-
Mwigeni Yehova, Mungu Wetu Asiye na UbaguziMnara wa Mlinzi—2003 | Juni 15
-
-
Mwigeni Yehova, Mungu Wetu Asiye na Ubaguzi
“Hakuna ubaguzi kwa Mungu.”—WAROMA 2:11.
1, 2. (a) Yehova alikuwa na kusudi gani kuhusiana na Wakanaani kwa ujumla? (b) Yehova alifanya nini, na ni maswali gani yanayotokea?
WAISRAELI walimsikiliza Musa kwa makini walipokuwa wamepiga kambi kwenye Nyanda za Moabu mwaka wa 1473 K.W.K. Hali ngumu ya vita iliwangojea ng’ambo ya pili ya Mto Yordani. Musa alitangaza kwamba Yehova alikusudia kuwasaidia Waisraeli wayashinde mataifa saba yenye nguvu ya Kanaani katika Nchi ya Ahadi. Maneno haya ya Musa yanatia moyo kama nini: ‘BWANA, Mungu wako, atawatoa mbele yako, nawe utawapiga’! Waisraeli hawakupaswa kufanya agano lolote pamoja nao, wala hawakupaswa kuwatendea kwa fadhili.—Kumbukumbu la Torati 1:1; 7:1, 2.
2 Hata hivyo, Yehova aliilinda familia moja katika jiji la kwanza ambalo Waisraeli walishambulia. Mungu aliwalinda pia watu wa miji mingine minne. Kwa nini? Tunajifunza nini kumhusu Yehova kutokana na matukio ya ajabu yanayohusiana na kuokoka kwa Wakanaani hao? Nasi tunaweza kumwiga jinsi gani?
Watu Walitendaje Waliposikia Matendo ya Yehova?
3, 4. Habari za ushindi wa Waisraeli zilikuwa na uvutano gani juu ya watu wa Kanaani?
3 Yehova aliwalinda na kuwapigania watu wake Israeli walipokuwa nyikani kwa miaka 40 kabla ya kuingia Nchi ya Ahadi. Waisraeli walimkabili mfalme Mkanaani wa Aradi, kusini ya Nchi ya Ahadi. Yehova aliwasaidia Waisraeli kumshinda mfalme huyo na watu wake huko Horma. (Hesabu 21:1-3) Baadaye, Waisraeli walipita kando ya nchi ya Edomu, kisha wakasafiri kuelekea upande wa kaskazini, hadi kaskazini-mashariki ya Bahari ya Chumvi. Waamori waliishi katika eneo hilo ambalo zamani lilikaliwa na Wamoabu. Mfalme Sihoni Mwamori hakuwaruhusu Waisraeli wapite katika nchi yake. Waisraeli walipigana na mfalme huyo katika jiji la Yahasa, ambapo Sihoni aliuawa. Yaelekea jiji hilo lilikuwa kaskazini ya Bonde la Mto la Arnoni. (Hesabu 21:23, 24; Kumbukumbu la Torati 2:30-33) Upande wa kaskazini, Ogu aliwatawala Waamori huko Bashani. Ingawa Ogu alikuwa mtu mwenye kimo kikubwa isivyo kawaida, hakuweza kumshinda Yehova. Ogu aliuawa huko Edrei. (Hesabu 21:33-35; Kumbukumbu la Torati 3:1-3, 11) Habari za ushindi huo pamoja na masimulizi kuhusu jinsi Waisraeli walivyotoka katika nchi ya Misri, zilikuwa na uvutano mkubwa juu ya watu walioishi Kanaani.a
4 Baada ya kuvuka Yordani na kuingia Kanaani mara ya kwanza, Waisraeli walipiga kambi huko Gilgali. (Yoshua 4:9-19) Karibu na hapo palikuwa na jiji la Yeriko lililozungukwa na ukuta. Rahabu Mkanaani alichochewa kutenda kwa imani aliposikia matendo ya Yehova. Kwa hiyo, Yehova alipoharibu Yeriko, alimlinda Rahabu na watu waliokuwa katika nyumba yake.—Yoshua 2:1-13; 6:17, 18; Yakobo 2:25.
5. Ni nini kilichowafanya Wagibeoni watende kwa hila?
5 Kisha, Waisraeli wakapanda kutoka nchi tambarare karibu na mto hadi vilima vilivyokuwa katikati ya eneo hilo. Kwa kufuata mwelekezo wa Yehova, Yoshua alitumia mbinu za kuvizia aliposhambulia jiji la Ai. (Yoshua, sura ya 8) Wafalme wengi Wakanaani walikusanyika kwa ajili ya vita waliposikia habari ya ushindi mkubwa ambao Yoshua alipata. (Yoshua 9:1, 2) Wakaaji wa jiji la Gibeoni la Wahivi walitenda kwa njia tofauti. Andiko la Yoshua 9:4 linasema kwamba ‘walitenda kwa hila.’ Kama Rahabu, walikuwa wamesikia jinsi Yehova alivyowakomboa watu wake kutoka Misri na jinsi alivyomshinda Sihoni na Ogu. (Yoshua 9:6-10) Wagibeoni walitambua kwamba ingekuwa kazi bure kuwapinga Waisraeli. Kwa hiyo, kwa niaba ya Gibeoni na kwa niaba ya miji mitatu iliyokuwa karibu, yaani, Kefira, Beerothi, na Kiriath-yearimu, waliwatuma watu fulani kwa Yoshua huko Gilgali ambao walijifanya waonekane kama wametoka nchi ya mbali. Mbinu hiyo ilifanikiwa. Yoshua alifanya agano pamoja nao ambalo liliwahakikishia kwamba hawangeuawa. Siku tatu baadaye Yoshua na Waisraeli walitambua kwamba walikuwa wamedanganywa. Hata hivyo, walikuwa wameapa kwa Yehova kwamba wangeshika agano hilo, hivyo wakatenda kupatana nalo. (Yoshua 9:16-19) Je, Yehova alikubali jambo hilo?
6. Yehova alifanyaje kuhusu lile agano ambalo Yoshua alifanya pamoja na Wagibeoni?
6 Wagibeoni waliruhusiwa kuwa wakataji wa kuni na watekaji wa maji wa Waisraeli, hata “kwa ajili ya madhabahu ya BWANA” kwenye hema la kukutania. (Yoshua 9:21-27) Isitoshe, Yehova aliingilia kati kwa kufanya mwujiza, wakati wafalme watano Waamori na majeshi yao walipotisha kuwashambulia Wagibeoni. Mvua ya mawe iliwaua adui wengi kuliko wale waliouawa na wanajeshi wa Yoshua. Yehova hata alijibu sala ya Yoshua kwamba jua na mwezi visimame tuli ili aweze kukamilisha ushindi wake. “Haikuwapo siku nyingine mfano wa siku hiyo katika siku zilizotangulia mbele yake wala katika hizo zilizoandama baada yake,” akasema Yoshua, “hata ikawa yeye BWANA kuisikia sauti ya binadamu, kwa kuwa BWANA alipiga vita kwa ajili ya Israeli.”—Yoshua 10:1-14.
7. Petro alitambua ukweli gani ambao ulionyeshwa katika kisa cha Wakanaani fulani?
7 Rahabu Mkanaani, familia yake, na pia Wagibeoni, walimwogopa Yehova na kuchukua hatua ifaayo. Kile kilichowapata kinaonyesha wazi kwamba maneno haya ya mtume Mkristo Petro ni ya kweli: “Mungu si mwenye ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye humhofu na kutenda uadilifu akubalika kwake.”—Matendo 10:34, 35.
Jinsi Yehova Alivyomtendea Abrahamu na Waisraeli
8, 9. Jinsi Yehova alivyomtendea Abrahamu na taifa la Israeli ilionyeshaje kwamba hana ubaguzi?
8 Mwanafunzi Yakobo alikazia jinsi Mungu alivyomtendea kwa fadhili zisizostahiliwa Abrahamu na wazao wake. Abrahamu alikuwa “rafiki ya Yehova” kwa sababu ya imani yake, wala si kwa sababu ya asili yake. (Yakobo 2:23) Imani ya Abrahamu na upendo wake kwa Yehova ziliwaletea wazao wake baraka. (2 Mambo ya Nyakati 20:7) Yehova alimwahidi Abrahamu hivi: “Katika kubariki nitakubariki, na katika kuzidisha nitauzidisha uzao wako kama nyota za mbinguni, na kama mchanga ulioko pwani.” Lakini ona ahadi inayotolewa katika mstari unaofuata: “Katika uzao wako mataifa yote ya dunia watajibarikia.”—Mwanzo 22:17, 18; Waroma 4:1-8.
9 Matendo ya Yehova kuhusiana na Waisraeli hayakuonyesha ubaguzi, bali yalionyesha yale anayoweza kuwatendea watu wanaomtii. Matendo hayo yanaonyesha jinsi ambavyo Yehova huwatendea watumishi wake waaminifu kwa upendo mshikamanifu. Ingawa taifa la Israeli lilikuwa ‘mali ya Yehova mwenyewe,’ jambo hilo halikumaanisha kwamba watu wengine wametengwa wasiweze kunufaika na fadhili za Mungu. (Kutoka 19:5; Zaire Swahili Bible; Kumbukumbu la Torati 7:6-8) Naam, Yehova aliwakomboa Waisraeli kutoka utumwani huko Misri kisha akasema: “Ni ninyi tu niliowajua katika jamaa zote zilizo duniani.” Lakini kupitia nabii Amosi na wengine, Yehova pia aliwatolea “mataifa yote” tumaini zuri.—Amosi 3:2; 9:11, 12; Isaya 2:2-4.
Yesu Ni Mwalimu Asiye na Ubaguzi
10. Yesu alimwigaje Baba yake kwa kutoonyesha ubaguzi?
10 Yesu aliye mwakilisho sawasawa wa Baba yake alimwiga Yehova kwa kutoonyesha ubaguzi katika huduma yake duniani. (Waebrania 1:3) Wakati huo hangaiko lake kuu lilikuwa kuwatafuta “kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli.” Hata hivyo, hakusita kumhubiria mwanamke Msamaria kwenye kisima. (Mathayo 15:24; Yohana 4:7-30) Pia alifanya mwujiza alipoombwa na ofisa mmoja wa jeshi, ambaye yaelekea hakuwa Myahudi. (Luka 7:1-10) Zaidi ya hayo alionyesha kwa matendo kwamba aliwapenda watu wa Mungu. Wanafunzi wa Yesu walihubiri pia kotekote. Ikawa wazi kwamba kustahili kupata baraka za Yehova kulitegemea mtazamo wa mtu wala si taifa lake. Watu wanyenyekevu na wenye moyo mweupe ambao walikuwa na hamu kubwa ya kujua kweli, walikubali habari njema ya Ufalme. Lakini watu wenye kiburi walimdharau Yesu na ujumbe wake. Yesu alisema: “Nakusifu hadharani wewe, Baba, Bwana wa mbingu na dunia, kwa sababu umeficha mambo hayo kwa uangalifu kutoka kwa wenye hekima na walio na akili, nawe umeyafunua kwa vitoto. Ndiyo, Ee Baba, kwa sababu kufanya hivyo kulikuja kuwa ndiyo njia ikubaliwayo na wewe.” (Luka 10:21) Tunapowatendea wengine kwa upendo na imani, tunaonyesha hatuna ubaguzi, na tunajua kwamba hivyo ndivyo Yehova anavyopenda.
11. Kutendea watu bila ubaguzi kulionyeshwaje katika kutaniko la kwanza la Kikristo?
11 Katika kutaniko la kwanza la Kikristo, Wayahudi na watu wa mataifa walikuwa sawasawa. Paulo alieleza hivi: “Utukufu na heshima na amani kwa kila mtu afanyaye lililo jema, kwa Myahudi kwanza na pia kwa Mgiriki. Kwa maana hakuna ubaguzi kwa Mungu.”b (Waroma 2:10, 11) Kile kilichoamua kama wangenufaika na fadhili zisizostahiliwa za Yehova, si asili yao, bali ni jinsi walivyotenda baada ya kujifunza kumhusu Yehova na matarajio yaliyotolewa na fidia ya Mwana wake Yesu. (Yohana 3:16, 36) Paulo aliandika: “Kwa maana yeye si Myahudi aliye hivyo kwa nje, wala tohara si ile ambayo ni ya nje juu ya mwili. Bali yeye ni Myahudi aliye hivyo kwa ndani, na tohara yake ni ile ya moyo kwa roho, wala si kwa mfumo fulani wa sheria iliyoandikwa.” Kisha kwa kubadili maneno yanayohusu jina “Myahudi” (linalomaanisha “wa Yuda,” yaani, aliyesifiwa), Paulo aliongeza kusema hivi: “Sifa ya huyo huja, si kutoka kwa wanadamu, bali kutoka kwa Mungu.” (Waroma 2:28, 29) Yehova huwasifu watu bila ubaguzi. Je, sisi nasi hufanya hivyo?
12. Andiko la Ufunuo 7:9 linatoa tazamio gani, na kwa nani?
12 Baadaye, katika maono, mtume Yohana aliona Wakristo waaminifu watiwa-mafuta wakifananishwa na taifa la kiroho lenye washiriki 144,000, “waliotiwa muhuri kutoka katika kila kabila la wana wa Israeli.” Baada ya hayo, Yohana akaona “umati mkubwa . . . kutoka katika mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha, wamesimama mbele ya kiti cha ufalme na mbele ya Mwana-Kondoo, wamevaa kanzu nyeupe; na kulikuwa na matawi ya mitende mikononi mwao.” (Ufunuo 7:4, 9) Kwa hiyo, hakuna kikundi chochote cha kijamii ambacho kimetengwa kisipatikane katika kutaniko la Kikristo la siku hizi. Watu kutoka jamii zote wanatazamia kuokoka “dhiki kubwa” inayokuja na kunywa kutoka katika “mabubujiko ya maji ya uhai” katika ulimwengu mpya.—Ufunuo 7:14-17.
Matokeo Mazuri
13-15. (a) Tunawezaje kushinda tofauti za kijamii na kitamaduni? (b) Taja mifano ya faida zinazotokana na kuonyesha urafiki.
13 Yehova anatujua vema, kama vile baba mwema anavyowajua watoto wake. Vivyo hivyo, tunapowaelewa wengine kwa kupendezwa na utamaduni na malezi yao, hali za kutofautiana hutoweka. Vizuizi vya kijamii hutoweka pia, na urafiki na upendo huimarishwa. Umoja huzidishwa. (1 Wakorintho 9:19-23) Jambo hilo huonyeshwa na kazi ya mishonari wanaotumikia katika nchi za kigeni. Wao hupendezwa na watu wanaoishi katika nchi hizo, na kwa sababu hiyo, muda si muda mishonari hao huchangamana na makutaniko ya wenyeji.—Wafilipi 2:4.
14 Matokeo mazuri ya kutokuwa na ubaguzi huonekana wazi katika nchi nyingi. Aklilu, ambaye ametoka Ethiopia, alijikuta akiwa mpweke huko London, jiji kuu la Uingereza. Hisia zake za upweke zilizidishwa na kile ambacho alikiona kuwa ukosefu wa urafiki kuelekea watu wa nchi zingine, jambo ambalo linaonekana katika majiji makubwa mengi ya Ulaya ya sasa. Aklilu alikuta hali tofauti kama nini alipohudhuria mkutano wa Kikristo katika Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova! Waliokuwapo walimkaribisha, na baada ya muda mfupi akajisikia mwenye kustarehe. Alifanya maendeleo ya haraka katika kuzidisha uthamini wake kwa Muumba. Muda si muda akatafuta nafasi za kueneza habari njema za Ufalme kwa wengine katika eneo hilo. Siku moja mwenzake aliyekuwa akihubiri pamoja naye alimwuliza Aklilu miradi yake maishani. Aklilu akajibu mara moja kwamba alitazamia siku moja kuwa katika kutaniko linaloongea lugha ya Kiamhari. Wazee wa kutaniko hilo la Kiingereza waliposikia jambo hilo wakapanga haraka hotuba ya watu wote iliyotegemea Biblia itolewe kwa lugha ya Aklilu. Walipoalikwa, wageni na watu wa eneo hilo walihudhuria kwa wingi ili kuunga mkono mkutano wa kwanza wa lugha ya Kiamhari huko Uingereza. Leo, Waethiopia na watu wengine wanaozungumza Kiamhari katika eneo hilo wameungana katika kutaniko hilo linalozidi kukua. Wengi hapo wameona kwamba hakuna jambo lolote linaloweza kuwazuia kuwa upande wa Yehova na wameonyesha hilo kupitia ubatizo wa Kikristo.—Matendo 8:26-36.
15 Kuna tabia na malezi mbalimbali. Lakini mambo hayo hayaonyeshi kwamba mtu ni wa hali ya juu au ni wa hali ya chini; hizo ni hali zinazotofautiana tu. Walipokuwa wakitazama ubatizo wa watumishi wapya wa Yehova katika kisiwa cha Malta, kelele za shangwe za Mashahidi wa kisiwa hicho ziliongezea machozi ya furaha yaliyotiririka machoni pa wageni kutoka Uingereza. Watu wa Malta na wa Uingereza walionyesha hisia zao kwa njia tofauti, na upendo wao thabiti kwa Yehova uliimarisha vifungo vya ushirika wa Kikristo.—Zaburi 133:1; Wakolosai 3:14.
Kushinda Ubaguzi
16-18. Simulia jambo lililoonwa linaloonyesha jinsi ubaguzi unavyoweza kushindwa katika kutaniko la Kikristo.
16 Upendo wetu kwa Yehova na ndugu zetu Wakristo unapoongezeka, tunaweza kumwiga Yehova kwa ukaribu zaidi kuhusiana na maoni yetu kuwaelekea wengine. Tunaweza kushinda ubaguzi wowote ambao huenda tulikuwa nao zamani kuelekea watu wa mataifa, jamii, au tamaduni fulani. Kwa mfano, fikiria kisa cha Albert aliyetumikia Jeshi la Uingereza wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu na ambaye alikamatwa na Wajapani wakati Singapore ilipotekwa mwaka wa 1942. Baadaye akafanya kazi kwa muda wa miaka mitatu hivi kwenye “reli ya kifo,” karibu na lile lililokuja kuitwa daraja la mto Kwai. Alipoachiliwa huru mwishoni mwa vita, alikuwa na uzito wa kilogramu 32, utaya na pua lake lilikuwa limevunjika, na alikuwa akiugua ugonjwa wa kuhara damu, choa, na malaria. Hali ya maelfu ya wafungwa wenzake ilikuwa mbaya hata zaidi; wengi wao walikufa. Kwa sababu ya ukatili ambao Albert aliona na kutendewa, alirudi nyumbani mwaka wa 1945 akiwa mwenye uchungu mwingi na hakutaka kusikia lolote kuhusu Mungu wala dini.
17 Irene, mke wa Albert, alikuja kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Ili kumpendeza mke wake, Albert alihudhuria mikutano kadhaa katika kutaniko la Mashahidi wa Yehova la eneo hilo. Mkristo mmoja kijana aliyeitwa Paul, ambaye alikuwa mhudumu wa wakati wote, alimtembelea Albert ili ajifunze Biblia pamoja naye. Muda si muda Albert akatambua kwamba Yehova huwatazama watu kulingana na hali ya mioyo yao. Alijiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa.
18 Baadaye Paul alihamia London, akajifunza Kijapani, naye akashirikiana na kutaniko la lugha ya Kijapani. Alipopendekeza kwamba awapeleke Mashahidi kadhaa Wajapani katika kutaniko lake la zamani, ndugu wa huko walikumbuka kwamba Albert alikuwa mwenye ubaguzi sana kuwaelekea Wajapani. Tangu arudi Uingereza, Albert alikuwa ameepuka kukutana uso kwa uso na mtu yeyote kutoka Japani, kwa hiyo ndugu hao wakawa na wasiwasi kuhusu jinsi ambavyo angewatendea Wajapani hao. Haikuwa lazima wawe na wasiwasi—Albert aliwapokea wageni hao kwa upendo kamili wa kidugu.—1 Petro 3:8, 9.
“Panukeni”
19. Ni shauri gani la mtume Paulo linaloweza kutusaidia ikiwa tuna mwelekeo wowote wa ubaguzi?
19 Mfalme Sulemani mwenye hekima aliandika: “Kupendelea watu si kwema.” (Mithali 28:21) Ni rahisi kuwa na urafiki na watu ambao tunawajua vizuri. Hata hivyo, nyakati nyingine sisi huwa na mwelekeo wa kutovutiwa sana na wale ambao hatuwajui vizuri. Mtumishi wa Yehova hapaswi kuwa na ubaguzi wa aina hiyo. Kwa kweli, sote tunapaswa kufuata shauri la Paulo lililo wazi kwamba ‘tupanuke.’ Naam, na tupanuke katika upendo wetu kwa Wakristo wenzetu wa malezi mbalimbali.—2 Wakorintho 6:13.
20. Ni katika hali gani za maisha tunazopaswa kumwiga Yehova, Mungu wetu asiye na ubaguzi?
20 Hata kama tuna pendeleo la mwito wa mbinguni au tazamio la kuishi milele duniani, tunaweza kuwa na umoja katika kundi moja chini ya Mchungaji mmoja, ikiwa hatuna ubaguzi. (Waefeso 4:4, 5, 16) Kujitahidi kumwiga Yehova, Mungu wetu asiye na ubaguzi, kunaweza kutusaidia katika huduma yetu ya Kikristo, katika familia zetu, na kutanikoni, na katika hali zote za maisha. Tunawezaje kufanya hivyo? Makala inayofuata itazungumzia habari hiyo.
[Maelezo ya Chini]
a Baadaye, watu walitunga nyimbo takatifu ili kusifu matendo makuu ya Yehova.—Zaburi 135:8-11; 136:11-20.
-
-
Tafuta Mema Ndani ya Watu WoteMnara wa Mlinzi—2003 | Juni 15
-
-
Tafuta Mema Ndani ya Watu Wote
“Nikumbuke, Ee Mungu wangu, ili unitendee mema.”—NEHEMIA 13:31.
1. Yehova huwatendeaje wote kwa wema?
BAADA ya siku nyingi zenye mawingu na weusi, mwangaza wa jua huleta badiliko zuri. Watu huchangamka na kufurahi. Vivyo hivyo, baada ya vipindi virefu vya jua kali na kiangazi, manyunyu, au hata mvua kubwa, huburudisha sana. Yehova, Muumba wetu mwenye upendo ameweka duniani zawadi hii nzuri ya hali ya hewa. Yesu alikazia ukarimu wa Mungu alipofundisha hivi: “Endeleeni kupenda maadui wenu na kusali kwa ajili ya wale wanaowanyanyasa nyinyi; ili mpate kujithibitisha wenyewe kuwa wana wa Baba yenu aliye katika mbingu, kwa kuwa yeye hufanya jua lake lichomoze juu ya watu waovu na wema na kufanya mvua inyeshe juu ya watu waadilifu na wasio waadilifu.” (Mathayo 5:43-45) Yehova huwatendea wote kwa wema. Watumishi wake wanapaswa kujitahidi kumwiga kwa kutafuta mema ndani ya wengine.
2. (a) Ni kwa msingi gani Yehova hutenda kwa wema? (b) Yehova huona nini kuhusiana na jinsi tunavyoitikia wema wake?
2 Ni kwa msingi gani Yehova hutenda kwa wema? Tangu Adamu atende dhambi, Yehova hakuacha kutafuta wema ndani ya wanadamu. (Zaburi 130:3, 4) Kusudi lake ni kurudisha wanadamu watiifu waishi katika Paradiso. (Waefeso 1:9, 10) Fadhili zake zisizostahiliwa zimetupatia tumaini la kukombolewa katika dhambi na hali ya kutokamilika kupitia Mbegu iliyoahidiwa. (Mwanzo 3:15; Waroma 5:12, 15) Kukubali mpango wa fidia hutuwezesha kurudia ukamilifu. Kati ya mambo mengine, sasa Yehova anachunguza kila mmoja wetu aone jinsi tunavyoitikia ukarimu wake. (1 Yohana 3:16) Yeye huona yote tufanyayo ili tuonyeshe tunathamini wema wake. Mtume Paulo aliandika: “Mungu si asiye mwadilifu ili asahau kazi yenu na upendo mlioonyesha kwa ajili ya jina lake.”—Waebrania 6:10.
3. Tunapaswa kufikiria swali gani?
3 Hivyo basi, tunawezaje kumwiga Yehova tunapotafuta mema ndani ya wengine? Na tufikirie jibu la swali hili katika sehemu tatu za maisha: (1) huduma ya Kikristo, (2) familia, (3) kutaniko, na (4) uhusiano wetu na wengine.
Katika Kuhubiri na Kufanya Wanafunzi
4. Ni katika njia gani kushiriki katika huduma ya Kikristo ni wonyesho wa kutafuta mema ndani ya wengine?
4 Alipokuwa akijibu maswali ya wanafunzi wake kuhusu maana ya mfano wa ngano na magugu, Yesu alisema kwamba “shamba ndio ulimwengu.” Tukiwa wanafunzi wa Kristo wa siku hizi, tunaona jambo hilo kuwa kweli wakati tunaposhiriki katika huduma. (Mathayo 13:36-38; 28:19, 20) Huduma yetu ya shambani inatia ndani kutangaza hadharani imani yetu. Mashahidi wa Yehova wanajulikana vizuri kwa sababu ya huduma yao ya kuhubiri nyumba kwa nyumba na barabarani. Jambo hilo huthibitisha kwamba sisi tuna bidii katika kutafuta wote wanaostahili ujumbe wa Ufalme. Yesu aliagiza hivi: “Katika jiji lolote lile au kijiji chochote kile mwingiamo, tafuteni kabisa ni nani humo anayestahili.”—Mathayo 10:11; Matendo 17:17; 20:20.
5, 6. Kwa nini sisi huendelea kuwatembelea watu tena na tena nyumbani kwao?
5 Tunapowatembelea watu bila kutarajiwa, sisi huona jinsi wanavyoitikia ujumbe wetu. Nyakati nyingine mtu mmoja katika familia atatusikiliza, huku mwingine katika nyumba hiyohiyo akikataa na kusema, “Sisi hatupendezwi,” na hivyo tunaondoka. Tunasikitika kama nini wakati mtu mmoja anayepinga au asiyependezwa anapofanya mwingine asisikilize! Hivyo basi, tunaweza kufanya nini ili kuendelea kutafuta mema ndani ya wote?
6 Huenda kutembelea nyumba hiyo tena tunapohubiri eneo hilo, kukatupatia nafasi ya kuzungumza moja kwa moja na yule aliyekatiza ziara ya kwanza. Kukumbuka yaliyotukia wakati huo kunaweza kutusaidia tujitayarishe. Huenda mpinzani huyo alitenda hivyo kwa nia nzuri, akiona kwamba anapaswa kumzuia yule mwenye kuitikia asisikilize ujumbe wa Ufalme. Labda maoni yake yaliathiriwa na habari za uwongo kuhusu nia yetu. Lakini jambo hilo halituzuii kuendelea kuhubiri habari njema za Ufalme katika nyumba hiyo nasi hujaribu kwa busara kurekebisha maoni yasiyofaa. Lengo letu ni kuwasaidia wote wapate ujuzi sahihi kumhusu Mungu. Kisha huenda Yehova akamvuta mtu huyo kwake.—Yohana 6:44; 1 Timotheo 2:4.
7. Ni nini kinachoweza kutusaidia tuwe na maoni yanayofaa tunapowafikia watu?
7 Katika maagizo aliyowatolea wanafunzi wake, Yesu alitaja upinzani wa watu wa familia. Alisema hivi: “Nilikuja kusababisha mgawanyiko, na mtu dhidi ya baba yake, na binti dhidi ya mama yake, na mke kijana dhidi ya mama-mkwe wake.” Yesu aliendelea kusema: “Maadui wa mtu watakuwa watu wa nyumbani mwake mwenyewe.” (Mathayo 10:35, 36) Hata hivyo, hali na mitazamo ya watu hubadilika. Ugonjwa usiotarajiwa, kufiwa na mtu wa ukoo, misiba, matatizo ya kihisia moyo, na kadhalika, huathiri jinsi watu wanavyoitikia mahubiri yetu. Ikiwa tuna maoni yasiyofaa kwamba watu tunaowahubiria hawataitikia, je, kweli tunatafuta mema ndani yao? Mbona tusiwatembelee wakati mwingine tukiwa wenye furaha? Huenda itikio lao likawa tofauti. Wakati mwingine, watu wanaweza kuitikia kwa njia nzuri ikitegemea yale tunayosema na jinsi tunavyoyasema. Bila shaka, kusali kwa bidii kwa Yehova kabla ya kuanza mahubiri kutatusaidia kuwa na maoni yanayofaa na kutoa ujumbe wa Ufalme kwa njia yenye kuvutia wote.—Wakolosai 4:6; 1 Wathesalonike 5:17.
8. Kunaweza kuwa na matokeo gani Wakristo wanapotafuta mema ndani ya watu wa ukoo wasioamini?
8 Katika makutaniko fulani, wengi wanaomtumikia Yehova ni watu wa familia moja. Mara nyingi, kile kilichowavutia vijana na kuwafanya wawe na heshima ni ule uvumilivu wa mtu wa ukoo mwenye umri mkubwa ambaye uhusiano wake mwema na watu wa familia na katika ndoa ulifanya vijana hao wabadilishe mioyo yao “bila neno.” Kupitia shauri la mtume Petro, wake wengi Wakristo wamesaidiwa kuwavuta waume zao “bila neno.”—1 Petro 3:1, 2.
Katika Familia
9, 10. Yakobo na Yosefu walitafuta mema katika familia yao jinsi gani?
9 Uhusiano wa karibu unaowaunganisha watu wa familia ni sehemu nyingine inayoweza kutusaidia kutafuta mema ndani ya wengine. Fikiria jambo tunaloweza kujifunza kutokana na jinsi Yakobo alivyowatendea wanawe. Kwenye Mwanzo sura ya 37, mstari wa 3 na 4, Biblia husema kwamba Yakobo alimpenda Yosefu sana. Ndugu za Yosefu walimwonea wivu sana hivi kwamba wakapanga njama ya kumuua. Hata hivyo, ona mtazamo ambao Yakobo na Yosefu walionyesha baadaye maishani. Wote walitafuta mema katika familia zao.
10 Yosefu aliwakaribisha ndugu zake alipokuwa msimamizi mkuu wa chakula wakati wa njaa huko Misri. Ingawa hakujitambulisha kwao mara moja, Yosefu alipanga mambo ili kuhakikisha kwamba walitunzwa vizuri na kupata chakula cha kumpelekea baba yao mzee. Naam, ingawa zamani ndugu zake walimchukia, Yosefu alitenda kwa njia iliyowanufaisha. (Mwanzo 41:53–42:8; 45:23) Vivyo hivyo, alipokuwa anakaribia kufa, Yakobo aliwatangazia wanawe wote baraka za unabii. Ingawa matendo yao mabaya yalifanya wanyimwe mapendeleo fulani, wote walipata urithi katika nchi waliyoahidiwa. (Mwanzo 49:3-28) Kwa kufanya hivyo Yakobo alionyesha upendo wenye kudumu.
11, 12. (a) Ni mfano gani wa unabii unaokazia umuhimu wa kutafuta mema katika familia? (b) Tunajifunza jambo gani kutokana na kielelezo cha baba katika mfano wa Yesu wa mwana mpotevu?
11 Ustahimilivu wa Yehova katika kushughulika na taifa la Israeli lisilo na imani hutusaidia kupata ufahamu zaidi kuhusiana na kutafuta mema ndani ya watu wake. Kwa kutumia hali katika familia ya nabii Hosea, Yehova alionyesha upendo wake wenye kudumu. Gomeri, mke wa Hosea, alifanya uzinzi tena na tena. Licha ya hayo, Yehova alimwagiza Hosea hivi: “Enenda tena, mpende mwanamke apendwaye na rafiki yake, naye ni mzinzi; kama vile BWANA awapendavyo wana wa Israeli, ingawa wanaigeukia miungu mingine, na kupenda mikate ya zabibu kavu.” (Hosea 3:1) Kwa nini alitoa maagizo hayo? Yehova alijua kwamba watu kutoka katika mataifa yaliyoziacha njia zake, wangeitikia fadhili zake ifaavyo. Hosea alitangaza: “Baada ya hayo wana wa Israeli watarejea, na kumtafuta BWANA, Mungu wao, na Daudi, mfalme wao; nao watamwendea BWANA na wema wake kwa kicho siku za mwisho.” (Hosea 3:5) Kwa hakika, huu ni mfano mzuri wa kutafakari unapokuwa na matatizo ya familia. Utaweka mfano mzuri wa subira kwa kuendelea kutafuta mema ndani ya watu wengine wa familia.
12 Mfano wa Yesu wa mwana mpotevu unatupatia ufahamu zaidi juu ya jinsi tuwezavyo kutafuta mema kuhusiana na familia yetu. Yule mwana mdogo alirudi nyumbani baada ya kuacha maisha mapotovu. Baba yake alimtendea kwa huruma. Baba huyo aliitikiaje malalamiko ya mwana wake mkubwa ambaye hakuwa amewahi kuiacha familia yao? Akizungumza na mwana wake mkubwa, baba huyo alisema: “Mtoto, wewe umekuwa pamoja nami sikuzote, na vitu vyote vilivyo vyangu ni vyako.” Hilo halikuwa jibu la ukali lakini baba huyo alikuwa anamthibitishia tu kwamba anampenda. “Ilitupasa tu kujifurahisha wenyewe na kushangilia,” akaendelea kusema, “kwa sababu huyu ndugu yako alikuwa amekufa naye akaja kwenye uhai, naye alikuwa amepotea naye akapatikana.” Vivyo hivyo, tunaweza kuendelea kutafuta mema ndani ya wengine.—Luka 15:11-32.
Katika Kutaniko la Kikristo
13, 14. Tunaweza kufuata sheria ya kifalme kwa njia gani katika kutaniko la Kikristo?
13 Tukiwa Wakristo, tunajitahidi kufuata sheria ya kifalme ya upendo. (Yakobo 2:1-9) Ni kweli kwamba huenda tukashirikiana na watu ambao hali zao ni tofauti na zetu kuhusiana na vitu vya kimwili. Lakini je, bado tunakuwa na “tofauti za kitabaka” zinazotegemea jamii, utamaduni, au hata dini ya mtu ya zamani? Ikiwa ndivyo, tunaweza kufuata shauri la Yakobo jinsi gani?
14 Sisi huonyesha ukarimu wetu wa Kikristo tunapowakaribisha wote waliohudhuria mikutano yetu ya Kikristo. Tunapochukua hatua ya kwanza kuzungumza na wapya wanaokuja kwenye Jumba la Ufalme, huenda wasiwasi na haya waliokuwa nayo mwanzoni ikaisha. Naam, baadhi ya wale wanaohudhuria mikutano ya Kikristo kwa mara ya kwanza husema hivi: “Kila mtu alipendezwa nami. Ni kana kwamba kila mtu alikuwa ananijua. Nilijisikia mwenye kustarehe sana.”
15. Vijana kutanikoni wanaweza kusaidiwaje ili wapendezwe na walio wazee?
15 Katika makutaniko fulani, huenda vijana kadhaa wakawa wanakusanyika pamoja nje ya Jumba la Ufalme baada ya mikutano, wakiepuka kushirikiana na wale wenye umri mkubwa. Ni jambo gani lifaalo linaloweza kufanywa ili kuacha zoea hilo? Hatua ya kwanza ni wazazi kuwazoeza watoto hao nyumbani na kuwatayarisha kwa ajili ya mikutano. (Mithali 22:6) Wanaweza kuwapa kazi ya kupanga vichapo ili wote wabebe vichapo vinavyohitajiwa kwenye mikutano. Wazazi pia wana nafasi nzuri ya kuwatia moyo watoto wao wazungumze kidogo na walio wazee na wagonjwa kwenye Jumba la Ufalme. Watoto wanaweza kujisikia wenye furaha wanapokuwa na jambo la maana la kuzungumza na watu hao.
16, 17. Watu wazima wanawezaje kutafuta mema ndani ya vijana kutanikoni?
16 Ndugu na dada walio na umri mkubwa wanapaswa pia kupendezwa na vijana kutanikoni. (Wafilipi 2:4) Wanaweza kuchukua hatua ya kwanza kuongea na vijana kwa njia yenye kuwatia moyo. Kwa kawaida mambo fulani muhimu huzungumziwa kwenye mikutano. Vijana wanaweza kuulizwa kama walifurahia mikutano na kama kuna mambo yoyote hasa waliyothamini na wanayoweza kufuata maishani. Vijana ni sehemu muhimu kutanikoni, hivyo wanahitaji kupewa shukrani wanaposikiliza kwa makini na kusifiwa wanapotoa maelezo au wanaposhughulikia mgawo wowote wakati wa mikutano. Baadaye maishani, kile kitakachoamua kama vijana wanaweza kushughulikia vizuri migawo mikubwa zaidi ni jinsi wanavyochangamana na wale walio na umri mkubwa kutanikoni na jinsi wanavyofanya kazi ndogo-ndogo nyumbani.—Luka 16:10.
17 Kwa kukubali migawo, vijana fulani hufanya maendeleo na kufikia kuwa na sifa za kiroho zinazowawezesha kupewa migawo mikubwa hata zaidi. Ikiwa wana jambo la kufanya, vijana wanaweza kuepuka mwenendo mpumbavu. (2 Timotheo 2:22) Migawo hiyo inaweza ‘kujaribu kufaa’ kwa ndugu wanaojitahidi kufikia kuwa watumishi wa huduma. (1 Timotheo 3:10) Utayari wao wa kushiriki kwenye mikutano na bidii yao katika huduma, na vilevile mtazamo wa kuwajali wengine wote kutanikoni, huwawezesha wazee kutambua uwezo wa vijana hao wanapofikiria kuwapa migawo zaidi.
Tafuta Mema Ndani ya Wote
18. Ni mtego gani unaopaswa kuepukwa wakati wa hukumu, na kwa nini?
18 “Kupendelea watu katika hukumu si kwema,” yasema Mithali 24:23. Hekima ya kimbingu hutaka kwamba wazee waepuke ubaguzi wanapohukumu mambo katika kutaniko. Yakobo alisema: “Hekima ya kutoka juu kwanza kabisa ni safi kiadili, kisha yenye kufanya amani, yenye kukubali sababu, tayari kutii, yenye kujaa rehema na matunda mema, isiyofanya tofauti zenye ubaguzi, si ya kinafiki.” (Yakobo 3:17) Ni wazi, basi, kwamba wazee wanapotafuta mema ndani ya wengine, wanahitaji kuhakikisha kwamba hukumu yao haiathiriwi na urafiki au hisia za kibinafsi. “Mungu asimama katika kusanyiko la Mungu,” akaandika mtunga-zaburi Asafu. “Katikati ya miungu [au “walio kama miungu,” yaani, mahakimu wa kibinadamu] anahukumu. Hata lini mtahukumu kwa dhuluma, na kuzikubali nyuso za wabaya?” (Zaburi 82:1, 2) Vivyo hivyo, wazee Wakristo huepuka kuonyesha upendeleo wa aina yoyote wanaposhughulikia mambo yanayohusu marafiki au watu wao wa ukoo. Hivyo wanadumisha umoja kutanikoni na kuiruhusu roho ya Yehova kufanya kazi bila kizuizi.—1 Wathesalonike 5:23.
19. Ni katika njia zipi tunaweza kutafuta mema ndani ya wengine?
19 Tunapotafuta mema ndani ya ndugu zetu, tutakuwa tunaonyesha mtazamo kama wa Paulo alipozungumza na kutaniko la Wathesalonike. Alisema: “Zaidi ya hayo, tuna uhakika katika Bwana kuhusu nyinyi, kwamba mnafanya na mtaendelea kufanya mambo tuagizayo.” (2 Wathesalonike 3:4) Tutakuwa tayari zaidi kufunika makosa ya wengine tunapotafuta mema ndani yao. Na tutafute mambo ambayo tunaweza kuwapongeza ndugu zetu, na kuepuka kabisa roho ya kuchambua-chambua wengine. Paulo aliandika, “Kitafutwacho katika wasimamizi-nyumba ni mtu kupatwa akiwa mwaminifu.” (1 Wakorintho 4:2) Imani ya wale wanaosimamia kutaniko, na pia imani ya ndugu na dada zetu wote Wakristo hutufanya tuwapende. Hivyo tunakuwa na ukaribu nao, na urafiki wetu wa Kikristo huimarishwa. Tunakuwa na maoni kama yale ambayo Paulo alikuwa nayo kuelekea akina ndugu katika siku zake. Wao ni ‘wafanyakazi wenzetu kwa ajili ya ufalme wa Mungu’ na ‘msaada wenye kututia nguvu.’ (Wakolosai 4:11) Hivyo tunaonyesha mtazamo wa Yehova.
20. Wale wanaotafuta mema ndani ya wengine watapata baraka gani?
20 Hakika sisi tunairudia sala ya Nehemia: “Nikumbuke, Ee Mungu wangu, ili unitendee mema.” (Nehemia 13:31) Tunafurahi kama nini kwamba Yehova hutafuta mema ndani ya watu! (1 Wafalme 14:13) Na tufanye vivyo hivyo tunaposhughulika na wengine. Kufanya hivyo kunatupa tazamio la kukombolewa na kuishi milele katika ulimwengu mpya ulio karibu sana.—Zaburi 130:3-8.
-