-
Watoto Wetu Ni Urithi Wenye ThamaniMnara wa Mlinzi—2005 | Aprili 1
-
-
Watoto Wetu Ni Urithi Wenye Thamani
“Tazama! Wana ni urithi kutoka kwa Yehova; uzao wa tumbo ni thawabu.”—ZABURI 127:3.
1. Mtoto wa kwanza wa kibinadamu alitokeaje?
HEBU wazia matukio ya ajabu ambayo Yehova Mungu alifanya yawezekane kwa kumuumba mwanamume na mwanamke wa kwanza. Adamu na Hawa, waliungana na kuanzisha chembe ambayo ilikua ndani ya tumbo la uzazi la Hawa na kuwa mtu mpya—mtoto wa kwanza wa kibinadamu. (Mwanzo 4:1) Hadi leo hii, kutungwa mimba na kuzaliwa kwa mtoto ni jambo la ajabu ambalo wengi huliita muujiza.
2. Kwa nini tunaweza kusema kwamba jinsi mtoto anavyokua katika tumbo la mwanamke mjamzito ni muujiza?
2 Kwa siku 270 hivi, yai la mama lililotungishwa mimba, hukua na kuwa mtoto mwenye matrilioni ya chembe. Chembe ya kwanza, ina maagizo yanayohitajiwa ili kufanyiza chembe za aina zaidi ya 200. Chembe hizo za ajabu hufuata maagizo hayo ya ajabu ambayo wanadamu hawawezi kuelewa, na hukua kwa utaratibu sana katika njia inayofaa ili kufanyiza mtu mpya anayeishi!
3. Kwa nini watu wengi wanakubali kwamba Mungu ndiye anayewezesha kuzaliwa kwa mtoto?
3 Unafikiri mtoto huyo ametoka wapi hasa? Bila shaka, ni kwa Yule aliyeuanzisha uhai. Mtunga-zaburi wa Biblia aliimba hivi: “Jueni kwamba Yehova ni Mungu. Yeye ndiye aliyetufanya, wala si sisi wenyewe.” (Zaburi 100:3) Ninyi wazazi, mnajua vizuri kwamba hamkumtokeza mtoto huyo kwa uwezo wenu. Ni Mungu tu mwenye hekima isiyo na kikomo anayeweza kufanya muujiza wa kumuumba mtu. Kwa maelfu ya miaka, watu wengi hawana shaka kwamba mtoto aliye ndani ya tumbo la uzazi la mama yake aliumbwa na Muumba Mtukufu. Vipi wewe?—Zaburi 139:13-16.
4. Ni udhaifu gani walio nao wanadamu ambao Yehova hana?
4 Hata hivyo, je, Yehova ni Muumba tu asiye na hisia ambaye aliwapa wanaume na wanawake uwezo wa kuzaa watoto? Baadhi ya wanadamu hawana hisia, lakini sivyo alivyo Yehova. (Zaburi 78:38-40) Biblia inasema hivi kwenye Zaburi 127:3: “Tazama! Wana [na binti pia] ni urithi kutoka kwa Yehova; uzao wa tumbo ni thawabu.” Urithi ni nini, nao huthibitisha nini? Na tuone.
Urithi na Thawabu
5. Kwa nini watoto ni urithi?
5 Urithi ni kama zawadi. Mara nyingi wazazi hufanya kazi kwa bidii ili kuwaachia watoto wao urithi. Huenda urithi huo ukawa pesa, mali, au kitu fulani kinachothaminiwa sana. Vyovyote vile, urithi ni uthibitisho wa upendo wa wazazi. Biblia inasema kwamba watoto ni urithi ambao Mungu amewapa wazazi. Urithi huo ni zawadi yenye thamani kutoka kwa Mungu. Ikiwa wewe ni mzazi, je, matendo yako yanathibitisha kwamba unawaona watoto wako kuwa zawadi ambayo Muumba wa ulimwengu amekukabidhi?
6. Kwa nini Mungu aliwaumba wanadamu wakiwa na uwezo wa kuzaa watoto?
6 Yehova alipowapa wazazi zawadi hiyo, alikusudia wazao wa Adamu na Hawa waijaze dunia. (Mwanzo 1:27, 28; Isaya 45:18) Yehova hakumuumba mwanadamu mmoja-mmoja kama alivyowaumba mamilioni ya malaika. (Zaburi 104:4; Ufunuo 4:11) Badala yake, Mungu aliwaumba wanadamu wakiwa na uwezo wa kuzaa watoto ambao wanafanana nao. Ni pendeleo kubwa sana kwa mama na baba kumzaa na kumtunza mtoto! Je, ninyi wazazi, mnamshukuru Yehova kwa kuwakabidhi urithi huo wenye thamani?
