Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Wasaidieni Kondoo Waliopotea
    Mnara wa Mlinzi—2008 | Novemba 15
    • Wasaidieni Kondoo Waliopotea

      “Shangilieni pamoja nami, kwa sababu nimempata kondoo wangu aliyekuwa amepotea.”—LUKA 15:6.

      1. Yesu ameonyesha jinsi gani kwamba yeye ni mchungaji mwenye upendo?

      YESU KRISTO, Mwana mzaliwa-pekee wa Yehova, anaitwa “mchungaji mkuu wa kondoo.” (Ebr. 13:20) Maandiko yalitabiri kuja kwake na yalionyesha kwamba alikuwa Mchungaji wa pekee aliyejitahidi kuwatafuta “kondoo waliopotea” wa Israeli. (Mt. 2:1-6; 15:24) Zaidi ya hayo, kama vile mchungaji halisi anavyoweza kuwa tayari kufa ili kulinda kondoo wake, Yesu alikufa akiwa dhabihu ya fidia kwa ajili ya watu walio kama kondoo ambao wangefaidika kupitia dhabihu yake.—Yoh. 10:11, 15; 1 Yoh. 2:1, 2.

      2. Ni mambo gani ambayo huenda yamewafanya Wakristo fulani kuwa wasiotenda?

      2 Inasikitisha kwamba watu fulani ambao walionekana kuwa wanathamini dhabihu ya Yesu na wakajiweka wakfu kwa Mungu hawashirikiani tena na kutaniko la Kikristo. Pengine kuvunjika moyo, matatizo ya afya, au mambo mengine yalipunguza bidii yao na hivyo wakawa wasiotenda. Hata hivyo, ni katika kundi la Mungu tu ndipo wanapoweza kupata amani na furaha iliyotajwa na Daudi katika Zaburi ya 23. Kwa mfano, Daudi aliimba hivi: “Yehova ni Mchungaji wangu. Sitakosa chochote.” (Zab. 23:1) Wale walio katika kundi la Mungu hawakosi maandalizi yoyote ya kiroho, lakini kondoo waliopotea wanayakosa. Ni nani anayeweza kuwasaidia? Msaada unaweza kutolewa jinsi gani? Kwa kweli, tunaweza kufanya nini ili kuwasaidia warudi katika kundi?

      Ni Nani Anayeweza Kusaidia?

      3. Yesu alionyesha jinsi gani kile ambacho kinahitajiwa ili kuokoa kondoo wa malisho ya Mungu?

      3 Jitihada nyingi zinahitajiwa ili kuokoa kondoo waliopotea wa malisho ya Mungu. (Zab. 100:3) Yesu alitoa mfano kuhusu jambo hilo aliposema hivi: “Mtu akiwa na kondoo 100 na mmoja apotee, je, hatawaacha wale 99 milimani na kuondoka kwenda kumtafuta yule anayepotea? Naye akimpata, hakika ninawaambia ninyi, yeye humshangilia huyo zaidi kuliko wale 99 ambao hawakupotea. Vivyo hivyo Baba yangu aliye mbinguni hatamani kwamba mmoja wa wadogo hawa aangamie.” (Mt. 18:12-14) Ni nani anayeweza kuwasaidia watu walio kama kondoo waliopotea?

      4, 5. Wazee wanapaswa kuwa na mtazamo gani kuhusu kundi la Mungu?

      4 Ili wazee Wakristo wawasaidie kondoo waliopotea, ni lazima wakumbuke kwamba kundi la Mungu ni kutaniko la watu waliojiweka wakfu kwa Yehova—ndiyo, ni ‘kundi lenye thamani la malisho ya Mungu.’ (Zab. 79:13) Kondoo hao wapendwa wanahitaji kutunzwa kwa upendo, hivyo ni lazima wachungaji wenye upendo wamjali kila kondoo. Kufanya ziara za uchungaji zenye urafiki kunaweza kuwasaidia sana kondoo hao. Mchungaji anapowatia moyo kwa upendo, hilo linaweza kuwajenga kiroho na kuchochea tamaa yao ya kurudi katika kundi.—1 Kor. 8:1.

      5 Wachungaji wa kundi la Mungu wana daraka la kuwatafuta kondoo waliopotea na kujitahidi kuwasaidia. Mtume Paulo aliwakumbusha wazee Wakristo wa jiji la kale la Efeso kuhusu madaraka yao ya uchungaji aliposema hivi: “Jiangalieni ninyi wenyewe na kundi lote, ambalo roho takatifu imewaweka ninyi rasmi kuwa waangalizi kati yake, kulichunga kutaniko la Mungu, ambalo alilinunua kwa damu ya Mwana wake mwenyewe.” (Mdo. 20:28) Vivyo hivyo, mtume Petro aliwapa wanaume wazee watiwa-mafuta himizo hili: “Lichungeni kundi la Mungu lililo chini ya uangalizi wenu, si kwa kulazimishwa, bali kwa kupenda; wala si kwa kupenda pato lisilo la haki, bali kwa hamu; wala si kama kwa kupiga ubwana juu ya wale ambao ni urithi wa Mungu, bali kuwa vielelezo kwa kundi.”—1 Pet. 5:1-3.

      6. Kwa nini kondoo wa Mungu wanahitaji kutunzwa na wachungaji hasa leo?

      6 Wachungaji Wakristo wanahitaji kumwiga yule “mchungaji mwema,” Yesu. (Yoh. 10:11) Alihangaikia sana kondoo wa Mungu na akakazia umuhimu wa kuwatunza alipomwambia Simoni Petro ‘achunge kondoo Wake wadogo.’ (Soma Yohana 21:15-17.) Kondoo wanahitaji kutunzwa hasa leo, kwa kuwa Ibilisi amezidisha jitihada zake za kuvunja utimilifu wa wale waliojiweka wakfu kwa Mungu. Shetani anatumia udhaifu wa kimwili na anautumia pia ulimwengu ili kujaribu kuwashawishi kondoo wa Yehova watumbukie katika dhambi. (1 Yoh. 2:15-17; 5:19) Kwa kuwa wale wasiotenda wanaweza kushambuliwa kwa urahisi, wanahitaji kusaidiwa ili wafuate shauri la ‘kutembea kwa roho.’ (Gal. 5:16-21, 25) Ili tuwasaidie kondoo hao tunahitaji kumtegemea Mungu kupitia sala, tunahitaji mwongozo wa roho yake, na kutumia Neno lake kwa ustadi.—Met. 3:5, 6; Luka 11:13; Ebr. 4:12.

      7. Ni jambo la maana kadiri gani kwa wazee kuwachunga kondoo walio chini ya utunzaji wao?

      7 Mchungaji katika Israeli la kale alitumia fimbo au bakora ndefu iliyopindika ili kuliongoza kundi lake. Kondoo walipoingia au kutoka katika zizi, ‘walipita chini ya bakora’ hiyo na kuhesabiwa na mchungaji. (Law. 27:32; Mika 2:12; 7:14) Vivyo hivyo, mchungaji Mkristo anahitaji kujua hali ya kundi la Mungu lililo chini ya utunzaji wake. (Linganisha na Methali 27:23.) Ndiyo sababu uchungaji ni kati ya mambo ya maana ambayo baraza la wazee linazungumzia. Hilo linatia ndani kufanya mipango ya kusaidia kondoo waliopotea. Yehova mwenyewe alisema kwamba atawatafuta kondoo wake na kuwatunza. (Eze. 34:11) Kwa hiyo, Mungu anafurahi wazee wanapochukua hatua kama hizo ili kuwasaidia kondoo waliopotea warudi katika kundi.

      8. Wazee wanaweza kufanya mambo gani ili kuwapa kondoo uangalifu wa pekee?

      8 Mchungaji wa kundi la Mungu anapomtembelea mwamini mwenzake ambaye ni mgonjwa, mgonjwa huyo anaweza kuchangamka na kutiwa moyo. Inakuwa hivyo pia wakati kondoo ambaye ni mgonjwa kiroho anapopewa uangalifu wa pekee. Wazee wanaweza kusoma maandiko, kuzungumzia habari fulani zilizochapishwa, kuzungumzia mambo makuu ya mikutano, kusali pamoja na asiyetenda, na kadhalika. Wanaweza kumweleza kwamba washiriki wa kutaniko watafurahi kumwona akianza tena kuhudhuria mikutano ya kutaniko. (2 Kor. 1:3-7; Yak. 5:13-15) Kumtembelea, kumpigia simu, au kumwandikia barua kunaweza kumtia moyo sana! Kumsaidia kondoo aliyepotea kunaweza pia kuongeza shangwe ya mchungaji Mkristo mwenye huruma.

      Jitihada za Pamoja

      9, 10. Kwa nini unaweza kusema kwamba si wazee tu wanaopaswa kumjali kondoo aliyepotea?

      9 Tunaishi katika nyakati hatari na zenye shughuli nyingi, hivyo huenda tusitambue kwamba mwamini mwenzetu anapeperushwa kutoka katika kutaniko. (Ebr. 2:1) Hata hivyo, kondoo wa Yehova ni wenye thamani sana machoni pake. Kila mmoja wao ni mwenye thamani, kama vile kila sehemu au kiungo cha mwili wa mwanadamu kilivyo chenye thamani. Hivyo, sote tunahitaji kuwajali ndugu zetu na kutunzana kikweli. (1 Kor. 12:25) Je, una mtazamo kama huo?

      10 Ingawa wazee wanaongoza katika jitihada za kuwatafuta na kuwasaidia kondoo waliopotea, si waangalizi Wakristo tu wanaopaswa kuwajali waamini wenzao waliopotea. Wengine pia wanaweza kushirikiana na wachungaji hao. Tunaweza na tunapaswa kuwatia moyo na kuwasaidia kiroho ndugu na dada zetu wanaohitaji kusaidiwa kurudi katika kundi. Tunaweza kufanya nini ili kuwasaidia?

      11, 12. Unaweza kupata pendeleo gani la kumsaidia mtu anayehitaji msaada wa kiroho?

      11 Nyakati nyingine, wazee wanaweza kufanya mipango ili wahubiri wa Ufalme wenye uzoefu wajifunze Biblia pamoja na watu wasiotenda ambao wangependa kusaidiwa. Kusudi la jitihada hizo ni kuamsha tena ‘upendo waliokuwa nao mwanzoni.’ (Ufu. 2:1, 4) Waamini hao wenzetu wanaweza kujengwa na kutiwa nguvu kiroho kwa kuchunguza habari zilizochapishwa ambazo hawakupata wakati ambapo hawakuwa wakishirikiana na kutaniko.

      12 Wazee wakikuomba ujifunze pamoja na mwamini mwenzako anayehitaji msaada wa kiroho, sali ili Yehova aongoze na kubariki jitihada zako. Ndiyo, “mkabidhi Yehova mwenyewe kazi zako nayo mipango yako itafanywa imara.” (Met. 16:3) Tafakari kuhusu maandiko ya Biblia na hoja zenye kuimarisha imani ambazo unaweza kutumia unapozungumza pamoja na wale wanaohitaji msaada wa kiroho. Tafakari kuhusu mfano bora wa mtume Paulo. (Soma Waroma 1:11, 12.) Paulo alitamani sana kuwaona Wakristo huko Roma ili awape zawadi fulani ya kiroho kusudi wafanywe imara. Pia, alitazamia sana kutiana moyo nao. Je, hatupaswi kuwa na mtazamo huo tunapojitahidi kuwasaidia kondoo walioliacha kundi la Mungu?

      13. Unaweza kuzungumzia mambo gani pamoja na mtu asiyetenda?

      13 Katika mazungumzo yenu, unaweza kuuliza, “Ulipata kweli jinsi gani?” Msaidie mtu huyo asiyetenda kukumbuka mambo yaliyomletea shangwe zamani na umtie moyo kuzungumzia mambo aliyoyafurahia katika mikutano, mahubiri, na makusanyiko. Zungumzieni mambo yenye kufurahisha ambayo huenda mmefurahia pamoja katika utumishi wa Yehova. Zungumzia shangwe unayopata kwa kumkaribia Yehova. (Yak. 4:8) Mweleze jinsi unavyothamini njia ambayo Mungu anatumia kututunza tukiwa watu wake, hasa kwa kutupa faraja na tumaini katika dhiki zetu.—Rom. 15:4; 2 Kor. 1:3, 4.

      14, 15. Huenda ikafaa kuwakumbusha wasiotenda kuhusu baraka gani walizokuwa nazo?

      14 Inaelekea sana kwamba itafaa kumkumbusha yule asiyetenda baraka fulani ambazo alipata aliposhirikiana kwa ukaribu na kutaniko. Kwa mfano, alibarikiwa kwa kulijua zaidi Neno la Mungu na makusudi yake. (Met. 4:18) Alipokuwa ‘akitembea kwa roho,’ inaelekea ilikuwa rahisi zaidi kwake kupinga vishawishi vya kutenda dhambi. (Gal. 5:22-26) Kwa sababu hiyo alikuwa na dhamiri safi, na hilo lilimwezesha kusali kwa Yehova na kupata ‘amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote ambayo inalinda mioyo yetu na nguvu zetu za akili.’ (Flp. 4:6, 7) Kumbuka hoja hizo, onyesha kwamba unamjali kikweli, na usikose kamwe kumtia moyo kwa upendo ndugu au dada yako wa kiroho arudi katika kundi.—Soma Wafilipi 2:4.

      15 Tuseme wewe ni mzee na unafanya ziara ya uchungaji. Unaweza kuwatia moyo wenzi wa ndoa wasiotenda wakumbuke wakati ambapo walijifunza kweli ya Neno la Mungu kwa mara ya kwanza. Kweli ilikuwa nzuri ajabu, ilieleweka wazi, iliridhisha, na iliwaweka huru kiroho! (Yoh. 8:32) Mioyo yao ilijaa shukrani kwa sababu ya mambo ambayo walikuwa wakijifunza kumhusu Yehova, upendo wake, na makusudi yake bora! (Linganisha na Luka 24:32.) Wakumbushe kwamba Wakristo waliojiweka wakfu wanafurahia uhusiano wa karibu pamoja na Yehova na pendeleo zuri la sala. Fanya yote unayoweza kuwatia moyo wasiotenda wakubali tena “habari njema yenye utukufu ya Mungu mwenye furaha,” Yehova.—1 Tim. 1:11.

      Endeleeni Kuwaonyesha Upendo

      16. Eleza mfano unaoonyesha kwamba jitihada za kuwasaidia wengine kiroho zina manufaa.

      16 Je, kweli mapendekezo hayo yanafanya kazi? Ndiyo. Kwa mfano, kijana mmoja aliyeanza kuwa mhubiri wa Ufalme akiwa na umri wa miaka 12 alikuwa asiyetenda alipofikia umri wa miaka 15. Hata hivyo, baadaye alianza kutenda na amekuwa katika utumishi wa wakati wote kwa miaka zaidi ya 30. Alipona kiroho hasa kwa sababu alisaidiwa na mzee Mkristo. Alithamini sana msaada wa kiroho aliopokea!

      17, 18. Ni sifa gani ambazo zitakuwezesha kumsaidia mtu aliyeacha kushirikiana na kundi la Mungu?

      17 Upendo ndio unaowachochea Wakristo kuwasaidia wasiotenda warudi katika kutaniko. Yesu alisema hivi kuhusu wafuasi wake: “Ninawapa ninyi amri mpya, kwamba mpendane; kama vile ambavyo nimewapenda ninyi, ninyi nanyi mpendane vivyo hivyo. Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.” (Yoh. 13:34, 35) Ndiyo, upendo ni sifa inayowatambulisha Wakristo wa kweli. Je, Wakristo ambao wameacha kutenda hawapaswi kuonyeshwa upendo kama huo? Bila shaka wanapaswa kuonyeshwa upendo huo! Lakini, ili kuwasaidia, tunahitaji sifa fulani za Kikristo.

      18 Ili umsaidie mtu fulani ambaye ameacha kushirikiana na kundi la Mungu, unahitaji kuonyesha sifa gani? Zaidi ya upendo, huenda ukahitaji kuonyesha huruma, fadhili, upole, na ustahimilivu. Ikitegemea hali, huenda ukahitaji pia kuwa mwenye kusamehe. Paulo aliandika hivi: “Jivikeni upendo mwororo wenye huruma, fadhili, unyenyekevu wa akili, upole, na ustahimilivu. Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika juu ya mwingine. Kama vile Yehova alivyowasamehe ninyi kwa hiari, nanyi fanyeni vivyo hivyo pia. Lakini, zaidi ya mambo haya yote, jivikeni upendo, kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha muungano.”—Kol. 3:12-14.

      19. Kwa nini si kazi bure kujitahidi kuwasaidia kondoo waliopotea warudi katika kundi la Kikristo?

      19 Habari inayofuata itazungumzia kwa nini watu fulani wanaacha kushirikiana na kundi la Mungu. Pia, itaonyesha jinsi ambavyo wale wanaorudi wanaweza kutarajia kupokewa. Unapojifunza habari hiyo na kutafakari kuhusu funzo hili, uwe na hakika kwamba jitihada zozote zile unazofanya ili kuwasaidia watu walio kama kondoo warudi katika kundi la Kikristo si za bure. Katika mfumo huu wa mambo, watu wengi wanatumia maisha yao yote kujirundikia mali, lakini uhai wa mtu mmoja ni wenye thamani kuliko pesa zote ulimwenguni. Yesu alikazia jambo hilo katika mfano wake kuhusu kondoo aliyepotea. (Mt. 18:12-14) Kumbuka hilo unapofanya jitihada za haraka na za moyo wote za kuwasaidia kondoo wapendwa wa Yehova waliopotea warudi katika kundi.

  • Wasaidieni Warudi Haraka!
    Mnara wa Mlinzi—2008 | Novemba 15
    • Wasaidieni Warudi Haraka!

      “Bwana, tutaenda kwa nani? Wewe una maneno ya uzima wa milele.”—YOH. 6:68.

      1. Petro alisema nini wanafunzi wengi walipomwacha Yesu?

      WAKATI fulani, wanafunzi wengi wa Yesu Kristo walimwacha kwa sababu ya jambo fulani ambalo alifundisha. Yesu aliwauliza mitume wake: “Je, ninyi pia mnataka kwenda?” Petro akamjibu: “Bwana, tutaenda kwa nani? Wewe una maneno ya uzima wa milele.” (Yoh. 6:51-69) Hawangeweza kwenda mahali pengine. Dini ya Kiyahudi haikuwa na “maneno ya uzima wa milele,” na kwa hakika maneno hayo hayawezi kupatikana leo katika Babiloni Mkubwa, milki ya ulimwengu ya dini ya uwongo. Mtu yeyote ambaye ameacha kushirikiana na kundi la Mungu lakini anataka kumpendeza Yehova anapaswa kutambua kwamba hii ndiyo ‘saa ya kuamka kutoka katika usingizi’ na kurudi katika kundi.—Rom. 13:11.

      2. Ni jambo gani tunalopaswa kukumbuka kuhusu mambo ya siri au ya kihukumu?

      2 Yehova aliwahangaikia kondoo waliopotea wa Israeli. (Soma Ezekieli 34:15, 16.) Vivyo hivyo, wazee Wakristo wanataka na wana wajibu wa kumsaidia mtu aliye kama kondoo ambaye ameacha kushirikiana na kundi. Wakimpa mhubiri mgawo wa kujifunza na mtu asiyetenda ambaye anataka kusaidiwa, mhubiri huyo anapaswa kufanya nini akigundua kwamba mtu huyo amefanya dhambi nzito? Badala ya kutoa shauri kuhusu jambo lolote la kihukumu au la siri, mhubiri huyo anapaswa kumpendekezea azungumze na wazee. Asipofanya hivyo, mhubiri mwenyewe anapaswa kuwajulisha wazee.—Law. 5:1; Gal. 6:1.

      3. Mtu aliyekuwa na kondoo 100 alifanya nini alipompata kondoo aliyepotea?

      3 Katika habari iliyotangulia, tulitaja mfano wa Yesu kuhusu mtu aliyekuwa na kondoo 100. Kondoo mmoja alipopotea, mtu huyo aliacha wale 99 na kumtafuta huyo kondoo mmoja. Mtu huyo alishangilia sana alipompata kondoo huyo! (Luka 15:4-7) Sisi pia tunashangilia kondoo mmoja aliyepotea wa Mungu anaporudi katika kundi. Wakichochewa na upendo, wazee na wengine katika kutaniko huenda wamemtembelea mtu asiyetenda. Wao pia wanataka kumwona mtu huyo akirudi katika kundi, akitegemezwa, kulindwa, na kubarikiwa na Mungu. (Kum. 33:27; Zab. 91:14; Met. 10:22) Ni mambo gani wanayoweza kufanya ili kumsaidia mtu huyo?

      4. Tunajifunza nini katika Wagalatia 6:2, 5?

      4 Labda wanaweza kumtia moyo mtu huyo arudi katika kutaniko kwa kumwonyesha kwa fadhili kwamba Yehova anawapenda kondoo Wake na anataka tufanye tu mambo tunayoweza kufanya. Mambo hayo yanatia ndani kujifunza Biblia, kuhudhuria mikutano ya Kikristo, na kuhubiri habari njema ya Ufalme. Huenda ikafaa kusoma Wagalatia 6:2, 5 na kutaja kwamba Wakristo wanaweza kubebeana mizigo mizito, lakini “kila mmoja ataubeba mzigo wake mwenyewe” wa kuwa na wajibu mbele za Yehova. Hakuna mtu yeyote yule anayeweza kuwa mwaminifu kwa Mungu kwa ajili yetu.

      Je, “Mahangaiko ya Maisha” Yamepunguza Bidii Yao?

      5, 6. (a) Kwa nini ni jambo la maana tusikilize kwa makini waamini wenzetu wasiotenda wanapotueleza hisia zao? (b) Unaweza kuwasaidia jinsi gani wasiotenda waone kwamba wamepata hasara kwa kutoshirikiana na watu wa Mungu?

      5 Ili kujua jinsi ambavyo watawasaidia waamini wenzao wasiotenda, wazee na wahubiri wengine wakomavu wanahitaji kusikiliza kwa makini wakati watu hao wasiotenda wanapoeleza hisia zao. Tuseme wewe ni mzee na umewatembelea wenzi wa ndoa ambao wameacha kushirikiana na kutaniko kwa sababu ya “mahangaiko ya maisha.” (Luka 21:34) Huenda matatizo ya kifedha au madaraka ya familia yameongezeka na kuwafanya wawe wasiotenda kiroho. Labda wanahisi kwamba wanahitaji kupumzika kiroho, lakini unaweza kuwaeleza kwamba suluhisho si kujitenga na wengine. (Soma Methali 18:1.) Unaweza kuwauliza hivi kwa busara: “Je, mmepata furaha zaidi tangu mlipoacha kuhudhuria mikutano? Je, familia yenu imefanikiwa zaidi? Je, bado shangwe ya Yehova ni ngome yenu?”—Neh. 8:10.

      6 Kutafakari kuhusu maswali hayo kunaweza kuwasaidia wasiotenda kuona kwamba kwa sababu ya kuacha kushirikiana na kutaniko, hali yao ya kiroho na furaha yao imepungua. (Mt. 5:3; Ebr. 10:24, 25) Unaweza kuwasaidia kuona kwamba shangwe yao imepungua pia kwa sababu ya kuacha kuhubiri habari njema. (Mt. 28:19, 20) Hivyo basi, ni hatua gani ya hekima wanayopaswa kuchukua?

      7. Tunaweza kuwatia moyo wale walioacha kushirikiana na kundi wafanye nini?

      7 Yesu alisema hivi: “Jiangalieni ninyi wenyewe kwamba mioyo yenu isilemewe kamwe na kula kupita kiasi na kunywa sana na mahangaiko ya maisha . . . Endeleeni kukesha wakati wote mkiomba dua ili mpate kufanikiwa kuponyoka mambo yote hayo yaliyokusudiwa kutukia.” (Luka 21:34-36) Wale ambao wameacha kushirikiana na kundi na wanataka tena kupata furaha wanaweza kutiwa moyo kusali kwa ajili ya roho takatifu na msaada kutoka kwa Mungu na kutenda kupatana na sala zao.—Luka 11:13.

      Je, Walikwazwa?

      8, 9. Mzee anaweza kumsaidia jinsi gani mtu aliyekwazwa?

      8 Kwa kuwa wanadamu si wakamilifu, nyakati nyingine wanaweza kukosana, na mmoja wao anaweza kukwazika. Wengine wamekwazwa kwa sababu mtu mwenye kuheshimika katika kutaniko hakufuata kanuni za Biblia. Ikiwa mtu asiyetenda amekwazwa kwa sababu hiyo, mzee ambaye amemtembelea anaweza kutaja kwamba Yehova hamkwazi mtu yeyote. Kwa hiyo, kwa nini mtu avunje uhusiano wake pamoja na Mungu na watu Wake? Badala yake, anapaswa kuendelea kumtumikia Mungu, na kuwa na uhakika kwamba “Mwamuzi wa dunia yote” anajua mambo yaliyotendeka na atayashughulikia kwa njia inayofaa. (Mwa. 18:25; Kol. 3:23-25) Mtu akijikwaa kihalisi na kuanguka, hawezi kuendelea kukaa chini bila hata kujaribu kusimama.

      9 Katika jitihada zake za kutoa msaada wa kiroho, mzee anaweza kutaja kwamba baada ya muda, watu fulani wanagundua kwamba mambo yaliyowafanya wakwazike si ya maana sana kama walivyoyaona mbeleni. Na kwa kweli, huenda hali iliyowakwaza haipo tena. Ikiwa mtu alikwazika kwa sababu alitiwa nidhamu, kusali na kutafakari kunaweza kumfanya atambue kwamba yeye mwenyewe alikosea kwa kadiri fulani na kwamba hakupaswa kuruhusu nidhamu imkwaze.—Zab. 119:165; Ebr. 12:5-13.

      Je, Walikwazwa na Fundisho Fulani?

      10, 11. Ni hoja gani zinazoweza kumsaidia mtu ambaye alielewa fundisho fulani la Biblia kwa njia tofauti?

      10 Huenda wengine waliliacha kundi la Mungu kwa sababu hawakukubaliana na fundisho fulani la Biblia. Waisraeli waliowekwa huru kutoka utekwani huko Misri ‘walisahau kazi’ ambazo Mungu alifanya kwa ajili yao, nao “hawakungojea shauri lake.” (Zab. 106:13) Unaweza kumsaidia mtu asiyetenda kwa kumkumbusha kwamba “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ndiye anayeandaa chakula bora cha kiroho. (Mt. 24:45) Hivyo ndivyo mtu huyo alivyojifunza kweli. Kwa hiyo, kwa nini asiazimie kutembea tena katika kweli?—2 Yoh. 4.

      11 Anapojitahidi kuwasaidia wale ambao wameacha kushirikiana na kundi la Mungu, mzee anaweza kuzungumzia jinsi wanafunzi walivyomwacha Yesu kwa sababu walikataa jambo fulani ambalo alifundisha. (Yoh. 6:53, 66) Walipoacha kushirikiana na Kristo na wafuasi wake waaminifu, hawakuthamini tena mambo ya kiroho nao wakapoteza shangwe yao. Je, wale ambao wameacha kushirikiana na kutaniko la Kikristo wamepata mahali pengine penye chakula kingi cha kiroho? Hapana, kwa maana hakuna pengine!

      Je, Walifanya Dhambi Nzito?

      12, 13. Mtu aliyeacha kushirikiana na kundi akikubali kwamba ametenda dhambi nzito, anaweza kusaidiwa jinsi gani?

      12 Watu fulani wanaacha kuhubiri na kuhudhuria mikutano kwa sababu wamefanya dhambi nzito. Huenda wakahisi kwamba wakiungama dhambi yao kwa wazee, watatengwa na ushirika. Lakini hawawezi kutengwa na ushirika wa kutaniko ikiwa wameacha zoea hilo lisilopatana na Maandiko na ikiwa wametubu kikweli. (2 Kor. 7:10, 11) Badala yake, watakaribishwa tena, na wazee watawapa msaada wa kiroho ambao wanahitaji.

      13 Ikiwa wewe ni mhubiri mkomavu na umepewa mgawo wa kumsaidia mtu asiyetenda, unapaswa kufanya nini akikuambia kwamba amefanya dhambi nzito? Kama ilivyotajwa mapema, badala ya kujihusisha zaidi na kisa hicho, mpendekezee awafikie wazee. Ikiwa hataki kufanya hivyo, onyesha kwamba unalihangaikia jina la Yehova na hali ya kiroho ya kutaniko kwa kufuata mwelekezo wa Mungu kuhusu kushughulikia kisa cha aina hiyo. (Soma Mambo ya Walawi 5:1.) Wazee watajua jinsi ya kumsaidia mtu yeyote anayetaka kurudi na kuishi kupatana na mapenzi ya Mungu. Huenda nidhamu yenye upendo ikahitajiwa. (Ebr. 12:7-11) Mtu huyo akikubali kwamba amemtendea Mungu dhambi, ameacha kutenda dhambi, na ametubu kikweli, wazee watamsaidia, na Yehova anaweza kumsamehe.—Isa. 1:18; 55:7; Yak. 5:13-16.

      Walishangilia Mwana Aliporudi

      14. Simulia kwa maneno yako mwenyewe mfano wa Yesu kuhusu mwana mpotevu.

      14 Mhubiri aliyepewa mgawo wa kumsaidia kondoo aliyepotea anaweza kusimulia mfano wa Yesu katika Luka 15:11-24. Katika mfano huo, kijana anapoteza urithi wake wote kwa kuponda raha. Mwishowe, anachukia maisha yake ya upotovu. Ana njaa, anatamani sana kuona watu wa familia yao, naye anaazimia kurudi nyumbani! Akiwa mbali, baba yake anamwona, kisha anakimbia, anamwangukia shingoni, anambusu kwa wororo, na kujawa na shangwe. Mtu aliyeacha kushirikiana na kundi akitafakari kuhusu mfano huo anaweza kuchochewa kurudi katika kundi. Kwa kuwa mfumo huu wa mambo utaharibiwa hivi karibuni, anapaswa “kurudi nyumbani” haraka.

      15. Kwa nini watu fulani wanaacha polepole kushirikiana na kutaniko?

      15 Wengi wanaoacha kushirikiana na kutaniko si kama yule mwana mpotevu. Wengine wanaliacha kundi hatua kwa hatua kama mashua iliyo baharini inayokwenda polepole mbali na nchi kavu. Wengine wanalemewa sana na mahangaiko hivi kwamba wanapuuza mambo ya kiroho. Zaidi ya hayo, wengine wanajiruhusu wakwazwe na mtu fulani katika kutaniko, au wanaacha kushirikiana na kutaniko kwa sababu hawakubaliani na fundisho fulani la Biblia. Wachache wanatumbukia katika mwenendo usiopatana na maandiko. Hata hivyo, mambo yote tuliyoyazungumzia yanaweza kukusaidia katika jitihada zako za kuwasaidia wale walioliacha kundi kwa sababu hizo au nyinginezo ili warudi kungali na wakati.

      “Mwanangu, Karibu Nyumbani!”

      16-18. (a) Mzee mmoja Mkristo alimsaidia jinsi gani ndugu fulani ambaye kwa miaka mingi alikuwa asiyetenda? (b) Ni nini kilichomfanya ndugu huyo awe asiyetenda, na kutaniko lilimpokea jinsi gani?

      16 Mzee mmoja Mkristo alisema hivi: “Baraza letu la wazee linajitahidi sana kuwatembelea wasiotenda. Pindi moja, nilimkumbuka ndugu fulani ambaye nilijifunza Biblia pamoja naye na kumsaidia kupata ujuzi wa kweli. Alikuwa mhubiri asiyetenda kwa miaka 25 hivi naye alikuwa akikabili hali ngumu sana, hivyo nilimweleza jinsi kufuata kanuni za Biblia kunavyoweza kumsaidia. Baada ya muda fulani, alianza kuja kwenye Jumba la Ufalme naye akakubali kujifunza Biblia ili aimarishe azimio lake la kurudi katika kundi.”

      17 Ni nini kilichomfanya ndugu huyo awe asiyetenda? Anakubali hivi: “Nilianza kukazia fikira zaidi mambo ya ulimwengu kuliko mambo ya kiroho. Kisha nikaacha kujifunza, kushiriki katika huduma, na kuhudhuria mikutano. Punde si punde, nikaacha kushirikiana kabisa na kutaniko la Kikristo. Lakini nilisaidiwa kurudi kwa sababu mzee huyo alinihangaikia na kunijali kwa moyo wote.” Matatizo ya ndugu huyo yalianza kupungua alipokubali kujifunza tena Biblia. Alisema hivi: “Nilitambua kwamba kile nilichokosa maishani ni upendo na mwongozo wa Yehova na wa tengenezo lake.”

      18 Ndugu huyo alipokewa jinsi gani katika kutaniko? Anasema hivi: “Ninahisi kama yule mwana mpotevu aliyetajwa na Yesu Kristo. Kwa hakika, dada mmoja mwenye umri mkubwa ambaye alikuwapo miaka 30 iliyopita na ambaye bado anamtumikia Yehova kwa uaminifu aliniambia, ‘Mwanangu, karibu nyumbani!’ Hilo lilinigusa moyo sana. Kwa kweli, nilikuwa nimerudi nyumbani. Ningependa kumshukuru kutoka moyoni mzee huyo na kutaniko lote kwa sababu ya kunionyesha upendo, uchangamfu, subira, na kunijali. Upendo wao kwa Yehova na jirani ulinisaidia kwelikweli kurudi katika kundi.”

      Wahimizeni Wachukue Hatua Sasa!

      19, 20. Unaweza kuwatia moyo jinsi gani watu wasiotenda warudi haraka katika kundi, na unaweza kuwaonyesha jinsi gani kwamba Mungu hatazamii tufanye mambo ambayo hatuwezi?

      19 Tunaishi katika siku za mwisho, na mwisho wa mfumo huu wa mambo uko karibu. Kwa hiyo, watieni moyo wale wasiotenda wahudhurie mikutano ya Kikristo. Wahimizeni waanze kuhudhuria bila kukawia. Wakumbusheni kwamba Shetani anajaribu kuharibu uhusiano wao pamoja na Mungu na kuwafanya wafikiri kwamba matatizo yao yanaweza kusuluhishwa wakiacha ibada ya kweli. Wahakikishieni kwamba wanaweza kupata burudisho la kweli ikiwa tu wataendelea kuwa wafuasi waaminifu wa Yesu.—Soma Mathayo 11:28-30.

      20 Wakumbusheni wasiotenda kwamba Mungu anatazamia tufanye yale tu ambayo tunaweza. Maria, dada ya Lazaro, aliposhutumiwa kwa kumpaka Yesu mafuta yenye marashi ya bei ghali, Yesu alisema hivi: “Mwacheni. . . . Alifanya jambo ambalo aliweza.” (Marko 14:6-8) Yesu alimsifu mjane mwenye uhitaji ambaye alitoa mchango mdogo sana katika hekalu. Yeye pia alifanya jambo ambalo aliweza. (Luka 21:1-4) Wengi wetu tunaweza kuhudhuria mikutano ya Kikristo na kufanya kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme. Kwa msaada wa Yehova, watu wengi ambao sasa ni wasiotenda wataweza kufanya mambo hayo.

      21, 22. Unaweza kuwahakikishia nini wale wanaomrudia Yehova?

      21 Ikiwa kondoo aliyeacha kushirikiana na kundi anaogopa kukutana tena na ndugu zake, unaweza kumkumbusha jinsi watu walivyoshangilia wakati mwana mpotevu aliporudi nyumbani. Wale wanaorudi katika kutaniko wanawachochea wengine kuwa na shangwe kama hiyo. Watie moyo wachukue hatua sasa ya kumpinga Ibilisi na kumkaribia Mungu.—Yak. 4:7, 8.

      22 Wale wanaomrudia Yehova watakaribishwa kwa shangwe. (Omb. 3:40) Bila shaka, mambo waliyofanya zamani katika utumishi wa Mungu yaliwaletea shangwe kubwa. Wale wanaorudi haraka katika kundi watapata baraka nyingi wakati ujao!

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki