-
Tunaweza Kufufuliwa!Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu
-
-
Sura Ya 35
Tunaweza Kufufuliwa!
TUKIFA, je, Mungu angependa kutufufua, yaani, kuturudisha hai tena?— Ayubu yule mtu mwema aliamini kwamba Mungu angependa kutufufua. Kwa hiyo, Ayubu alipoona anakaribia kufa, alimwambia Mungu hivi: ‘Utaita, na mimi mwenyewe nitakujibu.’ Ayubu alisema kwamba Yehova Mungu angetamani sana kumfufua.—Ayubu 14:14, 15.
Yesu ni kama Baba yake, Yehova Mungu. Yesu anataka kutusaidia. Mtu mwenye ukoma alipomwambia, “Ikiwa tu unataka, unaweza kunitakasa,” Yesu alijibu: “Ninataka.” Naye akamponya mtu huyo ukoma wake.—Marko 1:40-42.
Yesu alijifunza kutoka kwa Baba yake kuwapenda watoto. Mara mbili hapo zamani, Yehova aliwatumia watumishi wake kuwafufua watoto wadogo. Eliya alimsihi Yehova amfufue mwana wa mwanamke mmoja aliyekuwa amemkaribisha Eliya. Naye Yehova akamfufua. Yehova pia alimtumia mtumishi wake Elisha kumfufua mvulana mdogo.—1 Wafalme 17:17-24; 2 Wafalme 4:32-37.
Je, haifurahishi kujua kwamba Yehova anatupenda sana?— Yeye hatufikirii tu tunapokuwa hai. Iwapo tutakufa atatukumbuka. Yesu alisema kwamba Baba yake hata anawaona watu anaowapenda kuwa hai hata kama tayari wamekufa! (Luka 20:38) Biblia inasema kwamba ‘wala kifo wala uzima wala mambo yaliyo hapa sasa wala mambo yatakayokuja hayataweza kututenga na upendo wa Mungu.’—Waroma 8:38, 39.
Yesu alipokuwa duniani, alionyesha kwamba Yehova anawajali watoto wadogo. Kumbuka kwamba Yesu alitumia wakati kuzungumza na watoto kumhusu Mungu. Lakini, je, unajua kwamba Mungu alimpa Yesu nguvu za kufufua watoto?— Na tuzungumze kuhusu wakati Yesu alipomfufua binti mwenye umri wa miaka 12 wa mtu aitwaye Yairo.
Yairo aliishi na mke wake na binti yao mmoja tu karibu na Bahari ya Galilaya. Siku moja huyo binti mdogo akawa mgonjwa sana, na Yairo akatambua kwamba atakufa. Akaanza kumfikiria Yesu, yule mtu mzuri sana ambaye Yairo alisikia habari zake kwamba ana uwezo wa kuwaponya watu. Basi Yairo akaenda kumtafuta. Akampata Yesu akiwafundisha watu wengi ufuoni mwa Bahari ya Galilaya.
Yairo anapita katikati ya umati na kumpigia Yesu magoti. Anamwambia Yesu hivi: ‘Binti yangu mdogo ni mgonjwa sana. Njoo tafadhali umsaidie? Nakusihi uje.’ Mara moja Yesu akaenda na Yairo. Umati uliokuja kumwona Mwalimu Mkuu unamfuata pia. Lakini baada ya kwenda umbali fulani, watu fulani kutoka kwa Yairo wanakuja na kumwambia: ‘Binti yako amekufa! Usimsumbue mwalimu.’
Yesu akawasikia watu hao wakisema hivyo. Anajua jinsi Yairo anavyohuzunika kuhusu kifo cha mtoto wake wa pekee. Basi Yesu anamwambia: ‘Usiogope. Uwe tu na imani katika Mungu, na binti yako atakuwa mzima.’ Wanaendelea kwenda mpaka kwa Yairo. Rafiki zao wanalia. Wanahuzunika kwa sababu rafiki yao mchanga amekufa. Lakini Yesu anawaambia: ‘Acheni kulia. Mtoto huyu hakufa, bali amelala usingizi.’
Yesu anaposema maneno hayo, watu wanaanza kucheka, kwani wanajua kwamba msichana huyo amekufa. Basi, unafikiri ni kwa nini Yesu anasema kwamba amelala usingizi?— Unafikiri anataka kuwafunza watu somo gani?— Anataka wajue kwamba kifo kinaweza kuwa kama usingizi mzito. Anataka kuwafundisha kwamba kupitia nguvu za Mungu, anaweza kumfufua mtu aliyekufa kwa njia rahisi sana kama vile tunavyoweza kumwamsha mtu kutoka usingizini.
Yesu anawaambia watu wote watoke nje ila mitume wake Petro, Yakobo, na Yohana na baba na mama ya msichana huyo. Kisha anaingia ndani alimo huyo mtoto. Anamshika kwa mkono wake na kusema: “Msichana, inuka!” Na mara moja akainuka na kuanza kutembea! Baba yake na mama yake wanajawa na shangwe wee!—Marko 5:21-24, 35-43; Luka 8:40-42, 49-56.
Hebu fikiria jambo hili. Ikiwa Yesu aliweza kumfufua msichana huyo mdogo, je, anaweza kuwafufua wengine pia?— Unafikiri kweli atafanya hivyo?— Ndiyo, atawafufua. Yesu mwenyewe alisema: “Saa inakuja ambayo wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti [yangu] na kutoka.”—Yohana 5:28, 29.
Unafikiri Yesu anataka kuwafufua watu?— Mfano mwingine katika Biblia unasaidia kujibu swali hilo. Jambo fulani lililotokea siku moja karibu na jiji la Naini linaonyesha jinsi Yesu anavyohisi kuhusu watu wanaoomboleza wakati wa mazishi.
Mwanamke mmoja yuko katika msafara wa mazishi ya mwana wake katika umati unaoondoka Naini. Mume wake alikuwa tayari amekufa, na sasa mwana wake wa pekee amekufa. Amehuzunika sana! Watu wengi wa Naini wanaambatana naye mwili wa mwana wake unapopelekwa nje ya jiji. Mwanamke huyo anaomboleza na hakuna mtu anayeweza kumtuliza.
Ikatukia kwamba siku hiyo Yesu na wanafunzi wake nao walikuwa wakielekea jiji la Naini. Wakiwa karibu na lango la jiji, wanakutana na umati ukienda kumzika mwana wa yule mwanamke. Yesu anapomwona huyo mwanamke anayeomboleza, anamhurumia. Moyo wake unaguswa anapoona huzuni kubwa aliyo nayo mwanamke huyo. Anataka kumsaidia.
Yesu akamwambia hivi kwa huruma na kwa uthabiti ili mwanamke huyo amsikilize: “Acha kulia.” Namna alivyozungumza na kutenda kunafanya watu wote wamtazame kwa shauku. Yesu anapoukaribia mwili huo, ni lazima watu wote wanashangaa kuhusu kile atakachofanya. Yesu anaamuru hivi: “Kijana, ninakuambia, Inuka!” Mara moja anaketi! Anaanza kuzungumza.—Luka 7:11-17.
Hebu wazia jinsi mwanamke huyo alivyohisi! Unaweza kuhisije kumpokea tena mpendwa aliyekufa?— Je, hiyo haionyeshi kwamba Yesu kwa kweli anawapenda watu na anataka kuwasaidia?— Hebu wazia jinsi itakavyopendeza katika ulimwengu mpya wa Mungu kuwakaribisha watakaofufuliwa!—2 Petro 3:13; Ufunuo 21:3, 4.
Wakati huo baadhi ya watu watakaofufuliwa watakuwa watu tuliowajua hapo awali, kutia ndani watoto. Tutawajua kama vile tu Yairo alivyomjua binti yake alipofufuliwa na Yesu. Wengine watakuwa watu waliokufa mamia au maelfu ya miaka iliyopita. Lakini Mungu hatawasahau hata kama waliishi zamani sana.
Je, haipendezi kujua kwamba Yehova Mungu na Mwana wake Yesu wanatupenda sana?— Wanataka tuishi, si kwa miaka michache tu, bali milele!
Kuhusu tumaini ajabu la Biblia kuhusu wafu, tafadhali soma Isaya 25:8; Matendo 24:15; na 1 Wakorintho 15:20-22.
[Picha katika ukurasa wa 182]
Yehova alionyeshaje kwamba anapenda watoto wadogo?
[Picha katika ukurasa wa 184]
Hatua ya Yesu ya kumfufua binti ya Yairo inatufundisha nini?
[Picha katika ukurasa wa 186]
Ufufuo wa mtoto wa pekee wa mwanamke huyu unaonyesha nini?
-
-
Ni Nani Watakaofufuliwa? Nao Wataishi Wapi?Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu
-
-
Sura Ya 36
Ni Nani Watakaofufuliwa? Nao Wataishi Wapi?
KATIKA sura mbili zilizotangulia, tulisoma kuhusu watu wangapi waliofufuliwa?— Watano. Ni wangapi waliokuwa watoto?— Watatu. Na wa nne anaitwa kijana. Unafikiri hiyo inamaanisha nini?—
Inamaanisha kwamba Mungu anawapenda watoto na vijana. Lakini atawafufua watu wengine pia. Je, Mungu atawafufua watu waliofanya mema tu?— Tunaweza kufikiria hivyo. Lakini, watu wengi hawakujifunza ukweli kumhusu Yehova Mungu na Mwana wake. Kwa hiyo walifanya mabaya kwa sababu walifundishwa mambo yasiyo ya kweli. Unafikiri Yehova atawafufua watu kama hao?—
Biblia inasema: “Kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.” (Matendo 24:15) Kwa nini wale ambao hawakuwa waadilifu, au wale ambao hawakufanya mema, wafufuliwe?— Wao watafufuliwa kwa sababu hawakupata nafasi kamwe ya kujifunza kumhusu Yehova na yale anayotaka watu wafanye.
Unafikiri watu watafufuliwa lini?— Fikiria wakati Lazaro alipokufa na ahadi ambayo Yesu alimpa Martha dada yake: “Ndugu yako atafufuka.” Martha akajibu: “Ninajua atafufuka katika ufufuo siku ya mwisho.” (Yohana 11:23, 24) Martha alimaanisha nini aliposema Lazaro atafufuka katika “siku ya mwisho”?—
Martha alikuwa amesikia ahadi hii ya Yesu: ‘Wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho watatoka.’ (Yohana 5:28, 29) Kwa hiyo “siku ya mwisho” ni wakati wale wote walio katika kumbukumbu la Mungu watakapofufuliwa. Siku hiyo ya mwisho si siku yenye muda wa saa 24. Itakuwa kipindi cha miaka elfu moja. Biblia inasema kwamba katika siku hiyo ‘Mungu atawahukumu watu wa dunia.’ Watakaohukumiwa watatia ndani wale watakaofufuliwa.—Matendo 17:31; 2 Petro 3:8.
Hebu wazia jinsi itakavyokuwa siku yenye furaha ajabu! Wakati wa kipindi cha hiyo siku ya miaka elfu moja, mamilioni ya watu waliokufa watafufuliwa. Yesu anapaita mahali ambapo watu hao wataishi kuwa Paradiso. Na tuone Paradiso itakuwa wapi na jinsi hali itakavyokuwa.
Karibu saa tatu kabla ya Yesu kufa katika mti wa mateso, anamwambia mtu aliye kwenye mti wa mateso karibu naye kuhusu Paradiso. Mtu huyo anauawa kwa sababu ya uhalifu aliofanya. Lakini mhalifu huyu anapomwona Yesu na kusikia yanayosemwa juu Yake, anaanza kumwamini Yesu. Basi mhalifu huyo anasema: “Unikumbuke utakapoingia katika ufalme wako.” Yesu anamjibu: “Kwa kweli mimi nakuambia leo, Utakuwa pamoja nami katika Paradiso.”—Luka 23:42, 43.
Yesu anamaanisha nini anaposema hivyo? Paradiso iko wapi?— Hebu fikiria. Kwanza kabisa hii Paradiso ilikuwa wapi?— Kumbuka kwamba Mungu aliwapa watu wa kwanza, Adamu na mke wake, paradiso papa hapa duniani ili waishi ndani yake. Iliitwa bustani ya Edeni. Kulikuwa na wanyama katika bustani hiyo, lakini hawakuwa hatari. Kulikuwa na miti yenye matunda mengi matamu, na vilevile mto mkubwa. Palikuwa mahali pazuri ajabu pa kuishi!—Mwanzo 2:8-10.
Tunaposoma kwamba mhalifu huyo atakuwa katika Paradiso, tunapaswa kuona akilini dunia hii ikiwa mahali maridadi pa kuishi. Je, Yesu atakuwa katika Paradiso hapa duniani pamoja na huyo mtu ambaye zamani alikuwa mhalifu?— La. Je, unajua ni kwa nini hatakuwa duniani?—
Ni kwa sababu Yesu atakuwa mbinguni akitawala akiwa Mfalme juu ya dunia Paradiso. Kwa hiyo, Yesu atakuwa pamoja na mtu huyo katika maana ya kwamba Yesu atamfufua na kumtimizia mahitaji yake. Lakini kwa nini Yesu atamruhusu mtu aliyekuwa mhalifu aishi katika Paradiso?— Hebu tuone jibu.
Kabla ya mhalifu huyo kuzungumza na Yesu, je, alijua makusudi ya Mungu?— La. Alifanya mabaya kwa sababu hakujua kweli kumhusu Mungu. Akiwa katika Paradiso atafundishwa makusudi ya Mungu. Kisha atapata nafasi ya kuthibitisha kwamba kwa kweli anampenda Mungu kwa kufanya mapenzi Yake.
Je, kila mtu atakayefufuliwa ataishi katika dunia Paradiso?— La. Unajua ni kwa nini?— Kwa sababu wengine watafufuliwa wakaishi na Yesu mbinguni. Watatawala na yeye juu ya dunia Paradiso wakiwa wafalme. Tunajuaje jambo hilo? Hebu tuone.
Usiku kabla ya kifo chake, Yesu aliwaambia mitume wake hivi: ‘Katika nyumba ya Baba yangu mbinguni, mna makao mengi, nami naenda kuwatayarishia ninyi mahali.’ Kisha Yesu anawaahidi: “Nitakuja tena nami nitawapokea ninyi nyumbani kwangu mwenyewe, ili mahali nilipo mimi, ninyi pia muwe hapo.”—Yohana 14:2, 3.
Yesu anaenda wapi baada ya kufufuliwa?— Anarudi mbinguni kuwa na Baba yake. (Yohana 17:4, 5) Kwa hiyo Yesu anawaahidi mitume wake na wanafunzi wengine kwamba atawafufua ili wawe pamoja naye mbinguni. Watafanya nini pamoja na Yesu huko?— Biblia inasema kwamba wanafunzi wake ambao watafufuliwa katika “ufufuo wa kwanza” wataishi mbinguni na watatawala juu ya dunia “wakiwa wafalme pamoja naye ile miaka elfu.”—Ufunuo 5:10; 20:6; 2 Timotheo 2:12.
Ni wangapi watakaofufuliwa katika “ufufuo wa kwanza” na watawale pamoja na Yesu wakiwa wafalme?— Yesu aliwaambia wanafunzi wake: “Msiogope, kundi dogo, kwa sababu Baba yenu amekubali kuwapa ninyi ufalme.” (Luka 12:32) Kuna idadi hususa ya “kundi dogo” wanaofufuliwa ili kuwa na Yesu katika Ufalme wa mbinguni. Biblia inaonyesha kwamba watu “144,000” wanafufuliwa kutoka duniani.—Ufunuo 14:1, 3.
Ni wangapi watakaoishi katika dunia Paradiso?— Biblia haisemi. Lakini Mungu aliwaambia Adamu na Hawa walipokuwa katika bustani ya Edeni wazae watoto na kuijaza dunia. Wakakosa kufanya hivyo. Lakini Mungu atahakikisha kwamba kusudi lake la kuijaza dunia watu waadilifu linatimizwa.—Mwanzo 1:28; Isaya 45:18; 55:11.
Hebu wazia tu jinsi itakavyopendeza kuishi katika Paradiso! Dunia yote itakuwa kama bustani. Itakuwa na ndege na wanyama na miti na maua maridadi ya kila aina. Hakuna mtu atakayekuwa na maumivu kwa sababu ya ugonjwa wala hakuna mtu atakayekufa. Watu wote watakuwa marafiki. Ikiwa tunataka kuishi milele katika Paradiso, basi tujitayarishe wakati huu.
Soma habari zaidi kuhusu kusudi la Mungu kwa dunia katika Mithali 2:21, 22; Mhubiri 1:4; Isaya 2:4; 11:6-9; 35:5, 6; na 65:21-24.
[Picha katika ukurasa wa 187]
Kwa nini Mungu atafufua watu wengine ambao hawakufanya mema?
[Picha katika ukurasa wa 188]
Paradiso ambayo Yesu anamwambia mtu huyu iko wapi?
[Picha katika ukurasa wa 189]
Tunaposoma kuhusu Paradiso, tunapaswa kuona nini akilini?
[Picha katika ukurasa wa 190]
Watakaofufuliwa wataishi wapi, nao watafanya nini?
-