Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Unaweza Kupata Furaha ya Kweli!
    Amkeni!—2006 | Aprili
    • Unaweza Kupata Furaha ya Kweli!

      WATU wengi ulimwenguni pote wanaamini kwamba ili mtu awe na furaha anahitaji gari zuri, akaunti nono ya benki, kazi nzuri, nyumba kubwa, na vifaa vya kisasa vya elektroniki, pamoja na sura au umbo zuri. Lakini, je, furaha inategemea kuwa na vitu hivyo vya kimwili?

      Ripoti moja ya pekee katika gazeti Time inasema kwamba “utafiti mwingi sana umefanywa kuhusu furaha, kutazamia mema, na sifa zinazochangia maadili mema, afya nzuri ya kimwili na kiakili.” Wengi wameshangazwa na matokeo ya utafiti huo. Uthibitisho unaonyesha kwamba watu wanaofikiri kwamba watakuwa wenye furaha kwa kuwa na pesa, umashuhuri, au urembo wanajidanganya wenyewe. Kwa kweli, wanategemeza maisha yao juu ya mambo ambayo huenda yakadhuru afya yao ya kiakili na hata kufanya washuke moyo.

      Watu wengi nchini Marekani ni matajiri zaidi kuliko wakati mwingine wowote. “Lakini hilo halijafanya tuwe wenye furaha zaidi,” linasema gazeti Time. Hali iko hivyo katika nchi nyingine. Licha ya ukuzi wa haraka wa kiuchumi nchini China, kumekuwa na watu wengi zaidi wasio na furaha. Gazeti Access Asia linalochapishwa mara nne kwa mwaka linasema kwamba nchini humo, kujiua kumekuwa “kisababishi kikubwa zaidi cha vifo kati ya watu wenye umri wa miaka 15 na 34.” Sababu moja inayochangia jambo hilo ni mikazo ambayo vijana wanakabili wanapojaribu kupata mafanikio katika mazingira ya kazi yenye ushindani mwingi.

      Ni wazi kwamba kuwa na mali hakupunguzi mahangaiko na mfadhaiko; badala yake kunaongeza mambo hayo. Uchunguzi mmoja wa chuo kikuu unaonyesha kwamba, “Mtindo wetu wa maisha sasa umekuwa chanzo kikuu cha mahangaiko ya kihisia na kiakili.” Mchanganuzi wa mambo ya kijamii Van Wishard anasema kwamba “kampuni nyingi hutumia bima ya afya kulipia hasa matibabu ya kiakili na kihisia.”

      Hata watoto wanaathiriwa na ulimwengu huu unaobadilika haraka-haraka. Sasa kuna vitabu vya watoto wenye umri wa miaka minane vinavyowashauri kuhusu “jinsi ya kutambua dalili za mfadhaiko na jinsi ya kukabiliana nao,” anasema Wishard. Na kulingana na orodha moja kuhusu kushuka moyo, katika nchi kadhaa za Magharibi, idadi ya watoto walio na mshuko-moyo inaongezeka kwa asilimia 23 kwa mwaka. Isitoshe “watoto ambao hawajaanza kwenda shule ndio wanaotumia zaidi dawa za kukabiliana na mshuko-moyo.”

      Pia woga unaongezeka, na si woga unaosababishwa tu na mahangaiko ya kiuchumi. Huku ushupavu wa kisiasa na wa kidini ukiongezeka, watu wengi wanaogopa mambo mabaya ambayo huenda yakatokea wakati ujao. Je, kuna msaada wowote?

      Karibu miaka elfu mbili iliyopita, Yesu Kristo alifundisha njia ya maisha ambayo huburudisha na kupunguza mfadhaiko. Ukweli aliofundisha ulikuwa rahisi lakini wenye nguvu. Alisema hivi: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.” (Mathayo 5:3) Naam, Yesu aliwatia moyo wasikilizaji wake wakazie fikira uhitaji mkubwa zaidi wa wanadamu, yaani, kweli ya kiroho kuhusu Muumba wetu na kusudi Lake kutuelekea.

      Kama tutakavyoona katika makala zinazofuata, kweli hiyo inaweza kutusaidia kutambua mambo muhimu zaidi, na hivyo kufanya tuwe na maisha yenye furaha na yenye kusudi. Pia ukweli huo wa kiroho hutupa tumaini zuri ajabu.

  • Siri ya Kupata Furaha ya Kweli
    Amkeni!—2006 | Aprili
    • Siri ya Kupata Furaha ya Kweli

      ILI kupika chakula kitamu, kunahitajika maelezo mazuri ya upishi na vilevile mpishi bora! Kwa njia fulani, furaha inahitaji mambo kama hayo. Haitokezwi na jambo moja tu bali na mchanganyiko wa mambo mengi maishani. Mambo hayo yanatia ndani kazi, kucheza, kuwa pamoja na watu wa familia na marafiki, na utendaji wa kiroho. Lakini pia kuna mambo mengine yasiyoonekana waziwazi kama vile, mtazamo, tamaa, na miradi katika maisha.

      Tunaweza kushukuru kwamba hatuhitaji kutafuta siri ya kupata furaha ya kweli pasipo msaada. Kwa nini? Kwa sababu Muumba wetu ametupa kitabu kizuri sana cha maagizo, yaani, Biblia, ambayo sasa inapatikana ikiwa nzima au sehemu katika lugha na lahaja 2,377. Hakuna kitabu kingine ulimwenguni kinachopatikana katika lugha nyingi hivyo!

      Idadi ya Biblia na lugha ambazo imetafsiriwa inaonyesha jinsi Mungu anavyohangaikia furaha na hali nzuri ya kiroho ya watu wote. (Matendo 10:34, 35; 17:26, 27) Mungu anasema: ‘Mimi, ndiye ninayekufundisha ili ujifaidi mwenyewe.’ Tukitii amri zake, anatuahidi utulivu na amani “kama mto.”—Isaya 48:17, 18.

      Ahadi hiyo inatukumbusha maneno haya ya Yesu ambayo yalinukuliwa katika makala iliyotangulia: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.” (Mathayo 5:3) Hali ya kiroho inayotajwa hapa si kujionyesha kijuu-juu tu kuwa mtakatifu. Badala yake, inaathiri maisha yetu kwa ujumla. Inaonyesha utayari wetu wa kusikiliza na kufundishwa na Mungu, kwa sababu tunatambua kwamba anatujua vizuri zaidi kuliko jinsi tunavyojijua. Errol, ambaye amekuwa mwanafunzi wa Biblia kwa zaidi ya miaka 50 anasema: “Jambo linalonisadikisha kabisa kwamba Biblia imetoka kwa Mungu ni kwamba unapofuata mafundisho yake, yanafanya kazi!” Kwa mfano, fikiria shauri bora la Biblia kuhusu mambo kama vile ufuatiaji wa mali na raha.

      Mwongozo wa Hekima Kuhusu Pesa

      Yesu alisema, “Hata wakati mtu ana vitu vingi uzima wake hautokani na vitu alivyo navyo.” (Luka 12:15) Naam, thamani yako, hasa machoni pa Mungu, haitegemei kiasi cha pesa ulicho nacho kwenye benki. Kwa kweli, mara nyingi kufuatia utajiri huongeza mahangaiko ambayo hupunguza furaha maishani na kumnyima mtu wakati wa kufuatia mambo muhimu zaidi.—Marko 10:25; 1 Timotheo 6:10.

      Richard Ryan, profesa wa saikolojia nchini Marekani anasema kwamba kadiri watu wanavyotafuta uradhi katika vitu vya kimwili ndivyo unavyoadimika. Mwandikaji wa Biblia Sulemani anasema hivi: “Mtu anayependa pesa hawezi kutosheka nazo kamwe, na mtu ambaye anapenda mali nyingi hapati faida yoyote kutokana nazo.” (Mhubiri 5:10, The New English Bible) Hali hiyo inaweza kulinganishwa na mwasho wa kuumwa na mbu. Kadiri unavyojikuna, ndivyo unavyowashwa zaidi, na kutokeza kidonda.

      Biblia inatutia moyo tufanye kazi kwa bidii na kufurahia matunda ya kazi yetu. (Mhubiri 3:12, 13) Kwa kufanya hivyo, tunajiheshimu zaidi, jambo ambalo ni muhimu ili kuwa na furaha. Pia tunaweza kupata raha fulani zinazofaa maishani. Hata hivyo, kufurahia mambo fulani mazuri ambayo tunaweza kupata kwa sababu tuna pesa ni tofauti na kukimbizana na utajiri maishani.

      Kuweka Raha Mahali Pake

      Kuwa na mtazamo wa kiroho maishani hutusaidia kunufaika kabisa na vitumbuizo, burudani, na raha nyingine. Yesu alikuwa na pindi zenye kufurahisha ambazo zilitia ndani kula na kunywa. (Luka 5:29; Yohana 2:1-10) Lakini si mambo hayo yaliyokuwa chanzo kikuu cha furaha maishani mwake. Badala yake, alipata furaha nyingi zaidi kwa kufuatia mambo ya kiroho, ambayo yalitia ndani kuwasaidia wengine wajifunze kumhusu Mungu na kusudi lake kwa ajili ya wanadamu.—Yohana 4:34.

      Mfalme Sulemani alijiingiza katika raha mbalimbali ili kuona kama angepata furaha. Alisema: ‘Nitajitumbukiza katika starehe nijifurahishe.’ Mfalme huyo tajiri hakujiingiza katika raha kwa kiasi kidogo tu. Alijitumbukiza katika starehe! Lakini alihisije baadaye? Aliandika: “Niligundua kwamba kufanya hivyo ni bure kabisa.”—Mhubiri 2:1, Biblia Habari Njema.

      Kwa kawaida, wale wanaotanguliza raha huhisi kuwa hawatosheki. Watafiti walipolinganisha kufuatia raha na mambo kama kazi yenye kusudi, utendaji wa kiroho, na kujihusisha katika utendaji wa familia, waliona kwamba kufuatia raha kulichangia kiasi kidogo sana cha furaha maishani mwa waliochunguzwa.

      Uwe Mkarimu na Mwenye Shukrani

      Badala ya kujifikiria tu, watu wenye furaha huwa wakarimu na hupendezwa na wengine. Yesu alisema, “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35) Mbali na kuwapa wengine vitu vya kimwili, tunaweza kutoa wakati na nguvu zetu, ambazo huenda zikathaminiwa zaidi, hasa katika familia. Waume na wake wanapaswa kutumia wakati pamoja ili kuimarisha ndoa yao na kuifanya iwe yenye furaha, nao wazazi wanahitaji kutumia wakati wa kutosha pamoja na watoto wao, wakizungumza nao, kuwaonyesha upendo, na kuwafundisha. Washiriki wa familia wanapojitoa katika njia hizo, wao hufanikiwa sana na familia zao huwa zenye furaha.

      Kwa upande mwingine, wengine wanapotumia wakati au nguvu zao kwa ajili yako, je, wewe ‘hujionyesha kuwa mwenye shukrani’? (Wakolosai 3:15) Kufuata maneno hayo manne kunaweza kutokeza tofauti kubwa sana katika mahusiano yetu na wengine na kunaweza kuongeza sana shangwe yako. Mtu anapokushukuru kutoka moyoni, je, moyo wako haujawi na furaha?

      Kuonyesha shukrani pia hufanya tutambue kwa urahisi zaidi mambo mazuri ambayo watu hutufanyia. Katika jaribio lililofanywa kwa makini sana, mtafiti mmoja kwenye Chuo Kikuu cha California huko Riverside, Marekani, aliuliza watu aliowahoji wawe na mahali pa kuandika mambo waliyoshukuru kufanyiwa. Haishangazi kwamba katika muda unaozidi majuma sita, watu hao walihisi kuwa na uradhi zaidi maishani.

      Unaweza kujifunza nini kutokana na hilo? Hata hali yako iweje, fikiria baraka ambazo umepata. Kwa kweli, Biblia inakuhimiza ufanye hivyo, inaposema: ‘Shangilia sikuzote. . . . Kuhusiana na kila jambo toa shukrani.’ (1 Wathesalonike 5:16, 18) Bila shaka, ili kufanya hivyo tunahitaji kujitahidi kukumbuka mambo mazuri tunayofanyiwa. Mbona usiweke mradi wa kufanya hivyo?

      Upendo na Tumaini Ni Muhimu ili Kupata Furaha

      Imesemwa kwa usahihi kwamba wanadamu wanahitaji kuonyeshwa upendo tangu wanapozaliwa hadi kufa. Bila upendo, watu hudhoofika. Lakini upendo ni nini hasa? Ingawa siku hizi neno hilo hutumiwa kiholela, Biblia inaufafanua hivi kwa njia yenye kupendeza: “Upendo ni wenye ustahimilivu na wenye fadhili,” inasema. “Upendo hauna wivu, haujigambi, haujivuni, haujiendeshi bila adabu, hautafuti faida zake wenyewe, hauchokozeki. Hauweki hesabu ya ubaya. Haushangilii juu ya ukosefu wa uadilifu, bali hushangilia pamoja na kweli. Huhimili mambo yote, huamini mambo yote, hutumaini mambo yote, huvumilia mambo yote.”—1 Wakorintho 13:4-8.

      Upendo wa kweli hauna ubinafsi hata kidogo. Kwa sababu “hautafuti faida zake wenyewe,” unatanguliza mapendezi ya wengine. Kwa kusikitisha, upendo huo unazidi kukosekana. Kwa kweli, katika unabii wake muhimu kuhusu mwisho wa mfumo huu wa mambo, Yesu alisema kwamba ‘upendo wa walio wengi zaidi ungepoa.’—Mathayo 24:3, 12; 2 Timotheo 3:1-5.

      Hata hivyo, hali hiyo haitaendelea milele, kwa kuwa ni jambo linalomshushia Muumba heshima, kwani yeye ni upendo! (1 Yohana 4:8) Hivi karibuni, Mungu ataondoa watu wote ambao wana chuki kali au wanaoongozwa na pupa. Atahifadhi tu wale wanaojitahidi kusitawisha upendo uliofafanuliwa juu. Matokeo ni kwamba kutakuwa na amani na furaha duniani pote. Ahadi hii ya Biblia itatimizwa hakika: “Bado muda kidogo tu, na mtu mwovu hatakuwako tena; nawe hakika utapaangalia mahali pake, naye hatakuwapo. Bali wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.”—Zaburi 37:10, 11.

      Hebu wazia kila siku kukiwa na ‘furaha tele’! Haishangazi kwamba Biblia husema: “Shangilieni katika tumaini.” (Waroma 12:12) Je, ungependa kujifunza mengi zaidi kuhusu tumaini zuri ambalo Mungu anawapa wanadamu watiifu? Basi tafadhali soma makala inayofuata.

      [Blabu katika ukurasa wa 7]

      “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”—Matendo 20:35

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 5]

      Masimulizi ya Watu Waliofanikiwa—Je, Ni ya Kweli?

      Mara kwa mara tunasikia masimulizi kuhusu watu ambao walilelewa katika familia zenye matatizo lakini wakapambana na hali hizo ngumu na mwishowe wakawa matajiri kupindukia. “Nyakati nyingine masimulizi hayo hutajwa ili kuthibitisha kwamba walifanya yote waliyoweza licha ya magumu, wakafanikiwa licha ya au kwa sababu ya kuwa na malezi mabaya,” inasema ripoti moja kuhusu furaha katika kichapo San Francisco Chronicle. “Kulingana na utafiti, tatizo la ufafanuzi huo ni kwamba huenda watu hao hawakupata furaha. Walikuwa tu matajiri.”

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 6]

      Furaha Huchangia Afya Nzuri

      Kuwa na furaha huchangia afya nzuri. Ripoti moja katika gazeti Time inasema hivi: “Inaonekana kwamba furaha au kuwa na matumaini, kutazamia mema, na kuridhika hupunguza hatari ya kupatwa na ugonjwa wa moyo, ugonjwa wa mapafu, kisukari, kupanda kwa shinikizo la damu, mafua, na maambukizo ya mfumo wa kupumua.” Isitoshe, uchunguzi mmoja uliofanyiwa wagonjwa wazee nchini Uholanzi ulifunua kwamba watu walipodumisha furaha na mtazamo mzuri kwa kipindi cha miaka tisa, walipunguza hatari ya kufa kwa asilimia 50!

      Haijulikani jinsi ambavyo hali ya akili huathiri mwili. Hata hivyo, utafiti unaonyesha kwamba watu wanaotarajia mema nyakati zote huwa na kiasi kidogo cha homoni inayosababisha mfadhaiko. Homoni hiyo hupunguza nguvu za mfumo wa kinga.

  • Shangilia Katika Tumaini
    Amkeni!—2006 | Aprili
    • Shangilia Katika Tumaini

      JOE alikuwa mahututi akiugua kansa. Mke wake, Kirsten, na marafiki wachache walikuwa kando ya kitanda chake wakizungumza. Kirsten alimtazama mume wake na akaona akidondokwa na machozi. Mwanzoni, alifikiri kwamba Joe alikuwa na maumivu. Huenda Joe alikuwa akihisi maumivu, lakini machozi hayo hayakuwa ya maumivu.

      Kirsten anasema: “Wakati huo mgumu, Joe alikuwa amezungukwa na marafiki wa karibu waliokuja kumtembelea. Pia alikuwa na tumaini zuri ambalo alikuwa na uhakika kwamba litatimizwa, na alijua kwamba hakuna mtu anayeweza kumpokonya tumaini hilo. Alikiri kwamba machozi yake yalikuwa ya furaha. Joe alikufa usiku huo.”

      Ni tumaini gani hilo lililomtegemeza Joe alipokuwa akiugua? Ni ahadi ya Yehova Mungu ya uzima wa milele katika paradiso duniani tukiwa na afya kamilifu. (Zaburi 37:10, 11, 29) Andiko la Ufunuo 21:3, 4 linasema hivi: “Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu. . . Atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani [kutia ndani matatizo mengi ya leo] yamepitilia mbali.”

      Tumaini Hata kwa Wafu

      Kutimizwa kwa ahadi hiyo kunamaanisha kwamba Joe atafufuliwa. Kwa kweli, alifarijiwa na ahadi ya Yesu kwamba “wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho,” yaani, wafu ambao wako katika kumbukumbu la Mungu, watafufuliwa. (Yohana 5:28, 29) Je, unahuzunika kwa sababu umefiwa na mshiriki wa familia au rafiki? Ikiwa ndivyo, tumaini la ufufuo linaweza kukuchangamsha. Ni kweli kwamba tumaini hilo haliondoi uchungu mwingi tunaohisi tunapompoteza mpendwa wetu. Yesu ‘alitokwa na machozi’ rafiki yake Lazaro alipokufa. Lakini tumaini letu hupunguza uchungu tunaohisi.—Yohana 11:14, 34, 35; 1 Wathesalonike 4:13.

      “Joe alipokufa kutokana na kansa, nilihisi kwamba sitakuwa na furaha tena,” anasema Kirsten. “Hata sasa, miaka michache baadaye, ninatambua kwamba maisha yangu katika mfumo huu hayatakuwa sawa tena. Joe aliacha pengo ambalo haliwezi kuzibwa. Hata hivyo, ninaweza kusema kwa unyoofu kwamba sasa nina amani ya akili na uradhi tena.”

      Maneno ya Kirsten yanatukumbusha kwamba katika mfumo wa sasa hatuwezi kububujika kwa furaha kila wakati. Maisha ni kupanda na kushuka. Kuna nyakati ambazo tunapaswa kuhuzunika, ambapo haingefaa kabisa kufurahi. (Mhubiri 3:1, 4; 7:2-4) Pia, huenda baadhi yetu tunakabiliana na mshuko-moyo, ambao unaweza kusababishwa na mambo mbalimbali. Hata hivyo, ahadi za Biblia hufariji sana, na hekima ya Biblia isiyo na kifani inaweza kutusaidia tuepuke hatari ambazo hufanya tusiwe wenye furaha. Mungu anasema: “Kwa habari yake mtu anayenisikiliza, yeye atakaa salama wala hatasumbuliwa na hofu ya msiba.”—Methali 1:33.

      Naam, Yehova anapendezwa nasi kikweli. Anataka tuwe na furaha, si ya kijuu-juu tu, bali ya moyoni na, si kwa miaka michache tu, bali milele! Kwa hiyo, Mwana wake alisema maneno haya yasiyoweza kupitwa na wakati: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.” (Mathayo 5:3) Ni jambo la hekima kutenda kupatana na maneno yake.

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]

      Mambo Tisa Yanayochangia Furaha

      1. Kusitawisha uthamini kwa ajili ya mambo ya kiroho.—Mathayo 5:3.

      2. Kuridhika, na kuepuka “kupenda pesa.”—1 Timotheo 6:6-10.

      3. Kuweka raha mahali panapofaa.—2 Timotheo 3:1, 4.

      4. Kuwa mkarimu, na kujitahidi kuwafurahisha wengine.—Matendo 20:35.

      5. Kuwa mwenye shukrani, na kufikiria baraka zako.—Wakolosai 3:15.

      6. Kuwa mwenye kusamehe.—Mathayo 6:14.

      7. Kuchagua marafiki kwa hekima.—Methali 13:20.

      8. Kutunza mwili wako, na kuepuka mazoea mabaya.—2 Wakorintho 7:1.

      9. ‘Kushangilia katika tumaini’ linalotajwa katika Biblia.—Waroma 12:12.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki