-
Kukabiliana na Matokeo YakeAmkeni!—1998 | Februari 8
-
-
Watunzaji Wapata Tegemezo
Watunzaji wahitaji tegemezo katika fungu lao la maana. Wanaweza kugeukia wapi ili kupata tegemezo? Mahali pamoja ni katika familia. Kila mshiriki ahitaji kushiriki mzigo wa kutunza. Yoshiko aeleza jinsi wana wake walivyompa tegemezo la kihisia-moyo: “Walikuwa wakiyasikiliza matatizo yangu kana kwamba yalikuwa yao.” Washiriki wa familia wahitaji kupata habari yote iwezayo kupatikana ili wajifunze jinsi ya kumtunza mhasiriwa wa mshtuko wa akili na pia jinsi ya kukabiliana na mabadiliko ya utu wa mpendwa wao.
-
-
Kukabiliana na Matokeo YakeAmkeni!—1998 | Februari 8
-
-
Tegemezo la Familia na Marafiki
Erikka alishiriki katika mazoezi ya kumsaidia aweze kuishi maisha ya kawaida kwa muda wa miaka mitatu, akijifunza kutembea na kutumia mkono wake wa kulia kufidia mkono wa kushoto uliopooza. Aeleza kilichomsaidia kukabiliana na hali: “Jambo lililokuwa la maana zaidi lilikuwa kwamba mume wangu na marafiki wangu walibaki wakiwa waaminifu-washikamanifu kwangu. Kujua kwamba walinipenda kulinipa nguvu, na waliponitia moyo nisikate tamaa, hilo lilinichochea.”
Washiriki wa familia hupata kuwa wenzi katika hatua za kupona za mpendwa wao. Wanahitaji kuwauliza maswali watumishi wa kitiba na kuchunguza kwa makini tiba ambazo huenda zikahitaji kuendelezwa nyumbani ili kwamba asipoteze maendeleo ambayo tayari yamefanywa. Subira, fadhili, uelewevu, na shauku zionyeshwazo na washiriki wa familia na marafiki huandaa mazingira ya kihisia-moyo yaliyo salama ya kujifunzia upya usemi, kusoma, na kazi nyingine za maisha ya kila siku.
Akijaribu kuwa mwenye usawaziko kati ya kulazimisha na kubembeleza, John alifanya bidii kumsaidia mke wake Ellen na mazoezi na tiba. Aelezea jitihada za familia yake: “Hatungemruhusu Ellen ajisikitikie kupita kiasi. Nyakati nyingine tulikuwa wasimamizi wakali, lakini sikuzote tuliangalia vizuizi vyake na kutoa usaidizi. Yeye ni mwenye hisia nyepesi, kwa hiyo huwa najitahidi nisimsababishie mkazo.”
Kadiri Ellen alivyoendelea kujifunza tena kuzungumza kwa msaada wa mtaalamu wa matibabu ya usemi, John alimsaidia. “Kufanya mambo pamoja kulikuwa kitia-moyo, kwa hiyo tulisoma Biblia pamoja kwa sauti, jambo ambalo lilisaidia kuboresha usemi wake. Pia, pole kwa pole mwanzoni, tulishiriki katika huduma, kwani sisi tu Mashahidi wa Yehova. Kwa njia hii Ellen angeweza kushiriki na wengine tumaini tulilo nalo la wakati ujao. Kufanya hivyo kwenyewe kulikuwa tiba kwa Ellen.” Kufikia mwishoni mwa miaka mitatu, Ellen alikuwa amefanya maendeleo sana.
Kitia-moyo na nguvu ambazo marafiki waweza kutoa hazipasi kudharauliwa kamwe, kwa sababu zaweza kuwa na athari kubwa kuelekea kupona kwa mtu aliyepatwa na mshtuko wa akili. Jarida la kitiba Stroke liliripoti kwamba “Utegemezo mwingi wa kijamii ulipatikana kuwa unaashiria kupona kwa haraka zaidi na maendeleo makubwa zaidi katika kuweza kufanya mambo, hata miongoni mwa wagonjwa waliokuwa na mshtuko wa akili mbaya sana.”
Bernie alithamini sana tegemezo ambalo marafiki wake walimpa. Yeye atukumbusha: “Ziara za marafiki husaidia kukabiliana na hali. Sauti yenye kusikitikia na mwelekeo wenye kujali huuchangamsha moyo. Ingawa mtu hapaswi kufikiria sana kutojiweza kwake, kutambua maendeleo yoyote kwatia moyo sana.” Sisi sote twaweza kufanya nini ili kutoa tegemezo kwa wale wanaokabiliana na matokeo ya baadaye ya mshtuko wa akili? “Wapelekee maua,” apendekeza Bernie, “au shiriki nao wazo la Kimaandiko au jambo lililoonwa. Hayo yalikuwa yenye msaada sana kwangu.”
Melva, mzee-mzee aliyepatwa na mshtuko wa akili aliona kuwa jambo la msaada kwa mmoja wa ndugu zake wa kiroho kusali pamoja naye. Gilbert pia apendekeza hili, akieleza: “Yaonyesha kuwa kwa kweli wajali unaposali pamoja na mtu.” Peter, ambaye mshtuko wa akili ulimwacha akiwa haoni vizuri, huthamini sana wakati ambapo watu wengine wanafahamu kizuizi chake na kuchukua wakati kumsomea.
Pia kumsaidia mtu kwenda na kutoka mahali pa kumsaidia kuweza kuishi maisha ya kawaida ni ishara ya upendo. Kuhakikisha kwamba nyumba ya mhasiriwa wa mshtuko wa akili ni mahali salama ni muhimu pia. Kuanguka ni tisho la daima wakati usawaziko wa mwili unapokuwa tatizo. Kwa kielelezo, Gilbert, alithamini msaada wenye fadhili wa marafiki ambao, kati ya mambo mengine, walimwekea pao la kujishikilia kwenye bafu yake kwa ajili ya usalama.
Kujifunza Kutoa Tegemezo
Mabadiliko ya hali ya moyo na mwelekeo mkubwa wa kulia waweza kuwa wenye kuaibisha mhasiriwa wa mshtuko wa akili, na pia kutatanishwa kwa watu walio kando ambao huenda wasijue jinsi ya kutenda. Hata hivyo, kwa kujifunza kuwa mwenye kutegemeza, marafiki waweza kumwokoa mhasiriwa wa mshtuko wa akili ambaye aweza kujitenga na wengine. Kwa kawaida vipindi vya kulia hupunguka. Lakini machozi yajapo, baki ukiwa mtulivu na ukae na mtu huyo, ukimwambia yale ungependa kusikia ikiwa ungekuwa katika hali yake.
Zaidi ya yote, kuza upendo wa kimungu kwa wale ambao udhaifu wao huenda ukawa umebadili utu ambao uliujua hapo awali. Wao hutambua unavyohisi, na hilo, nalo, huathiri itikio lao kukuelekea. Erikka aeleza: “Huenda nisipate kuwa mtu yuleyule tena. Lakini hakuna yeyote anayepaswa kudai hilo kutoka kwa mhasiriwa wa mshtuko wa akili. Jamaa na marafiki wapaswa kujifunza kumpenda mtu huyo jinsi alivyo. Wakichunguza kwa uangalifu utu wake, watagundua kuwa sifa nyingi zenye kupendeza za wakati uliopita zingali zipo.”
Mtu awapo hawezi kuzungumza au kueleweka staha ya kibinafsi hushuka. Kwa kufanya jitihada ya kuzungumza nao, marafiki waweza kuwahakikishia wale ambao usemi wao umedhoofika. Takashi aeleza: “Ninachofikiria na kuhisi moyoni hakijabadilika. Hata hivyo, watu huelekea kuniepuka kwa sababu hawawezi kuwa na mazungumzo ya kawaida nami. Ni vigumu kwangu kuwafikia watu, lakini mtu ajapo kuzungumza nami, huwa ni kitia-moyo kikubwa sana kwangu na hilo hunifurahisha sana sana!”
Ifuatayo ni miongozo fulani iwezayo kutusaidia sote tuweze kuwategemeza na kuwatia moyo wale wenye udhaifu wa usemi.
Mishtuko mingi ya akili haiathiri uwezo wa kufikiri. Watu wengi ambao wamepatwa na mshtuko wa akili hubaki wakiwa chonjo kiakili, hata ingawa huenda usemi wao ukawa mgumu kuuelewa. Usiseme nao kwa njia yenye kushusha au kusema kana kwamba wasema na mtoto. Watendee kwa adhama.
Sikiliza kwa subira. Huenda wakahitaji wakati ili kupanga upya wazo au kumaliza neno, fungu la maneno, au sentensi. Kumbuka kwamba msikilizaji mwenye kujali zaidi hana haraka ya kusikia.
Usijifanye kuwa waelewa ikiwa huelewi. Kiri kwa ufadhili: “Samahani. Yaonekana sipati kukuelewa. Tujaribu tena baadaye.”
Sema polepole na waziwazi kwa sauti ya kawaida.
Tumia sentensi fupi na maneno yajulikanayo.
Tumia maswali ambayo yanahitaji jibu la ndiyo au la, na umtie moyo kujibu. Kumbuka kwamba huenda wasiweze kufahamu maneno yako.
Punguza kelele za kando-kando.
-