Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Huzuni Yenye Kulemea Sana
    Amkeni!—2011 | Aprili
    • Huzuni Yenye Kulemea Sana

      Nicolle alikuwa msichana mwenye afya. Lakini jioni moja alisema kwamba anaumwa na kichwa, na wazazi wake wakampeleka hospitalini. Jioni iliyofuata, akiwa bado anapata matibabu, Nicolle alipatwa na mshtuko wa moyo. Uchunguzi zaidi ulionyesha kwamba alikuwa na maambukizo ya bakteria yasiyojulikana sana na maambukizo hayo yalikuwa yameenea kwenye mapafu, figo, na moyo wake. Katika muda wa saa 48, Nicolle alikuwa amekufa. Alikuwa na umri wa miaka mitatu tu.

      KIFO cha mpendwa ni mojawapo ya mambo yenye kuumiza sana ambayo mwanadamu anaweza kukabili. Nyakati nyingine, huzuni hiyo inaweza kuwa yenye kulemea sana. “Ninamkosa sana Nicolle,” anasema Isabelle, mama ya msichana huyo. “Ninakosa kumbatio lake, harufu yake, wororo wake. Ninakosa ua alilokuwa akinipa kila siku. Mimi humfikiria Nicolle kila siku.”

      Je, umefiwa na mpendwa wako—iwe ni mtoto, mwenzi wa ndoa, ndugu au dada, mzazi, au rafiki wa karibu? Ikiwa ndivyo, unaweza kukabiliana jinsi gani na huzuni yako?

  • Kukabiliana na Hisia Mpendwa Anapokufa
    Amkeni!—2011 | Aprili
    • Kukabiliana na Hisia Mpendwa Anapokufa

      “Nilishtuka na kuwa hoi nilipopata habari za kifo cha baba yangu. Nililemewa na hisia za hatia kwa kuwa sikuwa karibu alipokufa. Hakuna kitu kinachoweza kulinganishwa na uchungu mwingi sana ambao mtu huhisi anapofiwa na mpendwa wake. Ninamkosa sana baba yangu!”—Sara.

      WATU wengi huona kuwa ni vigumu kuzungumza kuhusu kifo, wawe ni wa dini au utamaduni gani. Lugha fulani hutumia maneno ya badala kuzungumzia kifo. Katika Kiswahili, badala ya kusema mtu “amekufa,” watu watasema “ametuacha,” “ameaga,” au “hayupo nasi tena.”

      Lakini, hata watu watumie maneno gani, hakuna neno linaloweza kupunguza huzuni kali ambayo watu waliofiwa na mpendwa wao huhisi. Watu fulani hulemewa sana na huzuni hivi kwamba hawakubali kuwa mpendwa wao amekufa.

      Ikiwa umefiwa na mpendwa wako, huenda wewe pia ukashindwa kukabiliana na hisia zako. Huenda ukaonyesha kwamba umekubali ukweli wa mambo, lakini huenda moyoni ukawa unahisi vingine. Bila shaka, watu wote hawaombolezi kwa njia ileile, kwa hiyo, ikiwa huonyeshi huzuni yako waziwazi, hilo halimaanishi kwamba huna huzuni.a Tatizo linaweza kutokea unapojilazimisha kuonyesha hisia fulani kwa sababu ya watu wengine—labda watu wa familia wanaoomboleza ambao wanatarajia ufanye hivyo.

      “Sikupata Nafasi ya Kuomboleza”

      Fikiria kisa cha Nathaniel, mwanamume ambaye alifiwa na mama yake alipokuwa na umri wa miaka 24. Anasema: “Kwanza nilichanganyikiwa. Nilihisi kwamba ninapaswa kumfariji baba yangu na marafiki wengi wa mama ambao walikuwa na huzuni. Sikupata nafasi ya kuomboleza.”

      Baada ya zaidi ya mwaka mmoja, Nathaniel aligundua kwamba bado hakuwa amekabiliana na hisia za kifo cha mama yake. Anasema: “Bado Baba hunipigia simu mara kwa mara kunieleza hisia zake, na ni vizuri kwamba anafanya hivyo. Anahitaji kuzungumza kuhusu hisia zake, nami ninafurahi kumsaidia. Lakini mimi ninapohitaji faraja, ninahisi kwamba sina yeyote wa kunifariji.”

      Wale wanaowatunza wagonjwa—kutia ndani madaktari na wengine ambao mara nyingi huona watu wakifa—huenda wakahisi kwamba wanapaswa kufungia hisia zao. Fikiria mfano wa Heloisa, ambaye amekuwa daktari kwa zaidi ya miaka 20. Alifanya kazi katika jamii ambayo ina desturi ya kushirikiana kwa ukaribu, naye alikuwa na uhusiano wa karibu na wagonjwa wake. Anasema: “Niliketi pamoja na wengi wao walipokuwa wakifa, na baadhi yao walikuwa marafiki wangu wapendwa.”

      Heloisa alitambua kwamba kulia ni njia ya kawaida ya kupata kitulizo. “Lakini ilikuwa vigumu kwangu kulia,” anasema. “Nilihangaikia sana kuwategemeza wengine hivi kwamba nilihisi ninapaswa kufungia hisia zangu. Niliamini kwamba wengine walitazamia nifanye hivyo.”

      “Nilijihisi Nikiwa Mpweke Bila Mama”

      Huenda upweke ndilo tatizo kubwa zaidi ambalo huwapata wale ambao wamefiwa na mpendwa wao. Kwa mfano, Ashley alikuwa na umri wa miaka 19 mama yake alipokufa kutokana na kansa. Anasema: “Baadaye nilijihisi nikiwa nimechanganyikiwa kabisa na mpweke sana. Mama alikuwa ndiye rafiki yangu wa karibu zaidi. Tulikuwa pamoja mara nyingi!”

      Inaeleweka kwamba Ashley aliona ugumu wa kurudi nyumbani kila siku na kutambua kwamba mama yake hayupo. Anasema: “Nilijihisi nikiwa mpweke bila mama. Mara nyingi nilienda chumbani na kulia huku nikitazama picha zake na kufikiria kuhusu mambo ambayo tulikuwa tukifanya pamoja.”

      Ikiwa umefiwa na mtu wa familia au rafiki mpendwa, usijihisi kwamba ni wewe tu unayelemewa na hisia za huzuni. Kama tutakavyoona, wengine pia wamekabiliana na hali hiyo kwa njia inayofaa.

      [Maelezo ya Chini]

      a Kwa kuwa kila mtu huomboleza kwa njia tofauti, haingefaa kuwahukumu wale ambao hawaonyeshi hisia zao waziwazi wanapofiwa na mpendwa.

      [Blabu katika ukurasa wa 5]

      “Nilijihisi nikiwa nimechanganyikiwa kabisa na mpweke sana. Mama alikuwa ndiye rafiki yangu wa karibu zaidi”—Ashley

  • Msaada kwa Wale Wanaoomboleza
    Amkeni!—2011 | Aprili
    • Msaada kwa Wale Wanaoomboleza

      “Yehova yuko karibu na wale waliovunjika moyo.”—Zaburi 34:18.

      MPENDWA wako anapokufa, huenda ukalemewa na hisia mbalimbali, kutia ndani kushtuka, kuhisi ni kana kwamba hisia zako zimekufa ganzi, huzuni, na labda hasira au kuhisi una hatia. Kama ilivyotajwa katika habari iliyotangulia, watu wote hawaombolezi kwa njia ileile. Kwa hiyo, huenda usihisi hisia hizo zote, na huenda usionyeshe huzuni yako kwa njia ileile kama wengine. Hata hivyo, hakuna ubaya wowote kuonyesha huzuni unapohitaji kufanya hivyo.

      “Omboleza!”

      Heloisa, daktari aliyenukuliwa katika habari iliyotangulia alijaribu kufungia hisia zake baada ya mama yake kufa. “Mwanzoni nililia,” anasema, “lakini nikaanza kufungia hisia zangu kama tu nilivyokuwa nikifanya mgonjwa alipokufa. Labda kufanya hivyo kumechangia sana kuzorota kwa afya yangu. Ninawashauri hivi wale ambao wamefiwa na mpendwa wao: Omboleza! Usifiche huzuni. Kufanya hivyo kutakuletea kitulizo.”

      Hata hivyo, kadiri siku na majuma yanavyopita, huenda ukahisi kama Cecília, ambaye mume wake alikufa kutokana na kansa. Anasema hivi: “Nyakati nyingine ninatamauka kwa sababu inaonekana kwamba watu fulani wanahisi ninapaswa kuwa nimeacha kuomboleza.”

      Ikiwa unapatwa na mawazo kama hayo, kumbuka kwamba hakuna njia “hususa” iliyowekwa ya kuomboleza. Wengine wanaweza kurudia maisha yao ya kawaida kwa urahisi. Wengine hawawezi. Katika visa kama hivyo, mtu hawezi kuharakisha kipindi cha kuomboleza, kwa hiyo usihisi ni kana kwamba unapaswa kuwa umeacha kuomboleza kufikia wakati fulani hususa.a

      Lakini namna gani ikiwa huzuni yako inaonekana ni kama haitawahi kwisha na unahisi ni kama imekulemea? Huenda ukawa kama Yakobo, mwanamume mwadilifu ambaye, alipoambiwa kwamba mwana wake Yosefu alikuwa amekufa, ‘alizidi kukataa kufarijiwa.’ (Mwanzo 37:35) Ikiwa umetenda kwa njia hiyo, unaweza kuchukua hatua gani ili usilemewe na huzuni?

      Tunza afya yako. Cecília anasema hivi: “Nyakati nyingine ninapojihisi mchovu sana, mimi hutambua kwamba nimepita mipaka.” Kama anavyosema, huzuni inaweza kumchosha sana mtu kimwili na kihisia. Kwa hiyo, ni vizuri utunze afya yako. Pumzika kiasi cha kutosha na ule vyakula vyenye lishe.

      Ni kweli kwamba huenda usiwe na hamu ya kula, kwenda kununua vitu, au kupika. Lakini usipokula chakula chenye lishe, huenda ikawa rahisi kwako kupatwa na maambukizo au magonjwa, na hilo litaongeza huzuni yako. Jaribu kula angalau chakula kidogo ili udumishe afya nzuri.b

      Ikiwezekana, fanya mazoezi ya aina fulani, hata kama ni kutembea tu. Kufanya mazoezi kutakulazimisha utoke nje. Isitoshe, mazoezi yanayofanywa kwa kiasi huchochea kutokezwa kwa kemikali inayopatikana katika ubongo inayoitwa endorphin ambayo inaweza kukufanya uhisi vizuri zaidi.

      Kubali msaada kutoka kwa wengine. Hilo ni muhimu hasa mwenzi wa ndoa anapokufa. Huenda kuna mambo fulani ambayo alikuwa akishughulikia, na sasa hayafanywi. Kwa mfano, ikiwa mwenzi wako alikuwa akishughulikia mambo ya pesa au kazi za nyumbani, huenda mwanzoni ikawa vigumu kwako kufanya mambo hayo. Katika hali kama hiyo, shauri la marafiki wenye busara litakusaidia sana.—Methali 25:11.

      Biblia inasema kwamba rafiki wa kweli ni “ndugu aliyezaliwa kwa ajili ya wakati wa taabu.” (Methali 17:17) Hivyo, usijitenge na wengine, ukidhani kwamba utakuwa mzigo kwao. Badala yake, kushirikiana na wengine kunaweza kuwa kama daraja ambalo litakusaidia uache kuwa na huzuni na urudie maisha yako ya kawaida. Baada ya mama yake kufa, msichana mmoja anayeitwa Sally, aliona kwamba kushirikiana na wengine kulimtia sana moyo. Anasema: “Marafiki wengi walinialika kwenye tafrija zao. Hilo lilinisaidia sana kukabiliana na upweke mwingi niliohisi. Nilithamini sana watu waliponiuliza maswali rahisi kama, ‘Unakabiliana jinsi gani na kifo cha mama yako?’ Niliona kwamba kuzungumza kumhusu mama yangu kulinisaidia kupona.”

      Jikumbushe mambo yaliyopita. Jaribu kujikumbusha mambo yenye kufurahisha ambayo ulifanya pamoja na mpendwa wako, labda kwa kutazama picha. Ni kweli kwamba mwanzoni huenda ukahuzunika unapokumbuka pindi hizo. Ingawa hivyo, baada ya muda, kujikumbusha mambo kwa njia hiyo kutakusaidia kupona badala ya kukuumiza.

      Huenda hata ukajaribu kuandika mambo kwenye kitabu. Unaweza kuandika kuhusu mambo yenye kufurahisha, na hata utie ndani mambo ambayo unatamani ungemwambia mpendwa wako alipokuwa hai. Huenda ikawa rahisi kuelewa hisia zako unaposoma yale uliyoandika. Kuandika pia kunaweza kukusaidia kuondoa hisia zako kwa njia inayofaa.

      Je, ni sawa kuhifadhi vitu vitakavyokukumbusha kuhusu mpendwa wako aliyekufa? Watu wana maoni mbalimbali kuhusu jambo hilo, na haishangazi kwa kuwa kila mtu huomboleza kwa njia tofauti. Watu fulani huona kwamba kuweka vitu vya mpendwa wao huwazuia kupona. Wengine husema kwamba kufanya hivyo huwasaidia kupona. Sally, aliyenukuliwa awali anasema: “Nimehifadhi vitu vingi vilivyokuwa vya mama yangu. Hilo hunisaidia kukabiliana na kifo chake!”c

      Mtegemee “Mungu wa faraja yote.” Biblia inasema hivi: “Mtupie Yehova mzigo wako, naye mwenyewe atakutegemeza.” (Zaburi 55:22) Kusali kwa Mungu si kama miti-shamba ya kutusaidia tujihisi vizuri. Ni njia halisi na muhimu ya kuwasiliana na “Mungu wa faraja yote, ambaye hutufariji katika dhiki yetu yote.”—2 Wakorintho 1:3, 4.

      Neno la Mungu, Biblia, linatupa faraja bora zaidi. Mtume Mkristo Paulo, alisema hivi: “Nina tumaini kwa Mungu . . . kwamba kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.” (Matendo 24:15) Kutafakari kuhusu tumaini la Biblia la ufufuo kunaweza kuwa ndiyo njia bora zaidi ya kuwafariji wale wanaoomboleza kifo cha mpendwa wao.d Hivyo ndivyo Lauren, ambaye ndugu yake mdogo alikufa katika aksidenti alivyohisi. Anasema hivi: “Hata nilipohisi huzuni nyingi sana, nilichukua Biblia na kuisoma, hata kama ni mstari mmoja tu. Nilichagua mistari ambayo ilinitia moyo, na niliisoma tena na tena. Kwa mfano, nilifarijiwa na maneno ambayo Yesu alimwambia Martha baada ya Lazaro kufa. Alimwambia: ‘Ndugu yako atafufuka.’”—Yohana 11:23.

      “Usiache Ikutawale”

      Ingawa huenda ikaonekana kuwa vigumu kushinda huzuni, kufanya hivyo kutakusaidia kurudia maisha yako ya kawaida. Usijihisi ukiwa na hatia eti ni kana kwamba unamsaliti au unamsahau mpendwa wako kwa kujaribu kurudia maisha yako. Ukweli ni kwamba hutawahi kumsahau mpendwa wako. Nyakati nyingine utakumbuka mambo fulani kumhusu, lakini hatua kwa hatua, hisia za huzuni zitapungua.

      Huenda pia ukakumbuka kwa shauku pindi zenye kufurahisha na kuhuzunisha. Kwa mfano, Ashley, aliyenukuliwa katika habari iliyotangulia, anasema hivi: “Nakumbuka siku moja kabla ya mama yangu kufa. Alionekana kuwa anapata nafuu, na siku hiyo alitoka kitandani ingawa hakuwa amefanya hivyo kwa siku nyingi. Dada yangu alipokuwa akichana nywele za Mama, sote watatu tulianza kucheka kuhusu jambo fulani, na niliona mama yangu akitabasamu, jambo ambalo hakuwa amefanya kwa muda mrefu. Aliridhika sana kuwa na binti zake.”

      Utaweza pia kukumbuka mambo muhimu uliyojifunza ulipokuwa na mpendwa wako. Kwa mfano, Sally anasema hivi: “Mama alikuwa mwalimu mzuri sana. Alinishauri bila kunilazimisha kufuata shauri lake, na alinifundisha jinsi ya kufanya maamuzi mazuri ambayo yalikuwa maamuzi yangu mwenyewe na si yale tu yeye au baba walisema.”

      Huenda jambo unalohitaji ili urudie maisha yako ya kawaida ni kujikumbusha mambo fulani kuhusu mpendwa wako. Kijana mmoja anayeitwa Alex aligundua jambo hilo. Anasema hivi: “Baada ya baba yangu kufa, niliazimia kuishi kama alivyonifundisha, yaani, nisiache kamwe kufurahia maisha. Kwa wale ambao wamefiwa na mzazi, ningesema hivi: Kwa kweli, hutawahi kuacha kuwa na huzuni ya kufiwa na mzazi wako, lakini usiache ikutawale. Omboleza na ulie, lakini usisahau kwamba bado unapaswa kutumia vizuri maisha yaliyo mbele yako.”

      [Maelezo ya Chini]

      a Kuhusiana na jambo hilo, hupaswi kufanya uamuzi wa haraka-haraka kuhusu mambo kama vile kuhamia nyumba nyingine au kutafuta mwenzi mwingine. Mabadiliko hayo yanapaswa kufanywa baada ya kuwa na wakati wa kutosha kuzoea hali yako mpya maishani.

      b Ingawa huenda kunywa kileo kukasaidia kutuliza uchungu wa kufiwa na mpendwa, hicho ni kitulizo cha muda tu. Kileo hakiwezi kukusaidia kukabiliana na huzuni, na unaweza kuwa mraibu.

      c Kwa kuwa kila mtu huomboleza kwa njia tofauti, marafiki na watu wa familia hawapaswi kumfanyia uamuzi yule aliyefiwa.—Wagalatia 6:2, 5.

      d Kuhusu hali ya wafu na ahadi ya Mungu ya ufufuo, ona sura ya 6 na 7 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

      [Blabu katika ukurasa wa 8]

      “Hata nilipohisi huzuni nyingi sana, nilichukua Biblia na kuisoma, hata kama ni mstari mmoja tu”—Lauren

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 7]

      KUSHUGHULIKA KWA NJIA INAYOFAA NA HISIA ZA HATIA

      Labda unahisi kwamba uzembe fulani upande wako ulichangia kifo cha mpendwa wako. Kutambua kwamba hisia za hatia—halisi au za kuwaziwa—ni jambo la kawaida kwa mtu anayehuzunika kunaweza kusaidia. Usihisi kwamba hupaswi kuonyesha hisia hizo. Kuzungumza kuhusu hisia zako za hatia kunaweza kukusaidia sana kupunguza huzuni.

      Hata hivyo, tambua kwamba hata kama unapenda sana mtu mwingine, huwezi kudhibiti maisha yake, wala huwezi kuzuia “wakati na tukio lisilotazamiwa” lisiwapate wale unaowapenda. (Mhubiri 9:11) Isitoshe, hukuwa na nia mbaya. Kwa mfano, ulipokosa kumpeleka mpendwa wako kumwona daktari mapema zaidi, je, ulikusudia kwamba awe mgonjwa na kufa? Bila shaka sivyo! Basi, je, kweli una hatia ya kusababisha kifo chake? La.

      Mama mmoja alijifunza jinsi ya kushughulika na hisia za hatia baada ya binti yake kufa katika aksidenti ya gari. Anaeleza hivi: “Nilihisi nina hatia kwa sababu nilimtuma. Lakini nikaja kutambua kwamba ulikuwa upuuzi kuhisi hivyo. Hakukuwa na kosa kumtuma aende na baba yake kufanya shughuli fulani. Ilikuwa tu aksidenti mbaya sana.”

      Huenda ukasema, ‘Lakini kuna mambo mengi sana ambayo ninatamani ningalikuwa nimemwambia au kumfanyia.’ Ni kweli, lakini ni nani kati yetu anayeweza kusema kwamba amekuwa baba, mama, au mtoto mkamilifu? Biblia inatukumbusha hivi: “Sisi sote hujikwaa mara nyingi. Ikiwa yeyote hajikwai katika neno, huyo ni mtu mkamilifu.” (Yakobo 3:2; Waroma 5:12) Kwa hiyo kubali uhakika wa kwamba wewe si mkamilifu. Kuendelea kufikiri-fikiri ati “laiti tu ningalifanya hivi au vile” hakutabadili chochote, lakini huenda kukuzuie kupona upesi.e

      [Maelezo ya Chini]

      e Habari iliyo katika sanduku hili inapatikana katika broshua Mtu Fulani Umpendaye Anapokufa, iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

      [Picha katika ukurasa wa 6]

      Nyakati nyingine, lazima mzazi anayeomboleza amfariji mtoto wake anayeomboleza pia ambaye ni mtu mzima

      [Picha katika ukurasa wa 9]

      Kuandika kwenye kitabu, kutazama picha, na kukubali msaada wa wengine ni baadhi ya njia za kukabiliana na kifo cha mpendwa

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki