Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Je, Sayansi Itamaliza Magonjwa?
    Amkeni!—2007 | Januari
    • Vikwazo Vikubwa

      Tabia ya wanadamu inaweza kusababisha magonjwa yasiondolewe haraka. Kwa mfano, wanasayansi wanaamini kwamba kwa sababu ya wanadamu kuharibu mazingira fulani, magonjwa mapya na yaliyo hatari yametokea. Alipohojiwa katika gazeti Newsweek, Mary Pearl, msimamizi wa shirika la Wildlife Trust alieleza hivi: “Tangu miaka ya katikati ya 1970 zaidi ya magonjwa 30 mapya yameibuka, kutia ndani UKIMWI, Ebola, ugonjwa wa Lyme, na Mafua ya Ndege (SARS). Inaaminika kwamba wanadamu waliambukizwa mengi ya magonjwa hayo kutoka kwa wanyama.”

      Isitoshe, watu wanakula matunda na mboga kidogo sana huku wakila sukari, chumvi, na mafuta mengi. Pia, magonjwa ya moyo yameongezeka kwa kuwa watu hawafanyi mazoezi wala kazi zinazohusisha nguvu na wanajihusisha katika mazoea mengine yanayodhuru afya. Kuvuta sigara kumeongezeka na kutokeza madhara kwa afya au hata kifo kwa mamilioni ulimwenguni pote. Kila mwaka, watu milioni 20 hivi wamejeruhiwa au kufa katika aksidenti. Vita na aina nyingine za jeuri vinaua na kujeruhi watu wengi. Mamilioni wengine wana afya mbaya kwa sababu ya matumizi mabaya ya kileo au madawa ya kulevya.

      Ijapokuwa kuna maendeleo mengi sana katika teknolojia ya kitiba bado magonjwa fulani yanaendelea kusababisha kuteseka kwingi. Kulingana na Shirika la Afya Ulimwenguni (WHO), ‘zaidi ya watu milioni 150 wanakumbwa na mshuko wa moyo, watu milioni 25 hivi wanakumbwa na schizophrenia, na wengine milioni 38 wana kifafa.’ Mamilioni ya watu huambukizwa UKIMWI, magonjwa ya kuharisha, malaria, surua, nimonia na kifua kikuu. Magonjwa hayo huua watoto na vijana wengi sana.

      Bado kuna vikwazo vingine vikubwa ambavyo vinazuia kuondolewa kabisa kwa magonjwa. Vikwazo viwili vikubwa ni umaskini na utawala mbaya. Katika ripoti ya karibuni shirika la WHO lilisema kwamba mamilioni ambao hufa kwa sababu ya magonjwa ya kuambukiza wangeweza kuokolewa ikiwa serikali zingefanya kazi vizuri na ikiwa kungekuwa na pesa za kutosha.

  • Je, Sayansi Itamaliza Magonjwa?
    Amkeni!—2007 | Januari
    • [Sanduku katika ukurasa wa 8, 9]

      Maadui Sita Ambao Hawajashindwa

      Ujuzi wa kitiba na teknolojia inayohusiana nayo inaendelea kuongezeka kwa kiwango kisichotazamiwa. Licha ya hayo, magonjwa ya kuambukizwa yanaendelea kuikumba dunia. Magonjwa yanayosababisha vifo yaliyoorodheshwa hapa chini bado hayajashindwa.

      UKIMWI

      Watu milioni 60 wameambukizwa virusi vya UKIMWI na milioni 20 hivi wamekufa kutokana na UKIMWI. Katika mwaka wa 2005 watu milioni tano waliambukizwa na zaidi ya watu milioni tatu walikufa kutokana na UKIMWI. Watoto zaidi ya 500,000 walikuwa kati ya watu waliokufa. Watu wengi kati ya wale walioambukizwa virusi vya UKIMWI hawawezi kupata matibabu yanayofaa.

      Kuharisha

      Unasemekana kuwa ugonjwa unaowaua maskini kwani kila mwaka watu bilioni nne hivi huambukizwa. Ugonjwa huo unasababishwa na magonjwa mbalimbali ya kuambukiza yanayoweza kupitishwa kwa maji au chakula kilichochafuliwa au kwa sababu ya kutotunza usafi. Watu zaidi ya milioni mbili hufa kila mwaka kutokana na maambukizo hayo.

      Malaria

      Kila mwaka, watu milioni 300 hivi hupatwa na malaria. Milioni moja hivi kati yao hufa kila mwaka, na wengi wao ni watoto. Kila sekunde 30 mtoto mmoja Afrika hufa kutokana na malaria. Kulingana na Shirika la Afya Ulimwenguni (WHO), “bado sayansi haina dawa yenye nguvu ya kukabiliana na malaria na wengi wanashuku ikiwa kutawahi kuwa na dawa kama hiyo.”

      Surua

      Katika mwaka wa 2003, surua iliua zaidi ya watu 500,000. Ni rahisi sana kuambukizwa ugonjwa huo ambao huwaua watoto wengi. Kila mwaka watu milioni 30 hupatwa na surua. Kwa kushangaza, kwa miaka 40 iliyopita kumekuwa na chanjo ya ugonjwa huo inayofanya kazi na isiyogharimu pesa nyingi.

      Nimonia

      Shirika la WHO linasema kwamba watoto wengi zaidi hufa kutokana na nimonia kuliko ugonjwa mwingine wa kuambukizwa. Watoto milioni mbili hivi walio na umri usiozidi miaka miwili hufa kila mwaka kutokana na nimonia. Wengi wao hufa Afrika na Kusini-Mashariki mwa Asia. Katika sehemu nyingi ulimwenguni, wagonjwa wengi hawapati matibabu yenye kuokoa uhai kwa sababu ya kukosekana kwa huduma za afya.

      Kifua Kikuu

      Katika mwaka wa 2003, kifua kikuu kilisababisha vifo vya watu zaidi ya 1,700,000. Kutokea kwa viini vya ugonjwa huo vinavyoweza kustahimili dawa kumewahangaisha sana maofisa wa afya. Bakteria fulani zimesitawisha uwezo wa kujikinga dhidi ya dawa fulani za kupigana na kifua kikuu. Bakteria hizo hujitokeza katika miili ya wagonjwa ambao hawatibiwi inavyofaa au ambao hawatibiwi kikamili.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki