-
Mfalme Apata Thawabu kwa Sababu ya Imani YakeUnabii wa Isaya I—Nuru kwa Wanadamu Wote
-
-
Imani Yajaribiwa
4, 5. (a) Hezekia ameonyeshaje uhuru wake kutoka kwa Ashuru? (b) Senakeribu amechukua hatua gani ya kijeshi dhidi ya Yuda, na Hezekia achukua hatua gani ili kuepuka shambulio la upesi dhidi ya Yerusalemu? (c) Hezekia afanya matayarisho gani ya kulinda Yerusalemu dhidi ya Waashuri?
4 Majaribu mazito yalikuwa mbele ya Yerusalemu. Hezekia amevunja mwungano ambao Ahazi, baba yake asiye na imani, alifanya pamoja na Waashuri. Hata amewatiisha Wafilisti, ambao ni washirika wa Ashuru. (2 Wafalme 18:7, 8) Hayo yamemkasirisha mfalme wa Ashuru. Basi twasoma: “Ikawa, katika mwaka wa kumi na nne wa kumiliki kwake mfalme Hezekia, Senakeribu, mfalme wa Ashuru, akapanda ili kupigana na miji yote ya Yuda yenye boma, akaitwaa.” (Isaya 36:1) Hezekia, labda akitumaini kulinda jiji la Yerusalemu lisishambuliwe upesi na jeshi lenye ukatili la Ashuru, akubali kumpa Senakeribu ushuru mkubwa wa talanta 300 za fedha na 30 za dhahabu.a—2 Wafalme 18:14.
5 Kwa kuwa hazina ya mfalme haina dhahabu na fedha ya kutosha kulipa ushuru huo, Hezekia atwaa vito vyovyote awezavyo kupata hekaluni. Yeye pia aing’oa milango ya hekalu, ambayo imetandwa kwa dhahabu, na kuipeleka kwa Senakeribu. Hilo lamridhisha Mwashuri, lakini kwa muda mfupi tu. (2 Wafalme 18:15, 16) Labda Hezekia atambua kuwa Waashuri hawataachana na Yerusalemu kwa muda mrefu. Kwa hiyo, sharti matayarisho yafanywe. Watu waziba chemchemi za maji ambapo Waashuri wanaovamia waweza kupata maji. Hezekia pia aimarisha ngome za Yerusalemu na kukusanya zana za vita, zikiwemo “silaha na ngao tele.”—2 Mambo ya Nyakati 32:4, 5.
6. Hezekia amtumaini nani?
6 Hata hivyo, Hezekia hatumaini mbinu za vita zenye ujanja wala katika ngome, bali amtumaini Yehova wa majeshi. Awahimiza wakuu wake wa kijeshi: “Iweni hodari, na wa moyo mkuu, msiogope, wala msifadhaike kwa sababu ya mfalme wa Ashuru, wala kwa majeshi yote walio pamoja naye; kwa maana yupo mkuu pamoja nasi kuliko aliye pamoja naye; kwake upo mkono wa mwili; ila kwetu yupo BWANA [“Yehova,” NW], Mungu wetu, kutusaidia, na kutupigania mapigano yetu.” Kwa kuitikia, watu waanza ‘kuyategemea maneno ya Hezekia, mfalme wa Yuda.’ (2 Mambo ya Nyakati 32:7, 8) Hebu piga picha ya matukio yenye kusisimua yanayofuata tuchunguzapo sura ya 36 hadi 39 ya unabii wa Isaya.
Rabshake Atoa Hoja Yake
7. Rabshake ni nani, na kwa nini atumwa Yerusalemu?
7 Senakeribu amtuma Rabshake (ni jina la cheo cha kijeshi, wala si jina la mtu binafsi) pamoja na wakuu wengine wawili kwenda Yerusalemu ili kulilazimisha jiji kusalimu amri. (2 Wafalme 18:17) Eliakimu msimamizi wa nyumba ya Hezekia, Shebna mwandishi, na Yoa mwana wa Asafu mwenye kuandika tarehe, ambao ni wawakilishi watatu wa Hezekia wawalaki watu hao nje ya ukuta wa jiji.—Isaya 36:2, 3, kielezi-chini.
8. Rabshake ajaribu kuuvunjaje upinzani wa Yerusalemu?
8 Lengo la Rabshake ni moja tu, yaani, kushawishi Yerusalemu kusalimu amri pasipo pigano. Huku akiongea katika Kiebrania, kwanza apaaza sauti: “Ni tumaini gani hili unalolitumainia? . . . Unamtumaini nani hata ukaniasi mimi?” (Isaya 36:4, 5) Kisha Rabshake awadhihaki Wayahudi waliojaa woga, akiwakumbusha kuwa wameachwa peke yao kabisa. Waweza kumwendea nani awasaidie? Je, wauendee ‘mwanzi uliopondeka,’ yaani, Misri? (Isaya 36:6) Wakati huu, Misri yafanana na mwanzi uliopondeka; kwa kweli, Ethiopia imeishinda kwa muda serikali hiyo ya ulimwengu ya awali, na Farao wa sasa wa Misri, Mfalme Tirhaka, si Mmisri bali ni Mwethiopia. Na Ashuru yakaribia kumshinda. (2 Wafalme 19:8, 9) Kwa kuwa Misri haiwezi kujiokoa, haitafaa kitu kwa Yuda.
9. Yaelekea ni nini kinachomfanya Rabshake aamue kwamba Yehova atawaacha watu Wake, lakini ukweli wa mambo ni nini?
9 Rabshake sasa abisha kwamba Yehova hatawapigania watu Wake kwa sababu wamemchukiza Yeye. Rabshake asema: “Lakini ukiniambia, Tunamtumaini BWANA [“Yehova,” “NW”], Mungu wetu, je! si yeye ambaye Hezekia ameondoa mahali pake mlimoinuka, na madhabahu zake?” (Isaya 36:7) Ni wazi kwamba Wayahudi wamemrudia, wala siyo kumkataa, Yehova hasa kwa kuondoa mahali pa juu na madhabahu nchini.
10. Kwa nini si kitu iwapo walinzi wa Yuda ni wengi au ni wachache?
10 Kisha Rabshake awakumbusha Wayahudi kwamba wao ni hoi kabisa kijeshi. Atoa mwito huu wenye dhihaka: “Nitakupa farasi elfu mbili, ikiwa wewe kwa upande wako waweza kupandisha watu juu yao.” (Isaya 36:8) Hata hivyo je, kweli ni kitu iwapo askari wapanda-farasi waliozoezwa wa Yuda ni wengi au ni wachache? La, kwa sababu wokovu wa Yuda hautegemei nguvu kubwa za kijeshi. Andiko la Mithali 21:31 laeleza mambo hivi: “Farasi huwekwa tayari kwa siku ya vita; lakini BWANA [“Yehova,” NW] ndiye aletaye wokovu.” Kisha Rabshake asema Yehova awabariki Waashuri, wala si Wayahudi. Kama sivyo, yeye adai, Waashuri wasingaliweza kamwe kupenya kadiri hiyo katika eneo la Yuda.—Isaya 36:9, 10.
11, 12. (a) Kwa nini Rabshake asisitiza kusema katika “lugha ya Kiyahudi,” naye ajaribuje kuwashawishi Wayahudi wanaosikiliza? (b) Huenda maneno ya Rabshake yakawaathirije Wayahudi?
11 Wawakilishi wa Hezekia wahangaikia athari za hoja za Rabshake juu ya watu wanaomsikia wakiwa juu ya ukuta wa jiji. Maofisa hao Wayahudi waomba hivi: “Tafadhali, sema na watumishi wako kwa lugha ya Kiashuri; maana tunaifahamu; wala usiseme nasi kwa lugha ya Kiyahudi, masikioni mwa watu wote walio ukutani.” (Isaya 36:11) Lakini Rabshake hanuii kusema katika lugha ya Kiashuri. Ataka kutia shaka na hofu katika Wayahudi ili wasalimu amri na jiji la Yerusalemu lishindwe pasipo pigano! (Isaya 36:12) Kwa hiyo, Mwashuri asema tena katika “lugha ya Kiyahudi.” Awaonya wakazi wa Yerusalemu: “Hezekia asiwadanganye, kwa maana hataweza kuwaokoa.” Baada ya kusema hayo, ajaribu kuwashawishi wale wanaomsikiliza kwa kufafanua jinsi ambavyo maisha yangekuwa kwa Wayahudi chini ya utawala wa Ashuru: “Fanyeni suluhu na mimi, mkatoke mnijie, mkale kila mtu matunda ya mzabibu wake na matunda ya mtini wake, mkanywe kila mmoja maji ya birika yake mwenyewe; hata nije nikawachukue mpaka nchi iliyo kama nchi yenu wenyewe, nchi ya nafaka na divai, nchi ya mkate na mashamba ya mizabibu.”—Isaya 36:13-17.
12 Wayahudi hawatavuna mwaka huu—uvamizi wa Ashuru umewazuia wasipande mimea. Hapana budi kwamba tazamio la kula zabibu tamu na kunywa maji safi lawavutia sana watu wanaosikiliza ukutani. Lakini Rabshake bado aendelea kujaribu kuwadhoofisha Wayahudi.
13, 14. Licha ya hoja za Rabshake, kwa nini mambo yaliyolikumba Samaria hayafai kwa hali ya Yuda?
13 Rabshake atoa silaha nyingine ya maneno kutoka katika ghala ya hoja zake. Awaonya Wayahudi wasimwamini Hezekia iwapo asema: “BWANA [“Yehova mwenyewe,” “NW”] atatuokoa.” Rabshake awakumbusha Wayahudi kuwa miungu ya Samaria haikuweza kuwazuia Waashuri wasiyashinde yale makabila kumi. Na je, vipi kuhusu miungu ya mataifa mengine ambayo Ashuru imeshinda? “Wako wapi miungu ya Hamathi na ya Arpadi?” yeye adai. “Wako wapi miungu ya Sefarvaimu? Je! wameiokoa Samaria na mkono wangu?”—Isaya 36:18-20.
14 Ni wazi kwamba Rabshake, mwabudu wa miungu isiyo ya kweli haelewi kwamba kuna tofauti kubwa kati ya Samaria lenye kuasi na Yerusalemu linalotawaliwa na Hezekia. Miungu isiyo ya kweli ya Samaria haikuwa na nguvu zozote za kuuokoa ufalme huo wa makabila kumi. (2 Wafalme 17:7, 17, 18) Kwa upande mwingine, Yerusalemu linalotawaliwa na Hezekia limeikataa miungu isiyo ya kweli nalo limerudia kumtumikia Yehova. Hata hivyo, wale wawakilishi watatu Wayudea hawajaribu kumweleza Rabshake jambo hilo. “Wakanyamaza kimya; wala hawakumjibu hata neno moja; maana ilikuwa amri ya mfalme, kwamba, Msimjibu neno.” (Isaya 36:21) Eliakimu, Shebna, na Yoa wamrudia Hezekia na kutoa ripoti rasmi ya maneno ya Rabshake.—Isaya 36:22.
Hezekia Afanya Uamuzi
15. (a) Hezekia akabili uamuzi gani sasa? (b) Yehova awapaje watu wake uhakikishio?
15 Mfalme Hezekia apaswa kufanya uamuzi sasa. Je, Yerusalemu litajisalimisha kwa Waashuri? litaungana na Misri? au litakazana na kupigana? Hezekia amebanwa sana. Aenda kwa hekalu la Yehova huku akiwatuma Eliakimu na Shebna, pamoja na wazee wa makuhani, kupata habari kwa Yehova kupitia nabii Isaya. (Isaya 37:1, 2) Huku wakiwa wamevaa nguo za magunia, wajumbe wa mfalme wamwendea Isaya, wakisema: “Siku hii ni siku ya dhiki, na aibu, na matukano . . . Yamkini BWANA, Mungu wako, atayasikia maneno ya huyo amiri ambaye mfalme wa Ashuru, bwana wake, amemtuma ili amtukane Mungu aliye hai; na BWANA, Mungu wako atayakemea maneno aliyoyasikia.” (Isaya 37:3-5) Naam, Waashuri wanashindana na Mungu aliye hai! Je, Yehova atazingatia dhihaka zao? Yehova awahakikishia Wayahudi hivi kupitia Isaya: “Usiyaogope maneno uliyoyasikia, ambayo watumishi wa mfalme wa Ashuru wamenitukana. Tazama, nitatia roho ndani yake, naye atasikia kivumi, na kurudi hata nchi yake mwenyewe, nami nitamwangusha kwa upanga katika nchi yake mwenyewe.”—Isaya 37:6, 7.
16. Senakeribu atuma barua za aina gani?
16 Wakati huohuo, Rabshake aitwa kwenda kumsaidia Senakeribu mfalme wakati huyo anapopigana vitani huko Libna. Senakeribu atalishughulikia Yerusalemu baadaye. (Isaya 37:8) Ingawa hivyo, kuondoka kwa Rabshake hakuondoi mkazo juu ya Hezekia. Senakeribu atuma barua zenye vitisho zinazoeleza mambo ambayo wakazi wa Yerusalemu waweza kutarajia iwapo wakataa kusalimu amri: “Umesikia habari ya mambo yote, ambayo wafalme wa Ashuru wamezitenda nchi zote, kwa kuziangamiza kabisa je! utaokoka wewe? Je! miungu ya mataifa, ambao baba zangu waliwaangamiza kabisa, wamewaokoa? . . . Yuko wapi mfalme wa Hamathi, na mfalme wa Arpadi na mfalme wa mji wa Sefarvaimu, wa Hena, na wa Iva?” (Isaya 37:9-13) Kwa jumla, Mwashuri amaanisha kwamba ni upumbavu kupinga—upinzani utaleta matata zaidi tu!
17, 18. (a) Hezekia ana nia gani amwombapo Yehova ulinzi? (b) Yehova amjibuje Mwashuri kupitia Isaya?
17 Akiwa anahangaikia sana matokeo ya uamuzi ambao lazima afanye, Hezekia azitandaza barua za Senakeribu mbele za Yehova hekaluni. (Isaya 37:14) Yeye amwomba Yehova kwa dhati ili asikie vitisho vya Mwashuri, akimaliza sala yake kwa maneno: “Basi sasa, BWANA, Mungu wetu, utuokoe na mkono wake, falme zote za dunia zipate kujua ya kuwa wewe ndiwe BWANA [“Mungu,” “NW”], wewe peke yako.” (Isaya 37:15-20) Ni wazi kutokana na hayo kwamba Hezekia hahangaikii hasa ukombozi wake mwenyewe, bali aibu itakayolipata jina la Yehova iwapo Ashuru itashinda Yerusalemu.
18 Yehova ajibu sala ya Hezekia kupitia Isaya. Yerusalemu halipasi kujisalimisha kwa Ashuru; lazima lisimame imara. Akizungumza kana kwamba anasema na Senakeribu, Isaya ataarifu kwa ujasiri ujumbe wa Yehova kwa Mwashuri: “Bikira, binti Sayuni, anakudharau, anakudhihaki sana; binti Yerusalemu anatikisa kichwa chake [kwa dhihaka] juu yako.” (Isaya 37:21, 22) Ni kana kwamba Yehova aongeza kusema: ‘Wewe ni nani hata umdhihaki Mtakatifu wa Israeli? Nayajua matendo yako. Una tamaa kubwa za makuu; unajisifu sana. Umezitumaini nguvu zako za kijeshi nawe umeshinda nchi nyingi. Lakini wewe waweza kushindwa. Nitabatilisha mipango yako. Nitakushinda. Ndipo nitakapokutenda wewe kama ulivyowatenda wengine. Nitatia kulabu katika pua yako na kukurudisha hadi Ashuru!’—Isaya 37:23-29.
“Kwako Wewe Dalili Ndiyo Hii”
19. Yehova ampa Hezekia dalili gani, nayo yamaanisha nini?
19 Hezekia ana uhakika gani wa kwamba unabii wa Isaya utatimia? Yehova ajibu: “Kwako wewe dalili ndiyo hii; mwaka huu mtakula vitu vimeavyo vyenyewe; na mwaka wa pili mtakula mazao ya mbegu za vitu hivyo; na mwaka wa tatu pandeni mbegu, kavuneni; mkapande mizabibu katika mashamba, mkale matunda yake.” (Isaya 37:30) Yehova atawapa chakula Wayahudi waliozuiliwa. Ijapokuwa hawawezi kupanda mbegu kwa sababu ya uvamizi wa Waashuri, watakula masazo ya mavuno ya mwaka uliotangulia. Mwaka unaofuata, ambao ni mwaka wa sabato, lazima wayaache mashamba yao yapumzike, licha ya hali yao ngumu. (Kutoka 23:11) Yehova aahidi kuwa watu wakiitii sauti yake, nafaka ya kutosha kuwalisha itamea mashambani. Kisha, mwaka unaofuata, watu watapanda mbegu kama kawaida na kupata matunda ya kazi yao.
20. Wale wanaookoka shambulizi la Ashuru ‘watatiaje mizizi chini na kuzaa matunda juu’?
20 Sasa Yehova awalinganisha watu wake na mmea usioweza kung’olewa rahisi: “Mabaki yaliyookoka . . . ya nyumba ya Yuda, yatatia mizizi chini, na kuzaa matunda juu.” (Isaya 37:31, 32) Naam, wanaomtumaini Yehova hawana cha kuhofu. Wao pamoja na wazao wao watadumu imara nchini.
21, 22. (a) Ni unabii gani unaotolewa kumhusu Senakeribu? (b) Maneno ya Yehova kuhusu Senakeribu yatimizwa lini na jinsi gani?
21 Namna gani vitisho vya Waashuri dhidi ya Yerusalemu? Yehova ajibu: “Yeye hataingia ndani ya mji huu, wala hatapiga mshale hapa, wala hatakuja mbele yake kwa ngao, wala hatajenga boma juu yake. Njia ile ile aliyoijia, kwa njia hiyo atarudi zake, wala hataingia ndani ya mji huu.” (Isaya 37:33, 34) Kwani, hapana pigano litakalotokea kati ya Ashuru na Yerusalemu. Kwa kushangaza, Waashuri, wala si Wayahudi, ndio wanaoshindwa pasipo pigano.
22 Kupatana na neno lake, Yehova atuma malaika anayewaua watu hodari katika jeshi la Senakeribu—watu 185,000. Yaonekana hayo yafanyika huko Libna, na Senakeribu mwenyewe aamka na kukuta viongozi, wakuu, na watu hodari wa jeshi lake wamekufa. Yeye arudi Ninawi akiwa na aibu, lakini licha ya kushindwa kabisa, aendelea kwa ushupavu kumwabudu Nisroki, mungu wake asiye wa kweli. Miaka kadhaa baadaye, wana wawili wa Senakeribu wamwua akiabudu katika hekalu la Nisroki. Mara nyingine tena, Nisroki asiye na uhai athibitika kuwa hana nguvu za kuokoa.—Isaya 37:35-38.
-
-
Mfalme Apata Thawabu kwa Sababu ya Imani YakeUnabii wa Isaya I—Nuru kwa Wanadamu Wote
-
-
[Picha katika ukurasa wa 383]
Mfalme Hezekia amtumaini Yehova akabilipo jeshi la Ashuru
[Picha ya ukurasa mzima katika ukurasa wa 384]
[Picha katika ukurasa wa 389]
Mfalme atuma wajumbe kwa Isaya ili kusikia shauri la Yehova
[Picha katika ukurasa wa 390]
Hezekia asali kwamba jina la Yehova litukuzwe kupitia kushindwa kwa Ashuru
[Picha katika ukurasa wa 393]
Malaika wa Yehova aua Waashuri 185,000
-