-
Fundisho LililoeneaMnara wa Mlinzi—2008 | Novemba 1
-
-
Fundisho Lililoenea
“Niliota kwamba nilikuwa nikiungua katika moto wa mateso! Nilipokuwa nikiota niligutuka na kuamka nikipiga mayowe. Kwa sababu hiyo, nilijaribu sana nisitende dhambi.”—Arline.
JE, UNAAMINI kwamba watenda-dhambi watateswa katika moto wa mateso? Watu wengi wanaamini hivyo. Kwa mfano, mnamo 2005 msomi mmoja katika Chuo Kikuu cha St. Andrews huko Scotland aligundua kwamba asilimia 33 hivi ya viongozi wa kidini nchini humo waliamini kwamba moto wa mateso ni mahali ambapo watu wanaojitenga na Mungu watateseka milele kiakili. Asilimia 20 kati yao waliamini kwamba watu wanaoenda kwenye moto wa mateso watateseka kimwili.
Katika nchi nyingi, watu wengi wanaamini kuna moto wa mateso. Kwa mfano, kura ya maoni iliyofanywa nchini Marekani mnamo 2007 ilionyesha kwamba asilimia 70 hivi ya watu waliohojiwa wanaamini kuna moto wa mateso. Hata katika nchi ambazo watu wengi hawapendezwi na dini, bado wengi wanaamini kuna moto wa mateso. Kura ya maoni iliyofanywa mnamo 2004 ilionyesha kwamba nchini Kanada, asilimia 42 ya watu wanaamini kuna moto wa mateso. Na nchini Uingereza, asilimia 32 wana uhakika kwamba kuna moto wa mateso.
Viongozi wa Kidini Wanafundisha Nini?
Viongozi wengi wa kidini wameacha kufundisha kwamba moto wa mateso ni mahali ambapo watu wanateswa kimwili. Badala yake, wanaunga mkono ufafanuzi unaotolewa katika kitabu kimoja cha Kikatoliki kilichochapishwa mnamo 1994 (Catechism of the Catholic Church). “Adhabu kuu ya moto wa mateso,” kinasema kitabu hicho, “ni kutenganishwa milele na Mungu.”
Hata hivyo, fundisho la kwamba moto wa mateso ni mahali watu wanateswa kiakili au kimwili bado linaendelezwa. Watu wanaounga mkono fundisho hilo wanasema linatoka katika Biblia. R. Albert Mohler, msimamizi wa Seminari ya Theolojia ya Southern Baptist anasema: “Ni fundisho hakika la Biblia.”
Imani Yako Ni Muhimu Kadiri Gani?
Ikiwa kweli kuna moto wa mateso, unapaswa kuogopa moto huo. Hata hivyo, ikiwa fundisho hilo si la kweli, viongozi wa kidini ambao wanalifundisha wanaleta mvurugo na kuwafanya watu waogope bila sababu. Pia wanalichafua jina la Mungu.
Biblia, Neno la Mungu, linasema nini kuhusu jambo hilo? Katika habari zinazofuata tutatumia Biblia za Kikatoliki na za Kiprotestanti kujibu maswali haya matatu: (1) Ni nini kinachompata mtu anapokufa? (2) Yesu alifundisha nini kuhusu moto wa mateso? (3) Kujifunza ukweli kuhusu moto wa mateso kunaweza kuwa na matokeo gani kwako?
-
-
Ni Nini Kinachompata Mtu Anapokufa?Mnara wa Mlinzi—2008 | Novemba 1
-
-
Ni Nini Kinachompata Mtu Anapokufa?
“Nafsi zote haziwezi kufa, hata za watu waovu . . . Wanaadhibiwa kwa moto usioweza kuzimwa, na kwa kuwa hawafi, hawawezi [kukomesha] mateso hayo.”—Clement wa Alexandria, mwandishi wa karne ya pili na ya tatu W.K.
KAMA vile Clement, wale wanaounga mkono fundisho la moto wa mateso wanaamini kwamba nafsi za wanadamu haziwezi kufa. Je, Biblia inaunga mkono fundisho hilo? Chunguza jinsi Neno la Mungu linavyojibu maswali yafuatayo.
Je, mwanamume wa kwanza, Adamu, alikuwa na nafsi isiyoweza kufa? Tafsiri ya Union Version inasema hivi kuhusu kuumbwa kwa Adamu: “BWANA Mungu akamfanya mtu kwa mavumbi ya ardhi, akampulizia puani pumzi ya uhai; mtu akawa nafsi hai.” (Mwanzo 2:7) Ona kwamba andiko hilo halisemi kwamba Adamu alipewa nafsi.
Ni nini kilichompata Adamu alipofanya dhambi? Mungu hakusema atamwadhibu milele katika moto wa mateso. Badala yake, Biblia Habari Njema inaeleza hivi kuhusu adhabu ambayo Mungu alitoa: “Kwa jasho lako utajipatia chakula, mpaka utakaporudi udongoni ulimotwaliwa; maana wewe ni mavumbi, na mavumbini utarudi.” (Italiki ni zetu; Mwanzo 3:19) Maneno hayo ya Mungu hayaonyeshi kwamba sehemu yoyote ya Adamu ingeendelea kuishi baada ya kifo. Adamu alipokufa, nafsi, yaani, Adamu mwenyewe alikufa.
Je, kuna mwanadamu aliye na nafsi isiyoweza kufa? Mungu alimwambia hivi nabii Ezekieli: “Nafsi inayofanya zambi, itakufa.” (Ezekieli 18:4, Zaire Swahili Bible) Mtume Paulo aliandika hivi: “Kwa njia ya mtu mmoja [Adamu] dhambi iliingia ulimwenguni, nayo ikasababisha kifo. Hivyo kifo kimeenea katika jumuiya yote ya binadamu, kwa maana wote wametenda dhambi.” (Waroma 5:12, BHN) Ikiwa wanadamu wote wametenda dhambi, basi nafsi zote zinakufa.
Je, nafsi iliyokufa inajua au kuhisi chochote? Neno la Mungu linasema: “Walio wazima hujua kwamba watakufa; wafu hawajui neno lo lote.” (Mhubiri 9:5, Verbum Bible) Ikifafanua kinachompata mtu anapokufa, Biblia inasema: “Huurudia udongo wake, siku hiyo mawazo yake yapotea.” (Zaburi 146:4, UV) Ikiwa wafu “hawajui neno lo lote” na ‘mawazo yao yanapotea,’ wanaweza kuteseka namna gani katika moto wa mateso?
Yesu Kristo hakusema kwamba mtu aliyekufa ana fahamu, bali alilinganisha kifo na usingizi.a (Yohana 11:11-14) Hata hivyo, huenda watu fulani wakakanusha hilo na kusema kwamba Yesu alifundisha kuna moto wa mateso na kwamba watenda-dhambi watatupwa humo. Acheni tuchunguze Yesu alisema nini hasa kuhusu moto wa mateso.
[Maelezo ya Chini]
a Ili ujue zaidi kuhusu jambo hilo, ona habari yenye kichwa “Tunayojifunza Kutoka kwa Yesu—Kuhusu Tumaini la Wafu” kwenye ukurasa wa 16 na 17.
-
-
Yesu Alifundisha Nini Kuhusu Moto wa Mateso?Mnara wa Mlinzi—2008 | Novemba 1
-
-
Yesu Alifundisha Nini Kuhusu Moto wa Mateso?
“Jicho lako likikukosesha,” akasema Yesu, “ling’oe, ulitupe; ni afadhali kuingia katika ufalme wa Mungu, una chongo, kuliko kuwa na macho mawili, na kutupwa katika jehanum; ambamo humo funza wao hafi, wala moto hauzimiki.”—MARKO 9:47, 48, Union Version.
Wakati mwingine, Yesu alitaja kuhusu kipindi cha hukumu wakati ambapo angewaambia hivi waovu: “Ondokeni mbele yangu enyi mliolaaniwa! Nendeni katika moto wa milele aliotayarishiwa Ibilisi na malaika wake.” Pia alisema kwamba hao “watakwenda kwenye adhabu ya milele.”—MATHAYO 25:41, 46, Biblia Habari Njema.
MTU anaposoma maneno hayo ya Yesu kwa mara ya kwanza huenda akaona ni kana kwamba yanaunga mkono fundisho la moto wa mateso. Bila shaka, Yesu hakutaka kupinga Neno la Mungu ambalo linasema hivi waziwazi: “Wafu hawajui neno lo lote.”—Mhubiri 9:5, Verbum Bible.
Basi, Yesu alimaanisha nini aliposema mtu anatupwa “katika Jehanam”? Je, Yesu alionya kuhusu “moto wa milele” ulio halisi au wa mfano? Ni katika njia gani waovu “watakwenda kwenye adhabu ya milele”? Acheni tuchunguze maswali hayo moja baada ya lingine.
Yesu alimaanisha nini aliposema mtu anatupwa “katika jehanum”? Neno la awali la Kigiriki linalotafsiriwa “jehanum” katika Marko 9:47 ni Geʹen·na. Neno la Kiebrania Geh Hin·nomʹ, linamaanisha “Bonde la Hinomu.” Bonde la Hinomu lilikuwa nje tu ya kuta za Yerusalemu la kale. Katika siku za wafalme Waisraeli, lilitumiwa kuwadhabihu watoto, zoea lenye kuchukiza ambalo Mungu alishutumu. Mungu alisema kwamba angewaharibu wote walioshiriki katika matendo kama hayo ya ibada ya uwongo. Wakati huo, Bonde la Hinomu lingeitwa “bonde la Machinjo,” ambapo “maiti za watu hawa” zingetapakaa bila kuzikwa. (Yeremia 7:30-34, Zaire Swahili Bible) Hivyo, Yehova alitabiri kwamba Bonde la Hinomu halingekuwa mahali pa kutesa watu walio hai, bali lingekuwa mahali pa kutupa maiti nyingi sana.
Katika siku za Yesu, wakaaji wa Yerusalemu walitupa takataka zao katika Bonde la Hinomu. Walitupa miili ya wahalifu sugu na kuhakikisha kwamba moto ulikuwa ukiwaka kila wakati ili uchome takataka na miili hiyo.
Yesu aliposema kuhusu funza wasiokufa na moto usiozimika, inaelekea alikuwa akirejelea andiko la Isaya 66:24. Kuhusu ‘mizoga ya watu waliomwasi Mungu,’ Isaya alisema kwamba “funza wao hatakufa, wala moto wao hautazimika.” (UV) Yesu na wasikilizaji wake walijua kwamba maneno hayo ya Isaya yalihusu mizoga ya watu wasiostahili kuzikwa.
Hivyo, Yesu alitumia Bonde la Hinomu, au Gehena, kuwa mfano unaofaa wa kifo kisicho na tumaini la ufufuo. Alikazia jambo hilo alipoonya kwamba Mungu ndiye “anayeweza kuharibu nafsi na mwili vilevile katika Gehena.” (Mathayo 10:28, ZSB) Gehena inawakilisha kifo cha milele, si mateso ya milele.
Je, Yesu alionya kuhusu “moto wa milele” ulio halisi au wa mfano? Ona kwamba “moto wa milele” unaotajwa na Yesu na kurekodiwa katika Mathayo 25:41 ulitayarishiwa “Ibilisi na malaika wake.” Je, unafikiri kwamba moto halisi unaweza kuwachoma viumbe wa roho? Au je, Yesu alikuwa akitumia neno “moto” kwa njia ya mfano? Kwa kweli, “kondoo” na “mbuzi” wanaotajwa katika mazungumzo hayo si halisi; ni mifano tu inayowakilisha aina mbili za watu. (Mathayo 25:32, 33) Moto wa milele ambao Yesu alitaja unateketeza kabisa waovu kwa njia ya mfano.
Ni katika njia gani waovu “watakwenda kwenye adhabu ya milele”? Ingawa tafsiri nyingi zinatumia neno “adhabu” katika Mathayo 25:46, maana ya msingi ya neno la Kigiriki koʹla·sin ni “kudhibiti ukuzi wa miti,” au kupogoa, kukata matawi yasiyohitajiwa. Kwa hiyo, watu wenye mfano wa kondoo wanapopokea uzima wa milele, watu wenye mfano wa mbuzi wasiotubu wanapatwa na “adhabu ya milele,” kukatiliwa mbali milele.
Una Maoni Gani?
Yesu hakufundisha kwamba wanadamu wana nafsi isiyoweza kufa. Hata hivyo, mara nyingi alifundisha kwamba wafu watafufuliwa. (Luka 14:13, 14; Yohana 5:25-29; 11:25) Kwa nini Yesu afundishe kwamba wafu watafufuliwa ikiwa aliamini kwamba nafsi zao hazijakufa?
Yesu hakufundisha kwamba Mungu angewatesa waovu kwa ukatili milele. Badala ya hivyo, Yesu alisema: “Maana Mungu aliupenda ulimwengu hivi hata akamtoa Mwana wake wa pekee, ili kila amwaminiye asipotee, bali awe na uhai wa milele.” (Yohana 3:16, BHN) Kwa nini Yesu alidokeza kwamba wale wasiomwamini wangekufa? Ikiwa alimaanisha kwamba wangeishi milele wakiteseka katika moto wa mateso, je, hangesema hivyo?
Fundisho la kwamba moto wa mateso ni mahali pa kuwatesa watu halitegemei Biblia. Badala yake, ni fundisho la kipagani linalodaiwa kuwa la Kikristo. (Ona sanduku “Historia Fupi ya Moto wa Mateso,” kwenye ukurasa wa 6.) La hasha, Mungu hawatesi watu milele katika moto wa mateso. Kujifunza ukweli kuhusu moto wa mateso kutakuwa na matokeo gani kwa maoni yako kumwelekea Mungu?
[Sanduku katika ukurasa wa 6]
HISTORIA FUPI YA MOTO WA MATESO
CHANZO CHA KIPAGANI: Wamisri wa kale waliamini kwamba kuna moto wa mateso. Kitabu kimoja (The Book Ȧm-Ṭuat) kinachokadiriwa kuwa cha 1375 K.W.K., kinasema kuhusu wale ambao “watatupwa kichwa chini ndani ya mashimo ya moto; na . . . hawatatoka humo, na . . . hawataweza kuepuka miale ya moto.” Mwanafalsafa Mgiriki Plutarch (karibu 46-120 W.K.) aliandika hivi kuhusu wale walio katika ulimwengu huo wa chini: “Walilia kwa sauti huku wakipatwa na mateso yenye kutisha na adhabu yenye kuaibisha na kuumiza sana.”
LAENEA KATIKA MADHEHEBU YA KIYAHUDI: Mwanahistoria Yosefo (37-karibu 100 W.K.) aliripoti kwamba madhehebu ya Kiyahudi iliyoitwa Waesene, iliamini kwamba “nafsi haziwezi kufa na zitaendelea milele.” Aliongeza hivi: “Hayo yanafanana na maoni ya Wagiriki . . . Wao wanafikiri kwamba nafsi mbaya zinafungwa ndani ya eneo lenye giza, linaloogopesha lililo na adhabu zisizokwisha.”
LAINGIZWA KATIKA “UKRISTO”: Katika karne ya pili W.K., kitabu cha kiapokrifa (Apocalypse of Peter) kilisema hivi kuhusu waovu: “Wametayarishiwa moto usioweza kuzimwa.” Pia kilisema: “Ezrael, malaika wa ghadhabu, anawaleta wanaume na wanawake huku nusu ya miili yao ikiungua na kuwatupa katika eneo la giza, moto wa mateso wa wanadamu; na roho wa ghadhabu anawaadhibu.” Wakati huohuo, mwandishi Theofilo wa Antiokia anamnukuu nabii Mgiriki wa kike Sibyl akitabiri adhabu ya waovu: “Juu yenu moto unaowaka utakuja, nanyi mtateketea kila siku daima dawamu.” Hayo ni baadhi ya maneno ambayo Theofilo anasema ni “ya kweli na yenye manufaa, ya haki, na yenye faida kwa wanadamu wote.”
LATUMIWA KUTETEA JEURI KATIKA ENZI ZA KATI: Inaripotiwa kwamba Malkia wa Uingereza Mary wa Kwanza (1553-1558), anayeitwa pia “Mary Mwuaji” kwa sababu ya kuwateketeza Waprotestanti karibu 300, alisema hivi: “Kwa kuwa baada ya hapa nafsi za wazushi zitakuwa zikiteketea milele katika moto wa mateso, hakuna jambo linalofaa zaidi kwangu kuliko kuiga kisasi cha Mungu kwa kuwateketeza duniani.”
UFAFANUZI WA KISASA: Katika miaka ya karibuni, dini fulani zimebadili msimamo wao kuhusu fundisho la moto wa mateso. Kwa mfano, mnamo 1995 Tume ya Mafundisho ya Kanisa la Anglikana ilisema hivi: “Moto wa mateso si mateso ya milele, bali ni kuchaguliwa kwa mwisho kusikoweza kubadilishwa kwa kile kinachompinga Mungu kabisa hivi kwamba mwisho wake ni kuharibiwa kabisa.”
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 7]
“ZIWA LA MOTO” NI NINI?
Ufunuo 20:10 inasema kwamba Ibilisi atatupwa ndani ya “ziwa la moto” na ‘kuteswa mchana na usiku hata milele na milele.’ (Union Version) Ikiwa Ibilisi angeteswa milele, Mungu angehitaji kumhifadhi hai, lakini Biblia inasema kwamba Yesu ‘atamharibu.’ (Waebrania 2:14, UV) Ziwa la mfano linalowaka moto linamaanisha “kifo cha pili.” (Ufunuo 21:8) Hiki si kifo kinachotajwa kwanza katika Biblia, yaani, kifo kinachosababishwa na dhambi ya Adamu, kifo ambacho mtu anaweza kufufuliwa. (1 Wakorintho 15:21, 22) Kwa kuwa Biblia haisemi kwamba “ziwa la moto” litawaachilia waliomo ndani yake, basi lazima “kifo cha pili” kiwe kinamaanisha kifo cha aina nyingine, kisicho na tumaini la ufufuo.
Ni katika njia gani wale waliomo katika “ziwa la moto” watateswa milele? Nyakati nyingine, “kutesa” kunaweza kumaanisha “kuzuia” mtu. Wakati fulani Yesu alipowakabili roho waovu, wao walipaaza sauti hivi: “Wewe umekuja hapa kututesa [kutuzuia katika abiso] mbele ya wakati?” (Mathayo 8:29; Luka 8:30, 31; Zaire Swahili Bible) Kwa hiyo, wote waliomo katika “ziwa” hilo watapata ‘mateso’ ya kuzuiwa milele, au “kifo cha pili.”
-
-
Faida za Kujifunza Ukweli Kuhusu Moto wa MatesoMnara wa Mlinzi—2008 | Novemba 1
-
-
Faida za Kujifunza Ukweli Kuhusu Moto wa Mateso
WALE ambao wanawafundisha watu kwamba moto wa mateso ni mahali ambapo watu wanateswa, wanaendeleza fundisho ambalo linamharibia Yehova Mungu sifa. Biblia inaonyesha wazi kwamba Mungu atawaharibu waovu wote. (2 Wathesalonike 1:6-9) Lakini hasira yenye uadilifu si sifa kuu ya Mungu.
Mungu si mkatili au asiye na fadhili. Hata anauliza: “Je! Mimi ninafurahia kufa kwake mtu mwovu?” (Ezekieli 18:23, Union Version) Ikiwa Mungu hafurahii kufa kwa mtu mwovu, anaweza namna gani kufurahia kuwaona waovu wakiteseka?
Sifa kuu ya Mungu ni upendo. (1 Yohana 4:8) Kwa kweli, “Mwenyezi-Mungu ni mwema kwa wote, ni mwenye huruma kwa viumbe vyake vyote.” (Zaburi 145:9, Biblia Habari Njema) Mungu anataka tumpende kutoka moyoni.—Mathayo 22:35-38.
Unachochewa na Nini—Kuogopa Moto wa Mateso au Kumpenda Mungu?
Fundisho la kwamba nafsi zinateseka katika moto wa mateso linawachochea watu wamwogope Mungu isivyofaa. Kwa kutofautisha, mtu anayejifunza ukweli kumhusu Mungu na kumpenda anamwogopa kwa njia inayofaa. “Woga wa BWANA ni mwanzo wa akili: na wote wanaofanya hivi wana akili njema,” inasema Zaburi 111:10. (Zaire Swahili Bible) Hiyo si hofu ya kupita kiasi, bali ni kumcha na kumheshimu sana Muumba. Inatufanya tuwe na woga unaofaa wa kutompendeza.
Fikiria jinsi kujifunza ukweli kuhusu moto wa mateso kulivyomsaidia Kathleen, mwenye umri wa miaka 32 ambaye hapo awali alikuwa akitumia dawa za kulevya. Maisha yake yalihusisha jeuri, kujichukia, ukosefu wa maadili, na kuhudhuria karamu. Anasema: “Ningemtazama binti yangu mwenye umri wa mwaka mmoja na kufikiri hivi, ‘Ona ninavyomtendea. Nitateketezwa kwa sababu ya kumtendea hivi.’” Kathleen alijaribu kuachana na dawa za kulevya, lakini hakufaulu. “Nilitaka kuwa mtu mzuri,” alisema, “lakini kila kitu maishani mwangu na ulimwenguni kilikuwa kibaya sana. Sikuona sababu ya kuwa mzuri.”
Kathleen alikutana na Mashahidi wa Yehova. “Nilijifunza kwamba hakukuwa na moto wa mateso. Uthibitisho wa Maandiko ulipatana na akili,” akasema Kathleen. “Nilitulizwa sana kujua kwamba singeteketezwa katika moto wa mateso.” Alijifunza pia ahadi ya Mungu kwamba wanadamu wataishi milele katika dunia iliyosafishwa uovu. (Zaburi 37:10, 11, 29; Luka 23:43) “Sasa nina tumaini halisi, tumaini la kuishi milele katika Paradiso!” akasema.
Je, Kathleen angeweza kuacha kutumia dawa za kulevya bila kuogopa moto wa mateso? Anaeleza hivi: “Nilipokuwa na hamu ya kutumia dawa za kulevya, nilisali, nikimwomba Yehova Mungu anisaidie. Nilifikiria maoni yake kuhusu mazoea kama hayo yenye kuchafua nami sikutaka kumhuzunisha. Alijibu sala zangu.” (2 Wakorintho 7:1) Kuogopa kutompendeza Mungu kulimsaidia Kathleen ashinde uraibu wake.
Naam, kumpenda na kumwogopa Mungu kwa njia inayofaa kunaweza kutuchochea kufanya mapenzi ya Mungu ili tuwe na furaha ya kudumu, bali si kuogopa moto wa mateso. Mtunga-zaburi alisema: “Heri ni kila mutu anayeogopa BWANA, anayetembea katika njia zake.”—Zaburi 128:1, ZSB.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]
NI NANI WATAKAOACHILIWA KUTOKA HADESI?
Tafsiri fulani za Biblia zinawachanganya watu kwa kutumia maneno mawili tofauti ya Kigiriki, yaani, Geʹen·na na Haiʹdes, kuwakilisha “moto wa mateso.” Katika Biblia, neno Geʹen·na linamaanisha kuharibiwa kabisa, bila tumaini la kufufuliwa. Tofauti na hilo, wale walio katika Haiʹdes, au Hadesi, wana tumaini la kufufuliwa.
Hivyo, baada ya Yesu kufa na kufufuliwa, mtume Petro aliwahakikishia wasikilizaji wake kwamba Yesu ‘hakuachwa Hadeze.’ (Matendo 2:27, 31, 32; Zaburi 16:10; Zaire Swahili Bible) Neno lililotafsiriwa “Hadeze” (hadesi) katika mstari huo ni neno la Kigiriki Haiʹdes. Yesu hakutupwa katika moto wa mateso. “Hadeze” lilikuwa kaburi. Lakini si Yesu tu anayeachiliwa na Mungu kutoka Hadesi.
Biblia inasema hivi kuhusiana na ufufuo: “Mauti na Hadeze zikatoa wafu waliokuwa ndani yao.” (Ufunuo 20:13, 14, ZSB) Kutoa watu katika “Hadeze” kutamaanisha kwamba Mungu atawarudisha hai wale anaoamua kuwa wanastahili kufufuliwa. (Yohana 5:28, 29; Matendo 24:15) Hilo ni tumaini zuri kama nini la wakati ujao, kuwaona wapendwa wetu waliokufa wakitoka kaburini! Yehova, Mungu wa upendo usio na kifani, atafanya hivyo.
-