-
Afrika Kusini2007 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Velloo Naicker alizaliwa mwaka wa 1915, akiwa wa nne katika familia yenye watoto tisa. Wazazi wake walifanya kazi katika mashamba ya miwa, nao walikuwa wafuasi thabiti wa dini ya Kihindu. Masomo ya Biblia yalimchochea Velloo alipokuwa shuleni, na alipokuwa kijana, mtu fulani alimpa Biblia. Aliisoma kila siku, akaimaliza baada ya miaka minne. Aliandika hivi: “Andiko la Mathayo 5:6 lilinivutia. Nilipolisoma, nilitambua kwamba Mungu hufurahi iwapo mtu ana njaa kwa ajili ya kweli na ya kufanya lililo sawa.”
Mwishowe Velloo alitembelewa na Shahidi naye akaanza kujifunza Biblia. Alikuwa miongoni mwa Wahindi wa kwanza kubatizwa Afrika Kusini, mwaka wa 1954. Jamii ya Wahindi, katika eneo aliloishi huko Actonville, Gauteng, iliwapinga vikali Mashahidi wa Yehova, na hata mtu fulani mashuhuri alitisha kumwua Velloo. Kwa sababu ya msimamo wake imara kwa ajili ya kweli ya Biblia, Velloo alipoteza kazi yake ya kusimamia biashara ya udobi. Hata hivyo, aliendelea kumtumikia Yehova kwa uaminifu hadi alipokufa mwaka wa 1981. Kielelezo chake kizuri kilikuwa na matokeo, kwa kuwa washiriki zaidi ya 190 wa familia yake (kutia ndani watu wa ukoo kupitia ndoa) kufikia vizazi vinne wanaendelea kumtumikia Yehova.
Gopal Coopsammy alikuwa na umri wa miaka 14 aliposikia kweli kwa mara ya kwanza kutoka kwa mjomba wake, Velloo. “Velloo alizungumza na vijana kadhaa kati yetu kuhusu Biblia, ingawa sikuwa nikijifunza Biblia rasmi,” akumbuka. “Nikiwa Mhindu, niliiona Biblia kuwa kitabu kigeni. Hata hivyo, baadhi ya mambo niliyojifunza yalionekana kuwa yenye hekima. Siku moja nilimwona Velloo akiondoka kwenda kwenye Funzo la Kitabu la Kutaniko. Nilimwomba niandamane naye. Alikubali, na tangu wakati huo nimekuwa nikihudhuria mikutano. Nilitaka kuongeza ujuzi wangu wa Biblia, hivyo nikaenda kwenye maktaba ya umma na kupata vichapo kadhaa vya Mashahidi wa Yehova. Nilipata upinzani mwingi kutoka kwa familia yangu, lakini sikuzote nilikumbuka maneno ya Zaburi 27:10: ‘Hata ikiwa baba yangu na mama yangu wangeniacha, Yehova mwenyewe angenichukua.’ Nilibatizwa mwaka wa 1955, nikiwa na umri wa miaka 15.”
Gopal ni mwangalizi-msimamizi katika kutaniko analoshirikiana nalo, pamoja na mke wake, Susila. Wamewasaidia watu wapatao 150 kujiweka wakfu na kumtumikia Yehova. Alipoulizwa walitimizaje hilo, alisema: “Kulikuwa na washiriki wengi wa familia waliokuwa wakiishi katika eneo letu, ambao niliwahubiria. Baadhi yao waliitikia. Pia nilikuwa na biashara yangu mwenyewe, na hilo liliniwezesha kuwa na wakati wa kutumia katika huduma. Nilifanya upainia kwa miaka minne. Nilihubiri sana na kufuatia kwa bidii watu wowote waliopendezwa.”
-
-
Afrika Kusini2007 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Isabella alisimulia jambo hili lililoonwa: “Nilipokuwa katika huduma ya shambani, nilizungumza na mtu aliyekubali magazeti. Mke wake, Darishnie, aliyekuwa ametoka kanisani, akajiunga naye. Alikuwa amebeba mtoto wao. Tulikuwa na mazungumzo mazuri, nami nikapanga kuwarudia. Hata hivyo, Darishnie hakupatikana nyumbani. Baadaye aliniambia kwamba pasta wao alimwambia awe akitoka kila mara ninapowatembelea. Pasta huyo alijua kwamba akifanya hivyo, basi ningeona kwamba hapendezwi. Nilienda Uingereza kutembelea familia yangu. Nilipokuwa huko, niliendelea kumfikiria Darishnie. Niliporudi Afrika Kusini, nilienda kumwona. Alitaka kujua nilikuwa nimepotelea wapi. Alisema: ‘Nilijua kabisa kwamba ulidhani sipendezwi. Nafurahi sana kukuona tena.’ Tulianza kujifunza, ingawa mume wake hakujiunga nasi. Darishnie alikuwa mwanafunzi makini na muda si muda akabatizwa.
“Kulingana na dini yake, mwanamke aliyeolewa anapaswa kuvaa shanga yenye kidani cha dhahabu na uzi wa manjano shingoni. Shanga hiyo inaitwa tali. Anapaswa kuitoa ikiwa tu mume wake amekufa. Darishnie alipotaka kuanza kuhubiri, alitambua kwamba anahitaji kuvua shanga hiyo. Aliniuliza afanye nini. Nilimshauri azungumze na mume wake kwanza, ajue maoni yake. Alimuuliza, lakini mume wake hakutaka aivue. Nikamwambia awe na subira, angoje kidogo, kisha mume wake atakapokuwa ametulia, amuulize tena. Hatimaye mumewe akamruhusu aivue. Tuliwatia moyo wanafunzi wetu wa Biblia wawe na busara na kuheshimu mafundisho ya Kihindu na wakati huohuo wachukue msimamo kwa ajili ya kweli ya Biblia. Hivyo, waliepuka kuwaudhi marafiki na watu wa ukoo ambao pia wangekubali mabadiliko ya kidini ya wanafunzi wa Biblia.”
-