-
Ni Kawaida Kuhuzunika Ninavyohuzunika?Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 1
-
-
“Mama alipokufa, nilichanganyikiwa sana. Yeye ndiye aliyeunganisha familia yetu.”—Karyn.
KUFIWA na mzazi ni mojawapo ya mambo yenye kuumiza sana yanayoweza kukupata. Baadaye, huenda ukawa na hisia mbalimbali ambazo hujawahi kuwa nazo wakati mwingine. Brian, aliyekuwa na umri wa miaka 13 baba yake alipokufa kutokana na mshutuko wa moyo, asema: “Usiku tuliopata habari, tulilia na kukumbatiana tu.” Natalie, aliyekuwa na umri wa miaka kumi baba yake alipokufa kutokana na kansa, akumbuka: “Sikujua la kufanya. Sikuwa na hisia zozote. Ni kana kwamba nilikuwa nimekufa ganzi.”
Kifo humwathiri kila mtu kwa njia tofauti. Biblia husema kwamba “kila mmoja” ana “pigo lake na maumivu yake mwenyewe.” (2 Mambo ya Nyakati 6:29) Ukiwa na hilo akilini, hebu fikiria jinsi ambavyo kifo cha mzazi wako kimekuathiri wewe. Andika hapa chini (1) jinsi ulivyohisi ulipopata habari kwamba mzazi wako amekufa na (2) jinsi unavyohisi sasa.a
1 ․․․․․
1 ․․․․․
Huenda majibu yako yanaonyesha kwamba hisia zako zinapungua kwa kadiri fulani. Hilo ni kawaida. Haimaanishi kwamba umemsahau mzazi wako. Ama, huenda bado hisia zako hazijabadilika au labda hata zimezidi. Huenda huzuni yako huja kama mawimbi, yanayopanda na kushuka. Hilo pia ni kawaida—hata ikiwa miaka kadhaa imepita tangu mzazi afe. Swali ni, Unaweza kukabiliana na huzuni jinsi gani?
Usijizuie kulia! Kulia husaidia kupunguza uchungu unaoletwa na huzuni. Hata hivyo, huenda ukahisi kama Alicia. Alikuwa na umri wa miaka 19 mama yake alipokufa. Alicia anasema, “Nilihisi kwamba nikionyesha hisia nyingi, wengine watafikiri sina imani.” Lakini fikiria hili: Yesu Kristo alikuwa mwanadamu mkamilifu aliyekuwa na imani yenye nguvu katika Mungu. Hata hivyo, ‘alitokwa na machozi’ alipowaona wale waliokuwa wakihuzunika juu ya kifo cha rafiki yake mpendwa Lazaro. (Yohana 11:35) Kwa hiyo, usiogope kulia. Haimaanishi kwamba huna imani! Alicia anasema: “Mwishowe, nililia. Tena sana. Kila siku.”b
Kabiliana na hisia za hatia. “Kila usiku nilikuwa nikimbusu mama yangu kabla ya kwenda kulala,” anasema Karyn, aliyekuwa na umri wa miaka 13 mama yake alipokufa. “Kuna siku ambayo sikufanya hivyo. Asubuhi iliyofuata, Mama alikuwa amekufa. Najua sipaswi kuwa na hisia za hatia, lakini nahisi nina hatia kwa kuwa sikumwona usiku huo wa mwisho na pia kwa sababu ya mambo yaliyotokea asubuhi iliyofuata. Baba yangu alikuwa ameenda safari ya kikazi na aliniomba mimi na dada yangu tumtunze Mama. Lakini tuliamka tukiwa tumechelewa. Nilipoingia chumbani mwake, Mama hakuwa akipumua. Nilihisi vibaya sana, kwa sababu alikuwa sawa Baba alipoondoka!”
Kama Karyn, huenda kwa kiasi fulani unahisi kwamba una hatia kwa sababu ya mambo ambayo ulipuuza kufanya. Huenda hata ukajitesa kwa kusema, “laiti.” ‘Laiti ningemhimiza Baba atafute ushauri wa daktari.’ ‘Laiti ningeenda kumwona Mama mapema.’ Ikiwa unasumbuliwa na mawazo kama hayo, kumbuka hili: Ni jambo la kawaida kujuta kwamba laiti ungefanya mambo kwa njia tofauti. Ukweli wa mambo ni kwamba ungefanya mambo kwa njia tofauti ikiwa ungejua mambo ambayo yangetokea. Lakini hukujua. Hivyo basi, hupaswi kujilemea na hisia za hatia. Hukusababisha kifo cha mzazi wako!c
-
-
Ni Kawaida Kuhuzunika Ninavyohuzunika?Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 1
-
-
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 113]
CHANTELLE
“Baba yangu alikuwa mgonjwa kwa miaka mitano hivi, na afya yake ilikuwa ikizidi kuzorota. Nilikuwa na umri wa miaka 16 alipojiua. Baadaye mama yangu alinieleza mimi na kakangu mambo yote yaliyokuwa yakiendelea. Hata alituruhusu tusaidie kufanya maamuzi kuhusu mipango ya mazishi. Hilo liliturahisishia mambo. Nafikiri kwamba watoto hawapendi kufichwa mambo yanayoendelea, hasa mambo makubwa kama haya. Kadiri muda ulivyopita ndivyo ilivyokuwa rahisi zaidi kwangu kuzungumza waziwazi kuhusu kifo cha baba yangu. Wakati wowote nilipohisi nataka kulia, ningeenda mahali fulani au kwa rafiki na kulia. Pendekezo langu ni hili: Ikiwa unahitaji kuzungumza kuhusu jambo hilo, zungumza na watu wa familia au marafiki. Unapokuwa na huzuni, usiizuilie.”
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 113, 114]
LEAH
“Mama alipatwa na kiharusi nilipokuwa na umri wa miaka 19, na miaka mitatu baadaye akafa. Baada ya kifo chake, nilihisi kwamba nahitaji kuwa na nguvu. Baba angelemewa hata zaidi ikiwa mimi pia ningelemewa na hisia. Nilipokuwa nikikua, Mama alikuwa nami sikuzote nilipokuwa mgonjwa au nilipokuwa sijisikii vizuri. Nakumbuka jinsi alivyokuwa akinigusa ili kuona ikiwa nina homa. Ninaumia sana ninapokumbuka kwamba hayupo. Mimi hujaribu kuficha hisia zangu, ijapokuwa najua haifai. Hivyo, nyakati nyingine mimi hutazama picha ili niweze kulia. Kuzungumza na marafiki husaidia pia. Biblia inaahidi kwamba wale ambao wamekufa watafufuliwa na waishi katika dunia itakayokuwa paradiso. (Yohana 5:28, 29) Ninapokazia fikira tumaini la kumwona mama yangu tena—na ninapokazia fikira kile ninachohitaji kufanya ili niwepo—huzuni yangu hupungua.”
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 114]
BETHANY
“Laiti ningeweza kukumbuka nikimwambia baba yangu ‘ninakupenda.’ Nina hakika nilimwambia, lakini sikumbuki, na ningependa kujua hivyo. Nilikuwa na umri wa miaka mitano tu baba yangu alipokufa. Baba yangu alipatwa na kiharusi akiwa usingizini, akakimbizwa hospitalini. Asubuhi, nikaambiwa kwamba amekufa. Baadaye ilikuwa vigumu sana kwangu kuzungumza kuhusu baba yangu, lakini nilifurahi niliposikia watu wakizungumza kumhusu kwa sababu hilo lilinisaidia kumjua vizuri. Ningemshauri yeyote ambaye amefiwa na mzazi wake akumbuke kwa furaha kila pindi waliyokuwa pamoja na mzazi wake na kuandika mambo waliyofanya pamoja ili asiyasahau. Kisha, afanye awezayo kujenga imani yake ili awepo wakati mzazi wake atakapofufuliwa katika ulimwengu mpya wa Mungu.”
-