Iga Mfano wa Yesu
7. Tofauti na jinsi wazazi fulani hufanya, Yesu alionyeshaje kwamba anawapenda na kuwajali “wana wa binadamu”?
7 Inasikitisha kwamba wazazi fulani hawawaoni watoto wao kuwa zawadi. Wengi hawawajali watoto wao. Wazazi hao hawamwigi Yehova wala Mwana wake. (Zaburi 27:10; Isaya 49:15) Ona mtazamo ambao Yesu alikuwa nao kuwaelekea watoto. Hata kabla ya Yesu kuja duniani—alipokuwa malaika mwenye nguvu huko mbinguni—Biblia inasema kwamba ‘vitu alivyopenda sana vilihusiana na wana wa binadamu.’ (Methali 8:31) Aliwapenda sana wanadamu hivi kwamba alikuwa tayari kutoa uhai wake ukiwa fidia ili tupate uzima wa milele.—Mathayo 20:28; Yohana 10:18.
8. Yesu aliwawekeaje wazazi mfano mzuri?
8 Alipokuwa duniani, Yesu aliwawekea wazazi mfano mzuri sana. Fikiria alilofanya. Alitumia wakati pamoja na watoto, hata alipokuwa na shughuli nyingi au mfadhaiko. Aliwatazama wakicheza sokoni na katika mafundisho yake alitaja baadhi ya mambo aliyoona wakifanya. (Mathayo 11:16, 17) Wakati wa safari yake ya mwisho kwenda Yerusalemu, Yesu alijua kwamba angeteseka na kuuawa. Kwa hiyo, watu walipowaleta watoto wamwone, wanafunzi wa Yesu, walijaribu kuwazuia wasimkaribie. Labda walifanya hivyo ili Yesu asipate mfadhaiko zaidi. Lakini Yesu aliwakemea wanafunzi wake. Ili kuonyesha kwamba ‘aliwapenda sana’ watoto, alisema hivi: “Waacheni watoto wachanga waje kwangu; msijaribu kuwazuia.”—Marko 10:13, 14.
9. Kwa nini mambo tunayofanya ni muhimu hata kuliko yale tunayosema?
9 Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Yesu? Watoto wanapotujia, tunatendaje—hata ikiwa tuna shughuli nyingi? Je, tunatenda kama alivyotenda Yesu? Mambo ambayo watoto wanahitaji hasa kutoka kwa wazazi wao ni wakati na usikivu, na Yesu alikuwa tayari kuwapa mambo hayo. Maneno kama vile “nakupenda” ni muhimu. Hata hivyo, matendo huwa na matokeo zaidi kuliko maneno. Upendo wako hautaonekana kupitia mambo unayoyasema tu bali utaonekana hata zaidi kupitia mambo unayofanya. Unaweza kuonyesha kwamba unawapenda watoto wako kwa kutumia wakati pamoja nao, kuwahangaikia, na kuwatunza. Hata hivyo, huenda wazazi wasione mara moja matokeo ya kazi yao hata baada ya kufanya mambo hayo yote. Subira inahitajiwa. Tunaweza kujifunza kuwa na subira kwa kuiga jinsi Yesu alivyowatendea wanafunzi wake.
Subira na Upendo wa Yesu
10. Yesu aliwafundishaje wanafunzi wake unyenyekevu, naye alipata matokeo gani mwanzoni?
10 Yesu alijua kwamba wanafunzi wake walikuwa wakishindana kupata umashuhuri na sifa. Siku moja, baada ya kufika Kapernaumu aliwauliza wanafunzi wake hivi: “‘Mlikuwa mkibishania nini barabarani?’ Wakakaa kimya, kwa maana barabarani walikuwa wamebishana wenyewe, ni nani aliye mkuu zaidi.” Badala ya kuwakemea kwa ukali, Yesu aliwafundisha maana ya unyenyekevu kwa kuwapa mfano. (Marko 9:33-37) Je, alipata matokeo aliyotarajia? Ilichukua muda. Miezi sita baadaye, Yakobo na Yohana walimhimiza mama yao amwombe Yesu awape cheo mashuhuri katika Ufalme. Tena, Yesu akawarekebisha kwa subira.—Mathayo 20:20-28.
11. (a) Mitume walikosa kufanya utumishi gani wa kidesturi baada ya kufika katika chumba cha juu pamoja na Yesu? (b) Yesu alifanya nini, je, jitihada zake zilifanikiwa wakati huo?
11 Punde si punde, wakati wa Pasaka ya mwaka wa 33 W.K. ukafika, naye Yesu akakutana faraghani na mitume wake ili kuisherehekea. Alipoingia katika chumba cha juu, hakuna hata mmoja kati ya mitume wake 12 aliyejitolea kuwaosha wengine miguu kama ilivyokuwa desturi. Kwa kawaida, hiyo ilionwa kuwa kazi ya hali ya chini iliyofanywa na mtumishi au mwanamke. (1 Samweli 25:41; 1 Timotheo 5:10) Lazima Yesu awe alihuzunika sana kuwaona wanafunzi wake wakiendelea kujitafutia cheo na umashuhuri! Kwa hiyo, Yesu akamwosha kila mmoja wao miguu na kuwasihi wamwige kwa kuwatumikia wengine. (Yohana 13:4-17) Je, walifanya hivyo? Biblia inasema kwamba baadaye jioni hiyohiyo “kukatokea pia bishano kali kati yao juu ya ni nani kati yao aliyeonekana kuwa mkuu zaidi ya wote.”—Luka 22:24.
