-
“Kifo Kitafanywa Kuwa Si Kitu”Mnara wa Mlinzi—1998 | Julai 1
-
-
Mwili wa Aina Gani?
3. Kwa nini watu fulani waliukataa ufufuo?
3 Kwa kuzusha swali hilo, huenda Paulo akawa alinuia kukinza uvutano wa falsafa ya Plato. Plato alifundisha kwamba mwanadamu ana nafsi isiyoweza kufa ambayo hubaki hai baada ya mwili kufa. Wale waliokua wakiwa na wazo kama hilo, bila shaka fundisho la Kikristo la ufufuo halikuonekana kuwa jambo la lazima. Ikiwa nafsi iliendelea kuwa hai baada ya kifo, ufufuo una maana gani? Na zaidi, yaelekea ufufuo ulionekana kuwa jambo lisilo la akili. Mwili unapooza na kuwa mavumbi, kunaweza kuwaje na ufufuo? Mwelezaji wa Biblia, Heinrich Meyer, asema kwamba ugomvi wa Wakorintho fulani labda ulitegemea “msingi wa falsafa ya kwamba, lilikuwa jambo lisilowezekana kurudisha vitu vinavyoufanyiza mwili.”
4, 5. (a) Kwa nini vipingamizi vya wasio na imani vilikuwa mambo yasiyo ya akili? (b) Eleza kielezi cha Paulo cha “punje tupu.” (c) Mungu huwapa watiwa-mafuta wenye kufufuliwa miili ya aina gani?
4 Paulo afichua upumbavu wa kusababu kwao: “Wewe mtu asiye na akili! Kile upandacho hakifanywi kuwa hai isipokuwa kwanza kife; na kwa habari ya kile upandacho, wapanda, si mwili utakaositawi, bali punje tupu, huenda ikawa, ya ngano au yoyote moja kati ya zile nyingine; lakini Mungu huipa mwili kama vile imempendeza, na kwa kila moja ya hizo mbegu mwili wayo yenyewe.” (1 Wakorintho 15:36-38) Mungu hangefufua miili ambayo watu walikuwa nayo walipokuwa duniani. Badala yake, kungekuwa na mgeuzo umbo.
5 Paulo alinganisha ufufuo na kumea kwa mbegu. Mbegu ndogo ya ngano huwa haifanani kwa vyovyote na mmea utakaoota kutoka kwake. Kichapo The World Book Encyclopedia chasema hivi: “Mbegu ianzapo kuota, hufyoza maji mengi sana. Hayo maji husababisha mabadiliko mengi ya kemikali ndani ya hiyo mbegu. Pia husababisha sehemu ya ndani ya mbegu kuvimba na kupasua ngozi ya nje ya mbegu.” Kwa kweli hiyo mbegu hufa ikiwa mbegu na kuwa mmea unaoibuka. “Mungu huipa mwili” kwa kuwa alizipanga sheria za kisayansi zinazoongoza kusitawi kwake, na kila mbegu hupokea mwili kulingana na aina yake. (Mwanzo 1:11) Vivyo hivyo, Wakristo watiwa-mafuta kwanza hufa wakiwa binadamu. Kisha, kwenye wakati wa Mungu uliowekwa, yeye huwafufua katika miili mipya kabisa. Kama vile Paulo alivyowaambia Wafilipi, “Yesu Kristo . . . ataufanya upya mwili wetu uliotwezwa ili upatanishwe na umbo la mwili wake wenye utukufu.” (Wafilipi 3:20, 21; 2 Wakorintho 5:1, 2) Wao hufufuliwa katika miili ya roho na huishi katika makao ya roho.—1 Yohana 3:2.
6. Kwa nini ni jambo la akili kuamini kwamba Mungu aweza kuwapa wenye kufufuliwa miili ifaayo ya roho?
6 Je, jambo hilo ni gumu mno kuamini? La. Paulo anasababu kwamba, wanyama wana miili mingi tofauti. Kwa kuongezea, yeye atofautisha malaika wa kimbingu na wanadamu wenye nyama na damu, akisema: “Kuna miili ya kimbingu, na miili ya kidunia.” Pia kuna tofauti kubwa kati ya uumbaji wa vitu visivyo na uhai. “Nyota hutofautiana na nyota kwa utukufu,” Paulo akasema, muda mrefu kabla sayansi haijagundua nyota kubwa kwa ndogo na zenye rangi tofauti-tofauti. Kwa kufikiria hilo, je, si jambo la akili kwamba Mungu aweza kuandaa miili ya roho ifaayo kwa ajili ya watiwa-mafuta wenye kufufuliwa?—1 Wakorintho 15:39-41.
7. Ni nini maana ya kutoharibika? na ya kutoweza kufa?
7 Kisha Paulo asema hivi: “Ndivyo pia ulivyo ufufuo wa wafu. Hupandwa katika uharibifu, hufufuliwa katika kutoharibika.” (1 Wakorintho 15:42) Mwili wa kibinadamu, hata unapokuwa mkamilifu, waweza kuharibika. Waweza kuuawa. Kwa mfano, Paulo alisema kwamba Yesu aliyefufuliwa “[ali]kusudiwa asirudi tena kwenye uharibifu.” (Matendo 13:34) Hangefufuliwa katika mwili wa kibinadamu wenye kuharibika, hata ingawa ni mkamilifu. Mungu huwapa watiwa-mafuta wenye kufufuliwa miili isiyoharibika—isiyoweza kufa au kuoza. Paulo aendelea kusema hivi: “Hupandwa katika fedheha, hufufuliwa katika utukufu. Hupandwa katika udhaifu, hufufuliwa katika nguvu. Hupandwa ukiwa mwili wa nyama, hufufuliwa ukiwa mwili wa kiroho.” (1 Wakorintho 15:43, 44) Na zaidi, Paulo asema hivi: “Huu uwezao kufa lazima uvae hali ya kutokufa.” Kutokufa humaanisha uhai wa milele usioweza kuhabiriwa. (1 Wakorintho 15:53; Waebrania 7:16) Katika njia hiyo, wenye kufufuliwa huchukua “mfano wa yule wa kimbingu,” yaani Yesu, aliyewezesha kufufuliwa kwao.—1 Wakorintho 15:45-49.
8. (a) Twajuaje kwamba wenye kufufuliwa watakuwa watu walewale waliokuwa hai duniani? (b) Ni unabii gani mbalimbali unaotimizwa ufufuo utokeapo?
8 Licha ya mgeuzo umbo huo, wenye kufufuliwa bado watakuwa watu walewale waliokuwa kabla ya kufa. Watafufuliwa na kumbukumbu zilezile na sifa zilezile bora za Kikristo. (Malaki 3:3; Ufunuo 21:10, 18) Katika hilo wanafanana na Yesu Kristo. Umbo lake la roho lilibadilika kuwa la kibinadamu. Kisha akafa na kufufuliwa akiwa roho. Hata hivyo, “Yesu Kristo ni yuleyule jana na leo, na milele.” (Waebrania 13:8) Watiwa-mafuta wana pendeleo lililoje! Paulo asema hivi: “Lakini wakati huu ulio wenye kuharibika uvaapo kutoharibika na huu uwezao kufa uvaapo hali ya kutokufa, ndipo usemi utakapotukia ambao umeandikwa: ‘Kifo kimemezwa milele.’ ‘Kifo, ushindi wako uko wapi? Kifo, kichomeo chako kiko wapi?’”—1 Wakorintho 15:54, 55; Isaya 25:8; Hosea 13:14.
-
-
“Kifo Kitafanywa Kuwa Si Kitu”Mnara wa Mlinzi—1998 | Julai 1
-
-
11. (a) Twajuaje kwamba Mungu aweza kuumba tena nafsi zilizokufa? (b) Watakaofufuliwa duniani watapewa miili ya aina gani?
11 Hilo lamaanisha kuumba tena nafsi za kibinadamu. Je, ni jambo lisilowezekana? La, kwa kuwa andiko la Zaburi 104:29, 30 latuhakikishia kwamba Mungu aweza kufanya hivyo: “Waiondoa pumzi yao, wanakufa, na kuyarudia mavumbi yao, waipeleka roho yako, wanaumbwa.” Ingawa wenye kufufuliwa watakuwa watu walewale waliokuwa kabla ya kufa, hawatahitaji kuwa na miili ileile. Sawa na wale watakaofufuliwa kwenda mbinguni, Mungu atawapa mwili kama vile impendezavyo. Bila shaka miili yao mipya itakuwa yenye afya na kwa kufaa itakuwa sawa na miili yao ya hapo awali, hivi kwamba wapendwa wao wataweza kuwatambua.
-