-
Afya Bora—Je, Kuna Mwelekeo Mpya?Amkeni!—2000 | Oktoba 22
-
-
Afya Bora—Je, Kuna Mwelekeo Mpya?
Afya ni suala muhimu sana kwa watu wengi. Nyakati nyingine, ni kana kwamba kuna maoni mengi ya kibinafsi kuhusu afya kama walivyo madaktari. Badala ya kuunga mkono upande wowote, Amkeni! linajaribu kuripoti kupitia kwa mfululizo huu wa makala kuongezeka kwa yale yanayoitwa matibabu ya asili. Hatupendekezi mojawapo ya matibabu tutakayozungumzia au mengine yoyote. Matibabu mengi hayatajwi—baadhi yake yanapendwa sana, mengine huzusha ubishi. Twaamini kwamba elimu kuhusu masuala ya afya ni muhimu kwa ujumla; maamuzi kuhusu masuala ya afya ni mambo ya kibinafsi.
KILA mtu ataka kuwa na afya bora. Lakini yaweza kuwa vigumu kuwa na afya bora, kama inavyothibitishwa na watu wengi wenye matatizo ya afya. Baadhi ya watu huona kwamba kuna wagonjwa wengi zaidi leo kuliko awali.
Madaktari wengi hutumaini sana kuponya magonjwa kwa kuwaagiza wagonjwa watumie madawa yanayotengenezwa na kutangazwa hima-hima na makampuni ya madawa. Jambo la kutokeza ni kwamba mauzo ya madawa ulimwenguni pote yameongezeka sana katika miongo ya karibuni, kutoka kwa mabilioni machache ya dola kwa mwaka hadi mamia ya mabilioni ya dola kwa mwaka. Tokeo limekuwa nini?
Madawa yanayoagizwa na madaktari kwa matibabu yamewasaidia watu wengi. Hata hivyo, baadhi ya watu wanaotumia madawa wangali na afya mbaya au hata imezorota. Kwa hiyo, hivi karibuni wengine wamegeukia njia nyingine za matibabu.
Matibabu Wanayogeukia Wengi
Katika sehemu ambako tiba ya kisasa isiyo ya asili imekuwa ikitumiwa kutibu magonjwa, watu wengi sasa wanageukia yale yanayoitwa matibabu ya asili, au ya ziada. “Yaonekana ukuta ambao umekuwa ukitofautisha kwa muda mrefu matibabu ya asili na matibabu yasiyo ya asili unaporomoka,” lasema gazeti la Consumer Reports la Mei 2000.
Jarida la The Journal of the American Medical Association (JAMA), la Novemba 11, 1998, lilisema hivi: “Matibabu ya asili, ambayo huonwa kuwa vizuizi vya magonjwa visivyofunzwa sana katika vyuo vya tiba wala kupatikana kwa ukawaida katika hospitali za Marekani, yamevutia vyombo vya habari nchini, wataalamu wa tiba, mashirika ya kiserikali, na umma.”
Hata hivyo, jarida la Journal of Managed Care Pharmacy lilieleza hivi mnamo mwaka wa 1997 kuhusu mwelekeo huo wa kisasa: “Hapo zamani madaktari wa matibabu yasiyo ya asili walikuwa wakishuku matibabu ya asili, lakini sasa shule 27 za tiba huko Marekani [ripoti ya karibuni zaidi yasema 75] zinaandaa mtalaa wa hiari wa matibabu ya asili, kutia ndani Chuo Kikuu cha Harvard, Chuo Kikuu cha Stanford, Chuo Kikuu cha Arizona, na Chuo Kikuu cha Yale.”
Jarida la JAMA lilitaja mambo ambayo wagonjwa wengi wanafanya ili kuboresha afya yao. Liliripoti hivi: “Mnamo mwaka wa 1990, takriban mtu 1 (asilimia 19.9) kati ya watu 5 waliopata ushauri wa daktari wa kitiba kuhusiana na ugonjwa fulani walitumia pia matibabu ya asili. Asilimia hiyo iliongezeka kufikia mtu 1 (asilimia 31.8) kati ya 3 mwaka wa 1997.” Makala hiyo ilisema hivi pia: “Uchunguzi wa kitaifa uliofanywa sehemu nyinginezo mbali na Marekani unadokeza kwamba matibabu ya asili yanapendwa sana katika nchi zote zilizositawi kiviwanda.”
Kwa mujibu wa JAMA, idadi ya watu waliotumia matibabu ya asili katika kipindi cha miezi 12 ya karibuni ilikuwa asilimia 15 nchini Kanada, asilimia 33 nchini Finland, na asilimia 49 nchini Australia. “Uhitaji wa matibabu ya asili umeongezeka sana,” lakiri JAMA. Hilo ni kweli hasa uzingatiapo uhakika wa kwamba ni nadra sana kampuni za bima kulipia gharama kwa matibabu ya aina hiyo. Makala hiyo ya jarida la JAMA ilimalizia kwa kusema: “Ikiwa malipo ya bima kwa matibabu ya asili yataongezeka wakati ujao, basi matumizi ya sasa huenda yasitoe picha kamili ya hali ya wakati ujao kuhusu idadi ya watu wanaopendelea matibabu hayo.”
Mwelekeo wa kuchanganya matibabu ya asili na yale yasiyo ya asili umekuwa desturi ya muda mrefu katika nchi nyingi. Dakt. Peter Fisher, wa Royal London Homeopathic Hospital, alisema kwamba matibabu maarufu ya asili yamekuwa “kama matibabu yasiyo ya asili katika sehemu nyingi. Sasa hakuna tena aina mbili za matibabu, ya asili na yale yasiyo ya asili,” akadai. “Kuna matibabu yanayofaa na yale yasiyofaa peke yake.”
Kwa hiyo, wataalamu wengi wa tiba leo wanatambua umuhimu wa matibabu yasiyo ya asili na yale ya asili. Badala ya kusisitiza kwamba mgonjwa atumie aina moja tu ya matibabu au nyingine, wanapendekeza kutumia njia yoyote ya matibabu kati ya njia zote zilizopo leo ambayo inaweza kumponya mgonjwa.
Ni nini baadhi ya njia za matibabu za yale yanayoitwa matibabu ya asili, au ya ziada? Baadhi ya matibabu hayo yalianzia wapi na lini? Na kwa nini watu wengi sana wanayatumia?
-
-
Matibabu ya Asili—Kinachowafanya Wengi WayatumieAmkeni!—2000 | Oktoba 22
-
-
Matibabu ya Asili—Kinachowafanya Wengi Wayatumie
MATIBABU ya asili, au ya ziada, huwa na mbinu chungu nzima za matibabu. Mengi huitwa kwa ujumla naturopathy (matibabu ya asili), hiyo ni njia ya matibabu inayotegemea sana vitu vya asili au mbinu nyingine za kuuweka mwili katika hali fulani na kuuruhusu upone pasipo dawa. Idadi kubwa ya matibabu hayo, ambayo yametumiwa sana kwa karne nyingi, sasa yameachwa au kupuuzwa katika matibabu ya kisasa.
Mathalani, jarida la Journal of the American Medical Association la Agosti 27, 1960, lilisema kwamba zoea la kutuliza majeraha ya kuchomeka kwa baridi “lilitumiwa na watu wa kale lakini yaonekana limepuuzwa na madaktari na watu wa kawaida vilevile. Licha ya kwamba vichapo hurejezea na kusifu matibabu hayo mara kwa mara, kwa ujumla hayatumiwi leo. Kwa kweli, madaktari wengi husema tu ‘hayatumiwi na yeyote leo,’ ingawa hakuna mtu ajuaye sababu.”
Hata hivyo, kutuliza majeraha ya kuchomeka kwa maji baridi au kwa barafu kumeungwa mkono tena na matibabu yasiyo ya asili katika miongo ya karibuni. Jarida la The Journal of Trauma, la Septemba 1963, liliripoti hivi: “Zoea la kutumia maji baridi katika matibabu ya mapema ya majeraha ya kuchomeka limesitawi tangu kutolewa kwa ripoti za Ofeigsson na Schulman mnamo mwaka wa 1959 na 1960. Tuliwatibu wagonjwa mwaka uliopita kwa kutumia njia hiyo; matokeo ya matibabu hayo yalikuwa yenye kutia moyo.”
Kutibu kwa maji baridi ni salama kwa kadiri fulani, na bila shaka humtuliza mgonjwa. Kutibu magonjwa kwa njia mbalimbali kwa kutumia maji (Hydrotherapy), hutumiwa katika matibabu ya asili, na sasa matibabu mbalimbali ya aina hiyo yanatambuliwa pia na matibabu ya kisasa.a
Vivyo hivyo, wataalamu wa matibabu ya asili mara nyingi hutibu magonjwa kwa kutumia mimea. Hilo ni zoea ambalo limedumu kwa mamia—hata maelfu—ya miaka katika sehemu fulani duniani. Kwa mfano, huko India mitishamba imekuwa nguzo muhimu ya matibabu kwa muda mrefu. Leo, uwezo wa kuponya wa mimea fulani umetambuliwa kotekote na wataalamu wengi wa afya.
Tukio Muhimu
Miaka 100 hivi iliyopita, Richard Willstätter, ambaye alikuja kuwa mwanafunzi wa biokemia ya mimea, alichochewa na mambo yaliyompata rafikiye wa karibu aliye mchanga, Sepp Schwab mwenye umri wa miaka kumi. Mguu wa Sepp ulikuwa umeambukizwa vibaya sana hivi kwamba daktari alisema mguu huo ulihitaji kukatwa ili kuokoa uhai wake, lakini wazazi wa Sepp waliahirisha shughuli hiyo hadi asubuhi iliyofuata. Wakati huohuo, walimfikia mchungaji mmoja aliyekuwa tabibu hodari wa madawa ya mitishamba. Mchungaji huyo alikusanya mimea mbalimbali, akaikatakata vipande vidogo sana hadi iliposhabihi mchicha uliopikwa, kisha akaitia penye jeraha.
Jeraha lilipata nafuu kabla ya alasiri, na shughuli ya kumkata mguu ikaahirishwa tena. Aliendelea kupata matibabu hayo, na baada ya muda, jeraha hilo likapona kabisa. Willstätter aliendelea kujifunza kemia katika Chuo Kikuu cha Munich huko Ujerumani, na baadaye akashinda tuzo ya Nobeli kwa sababu ya uvumbuzi aliofanya kuhusiana na rangi ya asili ya mimea, hususan klorofili. Jambo muhimu ni kwamba asilimia 25 ya madawa ya tiba yanayotumika sasa yametengenezwa kikamili au kwa sehemu kutokana na kemikali zinazopatikana kiasili katika mimea.
Uhitaji wa Kuwa na Usawaziko
Lakini yapasa kukumbukwa kwamba matibabu yanayomsaidia kabisa mtu mmoja huenda yasimsaidie sana mwingine. Kufaulu kwa matibabu yoyote hutegemea mambo mengi, kutia ndani aina ya ugonjwa na afya ya ujumla ya mgonjwa. Hata wakati waweza kuathiri matokeo.
Matibabu ya asili kwa ujumla hufanya kazi polepole kuliko matibabu yasiyo ya asili, kwa hiyo ugonjwa ambao huenda ungekomeshwa endapo ungegunduliwa na kutibiwa mapema waweza kukomaa na kuhitaji madawa yenye nguvu—labda hata upasuaji ufanywe—ili kuokoa uhai. Kwa hiyo huenda lisiwe jambo la hekima kushikilia tu aina moja ya matibabu kana kwamba hiyo pekee ndiyo inayoweza kuponya ugonjwa fulani.
Matibabu ya asili hutofautiana na matibabu yasiyo ya asili katika masuala ya afya. Kwa kawaida mbinu zake za kuponya hulenga kuzuia ugonjwa, nazo hukazia mtindo wa maisha na mazingira ya mtu na mambo hayo yanavyoathiri afya yake. Yaani, wataalamu wa matibabu ya asili kwa ujumla humchunguza mtu kikamili badala tu ya kiungo kinachougua au hali ya ugonjwa.
Bila shaka, wengi huvutiwa sana na matibabu ya asili kwa sababu ya dhana ya kwamba matumizi yake ya bidhaa za kiasili na mbinu zake za matibabu hutuliza, nazo si hatari sana kama zile zinazotumiwa katika matibabu yasiyo ya asili. Hivyo basi, kwa sababu ya watu wengi kutaka kujua matibabu yaliyo salama na yenye matokeo, makala ifuatayo itazungumzia mifano michache ya matibabu ya asili.
[Maelezo ya Chini]
a Ona Amkeni!, Juni 22, 1988, ukurasa wa 25-26, (la Kiingereza).
-
-
Kuchunguza Matibabu ya AsiliAmkeni!—2000 | Oktoba 22
-
-
Kuchunguza Matibabu ya Asili
“Kuanzisha mjadala wa kitaaluma kati ya matabibu wa matibabu yasiyo ya asili na wale wa matibabu ya asili ni muhimu sana katika kuboresha tiba ya wagonjwa wanaochagua matibabu ya asili.”
TAARIFA hiyo ilichapishwa katika jarida la The Journal of the American Medical Association (JAMA) katika toleo lake la Novemba 11, 1998. Makala hiyo ilisema hivi: “Uhitaji [wa mjadala] watarajiwa kuongezeka kadiri matibabu ya asili yanavyoongezeka, hasa makampuni ya bima ya afya yanapotoa malipo ya bima kwa matibabu hayo.”
Wagonjwa wengi zaidi wanatumia matibabu ya asili pamoja na matibabu mengine yasiyo ya asili. Lakini, wagonjwa wengine hawamfahamishi daktari wao. Kwa hiyo, gazeti la Tufts University Health & Nutrition Letter la Aprili 2000 lilisihi hivi: “Wapaswa kuhangaikia hali njema yako kwa kushirikiana na daktari wako badala ya kujifanyia mambo.” Liliongezea kusema: “Iwe atakubali uchaguzi wako au la, yaelekea utanufaika kwa kumpasha habari hiyo.”
Habari hiyo ilisemwa kwa sababu ya hatari za kiafya zinazoweza kuzuka unapochanganya mitishamba fulani na madawa yasiyo ya asili. Wataalamu wengi wa afya hujitahidi sana kutoruhusu maoni yao binafsi kuhusu utunzaji wa afya yawazuie kushirikiana na wataalamu wa matibabu ya asili kwa manufaa ya mgonjwa, kwa sababu wanang’amua kwamba baadhi ya wagonjwa wao wanachagua matibabu hayo.
Tutazungumzia kifupi baadhi ya matibabu ya asili kusudi tuwafahamishe wasomaji wetu kuhusu matibabu hayo ambayo sasa yanatumiwa na watu wengi zaidi katika nchi nyingi. Hata hivyo, tafadhali kumbuka kwamba Amkeni! halipendekezi yoyote ya matibabu hayo wala matibabu mengine yoyote.
Matibabu ya Mitishamba
Yaelekea kwamba matibabu haya ndiyo yanayopendwa sana kati ya matibabu yote ya asili. Licha ya kwamba mitishamba imetumiwa kwa matibabu kwa karne nyingi, ni mimea michache sana ambayo imechunguzwa kwa uangalifu na wanasayansi. Ni mimea michache sana na bidhaa zake ambazo zimechunguzwa sana hivi kwamba usalama na uwezo wake wa kuponya umethibitishwa. Habari zilizo nyingi kuhusu mitishamba hutegemea matokeo ya matumizi ya kale.
Lakini katika miaka ya majuzi, kumekuwako na uchunguzi kadhaa wa kisayansi unaoonyesha umuhimu wa mitishamba fulani katika kutibu matatizo kama vile mshuko-moyo wa kiasi, kupoteza kumbukumbu kwa sababu ya uzee, na dalili za uvimbe hafifu wa tezi-kibofu. Mtishamba mmoja uliochunguzwa ni black cohosh, ambao nyakati nyingine huitwa black snakeroot, bugbane, au rattleroot. Wahindi Wekundu walichemsha mizizi yake na kuitumia kuhusiana na matatizo ya hedhi na uzazi. Kwa mujibu wa gazeti la Harvard Women’s Health Watch la Aprili 2000, uchunguzi wa hivi karibuni unadokeza kwamba bidhaa ya black cohosh ya Ujerumani ambayo inauzwa madukani inaweza “kutuliza dalili za koma-hedhi.”
Yaonekana kwamba uhitaji mkubwa wa matibabu hayo ya kiasili hutegemea dhana ya kwamba ni salama kuliko madawa ya kemikali. Ijapokuwa hilo laweza kuwa kweli mara nyingi, mitishamba fulani ina athari mbaya, hasa inapotumiwa pamoja na madawa mengine. Kwa mfano, mtishamba unaojulikana sana ambao unasifiwa kuwa tiba ya kiasili ya mvilio wa damu na ya kupunguza uzito wa mwili unaweza kuzidisha shinikizo la damu na mpigo wa moyo.
Pia kuna mitishamba ambayo humfanya mgonjwa avuje damu nyingi zaidi. Endapo mitishamba hiyo itatumiwa pamoja na madawa ya kitiba ya “kuifanya damu iwe nyepesi,” basi hali hatari yaweza kuzuka. Watu wenye magonjwa ya kudumu, kama vile ugonjwa wa sukari au shinikizo la damu, au wale wanaotumia madawa mengine wapaswa kujihadhari kuhusu kutumia mitishamba.—Ona sanduku lililoonyeshwa.
Hangaiko jingine kuhusu mitishamba ni ukosefu wa uhakikishio wa usafi katika kutengeneza bidhaa hizo. Katika miaka ya karibuni kumekuwako na ripoti za bidhaa zilizochanganywa na metali nzito na vitu vingine vyenye sumu. Kwa kuongezea, bidhaa nyingine za mitishamba zimegunduliwa kuwa na vitu vichache au hata kukosa vitu vyote vilivyotajwa kwenye kibandiko chake. Mifano hiyo yakazia uhitaji wa kununua bidhaa za mitishamba, vilevile bidhaa zozote za afya, kutoka kwa vyanzo vinavyojulikana na vinavyotegemeka.
Nyongeza za Lishe
Imeripotiwa kwamba nyongeza za lishe, kama vile vitamini na madini, zimesaidia sana kuzuia na kutibu matatizo kadhaa ya afya, kutia ndani upungufu wa damu na kudhoofika kwa mifupa—na hata kuzuia kasoro fulani za kurithiwa. Vidonge vya vitamini na madini vinavyopendekezwa na serikali kwa matumizi ya kila siku vinaonwa kuwa salama zaidi na vyenye kufaa zaidi.
Kwa upande mwingine, kumeza vidonge vingi kupita kiasi ili kutibu magonjwa fulani kwaweza kuwa hatari kwa afya. Kwaweza hata kuvuruga ufyonzaji au utendaji wa virutubishi vingine na vyaweza pia kusababisha athari mbaya. Uwezekano huo, vilevile ukosefu wa uthibitisho wa kutosha kuunga mkono matumizi ya vitamini zenye nguvu sana, haupasi kupuuzwa.
Homeopathy
Matibabu ya homeopathy [matibabu ya kutumia viini vya ugonjwa wenyewe] yalibuniwa katika miaka ya 1700 yakiwa matibabu yenye kutuliza yasiyo makali, tofauti na yale yaliyopendwa nyakati hizo. Tiba ya homeopathy hutegemea kanuni ya “dawa sawa kwa ugonjwa sawa” na nadharia ya kutumia kiasi kidogo tu cha dawa. Matibabu ya homeopathy hutayarishwa kwa kupunguza kabisa nguvu za madawa yanayotumiwa kuponya—nyakati nyingine, hupunguzwa nguvu sana hata kufikia kusalia kiwango cha chini cha molekuli ya madawa hayo.
Hata hivyo, madawa ya homeopathy yalikuwa na matokeo katika kutibu matatizo kama vile pumu, mizio, na kuharisha kwa watoto wachanga kuliko madawa ya kutuliza. Madawa ya homeopathy huonwa kuwa salama sana, kwa kuwa yamepunguzwa nguvu kabisa. Makala moja iliyochapishwa katika toleo la Machi 4, 1998, la jarida la JAMA lilisema hivi: “Homeopathy yaweza kuwa matibabu muhimu na yanayofaa wagonjwa wengi wenye magonjwa ya kudumu ambayo hayawezi kupimwa kwa njia muafaka. Endapo yatumiwa kwa kiasi, matibabu ya homeopathy yanaweza kukamilisha matibabu ya kisasa yakiwa, ‘njia nyingine ya tiba.’” Lakini, huenda likawa jambo la hekima kutumia madawa mengine yasiyo ya asili ya matibabu, kunapokuwa na hali hatari ya dharura.
Matibabu ya Maungo
Kuna matibabu kadhaa ya asili ya kurekebisha maungo ya mwili. Matibabu ya maungo ni miongoni mwa matibabu ya asili yanayopendwa sana, hasa katika Marekani. Yanategemea wazo la kwamba mtu aweza kupona haraka uti wa mgongo unapolainishwa. Ndiyo sababu wataalamu wa matibabu ya maungo huwa hodari sana katika kurekebisha na kulainisha pingili za uti wa mgongo wa wagonjwa wao.
Matibabu yasiyo ya asili wakati mwingine hushindwa kutuliza maumivu ya sehemu ya chini ya mgongo. Lakini wakati mwingine, baadhi ya wagonjwa wanaopata matibabu ya maungo huridhika sana. Ni nadra sana kupata uthibitisho wa kuunga mkono matumizi ya kurekebisha maungo katika kutibu matatizo mengine mbali na maumivu.
Jambo la kutokeza ni kwamba kuna ripoti chache za athari zitokanazo na kurekebishwa maungo na tabibu mwenye uzoefu. Hata hivyo, mtu apaswa pia kukumbuka kwamba ulainishaji wa shingo huhusianishwa na hatari ya kuibuka kwa matatizo mengine makubwa sana, kama vile kiharusi na kupooza. Ili kupunguza hatari ya kuibuka kwa matatizo hayo, wataalamu fulani hupendekeza kwamba mtu apimwe kabisa ili kujua njia mahususi ya ulainishaji iliyo salama kwake.
Kukanda Mwili
Manufaa ya kukanda mwili yamejulikana kwa muda mrefu katika tamaduni karibu zote. Hata Biblia inaripoti zoea hilo. (Esta 2:12) “Mbinu za kukanda mwili hutimiza fungu muhimu katika matibabu ya kale ya Kichina na ya Kihindi,” lasema jarida la British Medical Journal (BMJ) la Novemba 6, 1999. “Kukanda mwili huko Ulaya kulianzishwa na Per Hendrik Ling mapema katika karne ya 19, alipobuni mbinu ambayo sasa inaitwa kukanda mwili kwa Sweden.”
Yasemekana kwamba kukanda mwili hulegeza misuli, huboresha mzunguko wa damu, na kuondoa kemikali zinazorundamana kwenye tishu. Sasa madaktari huagiza wagonjwa wenye matatizo kama vile maumivu ya mgongo, maumivu ya kichwa, na matatizo ya mmeng’enyo wa chakula waweze kukandwa mwili. Watu wengi wanaokandwa mwili hueleza jinsi kunavyowatuliza. Dakt. Sandra McLanahan asema kwamba “asilimia themanini ya ugonjwa inasababishwa na mkazo, na kukanda mwili hupunguza mkazo.”
“Mbinu nyingi za kukanda mwili hazina hatari kubwa ya kusababisha athari mbaya,” likaripoti jarida la BMJ. “Hali zinazoweza kukufanya uepuke kukandwa mwili kwa sehemu kubwa hutegemea maarifa ya kawaida (kwa mfano, kuepuka kusugua majeraha ya kuchomeka au kukanda kiungo chenye mshipa unaovuja damu kindani) . . . Hakuna uthibitisho wowote kwamba kukanda miili ya wagonjwa wenye kansa hueneza ugonjwa huo mwilini.”
“Kadiri ukandaji-mwili unavyozidi kupendwa, ndivyo wateja wanavyozidi kuhangaikia ujuzi wa matabibu wa kukanda mwili, na bila shaka hilo lafaa,” asema E. Houston LeBrun, aliyewahi kuwa msimamizi wa Shirika la Marekani la Tiba ya Kukanda Mwili. Jarida la BMJ lilishauri kwamba ili kuepuka tabia isiyo ya kitaaluma, “wagonjwa wapaswa kuhakikisha kwamba matabibu hao wamesajiliwa na shirika lifaalo linalotoa leseni.” Ripoti moja ya mwaka uliopita ilisema kwamba matabibu walikuwa wamepewa leseni katika majimbo 28 huko Marekani.
Matibabu ya Vitobo
Matibabu ya vitobo (Acupuncture) yameenea sana kotekote ulimwenguni. Japo “matibabu ya vitobo” yanatia ndani mbinu kadhaa mbalimbali, kwa kawaida huhusisha kutumia sindano nyembamba sana ambazo hudungwa sehemu hususa za mwili ili kutokeza hisia inayoponya. Utafiti uliofanywa katika miongo kadhaa iliyopita wadokeza kwamba matibabu ya vitobo yaweza kufanya kazi nyakati nyingine kwa kutokeza kemikali katika mishipa ya fahamu, kama vile protini za endorphin, ambazo zinaweza kutuliza maumivu na uvimbe mchungu.
Utafiti fulani wadokeza kwamba matibabu ya vitobo yaweza kutibu magonjwa kadhaa na ni salama kuliko unusukaputi. Shirika la Afya Ulimwenguni linatambua kwamba matibabu ya vitobo hutibu magonjwa 104. Na kamati iliyoteuliwa na Taasisi za Kitaifa za Afya za Marekani ilitaja uthibitisho wa kwamba matibabu ya vitobo ni tiba inayokubalika ya kutuliza maumivu ya baada ya upasuaji, maumivu ya misuli, mkakamao wa misuli wakati wa hedhi, kichefuchefu na kutapika kunakosababishwa na tiba ya kemikali au ujauzito.
Ingawa ni nadra sana kupata athari mbaya kutokana na matibabu ya vitobo, watu fulani huhisi uchungu, hufa ganzi, au huhisi mwasho. Kufisha ifaavyo viini vilivyo kwenye sindano au kutumia sindano zinazotupwa baada ya tiba kwaweza kupunguza hatari ya maambukizo. Wanatiba wengi wa vitobo hukosa ujuzi wa kitiba unaohitajiwa ili kupima ugonjwa ifaavyo au kupendekeza matibabu mengine yafaayo. Si jambo la hekima kupuuza ukosefu huo wa ujuzi wa kupima ugonjwa, hasa ikiwa unachagua matibabu ya vitobo kutuliza dalili za magonjwa ya kudumu.
Machaguo Ni Mengi Sana
Hayo ni matibabu machache tu kati ya matibabu mengi ambayo sasa hurejezewa katika sehemu nyingine kuwa matibabu ya asili. Baadhi ya matibabu hayo, pamoja na mengine ambayo hayakuzungumziwa, huenda yakaonwa kuwa matibabu yasiyo ya asili wakati ujao, kama yalivyo sasa katika sehemu nyingine za ulimwengu. Bila shaka, matibabu mengine huenda yakatokomea au hata kuchukiwa.
Jambo la kusikitisha ni kwamba maumivu na magonjwa ni mambo yanayowasumbua sana wanadamu, kama tu Biblia inavyotaarifu kwa usahihi: “Twajua kwamba viumbe vyote vinafuliza kupiga kite pamoja na kuwa katika maumivu pamoja hadi sasa.” (Waroma 8:22) Bila shaka wanadamu wanatarajiwa kutafuta kitulizo. Lakini twaweza kugeukia wapi? Tafadhali fikiria maoni fulani ambayo yanaweza kukusaidia unapochagua matibabu.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 8]
Kuchanganya Mitishamba na Madawa—KUNA HATARI ZIPI?
Mara kwa mara watu wameonywa dhidi ya kuchanganya madawa au kuyatumia pamoja na vileo. Je, kuna hatari pia kutumia mitishamba fulani pamoja na madawa ya kitiba? Zoea hilo limeenea kadiri gani?
Makala moja katika jarida la The Journal of the American Medical Association iliripoti juu ya “matumizi ya madawa ya kitiba pamoja na mitishamba.” Ilisema hivi: “Kati ya asilimia 44 ya watu wazima waliosema kwamba walitumia kwa kawaida madawa ya kitiba, takriban mtu 1 (asilimia 18.4) kati ya watu 5 alikiri kutumia angalau dawa 1 ya mitishamba, kibonge chenye vitamini nyingi, au vyote viwili.” Ni muhimu kujua hatari ziwezazo kusababishwa na zoea hilo.
Wale wanaotumia madawa fulani ya mitishamba wanapaswa kuwa na tahadhari wapatapo matibabu yanayohitaji unusukaputi. Dakt. John Neeld, msimamizi wa Shirika la Amerika la Wataalamu wa Unusukaputi alieleza hivi: “Watu fulani wameripoti kwamba mitishamba fulani inayopendwa sana, kama vile ginseng na St. John’s wort, yaweza kusababisha mabadiliko makubwa ya shinikizo la damu. Hilo laweza kuwa hatari sana wakati wa unusukaputi.”
Daktari huyo akaongezea kusema: “Mitishamba mingine kama vile ginkgo biloba, tangawizi na feverfew, yaweza kuvuruga kuganda kwa damu, na kuzusha hatari kubwa sana wakati wa tiba ya unusukaputi wa ngozi ya nje inayofunika ubongo na ya mshipa mkuu wa ufahamu katika uti wa mgongo—iwapo damu inavuja karibu na uti wa mgongo, yaweza kumfanya mgonjwa apooze. Mtishamba wa St. John’s wort waweza pia kuzidisha athari za madawa fulani ya kulevya au madawa ya unusukaputi.”
Kwa wazi, ni muhimu sana kujua hatari iwezayo kukupata unapotumia mchanganyiko wa mitishamba fulani na madawa. Wanawake wajawazito na wale wanyonyeshao wapaswa hasa kujihadhari na madhara yawezayo kuwapata watoto wao wachanga kwa sababu ya mchanganyo wa mitishamba fulani na madawa. Hivyo basi, wagonjwa wanatiwa moyo kuzungumza na madaktari wao kuhusu madawa wanayotumia, yawe ya asili au yasiyo ya asili.
[Picha katika ukurasa wa 7]
Mitishamba fulani imesaidia sana kutibu matatizo ya afya
“Black cohosh”
“Saint-John’s-wort”
[Hisani]
© Bill Johnson/Visuals Unlimited
[Picha katika ukurasa wa 7]
Ili kufaulu, wagonjwa wanapaswa kushirikiana na wataalamu wa matibabu
-
-
Matibabu UnayochaguaAmkeni!—2000 | Oktoba 22
-
-
Matibabu Unayochagua
KATIKA kitabu chake kuhusu matibabu ya asili, Dakt. Isadore Rosenfeld alikazia jambo hili: “Matibabu yoyote au kitulizo chochote kinachotolewa kwa kikundi chochote kile cha watu walio na uhakika kwamba ‘yatafanya kazi’ yaweza kuboresha hali yao katika asilimia 50 ya visa.”
Hayo yaitwa matibabu ya kutuliza akili, yaani hata kidonge cha sukari chaweza kufanya kazi mradi tu mtu anaamini hivyo. Matibabu ya kutuliza akili yaweza kuponya matatizo ya kihisia, kama vile maumivu, kichefuchefu, uchovu, kizunguzungu, wasiwasi, na mshuko wa moyo. Jambo hilo hakika lafunua nini?
Kwanza, laonyesha kwamba kuwa na uhakika kwamba matibabu yoyote yale unayopokea yatafanya kazi, mara nyingi ni muhimu sana katika kupata nafuu. Wakati huohuo, yamkini ni jambo la hekima kuchunguza iwapo matibabu yoyote yale yanalenga kiini cha tatizo wala si dalili tu. Hilo laweza kufanywa kwa kuchunguza matokeo ya matibabu hayo kwa njia muafaka, kama vile majaribio katika maabara na picha za eksirei.
Lakini, bado kuna mengi awezayo mtu kufanya anapochagua matibabu fulani.
Hatua Muhimu Unazohitaji Kuchukua
Ni jambo la hekima kufanya utafiti kabla ya kufanya uamuzi. Uliza maswali. Matokeo ni nini? Ni nini faida, hasara, gharama na muda wa matibabu? Zungumza na watu waliopokea matibabu unayozingatia. Waulize ikiwa yaliwasaidia. Hata hivyo, kumbuka kwamba uthibitisho unaotegemea maoni ya watu tu unaweza kupotosha.
Matibabu ya asili huenda yasifae ikiwa yanamfanya mtu asusie matibabu yanayojulikana kuwa na matokeo, hata kama kiwango cha matokeo cha matibabu hayo yasiyo ya asili kiko chini. Uthibitisho wa madhara yanayoweza kutokea uliandikwa kwenye ripoti moja katika gazeti la The New England Journal of Medicine. Gazeti hilo lilieleza hali ya wagonjwa wawili wachanga wenye kansa ambao walikataa matibabu yasiyo ya asili huku wakitumia madawa mengine ya asili. Mgonjwa mmoja kati yao alikufa.
Watu wenye magonjwa ya kudumu au yaliyo hatari kwa uhai wapaswa kujihadhari kwa hekima kwa sababu wanaweza kutumbukia katika mtego wa walaghai ambao wanaeneza matibabu ya hila. Jihadhari na bidhaa zozote ambazo zasemekana kutibu magonjwa mbalimbali. Mfano wa hivi karibuni ulihusu vitamini mpya ambayo ilisemwa kuwa “ilisaidia kutibu kila tatizo kuanzia kwa matatizo ya kupumua na kudhoofika hadi magonjwa hatari kwa uhai.” Uchunguzi wa “vitamini” hiyo ulifunua kwamba yalikuwa maji ya chumvi tu.
Bila shaka matibabu fulani ya asili yanaweza kusaidia kudumisha afya bora. Hata hivyo, usitarajie muujiza. Ni jambo la hekima kuzingatia mno kula mlo wenye lishe, kulala vya kutosha, kufanya mazoezi ya kutosha, na kuwa mwangalifu unapochagua matibabu.
Tamaa Hiyo Yatimizwa
Bila shaka, hakuna matibabu yoyote ya wanadamu yanayoweza kukomesha magonjwa yote na kifo. Hiyo ni kwa sababu tumerithi matatizo hayo kutoka kwa mzazi wetu wa kwanza, mtu wa kwanza, Adamu. (Ayubu 14:4; Zaburi 51:5; Waroma 5:12) Matibabu mengi—ya kila aina—huenda yakasaidia, lakini ni vitulizo tu vya muda ambavyo vinaweza kuendeleza uhai na kuufanya ufurahishe kwa muda mfupi tu. Lakini kuna tiba hakika ya tatizo la afya mbaya, na mamilioni ya watu wameipata tayari.
Tiba hiyo imeandaliwa na Muumba wetu, Yehova Mungu, yule Daktari Mkuu. Kwa kudhihirisha imani kumwelekea na kutumia kwa faida thamani ya dhabihu ya fidia ya Mwanaye, Yesu Kristo, ambayo inafunika dhambi, utaweza kufurahia afya kamilifu na uhai udumuo milele katika ulimwengu usio na magonjwa! (Mathayo 20:28) Biblia huahidi kwamba katika ulimwengu huo mpya, “hapana mwenyeji atakayesema, Mimi mgonjwa.”—Isaya 33:24.
[Blabu katika ukurasa wa 12]
Mamilioni wamepata tumaini hakika la pekee la afya kamilifu
-