Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Wenyeji wa Amerika—Mwisho wa Muhula
    Amkeni!—1996 | Septemba 8
    • Wenyeji wa Amerika—Mwisho wa Muhula

      NI NANI ambaye hajapata kuona sinema asili za cowboys na Wahindi? Watu ulimwenguni pote wamepata kusikia juu ya Wyatt Earp, Buffalo Bill, na Lone Ranger na Wahindi Geronimo, Fahali Aketiye, Farasi Mwehu, na Chifu Joseph, pamoja na wengine wengi. Lakini sinema za Hollywood zimekuwa sahihi kwa kadiri gani? Nazo zimekuwa zenye haki kadiri gani katika kuonyesha Wahindi?

      Hadithi ya ushindi wa watu wa Ulaya dhidi ya Wenyeji wa Amerika Kaskazini (Wahindi) huzusha maswali.a Je, vitabu vya historia vimeeleza juu ya Wahindi kwa njia ya haki? Je, kuna masomo yoyote ya kujifunza kuhusu pupa, udhalimu, ubaguzi wa rangi, na mambo ya ukatili? Ni nini hadithi ya kweli juu ya wale walioitwa eti cowboys na Wahindi?

      Upinzani wa Mwisho wa Custer na Machinjo Katika Wounded Knee

      Katika mwaka wa 1876, mganga aitwaye Fahali Aketiye wa Lakota (ambayo ni mmojawapo migawanyiko mitatu ya kabila la Sioux) alikuwa kiongozi kwenye vita maarufu ya Mto Little Bighorn, katika Montana. Akiwa na wanajeshi 650, Luteni Kanali Custer “Nywele Ndefu” alifikiri kwamba angeweza kushinda kwa urahisi wapiganaji Wasioux na Wacheyenne 1,000. Alikosea vibaya sana. Alikuwa akikabili labda kundi kubwa zaidi la wapiganaji Wenyeji wa Amerika ambalo lilipata kukusanywa—wapatao 3,000.

      Custer aligawanya Kikosi chake cha 7 katika vikundi vitatu. Bila kungoja utegemezo wa vile vikundi vingine viwili, kikundi chake kilishambulia pale Custer alipoona kuwa dhaifu katika kambi ya Wahindi. Wakiongozwa na wakuu wao Farasi Mwehu, Nyongo, na Farasi Aketiye, Wahindi hao waliangamiza Custer na kikundi chake cha wanajeshi wapatao 225. Huo ulikuwa ushindi wa muda tu kwa makabila ya Wahindi lakini ushinde mchungu kwa Jeshi la Marekani. Hata hivyo, kisasi kibaya sana kililipizwa miaka 14 baadaye.

      Hatimaye, Fahali Aketiye alisalimu amri, baada ya kuahidiwa kwamba atasamehewa. Badala ya hivyo, alifungwa kwa muda fulani Fort Randall, Eneo la Dakota. Katika miaka yake ya uzeeni, alitokea mbele ya umma katika maonyesho ya kusafiri ya Wild West ya Buffalo Bill. Huyo ambaye awali alikuwa kiongozi mwenye sifa sana alikuwa amepoteza umashuhuri wa uganga.

      Katika 1890, Fahali Aketiye (jina lake la Kilakota likiwa Tatanka Iyotake) alipigwa risasi akafa na polisi Wahindi ambao walikuwa wametumwa kumshika. Wauaji wake walikuwa Wasioux “Vifua Chuma” (polisi wenye beji), Luteni Kichwa Fahali na Sajini Shoka Jekundu.

      Katika mwaka uo huo, upinzani wa Wahindi kwa udhibiti wa wazungu hatimaye ulishindwa katika machinjo ya Wounded Knee Creek kwenye Nyanda Pana za Marekani. Huko, wanaume, wanawake, na watoto Wasioux wenye kutoroka wapatao 320 waliuawa na majeshi ya serikali wakitumia mizinga yao aina ya Hotchkiss ya kulipua haraka-haraka. Wanajeshi hao walijigamba kwamba hicho kilikuwa kisasi walicholipiza juu ya machinjo ya wenzao, Custer na watu wake, katika mabonde yanayokabili Mto Little Bighorn. Basi vikaisha vita na mapambano ya hapa na pale yaliyochukua zaidi ya miaka 200 kati ya masetla wa Amerika wenye kushambulia na makabila ya wenyeji wenye kushambuliwa.

      Lakini Wenyeji wa Amerika walikujaje kukaa Amerika Kaskazini? Walikuwa na mtindo-maisha wa aina gani kabla ya mzungu kufika Amerika Kaskazini?b Ni nini kilichofanya washindwe na kutiishwa hatimaye? Na hali ya sasa ya Wahindi ikoje katika nchi inayodhibitiwa na wazao wa wahamiaji wa mapema kutoka Ulaya? Maswali hayo pamoja na mengine yatazungumziwa katika makala zifuatazo.

  • Walitoka Wapi?
    Amkeni!—1996 | Septemba 8
    • Walitoka Wapi?

      “TULIJIITAJE kabla ya Columbus kuja? . . . Katika kila kabila, hata leo, ukitafsiri neno ambalo tulijiita katika kila kabila, bila kujua makabila mengine yamejiitaje, mara nyingi jina hilo lilimaanisha jambo lilelile. Katika lugha yetu [Kinarrangansett] tulijiita Ninuog, au watu [katika Kinavajo, Diné], yaani wanadamu. Ndivyo tulivyojiita. Hivyo wakoloni [watu wa Ulaya] walipofika hapa, tulijijua, lakini hatukujua wao ni nani. Basi tukawaita Awaunageesuck, au watu wasiojulikana, kwa sababu ni wao ambao hawakujulikana, ni wao ambao sisi hatukuwajua, lakini sisi tulijuana. Na ni sisi tuliokuwa wanadamu.”—Oki Mrefu, wa kabila la Narragansett.

      Kuna nadharia nyingi kuhusu asili ya Wenyeji wa Amerika.a Joseph Smith, mwanzilishi wa Wamormon, alikuwa mmojawapo watu kadhaa, kutia ndani mfuasi wa Quaker William Penn, walioamini kwamba Wahindi walikuwa Waebrania, wazao wa yale yaitwayo makabila kumi yaliyopotea ya Israeli. Leo, ufafanuzi unaokubaliwa na wengi wa waanthropolojia ni kwamba ama kwa kupitia ardhi inayounganisha Asia na Amerika au kwa mashua, makabila ya Asia yaliingia katika eneo linaloitwa sasa Alaska, Kanada, na Marekani. Hata uchunguzi wa DNA (kanuni za kuongoza urithi) waonekana kuunga mkono wazo hilo.

      Wenyeji wa Amerika —Asili na Itikadi Zao

      Wahariri ambao ni Wenyeji wa Amerika Tom Hill (wa kabila la Seneca) na Richard Hill, Sr., (wa kabila la Tuscarora) waandika katika kitabu chao Creation’s Journey—Native American Identity and Belief: “Wenyeji wengi wa Amerika huamini kimapokeo kwamba wao waliumbwa kutokana na dunia yenyewe, kutokana na maji, au kutokana na nyota. Kwa upande mwingine, waakiolojia wana nadharia ya ardhi kubwa iliyovuka Mlangobahari wa Bering, ambayo kuipitia, Waasia walihamia nchi za Amerika; Waasia hao, nadharia hiyo yasisitiza, walikuwa wazazi wa kale wa wenyeji wa Kizio cha Magharibi.” Baadhi ya wenyeji wa Amerika huelekea kutilia shaka nadharia ya mzungu ya Mlangobahari wa Bering. Wao hupendelea kuamini hekaya zao na masimulizi yao. Wao hujiona kuwa wakazi wa asili badala ya kuwa wavumbuzi waliohamia huko kutoka Asia.

      Katika kitabu chake An Indian Winter, Russell Freedman aeleza hivi: “Kulingana na itikadi ya Wamandan [kabila lililokuwa karibu na sehemu za juu za Mto Missouri], Mtu wa Kwanza alikuwa roho mwenye nguvu sana, kiumbe cha kimungu. Alikuwa ameumbwa zamani sana na Bwana wa Uhai, muumba wa vitu vyote, atende akiwa mpatanishi kati ya wanadamu wa kawaida na miungu mingi, au roho, zilizokuwa zikiishi mbinguni.” Itikadi ya Wamandan hata ilitia ndani hekaya ya furiko. “Pindi moja, furiko kubwa lilipojaza ulimwengu, Mtu wa Kwanza aliokoa watu kwa kuwafundisha kujenga mnara wa ulinzi, au ‘safina,’ ambao ungeinuka juu sana kupita maji ya furiko. Kwa heshima yake, kila kijiji cha Wamandan kilikuwa na kifananishi kidogo cha mnara huo wa kihekaya—nguzo ya mwerezi yenye kimo cha karibu futi tano, iliyozingirwa na ua wa mbao.”

      Wamandan walikuwa na mfano wa kidini pia “ufito mrefu uliofunikwa kwa manyoya nao ulikuwa na kichwa chenye kuogofya cha mbao, kilichopakwa rangi nyeusi.” Huo uliwakilisha nani? “Mfano huo uliwakilisha Ochkih-Haddä, roho mwovu ambaye alikuwa na uvutano mkubwa sana juu ya wanadamu lakini ambaye hakuwa na nguvu kama Bwana wa Uhai au Mtu wa Kwanza.” Kwa Wahindi wa Nyanda, “kuamini viumbe vya roho kulikuwa sehemu ya maisha isiyobishaniwa. . . . Hakuna uamuzi mkubwa ambao ungeweza kufanywa, hakuna mradi ambao ungeweza kuanzishwa, bila kwanza kutafuta msaada na kibali cha viumbe vitakatifu ambavyo viliongoza mambo ya wanadamu.”

      Katika kitabu chake The Mythology of North America, John Bierhorst aeleza: “Kabla ya mbari kuwapo, ilisemwa kwamba Waosage walienda huku na huku katika hali iitwayo ganítha (bila sheria au utaratibu). Maoni ya kimapokeo yalisema kwamba katika siku hizo za awali watu fulani wenye kufikiri walioitwa Wazee Wadogo . . . walifanyiza nadharia kwamba nguvu fulani yenye ukimya ya uumbaji hujaza anga na dunia na kufanya nyota, mwezi, na jua lisonge katika utaratibu kamili. Waliiita nguvu hiyo Wakónda (nguvu isiyofahamika) au Eáwawonaka (msababishi wa kuwapo kwetu).” Wazo kama hilo lashirikiwa na Wazuni, Wasioux, na Walakota katika Magharibi. Wawinnebago pia wana ngano ihusuyo “Mfanyi wa Dunia.” Hilo simulizi lasema: “Alitaka nuru nayo nuru ikaja. . . . Kisha tena akafikiri na kutaka dunia, na dunia hii ikawapo.”

      Kwa wanafunzi wa Biblia, ni jambo la kupendeza kuona baadhi ya ulinganifu uliopo kati ya itikadi za Wenyeji wa Amerika na mafundisho yanayoonyeshwa katika Biblia, hasa kwa habari ya Roho Mkuu, “msababishi wa kuwapo kwetu,” jambo ambalo linatukumbusha maana ya jina la kimungu, Yehova, “Yeye Husababisha Iwe.” Ulinganifu mwingine hutia ndani Furiko na roho mwovu aitwaye Shetani katika Biblia.—Mwanzo 1:1-5; 6:17; Ufunuo 12:9.

      Kuelewa Falsafa za Wenyeji wa Amerika

      Wale waandikaji ambao ni Wenyeji wa Amerika Tom Hill na Richard Hill wafafanua zawadi tano ambazo wao wasema Wenyeji wa Amerika wamepokea kutoka kwa wazazi wao wa kale. “Zawadi ya kwanza . . . ni ushikamano wetu mkubwa kwa ardhi.” Kwa kufikiria historia yao kabla ya na baada ya kufika kwa watu wa Ulaya, ni nani awezaye kukanusha jambo hilo? Ardhi yao, ambayo mara nyingi ilionwa kuwa takatifu na Wenyeji wa Amerika, ilichukuliwa hatua kwa hatua kwa kutumia nguvu, madanganyo, au mikataba ambayo haikutimizwa.

      “Zawadi ya pili ni uwezo na roho ambayo wanyama wanashiriki na watu wetu.” Staha ya Wenyeji wa Amerika kuelekea wanyama imeonyeshwa katika njia nyingi. Wao waliwinda kwa ajili ya chakula, nguo, na vibanda vyao pekee. Haikuwa wenyeji ambao karibu wamalize kabisa nyati-singa bali ni mzungu mwenye tamaa ya kumwaga damu na pupa isiyofikiria matokeo.

      “Zawadi ya tatu ni viumbe wa roho, ambao ni watu wetu wa ukoo wanaoishi na kuwasiliana nasi kupitia sanamu zao tunazofanyiza.” Hili ni jambo la kawaida kwa dini nyingi ulimwenguni pote—kuokoka kwa roho au nafsi baada ya kifo.b

      “Ya nne ni kujua sisi ni nani, jambo linaloonyeshwa na kuendelezwa katika mapokeo yetu ya kabila.” Leo jambo hilo laweza kuonekana katika sherehe za kikabila, ambako watu hukusanyikia kujadili mambo ya kabila, au kwenye makusanyiko ya kijamii, ambako watu hucheza dansi na muziki wa kikabila. Mavazi ya Wahindi, kupigwa kwa ngoma kwa mtindo fulani, michezo ya ngoma, kukutana tena kwa familia na mbari—zote zaonyesha pokeo la kikabila.

      “Zawadi ya mwisho ni uwezo wa kubuni—itikadi zetu hufanywa kuonekana kihalisi kupitia kufanyiza vitu vya asili kuwa vitu vya imani na fahari.” Iwe ni kutengeneza vikapu, ufumaji, kufinyanga na kuchora vyombo vya udongo, kutengeneza vito na mapambo, au utendaji mwingine wowote wa sanaa, unahusika na pokeo lao na utamaduni wao wa miaka mingi.

      Kuna makabila mengi sana hivi kwamba ingehitajika vitabu vingi kueleza itikadi zayo na matendo yayo yote ya kimapokeo. Sasa kile kinachotupendeza ni, Kuja kwa mamilioni ya watu wa Ulaya, wengi wakiitwa eti Wakristo, kuliathirije Wenyeji wa Amerika?

  • Jinsi Ulimwengu Wao Ulivyopotea
    Amkeni!—1996 | Septemba 8
    • Jinsi Ulimwengu Wao Ulivyopotea

      KWA miaka mingi hadithi ya Marekani ilielezwa kwa ufupi katika maneno haya, “Jinsi tulivyoshinda Magharibi.” Sinema za Hollywood zilionyesha masetla Wazungu wakivuka nyanda na milima ya Amerika, zikiwa na wanajeshi wanaofanana na John Wayne, cowboys, na masetla wakipigana na Wahindi wakali, wakatili, wenye mashoka ya vita. Mzungu alipokuwa akitafuta ardhi na dhahabu, makasisi wengine wa Jumuiya ya Wakristo na wahubiri eti walikuwa wakiokoa nafsi.

      Historia hiyo ikoje kulingana na maoni ya wakazi wa awali, wenyeji wa Amerika? Kwa kufika kwa watu wa Ulaya, Wahindi “walilazimika kukabiliana na kuingiliwa kwa mazingira yao na mshambulizi mbaya zaidi waliopata kukabili wakati wowote ule: washambulizi kutoka Ulaya,” chasema kitabu The Native Americans—An Illustrated History.

      Upatano Uliosababisha Mapambano

      Mwanzoni, wengi wa watu wa Ulaya waliofika kwanza Kaskazini-Mashariki mwa Amerika walitendewa kwa fadhili na ushirikiano na wenyeji. Simulizi moja lasema: “Bila msaada wa Wapowhatan, makao ya Waingereza katika Jamestown, Virginia, ambayo yalikuwa koloni ya kwanza ya kudumu ya Uingereza katika yale Mabara Mapya, hayangeokoka majira ya kwanza ya kipupwe ya 1607-1608. Vivyo hivyo, koloni ya Wahamiaji katika Plymouth, Massachusetts, ingeanguka kama haingesaidiwa na Wawampanoaga.” Wenyeji fulani waliwaonyesha wageni hao jinsi ya kurutubisha udongo na kukuza mimea. Na safari ya uvumbuzi ya Lewis na Clark ya 1804-1806—ingefanikiwaje kupata njia nzuri ya uchukuzi kati ya Eneo la Louisiana na kile kilichoitwa Eneo la Oregon bila msaada na kuingilia mambo kwa mwanamke Mshoshone aliyeitwa Sacagawea? Yeye alikuwa “ishara [yao] ya amani” walipokutana ana kwa ana na Wahindi.

      Hata hivyo, kwa sababu ya jinsi watu wa Ulaya walivyokuwa wakitumia ardhi na ugavi mdogo wa chakula, kuhamia Amerika Kaskazini kwa wingi kulisababisha uhasama kati ya washambulizi na wenyeji. Mwanahistoria Mkanada Ian K. Steele aeleza kwamba katika karne ya 17, kulikuwa na Wanarragansett wapatao 30,000 katika Massachusetts. Chifu wao Miantonomo, “akiona hatari, . . . alijaribu kujenga muungano wake pamoja na Wamohawk ili kufanyiza upinzani wa ujumla wa Wahindi wa Amerika.” Inaripotiwa kuwa aliwaambia Wamontauk hivi katika 1642: “Ni [lazima] tuungane kama vile wao [Waingereza] wameungana, la sivyo tutatokomea karibuni, kwa kuwa mwajua baba zetu walikuwa na dia wengi na ngozi nyingi, nyanda zetu zilijaa dia, na pia misitu yetu, na kujaa [bata mzinga], na ghuba zetu kujaa samaki na ndege. Lakini Waingereza hawa baada ya kunyakua ardhi yetu, walifyeka nyasi wakitumia vifyekeo, na kwa shoka wakakata miti; ng’ombe na farasi zao hula nyasi, na nguruwe zao huharibu fuo zetu za vivaaute, nasi tutakufa njaa.”—Warpaths—Invasions of North America.

      Jitihada za Miantonomo za kufanyiza muungano wa Wenyeji wa Amerika hazikufua dafu. Katika 1643, alishikwa katika vita ya kikabila na Chifu Uncas wa kabila la Mohegan, aliyempeleka kwa Waingereza kuwa yeye ni mwasi. Waingereza hawakuweza kumhukumu Miantonomo kisheria na kumuua. Wao wakafikiria suluhisho bora. Steele aendelea kusema: “Wakishindwa kumfisha [Miantonomo], ambaye hangehukumiwa na yoyote ya koloni zilizokuwapo, makamishna walimlazimisha Uncas amuue, kukiwa na mashahidi wa Uingereza kuthibitisha kwamba kweli ameuawa.”

      Jambo hili halionyeshi tu mapambano ya daima kati ya wakoloni wenye kushambulia na wenyeji bali pia uadui wa kuchinjana-chinjana na hila miongoni mwa makabila, ambao ulikuwapo hata kabla ya mzungu kupata kufika Amerika Kaskazini. Katika vita vyao na Ufaransa juu ya udhibiti wa koloni ya Amerika Kaskazini, Waingereza walifanya makabila fulani yaiunge mkono, huku mengine yakiunga mkono Wafaransa. Haidhuru ni upande gani ulioshindwa, makabila yote yalipata hasara.

      “Mgawanyiko Katika Uelewano”

      Lifuatalo ni oni moja juu ya ushambulizi wa watu wa Ulaya: “Kile ambacho viongozi wa makabila ya Wahindi hawakuelewa, mara nyingi mpaka kuchelewa mno, ni jinsi watu wa Ulaya walivyowaona Wahindi. Wao hawakuwa Wazungu wala Wakristo. Wao walikuwa wakatili—hayawani wakorofi—akilini mwa wengi, watu hatari wasio na ubinadamu ambao walifaa tu kuuzwa utumwani.” Mtazamo huu wa kuwa bora uliathiri sana hayo makabila.

      Wenyeji wa Amerika hawakuelewa maoni ya watu wa Ulaya. Kulikuwako, kama alivyouita mshauri fulani Mnavajo Philmer Bluehouse katika mahoji ya majuzi na Amkeni!, “mgawanyiko katika uelewano.” Wenyeji hawakuona ustaarabu wao ukiwa duni lakini badala ya hivyo, kuwa tofauti, ukiwa na maadili tofauti kabisa. Kwa kielelezo, kuuza ardhi kulikuwa jambo la kigeni sana kwa Wahindi. Je, unaweza kumiliki na kuuza hewa, upepo, na maji? Basi kwa nini uuze ardhi? Ardhi ni ya kutumiwa na kila mtu. Hivyo, Wahindi hawakuweka kingo kwenye ardhi zao.

      Kufika kwa Waingereza, Wahispania, na Wafaransa kukatokeza kile ambacho kimeitwa “kukutana kwenye msiba kwa tamaduni mbili za kigeni.” Wenyeji walikuwa watu ambao kwa mamia ya miaka wameishi kwa kupatana na ardhi na asili na ambao walijua jinsi ya kuishi bila kuharibu usawaziko wa mazingira. Lakini, upesi mzungu akaja kuona wakazi wenyeji kuwa viumbe vya hali ya chini na wakali—mzungu akisahau ukatili wake mwenyewe katika kuwatiisha! Katika 1831, Mwanahistoria Mfaransa Alexis de Tocqueville, alitaja kifupi maoni ya mzungu yaliyoenea juu ya Wahindi: “Mungu hajawafanya wastaarabike; ni lazima wafe.”

      Muuaji Hatari Zaidi

      Masetla wapya walipoendelea kwenda magharibi kuvuka Amerika Kaskazini, jeuri ikatokeza jeuri. Hivyo, iwe ni Wahindi au watu wa Ulaya walioshambulia kwanza, pande zote mbili zilifanya mambo ya ukatili. Hao Wahindi waliogopwa kwa sababu ya sifa yao ya kung’oa ngozi ya kichwa ikiwa na nywele, zoea ambalo watu wengine wanaamini kwamba walijifunza kutoka kwa watu wa Ulaya ambao walikuwa wakiwapa vitu kwa kubadilishana na ngozi za vichwa vya watu. Hata hivyo, hao Wahindi walikuwa wakishindwa vitani dhidi ya Wazungu waliokuwa wengi na wenye silaha bora. Katika visa vingi makabila hayo yalilazimika kuacha ardhi zao za uzaliwa au kufa. Mara nyingi hali hizo zote ziliwapata—waliacha ardhi zao kisha wakauawa au kufa kwa maradhi na njaa kali.

      Lakini, si vita vilivyowaua makabila ya wenyeji zaidi. Ian K. Steele aandika: “Silaha kali zaidi katika ushambulizi wa Amerika Kaskazini haikuwa bunduki, farasi, Biblia, au ‘ustaarabu’ wa Ulaya. Ilikuwa maradhi.” Kuhusu athari za maradhi ya Mabara ya Zamani katika Amerika, Patrica Nelson Limerick, ambaye ni profesa wa historia, aliandika: “Yalipopelekwa Mabara Mapya, maradhi yaleyale [ambayo watu wa Ulaya walikuwa wamesitawisha kinga kwayo baada ya karne nyingi]—tetekuwanga, surua, kamata, malaria, homa ya kimanjano, homa ya chawa, kifua kikuu, na zaidi ya yote, ndui—yaliwashika wenyeji. Kiwango cha vifo vijijini kikawa juu kufikia asilimia 80 na 90.”

      Russell Freedman asimulia mweneo wa ndui iliyotokea 1837. “Kwanza ni Wamandan walioshikwa, wakifuatwa kwa mfululizo na Wahidatsa, Waassiniboin, na Waarikara, Wasioux, na kabila la Blackfeet.” Wamandan karibu watokomee kabisa. Kutoka watu wapatao 1,600 katika 1834, wao walipunguka hadi 130 katika 1837.

      Ni Nini Kilichopata Mikataba?

      Hadi leo hii wazee wa makabila waweza kutaja tarehe za mikataba ambayo serikali ya Marekani ilifanya na babu zao wa kale katika karne ya 19. Lakini mikataba hiyo hasa iliandaa nini? Mara nyingi ilikuwa ni ubadilishano usiofaa wa ardhi nzuri kwa maeneo makavu na msaada kidogo kutoka kwa serikali.

      Kielelezo cha jinsi makabila ya wenyeji yalivyotendwa vibaya ni kisa cha makabila ya Wairoquois (toka mashariki hadi magharibi, Wamohawk, Waoneida, Waonondaga, Wacayuga, na Waseneca) baada ya Waingereza kushindwa na wakoloni wa Amerika katika vita ya uhuru, ambayo iliisha 1783. Wairoquois waliunga mkono Waingereza, nao walilipwa tu, kulingana na Alvin Josephy, Jr., kuachwa na matusi. Waingereza, “wakipuuza [Wairoquois], walikuwa wameipa Marekani enzi juu ya ardhi za Wairoquois.” Yeye aongeza kwamba hata Wairoquois ambao walikuwa wamependelea wakoloni dhidi ya Waingereza “walishawishiwa na makampuni ya kununua ardhi na wahatarishaji wa fedha ili kupata faida na serikali yenyewe ya Amerika.”

      Wakati mkutano wa mkataba ulipofanywa katika 1784, James Duane, aliyekuwa zamani mwakilishi wa Halmashauri ya Masuala ya Wahindi ya Bunge la Bara, alihimiza wawakilishi wa serikali “kudhoofisha kujistahi kokote kulikobaki miongoni mwa Wairoquois kwa kuwatendea kama watu wa hali ya chini kimakusudi.”

      Madokezo yake ya kiburi yalitekelezwa. Baadhi ya Wairoquois walishikwa mateka, na “majadiliano” yakafanywa wakielekezewa bunduki. Ingawa wanajiona kuwa hawakushindwa vitani, Wairoquois walilazimika kuacha ardhi yao yote magharibi ya New York na Pennsylvania na kukubali eneo dogo katika Jimbo la New York.

      Mbinu kama hizo zilitumiwa pia dhidi ya makabila mengine mengi ya wenyeji. Josephy asema pia kwamba wawakilishi wa Amerika walitumia “hongo, matisho, vileo, na hila za wawakilishi wasio rasmi kuwanyang’anya ardhi Wadelaware, Wawyandot, Waottawa, Wachippewa [au Waojibwa], Washawnee, na makabila mengine ya Waohio.” Si ajabu kwamba upesi Wahindi wakaja kukosa kumtumaini mzungu na ahadi zake zisizotimizwa!

      “Safari Ndefu” na Njia ya Machozi

      Vita ya Wenyewe kwa Wenyewe ya Marekani (1861-1865) ilipotokea, hiyo iliondoa majeshi kutoka nchi ya Wanavajo katika Kusini-Magharibi. Wanavajo wakatwaa pindi hiyo kushambulia makao ya Waamerika na Wamexico katika Bonde la Rio Grande katika eneo la New Mexico. Serikali ikampeleka Kanali Kit Carson na kikosi chake cha Wajitoleaji wa New Mexico kukomesha Wanavajo na kuwapeleka katika eneo fulani katika ukanda wa ardhi kavu iliyoitwa Bosque Redondo. Carson akafuatia sera ya kuharibu kabisa riziki ili kufanya Wanavajo wapate njaa na kuwaondosha kwenye ile Canyon de Chelly yenye kutisha, katika kaskazini-mashariki mwa Arizona. Hata aliharibu zaidi ya miti 5,000 ya pichi.

      Carson alikusanya watu wapatao 8,000 na kuwalazimisha kutembea “Safari Ndefu” ya maili zipatazo 300 hadi kambi ya kizuizi ya Bosque Redondo katika Fort Sumner, New Mexico. Ripoti moja yasema hivi: “Kulikuwa na baridi kali sana, na wengi wa wahamishwa hao wasiovalia vizuri na kupungukiwa chakula walikufa njiani.” Hali zilizokuwa katika kambi zilikuwa mbaya sana. Wanavajo walilazimika kuchimba mashimo ardhini ili kujaribu kupata himaya. Katika 1868, baada ya kugundua makosa makubwa iliyokuwa imefanya, serikali iliwapa Wanavajo ekari milioni 3.5 ya ardhi yao ya uzaliwa katika Arizona na New Mexico. Walirudi, lakini walikuwa wamelazimika kulipa gharama kubwa kama nini!

      Kati ya 1820 na 1845, makumi ya maelfu ya Wachoctaw, Wacherokee, Wachickasaw, Wacreek, na Waseminole waliondoshwa kutoka ardhi zao katika Kusini-Mashariki na kulazimishwa kutembea kuelekea magharibi, ng’ambo ya Mto Mississippi, hadi pale paitwapo sasa Oklahoma, wengine walitembea kufikia mamia ya maili. Wengi walikufa katika hali ngumu za kipupwe. Hiyo safari ya kulazimishwa kuelekea magharibi ikapata sifa mbaya ya Njia ya Machozi.

      Ukosefu wa haki waliotendewa Wenyeji wa Amerika wathibitishwa zaidi na maneno ya jenerali mmoja wa Amerika George Crook, ambaye alikuwa amewawinda Wasioux na Wacheyenne katika kaskazini. Yeye alisema: “Upande wa Wahindi katika kesi mara nyingi hausikilizwi. . . . Kisha wakati [Wahindi] wanapoasi ndipo uangalifu wa umma unaelekezewa Wahindi, uhalifu wao na ukatili wao pekee unashutumiwa, huku watu ambao ukosefu wao wa haki umewafanya watende hivyo huachwa bila kuadhibiwa . . . Hakuna mtu ajuaye jambo hili kwa njia bora kuliko Wahindi wenyewe, na kwa hiyo yeye hana hatia akiona ukosefu wa haki wa serikali ambayo inamwadhibu tu, huku ikimruhusu mzungu kumpora kama atakavyo.”—Bury My Heart at Wounded Knee.

      Wenyeji wa Amerika wanaendeleaje leo baada ya kudhibitiwa na watu wa Ulaya kwa zaidi ya miaka mia moja? Je, wako katika hatari ya kutoweka kwa sababu ya kuchanganyikana na wengine? Wao wana tumaini gani kwa wakati ujao? Makala ifuatayo itafikiria maswali haya na mengine.

  • Wakati Wao Ujao Una Nini?
    Amkeni!—1996 | Septemba 8
    • Wakati Wao Ujao Una Nini?

      KATIKA mahojiano na Amkeni!, chifu wa amani wa Wacheyenne Lawrence Hart alisema kwamba mojawapo matatizo yanayoathiri Wahindi ni kwamba “tumekabiliwa na kani za mchanganyo na mabadiliko ya utamaduni. Kwa kielelezo tunapoteza lugha yetu. Pindi fulani hii ilikuwa sera iliyofanywa kimakusudi na serikali. Jitihada nyingi zilifanywa za ‘kutustaarabisha’ kupitia elimu. Tulipelekwa shule za bweni na kukatazwa kusema lugha zetu za kienyeji.” Sandra Kinlacheeny akumbuka: “Nilipoongea kwa Kinavajo katika shule yetu ya bweni, mwalimu aliosha mdomo wangu kwa sabuni!”

      Chifu Hart aendelea kusema: “Jambo lenye kutia moyo ni kwamba makabila mbalimbali yameamka. Hayo yanatambua kwamba lugha zayo zitatoweka jitihada zozote zisipofanywa za kuzihifadhi.”

      Ni watu kumi tu wanaobaki ambao wanajua Kikaruk, lugha ya mojawapo makabila ya California. Mnamo Januari 1996, Wingu Radi-Nyekundu (Carlos Westez), Mhindi wa mwisho aliyejua lugha ya Kicatawba, alikufa akiwa na umri wa miaka 76. Hakuwa na mtu yeyote wa kuongea naye lugha hiyo kwa miaka mingi.

      Kwenye Majumba ya Ufalme ya Mashahidi wa Yehova katika maeneo ya Wanavajo na Wahopi katika Arizona, karibu kila mtu huzungumza Kinavajo na Kihopi na Kiingereza. Hata Mashahidi wasio Wahindi wanajifunza lugha ya Kinavajo. Mashahidi wanahitaji kujua Kinavajo ili waweze kufanya kazi yao ya elimu ya Biblia, kwa kuwa Wanavajo wengi wanajua vizuri lugha yao pekee. Lugha za Kihopi na Kinavajo bado hujulikana sana, na vijana wanatiwa moyo kuzitumia shuleni.

      Elimu ya Wenyeji wa Amerika

      Kuna vyuo 29 vya Wahindi Marekani vyenye wanafunzi 16,000. Chuo cha kwanza kilifunguliwa Arizona katika 1968. “Hilo ni mojawapo mabadiliko mazuri zaidi katika Eneo la Wahindi, haki ya kuelimisha chini ya hali zetu wenyewe,” akasema Dakt. David Gipp wa Halmashauri ya Elimu ya Juu ya Wahindi. Katika Chuo Kikuu cha Sinte Gleska, somo la lugha ya Kilakota ni takwa.

      Kulingana na Ron McNeil (Mhunkpapa wa Lakota), msimamizi wa Hazina ya Chuo ya Wahindi wa Amerika, idadi ya wasioajiriwa kazi miongoni mwa Wenyeji wa Amerika ni kati ya asilimia 50 hadi asilimia 85, nao Wahindi wana matarajio ya kuishi ya chini zaidi na viwango vya juu zaidi vya ugonjwa wa kisukari, kifua kikuu, na uraibu wa alkoholi kati ya kikundi kingine chochote katika Marekani. Elimu bora ni moja tu kati ya njia ziwezazo kusaidia.

      Ardhi Takatifu

      Kwa Wenyeji wengi wa Amerika, ardhi za mababu wao ni takatifu. Kama Radi Nyeupe alivyomwambia mbunge mmoja: “Ardhi yetu ndicho kitu tunachothamini zaidi duniani.” Walipokuwa wakifanya mikataba na mapatano, mara nyingi Wahindi walifikiria kwamba hayo yalikuwa ya kuruhusu wazungu watumie ardhi zao bali si kuzimiliki. Wahindi wa Sioux walipoteza ardhi yenye thamani sana katika Black Hills ya Dakota katika miaka ya 1870, wachimbaji walipomiminika huko wakitafuta dhahabu. Katika 1980, Mahakama Kuu Zaidi ya Marekani iliamuru serikali ya Marekani kulipa karibu dola milioni 105 za ridhaa kwa makabila manane ya Sioux. Kufikia leo hii makabila hayo yamekataa malipo hayo—wao wanataka ardhi yao takatifu, Black Hills ya South Dakota, irudishwe.

      Wahindi wengi wa Sioux hawapendi kuona nyuso za marais wazungu zikiwa zimechongwa kwenye Mlima Rushmore, katika Black Hills. Katika mlima mmoja ulio karibu, wachongaji wanachonga mchongo mkubwa hata zaidi. Ni mchongo wa Farasi Mwehu, yule kiongozi wa vita wa Sioux wa Oglala. Mchongo huo utamalizika kufikia Juni 1998.

      Magumu ya Leo

      Ili kuokoka katika ulimwengu wa leo, Wenyeji wa Amerika wamelazimika kujirekebisha kupatana na hali katika njia mbalimbali. Wengi sasa wamesoma vizuri nao wamezoezwa katika vyuo, wakiwa na uwezo ambao wao waweza kutumia vizuri katika mazingira yao. Kielelezo kimoja ni Burton McKerchie aliye mwanana na ambaye ni Mchippewa kutoka Michigan. Yeye ametayarisha sinema za masimulizi za kutumiwa na Public Broadcasting Service na sasa anafanya kazi katika shule moja ya sekondari kwenye Eneo la Wahindi la Hopi katika Arizona, akiratibisha vipindi vya masomo kwa kutumia vidio katika jimbo hilo. Kielelezo kingine ni Ray Halbritter, kiongozi wa kabila la Oneida aliyesoma Harvard.

      Arlene Young Hatfield, akiandika katika Navajo Times, alisema kwamba kijana Mnavajo hana uzoefu au hawezi kujidhabihu jinsi wazazi wake au wazazi wake wa kale walivyofanya walipokuwa wakikua. Yeye aliandika: “Kwa sababu ya mafaa [ya kisasa] wao hawajapata kamwe kukusanya au kutema kuni, kubeba maji, au kuchunga kondoo kama wazazi wao wa kale. Wao hawachangii maisha ya familia kama watoto wa siku nyingi zilizopita walivyofanya.” Yeye amalizia hivi: “Haiwezekani kuepuka matatizo mengi ya kijamii ambayo bila shaka yataathiri watoto wetu. Hatuwezi kuepusha familia zetu, au maeneo yetu na ulimwengu wote, wala hatuwezi kurudia maisha ambayo babu zetu wa kale waliyaishi.”

      Hapo pana ugumu kwa Wenyeji wa Amerika—jinsi ya kushikilia mapokeo yao na maadili yao ya kipekee huku wakijipatanisha na ulimwengu wa nje unaobadilika haraka.

      Kukabiliana na Dawa za Kulevya na Alkoholi

      Hadi leo hii, uraibu wa alkoholi unaharibu kabisa jamii ya Wenyeji wa Amerika. Dakt. Lorraine Lorch, ambaye ametumikia miongoni mwa Wahopi na Wanavajo akiwa daktari wa watoto na wa kawaida kwa miaka 12, alisema hivi katika mahoji na Amkeni!: “Uraibu wa alkoholi ni tatizo kubwa sana kwa wanaume na wanawake. Miili yenye nguvu hushindwa na kunyauka kwa maini, vifo vya ghafula, ujiuaji kimakusudi, na mauaji. Inasikitisha kuona kwamba alkoholi inatangulizwa mbele ya watoto, mwenzi wa ndoa, na hata mbele ya Mungu. Kicheko hugeuka kuwa machozi, upole kuwa ujeuri.” Yeye aliongezea: “Hata baadhi ya sherehe, ambazo pindi moja zilionwa kuwa takatifu na Wanavajo na Wahopi, nyakati nyingine siku-hizi huchafuliwa na ulevi na uchafu. Alkoholi hunyang’anya watu hao wazuri afya yao, akili zao, uwezo wao wa kubuni, na utu wao wa kweli.”

      Philmer Bluehouse, mpatanishi wa amani katika Idara ya Sheria ya kabila la Navajo, katika Window Rock, Arizona, alifafanua kwa njia isiyoudhi kuwa dawa za kulevya na alkoholi ni “dawa za kujitibu.” Matumizi hayo mabaya ya vitu hivyo hufunika huzuni nayo husaidia mtu kufunika magumu ya maisha bila kazi na mara nyingi bila kusudi.

      Hata hivyo, Wenyeji wengi wa Amerika wamepigana kwa mafanikio dhidi ya hiki kinywaji cha “kishetani” ambacho kililetwa na mzungu nao wamejitahidi kushinda uraibu wa dawa za kulevya. Vielelezo viwili ni Clyde na Henrietta Abrahamson, kutoka Eneo la Wahindi la Waspokane katika Jimbo la Washington. Clyde ana mwili mnene, na nywele na macho meusi. Alieleza Amkeni! hivi:

      “Tumeishi katika eneo letu sehemu kubwa ya maisha zetu, kisha tukahamia jiji la Spokane kuhudhuria chuo. Hatukupenda mtindo wetu wa maisha, ambao ulitia ndani alkoholi na dawa za kulevya. Tulijua aina hii tu ya maisha. Tulikua tukichukia mavutano hayo mawili kwa sababu ya matatizo ambayo tuliona yametokeza katika familia.

      “Kisha tukakutana na Mashahidi wa Yehova. Hatukupata kusikia juu yao kabla ya kwenda jijini. Tulifanya maendeleo polepole. Labda kwa sababu hatukutumaini watu ambao hatukuwa tumewajua, hasa wazungu. Kwa kipindi cha miaka mitatu tulikuwa tukijifunza Biblia bila utaratibu. Tabia iliyokuwa ngumu zaidi kwangu kuacha ilikuwa kuvuta bangi. Nilikuwa mvutaji bangi tangu niwe na umri wa miaka 14, na nilikuwa na umri wa miaka 25 nilipoanza kujaribu kuacha. Nilikuwa nikilewa muda mwingi wa maisha yangu ya ujana. Katika 1986, nilisoma makala katika toleo la Januari 22 la Amkeni! (la Kiingereza), lenye kichwa “Kila Mtu Anavuta Bangi—Kwa Nini Nisivute?” Ilinifanya nifikirie jinsi ilivyokuwa upumbavu kuvuta bangi—hasa baada ya kusoma Mithali 1:22, ambalo lasema: ‘Enyi wajinga, hata lini mtapenda ujinga? Na wenye dharau kupenda dharau yao, na wapumbavu kuchukia maarifa?’

      “Nikaacha tabia hiyo, na katika masika ya 1986, tulifunga ndoa na Henrietta. Tulibatizwa mnamo Novemba 1986. Katika 1993 nikawa mzee kutanikoni. Binti zetu wote wawili walibatizwa kuwa Mashahidi 1994.”

      Je, Suluhisho Ni Kasino na Kucheza Kamari?

      Katika 1984 hakukuwa na kamari inayosimamiwa na Wahindi Marekani. Kulingana na The Washington Post, mwaka huu makabila 200 yanaendesha shughuli 220 za kamari katika majimbo 24. Tofauti kubwa sana ni Wanavajo na Wahopi, ambao kufikia sasa wamekataa vishawishi vya kamari. Lakini, je, majumba ya kasino na bingo ndiyo njia ya kupata ufanisi na kuleta kazi zaidi katika maeneo ya Wahindi? Philmer Bluehouse aliliambia Amkeni! hivi: “Kamari ni upanga wenye makali kuwili. Swali ni, Je, itafaidi watu wengi zaidi kuliko itakaowadhuru?” Ripoti moja yasema kwamba kasino za Wahindi zimewapa watu 140,000 kazi nchini kote lakini yasema kwamba ni asilimia 15 pekee kati ya kazi hizo zinazofanywa na Wahindi.

      Chifu wa Wacheyenne, Hart, aliliambia Amkeni! maoni yake juu ya jinsi kucheza kamari kunavyoathiri maeneo ya Wahindi. Yeye alisema hivi: “Nina hisia tofauti-tofauti. Jambo zuri pekee ni kwamba kamari hutokeza kazi na mapato kwa makabila. Kwa upande mwingine, nimeona kwamba wateja wengi ni watu wetu wenyewe. Najua wengine ambao walinaswa na bingo, nao huondoka mapema nyumbani ili kwenda huko, hata kabla ya watoto kurudi kutoka shuleni. Kisha wao wawa watoto wa kubeba funguo na wa kukaa peke yao nyumbani mpaka wazazi wao warudi kutoka kucheza bingo.

      “Tatizo kubwa ni kwamba familia zinaona kwamba zitashinda na kuongeza mapato yao. Kwa kawaida hawashindi; wao hupoteza. Nimewaona wakitumia pesa ambazo zimetengewa ununuzi wa bidhaa au mavazi ya watoto.”

      Wakati Ujao Una Nini?

      Tom Bahti aeleza kwamba kuna mambo mawili yapendwayo wakati wa kujadili wakati ujao wa makabila ya Kusini-Magharibi. “La kwanza latabiri kwa dhati kutoweka kunakokaribia kwa tamaduni za wenyeji katika maisha ya ujumla ya Waamerika. La pili halieleweki vizuri . . . Linasema kwa upole juu ya kuchanganyikana kwa tamaduni, likidokeza mchanganyiko wa uangalifu wa ‘utamaduni bora wa mapokeo ya zamani na mapya,’ aina fulani ya utamaduni bora kabisa ambao kwao Mhindi aweza kudumisha ustadi wake wa kale katika sanaa, na kuwa mwenye kuvutia katika dini yake na mwenye hekima katika falsafa yake—lakini mwenye kukubali sababu vya kutosha katika mahusiano yake nasi (utamaduni bora wa [mzungu]) na kuona mambo kwa njia yetu.”

      Kisha Bahti auliza swali. “Ni lazima badiliko litukie, lakini ni nani atakayebadilika na kwa kusudi gani? . . . Sisi [wazungu] tuna tabia yenye kuchukiza ya kuwaona watu wengine wote kuwa tu Waamerika ambao hawajasitawi. Tunadhani kwamba ni lazima hawatosheki na njia yao ya maisha na wanatamani kuishi na kufikiri jinsi sisi tunavyofanya.”

      Yeye aendelea kusema: “Jambo moja ni hakika—hadithi ya Mhindi wa Amerika haijaisha, lakini jinsi itakavyoisha au ikiwa itaisha ni jambo tunalongoja kuona. Labda, bado kuna wakati wa kuanza kufikiri juu ya jumuiya zetu za Wahindi kuwa vyanzo vyenye thamani vya utamaduni kuliko kuziona tu kuwa matatizo magumu ya kijamii.”

      Maisha Katika Ulimwengu Mpya wa Upatano na Haki

      Kutokana na maoni ya Biblia, Mashahidi wa Yehova wajua jinsi ulivyo wakati ujao wa Wenyeji wa Amerika na wa watu wa mataifa, makabila na lugha zote. Yehova Mungu ameahidi kuumba “mbingu mpya na nchi mpya.”—Isaya 65:17; 2 Petro 3:13; Ufunuo 21:1, 3, 4.

      Ahadi hii haimaanishi sayari mpya. Kama vile Wenyeji wa Amerika wanavyojua vema sana, dunia hii ni kito inapostahiwa na kutendewa ifaavyo. Badala ya hivyo, unabii wa Biblia waonyesha utawala mpya wa kimbingu ambao utachukua mahali pa serikali za wanadamu zenye kudhulumu. Dunia itafanyizwa kuwa paradiso yenye miti, nyanda, mito, na wanyama wa pori waliorudishwa. Watu wote watashiriki bila ubinafsi katika kutunza ardhi. Dhuluma na pupa hazitakuwapo tena. Kutakuwa na wingi wa chakula kizuri na utendaji wenye kujenga.

      Pamoja na ufufuo wa wafu, ukosefu wote wa haki wa wakati uliopita utaondolewa. Ndiyo, hata wale Anasazi (neno la Kinavajo la “wakale”), wazazi wa kale wa wengi wa Wahindi wa Pueblo, wanaoishi Arizona na New Mexico, watarudi kupata fursa ya uhai udumuo milele hapa kwenye dunia iliyorekebishwa. Pia, wale viongozi maarufu katika historia ya Wahindi—Geronimo, Fahali Aketiye, Farasi Mwehu, Tecumseh, Manuelito, Chifu Joseph na Chifu Seattle—na wengine wengi waweza kurudi katika ufufuo huo ulioahidiwa. (Yohana 5:28, 29; Matendo 24:15) Ni tazamio zuri kama nini ambalo ahadi za Mungu zawatolea hao pamoja na wale wote wanaomtumikia sasa!

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki