Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Ni Tatizo Kubwa Kadiri Gani?
    Amkeni!—2003 | Oktoba 22
    • Ni Tatizo Kubwa Kadiri Gani?

      MNAMO Oktoba 1997, Hollie Mullin, mtoto wa majuma matatu alipata ambukizo kwenye sikio. Kwa kuwa ambukizo halikupona baada ya siku chache, daktari alipendekeza apewe dawa ya kisasa ya kiuavijasumu (dawa ya kuua viini). Ambukizo lilitarajiwa kupona kwa urahisi lakini haikuwa hivyo. Liliendelea kila alipopewa viuavijasumu zaidi.

      Katika mwaka wake wa kwanza, Hollie alikuwa ametumia viuavijasumu 17. Kisha akiwa na umri wa miezi 21, alipata ambukizo baya zaidi. Baada ya kutiwa dawa kali zaidi mishipani kwa siku 14, ambukizo lilipona hatimaye.

      Visa kama hivi havijaongezeka miongoni mwa watoto na wazee pekee. Watu wa kila umri wanaugua na hata kufa kutokana na maambukizo ambayo hapo awali yalitibiwa kwa urahisi kwa kutumia viuavijasumu. Ama kwa hakika, tangu miaka ya 1950 viini sugu vimezusha matatizo makubwa katika hospitali fulani. Halafu katika miaka ya 1960 na 1970, viini vinavyokinza viuavijasumu vilienea katika jamii.

      Baada ya muda, watafiti wa kitiba walisema kwamba viini vinavyokinza viuavijasumu viliongezeka hasa kwa sababu dawa hizo zilitumiwa kupita kiasi kuwatibu wanadamu na wanyama. Mnamo mwaka wa 1978, mmoja wa watafiti hao alisema kwamba viuavijasumu vinatumiwa “kupita kiasi.” Kwa hiyo, kufikia miaka ya 1990, vichwa vifuatavyo vya habari vilionekana ulimwenguni pote: “Viini Sugu Vyaibuka,” “Viini Sugu Vinatawala,” “Dawa Hatari—Kutumia Viuavijasumu Kupita Kiasi Kunasababisha Viini Sugu.”

      Je, vichwa hivyo vilitia chumvi? Mashirika maarufu ya kitiba hayaoni hivyo. Katika mwaka wa 2000, mkurugenzi mkuu wa Shirika la Afya Ulimwenguni alisema hivi katika ripoti kuhusu magonjwa ya kuambukiza: “Wanadamu wanakabili tatizo jingine mwanzoni mwa milenia mpya. Magonjwa ambayo awali yalitibiwa . . . sasa yamepata nguvu zaidi za kukinza dawa.”

      Tatizo hilo ni kubwa kadiri gani? Shirika la Afya Ulimwenguni liliripoti hivi: “Tatizo hilo [la viini vinavyokinza dawa] linafanya jitihada za kutibu magonjwa ya kuambukiza zisifaulu.” Wataalamu fulani leo hata wanasema kwamba wanadamu watarudia kipindi ambacho hakukuwa na dawa za kuua viini.

      Viini sugu vimewezaje kutawala ulimwengu na kukinza maendeleo tata ya kisayansi? Je, mtu anaweza kufanya lolote ili kujilinda au kuwalinda wengine? Na je, kuna matazamio ya kukomesha viini sugu? Makala zinazofuata zitajibu maswali haya.

  • Jinsi Viini Sugu Vinavyoibuka Tena
    Amkeni!—2003 | Oktoba 22
    • Jinsi Viini Sugu Vinavyoibuka Tena

      YAMKINI virusi, bakteria, protozoa, kuvu, na viini vingine vimekuwapo tangu uhai ulipoanza duniani. Kwa kuwa viini hivyo ambavyo ni viumbe sahili zaidi vinaweza kustahimili hali zozote, vimeishi mahali ambapo viumbe wengine hawawezi kuishi. Vinapatikana katika matundu ya maji ya moto katika sakafu ya bahari na vilevile katika maji ya barafu ya Aktiki. Sasa viini hivyo vinakinza hata dawa kali zaidi za kuua viini.

      Miaka 100 iliyopita, ilijulikana kwamba viini fulani vilisababisha magonjwa, lakini watu walioishi wakati huo hawakuwa wamesikia kuhusu dawa yoyote ya kuua viini. Kwa hiyo endapo mtu aliambukizwa ugonjwa mbaya, madaktari wengi hawakuwa na lolote la kufanya ila tu kumfariji. Alitegemea tu mfumo wake wa kinga upigane na ambukizo hilo. Iwapo alikuwa na mfumo dhaifu, kwa kawaida matokeo yalikuwa mabaya sana. Mara nyingi hata mkwaruzo mdogo ulioambukizwa viini ulisababisha kifo.

      Hivyo, uvumbuzi wa dawa ya kwanza ya kuua viini ulileta mabadiliko makubwa ya kitiba. Matumizi ya dawa za sulfa katika miaka ya 1930 na dawa kama vile penisilini na streptomycin katika miaka ya 1940 yalichangia uvumbuzi mwingi katika miaka iliyofuata. Kufikia miaka ya 1990, kulikuwa na viuavijasumu vipatavyo 150 katika makundi 15.

      Mataraja Yaambulia Patupu

      Kufikia miaka ya 1950 na 1960, watu fulani walifikiria kwamba magonjwa ya kuambukiza yamekwisha. Hata wataalamu fulani wa viini waliamini kwamba muda si muda magonjwa hayo yangetokomea. Mnamo 1969, daktari mkuu wa Marekani aliliambia bunge kwamba baada ya muda huenda wanadamu “hawatahangaishwa tena na magonjwa ya kuambukiza.” Mnamo mwaka wa 1972, mshindi wa tuzo ya Nobeli Macfarlane Burnet na David White waliandika hivi: “Inaelekea sana kwamba wakati ujao hakutakuwa na jambo lolote la kuripoti kuhusu magonjwa ya kuambukiza kwa sababu hayatakuwepo.” Kwa kweli, wengine walidhani kwamba magonjwa hayo yangekomeshwa kabisa.

      Maoni ya kwamba magonjwa ya kuambukiza yangekomeshwa yaliwafanya wengi wawe na uhakika kupita kiasi. Muuguzi mmoja aliyefahamu madhara yaliyosababishwa na viini kabla viuavijasumu havijavumbuliwa, alisema kwamba wauguzi fulani vijana walianza kupuuza usafi. Alipowakumbusha wanawe mikono, walimjibu hivi: “Usijali, sasa tuna viuavijasumu.”

      Hata hivyo, kutegemea viuavijasumu na kuvitumia kupita kiasi kumetokeza madhara. Magonjwa ya kuambukiza yamesitawi. Isitoshe, yameibuka tena na kuwa kisababishi kikuu cha kifo ulimwenguni! Mambo mengine ambayo yamechangia kuenea kwa magonjwa ya kuambukiza ni vita, kuenea kwa utapiamlo katika nchi zinazoendelea, ukosefu wa maji safi, uchafu, usafiri wa haraka, na mabadiliko ya hali ya hewa ulimwenguni.

      Bakteria Sugu

      Viini vya kawaida vimekuwa sugu na hivyo kusababisha tatizo kubwa ambalo halikutarajiwa na wengi. Hata hivyo, kwa kuzingatia matukio ya zamani, watu walipaswa kutarajia kwamba viini vingekinza dawa. Kwa nini? Kwa mfano, hebu fikiria ilivyokuwa wakati dawa ya kuua wadudu ya DDT ilipoanza kutumiwa katikati ya miaka ya 1940.a Wafugaji walifurahi sana wakati nzi walipotoweka baada ya dawa hiyo kuanza kutumiwa. Lakini nzi wachache hawakufa, na watoto wao wakarithi uwezo wa kukinza dawa hiyo. Muda si muda, nzi hao waliongezeka sana kwa kuwa hawangeweza kuangamizwa na dawa ya DDT.

      Hata kabla ya dawa ya DDT kutumiwa, na kabla ya penisilini kutumiwa katika matibabu mwaka wa 1944, tayari ilikuwa imegunduliwa kwamba bakteria hatari zinaweza kuwa sugu. Dakt. Alexander Fleming, aliyevumbua penisilini, alijua hivyo. Alipokuwa katika maabara yake, aliona vizazi mbalimbali vya bakteria ya Staphylococcus aureus vikifanyiza kuta za chembe ambazo hazingeweza kupenywa na dawa aliyokuwa amegundua.

      Hivyo miaka 60 hivi iliyopita, Dakt. Fleming alionya kwamba bakteria hatari ndani ya mwili wa mgonjwa zinaweza kupata uwezo wa kukinza penisilini. Kwa hiyo ikiwa penisilini haikuua bakteria nyingi hatari, bakteria sugu ziliongezeka. Basi ugonjwa huo ambao haungeweza kutibiwa na penisilini ungerudi tena na kuwa sugu zaidi.

      Kitabu The Antibiotic Paradox kinaeleza hivi: “Utabiri wa Fleming ulitimia kwa kadiri kubwa zaidi kuliko alivyokuwa amesema.” Jinsi gani? Iligunduliwa kwamba chembe za urithi za aina fulani za bakteria zilitokeza vimeng’enya vinavyopunguza nguvu za penisilini. Hivyo, mara nyingi hata kumeza tembe nyingi za penisilini hakukusaidia. Hilo lilikuwa jambo lenye kusikitisha sana!

      Ili kupambana na magonjwa ya kuambukiza, dawa mpya za kuua viini zilianza kutumiwa kuanzia miaka ya 1940 hadi miaka ya 1970, na nyingine chache zikavumbuliwa katika miaka ya 1980 na 1990. Dawa hizo zingeweza kuua bakteria ambazo zilikinza dawa za awali. Lakini miaka michache baadaye, kukaibuka aina fulani za bakteria ambazo zilikinza dawa hizo mpya.

      Wanadamu wametambua kwamba bakteria hukinza dawa kwa njia ya ajabu sana. Bakteria zinaweza kubadili ukuta wa chembe ili kuzuia dawa isipenye au kubadili mfumo wake ili zisife. Pia bakteria inaweza kuondoa dawa mara tu inapoingia, au inaweza kuiharibu.

      Kadiri watu wanavyozidi kutumia dawa za kuua viini, ndivyo aina mbalimbali za bakteria sugu zimeongezeka na kuenea. Je, hiyo ni balaa tupu? La, nyakati nyingine haiwi hivyo. Dawa moja inaposhindwa kutibu ambukizo fulani, kwa kawaida dawa nyingine hufaulu. Ingawa tatizo la bakteria sugu limekuwa baya, mara nyingi kumekuwa na suluhisho.

      Kukinza Dawa za Aina Mbalimbali

      Wanasayansi wa kitiba wamesikitika kugundua kwamba bakteria hubadilishana chembe za urithi. Mwanzoni ilidhaniwa kwamba bakteria za aina moja tu ndizo hubadilishana chembe za urithi. Lakini baadaye chembe zilezile sugu ziligunduliwa katika bakteria tofauti. Kutokana na utaratibu huo wa kubadilishana chembe za urithi, bakteria za aina mbalimbali zimeweza kukinza dawa nyingi za kawaida.

      Isitoshe, uchunguzi uliofanywa katika miaka ya 1990 ulionyesha kwamba bakteria fulani zimekuwa sugu bila kusaidiwa na bakteria nyingine. Hata dawa moja inapotumiwa, bakteria fulani hupata uwezo wa kukinza dawa nyingi, za kiasili na zisizo za kiasili.

      Utabiri Wenye Kuhuzunisha

      Ingawa dawa nyingi za kuua viini hufaulu kutibu wagonjwa wengi, je, dawa hizo zitafaulu wakati ujao? Kitabu The Antibiotic Paradox kinasema hivi: “Hatuwezi kutarajia kwamba ambukizo lolote lile litakomeshwa na dawa ya kwanza inayotumiwa.” Kitabu hicho kinaendelea kusema: “Katika sehemu fulani za ulimwengu kuna dawa chache za kuua viini, hivyo hakuna dawa inayoweza kutibu ugonjwa kabisa . . . . Watu wanaugua na kufa kutokana na magonjwa ambayo miaka 50 iliyopita ilitabiriwa kwamba yangekomeshwa kabisa.”

      Mbali na bakteria, kuna viini vingine pia ambavyo vimepata uwezo wa kukinza dawa. Virusi, kuvu, na vimelea vingine vidogo vina uwezo huo wa ajabu. Hivyo kuna viini vingi sugu ambavyo vitafanya jitihada zote za kuvumbua na kutengeneza dawa ziambulie patupu.

      Basi, ni nini kinachoweza kufanywa? Je, inawezekana kukomesha au angalau kudhibiti viini sugu? Ni nini kinachoweza kufanywa ili dawa za kuua viini ziendelee kushinda magonjwa katika ulimwengu unaoendelea kukumbwa na magonjwa ya kuambukiza?

      [Maelezo ya Chini]

      a Dawa za kuua wadudu ni sumu kama dawa za matibabu. Dawa hizo zote zimesaidia na vilevile zimesababisha madhara. Ijapokuwa dawa zinaweza kuua viini hatari, zinaweza pia kuua bakteria muhimu.

  • Wakati Ambapo Viini Havitamdhuru Yeyote
    Amkeni!—2003 | Oktoba 22
    • Wakati Ambapo Viini Havitamdhuru Yeyote

      VIINI ni muhimu kwa uhai. Sehemu kubwa ya udongo na ya miili yetu imefanyizwa kwa viini. Kama vile sanduku “Aina za Viini” kwenye ukurasa wa 7 linavyosema “kuna trilioni nyingi za bakteria mwilini mwetu.” Nyingi ni muhimu kwa afya. Ingawa viini vichache husababisha magonjwa, tuna hakika kwamba siku moja viini havitamdhuru mtu yeyote.

      Kabla ya kuchunguza jinsi madhara ya viini yatakavyokomeshwa, hebu tuone jitihada ambazo zimefanywa hivi majuzi kupambana na viini vinavyosababisha magonjwa. Zaidi ya kuchunguza sanduku lenye kichwa “Mambo Unayoweza Kufanya,” hebu fikiria jitihada ambazo wataalamu wa afya wamefanya kupambana na viini sugu.

      Mikakati ya Ulimwenguni Pote

      Dakt. Gro Harlem Brundtland, aliyekuwa mkurugenzi mkuu wa Shirika la Afya Ulimwenguni, alieleza jitihada ambazo zinafanywa. Katika ripoti inayoitwa Report on Infectious Diseases 2000, yenye kichwa “Kupambana na Viini Sugu,” alionyesha uhitaji wa kuanzisha ‘mkakati wa ulimwenguni pote wa kudhibiti viini sugu.’ Pia alieleza juu ya kuanzisha “mashirika yatakayohusisha wataalamu wote wa afya,” na akakazia hivi: “Tuna nafasi ya kuanzisha jitihada kabambe ya kupambana na magonjwa ya kuambukiza.”

      Mnamo mwaka wa 2001, Shirika la Afya Ulimwenguni lilichapisha hati yenye kichwa “Mkakati wa Ulimwenguni Pote wa Kudhibiti Viini Sugu.” Hati hiyo ilionyesha mambo ambayo wataalamu wa kitiba na watu kwa ujumla “wanaweza kufanya na jinsi ya kuyafanya.” Mkakati huo ulitilia maanani kuwaelimisha watu kujikinga na magonjwa, na vilevile kuwapa maagizo ya kutumia viuavijasumu na dawa nyingine za kuua viini wanapokuwa wagonjwa.

      Isitoshe, wataalamu wa kitiba, yaani madaktari, wauguzi, na wafanyakazi wengine wa hospitali, walishauriwa kuchukua hatua zinazofaa ili kuzuia magonjwa yasienee. Kwa kusikitisha, uchunguzi mbalimbali unaonyesha kwamba wataalamu wengi wa afya wanapuuza kunawa mikono au kubadilisha glavu baada ya kuwatibu wagonjwa.

      Uchunguzi pia umeonyesha kwamba madaktari huwapendekezea wagonjwa viuavijasumu wakati ambapo hawavihitaji. Sababu moja ni kwamba wagonjwa huwasihi madaktari wawapendekezee viuavijasumu ili wapone haraka. Kwa hiyo madaktari hukubali maombi yao, ili kuwafurahisha. Mara nyingi madaktari hawawaelimishi wagonjwa na hawana vifaa vya kutambua viini vinavyosababisha magonjwa. Pia huenda wakawapendekezea viuavijasumu vipya na vya bei ghali ambavyo vinaweza kutibu magonjwa mengi. Na hilo huchangia tatizo la viini sugu.

      Mkakati wa Shirika la Afya Ulimwenguni ulizungumzia pia hospitali, mifumo ya kitaifa ya afya, wazalishaji wa chakula, makampuni ya kutengeneza dawa, na wabunge. Ripoti hiyo ilisema kwamba wote wanapaswa kushirikiana ili kupambana na tatizo la viini sugu ulimwenguni pote. Lakini je, mpango huo utafaulu?

      Vizuizi vya Mafanikio

      Mkakati wa Shirika la Afya Ulimwenguni ulitaja jambo kuu linalozuia matatizo ya afya yasisuluhishwe. Jambo hilo ni pesa. Biblia inasema kwamba kupenda pesa ndiko kunakosababisha “mambo mabaya ya namna zote.” (1 Timotheo 6:9, 10) Shirika hilo linasema hivi: “Inafaa pia kuzingatia ushirikiano na makampuni ya kutengeneza dawa, na vilevile kudhibiti ushirikiano kati ya maafisa wa mauzo na wafanyakazi wa hospitali na mipango ya makampuni hayo ya kuelimisha wafanyakazi wa hospitali.”

      Makampuni ya kutengeneza dawa yamesisitiza madaktari wanunue dawa zao. Sasa wanashawishi umma moja kwa moja kupitia matangazo ya biashara kwenye televisheni. Hilo limechangia matumizi ya dawa kupita kiasi, na hivyo kusababisha ongezeko la viini sugu.

      Mkakati wa Shirika la Afya Ulimwenguni unasema hivi kuhusu matumizi ya dawa za kuua viini katika kutibu mifugo: “Kwa kuwa katika nchi fulani madaktari wa mifugo hupata asilimia 40 au zaidi ya mapato yao kwa kuuza dawa, hawataki kuwazuia watu kutumia dawa za kuua viini.” Kama inavyojulikana, viini sugu vimeibuka na kuongezeka kwa sababu dawa za kuua viini zinatumiwa kupita kiasi.

      Idadi ya viuavijasumu vinavyotengenezwa ni kubwa ajabu. Nchini Marekani pekee, kilogramu zipatazo milioni 20 hutengenezwa kila mwaka! Kati ya viuavijasumu vyote ambavyo hutengenezwa ulimwenguni, karibu nusu tu ndivyo hutumiwa kuwatibu wanadamu. Nusu inayosalia hunyunyiziwa mimea au hulishwa wanyama. Viuavijasumu huchanganywa na chakula cha mifugo ili kuharakisha ukuzi.

      Jukumu la Serikali

      Umalizio wa Mkakati wa Shirika la Afya Ulimwenguni unasema hivi: “Nchi mojamoja zina jukumu kubwa la kutekeleza mkakati huu. Serikali zina daraka muhimu sana.”

      Kwa hakika, serikali kadhaa zimeanzisha miradi ya kudhibiti viini sugu, huku zikitilia maanani ushirikiano nje na ndani ya nchi zao. Miradi hiyo inahusisha kuchunguza matumizi ya dawa za kuua viini na viini sugu, kuboresha njia za kudhibiti magonjwa, kutumia vizuri dawa za kuua viini katika tiba na kilimo, kufanya utafiti ili kuelewa jinsi viini vinavyokuwa sugu, na kubuni dawa mpya. Kulingana na Report on Infectious Diseases 2000 ya Shirika la Afya Ulimwenguni, haielekei mradi huo ungetekelezwa. Kwa nini?

      Ripoti hiyo ilisema kwamba “serikali fulani hazitaki kutilia maanani afya ya umma.” Iliongezea hivi: “Magonjwa—na viini sugu—huenea kunapokuwa na vita, umaskini, uhamaji mkubwa na uharibifu wa mazingira, wakati ambapo watu wengi huwa katika hatari ya kuambukizwa magonjwa.” Kwa kusikitisha, serikali za wanadamu hazijafaulu kamwe kusuluhisha matatizo hayo.

  • Wakati Ambapo Viini Havitamdhuru Yeyote
    Amkeni!—2003 | Oktoba 22
    • [Sanduku katika ukurasa wa 9]

      Mambo Unayoweza Kufanya

      Unaweza kufanya nini ili kupunguza uwezekano wa kuathiriwa na viini sugu? Shirika la Afya Ulimwenguni limetoa madokezo kadhaa. Kwanza, lilidokeza mambo tunayoweza kufanya kupunguza magonjwa na kuzuia maambukizo yasienee. Pili, lilieleza jinsi watu wanavyoweza kutumia vizuri dawa za kuua viini.

      Njia bora ya kupunguza na kuzuia magonjwa yasienee ni kujitahidi juu chini kutunza afya. Unaweza kufanya nini ili kujikinga na magonjwa?

      Madokezo ya Kujikinga na Magonjwa

      1. Jitahidi kadiri uwezavyo kufanya mambo haya matatu: kula vizuri, kufanya mazoezi ya kutosha, na kupumzika vya kutosha.

      2. Dumisha usafi. Wataalamu wa afya husema kwamba kunawa mikono ndiyo njia bora ya kujikinga na magonjwa au kuepuka kueneza maambukizo.

      3. Hakikisha kwamba chakula mnachokula na familia yako ni salama. Hakikisha mikono yako na mahali unapotayarishia chakula ni safi. Pia, hakikisha kwamba unatumia maji safi kunawa mikono na kusafisha chakula. Kwa kuwa viini huzaana ndani ya chakula, pika nyama kabisa. Hifadhi vyakula vizuri.

      4. Katika maeneo ambayo magonjwa hatari huenezwa na wadudu wanaoruka, epuka kuwa nje usiku au mapema asubuhi wakati ambapo wadudu ni wengi. Jikinge kwa chandarua sikuzote.

      5. Kupata chanjo kunaweza kuimarisha mfumo wako wa kinga ili upambane na viini vinavyopatikana mahali unapoishi.

      Kutumia Dawa za Kuua Viini

      1. Omba mashauri ya daktari kabla ya kununua au kutumia viuavijasumu au dawa yoyote ya kuua viini. Dawa zinazouzwa na wachuuzi mara nyingi huwafaidi wauzaji badala ya wanunuzi.

      2. Usimsihi daktari akupendekezee viuavijasumu. Ukifanya hivyo, huenda akakupendekezea kwa sababu hataki kumpoteza mteja. Kwa mfano, mafua husababishwa na virusi, na viuavijasumu haviponyi mafua. Kumeza viuavijasumu unapokuwa na virusi kunaweza kuua bakteria muhimu, na labda kufanya viini sugu viongezeke.

      3. Usiwe na zoea la kutumia dawa mpya kabisa kwani huenda isikufae na huenda ukatumia pesa nyingi isivyo lazima.

      4. Pata habari kuhusu dawa yoyote kutoka kwa mtu mwenye kutegemeka: Inatibu nini? Inaweza kuleta madhara gani? Inapaswa kutumiwa na dawa gani, ni mambo gani mengine yanayoweza kuifanya iwe hatari?

      5. Iwapo kweli unahitaji kutumia viuavijasumu, inapendekezwa utumie dozi nzima, hata ukihisi nafuu kabla ya kuimaliza. Dawa za mwisho za dozi humaliza kabisa maambukizo.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki