-
Tumaini Je, Linaweza Kutusaidia?Amkeni!—2004 | Aprili 22
-
-
Tumaini—Je, Linaweza Kutusaidia?
DANIEL alikuwa ameugua kansa kwa mwaka mmoja alipokuwa na umri wa miaka kumi tu. Madaktari na rafiki zake wa karibu walikuwa wamekata tamaa. Hata hivyo, Daniel aliendelea kuwa na tumaini. Aliamini kwamba siku moja angekuwa mkubwa na kuwa mtafiti ambaye angesaidia kupata tiba ya kansa. Alitarajia sana kuja kwa daktari ambaye ni mtaalamu wa kutibu aina ya kansa aliyokuwa nayo. Hata hivyo, siku hiyo ilipofika, daktari huyo alilazimika kuvunja safari yake kwa sababu ya hali mbaya ya hewa. Daniel akakata tamaa. Kwa mara ya kwanza, akafadhaika. Akafa siku chache baadaye.
Kisa cha Daniel kilisimuliwa na mfanyakazi wa afya ambaye alichunguza jinsi kuwa na tumaini au kupoteza tumaini kunavyoathiri afya. Huenda umesikia visa kama hivyo. Kwa mfano, fikiria mzee anayekaribia kufa ambaye anatarajia kwa hamu tukio fulani muhimu ambalo amengojea kwa muda mrefu, labda kutembelewa na mpendwa au sherehe fulani. Tukio hilo linapofika na kupita, mzee huyo hufa baada ya muda mfupi. Ni nini husababisha jambo hilo? Je, ni kukosa tumaini kama wengine wanavyoamini?
Watafiti wengi wa kitiba husema kwamba matazamio mema, tumaini, na maoni mazuri huboresha maisha na afya ya mtu. Lakini si wote wenye maoni hayo. Watafiti fulani hupinga jambo hilo wakisema kwamba halipatani na sayansi. Wao husema kwamba magonjwa hayawezi kusababishwa na hisia.
Bila shaka, maoni hayo yanayopinga umuhimu wa tumaini si mapya. Maelfu ya miaka iliyopita, mwanafalsafa Mgiriki Aristotle alipoulizwa maana ya tumaini, alijibu: “Ni ndoto ya mchana.” Na muda mrefu baadaye, mwanasiasa wa Marekani, Benjamin Franklin, alisema hivi waziwazi: “Anayeishi kwa tumaini atakufa njaa.”
-
-
Kwa Nini Tunahitaji Kuwa na Tumaini?Amkeni!—2004 | Aprili 22
-
-
Kwa Nini Tunahitaji Kuwa na Tumaini?
VIPI ikiwa Daniel, yule mtoto aliyeugua kansa ambaye alitajwa mwanzoni mwa makala ya kwanza, angedumisha matumaini yake makubwa? Je, angepona kansa? Je, angekuwa hai leo? Hata watu wanaosema tumaini ni muhimu sana hawangedai hivyo. Na hapo kuna jambo muhimu. Tumaini si mambo yote. Tumaini si dawa ya kila kitu.
Akihojiwa na Shirika la Habari la CBS Dakt. Nathan Cherney alionya kuhusu hatari za kukazia umuhimu wa tumaini kupita kiasi unaposhughulikia watu wagonjwa sana: “Tumesikia kuhusu waume wanaowakemea wake zao eti kwa sababu hawajatafakari vya kutosha, yaani, hawajawa na maoni yanayofaa.” Dakt. Cherney aliongezea hivi: “Maoni hayo yaliwafanya watu wafikiri kimakosa kwamba mtu anaweza kudhibiti ukuzi wa uvimbe wa kansa, na anapodhoofika, huenda wengine wakafikiri kwamba alishindwa kudhibiti uvimbe huo, lakini maoni hayo hayafai.”
Kwa kweli, wale wanaougua ugonjwa usiotibika wanakabili pambano kali. Bila shaka wapendwa wao hawangependa kuzidisha matatizo yao kwa kuwafanya wahisi kwamba wana hatia. Basi, je, tukate kauli kwamba hakuna haja ya kuwa na tumaini?
Hapana. Kwa mfano, badala ya kuutibu ugonjwa au kujaribu kurefusha maisha ya wagonjwa, daktari aliyetajwa juu, hupunguza maumivu yao na kuwafanya wastarehe kwa muda ambao watakuwa hai. Madaktari kama hao huamini sana umuhimu wa tiba zinazosaidia mtu kuwa mwenye furaha hata akiwa mgonjwa mahututi. Kuna uthibitisho wa kutosha kwamba tumaini linaweza kufanya hivyo na zaidi.
Umuhimu wa Tumaini
Dakt. W. Gifford-Jones, ambaye huandika habari za tiba, anasema: “Tumaini ni tiba yenye nguvu.” Alichunguza matokeo ya utafiti mbalimbali uliofanywa kubainisha umuhimu wa kuwategemeza kihisia watu wenye ugonjwa usio na tiba. Inasemekana kwamba utegemezo huo huwasaidia watu kudumisha tumaini na mtazamo unaofaa. Uchunguzi mmoja wa mwaka wa 1989 ulionyesha kwamba wagonjwa waliotegemezwa hivyo waliishi muda mrefu zaidi, lakini uchunguzi wa karibuni haujathibitisha wazi jambo hilo. Hata hivyo, uchunguzi mbalimbali umethibitisha kwamba wagonjwa wanaotegemezwa kihisia hawashuki moyo sana na hawapati maumivu mengi kama wale wasiotegemezwa.
Fikiria uchunguzi mwingine uliokazia jinsi tumaini au kutokuwa na tumaini kunavyowaathiri watu wenye ugonjwa wa mishipa ya moyo. Wanaume zaidi ya 1,300 walichunguzwa kwa makini ili kubainisha ikiwa wana tumaini au hawana. Uchunguzi uliofanywa miaka kumi baadaye ulithibitisha kwamba zaidi ya asilimia 12 ya wanaume hao wanaugua ugonjwa fulani wa mishipa ya moyo. Kati ya hao, wale ambao hawakuwa na tumaini walikuwa maradufu ya wale waliokuwa na tumaini. Profesa-msaidizi wa afya na tabia katika Shule ya Afya ya Umma ya Harvard, Laura Kubzansky, anasema hivi: “Uthibitisho mwingi unaounga mkono kwamba ‘kuwa na maoni yanayofaa’ ni muhimu kwa afya hautokani na utafiti wa moja kwa moja, lakini huo ndio uchunguzi wa kwanza wa magonjwa ya moyo unaothibitisha jambo hilo.”
Uchunguzi mwingine unaonyesha kwamba wale wanaoona afya yao kuwa mbaya hawaponi upesi baada ya upasuaji kama wale wenye maoni yanayofaa. Hata imeonekana kwamba watu wenye maoni mazuri huishi kwa muda mrefu. Utafiti mmoja ulionyesha jinsi wazee wanavyoathiriwa na maoni yanayofaa na yasiyofaa kuhusu kuzeeka. Wazee walipoonyeshwa habari zinazosema kwamba uzee unaleta hekima na uzoefu, walitembea wakiwa na nguvu nyingi zaidi. Matokeo hayo yalikuwa sawa na kufanya mazoezi kwa majuma 12!
Kwa nini inaonekana kwamba tumaini na maoni mazuri huboresha afya? Huenda wanasayansi na madaktari hawaelewi vizuri akili na mwili wa wanadamu ili kujibu swali hilo kwa usahihi. Hata hivyo, wataalamu wanaochunguza jambo hilo wanaweza kutumia ujuzi wao kukisia. Kwa mfano, profesa mmoja wa mfumo wa neva anasema: “Inapendeza kuwa na furaha na tumaini. Ni hali nzuri ambayo haileti mfadhaiko mwingi, na humfanya mtu awe na afya bora. Hilo ni jambo moja ambalo watu wanaweza kujifanyia ili wajaribu kudumisha afya bora.”
Huenda madaktari fulani, wanasaikolojia, na wanasayansi wakaona maoni hayo kuwa mapya, lakini si mapya kwa wanafunzi wa Biblia. Karibu miaka 3,000 iliyopita, Mfalme Sulemani mwenye hekima aliongozwa na roho ya Mungu kuandika hivi juu ya jambo hilo: “Moyo wenye shangwe ni dawa nzuri, lakini roho iliyopondeka huikausha mifupa.” (Methali 17:22) Ona usawaziko unaoonyeshwa hapa. Mstari huo hausemi kwamba moyo wenye shangwe ni dawa ya kila ugonjwa lakini unasema tu ni “dawa nzuri.”
Kwa kweli, huenda ikafaa kuuliza, Ikiwa tumaini lingekuwa dawa, ni daktari yupi ambaye hangeipendekeza? Isitoshe, zaidi ya kuboresha afya, tumaini lina faida nyingine.
Jinsi Maoni Mazuri na Mabaya Huathiri Maisha Yako
Watafiti wamegundua kwamba watu wenye maoni mazuri hufaidika kwa njia nyingi. Wao hufaulu shuleni, kazini, na hata michezoni. Kwa mfano, uchunguzi ulifanywa kuhusu wanawake wanariadha. Makocha walitoa maoni yao kuhusu uwezo wa wanawake hao katika michezo. Wakati huohuo, wanawake hao walichunguzwa kwa makini ili kuona ikiwa wana tumaini. Matokeo yalikuwa kwamba matumaini yao yalionyesha kwa usahihi jinsi walivyofanya michezoni kuliko habari zote zilizotolewa na makocha wao. Kwa nini tumaini lina nguvu nyingi kadiri hiyo?
Uchunguzi kuhusu maoni mabaya umefunua mambo mengi. Katika miaka ya 1960, uchunguzi ulifunua habari za ajabu kuhusu tabia za wanyama na kuwafanya watafiti kubuni dhana ya “kujifunza kuwa hoi.” Waligundua kwamba wanadamu pia wanaweza kupatwa na hali hiyo. Kwa mfano, katika uchunguzi mmoja kikundi kimoja cha watu kiliwekwa mahali penye kelele na kuambiwa kwamba wanaweza kuzima kelele hizo kwa kubonyeza vidude fulani. Walifaulu kuzizima.
Kikundi cha pili kiliambiwa kifanye vivyo hivyo, lakini vidude hivyo havikufanya kazi. Kama unavyoweza kuwazia, wengi katika kikundi hicho cha pili walikata tamaa. Baadaye hata hawakutaka kuchukua hatua yoyote. Waliamini kwamba hawangefaulu hata wafanye nini. Hata katika kikundi hicho cha pili, wale waliokuwa na maoni mazuri hawakukata tamaa.
-