-
Njia za Kuhubiri Habari NjemaTengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
-
-
46 Mahubiri ya vikundi huwasaidia wahubiri kufanya kazi pamoja na hivyo ‘kutiana moyo.’ (Rom. 1:12) Wahubiri wapya wanaweza kuhubiri na wahubiri wenye ustadi na uzoefu ili wasaidiwe. Katika maeneo fulani huenda ikawa jambo la hekima kwa wahubiri wawili au zaidi kuhubiri pamoja kwa sababu ya usalama. Hata ikiwa unapanga kuhubiri peke yako katika eneo, kukutana na wengine katika kikundi kunaweza kuwatia moyo. Kujua tu kwamba wengine wanahubiri katika eneo lilelile kunaweza kukupa ujasiri. Mapainia na wengine hawapaswi kuhisi kwamba ni lazima wahudhurie kila mkutano wa utumishi wa shambani uliopangwa na kutaniko, hasa ikiwa mikutano hiyo hufanywa kila siku. Hata hivyo, inaelekea kwamba wanaweza kuunga mkono angalau mikutano kadhaa ya utumishi wa shambani kila juma.
47 Acheni sote tuige mfano uliowekwa na Yesu na mitume wake! Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atabariki jitihada zetu za kushiriki kikamili katika kazi muhimu ya kuhubiri habari njema ya Ufalme.—Luka 9:57-62.
-
-
Njia za Kupanua Huduma YakoTengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
-
-
SURA YA 10
Njia za Kupanua Huduma Yako
YESU alipowaagiza wanafunzi wake wahubiri Ufalme, aliwaambia hivi: “Mavuno ni mengi, lakini wafanyakazi ni wachache.” Kulikuwa na kazi nyingi, basi akaongeza hivi: “Mwombeni Bwana wa mavuno awatume wafanyakazi katika mavuno yake.” (Mt. 9:37, 38) Yesu aliwapa wanafunzi wake maagizo ya kutimiza huduma yao. Alionyesha umuhimu wa kazi hiyo aliposema: “Hamtamaliza kamwe kuzunguka majiji ya Israeli kabla ya Mwana wa binadamu kufika.”—Mt. 10:23.
2 Leo pia, kuna kazi nyingi ya kufanya katika huduma ya shambani. Lazima habari njema ya Ufalme ihubiriwe kabla ya mwisho kuja, na muda unayoyoma! (Marko 13:10) Kwa kuwa shamba ni ulimwengu, tunakabili hali kama ya Yesu na wanafunzi wake, ingawa kwa kiwango kikubwa zaidi. Idadi yetu ni ndogo ikilinganishwa na mabilioni ya wanadamu ulimwenguni, lakini tuna hakika kwamba Yehova atatusaidia. Habari njema ya Ufalme itahubiriwa ulimwenguni pote, na wakati uliowekwa na Yehova utakapofika, mwisho utakuja. Je, tutatanguliza Ufalme wa Mungu maishani ili tutimize huduma yetu kikamili? Tunaweza kujiwekea malengo gani ya kitheokrasi?
3 Akieleza matakwa ya Yehova kwa watumishi wake waliojiweka wakfu, Yesu alisema: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote na kwa nguvu zako zote.” (Marko 12:30) Tunapaswa kumtumikia Mungu kwa nafsi yote. Hilo linamaanisha kuwa tunaonyesha kwamba tumejiweka wakfu na tumejitoa kikamili kwa kufanya yote tunayoweza katika utumishi wa Yehova. (2 Tim. 2:15) Kila mmoja wetu anaweza kupanua utumishi wake katika njia mbalimbali ikitegemea hali na uwezo wake. Hebu fikiria baadhi ya njia hizo, na uamue malengo ya kitheokrasi unayoweza kujiwekea unapotimiza huduma yako.
KUWA MHUBIRI WA KUTANIKO
4 Wote wanaokubali kweli wana pendeleo la kutangaza habari njema. Hiyo ndiyo kazi kuu ambayo Yesu aliwapa wanafunzi wake. (Mt. 24:14; 28:19, 20) Kwa kawaida, mwanafunzi wa Yesu Kristo huanza kuzungumza na wengine kuhusu habari njema mara tu anaposikia ujumbe huo. Hivyo ndivyo Andrea, Filipo, Kornelio, na wengine walivyofanya. (Yoh. 1:40, 41, 43-45; Mdo. 10:1, 2, 24; 16:14, 15, 25-34) Je, inamaanisha kwamba mtu anaweza kuzungumza na wengine kuhusu habari njema kabla hajabatizwa? Ndiyo! Mara tu mtu anapostahili kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa kutanikoni, anaweza kuanza kuhubiri nyumba kwa nyumba. Anaweza pia kushiriki katika sehemu mbalimbali za huduma ikitegemea hali na uwezo wake.
5 Mhubiri anapobatizwa, bila shaka yuko tayari kufanya yote anayoweza ili awasaidie wengine wajifunze habari njema. Wanaume na wanawake wana pendeleo la kushiriki katika kazi ya kuhubiri. Ni pendeleo kushiriki hata kwa sehemu ndogo katika kuendeleza kazi ya Ufalme wa Mungu. Bila shaka, tukipanua huduma yetu na kufikia mapendeleo zaidi ya utumishi tutakuwa na furaha sana.
KUTUMIKIA KATIKA MAENEO YENYE UHITAJI MKUBWA
6 Huenda eneo la kutaniko lenu huhubiriwa kwa ukawaida na ushahidi mzuri unatolewa. Ikiwa ndivyo, huenda ukahisi kwamba unaweza kupanua huduma yako kwa kuhamia eneo lenye uhitaji mkubwa wa wahubiri. (Mdo. 16:9) Ikiwa unatumikia ukiwa mzee au mtumishi wa huduma, huenda kuna kutaniko lingine ambalo litathamini msaada wako. Mwangalizi wenu wa mzunguko anaweza kukupendekezea jinsi ya kusaidia kutaniko lingine katika mzunguko wenu. Ikiwa ungependa kutumikia katika eneo lingine nchini kwenu, ofisi ya tawi inaweza kukupatia habari zaidi.
7 Je, ungependa kutumikia katika nchi nyingine? Ikiwa ndivyo, unapaswa kufikiria jambo hilo kwa makini. Kwa nini usizungumzie jambo hilo na wazee wa kutaniko lenu? Bila shaka, hilo litakuwa badiliko kubwa kwako na kwa wale watakaoenda nawe. (Luka 14:28) Hata hivyo, ikiwa hukusudii kukaa kwa muda mrefu, huenda ikafaa ufikirie kutumikia katika eneo lililo nchini kwenu.
8 Katika nchi fulani, ndugu wanaosimamia kazi ni wapya katika kweli. Kwa unyenyekevu, ndugu wenyeji wako tayari kuwaachia wazee wenye uzoefu wanaohamia katika makutaniko yao waongoze mambo. Ikiwa wewe ni mzee na unafikiria kuhamia katika nchi kama hizo, kumbuka kwamba lengo lako si kuchukua mapendeleo ya ndugu wenyeji. Badala yake, tumikia pamoja nao. Watie moyo wafanye maendeleo na wakubali majukumu kutanikoni. (1 Tim. 3:1) Uwe na subira ikiwa mambo fulani hayafanywi kama yanavyofanywa katika nchi yenu. Tumia uzoefu wako ukiwa mzee kuwasaidia akina ndugu. Kisha, ikiwa wakati fulani utalazimika kurudi katika nchi yenu, wazee wenyeji watakuwa na uwezo wa kusimamia kutaniko.
9 Kabla ofisi ya tawi haijakupa majina ya makutaniko yanayoweza kufaidika na msaada wako, Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko lenu itahitaji kutuma barua ya kukupendekeza. Barua hiyo inahitajiwa hata kama wewe ni mzee, mtumishi wa huduma, painia, au mhubiri. Halmashauri ya utumishi itatuma barua ya kukupendekeza pamoja na ombi lako moja kwa moja kwenye ofisi ya tawi ya nchi unayotaka kutumikia.
KUHUBIRI KATIKA LUGHA NYINGINE
10 Ili upanue huduma yako, huenda ukafikiria kujifunza lugha nyingine, kutia ndani lugha ya alama. Kama una lengo la kujifunza kuhubiri katika lugha nyingine, unaweza kuzungumza na wazee na mwangalizi wa mzunguko. Wanaweza kukupa madokezo na kukutia moyo. Kupitia mwelekezo wa ofisi ya tawi, mizunguko fulani imepanga madarasa ya lugha ili kuwazoeza wahubiri wenye uwezo na mapainia kuhubiri katika lugha nyingine.
UTUMISHI WA PAINIA
11 Wahubiri wote wanapaswa kujua matakwa ya msingi ya utumishi wa painia msaidizi, wa kawaida, na wa pekee na pia utumishi mwingine wa wakati wote. Painia anapaswa kuwa Mkristo aliyebatizwa mwenye mfano
-