-
Dunia Je, Ni Mahali pa Kujaribu Wanadamu?Mnara wa Mlinzi—2000 | Oktoba 1
-
-
Dunia Je, Ni Mahali pa Kujaribu Wanadamu?
NI FURAHA kama nini! Alipita mitihani. Mwanafunzi aliyekuwa amefanya mitihani migumu kwa majuma mawili aliambiwa kwamba amepita. Sasa angeweza kupata kazi aliyokuwa ametamani sikuzote.
Wengi huyaona maisha duniani kwa njia hiyo. Wao huona maisha duniani kuwa mtihani ambao lazima kila mtu apitie. “Wanaopita” hupata maisha bora ya baada ya kifo. Lingekuwa jambo la kusikitisha kwelikweli ikiwa maisha ya sasa yangekuwa ndiyo tu ambayo wanadamu wangeweza kutarajia, kwa kuwa wengi hawayafurahii. Ingawa alikuwa tajiri mwenye afya nzuri kwa karibu muda wote wa maisha yake, Ayubu, anayetajwa katika Biblia alisema hivi: “Mwanadamu aliyezaliwa na mwanamke siku zake za kuishi si nyingi, naye hujaa taabu.”—Ayubu 14:1.
Kamusi ya New Catholic Encyclopedia yaonyesha maoni ya wengi inaposema hivi: “Mungu amekusudia wanadamu maisha ya utukufu wa mbinguni. . . . Furaha ya wanadamu inategemea furaha kamili atakayopata mbinguni.” Uchunguzi mmoja uliofanywa na kanisa la Church of Christ ulionyesha kwamba asilimia 87 ya waliohojiwa wanaamini kwamba huenda watakwenda mbinguni baada ya kifo.
Wengi wasio Wakristo pia wanatarajia kuhama duniani na kwenda mahali pazuri zaidi baada ya kifo. Waislamu kwa mfano, huamini kwamba watakwenda paradiso ya mbinguni. Wafuasi wa madhehebu ya Bara la Utakato ya dini ya Buddha nchini China na Japani huamini kwamba kwa kurudia-rudia kutaja bila kukoma “Amitabha,” jina la Buddha wa Nuru Isiyo na Ukomo, watazaliwa upya katika Bara la Utakato, au Paradiso ya Magharibi, watakapoishi kwa shangwe nyingi sana.
Kwa kupendeza, Biblia, kitabu kitakatifu ambacho kimetafsiriwa na kusambazwa kuliko kitabu kingine chochote ulimwenguni, haisemi kwamba dunia ni mahali ambapo twapaswa kutoroka, mahali pa kupitia tu ili kwenda pengine. Kwa mfano, Biblia yasema hivi: “Wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele.” (Zaburi 37:29) Katika Biblia twaweza pia kusoma maneno haya ya Yesu yanayojulikana sana: “Heri wenye upole; maana hao watairithi nchi.”—Mathayo 5:5, Union Version.
Maoni ya watu wengi ya kwamba dunia ni makao yetu ya muda tu yamaanisha kwamba kifo ni njia ya kufikia maisha yenye furaha kamili ya baada ya kifo. Ikiwa ndivyo ilivyo, basi kwa hakika kifo ni baraka. Lakini je, watu huona kifo kuwa baraka, au wao hujaribu kurefusha maisha ya sasa? Kwa kawaida, watu wakiwa na afya njema na maisha salama kadiri fulani, hawataki kufa.
Hata hivyo, kwa sababu maisha duniani yanajaa maovu na mateso, bado wengi waona kwamba amani ya kweli na furaha zapatikana tu mbinguni. Je, mbinguni ni mahali penye usalama na furaha tupu, ambapo uovu na migogoro haziwezi kuwapo kabisa? Na je, maisha ya baada ya kifo yatapatikana tu mbinguni? Huenda ukashangaa kujua majibu ya Biblia. Tafadhali endelea kusoma.
-
-
Furaha ya Milele Mbinguni Au Duniani?Mnara wa Mlinzi—2000 | Oktoba 1
-
-
Furaha ya Milele Mbinguni Au Duniani?
JE, FURAHA yako hutegemea hasa mahali unapoishi? Watu wengi huenda wakakubali bila kusita kwamba furaha hutegemea mambo kama afya nzuri, kuwa na kusudi maishani, na uhusiano mzuri pamoja na wengine. Mithali moja ya Biblia yasema hivi: “Chakula cha mboga penye mapendano; ni bora kuliko ng’ombe aliyenona pamoja na kuchukiana.”—Mithali 15:17.
Hata hivyo, makao yetu ya kidunia yamekuwa mahali penye chuki, ujeuri, na aina nyingine za maovu kwa muda mrefu. Namna gani mbinguni, mahali penye viumbe wa kiroho ambapo wengi wanatarajia kwenda baada ya kifo? Je, mbinguni pamekuwa sikuzote mahali penye amani, furaha na utulivu, bila mzozo wa aina yoyote, jinsi watu wengi wanavyodhani?
Biblia yafundisha kwamba Mungu anakaa mbinguni pamoja na mamilioni ya viumbe wa roho waitwao malaika. (Mathayo 18:10; Ufunuo 5:11) Hao wanaelezwa kuwa ‘wana [wa roho] wa Mungu’. (Ayubu 38:4, 7) Kama wanadamu, malaika pia wana uhuru wa kuchagua, hao si mashine zifanyazo kazi bila hiari ya kuchagua. Kwa hiyo, wao pia waweza kuchagua kufanya mema au mabaya. Je, malaika wangechagua kufanya mabaya? Huenda baadhi ya watu wakastaajabu kujua kwamba maelfu ya miaka iliyopita, idadi kubwa ya malaika walifanya dhambi dhidi ya Mungu—walimwasi Mungu!—Yuda 6.
Waasi Mbinguni
Dhambi ilianza mbinguni kwa sababu ya uasi wa malaika ambaye alikuja kuitwa Shetani (Mkinzani) na Ibilisi (Mchongezi). Huyo malaika ambaye mwanzoni alikuwa mwaminifu alichagua kwa hiari yake mwenyewe kufanya mabaya. Kuanzia hapo alianza kupotosha viumbe wengine wa kiroho, hivi kwamba katika siku za Noa, kabla ya Gharika, malaika wengi walijiunga naye kumwasi Mungu.—Mwanzo 6:2, NW, kielezi-chini; 2 Petro 2:4.
Malaika hao waliofanya dhambi hawakufukuzwa mbinguni mara moja. Badala yake, kwa maelfu ya miaka malaika hao waliruhusiwa kuingia mbinguni, ijapokuwa yaelekea waliwekewa mipaka fulani.a Hata hivyo, wakati uvumilivu wa Mungu kwa watenda waovu hao ulipokoma, ‘walivurumishwa’ chini kutoka mbinguni ili hatimaye waharibiwe. Kisha sauti mbinguni ikasema hivi: “Kwa ajili ya hili teremeni, nyinyi mbingu nanyi mkaao ndani yazo!” (Ufunuo 12:7-12) Kwa wazi, malaika waaminifu mbinguni walishangilia sana kwamba, mwishowe, wachochezi hao waovu walikuwa wametupwa nje!
Tukizingatia mambo haya ambayo watu wengi hawayajui, ni wazi kwamba hakuwezi kuwa na amani ya kweli wakati wowote ule ambapo viumbe wenye akili wanavunja sheria na kanuni za Mungu. (Isaya 57:20, 21; Yeremia 14:19, 20) Kwa upande mwingine, watu wote wafuatapo sheria za Mungu, amani na utulivu huenea. (Zaburi 119:165; Isaya 48:17, 18)
-