Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • “Fuateni Mwendo wa Ukaribishaji-Wageni”
    Mnara wa Mlinzi—1996 | Oktoba 1
    • “Fuateni Mwendo wa Ukaribishaji-Wageni”

      “Shirikini pamoja na watakatifu kulingana na mahitaji yao. Fuateni mwendo wa ukaribishaji-wageni.”—WARUMI 12:13, NW.

      1. Uhitaji wa msingi wa kibinadamu ni nini, nao waonyeshwaje?

      KUTEMBEA usiku sana katika barabara isiyo na watu katika ujirani wa kigeni kwaweza kuwa jambo lenye kufadhaisha siku hizi. Lakini kuwa katika umati bila kujua yeyote wala kutambuliwa kwaweza kuleta mkazo vilevile. Kwa kweli, sehemu muhimu ya asili ya kibinadamu ni ule uhitaji wa kushughulikiwa, wa kutakikana, na wa kupendwa. Hakuna atakaye kutendwa kama mgeni au mtu wa kutoka nje.

      2. Yehova ameandaliaje uhitaji wetu wa uandamani?

      2 Yehova Mungu, Mfanyi na Muumba wa vitu vyote, ajua vema uhitaji wa kibinadamu wa kutaka uandamani. Akiwa Mbuni wa uumbaji wake wa kibinadamu, tangu mwanzo kabisa Mungu alijua kwamba haikuwa ‘vema mtu awe peke yake,’ naye akashughulikia hilo. (Mwanzo 2:18, 21, 22) Rekodi ya Biblia imejaa vielelezo vya matendo ya fadhili ya Yehova na ya watumishi wake kuelekea wanadamu. Hilo hutuwezesha kujifunza jinsi ya ‘kufuata mwendo wa ukaribishaji-wageni,’ kwa shangwe na furaha ya wengine na kwa uradhi wetu wenyewe.—Warumi 12:13, NW.

      Kuwapenda Wageni

      3. Eleza maana ya msingi ya ukaribishaji-wageni.

      3 Neno “ukaribishaji-wageni” kama litumiwavyo katika Biblia limetafsiriwa kutoka neno la Kigiriki phi·lo·xe·niʹa, ambalo limefanyizwa kwa maneno mawili ya msingi yanayomaanisha “upendo” na “mgeni.” Hivyo, ukaribishaji-wageni humaanisha kwa msingi “kupenda wageni.” Hata hivyo, hilo si jambo rasmi tu au jambo la hisani. Huo huhusisha hisia na shauku za mtu. Kulingana na Exhaustive Concordance of the Bible ya James Strong, kitenzi phi·leʹo, humaanisha “kuwa rafiki ya (kupenda [mtu au kitu]), yaani, kuwa na shauku kwa ajili ya (ikidokeza ushikamano wa kibinafsi, likiwa jambo la maelekeo au hisia).” Basi, ukaribishaji-wageni hupita upendo unaotegemea kanuni, ambao huenda unatokana na wajibu au jukumu. Kwa kawaida huo ni wonyesho halisi wa upendo, shauku, na urafiki.

      4. Ukaribishaji-wageni uonyeshwe nani?

      4 Aonyeshwaye upendo na shauku hiyo ndiye “mgeni” (Kigiriki, xeʹnos). Huyo aweza kuwa nani? Tena, Concordance ya Strong yafasili neno xeʹnos kuwa ‘-a kigeni (kihalisi -a nchi nyingine, au kusema kitamathali -pya); kwa kudokeza mtu aliyealikwa au (vilevile) mgeni.’ Kwa hiyo ukaribishaji-wageni, kama uonyeshwavyo katika Biblia, waweza kuonyesha fadhili kumwelekea mtu fulani tumpendaye, au waweza kuonyeshwa hata kwa mtu aliye mgeni kabisa. Yesu alieleza hivi: “Maana mkiwapenda wanaowapenda ninyi, mwapata thawabu gani? Hata watoza ushuru, je! nao hawafanyi yayo hayo? Tena mkiwaamkia ndugu zenu tu, mnatenda tendo gani la ziada? Hata watu wa mataifa, je! nao hawafanyi kama hayo?” (Mathayo 5:46, 47) Ukaribishaji-wageni halisi hupita migawanyiko na upendeleo utokanao na ubaguzi na hofu.

      Yehova, Mkaribishaji-Wageni Mkamilifu

      5, 6. (a) Yesu alimaanisha nini aliposema, “Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu”? (b) Ukarimu wa Yehova huonekanaje?

      5 Baada ya kuonyesha upungufu mbalimbali wa upendo ambao wanadamu huonyeshana, kama ilivyoonyeshwa juu, Yesu aliongeza maneno haya: “Basi ninyi mtakuwa wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu.” (Mathayo 5:48) Bila shaka, Yehova ni mkamilifu kwa kila njia. (Kumbukumbu la Torati 32:4) Hata hivyo, Yesu alikuwa akikazia sehemu moja hasa ya ukamilifu wa Yehova, kama alivyosema mapema: “[Mungu] huwaangazia jua lake waovu na wema, huwanyeshea mvua wenye haki na wasio haki.” (Mathayo 5:45) Kuhusu jambo la kuonyesha fadhili, Yehova hana upendeleo.

      6 Akiwa Muumba, Yehova ndiye mwenye kila kitu. “Maana kila hayawani ni wangu, na makundi juu ya milima elfu. Nawajua ndege wote wa milima, na wanyama wote wa mashamba ni wangu,” asema Yehova. (Zaburi 50:10, 11) Hata hivyo, yeye hajiwekei chochote kwa ubinafsi. Katika ukarimu wake, yeye huandalia viumbe vyake vyote. Mtunga-zaburi alisema hivi juu ya Yehova: “Waufumbua mkono wako, wakishibisha kila kilicho hai matakwa yake.”—Zaburi 145:16.

      7. Twaweza kujifunza nini kutokana na njia ambayo Yehova huwatendea wageni na wale wenye uhitaji?

      7 Yehova huwapa watu wanachohitaji—hata watu wasiomjua, walio wageni kwake. Paulo na Barnaba waliwakumbusha waabudu-sanamu katika jiji la Listra kwamba Yehova “hakujiacha pasipo ushuhuda, kwa kuwa alitenda mema, akiwapeni mvua kutoka mbinguni, na nyakati za mavuno, akiwashibisha mioyo yenu chakula na furaha.” (Matendo 14:17) Yehova ni mwenye fadhili na mkarimu, hasa kuelekea wale wenye uhitaji. (Kumbukumbu la Torati 10:17, 18) Twaweza kujifunza mengi kutokana na Yehova katika kuonyesha fadhili na ukarimu—kuwa wakaribishaji-wageni—kwa wengine.

      8. Yehova ameonyeshaje ukarimu wake katika kushughulikia mahitaji yetu ya kiroho?

      8 Zaidi ya kuandaa mahitaji ya kimwili ya viumbe wake kwa wingi, Yehova hushughulikia mahitaji yao kwa njia ya kiroho. Yehova alitenda katika njia ya wema zaidi kwa ajili ya hali njema yetu ya kiroho, hata kabla ya yeyote wetu kutambua kwamba tulikuwa katika hali mbaya sana kiroho. Twasoma hivi kwenye Warumi 5:8, 10: “Mungu aonyesha pendo lake yeye mwenyewe kwetu sisi, kwa kuwa Kristo alikufa kwa ajili yetu, tulipokuwa tungali wenye dhambi. . . . Tulipokuwa adui tulipatanishwa na Mungu kwa mauti ya Mwana wake.” Uandalizi huo huwawezesha wanadamu wenye dhambi kuingia katika uhusiano wa kifamilia wenye furaha pamoja na Baba yetu wa kimbingu. (Warumi 8:20, 21) Yehova pia alihakikisha kwamba tunaandaliwa mwongozo na mwelekezo ufaao ili kwamba tuweze kufanya maisha yafanikiwe licha ya hali yetu yenye dhambi na ya kutokamilika.—Zaburi 119:105; 2 Timotheo 3:16.

      9, 10. (a) Kwa nini twaweza kusema kwamba Yehova ndiye mkaribishaji-wageni mkamilifu? (b) Waabudu wa kweli wapaswa kumwigaje Yehova katika hilo?

      9 Kwa kufikiria hilo, twaweza kusema kwamba Yehova kwa kweli ndiye mkaribishaji-wageni mkamilifu katika njia nyingi sana. Yeye hawapuuzi wale wenye uhitaji, wale wenye hali ya chini, na wanyonge. Yeye huonyesha upendezi na ufikirio halisi kwa ajili ya wageni, hata kwa ajili ya adui zake, naye hatafuti zawadi yoyote ya kimwili. Katika yote hayo, je, yeye siye kielelezo kikuu zaidi cha mkaribishaji-wageni mkamilifu?

      10 Akiwa Mungu mwenye fadhili-upendo na mkarimu hivyo, Yehova hutaka waabudu wake wamwige yeye. Kotekote katika Biblia, twaona vielelezo vyenye kutokeza vya sifa hiyo yenye fadhili. Kichapo Encyclopaedia Judaica chaonelea kwamba “katika Israeli la kale, ukaribishaji-wageni haukuwa tu jambo la adabu njema, bali la sheria ya kiadili . . . Desturi za kibiblia za kumkaribisha msafiri mchovu na kumpokea mgeni kulikuwa chanzo ambacho kutoka hicho ukaribishaji-wageni na pande zao zote zilisitawi kuwa wema-adili uliostahiwa sana katika mapokeo ya Kiyahudi.” Zaidi ya kuwa alama ya kutambulisha taifa au kikundi cha kikabila chochote hususa, ukaribishaji-wageni wapaswa kuwa sifa ya kutambulisha waabudu wote wa kweli wa Yehova.

      Akiwa Mkaribishaji-Wageni wa Malaika

      11. Ni kielelezo gani chenye kutokeza kionyeshacho kwamba ukaribishaji-wageni ulileta baraka zisizotazamiwa? (Ona pia Mwanzo 19:1-3; Waamuzi 13:11-16.)

      11 Mojapo masimulizi yajulikanayo sana ya Biblia juu ya wonyesho wa ukaribishaji-wageni ni lile la Abrahamu na Sara walipokuwa wamepiga kambi kati ya miti mikubwa ya Mamre, karibu na Hebroni. (Mwanzo 18:1-10; 23:19) Bila shaka mtume Paulo alikuwa akifikiria tukio hilo alipotoa onyo hili la upole: “Msisahau ukaribishaji-wageni, kwa maana kupitia huo wengine, bila kujulikana kwao wenyewe, waliwapokea malaika.” (Waebrania 13:2, NW) Uchunguzi wa simulizi hilo utatusaidia kuona kwamba ukaribishaji-wageni si jambo la desturi tu au la malezi. Bali, ni sifa ya kimungu iletayo baraka za ajabu.