12. Wazazi wanawezaje kumwiga Yesu katika jitihada za kuwazoeza watoto wao?
12 Watoto wenu wasipofuata mashauri yenu, je, ninyi wazazi mnaelewa jinsi Yesu alivyohisi? Kumbuka kwamba Yesu aliendelea kuwasaidia mitume wake bila kukata tamaa licha ya kwamba walichukua muda mrefu kurekebisha makosa yao. Mwishowe subira yake ilikuwa na matokeo. (1 Yohana 3:14, 18) Wazazi mnapaswa kuiga upendo na subira ya Yesu. Msikate tamaa kamwe na kuacha kujitahidi kuwazoeza watoto wenu.
13. Kwa nini mzazi hapaswi kumkemea kwa ukali mtoto anapouliza swali?
13 Watoto wanapaswa kuhisi kwamba wazazi wao wanawapenda na kuwajali. Kwa kuwa Yesu alitaka kujua maoni ya wanafunzi wake, aliwasikiliza walipouliza maswali. Aliwauliza maoni yao kuhusu mambo fulani. (Mathayo 17:25-27) Naam, njia bora ya kufundisha inatia ndani kusikiliza kwa makini na kupendezwa kikweli. Mtoto anapouliza swali, mzazi anapaswa kuepuka mwelekeo wowote wa kumfukuza kwa kumkemea kwa ukali na kumwambia: “Ondoka! Huoni nina kazi?” Ikiwa kwa kweli mzazi ana kazi, anapaswa kumwambia mtoto kwamba watazungumzia jambo hilo baadaye. Kisha wazazi wanapaswa kuhakikisha kwamba wanalizungumzia. Akifanya hivyo, mtoto ataona kwamba kwa kweli mzazi anapendezwa naye, na itakuwa rahisi zaidi kwake kumfunulia mzazi yaliyo moyoni mwake.
14. Wazazi wanaweza kujifunza nini kutoka kwa Yesu kuhusu kuwaonyesha watoto wao upendo?
14 Je, inafaa wazazi kuwaonyesha watoto wao upendo kwa kuwakumbatia? Wazazi wanaweza tena kumwiga Yesu kwa kufanya hivyo. Biblia inasema kwamba ‘alichukua watoto akawakumbatia na kuanza kuwabariki, akiweka mikono yake juu yao.’ (Marko 10:16) Unafikiri watoto walihisije? Bila shaka, walichangamka na kuvutiwa na Yesu! Wazazi, ikiwa kuna upendo wa kweli kati yenu na watoto, watakubali kwa urahisi nidhamu na mafundisho yenu.
Suala la Wakati
15, 16. Ni dhana gani imezuka kuhusu kulea watoto, na huenda imetokana na nini?
15 Watu fulani wanadai kwamba watoto hawahitaji wakati mwingi na upendo kutoka kwa wazazi wao. Dhana fulani imezuka kwamba wazazi wanahitaji tu kuutumia vizuri wakati wanaopata wa kuwa pamoja na watoto wao. Wanaoiunga mkono dhana hiyo wanasema kwamba wazazi hawahitaji kutumia wakati mwingi na watoto wao maadamu wazazi wanafanya matayarisho na mipango mizuri na kuutumia vilivyo wakati wanaopata. Je, unakubaliana na maoni hayo, na je, yanazingatia hali bora ya watoto?
16 Mwandishi mmoja ambaye alikuwa amezungumza na watoto wengi alisema kwamba kile ambacho “watoto wanahitaji sana ni kutumia wakati mwingi pamoja na wazazi wao,” pasipo “vikengeusha fikira.” Profesa mmoja alisema hivi: “Dhana ya kuutumia vizuri wakati imetokana na wazazi wanaohisi kwamba hawatimizi jukumu lao. Watu walikuwa wakitafuta udhuru wa kutumia wakati mchache zaidi na zaidi pamoja na watoto wao.” Wazazi wanapaswa kutumia kiasi gani cha wakati pamoja na watoto wao?
17. Watoto wanahitaji nini kutoka kwa wazazi wao?
17 Biblia haitaji. Hata hivyo, wazazi Waisraeli walihimizwa wazungumze na watoto wao nyumbani mwao, wanapotembea barabarani, wanapolala, na wanapoamka. (Kumbukumbu la Torati 6:7) Ni wazi kwamba wazazi wanapaswa kuzungumza na watoto na kuwafundisha daima kila siku.
18. Yesu alitumiaje kila nafasi kuwafundisha wanafunzi wake, na wazazi wanaweza kujifunza nini kutokana na hilo?
18 Yesu alifaulu kuwafundisha wanafunzi wake alipokuwa akila pamoja nao, akisafiri pamoja nao, na hata kupumzika pamoja nao. Kwa hiyo, alitumia vizuri kila nafasi aliyopata ili kuwafundisha. (Marko 6:31, 32; Luka 8:1; 22:14) Vivyo hivyo, wazazi Wakristo wanapaswa kuwa tayari kutumia kila nafasi kukuza na kudumisha mawasiliano mazuri kati yao na watoto wao na kuwafundisha njia za Yehova.
Mambo ya Kufundisha na Jinsi ya Kufundisha
19. (a) Mbali na kutumia wakati pamoja na watoto ni nini kingine kinachohitajiwa? (b) Ni mambo gani hasa ambayo wazazi wanapaswa kuwafundisha watoto wao?
19 Ili kufanikiwa kuwalea watoto, mengi zaidi yanahitajiwa kuliko tu kutumia wakati pamoja nao na kuwafundisha. Mambo wanayofundishwa ni muhimu pia. Ona jinsi Biblia inavyokazia mambo ambayo watoto wanapaswa kufundishwa. Inasema: ‘Maneno haya ninayokuamuru leo lazima uyakazie kwa mwana wako.’ Ni “maneno” gani hayo ambayo watoto wanapaswa kufundishwa? Haikosi ni maneno haya yaliyotoka tu kutajwa: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa nguvu zako zote.” (Kumbukumbu la Torati 6:5-7) Yesu alisema kwamba hiyo ndiyo amri iliyo kuu kati ya amri zote za Mungu. (Marko 12:28-30) Wazazi wanapaswa kuwafundisha watoto wao kumhusu Yehova hasa na kuwaeleza ni kwa nini ni yeye peke yake tunayepaswa kumpenda na kufanya mapenzi yake kwa nafsi yote.
20. Mungu aliwaagiza wazazi wa zamani wawafundishe watoto wao nini?
20 Hata hivyo, “maneno” ambayo wazazi wanahimizwa wawafundishe watoto wao yanatia ndani mengi zaidi ya kumpenda Mungu kwa nafsi yao yote. Utaona kwamba katika sura inayotangulia ya kitabu cha Kumbukumbu la Torati, Musa anataja tena zile sheria ambazo Mungu aliandika kwenye mabamba ya mawe—zile Amri Kumi. Sheria hizo zinatia ndani amri kama vile usiseme uwongo, usiibe, usiue, na usifanye uzinzi. (Kumbukumbu la Torati 5:11-22) Kwa hiyo, wazazi wa zamani walikaziwa umuhimu wa kuwafundisha watoto wao maadili mazuri. Wazazi Wakristo leo wanapaswa kuwafundisha vivyo hivyo watoto wao ili wawe na wakati ujao ulio salama, na wenye furaha.
21. Agizo la wazazi ‘kuyakazia’ maneno ya Mungu kwa watoto wao linamaanisha nini?
21 Ona kwamba wazazi wanaelezwa jinsi ya kuwafundisha watoto wao “maneno” au amri hizo: “Lazima uyakazie kwa mwana wako.” Neno linalotafsiriwa ‘-kazia’ linamaanisha “kufundisha na kukazia jambo kwa kurudia-rudia au kuhimiza: kuchochea au kukaza akilini.” Kwa hiyo, ni kana kwamba Mungu anawaambia wazazi wawe na mpango wa kuwafundisha watoto wao Biblia, mpango ambao kusudi lake la pekee ni kukazia mambo ya kiroho katika akili za watoto wao.
22. Wazazi wa Israeli waliambiwa wafanye nini ili kuwafundisha watoto wao, na hilo linamaanisha nini?
22 Wazazi wanahitaji kujitahidi ili kuwa na mpango mzuri wa kuwafundisha watoto wao. Biblia inasema: “Nawe uyafunge [“maneno,” au amri za Mungu] kama ishara kwenye mkono wako, na yawe kama utepe wa kipaji katikati ya macho yako; nawe uyaandike juu ya miimo ya mlango wa nyumba yako na juu ya malango yako.” (Kumbukumbu la Torati 6:8, 9) Hiyo haimaanishi kwamba wazazi wanapaswa kuandika kihalisi sheria za Mungu katika miimo ya milango na malango au kufunga nakala ya sheria hizo kwenye mikono ya watoto wao au katikati ya macho yao. Badala yake, inamaanisha kwamba wazazi wanapaswa kuwakumbusha daima watoto wao mafundisho ya Mungu. Wazazi wanapaswa kuwafundisha watoto kwa ukawaida sana hivi kwamba ni kana kwamba mafundisho ya Mungu yako mbele ya watoto wao nyakati zote.
23. Ni mambo gani yatakayozungumziwa katika funzo la juma lijalo?
23 Ni mambo gani muhimu ambayo wazazi wanapaswa kuwafundisha watoto wao? Kwa nini watoto wanapaswa kufundishwa na kuzoezwa kujilinda leo? Ni nini kinachoweza kuwasaidia wazazi kuwafundisha watoto wao ifaavyo leo? Maswali hayo pamoja na mengine yanayowahangaisha wazazi wengi yatazungumziwa katika makala inayofuata.
-
-
Wazazi, Ulindeni Urithi Wenu Wenye ThamaniMnara wa Mlinzi—2005 | Aprili 1
-
-
Wazazi, Ulindeni Urithi Wenu Wenye Thamani
“Hekima ni ulinzi . . . huwahifadhi hai waliyo nayo.”—MHUBIRI 7:12.
1. Kwa nini wazazi wanapaswa kuwaona watoto wao kuwa zawadi?
WAZAZI huzaa watoto wanaofanana nao, wenye sifa na utu kama wao. Biblia inawaita watoto hao “urithi kutoka kwa Yehova.” (Zaburi 127:3) Kwa kweli Yehova ndiye Mpaji-Uhai, hivyo anawakabidhi wazazi mali yake. (Zaburi 36:9) Wazazi mnaionaje zawadi hiyo yenye thamani kutoka kwa Mungu?
2. Manoa alitendaje alipoambiwa kwamba atapata mtoto?
2 Kwa kweli, zawadi hiyo inapaswa kuthaminiwa sana. Zaidi ya miaka 3,000 iliyopita, Mwisraeli aliyeitwa Manoa alifanya hivyo mke wake alipoambiwa na malaika kwamba atazaa mtoto. Baada ya kusikia habari hizo njema, Manoa alisali hivi: “Nakuomba radhi, Yehova. Tafadhali, yule mtu wa Mungu wa kweli ambaye ulimtuma na arudi kwetu tena, atufundishe yale tunayopaswa kumtendea huyo mtoto atakayezaliwa.” (Waamuzi 13:8) Wazazi, mnaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Manoa?
Kwa Nini Wazazi Wanahitaji Msaada wa Mungu Leo?
3. Kwa nini wazazi wanahitaji msaada wa Mungu katika kulea watoto wao hasa leo?
3 Leo hasa, wazazi wanahitaji msaada wa Yehova katika kuwalea watoto wao. Kwa nini? Shetani Ibilisi na malaika zake wametupwa duniani kutoka mbinguni. Biblia inaonya hivi: “Ole wa dunia . . . kwa sababu Ibilisi ameshuka kwenu, akiwa na hasira kali, akijua kwamba ana kipindi kifupi cha wakati.” (Ufunuo 12:7-9, 12) Biblia inasema kwamba Shetani ni “kama simba anayenguruma, akitafuta kummeza mtu.” (1 Petro 5:8) Kwa kawaida simba huwinda wanyama walio dhaifu, hasa walio wachanga. Basi, wazazi Wakristo wenye hekima humtegemea Yehova awafundishe jinsi ya kuwalinda watoto wao. Unajitahidi kadiri gani kuwalinda watoto wako?
4. (a) Wazazi wangetendaje ikiwa wangejua kwamba kuna simba anayetembea-tembea mtaani? (b) Watoto wanahitaji nini ili wawe salama?
4 Ikiwa ungejua kwamba kuna simba anayetembea-tembea mtaani, jambo la kwanza ambalo ungefanya ni kuwalinda watoto wako. Shetani ni mwindaji hatari. Yeye hujaribu kuwapotosha watu wa Mungu, na hivyo kuwafanya wakose kibali cha Mungu. (Ayubu 2:1-7; 1 Yohana 5:19) Watoto ni mawindo rahisi. Ili waepuke mitego ya Ibilisi, lazima watoto wamjue na kumtii Yehova. Wanahitaji ujuzi wa Biblia. Yesu alisema: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yohana 17:3) Isitoshe, watoto wanahitaji hekima, yaani, uwezo wa kuelewa na kutumia mambo wanayojifunza. Kwa kuwa “hekima huwahifadhi hai waliyo nayo,” ninyi wazazi mnahitaji kuingiza kweli mioyoni mwa watoto wenu. (Mhubiri 7:12) Mnawezaje kufanya hivyo?
5. (a) Wazazi wanawezaje kuwafundisha watoto wao ili wawe na hekima? (b) Methali inaelezaje thamani ya hekima?
5 Unaweza na unapaswa kuwasomea watoto wako Neno la Mungu. Lakini mengi zaidi yanahitajiwa ili kuwasaidia kumpenda na kumtii Yehova. Wanahitaji uelewaji. Kwa mfano: Mtoto anaweza kuambiwa asivuke barabara kabla ya kuangalia upande wa kushoto na wa kulia. Hata hivyo, watoto fulani hawatii. Kwa nini? Kwa sababu huenda hawakuambiwa tena na tena matokeo ya kugongwa na gari au hawakuelezwa kwa njia ambayo itawasaidia kuelewa vizuri hatari yenyewe na hivyo kuepuka “ujinga” unaoweza kuwafanya wagongwe na gari. Ili kuwafundisha watoto kuwa na hekima, wazazi wanahitaji wakati na subira nyingi. Hata hivyo, hekima ni yenye thamani sana! Biblia inasema, “njia zake ni njia za uzuri, na barabara zake zote ni amani. Ni mti wa uzima kwa wale wanaoishika, na wale wanaoishika sana wataitwa wenye furaha.”—Methali 3:13-18; 22:15.
Njia Bora ya Kuwafundisha Watoto Kuwa na Hekima
6. (a) Kwa nini mara nyingi watoto hutenda kipumbavu? (b) Ni vita gani vinavyoendelea?
6 Mara nyingi watoto hufanya kosa, si kwa sababu hawajafundishwa lililo sawa, bali kwa sababu mafundisho hayo hayajaingia moyoni mwao. Ibilisi anajitahidi sana kuipotosha mioyo ya vijana. Anajaribu kuwanasa kwa kutumia uvutano wa kilimwengu. Pia hujaribu kutumia mielekeo yao yenye dhambi ili kuwashawishi kutenda maovu. (Mwanzo 8:21; Zaburi 51:5) Wazazi wanapaswa kutambua kwamba kuna vita vikali vya kuipotosha mioyo ya watoto wao.
7. Kwa nini haitoshi tu kumwambia mtoto yaliyo mema au mabaya?
7 Kwa kawaida wazazi humwambia mtoto yaliyo mema na mabaya, wakiamini kwamba wamemfundisha kanuni fulani ya maadili. Huenda wakamwambia mtoto kwamba ni kosa kusema uwongo, kuiba, au kufanya ngono na mtu yeyote ambaye si mwenzi wake wa ndoa. Hata hivyo, kuambiwa tu na wazazi wake jambo la kufanya hakutoshi kumchochea mtoto kutii. Hizo ni sheria za Yehova. Mtoto anapaswa kujua kwamba ni jambo la hekima kutii amri za Mungu.—Methali 6:16-19; Waebrania 13:4.
8. Ni njia gani ya kufundisha inayoweza kuwasaidia watoto watende kwa hekima?
8 Mtoto anaweza kusaidiwa kuelewa kuwapo kwa Muumba mwenye hekima kutokana na mambo kama vile maajabu ya ulimwengu, aina mbalimbali za viumbe, na mabadiliko ya majira. (Waroma 1:20; Waebrania 3:4) Isitoshe, mtoto anapaswa kufundishwa kwamba Mungu anampenda na amefanya mpango wa kumpa uzima wa milele kupitia dhabihu ya Mwana Wake na kwamba anaweza kumfurahisha Mungu kwa kumtii. Huenda kufanya hivyo kutamchochea mtoto aamue kumtumikia Yehova zijapokuwa jitihada za Ibilisi za kujaribu kumzuia.—Methali 22:6; 27:11; Yohana 3:16.
9. (a) Ni ufundishaji gani unaookoa uhai? (b) Akina baba wanaagizwa wafanye nini, na hilo linatia ndani nini?
9 Ili kumpa mtoto mafundisho yanayomlinda na kumchochea kufanya yaliyo sawa, mzazi anahitaji kutumia wakati, kuwa msikivu, na kufanya mipango mizuri. Wazazi wanapaswa kukubali mwongozo wa Mungu. Biblia inasema: “Nanyi, akina baba, . . . endeleeni kuwalea [watoto wenu] katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova.” (Waefeso 6:4) Hilo linamaanisha nini? Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “mwongozo wa akilini” linatoa wazo la “kuingiza akili [nyingine] ndani ya.” Kwa hiyo, akina baba wanahimizwa waingize akili ya Yehova ndani ya watoto wao. Huo utakuwa ulinzi ulioje! Ikiwa maoni ya Mungu na njia yake ya kufikiri itakaziwa katika akili za watoto, watalindwa wasipatwe na mabaya.
Tamaa Inayochochewa na Upendo
10. Ili kumfundisha mtoto wako ifaavyo, ni muhimu kujua nini?
10 Hata hivyo, ili ufanikiwe kumlea mtoto wako kwa njia inayofaa, unapaswa kuchochewa na upendo. Mojawapo ya mambo muhimu ni kuwa na mawasiliano mazuri. Mwelewe mtoto wako na ujue maoni yake. Mchochee kwa busara mtoto wako ajieleze katika hali yenye kustarehesha. Wakati mwingine huenda ukashangaa kusikia anayosema. Dhibiti hisia zako. Msikilize kwa makini.
11. Mzazi anawezaje kuingiza akili ya Mungu ndani ya mtoto?
11 Ni kweli kwamba huenda umemsomea mtoto wako sheria za Mungu zinazokataza uasherati katika Biblia. Huenda hata umefanya hivyo mara kadhaa. (1 Wakorintho 6:18; Waefeso 5:5) Huenda watoto wako wanaelewa mambo yanayompendeza Yehova na yale yasiyompendeza. Hata hivyo, unahitaji kufanya mengi zaidi ili kuingiza akili ya Yehova ndani ya mtoto. Watoto wanahitaji kusaidiwa ili wajue umuhimu wa sheria za Yehova. Wanahitaji kusadikishwa kwamba sheria zake ni nzuri na zenye manufaa na kwamba wanapaswa kuzitii. Unapowafundisha watoto wako, wasaidie waelewe sababu za Kimaandiko na kukubali maoni ya Mungu. Ukifanya hivyo, basi utakuwa ukiingiza akili ya Yehova ndani yao.
12. Mzazi anawezaje kumsaidia mtoto wake awe na maoni yanayofaa kuhusu ngono?
12 Unapozungumza kuhusu ngono, unaweza kumuuliza, “Je, unafikiri kutii sheria ya Mungu inayokataza kufanya ngono kabla ya ndoa kunamnyima mtu furaha?” Mtie moyo mtoto wako afafanue jibu lake. Baada ya kuzungumzia utaratibu wa Mungu wa kutokeza mtoto, unaweza kumuuliza: “Je, unafikiri Mungu wetu mwenye upendo angetunga sheria ili kutuzuia tusifurahie maisha? Au unafikiri sheria hizo zimekusudiwa kutufanya tuwe na furaha na kutulinda?” (Zaburi 119:1, 2; Isaya 48:17) Jitahidi kujua maoni ya mtoto wako kuhusu jambo hilo. Kisha unaweza kumsimulia mifano inayoonyesha jinsi mwenendo mpotovu katika ngono umesababisha maumivu na matatizo. (2 Samweli 13:1-33) Kwa kumsaidia mtoto wako aelewe na kukubali maoni ya Mungu, utakuwa umejitahidi sana kuingiza akili ya Mungu ndani yake. Hata hivyo, kuna jambo lingine unaloweza kufanya.
13. Mtoto anaweza kuchochewa kumtii Yehova akielewa nini hasa?
13 Mbali na kumfundisha mtoto wako matokeo mabaya ya kutomtii Yehova, ni jambo la hekima kumweleza jinsi Yehova anavyohisi kuhusu mwenendo wetu maishani. Mwonyeshe mtoto wako katika Biblia kwamba tunaweza kumtia Yehova uchungu tusipofanya mapenzi yake. (Zaburi 78:41) Huenda ukamuuliza, “Kwa nini hungependa kumtia Yehova uchungu?” Kisha mweleze: “Adui ya Mungu, Shetani anadai kwamba tunamtumikia Mungu kwa sababu ya ubinafsi wala si kwa sababu tunampenda.” Kisha mweleze jinsi Ayubu alivyomfurahisha Yehova kwa kuwa mwaminifu na hivyo kupinga mashtaka ya uwongo ya Shetani. (Ayubu 1:9-11; 27:5) Mtoto wako anahitaji kuelewa kwamba mwenendo wake unaweza kumfurahisha Yehova au kumhuzunisha. (Methali 27:11) Watoto wanaweza kufundishwa mambo hayo muhimu na mengine mengi kwa kutumia kitabu Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu.a
Matokeo Yenye Kuridhisha
14, 15. (a) Ni mambo gani yaliyo katika kitabu Mwalimu ambayo yamewachochea watoto? (b) Umepata matokeo gani mazuri kwa kutumia kitabu hicho? (Pia ona sanduku kwenye ukurasa wa 18-19.)
14 Babu mmoja huko Kroatia ambaye humsomea mjukuu wake mwenye umri wa miaka saba kitabu Mwalimu, anasema kwamba mtoto huyo alimwambia yafuatayo: “Mama aliniambia nifanye jambo fulani, lakini sikutaka kulifanya. Kisha nikakumbuka sura yenye kichwa ‘Utii Unakulinda Wewe,’ na hivyo nikarudi na kumwambia kwamba nitamtii.” Kuhusu ile sura yenye kichwa “Kwa Nini Hatupaswi Kusema Uwongo,” wenzi fulani wa ndoa huko Florida, Marekani walisema hivi: “Ina maswali yanayowachochea watoto waeleze yaliyo moyoni mwao na kukubali makosa ambayo huenda hawangeyakubali.”
15 Kitabu Mwalimu kina picha zaidi ya 230, pia kuna maelezo, au ufafanuzi, kwenye kila picha au picha kadhaa. Mama mmoja anayethamini kitabu hicho alisema: “Mara nyingi mwana wangu akiona picha huiangalia kwa muda mrefu na hataki ukurasa mwingine ufunguliwe. Mbali na kuvutia, picha hizo hufundisha na kuwachochea watoto waulize maswali. Mwanangu alipoona ile picha inayoonyesha mtoto akitazama televisheni kwenye chumba chenye giza, aliuliza, ‘Mama, huyu mvulana anafanya nini?’ kwa sauti inayoonyesha kwamba anaelewa kuna tatizo.” Kando ya picha hiyo kuna swali: “Ni nani anayeweza kuona kila kitu tunachofanya?”
Elimu Muhimu Leo
16. Ni jambo gani muhimu ambalo watoto wanapaswa kufundishwa leo na kwa nini?
16 Watoto wanapaswa kujua matumizi yanayofaa na yasiyofaa ya viungo vyao vya siri. Hata hivyo, kuzungumzia mambo hayo si rahisi. Mwandishi wa gazeti moja alisema kwamba alipokuwa mchanga ilikuwa mwiko kutaja viungo vya uzazi. Aliandika hivi kuhusu kuwafundisha watoto wake: “Lazima nishinde aibu yangu.” Kwa kweli, wazazi wanapoepuka kuzungumzia masuala ya ngono kwa sababu ya aibu, hawawalindi watoto wao. Watu wanaowatendea vibaya kingono watoto hutumia kwa faida yao kutojua kwa watoto. Kitabu Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu huzungumzia mambo hayo kwa staha na heshima. Kuwajulisha watoto juu ya ngono hakutawafanya wajiingize katika mambo hayo bali kunaweza kuwalinda na kuwaepusha na hatari.
17. Kitabu Mwalimu kinawasaidiaje wazazi kuwafundisha watoto wao mambo yanayohusu ngono?
17 Mnapozungumzia sura ya 10 kuhusu malaika waovu waliokuja duniani na kuzaa watoto, kuna swali ambalo mtoto anatakiwa ajibu, “Ngono ni nini?” Kitabu Mwalimu kinajibu kwa njia rahisi na yenye heshima. Baadaye, sura ya 32 inaeleza jinsi watoto wanavyoweza kulindwa kutokana na watu wanaotaka kuwatendea vibaya kingono. Watu wengi wameandika barua kusema kwamba mafundisho hayo ni muhimu. Mama mmoja aliandika: “Mwanangu Javan alipoenda kumwona daktari juma lililopita, daktari huyo aliniuliza ikiwa tumezungumza naye kuhusu matumizi yanayofaa ya viungo vya uzazi. Alifurahi sana kujua kwamba tulifanya hivyo tukitumia kitabu chetu kipya.”
18. Kitabu Mwalimu kinasema nini kuhusu kuheshimu nembo za kitaifa?
18 Sura nyingine inazungumzia masimulizi ya Biblia ya wale vijana watatu Waebrania, Shadraka, Meshaki, na Abednego ambao walikataa kuiinamia sanamu iliyowakilisha Serikali ya Babiloni. (Danieli 3:1-30) Huenda wengine wasione uhusiano kati ya kuabudu sanamu na kuisalimu bendera, kama kitabu Mwalimu kinavyosema. Hata hivyo, fikiria alivyosema mhariri Edward Gaffney, katika gazeti la U.S. Catholic. Alitaja kwamba binti yake alipomwambia amejifunza “sala mpya shuleni” siku ya kwanza, alimwomba amkaririe. Gaffney asema: “Aliuweka mkono wake kifuani na kusema hivi kwa fahari, ‘Naapa kwamba nitakuwa mwaminifu kwa bendera . . . ’” Mhariri huyo aendelea kusema: “Papo hapo nikaelewa. Mashahidi wa Yehova hawakuwa wamekosea. Tangu wakiwa na umri mchanga, watoto wanafundishwa kuabudu na kuwa waaminifu kabisa kwa taifa.”
Fanya Yote Uwezayo
19. Kuwafundisha watoto huleta thawabu gani?
19 Kwa kweli, unapaswa kufanya yote uwezayo ili kuwafundisha watoto wako. Mama mmoja huko Kansas, Marekani, alitokwa na machozi baada ya kupokea barua kutoka kwa mwanaye. Aliandika hivi: “Nafurahi sana kwamba malezi yangu yamenisaidia kuwa mtulivu na mwenye usawaziko. Bila shaka, wewe na Baba mnastahili pongezi.” (Methali 31:28) Kitabu Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu kinaweza kuwasaidia wazazi wengi zaidi waulinde urithi wao wenye thamani kwa kuwafundisha watoto wao.
20. Wazazi wanapaswa kukumbuka nini sikuzote, na hilo linapaswa kuwa na matokeo gani kwao?
20 Watoto wetu wanastahili wakati, usikivu, na jitihada zote tunazoweza kutoa. Hawatakuwa watoto milele. Tumia vizuri kila nafasi ili kuwa nao na kuwasaidia. Hutajuta kamwe kwa kufanya hivyo. Watakupenda sana. Kumbuka sikuzote kwamba watoto wako ni zawadi kutoka kwa Mungu. Nao ni urithi wenye thamani sana! (Zaburi 127:3-5) Kwa hiyo, watunze kana kwamba Mungu atakutoza hesabu, kwa kuwa kwa kweli, una wajibu mbele za Mungu.
[Maelezo ya Chini]
a Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova. Ona sura ya 40, yenye kichwa, “Jinsi ya Kumfurahisha Mungu.”
-