Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Je, Kweli Uhai Udumuo Milele Wawezekana?
    Mnara wa Mlinzi—1999 | Aprili 15
    • 2. Watu wengi huwaza juu ya tumaini gani, na kwa nini?

      2 Ni jambo la maana kwamba The New York Times Magazine la Septemba 28, 1997, lilikuwa na makala “Wao Wataka Kuishi.” Lilimnukuu mtafiti aliyesema haya: “Kwa kweli naamini kwamba huenda tukawa kizazi cha kwanza ambacho kitaishi milele”! Huenda wewe pia unaamini kwamba uhai udumuo milele wawezekana. Huenda ukafikiri hivyo kwa sababu Biblia yaahidi kwamba twaweza kuishi milele hapa duniani. (Zaburi 37:29; Ufunuo 21:3, 4) Ingawa hivyo, watu fulani huamini kwamba uhai udumuo milele wawezekana ikitegemea sababu nyingine mbali na zile zipatikanazo katika Biblia. Kuchunguza sababu mbili kati ya hizo kutatusaidia tutambue kwamba kweli uhai udumuo milele wawezekana.

      Tumebuniwa Tuishi Milele

      3, 4. (a) Kwa nini watu wengine huamini kwamba twapaswa kuishi milele? (b) Daudi alisema nini kuhusu jinsi alivyoumbwa?

      3 Sababu moja inayowafanya watu wengi waamini kwamba wanadamu wapaswa kuishi milele yahusiana na jinsi ambavyo tumeumbwa kwa namna ya ajabu. Kwa mfano, ni jambo la kimwujiza kweli jinsi tulivyoumbwa ndani ya tumbo la uzazi la mama yetu. Mtu mmoja mwenye ujuzi juu ya hali ya kuzeeka aliandika hivi: “Baada ya kufanya miujiza inayotupata kutoka kutungwa mimba hadi kuzaliwa kisha hadi upevuko wa kingono na utu uzima, hali-asili ilichagua kutounda kile kionekanacho kuwa mfumo wa utendaji ulio sahili zaidi ambao ungedumisha miujiza hiyo milele.” Ndiyo, tufikiriapo jinsi tulivyoumbwa kimwujiza, swali hili labaki, Kwa nini inakuwa lazima tufe?

      4 Maelfu ya miaka iliyopita, Daudi, mwandishi wa Biblia, alifikiria kwa makini miujiza hiyo, ingawa hangeweza kuona kihalisi ndani ya tumbo la uzazi kama wanasayansi wawezavyo kuona leo. Daudi alitafakari juu ya jinsi alivyoumbwa alipoandika kwamba alikuwa ‘amefichwa tumboni mwa mama yake.’ Alisema ‘figo zake zilifanyizwa’ wakati huo. Pia, yeye alisema kuhusu kuumbwa kwa “mifupa” yake wakati, kama alivyosema, “Nilipoumbwa kwa siri.” Kisha Daudi akasema juu ya “kiinitete changu” na kutaarifu kuhusu kiinitete hicho katika tumbo la uzazi la mama yake hivi: “Chuoni mwako ziliandikwa zote.”—Zaburi 139:13-16, NW.

      5. Ni miujiza gani huhusika katika kufanyizwa kwetu ndani ya tumbo la uzazi?

      5 Kwa wazi, hakukuwa ramani halisi iliyoandikwa kwa mkono kwa ajili ya kufanyizwa kwa Daudi ndani ya tumbo la uzazi la mama yake. Lakini katika kutafakari kwa Daudi juu ya kufanyizwa kwa “figo” zake, “mifupa” yake, na sehemu nyingine za mwili wake, kwake ilionekana kana kwamba ukuzi wa vitu hivi uliendelea kwa mpango—kwamba kila kitu kilikuwa, kusema kitamathali, ‘kimeandikwa chuoni.’ Ilikuwa kana kwamba chembe iliyotungishwa mimba ndani ya mama yake ilikuwa na chumba kikubwa kilichojaa vitabu vikiwa na maagizo mengi mno kuhusu namna ya kufanyiza mtoto wa kibinadamu na maagizo hayo tata yakapitishwa hadi kwa kila chembe iliyokuwa ikifanyizwa. Hivyo, gazeti Science World latumia mfano wa ‘kila chembe katika kiinitete kinachokua kuwa ina kabati iliyojaa ramani.’

      6. Kuna uthibitisho gani kwamba sisi, kama alivyoandika Daudi, ‘tumeumbwa kwa jinsi ya ajabu ya kutisha’?

      6 Je, umewahi kufikiria jinsi mwili wetu unavyofanya kazi kimwujiza? Mwanabiolojia Jared Diamond alitaarifu hivi: “Sisi hubadilisha chembe zilizo ukutani mwa matumbo yetu mara moja baada ya siku chache, zile zilizo ukutani mwa kibofu cha mkojo mara moja baada ya miezi miwili, na chembe zetu nyekundu za damu mara moja kwa miezi minne.” Alimalizia kusema hivi: “Nguvu za asili zatutawanya vipande-vipande na kutuunganisha tena kila siku.” Hilo lamaanisha nini hasa? Lamaanisha kwamba haidhuru huenda tukaishi miaka mingapi—iwe 8, 80, au hata 800—mwili wetu wabaki ukiwa mchanga sana. Wakati mmoja, mwanasayansi fulani alikadiria hivi: “Kwa mwaka mmoja atomi ambazo sisi hupata kupitia hewa, chakula, na maji tunayotumia, zitachukua mahali pa zile atomi zipatazo asilimia 98 tulizo nazo sasa.” Kwa kweli, kama Daudi alivyosifu, tumeumbwa kwa “jinsi ya ajabu ya kutisha.”—Zaburi 139:14.

      7. Kwa kutegemea jinsi ambavyo miili yetu imebuniwa, watu fulani wamefikia mkataa gani?

      7 Ikitegemea muundo wa maumbile ya miili yetu, mamlaka yenye kuheshimika juu ya hali ya kuzeeka ilisema hivi: “Haiko wazi kwa nini kuzeeka kwapaswa kutokea.” Kwa kweli yaonekana kwamba twapaswa kuishi milele. Na hiyo ndiyo sababu watu wanajaribu kufikia lengo hilo kupitia tekinolojia zao. Muda mfupi uliopita, Dakt. Alvin Silverstein aliandika akiwa na uhakika katika kitabu chake Conquest of Death: “Tutavumbua mambo yanayotatanisha juu ya uhai. Tutafahamu . . . jinsi mtu anavyozeeka.” Kukiwa na matokeo gani? Alitabiri hivi: “Hakutakuwa tena na watu ‘wazee’ kwa kuwa ujuzi utakaoruhusu kushindwa kwa kifo utaleta pia ujana usio na mwisho.” Kwa kufikiria uchunguzi wa kisasa wa kisayansi kuhusu maumbile ya mwanadamu, je, wazo la uhai udumuo milele lasikika kuwa lisiloaminika? Kuna sababu nyingine yenye nguvu hata zaidi ya kuamini kwamba uhai udumuo milele wawezekana.

  • Je, Kweli Uhai Udumuo Milele Wawezekana?
    Mnara wa Mlinzi—1999 | Aprili 15
    • Makala ya gazeti The New York Times Magazine yenye kichwa “Wao Wataka Kuishi” ilizungumzia juu ya “mungu: tekinolojia” na ile “shauku juu ya uwezo wa tekinolojia.” Hata ilisemekana kwamba mtaalamu mmoja ana “uhakika kwa furaha . . . kwamba mbinu za utokezaji jeni zitapatikana mapema vya kutosha ku[tu]okoa kwa kukomesha kuzeeka, hata pengine kutokeza ujana.” Hata hivyo, kwa kweli jitihada za wanadamu za kukomesha uzee au kushinda kifo zimeshindwa kabisa.

      13. Muundo wa ubongo wetu huonyeshaje kwamba tulikusudiwa tuishi milele?

      13 Je, hilo lamaanisha kwamba hakuna njia ya kupata uhai udumuo milele? Sivyo kabisa! Njia ipo! Muundo wa ubongo wetu, ukiwa na uwezo usio na kikomo wa kujifunza mambo, wapaswa utusadikishe juu ya hilo. Mwanabiolojia wa molekuli James Watson aliuita ubongo wetu “kitu tata zaidi ambacho tumepata kugundua katika ulimwengu wetu.” Naye mtaalamu wa elimu ya mfumo wa neva Richard Restak alisema hivi: “Hakuna chochote katika ulimwengu ujulikanao kinachofanana nao hata kidogo.” Sababu gani tuwe na ubongo wenye uwezo wa kuhifadhi na kukusanya habari isiyoelekea kuwa na kikomo na mwili uliobuniwa kuishi milele ikiwa hatukukusudiwa kuishi milele?

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki