-
Ikiwa Muumba Anajali, Mbona Wanadamu Wanateseka Sana?Je, Kuna Muumba Anayekujali?
-
-
Je, Maisha ya Awali Yanasababisha Kuteseka?
Katika sehemu nyingi za ulimwengu, mamilioni ya watu huamini kwamba watu huteseka kwa sababu ya maisha yao ya awali; yaani mtu anateseka kwa sababu hiyo ni adhabu ya mambo aliyoyafanya katika maisha yaliyopita. “Tunateseka kwa sababu tumefungwa katika Karma, kwa kuwa punde tu tuzaliwapo, sisi sote hubeba mzigo mzito wa Karma iliyopita.”a Maoni hayo yalitolewa na Daisetz T. Suzuki, mwanafalsafa ambaye alieneza mafundisho ya Zen katika jamii ya Magharibi. Wenye hekima wa Kihindu walibuni “sheria ya Karma” walipokuwa wakijaribu kueleza sababu inayofanya wanadamu wateseke. Lakini, je, kweli maelezo yao juu ya kuteseka yanafaa au kuridhisha?
Mwanamke mmoja wa dini ya Buddha alisema: “Nilifikiri halikuwa sawa kulazimika kuteseka kwa ajili ya jambo fulani nililozaliwa nalo lakini ambalo silijui kamwe. Nililazimika kulikubali kuwa hatima yangu.” Yeye hakuridhika na maelezo hayo juu ya kuteseka. Huenda hata wewe umeona hivyo. Ingawa wazo la kuzaliwa upya huenda lisiwe kawaida katika eneo lenu, msingi wake ni fundisho ambalo linapatikana kila mahali katika Jumuiya ya Wakristo na kwingineko—fundisho la kwamba wanadamu wana nafsi isiyoweza kufa ambayo huendelea kuishi mwili unapokufa. “Nafsi” hiyo yasemwa kuwa imehusika katika kuteseka—ama katika maisha ya sasa au maisha ya baada ya kifo.
Mawazo kama hayo yameenea, lakini kuna uthibitisho gani wa kwamba mambo hayo ni kweli? Kwa mambo muhimu kama haya, je, si jambo la hekima kuongozwa na mambo ambayo Muumba asema? Ingawa mawazo ya wanadamu na itikadi zenye nguvu zaweza kukosea, tumeona ya kwamba taarifa za Mungu zinategemeka.
Kama tulivyoona katika sura iliyotangulia, dhambi ya wazazi wetu wa kwanza ilitokeza msiba mkuu zaidi kwa binadamu—kifo. Muumba alionya Adamu hivi: “Siku [utakapokosa kutii, au utakapofanya dhambi] utakufa hakika.” (Mwanzo 2:17; 3:19) Mungu hakusema lolote juu ya Adamu kuwa na nafsi isiyoweza kufa; yeye alikuwa binadamu. Kwa usemi wa Biblia hili lamaanisha kwamba yeye alikuwa nafsi. Basi, alipokufa, nafsi iitwayo Adamu ikafa. Baada ya kifo yeye hakuwa na ufahamu wala hakuteseka.
Muumba wetu hafundishi wala hakubaliani na fundisho la Karma, kuzaliwa upya mara nyingi, wala nafsi isiyoweza kufa ambayo baadaye inaweza kuteseka katika maisha ya baadaye. Lakini tukifahamu athari za dhambi ya Adamu, tunaweza kuelewa vizuri mbona wanadamu huteseka leo.
-
-
Ikiwa Muumba Anajali, Mbona Wanadamu Wanateseka Sana?Je, Kuna Muumba Anayekujali?
-
-
a Inasemwa kwamba Karma ni “tokeo la matendo ya mtu ya wakati uliopita yanayoathiri maisha yake mengi ya wakati ujao, au anapozaliwa upya mara nyingi katika maumbo mengine.”
-