani, Ubelgiji, na Ufaransa.

      Bw. Panos Bitsaxis, wakili wa Mashahidi, alizungumza juu ya “ukaidi wa daima na mtazamo wenye kudumu wa wenye mamlaka wa Ugiriki kutotambua kuwepo kwa dini moja ndogo,” yaani Mashahidi wa Yehova. Alishutumu mazoea ya wenye mamlaka wa Ugiriki ya kutegemeza maoni yao rasmi juu ya Mashahidi juu ya maoni ya wapinzani wao wakuu—Kanisa Othodoksi la Kigiriki! Aliendelea: “Hali hii itaruhusiwa kuendelea kwa kadiri gani? . . . Na hadi lini?” Alisema juu ya “kukataa kutambua jamii fulani ya kidini, kukataa ambako kwaonekana kuwa upuuzi, uonapo kwamba huja moja kwa moja, kwa wazi, na bila kusababu, dhidi ya sheria, dhidi ya makumi ya maamuzi ya Mahakama Kuu Zaidi ya Usimamizi.”

      Mwakilishi wa serikali ya Ugiriki alithibitisha huo mtazamo wenye upendeleo wa wenye mamlaka wa Ugiriki kwa kudai hivi: “Haipaswi kusahauliwa kwamba kihalisi watu wote wa Ugiriki wamekuwa sehemu ya Kanisa Othodoksi kwa karne kadhaa. Tokeo moja la kawaida ni kwamba muundo wa Kanisa hilo na hadhi ya wahudumu wake na majukumu yao katika Kanisa yako wazi kabisa. . . . Hadhi za wahudumu kutoka Kanisa la Mashahidi wa Yehova si wazi sana.” Ni hali iliyoje ya kukubali kwa wazi matendo ya ubaguzi dhidi ya dini ndogondogo katika Ugiriki!

      Uhuru wa Kidini Wategemezwa

      Hukumu ilitolewa Mei 29. Msimamizi wa Mahakama, Bw. Rolv Ryssdal, alisoma kwa sauti uamuzi huo. Mahakama, ikiwa imeundwa na majaji tisa, kwa kauli moja imeona kwamba Ugiriki ilikuwa imevunja Ibara ya 5 na ya 6 ya Mkataba wa Ulaya. Pia iliwapa wakata-rufani dola za Marekani 72,000 kwa fidia na gharama. Jambo la maana zaidi kuliko yote, uamuzi huo ulitia ndani mabishano mengi ya maana yakipendelea uhuru wa kidini.

      Mahakama ilisema kwamba “wenye mamlaka wa kijeshi walipuuza vibaya sana” ukweli wa kwamba Mashahidi wa Yehova wanatambuliwa kuwa “dini inayojulikana” katika Ugiriki, kulingana na maamuzi ya Mahakama Kuu Zaidi ya Usimamizi. Pia ilitoa maelezo haya: “Kudumu kukataa kwa wenye mamlaka waliohusika kutambua Mashahidi wa Yehova kuwa ‘dini inayojulikana’ na kudharau haki za walalamikaji kwa uhuru waliotaka kulikuwa ubaguzi kwa kulinganishwa na njia ambayo wahudumu wa Kanisa Othodoksi la Kigiriki hupata ruhusa.”

      Kesi hiyo ilitangazwa sana na vyombo vya habari vya Ugiriki. Gazeti la Athens News lilitangaza hivi: ‘Mahakama ya U[laya] yailaumu vikali Ugiriki kuhusu madai ya Yehova.’ Uamuzi wa kesi ya Tsirlis & Kouloumpas and Georgiadis v. Greece ulitoa matumaini kwamba Serikali ya Ugiriki itapatanisha sheria zake na Uamuzi wa Mahakama ya Ulaya, ili Mashahidi wa Yehova katika Ugiriki waweze kufurahia uhuru wa kidini bila kuingiliwa na usimamizi, jeshi au kanisa. Zaidi ya hayo, hii ni hukumu nyingine tena iliyotolewa na Mahakama ya Ulaya dhidi ya mahakama za Ugiriki juu ya masuala yahusuyo uhuru wa kidini.a

      Mashahidi wa Yehova huthamini sana uhuru wao, nao hujitahidi kuutumia katika kumtumikia Mungu na kuwasaidia jirani zao. Wahudumu wa kidini watatu walio Mashahidi walipeleka kesi zao hadi Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu, si kwa sababu ya kupata faida zozote za kimwili, lakini kwa sababu tu za kimaadili. Hivyo, wote watatu wameamua kwamba fidia waliyopata itatumika tu kwa ajili ya kuendeleza kazi ya kielimu ya Mashahidi wa Yehova.

  • Mahakama ya Ulaya Yasahihisha Ukiukwaji wa Sheria
    Amkeni!—1998 | Januari 8
    • Timotheos na Nafsika Kouloumpas

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki