Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kifo—Je, Kweli Ndio Mwisho?
    Amkeni!—2008 | Septemba
    • Kifo—Je, Kweli Ndio Mwisho?

      MNAMO Februari (Mwezi wa 2) 1987, mwanamume mwenye umri wa miaka 85 aliyekuwa na ugonjwa wa figo, aliacha kutumia mashine ya kusafisha damu iliyokuwa ikimsaidia kuishi. Majuma mawili baadaye, alikufa kwa utulivu nyumbani huku mwanaye wa pekee akiwa kando yake.

      Muda wao wa mwisho pamoja uliwapa nafasi ya kuzungumzia jambo walilokuwa wamezungumzia mapema: Je, wafu wanaweza kuishi tena? Baba aliyekuwa na elimu ya juu alikuwa na mashaka kuhusu jambo hilo. Aliamini fundisho la mageuzi na alichukizwa na unafiki wa kidini. Aliamini kwamba mambo ya Mungu hayawezi kujulikana.

      Akitamani kumfariji na kumpa tumaini baba yake, mwana huyo alimwonyesha kwa nini wafu wanaweza kuishi tena. Kifo chake kilipokaribia, baba huyo alikubali kwamba angetamani kuishi tena akiwa mwenye afya na nguvu.

      Faraja Tunapokabili Kifo

      Watu wengi wangetamani kuishi tena ikiwa wangerudishiwa afya na nguvu katika ulimwengu ulio na amani. Wanadamu ni tofauti na wanyama ambao wanafafanuliwa katika Biblia kuwa “wasiofikiri” au “viumbe wanaoongozwa na silika.” (2 Petro 2:12; New International Version) Sisi huwazika wafu. Sisi tunafikiri kuhusu wakati ujao. Sisi hatutaki kuzeeka, kuwa wagonjwa, na kufa. Hata hivyo, mambo hayo huwapata wanadamu.

      Tunahuzunishwa tunapofikiria kwamba sisi au mpendwa wetu anaweza kufa. Hata hivyo, Biblia inatutia moyo tukabiliane na kifo kwa ujasiri inaposema: “Ni afadhali kwenda katika nyumba ya maombolezo kuliko kwenda katika nyumba ya karamu.” Inaongezea hivi: “Aliye hai anapaswa kuliweka jambo hilo moyoni mwake.” (Mhubiri 7:2) Kwa nini tuliweke jambo hilo moyoni au tufikirie kifo kwa uzito?

      Sababu moja ni kwamba tumezaliwa na tamaa ya kuishi na kufurahia maisha ya amani na usalama. Hakuna mtu anayetaka kufa au kutokuwepo. Ni vigumu sana kufikiria kwamba tutaacha kuishi. Biblia inaeleza sababu inaposema: “[Mungu] ameweka umilele katika akili ya mwanadamu,” au “ndani ya moyo wao.” (Mhubiri 3:11, Revised Standard Version) Tunataka kuishi, si kufa. Hebu fikiria kuhusu hilo: Je, tamaa hiyo ingekuwa yenye nguvu sana ikiwa Muumba hakukusudia tuishi milele? Je, tunaweza kuishi tena tukiwa na afya na furaha milele?

      Kwa Nini Tuamini?

      Mwaka jana, gazeti AARP The Magazine, linalochapishwa na Shirika la Marekani la Wastaafu, lilikuwa na makala yenye kichwa “Uhai Baada ya Kifo.” Watu wengi wenye umri wa zaidi ya miaka 50 walihojiwa na “asilimia 73 hivi wanakubaliana na maneno haya, ‘Ninaamini kwamba kuna uhai baada ya kifo.’” Kwa upande mwingine, gazeti hilo liliripoti kwamba karibu asilimia 25 walikubaliana na maneno haya, “Ninaamini kwamba nikifa, huo ndio mwisho.” Lakini je, kweli hivyo ndivyo watu wanataka kuamini?

      Katika makala hiyohiyo, Tom ambaye ni Mkatoliki kutoka New York, aliripotiwa kusema hivi: “Viongozi wa kidini wanahubiri kwamba kuna uhai baada ya kifo. Mimi hujiambia, kila mtu ana maoni yake. Kwa hiyo, mtu hujiamulia atakachoamini. Mimi huhudhuria Misa. Ninaishi kana kwamba kuna uhai baada ya kifo lakini siamini hilo. Ikiwa kunao, basi nitafaidika.”

      Kama vile Tom, watu wengi wana mashaka kama baba aliyetajwa mwanzoni mwa makala hii alimwambia mwanaye hivi mara nyingi: “Kuwa na imani ya kidini ni sawa kwa watu wanaoshindwa kukubali kwamba kifo ni jambo halisi.” Hata hivyo, yeye pamoja na watu wengine walio na mashaka wamelazimika kukubali kwamba kumwamini Muumba mwenye nguvu zote kunatoa majibu kuhusu miujiza isiyoeleweka kwa njia nyingine yoyote.

      Kwa mfano, majuma matatu tu baada mimba kutungwa, kiini-tete cha mwanadamu huanza kutokeza chembe za ubongo. Chembe hizo huongezeka haraka sana, mara nyingine hata kufikia 250,000 kwa dakika. Miezi tisa baadaye, mtoto huzaliwa akiwa na uwezo wa ajabu wa kujifunza. Mwanabiolojia wa molekuli James Watson alisema kwamba ubongo wa mwanadamu ndicho “kitu tata zaidi ambacho tumepata kugundua katika ulimwengu wetu.”

      Watu wengi hustaajabu wanapofikiria maajabu kama hayo. Vipi wewe? Je, kutafakari kuhusu mambo hayo kumekusaidia kujibu swali hili lililoulizwa na mtu fulani miaka mingi iliyopita: “Mtu akifa, je, anaweza kuishi tena?” Mtu huyo alimjibu Mungu hivi kwa uhakika: “Wewe utaita, na mimi mwenyewe nitakujibu. Kwa kuwa utaitamani sana kazi ya mikono yako.”—Ayubu 14:14, 15.

      Kwa kweli, tuna sababu ya kuchunguza uthibitisho unaoonyesha kwamba inawezekana kuishi baada ya kifo.

  • Wafu Wataishi Tena!
    Amkeni!—2008 | Septemba
    • Wafu Wataishi Tena!

      KATIKA sinema miaka kadhaa iliyopita, kijana mmoja alionyeshwa akisimama kando ya kaburi la mpendwa wake. “Sikuzote Mama alisema kufa ni sehemu ya maisha,” akasema. Kisha kamera ilipoelekezwa kwenye kaburi, akaongezea: “Afadhali haingekuwa hivyo.”

      Maneno kama hayo huonyesha hisia za mabilioni ya watu ambao wamewapoteza wapendwa wao katika kifo. Ni adui mbaya kama nini! Hata hivyo, Mungu anaahidi hivi: “Adui wa mwisho atakayeangamizwa ni kifo.” (1 Wakorintho 15:26) Lakini kwa nini tunakufa licha ya kwamba tuna uwezo wa kuishi milele? Kifo kitaangamizwaje?

      Kwa Nini Tunazeeka na Kufa?

      Biblia inasema hivi kumhusu Yehova Mungu, Muumba wetu: “Kazi zake ni kamilifu.” (Kumbukumbu la Torati 32:4; Zaburi 83:18) Mtu wa kwanza, Adamu, aliumbwa akiwa mkamilifu na alikuwa na uwezo wa kuishi milele katika Edeni, iliyokuwa Paradiso duniani ambapo Mungu aliwaweka. (Mwanzo 2:7-9) Kwa nini Adamu alipoteza makao yake ya Paradiso, akazeeka, na kufa?

      Kwa ufupi: Adamu hakutii sheria ya kutokula tunda kutoka kwa mti fulani. Mungu alikuwa amemwambia Adamu waziwazi kuhusu adhabu ya kufanya hivyo, aliposema: “Utakufa hakika.” (Mwanzo 2:16, 17) Adamu alijiunga na mke wake, Hawa, kutotii amri hiyo, hivyo Mungu akawafukuza kutoka Edeni. Kuna sababu muhimu kwa nini Mungu alitenda hivyo. Biblia inasema: “Ili [Adamu] asije akanyoosha mkono wake achukue matunda kutoka pia katika mti wa uzima [ulio bustanini] na kula na kuishi [milele].”—Mwanzo 3:1-6, 22.

      Adamu na Hawa walikufa kwa sababu ya kutotii, lakini kwa nini wazao wao huzeeka na kufa? Kwa sababu walirithi dhambi kutoka kwa Adamu, na dhambi imetokeza kutokamilika na kifo kwa wazao wao wote. Biblia inaeleza hivi: “Kupitia mtu mmoja [Adamu] dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.”—Waroma 5:12.

      Inawezekana Kuishi Tena

      Kama tulivyosoma awali, ‘kifo kitaangamizwa,’ naam, kitaondolewa milele! (1 Wakorintho 15:26) Kitaondolewaje? Biblia inaeleza hilo ikisema: “Kupitia tendo moja la kutetewa kuwa haki matokeo kwa watu wa namna zote ni wao kutangazwa kuwa waadilifu kwa ajili ya uzima.” (Waroma 5:18) Ni nini linalotuwezesha tuwe na msimamo wa uadilifu mbele ya Mungu na kufurahia uzima wa milele?

      Ni maandalizi ya kuondoa kabisa dhambi ambayo wanadamu wote walirithi kutoka kwa mwanadamu wa kwanza, Adamu. Biblia inaeleza: “Zawadi ambayo Mungu hutoa ni uzima wa milele kupitia Kristo Yesu Bwana wetu.” (Waroma 6:23) Yesu alisema hivi kuhusu maandalizi hayo ya kuwatangaza watu kuwa waadilifu kwa ajili ya uzima: “Mungu aliupenda ulimwengu [wa wanadamu] sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.”—Yohana 3:16.

      Fikiri kuhusu kina cha upendo wa Mungu kwa ajili yetu, pia ule wa Mwana wake, Yesu Kristo, ambaye aliteseka sana kwa ajili yetu. Mtume Paulo aliandika: ‘Mwana wa Mungu alinipenda mimi na kujitoa mwenyewe kwa ajili yangu.’ (Wagalatia 2:20) Hata hivyo, kwa nini Yesu ndiye mwanadamu pekee ambaye ‘angetoa nafsi yake kuwa fidia’ kwa ajili yetu na hivyo kutuokoa kutokana na matokeo ya dhambi yanayosababisha kifo?—Mathayo 20:28.

      Yesu ndiye mtu pekee ambaye angeweza kutoa nafsi yake kuwa fidia kwa sababu yeye ndiye mwanadamu pekee ambaye hakurithi dhambi kutoka kwa mwanadamu wa kwanza, Adamu. Kwa nini? Kwa sababu uhai wa Yesu ulihamishwa kimuujiza kutoka mbinguni hadi kwenye tumbo la uzazi la Maria, aliyekuwa bikira. Kwa hiyo, kama malaika alivyomwambia Maria, mwana wake alikuwa ‘mtakatifu, Mwana wa Mungu.’ (Luka 1:34, 35) Hiyo ndiyo sababu Yesu anaitwa “Adamu wa mwisho” na ndiyo sababu hakurithi dhambi kutoka kwa “mtu wa kwanza Adamu.” (1 Wakorintho 15:45) Akiwa mwanadamu asiye na dhambi, Yesu angeweza kujitoa akiwa “fidia inayolingana,” yaani, uhai wake ulilingana na ule wa mtu wa kwanza aliyekuwa mkamilifu na asiye na dhambi.—1 Timotheo 2:6.

      Kupitia maandalizi ya fidia, Mungu ametuwezesha tupate kile ambacho Adamu wa kwanza alipoteza, yaani, uzima wa milele katika paradiso duniani. Hata hivyo, ili wapokee baraka hiyo, wanadamu wengi watahitaji kuishi tena. Hilo ni taraja zuri kama nini! Lakini je, kweli jambo hilo linawezekana?

      Msingi wa Kuamini

      Je, ni vigumu sana kuamini kwamba Yehova Mungu ambaye aliumba uhai ana uwezo wa kumuumba upya mtu aliyeishi hapo awali? Hebu fikiria uwezo wa kutunga mimba ambao Mungu alimpa mwanamke wa kwanza. “Adamu akalala na Hawa,” na miezi tisa hivi baadaye, wakazaa mtoto aliyefanana kabisa nao. (Mwanzo 4:1) Jambo lililotendeka katika tumbo la uzazi la Hawa ili kuumba sehemu zote za mtoto huyo na kuziunganisha bado huonwa kuwa muujiza ambao wanadamu hawawezi kuuelewa!—Zaburi 139:13-16.

      Watu hawaoni kuzaliwa kwa mtoto kuwa muujiza kwa sababu jambo hilo hutendeka mara nyingi sana kila siku. Hata hivyo, watu wengi wanaona kwamba haiwezekani kumfanya mtu aliyeishi hapo awali aishi tena. Yesu alipowaambia watu waliokuwa wakiomboleza kifo cha msichana mdogo waache kulia, ‘walianza kumcheka kwa dharau’ kwa sababu walijua kwamba alikuwa amekufa. Lakini Yesu alimwambia hivi msichana aliyekufa: “‘Simama!’ Na mara yule mwanamwali akasimama akaanza kutembea.” Tunaambiwa hivi: “Mara moja [wale waliokuwapo] wakawa na shangwe kubwa.”—Marko 5:39-43; Luka 8:51-56.

      Yesu alipoomba kaburi la Lazaro rafiki yake lifunguliwe, Martha dada ya Lazaro alipinga jambo hilo akisema: “Kufikia sasa lazima awe ananuka, kwa maana ni siku nne.” Hata hivyo, kulikuwa na shangwe kubwa kama nini Yesu alipomfufua Lazaro! (Yohana 11:38-44) Wengi walisikia kuhusu miujiza ya Yesu. Yohana mbatizaji alipokuwa gerezani, wanafunzi wa Yohana walimweleza kuhusu utendaji wa Yesu wakisema: “Wafu wanafufuliwa.”—Luka 7:22.

      Kuishi Tena Kupitia Ufufuo

      Kwa nini Yesu alifanya miujiza ya aina hiyo, ingawa watu aliowafufua walikuwa wagonjwa na kufa tena? Kwa sababu hilo lilithibitisha kwamba kile ambacho Adamu wa kwanza alipoteza, yaani, uzima wa milele katika paradiso duniani, kinaweza kurudishwa na kitarudishwa. Ufufuo ambao Yesu alifanya ulionyesha jinsi ambavyo hatimaye mamilioni ya wanadamu “wataimiliki dunia” na “watakaa milele juu yake.”—Zaburi 37:29.

      Inafurahisha kwamba tunaweza kuwa miongoni mwa wale walio na taraja la kuishi milele ikiwa tutajizoeza “ujitoaji-kimungu.” Biblia inasema kwamba ujitoaji kama huo, “una ahadi ya uzima wa sasa na ule utakaokuja.” ‘Uzima huo utakaokuja’ pia huitwa “uhai ambao ni uhai wa kweli” na “uzima ulio wa kweli.”—1 Timotheo 4:8; 6:19; Biblia Habari Njema.

      Acheni tuchunguze jinsi uzima huo wa kweli, uzima utakaokuja katika ulimwengu mpya wenye uadilifu utakavyokuwa.

      [Picha katika ukurasa wa 6]

      “Wakawa na shangwe kubwa”

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki