-
Unaweza Kupata Furaha ya Kweli!Amkeni!—2006 | Aprili
-
-
Karibu miaka elfu mbili iliyopita, Yesu Kristo alifundisha njia ya maisha ambayo huburudisha na kupunguza mfadhaiko. Ukweli aliofundisha ulikuwa rahisi lakini wenye nguvu. Alisema hivi: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.” (Mathayo 5:3) Naam, Yesu aliwatia moyo wasikilizaji wake wakazie fikira uhitaji mkubwa zaidi wa wanadamu, yaani, kweli ya kiroho kuhusu Muumba wetu na kusudi Lake kutuelekea.
Kama tutakavyoona katika makala zinazofuata, kweli hiyo inaweza kutusaidia kutambua mambo muhimu zaidi, na hivyo kufanya tuwe na maisha yenye furaha na yenye kusudi. Pia ukweli huo wa kiroho hutupa tumaini zuri ajabu.
-
-
Siri ya Kupata Furaha ya KweliAmkeni!—2006 | Aprili
-
-
Siri ya Kupata Furaha ya Kweli
ILI kupika chakula kitamu, kunahitajika maelezo mazuri ya upishi na vilevile mpishi bora! Kwa njia fulani, furaha inahitaji mambo kama hayo. Haitokezwi na jambo moja tu bali na mchanganyiko wa mambo mengi maishani. Mambo hayo yanatia ndani kazi, kucheza, kuwa pamoja na watu wa familia na marafiki, na utendaji wa kiroho. Lakini pia kuna mambo mengine yasiyoonekana waziwazi kama vile, mtazamo, tamaa, na miradi katika maisha.
Tunaweza kushukuru kwamba hatuhitaji kutafuta siri ya kupata furaha ya kweli pasipo msaada. Kwa nini? Kwa sababu Muumba wetu ametupa kitabu kizuri sana cha maagizo, yaani, Biblia, ambayo sasa inapatikana ikiwa nzima au sehemu katika lugha na lahaja 2,377. Hakuna kitabu kingine ulimwenguni kinachopatikana katika lugha nyingi hivyo!
Idadi ya Biblia na lugha ambazo imetafsiriwa inaonyesha jinsi Mungu anavyohangaikia furaha na hali nzuri ya kiroho ya watu wote. (Matendo 10:34, 35; 17:26, 27) Mungu anasema: ‘Mimi, ndiye ninayekufundisha ili ujifaidi mwenyewe.’ Tukitii amri zake, anatuahidi utulivu na amani “kama mto.”—Isaya 48:17, 18.
Ahadi hiyo inatukumbusha maneno haya ya Yesu ambayo yalinukuliwa katika makala iliyotangulia: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.” (Mathayo 5:3) Hali ya kiroho inayotajwa hapa si kujionyesha kijuu-juu tu kuwa mtakatifu. Badala yake, inaathiri maisha yetu kwa ujumla. Inaonyesha utayari wetu wa kusikiliza na kufundishwa na Mungu, kwa sababu tunatambua kwamba anatujua vizuri zaidi kuliko jinsi tunavyojijua. Errol, ambaye amekuwa mwanafunzi wa Biblia kwa zaidi ya miaka 50 anasema: “Jambo linalonisadikisha kabisa kwamba Biblia imetoka kwa Mungu ni kwamba unapofuata mafundisho yake, yanafanya kazi!”
-