-
Watumishi wa Yehova Wenye FurahaMnara wa Mlinzi—2004 | Novemba 1
-
-
Watumishi wa Yehova Wenye Furaha
“Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.”—MATHAYO 5:3.
1. Furaha ya kweli ni nini, nayo huonyesha nini?
WATU wa Yehova huthamini sana hali yao yenye furaha. Mtunga-zaburi Daudi alisema: “Wenye furaha ni watu ambao Mungu wao ni Yehova.” (Zaburi 144:15) Furaha ni kuchangamka kwa ajili ya jambo lenye kupendeza. Furaha kuu zaidi, inayogusa hisia zetu za ndani kabisa, hutokana na kule kufahamu kwamba tumekubaliwa na Yehova. (Methali 10:22) Furaha hiyo huonyesha kwamba tuna uhusiano wa karibu na Baba yetu wa mbinguni na kutambua kwamba tunafanya mapenzi yake. (Zaburi 112:1; 119:1, 2) Inapendeza kwamba Yesu alitaja sababu tisa zinazoweza kutufanya tuwe na furaha. Kuchunguza sababu za kuwa na furaha katika makala hii na ile inayofuata kutatusaidia tufahamu ni kwa kadiri gani tunaweza kuwa na furaha ikiwa tutamtumikia kwa uaminifu Yehova, yule “Mungu mwenye furaha.”—1 Timotheo 1:11.
Kutambua Uhitaji Wetu wa Kiroho
2. Ni pindi gani Yesu alizungumzia furaha, na ni yapi yaliyokuwa maneno yake ya utangulizi?
2 Mnamo mwaka wa 31 W.K., Yesu alitoa mojawapo ya hotuba maarufu zaidi kuwahi kutolewa. Inaitwa Mahubiri ya Mlimani kwa sababu Yesu aliitoa kwenye mlima ulioelekeana na Bahari ya Galilaya. Injili ya Mathayo inasema: “[Yesu] alipouona umati akapanda mlimani; na baada ya kuketi wanafunzi wake wakamjia; naye akafungua kinywa chake na kuanza kuwafundisha, akisema: ‘Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho, kwa kuwa ufalme wa mbinguni ni wao.’” Maneno ya Yesu ya utangulizi yanapotafsiriwa kihalisi, yanasema: “Wenye furaha ni wale walio maskini wa roho.” (Mathayo 5:1-3; Kingdom Interlinear) Tafsiri ya Today’s English Version inasema: “Wenye furaha ni wale wanaotambua kwamba wao ni maskini kiroho.”
3. Kuwa wanyenyekevu huchangiaje furaha yetu?
3 Katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu alisema kwamba mtu anakuwa mwenye furaha zaidi ikiwa anatambua kwamba ana uhitaji wa kiroho. Wakristo wanyenyekevu, wanaotambua kabisa hali yao yenye dhambi, humwomba Yehova msamaha kwa msingi wa dhabihu ya fidia ya Kristo. (1 Yohana 1:9) Hivyo, wao hupata amani ya akili na furaha ya kweli. “Mwenye furaha ni mtu ambaye amesamehewa maasi yake, ambaye dhambi yake imefunikwa.”—Zaburi 32:1; 119:165.
4. (a) Ni katika njia zipi tunaweza kuonyesha kwamba tunatambua uhitaji wetu wa kiroho na wa wengine? (b) Ni nini huongeza furaha yetu tunapotambua uhitaji wetu wa kiroho?
4 Kutambua uhitaji wetu wa kiroho hutuchochea tusome Biblia kila siku, tupate manufaa kamili kutokana na chakula cha kiroho kinachotolewa “kwa wakati unaofaa” na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” na tuhudhurie mikutano ya Kikristo kwa ukawaida. (Mathayo. 24:45; Zaburi 1:1, 2; 119:111; Waebrania 10:25) Upendo kwa jirani hufanya tutambue uhitaji wa kiroho wa wengine na kutuchochea tuwe wenye bidii katika kuhubiri na kufundisha habari njema ya Ufalme. (Marko 13:10; Warumi 1:14-16) Tunapata furaha kwa kuwaeleza wengine kweli za Biblia. (Matendo 20:20, 35) Furaha yetu huongezeka tunapotafakari kuhusu tumaini zuri la Ufalme na baraka ambazo Ufalme huo utaleta. Tumaini la “kundi dogo” la Wakristo watiwa-mafuta ni kupata uhai usioweza kufa huko mbinguni wakiwa sehemu ya serikali ya Ufalme ya Kristo. (Luka 12:32; 1 Wakorintho 15:50, 54) Nao “kondoo wengine” wana tumaini la kupata uzima wa milele katika paradiso duniani chini ya serikali hiyo ya Ufalme.—Yohana 10:16; Zaburi 37:11; Mathayo 25:34, 46.
Jinsi Wanaoomboleza Wanavyoweza Kuwa na Furaha
5. (a) Maneno “wale wanaoomboleza” yanamaanisha nini? (b) Watu hao wanaoomboleza hufarijiwaje?
5 Maneno yanayohusu furaha ambayo Yesu alifuatia kutaja yanaonekana kama yanajipinga. Alisema: “Wenye furaha ni wale wanaoomboleza, kwa kuwa watafarijiwa.” (Mathayo 5:4) Mtu anawezaje kuomboleza na wakati huohuo awe na furaha? Ili kuelewa maana ya maneno ya Yesu, tunahitaji kufikiria anazungumza kuhusu maombolezo ya aina gani. Mwanafunzi Yakobo anaeleza kwamba hali yetu wenyewe yenye dhambi inapaswa kutufanya tuomboleze. Aliandika: “Safisheni mikono yenu, ninyi watenda-dhambi, na takaseni mioyo yenu, ninyi wenye kusitasita. Iweni na taabu na kuomboleza na kulia. Kicheko chenu na kigeuzwe kuwa maombolezo, na shangwe yenu kuwa huzuni. Jinyenyekezeni machoni pa Yehova, naye atawainua ninyi.” (Yakobo 4:8-10) Wale wanaosikitishwa kikweli na hali yao yenye dhambi hufarijika wanapotambua kwamba wanaweza kusamehewa dhambi wakionyesha imani katika dhabihu ya fidia ya Kristo na kuonyesha toba ya kweli kwa kufanya mapenzi ya Yehova. (Yohana 3:16; 2 Wakorintho 7:9, 10) Hivyo wanaweza kuwa na uhusiano mzuri na Yehova na kuwa na tumaini la kuishi milele ili kumtumikia na kumsifu. Hiyo huwaletea furaha nyingi ya moyoni.—Waroma 4:7, 8.
6. Wengine huomboleza katika maana gani, nao hufarijiwaje?
6 Pia maneno ya Yesu yanatia ndani wale wanaoomboleza kwa sababu ya hali zenye kuchukiza zilizopo duniani. Yesu alisema kuwa maneno haya ya unabii wa Isaya 61:1, 2, yanamhusu: “Roho ya Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova iko juu yangu, kwa sababu Yehova amenitia mafuta niwatangazie wapole habari njema. Amenituma kufunga majeraha ya waliovunjika moyo, . . . kuwafariji wote wanaoomboleza.” Utume huo unawahusu pia Wakristo watiwa-mafuta walio duniani leo, ambao huutekeleza wakisaidiwa na waandamani wao, “kondoo wengine.” Wote wanashiriki katika kazi ya kutia alama kwa njia ya mfano kwenye mapaji ya nyuso za “watu wanaougua na kulia kwa sababu ya machukizo yote yanayofanywa katikati yake [Yerusalemu lililoasi, linalofananisha dini zinazojiita za Kikristo].” (Ezekieli 9:4) Watu hao wanaoomboleza hufarijiwa na “habari njema ya ufalme.” (Mathayo 24:14) Wanafurahi kujua kwamba hivi karibuni ulimwengu mpya wa Yehova wenye uadilifu utachukua mahali pa mfumo mwovu wa mambo wa Shetani.
Wenye Furaha Ni Wale Walio na Tabia-Pole
7. Neno “tabia-pole” halimaanishi nini?
7 Yesu aliendelea na Mahubiri yake ya Mlimani kwa kusema: “Wenye furaha ni wale walio na tabia-pole, kwa kuwa watairithi dunia.” (Mathayo 5:5) Nyakati nyingine tabia-pole huonwa kuwa udhaifu. Hata hivyo, sivyo ilivyo. Akieleza maana ya neno linalotafsiriwa “tabia-pole,” msomi mmoja wa Biblia aliandika hivi: “Sifa kuu ya mtu mwenye tabia-pole ni kwamba yeye hujizuia sana. Sifa hiyo haimaanishi kutojikakamua, kuongozwa na hisia tu, wala utulivu ambao hutokana na kutojiingiza katika jambo fulani. Ni nguvu zenye kuzuiwa.” Yesu alisema hivi kujihusu: “Mimi ni mwenye tabia-pole na mnyenyekevu moyoni.” (Mathayo 11:29) Hata hivyo, Yesu alikuwa jasiri katika kutetea kanuni za uadilifu.—Mathayo 21:12, 13; 23:13-33.
8. Sifa ya tabia-pole inahusianishwa kwa ukaribu na nini, na kwa nini tunahitaji sifa hiyo tunaposhughulika na wengine?
8 Kwa hiyo, tabia-pole inahusianishwa kwa ukaribu na kujizuia. Kwa kweli, mtume Paulo aliorodhesha tabia-pole pamoja na kujizuia alipotaja “matunda ya roho.” (Wagalatia 5:22, 23) Sifa ya tabia-pole inapaswa kusitawishwa kwa msaada wa roho takatifu. Ni sifa ya Kikristo ambayo huchangia amani pamoja na wasioamini kutia ndani wale walio kutanikoni. Paulo aliandika: “Jivikeni upendo mwororo wenye huruma, fadhili, unyenyekevu wa akili, upole, na ustahimilivu. Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari.”—Wakolosai 3:12, 13.
9. (a) Kwa nini kuwa mwenye tabia-pole hakuhusishi tu mahusiano yetu na wengine? (b) Watu wenye tabia-pole ‘watairithi dunia’ jinsi gani?
9 Hata hivyo, tabia-pole haihusu tu mahusiano yetu na wanadamu wengine. Sisi huonyesha kwamba tuna tabia-pole tunapojitiisha kwa hiari chini ya enzi kuu ya Yehova. Yesu Kristo ndiye kielelezo kikuu cha sifa hiyo kwa kuwa alipokuwa duniani alionyesha tabia-pole na kujitiisha kikamili kwa mapenzi ya Baba yake. (Yohana 5:19, 30) Yesu hasa anarithi dunia, kwa kuwa yeye ndiye Mtawala wa dunia aliyewekwa rasmi. (Zaburi 2:6-8; Danieli 7:13, 14) Anashiriki urithi huo akiwa na wale 144,000 walio ‘warithi pamoja naye,’ ambao wamechaguliwa “kati ya wanadamu” ili ‘watawale wakiwa wafalme juu ya dunia.’ (Waroma 8:17; Ufunuo 5:9, 10; 14:1, 3, 4; Danieli 7:27) Kristo pamoja na watawala wenzake watatawala mamilioni ya wanaume na wanawake walio mfano wa kondoo, ambao watapata utimizo wenye furaha wa unabii huu wa zaburi: “Wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.”—Zaburi 37:11; Mathayo 25:33, 34, 46.
Wenye Furaha Ni Wale Walio na Njaa kwa Ajili ya Uadilifu
10. Ni katika njia gani moja wale ‘walio na njaa na kiu kwa ajili ya uadilifu’ hutoshelezwa?
10 Sababu nyingine ya kuwa na furaha iliyotajwa na Yesu alipokuwa akizungumza kwenye mlima huo wa Galilaya ilikuwa: “Wenye furaha ni wale walio na njaa na walio na kiu kwa ajili ya uadilifu, kwa kuwa watashibishwa.” (Mathayo 5:6) Yehova ndiye huwawekea Wakristo kiwango cha uadilifu. Hivyo basi, wale walio na njaa na kiu kwa ajili ya uadilifu wana njaa na kiu ya kupata mwongozo wa Mungu. Watu hao wanatambua vizuri hali yao ya dhambi na kutokamilika, nao wanatamani kuwa na msimamo unaokubalika mbele za Yehova. Wao hufurahi kama nini wanapojifunza katika Neno la Mungu kwamba wakitubu na kutafuta msamaha kwa msingi wa dhabihu ya fidia ya Kristo, wataweza kuwa na nafasi ya kupata msimamo wenye uadilifu mbele za Mungu!—Matendo 2:38; 10:43; 13:38, 39; Waroma 5:19.
11, 12. (a) Wakristo watiwa-mafuta hupataje kuwa waadilifu? (b) Kiu ya waandamani wa watiwa-mafuta kwa ajili ya uadilifu hutoshelezwaje?
11 Yesu alisema kwamba watu hao wangekuwa na furaha kwa kuwa “watatoshelezwa.” (Mathayo 5:6, Kingdom Interlinear) Wakristo watiwa-mafuta ambao wamepewa mwito wa ‘kutawala wakiwa wafalme’ pamoja na Kristo mbinguni wanatangazwa kuwa “waadilifu kwa ajili ya uzima.” (Waroma 5:1, 9, 16-18) Yehova huwafanya kuwa wana wa kiroho. Wanakuwa warithi pamoja na Kristo, na kupewa mwito wa kuwa wafalme na makuhani katika serikali ya Ufalme wa mbinguni.—Yohana 3:3; 1 Petro 2:9.
12 Waandamani wa watiwa-mafuta bado hawajatangazwa kuwa waadilifu kwa ajili ya uzima. Hata hivyo, kupitia imani yao katika damu iliyomwagwa ya Kristo, Yehova huwahesabu kuwa waadilifu kwa kadiri fulani. (Yakobo 2:22-25; Ufunuo 7:9, 10) Wao huhesabiwa kuwa waadilifu wakiwa rafiki za Yehova nao wana taraja la kukombolewa wakati wa “dhiki kuu.” (Ufunuo 7:14) Chini ya “mbingu mpya,” kiu yao kwa ajili ya uadilifu itatoshelezwa hata zaidi wakati ambapo watakuwa sehemu ya dunia mpya ambamo “uadilifu utakaa.”—2 Petro 3:13; Zaburi 37:29.
Wenye Furaha Ni Wale Walio na Rehema
13, 14. Tunawezaje kuonyesha rehema katika njia halisi, nasi tutanufaikaje?
13 Yesu aliendelea kusema hivi katika Mahubiri yake ya Mlimani: “Wenye furaha ni wale walio na rehema, kwa kuwa wataonyeshwa rehema.” (Mathayo 5:7) Katika maana ya kisheria, rehema inaeleweka kuwa inarejelea huruma ya hakimu ambaye huepuka kumpa mkosaji adhabu kamili inayokubalika na sheria. Hata hivyo, katika Biblia, maneno ya awali yanayotafsiriwa “rehema” hurejelea hasa kuonyesha fadhili au sikitiko linalowaletea kitulizo wale walio katika hali mbaya. Hivyo, wale walio na rehema huonyesha huruma. Mfano wa Yesu kuhusu Msamaria mwenye ujirani ni kielelezo kizuri cha mtu “aliyemtendea kwa rehema” mtu mwenye uhitaji.—Luka 10:29-37.
14 Ili kupata furaha inayotokana na kuwa mwenye rehema, tunahitaji kuwafanyia mambo yenye fadhili wale wenye uhitaji. (Wagalatia 6:10) Yesu aliwahurumia watu aliowaona. ‘Aliwasikitikia, kwa sababu walikuwa kama kondoo wasio na mchungaji. Naye akaanza kuwafundisha mambo mengi.’ (Marko 6:34) Yesu alitambua kwamba uhitaji wa kiroho ndio muhimu zaidi kwa wanadamu. Sisi pia tunaweza kuonyesha huruma na rehema kwa kuwaeleza wengine kile wanachohitaji zaidi, yaani, “habari njema ya ufalme.” (Mathayo 24:14) Pia tunaweza kuwasaidia Wakristo wenzetu wenye umri mkubwa, wajane, na mayatima na ‘kusema kwa kuzifariji nafsi zilizohuzunika.’ (1 Wathesalonike 5:14; Methali 12:25; Yakobo 1:27) Hilo litatuletea furaha na pia Yehova ataturehemu.—Matendo 20:35; Yakobo 2:13.
Walio Safi Moyoni na Wanaofanya Amani
15. Tunawezaje kuwa safi moyoni na wenye kufanya amani?
15 Yesu alitaja sababu ya sita na ya saba ya kuwa na furaha kama ifuatavyo: “Wenye furaha ni wale walio safi moyoni, kwa kuwa watamwona Mungu. Wenye furaha ni wale wanaofanya amani, kwa kuwa wataitwa ‘wana wa Mungu.’” (Mathayo 5:8, 9) Moyo safi ni ule ambao umetakata kiadili na kiroho na ambao umeungana katika ujitoaji kwa Yehova. (1 Mambo ya Nyakati 28:9; Zaburi 86:11) Wale wanaofanya amani huishi kwa amani pamoja na ndugu zao Wakristo na, ikiwa wanaweza, pamoja na majirani wao. (Waroma 12:17-21) Wao ‘hutafuta amani na kuifuatilia.’—1 Petro 3:11.
16, 17. (a) Kwa nini watiwa-mafuta huitwa “wana wa Mungu,” nao ‘humwonaje Mungu’? (b) “Kondoo wengine” ‘humwonaje Mungu’? (c) “Kondoo wengine” watakuwa “wana wa Mungu” katika maana kamili lini na jinsi gani?
16 Wale wanaofanya amani ambao ni safi moyoni, wanaahidiwa kwamba “wataitwa ‘wana wa Mungu’” nao “watamwona Mungu.” Wakristo watiwa-mafuta huzaliwa kwa roho naye Yehova huwafanya kuwa “wana” wakiwa wangali duniani. (Waroma 8:14-17) Wanapofufuliwa ili wawe na Kristo mbinguni, wao hutumika mbele za Yehova na kumwona kihalisi.—1 Yohana 3:1, 2; Ufunuo 4:9-11.
17 “Kondoo wengine” wenye kufanya amani humtumikia Yehova chini ya Mchungaji Mwema, Kristo Yesu, ambaye anakuwa ‘Baba yao wa Milele.’ (Yohana 10:14, 16; Isaya 9:6) Wale watakaopita mtihani wa mwisho baada ya Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo watafanywa kuwa wana wa kidunia wa Yehova na “kuwa na uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.” (Waroma 8:21; Ufunuo 20:7, 9) Wanapongojea kwa hamu jambo hilo, wao humwita Yehova Baba yao, kwa kuwa wanajiweka wakfu kwake, na kumtambua kuwa Mpaji-Uhai wao. (Isaya 64:8) Kama vile Ayubu na Musa wa nyakati za kale, wanaweza ‘kumwona Mungu’ kwa macho ya imani. (Ayubu 42:5; Waebrania 11:27) Kupitia ‘macho ya mioyo yao’ na ujuzi sahihi kumhusu Mungu, wanaona sifa nzuri za Yehova na kujitahidi kumwiga kwa kufanya mapenzi yake.—Waefeso 1:18; Waroma 1:19, 20; 3 Yohana 11.
18. Kulingana na sababu za kwanza saba za kuwa na furaha ambazo Yesu alitaja, leo ni nani wanaopata furaha ya kweli?
18 Tumeona kwamba wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho, wale wanaoomboleza, wale walio na tabia-pole, wale walio na njaa na kiu kwa ajili ya uadilifu, wale walio na rehema, wale walio safi moyoni, na wale wanaofanya amani hupata furaha ya kweli katika kumtumikia Yehova. Hata hivyo, sikuzote wao wamepatwa na upinzani na hata wameteswa. Je, jambo hilo huvuruga furaha yao? Swali hilo litazungumziwa katika makala inayofuata.
-
-
Ni Wenye Furaha Ingawa WanateswaMnara wa Mlinzi—2004 | Novemba 1
-
-
Ni Wenye Furaha Ingawa Wanateswa
“Wenye furaha ni ninyi wakati watu wanapowashutumu na Kuwatesa na kusema kwa uwongo kila namna ya jambo baya juu yenu kwa ajili yangu.”—MATHAYO 5:11.
1. Yesu aliwapa wafuasi wake uhakikisho gani kuhusu furaha na kuteswa?
YESU alipowatuma mitume wake mara ya kwanza wakahubiri Ufalme, aliwaonya kwamba wangepingwa. Aliwaambia: “Mtachukiwa na watu wote kwa sababu ya jina langu.” (Mathayo 10:5-18, 22) Hata hivyo, mapema katika Mahubiri yake ya Mlimani, aliwahakikishia mitume wake na wengine kwamba haingekuwa lazima upinzani huo uhatarishe furaha yao ya kutoka moyoni. Kwa kweli, Yesu alihusianisha hali ya kuwa na furaha na kuteswa kwa Wakristo! Kuteswa kungewezaje kuleta furaha?
Kuteseka kwa Ajili ya Uadilifu
2. Kulingana na Yesu na mtume Petro, ni kuteseka kwa aina gani huleta furaha?
2 Sababu ya nane ya kuwa na furaha ambayo Yesu alitaja ni: “Wenye furaha ni wale ambao wameteswa kwa ajili ya uadilifu, kwa kuwa ufalme wa mbinguni ni wao.” (Mathayo 5:10) Kuteseka kwenyewe si jambo linaloleta sifa. Mtume Petro aliandika: “Kuna sifa gani katika jambo ikiwa mnapofanya dhambi na kupigwa makofi, mnavumilia? Lakini ikiwa, mnapotenda mema na kuteseka, mnavumilia, jambo hilo ni lenye kukubalika kwa Mungu.” Naye aliongeza kusema: “Hata hivyo, yeyote kati yenu asiteseke kwa sababu yeye ni muuaji au mwizi au mtenda-maovu au mwenye kujiingiza katika mambo ya watu wengine. Lakini akiteseka kwa sababu yeye ni Mkristo, asione aibu, bali na aendelee kumtukuza Mungu katika jina hili.” (1 Petro 2:20; 4:15, 16) Kulingana na maneno ya Yesu kuteseka huleta furaha tunapovumilia kwa ajili ya uadilifu.
3. (a) Kuteswa kwa ajili ya uadilifu humaanisha nini? (b) Mateso yalikuwa na matokeo gani juu ya Wakristo wa mapema?
3 Uadilifu wa kweli hukadiriwa kulingana na jinsi mtu anavyoshika amri za Mungu na kufanya mapenzi yake. Kwa hiyo, kuteseka kwa ajili ya uadilifu humaanisha kuteseka kwa sababu mtu anapinga mkazo wa kuvunja kanuni au matakwa ya Mungu. Mitume waliteswa na viongozi Wayahudi kwa sababu walikataa kuacha kuhubiri katika jina la Yesu. (Matendo 4:18-20; 5:27-29, 40) Je, hilo lilipunguza shangwe yao au kufanya waache kuhubiri? Hata kidogo! ‘Walitoka mbele ya Sanhedrini, wakishangilia kwa sababu walikuwa wamehesabiwa kuwa wenye kustahili kuvunjiwa heshima kwa ajili ya jina lake. Na kila siku katika hekalu na nyumba kwa nyumba wakaendelea bila kuacha kufundisha na kutangaza habari njema juu ya Kristo, Yesu.’ (Matendo 5:41, 42) Mateso hayo yaliwaletea shangwe na kuongeza bidii yao katika kazi ya kuhubiri. Baadaye, Wakristo wa mapema waliteswa na Waroma kwa sababu ya kukataa kumwabudu maliki.
4. Wakristo huteswa kwa sababu zipi?
4 Siku hizi Mashahidi wa Yehova wameteswa kwa sababu ya kukataa kuacha kuhubiri “habari njema ya ufalme.” (Mathayo 24:14) Mikutano yao ya Kikristo inapopigwa marufuku, wao huwa tayari kuteseka badala ya kuacha kukusanyika pamoja kama Biblia inavyoamuru. (Waebrania 10:24, 25) Wameteswa kwa sababu ya msimamo wao wa Kikristo wa kutokuwamo au kwa kukataa kutumia damu kwa njia isiyofaa. (Yohana 17:14; Matendo 15:28, 29) Hata hivyo, msimamo huo kwa ajili ya uadilifu huwaletea watu wa Mungu leo amani nyingi ya akili na furaha.—1 Petro 3:14.
Kushutumiwa kwa Ajili ya Kristo
5. Sababu ya msingi ya kuteswa kwa watu wa Yehova leo ni ipi?
5 Sababu ya tisa ya kuwa na furaha ambayo Yesu alitaja katika Mahubiri yake ya Mlimani inahusu pia suala la kuteswa. Alisema: “Wenye furaha ni ninyi wakati watu wanapowashutumu na kuwatesa na kusema kwa uwongo kila namna ya jambo baya juu yenu kwa ajili yangu.” (Mathayo 5:11) Sababu ya msingi ya kuteswa kwa watu wa Yehova ni kwamba wao si sehemu ya mfumo huu mwovu wa mambo. Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Kama mngekuwa sehemu ya ulimwengu, ulimwengu ungependa kilicho chake. Sasa kwa sababu ninyi si sehemu ya ulimwengu, bali nimewachagua ninyi kutoka ulimwenguni, kwa sababu hiyo ulimwengu unawachukia ninyi.” (Yohana 15:19) Vivyo hivyo, mtume Petro alisema: “Kwa sababu ninyi hamwendelei kukimbia pamoja nao katika mwendo huo kwenda kwenye dimbwi lilelile la chini la upotovu, wao wanashangaa na kuendelea kuwatukana ninyi.”—1 Petro 4:4.
6. (a) Kwa nini mabaki na waandamani wao hushutumiwa na kuteswa? (b) Je, shutuma hiyo hupunguza furaha yetu?
6 Tayari tumeona kwamba Wakristo wa mapema waliteswa kwa sababu walikataa kuacha kuhubiri katika jina la Yesu. Kristo aliwapa wafuasi wake kazi hii: “Mtakuwa mashahidi wangu . . . mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Matendo 1:8) Mabaki waaminifu wa ndugu za Yesu waliotiwa mafuta, wakisaidiwa na waandamani wao washikamanifu wa “umati mkubwa,” wanafanya kazi hiyo kwa bidii. (Ufunuo 7:9) Kwa hiyo, Shetani anapigana vita “na wale waliobaki wa uzao wake [uzao wa “mwanamke,” sehemu ya kimbingu ya tengenezo la Mungu], wanaoshika amri za Mungu na walio na kazi ya kutoa ushahidi kumhusu Yesu.” (Ufunuo 12:9, 17) Tukiwa Mashahidi wa Yehova, tunatoa ushahidi kumhusu Yesu, ambaye sasa ni Mfalme anayetawala wa serikali ya Ufalme, ambayo itaharibu serikali za wanadamu zinazopinga ulimwengu mpya wa Mungu wenye uadilifu. (Danieli 2:44; 2 Petro 3:13) Sisi hushutumiwa na kuteswa kwa sababu hiyo, lakini tunafurahi kuteswa kwa ajili ya jina la Kristo.—1 Petro 4:14.
7, 8. Wapinzani walisema nini kwa uwongo juu ya Wakristo wa mapema?
7 Yesu alisema kwamba wafuasi wake wanapaswa kujiona kuwa na furaha hata wakati watu ‘wanaposema kwa uwongo kila namna ya jambo baya’ juu yao kwa ajili yake. (Mathayo 5:11) Hivyo ndivyo ilivyotukia kwa Wakristo wa mapema. Mtume Paulo alipozuiliwa huko Roma, yapata mwaka wa 59-61 W.K., viongozi Wayahudi wa huko walisema hivi kuhusu Wakristo: “Kweli kwa habari ya madhehebu hii tunajua kwamba kila mahali huwa inasemwa vibaya.” (Matendo 28:22) Paulo na Sila walishutumiwa kuwa “wameipindua dunia inayokaliwa,” wakitenda ‘kwa kupingana na maagizo ya Kaisari.’—Matendo 17:6, 7.
8 Mwanahistoria K. S. Latourette alisema hivi alipoandika kuhusu Wakristo wakati wa Milki ya Roma: “Walishutumiwa kwa mambo tofauti-tofauti. Kwa sababu Wakristo walikataa kuhusika katika sherehe za kipagani waliitwa wakana-Mungu. Kwa kuwa hawakujihusisha na mambo mengi yaliyofanywa katika jamii, kama vile sherehe za kipagani, vitumbuizo vya umma . . . walidhihakiwa kuwa wenye kuwachukia wanadamu. . . . Ilisemekana kwamba wanaume kwa wanawake walikutana pamoja usiku na kwamba walifanya ngono kiholela-holela. . . . Kwa kuwa [Ukumbusho wa kifo cha Kristo] uliadhimishwa na waamini peke yao, kulikuwa na uvumi kwamba Wakristo walidhabihu kwa ukawaida watoto wachanga, wakanywa damu yao, na kula nyama yao.” Isitoshe, kwa kuwa Wakristo wa mapema walikataa kumwabudu maliki, walishutumiwa kuwa maadui wa Serikali.
9. Wakristo wa karne ya kwanza waliitikiaje shutuma za uwongo zilizotolewa juu yao, na hali ikoje leo?
9 Shutuma hizo za uwongo hazikuwazuia Wakristo wa mapema kutimiza kazi yao ya kuhubiri habari njema ya Ufalme. Mnamo mwaka wa 60-61 W.K., Paulo alisema juu ya “habari njema” ambayo ilikuwa ‘ikizaa matunda na kuongezeka katika ulimwengu’ na ambayo ilikuwa ‘imehubiriwa katika uumbaji wote ulio chini ya mbingu.’ (Wakolosai 1:5, 6, 23) Ndivyo ilivyo leo. Mashahidi wa Yehova wanashutumiwa kwa uwongo sawa na Wakristo wa karne ya kwanza. Hata hivyo, leo kazi ya kuhubiri ujumbe wa Ufalme inaendelea, nayo inawaletea furaha nyingi wale wanaoifanya.
Wanafurahi Kuteswa Kama Vile Manabii
10, 11. (a) Yesu alimaliziaje mazungumzo yake kuhusu sababu ya tisa ya kuwa na furaha, na kwa nini? (b) Kwa nini manabii waliteswa? Toa mifano.
10 Yesu alimalizia mazungumzo yake kuhusu sababu ya tisa ya kuwa na furaha kwa kusema: “Shangilieni . . . , kwa maana hivyo ndivyo walivyowatesa manabii waliokuwa kabla yenu.” (Mathayo 5:12) Manabii waliotumwa na Yehova kuwaonya Waisraeli wasio waaminifu walipokewa vibaya na mara nyingi wakateswa. (Yeremia 7:25, 26) Mtume Paulo alithibitisha jambo hilo kwa kuandika: “Nami nitasema nini zaidi? Kwa maana nitakosa wakati nikiendelea kusimulia juu ya . . . manabii wengine, ambao kupitia imani . . . walipata jaribu lao kwa dhihaka na mapigo kwa mijeledi, kwa kweli, zaidi ya hayo, kwa vifungo na magereza.”—Waebrania 11:32-38.
11 Wakati wa utawala wa Mfalme Ahabu mwovu na mke wake Yezebeli, manabii wengi wa Yehova waliuawa kwa upanga. (1 Wafalme 18:4, 13; 19:10) Nabii Yeremia alitiwa katika mikatale na baadaye akatupwa ndani ya tangi lenye matope. (Yeremia 20:1, 2; 38:6) Nabii Danieli alitupwa katika shimo la simba. (Danieli 6:16, 17) Manabii hao wote wa kabla ya Ukristo waliteswa kwa sababu walitetea ibada safi ya Yehova. Manabii wengi waliteswa na viongozi wa kidini Wayahudi. Yesu aliwaita waandishi na Mafarisayo “wana wa wale waliowaua manabii.”—Mathayo 23:31.
12. Kwa nini sisi Mashahidi wa Yehova huona kuwa ni heshima kuteswa kama vile manabii wa kale?
12 Leo, mara nyingi sisi Mashahidi wa Yehova huteswa kwa sababu ya kuhubiri kwa bidii habari njema ya Ufalme. Maadui wetu hutushutumu kwamba sisi “huwalazimisha watu wageuze imani yao,” lakini tunajua kwamba waabudu waaminifu wa Yehova waliokuwa kabla yetu walikabili shutuma kama hizo. (Yeremia 11:21; 20:8, 11) Tunaona ni heshima kuteswa kwa sababu ileile iliyofanya manabii waaminifu wa kale wateswe. Mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: “Akina ndugu, wachukueni manabii kuwa kielelezo cha kupatwa na uovu na kuonyesha subira, wale waliosema katika jina la Yehova. Tazama! Tunawatangaza kuwa wenye furaha wale ambao wamevumilia.”—Yakobo 5:10, 11.
Sababu Kuu za Kuwa na Furaha
13. (a) Kwa nini hatuvunjwi moyo na mateso? (b) Ni nini hutuwezesha kusimama imara, na hilo huthibitisha nini?
13 Badala ya kuvunjwa moyo na mateso, tunafarijika kujua kwamba tunafuata hatua za manabii, Wakristo wa mapema, na Yesu Kristo mwenyewe. (1 Petro 2:21) Tunapata uradhi mkubwa sana kutoka katika Maandiko, kama inavyoonyeshwa na maneno yafuatayo ya mtume Petro: “Wapendwa, msishangazwe juu ya moto unaowaka katikati yenu, unaowapata ninyi ili kuwa jaribu, kana kwamba jambo geni linawapata. Ikiwa mnashutumiwa kwa ajili ya jina la Kristo, ninyi ni wenye furaha, kwa sababu ile roho ya utukufu, yaani roho ya Mungu, inatulia juu yenu.” (1 Petro 4:12, 14) Tunajua kutokana na mambo ambayo yametupata kwamba tunaweza tu kusimama imara tunapopatwa na mateso kwa sababu roho ya Yehova inatulia juu yetu na kutuimarisha. Utegemezo wa roho takatifu huthibitisha kwamba Yehova anatubariki, na hilo hutuletea furaha nyingi.—Zaburi 5:12; Wafilipi 1:27-29.
14. Tuna sababu zipi za kushangilia tunapoteswa kwa ajili ya uadilifu?
14 Sababu nyingine inayofanya tuwe na furaha tunapopingwa na kuteswa kwa ajili ya uadilifu ni kwamba hilo huthibitisha tunaishi kama Wakristo wa kweli wenye ujitoaji-kimungu. Mtume Paulo aliandika: “Wote wanaotamani kuishi kwa ujitoaji-kimungu katika ushirika na Kristo Yesu watateswa pia.” (2 Timotheo 3:12) Tunafurahi sana kujua kwamba kudumisha utimilifu chini ya jaribu huandaa jibu zaidi kwa dai la Shetani kwamba viumbe wote humtumikia Yehova kwa faida za kibinafsi. (Ayubu 1:9-11; 2:3, 4) Tunashangilia kwamba tunashiriki, hata kama ni kwa kiwango kidogo, katika kutetewa kwa enzi kuu ya Yehova yenye uadilifu.—Methali 27:11.
Rukeni kwa Shangwe kwa Sababu ya Thawabu
15, 16. (a) Yesu alitupa sababu gani ya ‘kushangilia na kuruka kwa shangwe’? (b) Ni thawabu gani ambayo Wakristo watiwa-mafuta wanatarajia kupokea huko mbinguni, nao “kondoo wengine,” ambao ni waandamani wao, watathawabishwaje?
15 Yesu alitoa sababu nyingine ya kuwa na shangwe tunaposingiziwa na kuteswa kama manabii wa kale. Alipokuwa akimalizia mazungumzo yake kuhusu sababu ya tisa ya kuwa na furaha, alisema: “Shangilieni na kuruka kwa shangwe, kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa mbinguni.” (Mathayo 5:12) Mtume Paulo aliandika: “Mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo, lakini zawadi ambayo Mungu hutoa ni uzima wa milele kupitia Kristo Yesu Bwana wetu.” (Waroma 6:23) Naam, ‘thawabu hiyo kubwa’ ni uzima, nao si mshahara tunaoweza kufanyia kazi. Ni zawadi ya bure. Yesu alisema kwamba thawabu hiyo iko “mbinguni” kwa sababu inatoka kwa Yehova.
16 Watiwa-mafuta hupokea “taji la uzima,” yaani, uhai usioweza kufa huko mbinguni pamoja na Kristo. (Yakobo 1:12, 17) “Kondoo wengine,” ambao wana tumaini la kuishi duniani wanatazamia kwa hamu kupata uzima wa milele katika paradiso ya kidunia. (Yohana 10:16; Ufunuo 21:3-5) “Thawabu” hiyo si malipo kwa kazi ambayo jamii hizo mbili hufanya. Watiwa-mafuta na “kondoo wengine” hupokea thawabu yao kutokana na “fadhili nyingi zaidi zisizostahiliwa,” za Yehova, jambo lililomfanya mtume Paulo aseme: “Mungu apewe shukrani kwa ajili ya zawadi yake ya bure isiyoelezeka.”—2 Wakorintho 9:14, 15.
17. Kwa nini tunaweza kuwa na furaha tunapoteswa na “kuruka kwa shangwe” kwa njia ya mfano?
17 Mtume Paulo aliwaandikia hivi Wakristo ambao, baada ya muda mfupi, baadhi yao wangeteswa kwa ukatili na Maliki Nero: “Tufurahi tukiwa katika dhiki, kwa kuwa tunajua kwamba dhiki hutokeza uvumilivu; nao uvumilivu, hali yenye kukubaliwa; nayo hali yenye kukubaliwa, tumaini, nalo tumaini halikatishi tamaa.” Pia aliongeza: “Shangilieni katika tumaini. Vumilieni chini ya dhiki.” (Waroma 5:3-5; 12:12) Hata tumaini letu liwe la kimbingu au la kidunia, thawabu yetu ya kuwa waaminifu chini ya majaribu ni kubwa sana kuliko chochote tunachostahili kupata. Shangwe yetu kuhusu tarajio la kuishi milele ili kumtumikia na kumsifu Baba yetu mwenye upendo, Yehova, chini ya Mfalme wetu, Yesu Kristo haina kifani. Sisi ‘huruka kwa shangwe’ kwa njia ya mfano.
18. Mataifa yanatarajiwa kufanya nini mwisho ukaribiapo, naye Yehova atafanya nini?
18 Katika nchi fulani, Mashahidi wa Yehova wameteswa na bado wanateswa. Katika unabii wake kuhusu umalizio wa mfumo wa mambo, Yesu aliwaonya hivi Wakristo wa kweli: “Mtachukiwa na mataifa yote kwa sababu ya jina langu.” (Mathayo 24:9) Tunapokaribia mwisho, Shetani atafanya mataifa yaonyeshe chuki yao juu ya watu wa Yehova. (Ezekieli 38:10-12, 14-16) Hilo litadhihirisha wakati wa Yehova wa kutenda. “Hakika nitajitukuza mwenyewe na kujitakasa mwenyewe na kujijulisha mwenyewe mbele ya macho ya mataifa mengi; nao watalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova.” (Ezekieli 38:23) Hivyo, Yehova atalitakasa jina lake kuu na kuwakomboa watu wake kutoka katika mateso. Kwa hiyo, “mwenye furaha ni mtu anayeendelea kuvumilia.”—Yakobo 1:12.
19. Tunapaswa kufanya nini tunapongojea ile ‘siku kuu ya Yehova’?
19 Ile ‘siku kuu ya Yehova’ inapozidi kukaribia, acheni tushangilie kwa sababu ‘tumehesabiwa kuwa wenye kustahili kuvunjiwa heshima’ kwa ajili ya jina la Yesu. (2 Petro 3:10-13; Matendo 5:41) Kama Wakristo wa mapema, na tuendelee “bila kuacha kufundisha na kutangaza habari njema juu ya Kristo” na serikali yake ya Ufalme huku tukingojea thawabu yetu katika ulimwengu mpya wa Yehova wenye uadilifu.—Matendo 5:42; Yakobo 5:11.
-