      12. Abrahamu alionyeshaje upendo wake kwa wageni?

      12 Mwanzo 18:1, 2 hudokeza kwamba wageni hao hawakujulikana wala hawakutazamiwa na Abrahamu, sawa tu na kusema wageni watatu tu walikuwa wakipitia huko. Kulingana na wafafanuzi fulani, desturi ya Watu wa Mashariki ilikuwa kwamba msafiri katika nchi ngeni alikuwa na haki ya kutazamia ukaribishaji-wageni hata ikiwa hakujua mtu yeyote huko. Lakini Abrahamu hakungoja wageni watumie haki yao; alichukua hatua ya kwanza. Yeye “alipiga mbio” ili kuwalaki wageni hao waliokuwa mbali naye—yote hayo aliyafanya “mchana wakati wa hari,” naye Abrahamu alikuwa na umri wa miaka 99! Je, hilo halionyeshi sababu ya Paulo kumrejezea Abrahamu kwa njia isiyo ya moja kwa moja kuwa kigezo cha kufuatwa nasi? Hiyo ndiyo maana hasa ya ukaribishaji-wageni, kupendezwa na wageni au kuonyesha upendo kuelekea wageni, kuhangaikia mahitaji yao. Huo ni sifa chanya.

      13. Kwa nini Abrahamu “aliinama mpaka nchi” mbele ya wale waliozuru?

      13 Hilo simulizi latuambia pia kwamba baada ya kukutana na hao wageni, Abrahamu “akainama mpaka nchi.” Kuinamia watu ambao ni wageni kabisa? Kuinama, kama alivyofanya Abrahamu, kulikuwa njia ya kumsalimu mtu mwenye kuheshimiwa aliyekaribishwa au mtu mwenye wadhifa wa juu, nako kwapaswa kutofautishwa na tendo la ibada, ambalo ni la Mungu tu. (Linganisha Matendo 10:25, 26; Ufunuo 19:10.) Kwa kuinama, si kuinamisha kichwa tu bali kwa kuinama “mpaka nchi,” Abrahamu aliwapa wageni hao heshima ya kuwa watu wa maana. Yeye alikuwa kichwa cha familia kubwa ya kiukoo iliyositawi, na bado aliwaona wageni hao kuwa wastahilio heshima kubwa zaidi kuliko yeye mwenyewe. Hiyo ni tofauti kama nini na desturi ya kushuku wageni, ule mtazamo wa ngoja-tuone! Kwa kweli Abrahamu alionyesha maana ya taarifa hii: “Kwa heshima mkiwatanguliza wenzenu.”—Warumi 12:10.

      14. Ni jitihada na dhabihu zipi zilizohusika katika kule kuonyesha kwa Abrahamu ukaribishaji-wageni?

      14 Sehemu iliyosalia ya hilo simulizi yaonyesha kwamba hisia za Abrahamu zilikuwa halisi. Mlo wenyewe ulikuwa wenye kutokeza. Hata katika nyumba kubwa yenye mifugo mingi, “ndama wa ng’ombe aliye laini, mzuri” si mlo wa kila siku. Kuhusu desturi zilizoenea za eneo hilo, Daily Bible Illustrations cha John Kitto chaonelea hivi: “Watu hawakujihusisha katika starehe ila tu kwenye misherehekeo fulani, au mgeni afikapo; na ni katika pindi hizo tu kwamba nyama huliwa, hata na wale wenye makundi na mifugo mingi.” Tabia ya nchi yenye joto haikuruhusu chakula chochote kiwezacho kuharibika upesi kuhifadhiwa, kwa hiyo kuandaa mlo kama huo, kila kitu kilihitaji kufanywa papo hapo. Haishangazi kwamba katika simulizi hili fupi, neno “hima” au “himiza” laonekana mara tatu, naye Abrahamu “alipiga mbio” kihalisi ili kutayarisha huo mlo!—Mwanzo 18:6-8.

      15. Ni nini maoni yafaayo juu ya maandalizi ya kimwili katika kuonyesha ukaribishaji-wageni, kama ilivyotolewa kielelezo na Abrahamu?

      15 Hata hivyo, kusudi si kuandaa tu karamu kubwa ili kumvutia mtu. Ingawa Abrahamu na Sara walijitahidi sana kutayarisha na kuandaa huo mlo, ona jinsi Abrahamu alivyorejezea jambo hilo mapema: “Na yaletwe basi maji kidogo mkanawe miguu, mkapumzike chini ya mti huu. Nami nitaleta chakula kidogo, mkaburudishe moyo, baadaye mwendelee, iwapo mmemjia mtumwa wenu.” (Mwanzo 18:4, 5) “Chakula [hicho] kidogo” kikawa karamu ya ndama aliyenona pamoja na mikate ya unga safi, siagi, na maziwa—karamu istahiliyo mfalme. Somo ni nini? Ukaribishaji-wageni uonyeshwapo, jambo la maana, au lipaswalo kukaziwa, si jinsi chakula na vinywaji vitakavyokuwa vingi, au ni vitumbuizo gani vyenye madoido vitakavyoandaliwa, na kadhalika. Ukaribishaji-wageni hautegemei ikiwa mtu anaweza kununua vitu vya bei ghali. Bali, hutegemea hangaikio halisi la hali njema ya wengine na ile tamaa ya kufanyia wengine mema kwa kadiri mtu awezavyo. “Chakula cha mboga penye mapendano; ni bora kuliko ng’ombe aliyenona pamoja na kuchukiana,” yasema mithali ya Biblia, na katika hiyo mna ufunguo wa ukaribishaji-wageni halisi.—Mithali 15:17.

      16. Abrahamu alionyeshaje uthamini kwa ajili ya vitu vya kiroho katika yale aliyowafanyia wale waliozuru?

      16 Hata hivyo, twapaswa kutambua kwamba kulikuwa na dokezo la kiroho katika kisa chote. Kwa njia fulani Abrahamu alitambua kwamba hao waliozuru walikuwa wajumbe kutoka kwa Yehova. Hilo laonyeshwa kwa kule kuongea kwake nao kwa maneno haya: “Bwana wangu [“Yehova,” NW], kama nimeona fadhili machoni pako nakuomba usinipite sasa mimi mtumwa wako.”a (Mwanzo 18:3; linganisha Kutoka 33:20.) Abrahamu hakujua mapema ikiwa walikuwa na ujumbe wake au ikiwa walikuwa wakipitia tu mahali hapo. Hata hivyo, aling’amua kwamba utimizo wa kusudi la Yehova ulikuwa ukitendeka. Watu hao walikuwa katika utume fulani kutoka kwa Yehova. Yeye angefurahia kufanya lolote ili kuchangia hilo. Alitambua kwamba watumishi wa Yehova wanastahili kilicho bora zaidi, naye angeandaa kilicho bora zaidi chini ya hali hizo. Kwa kufanya hivyo, kungekuwa na baraka ya kiroho, iwe ni kwake mwenyewe au kwa mtu mwingine. Kama ilivyotokea, Abrahamu na Sara walibarikiwa kwa njia kubwa sana kwa ajili ya ukaribishaji-wageni wao wa moyo mweupe.—Mwanzo 18:9-15; 21:1, 2.

      Watu Walio Wakaribishaji-Wageni

      17. Yehova alitaka nini kutoka kwa Waisraeli kuhusiana na wageni na walio na uhitaji miongoni mwao?

      17 Kielelezo chenye kutokeza cha Abrahamu hakikupaswa kusahauliwa na taifa lililotokana naye. Sheria ambayo Yehova aliwapa Waisraeli ilitia ndani maandalizi ya kuonyesha ukaribishaji-wageni kuelekea wageni miongoni mwao. “Mgeni akaaye pamoja nawe atakuwa kama mzalia kwenu; mpende kama nafsi yako; kwa maana ninyi mlikuwa wageni katika nchi ya Misri; Mimi ndimi BWANA, Mungu wenu.” (Mambo ya Walawi 19:34) Watu walipaswa kuwatolea ufikirio wa pekee wale wenye uhitaji wa utegemezo wa kimwili na kutowapuuza tu. Yehova alipowabariki kwa mavuno mengi, waliposhangilia katika misherehekeo yao, walipopata pumziko kutoka kwa kazi zao katika miaka ya Sabato, na kwenye pindi nyinginezo, watu walipaswa kuwakumbuka wale ambao hawakuwa na mafanikio kama wao—wajane, mayatima, na wakazi-wageni.—Kumbukumbu la Torati 16:9-14; 24:19-21; 26:12, 13.

      18. Ukaribishaji-wageni ni wa maana kadiri gani kuhusu kupokea kibali na baraka za Yehova?

      18 Umaana wa fadhili, ukarimu, na ukaribishaji-wageni kuelekea wengine, hasa kuelekea wale wenye uhitaji, waweza kuonwa katika njia ambayo Yehova alishughulika na Waisraeli walipopuuza kudhihirisha sifa hizo. Yehova alijulisha wazi kwamba fadhili na ukarimu kuelekea wageni na walio na uhitaji ni baadhi ya matakwa kwa watu wake ili wapokee baraka zake kwa kuendelea. (Zaburi 82:2, 3; Isaya 1:17; Yeremia 7:5-7; Ezekieli 22:7; Zekaria 7:9-11) Taifa lilipokuwa lenye bidii katika kutimiza matakwa hayo na mengineyo, lilisitawi na kufurahia wingi wa vitu vya kimwili na kiroho. Walipojihusisha sana katika mifuatio ya kibinafsi ya kujipendelea na kupuuza kuonyesha sifa hizo zenye fadhili kwa wale wenye uhitaji, walipokea laana ya Yehova, na hatimaye hukumu kali ilitolewa juu yao.—Kumbukumbu la Torati 27:19; 28:15, 45.

      19. Ni lazima tuchunguze nini zaidi?

      19 Jinsi ilivyo muhimu, basi, tujichunguze wenyewe na kuona ikiwa twaishi kupatana na matazamio ya Yehova katika jambo hili! Hilo ni la maana hasa leo kwa kufikiria ile roho ya ulimwengu yenye ubinafsi na ya kugawanya. Twaweza kuonyeshaje ukaribishaji-wageni wa Kikristo katika ulimwengu uliogawanyika? Hiyo ndiyo habari inayozungumziwa katika makala ifuatayo.

  • Ukaribishaji-Wageni wa Kikristo Katika Ulimwengu Uliogawanyika
    Mnara wa Mlinzi—1996 | Oktoba 1
    • Ukaribishaji-Wageni wa Kikristo Katika Ulimwengu Uliogawanyika

      “Kwa hiyo, sisi, tuko chini ya wajibu wa kuwapokea watu wa namna hiyo kwa ukaribishaji-wageni, ili tupate kuwa wafanyakazi wenzi katika kweli.”—3 YOHANA 8, NW.

      1. Muumba amewapa wanadamu zawadi zipi zenye kutamanika zaidi?

      “MWANADAMU hana neno lo lote lililo jema chini ya jua, kuliko kula, na kunywa, na kucheka; na [ya kuwa] hilo likae naye katika amali yake, siku zote za maisha yake alizompa Mungu chini ya jua.” (Mhubiri 8:15) Kwa maneno hayo mkutanishi Mwebrania wa kale hutuambia kwamba Yehova Mungu hataki tu viumbe vyake vya kibinadamu viwe vyenye shangwe na furaha bali pia yeye huandaa njia ili viwe hivyo. Katika historia yote ya binadamu tamaa moja ya kawaida miongoni mwa watu kila mahali yaonekana kuwa ni kujifurahisha na kuwa na wakati mzuri.

      2. (a) Wanadamu wametumiaje vibaya yale aliyowakusudia Yehova? (b) Tokeo ni nini?

      2 Leo twaishi katika jamii ya anasa ambayo katika hiyo watu wanajishughulisha na ufuatiaji wa anasa mbalimbali na nyakati nzuri. Watu walio wengi wamekuwa “wenye kujipenda wenyewe, . . . wapendao anasa kuliko kumpenda Mungu,” kama ilivyotabiriwa katika Biblia. (2 Timotheo 3:1-4) Hilo bila shaka, ni upotovu mkubwa wa yale aliyokusudia Yehova Mungu. Kufuatia nyakati nzuri kunapokuwa kusudi kuu, au kujipendeza kunapokuwa lengo la pekee, hakuna uradhi wa kweli, na ‘mambo yote yanakuwa ubatili na kujilisha upepo.’ (Mhubiri 1:14; 2:11) Likiwa tokeo dunia imejawa na watu wapweke na waliotamaushwa, jambo ambalo huongoza kwenye yaliyo mengi ya matatizo katika jamii. (Mithali 18:1) Watu wanakuwa wenye kushukiana na wanagawanyika kirangi, kikabila, kijamii, na kiuchumi.

      3. Twaweza kupataje shangwe na uradhi wa kweli?

      3 Jinsi mambo yangekuwa tofauti ikiwa watu wangeiga njia ya Yehova ya kushughulika na wengine—kuwa wenye fadhili, wenye ukarimu, na wakaribishaji-wageni! Alijulisha wazi kwamba siri ya kupata furaha ya kweli haimo katika kujaribu kwetu kuridhisha tamaa zetu wenyewe. Bali, huu ndio ufunguo: “Ni heri kutoa kuliko kupokea.” (Matendo 20:35) Ili kupata shangwe na uradhi wa kweli, lazima tushinde vizuizi na migawanyiko iwezayo kutuwekea mipaka. Na lazima tuwafikie wale wanaomtumikia Yehova pamoja nasi. Ni muhimu tutii shauri hili: “Kwa hiyo, sisi, tuko chini ya wajibu wa kuwapokea watu wa namna hiyo kwa ukaribishaji-wageni, ili tupate kuwa wafanyakazi wenzi katika kweli.” (3 Yohana 8, NW) Kuonyesha ukaribishaji-wageni kwa wanaostahili, kwa kadiri hali zetu zinavyoruhusu, kuna faida katika njia mbili—hufaidi watoaji pamoja na wapokeaji. Ni nani basi, walio miongoni mwa wanaostahili tupaswao ‘kuwapokea kwa ukaribishaji-wageni’?

      “Kuwatazama Yatima na Wajane”

      4. Ni badiliko gani katika mahusiano ya familia ambalo huonekana hata miongoni mwa baadhi ya watu wa Yehova?

      4 Familia imara na ndoa zenye furaha ni adimu leo. Viwango vinavyoongezeka vya talaka na idadi inayoongezeka ya akina mama wasioolewa ulimwenguni pote imeibadili sana familia ya msingi. Likiwa tokeo, wengi ambao wamekuwa Mashahidi wa Yehova katika miaka ya majuzi wanatoka familia zilizovunjika. Ama wametalikana ama wametengana na wenzi wao wa ndoa, au wanaishi katika familia za mzazi mmoja. Kwa kuongezea, kama vile Yesu alivyotabiri, kweli aliyofundisha imetokeza migawanyiko katika familia nyingi.—Mathayo 10:34-37; Luka 12:51-53.

      5. Yesu alisema nini ambacho kingeweza kuwa chanzo cha kitia-moyo kwa wale walio katika familia zilizogawanyika?

      5 Kuona wapya wakichukua msimamo imara kwa ajili ya kweli huchangamsha mioyo yetu, nasi mara nyingi huwafariji kwa ahadi hii ya Yesu yenye kutia moyo: “Amin, nawaambieni, Hakuna mtu aliyeacha nyumba, au ndugu waume, au ndugu wake, au mama, au baba, au watoto, au mashamba, kwa ajili yangu, na kwa ajili ya Injili, ila atapewa mara mia sasa wakati huu, nyumba, na ndugu waume, na ndugu wake, na mama, na watoto, na mashamba, pamoja na udhia; na katika ulimwengu ujao uzima wa milele.”—Marko 10:29, 30.

      6. Twaweza kuwaje ‘ndugu, [“dada,” NW], mama, na watoto’ kwa “yatima na wajane” walio miongoni mwetu?

      6 Hata hivyo, ‘ndugu na [“dada na,” NW] mama na watoto’ ni akina nani? Kule kuona tu idadi kubwa ya watu kwenye Jumba la Ufalme, mara nyingi wakiwa watu mia moja au zaidi, wanaojiita wenyewe ndugu na dada hakumfanyi mtu ahisi mara moja kuwa hao ni ndugu, dada, mama, na watoto wake. Fikiria hoja hii: Mwanafunzi Yakobo anatukumbusha kwamba ili ibada yetu iwe yenye kukubalika kwa Yehova, ni lazima ‘tuwatazame yatima na wajane katika dhiki yao, na kujilinda na dunia pasipo mawaa.’ (Yakobo 1:27) Hilo lamaanisha kwamba hatupaswi kuruhusu mitazamo ya kilimwengu ya kujivuna kwa sababu ya kuwa matajiri na kuwa wa matabaka ya juu ya kijamii, ifunge mlango wetu wa huruma kuelekea “yatima na wajane.” Badala ya hivyo, ni lazima tuchukue hatua ya kwanza ya kuwaonyesha ushirika na ukaribishaji-wageni wetu.

      7. (a) Kusudi halisi la kuwa wenye ukaribishaji-wageni kuelekea “yatima na wajane” ni nini? (b) Ni nani pia wawezao kushiriki katika kuonyesha ukaribishaji-wageni wa Kikristo?

      7 Kuwaonyesha “yatima na wajane” ukaribishaji-wageni hakuhusishi sikuzote kuwapa wanayokosa kimwili. Familia za mzazi mmoja au zilizogawanyika kidini si lazima ziwe katika hali ngumu kifedha. Hata hivyo, ushirika wenye kujenga, mazingira ya familia, kushirikiana na watu wa umri mbalimbali, na kule kushiriki mambo mazuri ya kiroho—hizi ni sehemu mbalimbali za maisha zinazothaminika. Hivyo, tukumbukapo kwamba jambo la maana, si ukubwa wa pindi, bali roho ya upendo na muungano, yapendeza kama nini kwamba nyakati nyingi, hata “yatima na wajane” waweza kushiriki katika kuwaonyesha Wakristo wenzao ukaribishaji-wageni!—Linganisha 1 Wafalme 17:8-16.

      Je, Kuna Watu wa Kigeni Miongoni Mwetu?

      8. Ni badiliko gani lionekanalo katika makutaniko mengi ya Mashahidi wa Yehova?

      8 Twaishi katika wakati wa uhamaji wa watu wengi. “Zaidi ya watu milioni 100 ulimwenguni pote wanaishi katika nchi ambazo wao si wananchi wazo, na watu milioni 23 wamelazimika kuhama kutoka nyumbani katika nchi zao wenyewe,” lasema World Press Review. Tokeo la moja kwa moja la jambo hilo limekuwa kwamba katika maeneo mengi, hasa katika majiji makubwa-makubwa, makutaniko ya watu wa Yehova ambayo wakati mmoja yalifanyizwa kwa kiasi kikubwa na watu wa jamii au taifa moja sasa yana watu kutoka sehemu tofauti-tofauti za ulimwengu. Huenda hilo ni kweli kuhusu mahali ulipo. Hata hivyo, tuwaoneje watu hao “wa nchi nyingine” na “watu wa kigeni,” jinsi huenda ulimwengu ukawaita wale, ambao lugha yao, desturi zao, na mtindo-maisha wao huenda ukatofautiana na wetu?

      9. Ni mitego gani mizito iwezayo kutunasa kuhusiana na maoni juu ya “watu wa nchi nyingine” na “watu wa kigeni” waingiao katika kutaniko la Kikristo?

      9 Kwa usahili, hatupaswi kuruhusu mielekeo yoyote ya kuhofu wageni itufanye tuhisi kwamba kwa njia fulani twastahili zaidi lile pendeleo la kuijua kweli kuliko wale wanaotoka katika nchi ngeni au zile ziitwazo isivyofaa nchi za kipagani; wala hatupaswi kuhisi kana kwamba wageni hao wanahalifu utumizi wa Jumba la Ufalme au majengo mengineyo. Mtume Paulo alilazimika kuwakumbusha Wakristo Wayahudi fulani wa karne ya kwanza, waliokuwa na maoni kama hayo, kwamba kwa kweli hakuna aliyekuwa mwenye kustahili; ilikuwa fadhili isiyostahiliwa ya Mungu iliyofanya iwezekane kwa mtu yeyote kupata wokovu. (Warumi 3:9-12, 23, 24) Twapaswa kushangilia kwamba fadhili isiyostahiliwa ya Mungu sasa yawafikia watu wengi sana ambao, kwa njia moja au nyingine, walikuwa wamenyimwa fursa ya kusikia habari njema. (1 Timotheo 2:4) Twaweza kuonyeshaje kwamba twawapenda kihalisi?

      10. Twaweza kuonyeshaje kwamba tuna ukaribishaji-wageni halisi kuelekea “watu wa kigeni” walio miongoni mwetu?

      10 Twaweza kufuata onyo hili la upole la Paulo: “Mkaribishane ninyi kwa ninyi, kama naye Kristo alivyotukaribisha, ili Mungu atukuzwe.” (Warumi 15:7) Kung’amua kwamba watu kutoka nchi na malezi mengine mara nyingi hukosa mahitaji ya msingi twapaswa kuwaonyesha fadhili na hangaikio tuwezapo kufanya hivyo. Twapaswa kuwakaribisha miongoni mwetu, kutendea kila mmoja wao kama “mzali[w]a kwenu” na “mpende kama nafsi yako.” (Mambo ya Walawi 19:34) Huenda hilo lisiwe rahisi kufanya, lakini tutafanikiwa tukikumbuka shauri hili: “Wala msiifuatishe namna ya dunia hii; bali mgeuzwe kwa kufanywa upya nia zenu, mpate kujua hakika mapenzi ya Mungu yaliyo mema, ya kumpendeza, na ukamilifu.”—Warumi 12:2.

      Shiriki Pamoja na Watakatifu

      11, 12. Ni ufikirio gani wa pekee waliotolewa watumishi fulani wa Yehova katika (a) Israeli la kale (b) karne ya kwanza?

      11 Miongoni mwa wale wanaostahili kwelikweli ufikirio na ukaribishaji-wageni wetu ni Wakristo wakomavu wanaofanya kazi kwa bidii kwa ajili ya hali njema yetu ya kiroho. Yehova aliwatolea maandalizi ya pekee makuhani na Walawi katika Israeli la kale. (Hesabu 18:25-29) Katika karne ya kwanza, Wakristo walisihiwa sana pia kuwashughulikia wale waliowatumikia katika nyadhifa za pekee. Simulizi kwenye 3 Yohana 5-8 latuonyesha kidogo kile kifungo chenye ukaribu cha upendo kilichokuwako miongoni mwa Wakristo wa mapema.

      12 Mtume Yohana aliyekuwa amezeeka alithamini sana fadhili na ukaribishaji-wageni ambao Gayo alikuwa ameonyesha ndugu wasafirio fulani waliotumwa kuzuru kutaniko. Ndugu hao—kutia na Demetrio, ambaye yaonekana ndiye aliyepeleka barua ya Yohana—wote walikuwa wageni au wasiojulikana na Gayo hapo awali. Lakini walipokewa kwa ukaribishaji-wageni kwa sababu ilikuwa “kwa ajili ya Jina [la Mungu] hilo, walitoka.” Yohana alieleza hilo hivi: “Basi imetupasa sisi kuwakaribisha watu kama hao, ili tuwe watenda kazi pamoja na kweli.”—3 Yohana 1, 7, 8.

      13. Ni nani miongoni mwetu leo wanaostahili hasa kupokewa kwa ‘ukaribishaji-wageni’?

      13 Leo, katika tengenezo la Yehova, kuna wengi wanaojitahidi sana kwa niaba ya ushirika wote wa ndugu. Hao wanatia ndani waangalizi wasafirio, wanaotumia wakati na nishati zao juma baada ya juma katika kujenga makutaniko; wamishonari, wanaoacha familia na marafiki ili wahubiri katika nchi za kigeni; wale wanaotumika katika makao ya Betheli au ofisi za tawi, wanaotoa kwa hiari utumishi wao mbalimbali ili kutegemeza kazi ya kuhubiri ya ulimwenguni pote; na wale walio katika utumishi wa upainia, wanaotumia sehemu kubwa ya wakati na nishati zao katika huduma ya shambani. Kwa msingi, wote hao hufanya kazi kwa bidii, si kwa ajili ya utukufu au faida zozote za kibinafsi, bali kutokana na upendo kwa udugu wa Kikristo na kwa Yehova. Wao wanastahili kuigwa nasi kwa sababu ya ujitoaji wao wa nafsi yote na wanastahili ‘kupokewa kwa ukaribishaji-wageni.’

      14. (a) Tunakuwaje Wakristo bora tuwaonyeshapo waaminifu ukaribishaji-wageni? (b) Kwa nini Yesu alisema kwamba Mariamu alichagua “fungu lililo zuri”?

      14 ‘Tuwapokeapo watu wa namna hiyo kwa ukaribishaji-wageni,’ mtume Yohana alionyesha kwamba, ‘tunapata kuwa wafanyakazi wenzi katika kweli.’ (NW) Likiwa tokeo, kwa njia fulani tunakuwa Wakristo bora zaidi. Hilo ni kwa sababu kazi za Kikristo hutia ndani kuwafanyia waamini wenzetu mema. (Mithali 3:27, 28; 1 Yohana 3:18) Kuna thawabu katika njia nyingine pia. Mariamu na Martha walipompokea Yesu nyumbani mwao, Martha alitaka kuwa mkaribishaji-wageni mzuri kwa kumwandalia Yesu “vitu vingi.” Mariamu alionyesha ukaribishaji-wageni katika njia tofauti. Yeye ‘aliketi miguuni pake Yesu, akasikiliza maneno yake,’ naye Yesu alimpongeza kwa sababu ya kuchagua “fungu lililo jema.” (Luka 10:38-42) Maongezi na mazungumzo pamoja na wale walio na miaka mingi ya uzoefu mara nyingi huwa ndiyo mambo makuu ya jioni inayotumiwa pamoja nao.—Warumi 1:11, 12.

      Kwenye Pindi za Pekee

      15. Ni pindi zipi za pekee huenda zikathibitika kuwa nyakati za furaha kwa watu wa Yehova?

      15 Ingawa Wakristo wa kweli hawafuati desturi zijulikanazo sana wala hawaadhimishi sikukuu na misherehekeo ya kilimwengu, kuna pindi wanapokusanyika pamoja ili kufurahia ushirika wa mmoja na mwenzake. Kwa kielelezo, Yesu alihudhuria karamu ya ndoa katika Kana na akachangia shangwe ya pindi hiyo kwa kufanya muujiza wake wa kwanza huko. (Yohana 2:1-11) Vivyo hivyo leo, watu wa Yehova wanakuwa na nyakati za furaha pamoja kwenye pindi za pekee kama hizo, na miadhimisho na misherehekeo ifaayo huchanga mengi kwenye matukio hayo. Hata hivyo, ni mambo gani yafaayo?

      16. Ni miongozo gani tuliyo nayo kuhusu mwenendo ufaao hata wakati wa pindi za pekee?

      16 Kutokana na funzo letu la Biblia, twajifunza mwenendo uwafaao Wakristo, nao ndio tuufuatao nyakati zote. (Warumi 13:12-14; Wagalatia 5:19-21; Waefeso 5:3-5) Vikusanyiko vya kirafiki, viwe vyahusiana na arusi au kwa kusudi jingine lolote, havituruhusu kuacha viwango vyetu vya Kikristo au kufanya jambo ambalo kwa kawaida hatungefanya; wala hatuko chini ya wajibu kufuata desturi zote za nchi tunamoishi. Nyingi za desturi hizo zinategemea mazoea ya dini isiyo ya kweli au ushirikina, na nyingine huhusisha mwenendo ambao kwa wazi haukubaliwi na Wakristo.—1 Petro 4:3, 4.

      17. (a) Ni mambo gani yanayoonyesha kwamba ile karamu ya arusi katika Kana ilikuwa na mpango mzuri na ilisimamiwa ifaavyo? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba Yesu alikubali pindi hiyo?

      17 Tusomapo Yohana 2:1-11 (NW), si vigumu kwetu kuona kwamba tukio hilo lilikuwa limepangwa vizuri na kwamba idadi kubwa sana ya wageni ilikuwapo. Hata hivyo, Yesu na wanafunzi wake walikuwa wageni ‘walioalikwa’; wao hawakudoea, ingawa angalau baadhi yao yamkini walikuwa watu wa ukoo wa mkaribishaji-wageni. Twaona pia kwamba kulikuwa na wale waliokuwa “watumishi” na vilevile “mwelekezi” (NW), ambaye angetoa mielekezo juu ya kilichoandaliwa au kufanywa. Yote hayo yaonyesha kwamba tukio hilo lilikuwa na mpango mzuri na lilisimamiwa ifaavyo. Simulizi lamalizia kwa kutaarifu kwamba kwa lile alilofanya kwenye karamu hiyo, Yesu ‘aliudhihirisha utukufu wake.’ Je, angeamua kufanya hivyo kwenye pindi hiyo ikiwa ingekuwa karamu yenye makelele na isiyodhibitiwa? Bila shaka la.

      18. Twapaswa kufikiria nini kwa uzito kuhusiana na tukio lolote la kijamii?

      18 Basi, namna gani pindi zozote za pekee ambazo huenda tukaandaa? Twataka kukumbuka kwamba kusudi la kupokea wengine kwa ukaribishaji-wageni ni ili tupate kuwa “wafanyakazi wenzi katika kweli.” (NW) Hivyo, haitoshi tu kuita tukio fulani kusanyiko la “Mashahidi.” Swali hili laweza kuulizwa, Je, kwa kweli ni ushahidi wa jinsi tulivyo na wa yale tunayoamini? Hatupaswi kamwe kuona pindi hizo kuwa fursa za kuona hatua tuwezayo kufika katika kushindana na ulimwengu na njia zayo, katika kujihusisha na “tamaa ya mwili, na tamaa ya macho, na kiburi cha uzima.” (1 Yohana 2:15, 16) Badala ya hivyo, pindi hizo zapaswa kuonyesha ifaavyo fungu letu tukiwa Mashahidi wa Yehova, na twapaswa kuwa na uhakika kwamba tunalofanya humletea Yehova utukufu na heshima.—Mathayo 5:16; 1 Wakorintho 10:31-33.

      ‘Mkaribishane Pasipo Kunung’unika’

      19. Kwa nini twahitaji ‘kukaribishana pasipo kunung’unika’?

      19 Hali za ulimwengu zizidipo kuzorota na watu kuwa wenye kugawanyika zaidi na zaidi, twahitaji kufanya yote tuwezayo ili kutia nguvu kile kifungo cha karibu kilichomo miongoni mwa Wakristo wa kweli. (Wakolosai 3:14) Kwa kusudi hilo twapaswa kuwa na “juhudi nyingi katika kupendana,” jinsi Petro alivyotusihi sana. Kisha, kwa njia yenye kutumika aliongeza hivi: “Mkaribishane ninyi kwa ninyi, pasipo kunung’unika.” (1 Petro 4:7-9) Je, tuko tayari kuchukua hatua ya kwanza ya kuwa wakaribishaji-wageni kuelekea ndugu zetu, kujitahidi kuwa wenye fadhili na wenye kusaidia? Au twanung’unika fursa kama hizo zitokeapo? Ikiwa twanung’unika, twaifuta ile shangwe ambayo tungeweza kuwa nayo na pia twapoteza ile thawabu ya furaha ya kufanya mema.—Mithali 3:27; Matendo 20:35.

      20. Ni baraka zipi zinazotungoja tukizoea ukaribishaji-wageni katika ulimwengu wa leo uliogawanyika?

      20 Kufanya kazi karibu-karibu na Wakristo wenzetu, kuwa wenye fadhili na wakaribishaji-wageni sisi kwa sisi, kutaleta baraka zisizo na mipaka. (Mathayo 10:40-42) Kwa watu wa namna hiyo Yehova aliahidi kwamba “atatanda hema yake juu yao. Hawataona njaa tena, wala hawataona kiu tena.” Kuwa hemani mwa Yehova ni kufurahia ulinzi na ukaribishaji-wageni wake. (Ufunuo 7:15, 16; Isaya 25:6) Ndiyo, taraja la kufurahia ukaribishaji-wageni wa Yehova milele liko huko mbele tu.—Zaburi 27:4; 61:3, 4.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki