Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Ulimwengu Usio na Haki
    Mnara wa Mlinzi—2005 | Novemba 1
    • Ulimwengu Usio na Haki

      JE, UNAKUBALI kwamba tunaishi katika ulimwengu usio na haki? Bila shaka. Ukweli ni kwamba, hata tuwe na vipawa vya aina gani au kupanga maisha yetu kwa hekima kadiri gani, hatuwezi kuwa na uhakika kwamba tutapata utajiri au mafanikio au hata chakula. Mara nyingi maisha yanakuwa kama vile Mfalme Sulemani wa kale mwenye hekima alivyosema: “Si . . . wenye hekima wanaopata chakula, wala pia wenye uelewaji wanaokuwa na utajiri, wala wenye ujuzi wanaopata kibali.” Kwa nini? Kwa sababu, kama Sulemani anavyoendelea kusema, “wakati na tukio lisilotazamiwa huwapata wote.”—Mhubiri 9:11.

      ‘Wakati Wenye Msiba Unapoanguka kwa Ghafula’

      Naam, “wakati na tukio lisilotazamiwa,” ambao mara nyingi humaanisha kuwa mahali pasipofaa kwa wakati usiofaa, huharibu mambo tuliyopangia kwa uangalifu na matumaini yetu makubwa. Kulingana na Sulemani, sisi ni “kama vile samaki wanaonaswa katika wavu mbovu, na kama ndege wanaonaswa katika mtego,  . . . wakati wenye msiba, unapowaangukia ghafula.” (Mhubiri 9:12) Kwa mfano, mamilioni ya watu hufanya kazi ya kulima kwa bidii ili wapate chakula kwa ajili ya familia zao, halafu kwa ghafula wao hunaswa na “wakati wenye msiba” mvua inapokosa kunyesha na ukame unapoharibu mazao yao.

      Ingawa wengine hujaribu kusaidia, mara nyingi msaada unaotolewa na jamii ya kimataifa kwa wale wanaoathiriwa na “wakati wenye msiba” huonekana kuwa usio wa haki. Kwa mfano, katika jitihada za kupambana na njaa, katika mwaka mmoja hivi karibuni, “bara lote [la Afrika] lilipokea asilimia 20 tu ya pesa zilizotengwa kwa ajili ya vita vya Ghuba,” lasema shirika moja kubwa la kutoa misaada. Je, ni haki kwamba nchi zenye utajiri zilitumia mara tano ya kiasi hicho cha pesa kupigana vita katika nchi moja huku zikitumia sehemu moja tu ya kiasi hicho cha pesa ili kuondoa maumivu na kuteseka kunakosababishwa na njaa katika bara zima? Na je, ni haki kwamba katika enzi ambayo watu wengi ni matajiri, mkaaji 1 kati ya wakaaji 4 duniani bado ni maskini kupindukia au kwamba mamilioni ya watoto wanakufa kila mwaka kutokana na magonjwa yanayoweza kuzuiwa? La hasha!

      Bila shaka, mambo mengi zaidi ya “wakati na tukio lisilotazamiwa” yanahusika ‘wakati wenye msiba unapoanguka ghafula.’ Kuna watu wenye nguvu zaidi ambao wanatawala maisha yetu na kuamua yale yanayotupata. Hivyo ndivyo ilivyotukia huko Beslan, Alania, mwaka wa 2004, wakati mamia ya watu, wengi wao wakiwa watoto katika siku yao ya kwanza shuleni, walipokufa katika mapambano ya kinyama kati ya magaidi na askari wa usalama. Ni wazi kwamba lililotukia kwa wale waliokufa na kwa wale waliookoka msiba huo lilitokana hasa na wakati na tukio lisilotazamiwa. Hata hivyo, kilichosababisha hasa ‘wakati huo wenye msiba’ ni mapambano ya wanadamu.

      Je, Hali Zitakuwa Hivyo Sikuzote?

      Watu fulani husema hivi wanapozungumza kuhusu ukosefu wa haki: “Lakini hiyo ndiyo kawaida ya maisha. Sikuzote hali imekuwa hivyo, na itaendelea kuwa hivyo.” Kwa maoni yao, sikuzote watu wenye nguvu wataendelea kuwakandamiza wanyonge, na sikuzote matajiri watawatumia maskini kwa faida yao. Wao husema kwamba mambo hayo pamoja na “wakati na tukio lisilotazamiwa,” yataendelea kutuathiri maadamu tunaendelea kuishi.

      Lakini, je, hali kwa kweli inapaswa kuwa hivyo? Je, itawezekana kwa wale wanaotumia vizuri uwezo wao kwa akili na kwa hekima kupata thawabu iliyo ya haki kutokana na kazi yao yote ngumu? Je, kuna mtu anayeweza kuleta mabadiliko ya kudumu katika ulimwengu usio na haki? Kwa habari hiyo, chunguza yale yanayosemwa katika makala inayofuata.

  • Je, Kweli Kuna Mtu Anayeweza Kuubadili Ulimwengu?
    Mnara wa Mlinzi—2005 | Novemba 1
    • Je, Kweli Kuna Mtu Anayeweza Kuubadili Ulimwengu?

      “Maskini hutuambia kwamba jambo la kwanza kabisa wanalotaka ni amani na usalama, halafu njia za kuboresha maisha yao. Wanataka sera za kitaifa na kimataifa ziwe za haki ili jitihada zao zisizuiwe na nchi na makampuni tajiri.”

      HIVYO ndivyo mkurugenzi wa shirika moja la kimataifa la misaada alivyosema kuhusu matumaini na matarajio ya maskini. Kwa kweli, maneno yake yanaonyesha vizuri tamaa ya wote wanaoathiriwa na misiba na ukosefu wa haki ulimwenguni. Wote wanatamani sana ulimwengu wenye amani na usalama wa kweli. Je, ulimwengu kama huo utakuwepo? Kwa kweli, je, kuna mtu aliye na mamlaka na uwezo wa kuubadili ulimwengu huu usio na haki?

      Jitihada za Kuleta Mabadiliko

      Watu wengi wamejaribu. Kwa mfano, Florence Nightingale, mwanamke Mwingereza wa karne ya 19, alijitolea kuwatunza wagonjwa kwa huruma na kwa kudumisha usafi. Katika siku zake, kabla ya dawa za kuzuia na kuua bakteria kuvumbuliwa, hali za kuwatunza wagonjwa hazikuwa kama zilivyo leo. Kulingana na kitabu kimoja, “wauguzi hawakuwa wameelimishwa, hawakuwa safi, na walijulikana kuwa walevi na wenye kukosa maadili.” Je, Florence Nightingale alifanikiwa katika jitihada zake za kuubadili uuguzi? Naam. Vivyo hivyo, watu wengi wanaojali, wasio na ubinafsi, wamekuwa na mafanikio makubwa katika sehemu nyingi za maisha kama vile, kufundisha watu kusoma na kuandika, kuwaelimisha, kuwatibu, kuwapa makao, kuwalisha, na kadhalika. Kwa sababu hiyo, maisha ya mamilioni ya watu wa hali ya chini yameboreka sana.

      Hata hivyo, hatuwezi kupuuza jambo hili lenye kuhuzunisha: Mamia ya mamilioni ya watu bado wanateseka kutokana na vita, uhalifu, magonjwa, njaa, na matukio mengine yenye kuhuzunisha. Shirika la Ireland la kutoa misaada linaloitwa Concern linasema: “Watu 30,000 hufa kila siku kwa sababu ya umaskini.” Ingawa utumwa umeshutumiwa sana kwa karne nyingi na wateteaji wa marekebisho, bado unaendelea. Kitabu Disposable People—New Slavery in the Global Economy kinasema: “Leo kuna watumwa wengi kuliko wale watu wote walioibwa Afrika na kusafirishwa kupitia Bahari ya Atlantiki wakati wa biashara ya utumwa.”

      Ni nini kimezuia jitihada za wanadamu za kuleta mabadiliko kamili na ya kudumu? Je, ni matajiri na watu wenye mamlaka, au mambo mengi zaidi yanahusika?

      Vizuizi vya Mabadiliko

      Kulingana na Neno la Mungu, Shetani Ibilisi ndiye hasa anayezuia jitihada za mwanadamu za kuleta haki ulimwenguni. Mtume Yohana anatueleza kwamba “ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.” (1 Yohana 5:19) Kwa kweli, hata leo, Shetani ndiye “anayeipotosha dunia nzima inayokaliwa.” (Ufunuo 12:9) Kabla ya uvutano mwovu wa Shetani kuondolewa, watu wanaoathiriwa na uovu na ukosefu wa haki wataendelea kuwepo. Hata hivyo, hali hii yenye kuhuzunisha ilitokeaje?

      Wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa, walipewa dunia ambayo ilikusudiwa kuwa makao makamilifu ya paradiso kwa ajili ya jamii yote ya kibinadamu, yaani, ulimwengu ambao ulikuwa ‘mwema sana.’ (Mwanzo 1:31) Ni nani aliyebadili mambo? Ni Shetani. Alitilia shaka haki ya Mungu ya kuweka sheria kuhusu jinsi wanaume na wanawake wanavyopaswa kujiendesha maishani. Alidai kwamba njia ya Mungu ya kutawala haikuwa ya haki. Aliwashawishi Adamu na Hawa wachague njia ya kujitegemea ili kujiamulia yaliyo mema na yaliyo mabaya. (Mwanzo 3:1-6) Jambo hilo lilitokeza kizuizi cha pili kwa jitihada za mwanadamu za kuleta ulimwengu wenye haki, yaani, dhambi na kutokamilika.—Waroma 5:12.

      Kwa Nini Vimeruhusiwa?

      Huenda wengine wakauliza: ‘Hata hivyo, kwa nini Mungu aliruhusu dhambi na kutokamilika viendelee?’ ‘Kwa nini hakutumia nguvu zake zisizo na mipaka kuwaharibu waasi hao na kuanzisha mambo upya?’ Huenda hilo lingekuwa suluhisho rahisi. Hata hivyo, matumizi ya mamlaka hutokeza maswali mazito. Je, si kweli kwamba kutumia mamlaka vibaya ni mojawapo ya mambo yanayowahangaisha maskini na watu wanaoonewa ulimwenguni? Je, si kweli kwamba watu wanyoofu huhangaika wakati mtawala fulani katili anapotumia mamlaka kumwangamiza yeyote asiyekubaliana na sera zake?

      Ili kuwahakikishia watu wanyoofu kwamba Yeye si mtawala katili anayetumia vibaya mamlaka yake, Mungu aliamua, kwa muda mfupi tu, kumruhusu Shetani na wanadamu waasi watende bila kutegemea sheria na kanuni zake. Wakati ungethibitisha kwamba njia ya Mungu ya kutawala ndiyo tu iliyo sawa. Wakati ungeonyesha kwamba vizuizi vyovyote ambavyo Mungu hutuwekea vinatufaidi. Kwa kweli, matokeo mabaya ya uasi dhidi ya utawala wa Mungu tayari yamethibitisha ukweli huo. Matokeo hayo yamethibitisha kwamba Mungu ana haki kabisa ya kutumia nguvu zake kuu ili kukomesha uovu wote kwa wakati wake. Na hilo litatukia hivi karibuni.—Mwanzo 18:23-32; Kumbukumbu la Torati 32:4; Zaburi 37:9, 10, 38.

      Kabla ya Mungu kuchukua hatua, tunalazimika kuishi katika mfumo huu usio na haki ‘tukiugua pamoja na kuwa katika maumivu pamoja.’ (Waroma 8:22) Hata tufanye jitihada gani ili kubadili mambo, hatuna uwezo wa kumwondoa Shetani, wala kuondoa kabisa kutokamilika kunakosababisha mateso yetu yote. Ni wazi kwamba hatuwezi kuondoa madhara ya dhambi ya Adamu iliyorithiwa.—Zaburi 49:7-9.

      Yesu Kristo Ataleta Mabadiliko ya Kudumu

      Je, hilo linamaanisha kwamba hakuna tumaini kabisa? La hasha. Mtu aliye na nguvu sana kuliko mwanadamu duni anayeweza kufa amepewa daraka la kuleta mabadiliko ya kudumu. Ni nani huyo? Ni Yesu Kristo. Anaelezwa katika Biblia kuwa Wakili Mkuu wa Mungu kwa ajili ya wokovu wa wanadamu.—Matendo 5:31.

      Anangoja sasa “wakati uliowekwa” na Mungu ili kuchukua hatua. (Ufunuo 11:18) Atafanya nini hasa? Ataleta mabadiliko kwa ‘kurudisha mambo yote ambayo Mungu alisema kupitia kinywa cha manabii wake watakatifu wa nyakati za kale.’ (Matendo 3:21) Kwa mfano, Yesu “atamkomboa maskini anayelilia msaada, pia mwenye kuteseka na yeyote ambaye hana msaidizi. . . . Ataikomboa nafsi yao kutoka katika ukandamizaji na katika jeuri.” (Zaburi 72:12-16) Kupitia Yesu Kristo, Mungu anaahidi kukomesha “vita mpaka kwenye mwisho wa dunia.” (Zaburi 46:9) Anaahidi hivi: “Hakuna mkaaji [wa dunia yake iliyosafishwa] atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’” Vipofu, viziwi, vilema, naam, wote wanaoathiriwa na magonjwa watakuwa na afya kamilifu. (Isaya 33:24; 35:5, 6; Ufunuo 21:3, 4) Hata wale waliokufa karne nyingi zilizopita watafaidika. Mungu anaahidi kuwafufua wale walioathiriwa na ukosefu wa haki na ukandamizaji.—Yohana 5:28, 29.

      Yesu Kristo hataleta mabadiliko nusu-nusu na yasiyodumu. Ataondoa kabisa vizuizi vyote ili kutokeza ulimwengu wenye haki kwelikweli. Ataondoa dhambi na kutokamilika, naye atamharibu Shetani Ibilisi na wote wanaofuata njia zake za uasi. (Ufunuo 19:19, 20; 20:1-3, 10) Taabu na mateso ambayo Mungu ameruhusu kwa muda ‘hayatazuka mara ya pili.’ (Nahumu 1:9) Hilo ndilo Yesu alikuwa akifikiria alipotufundisha kusali Ufalme wa Mungu uje na mapenzi ya Mungu yatendeke “duniani kama ilivyo mbinguni.”—Mathayo 6:10.

      Lakini, huenda ukabisha hivi: ‘Yesu mwenyewe alisema kwamba “maskini watakuwepo sikuzote pamoja nasi.” Je, hilo halimaanishi kwamba sikuzote kutakuwepo na ukosefu wa haki na umaskini?’ (Mathayo 26:11) Naam, ni kweli kwamba Yesu alisema sikuzote kutakuwepo na watu maskini. Hata hivyo, muktadha wa maneno yake, kutia ndani ahadi za Neno la Mungu, huonyesha kwamba alimaanisha maskini watakuwepo sikuzote maadamu mfumo huu wa mambo unaendelea. Alijua kwamba hakuna mwanadamu anayeweza kuondoa umaskini na ukosefu wa haki ulimwenguni. Pia, alijua kwamba angebadili mambo yote hayo. Hivi karibuni, ataleta mfumo wa mambo ulio mpya kabisa, yaani, “mbingu mpya na dunia mpya” ambamo maumivu, magonjwa, umaskini, na kifo vitakoma.—2 Petro 3:13; Ufunuo 21:1.

      “Msisahau Kutenda Mema”

      Je, hilo humaanisha kwamba ni bure kabisa kufanya yote tuwezayo ili kuwasaidia wengine? La hasha. Biblia inatutia moyo tuwasaidie wengine wanapokabili majaribu na hali zenye kutaabisha. Mfalme Sulemani wa kale aliandika hivi: “Usiwanyime watu mema wanayostahili, mkono wako ukiwa na uwezo wa kuyafanya.” (Methali 3:27) Mtume Paulo anatuhimiza: “Msisahau kutenda mema na kushiriki vitu pamoja na wengine.”—Waebrania 13:16.

      Yesu Kristo mwenyewe alitutia moyo kufanya yote tuwezayo ili kuwasaidia wengine. Alieleza mfano wa Msamaria aliyemkuta mtu aliyepigwa na kuibiwa. Yesu alisema kwamba Msamaria huyo, ‘alimsikitikia’ mtu huyo hivi kwamba akatumia vitu vyake ili kufunga majeraha ya mtu huyo aliyepigwa, na kumsaidia kupata nafuu kutokana na shambulizi hilo. (Luka 10:29-37) Ni kweli kwamba Msamaria huyo mwenye huruma hakuubadili ulimwengu, lakini alileta badiliko kubwa katika maisha ya mtu huyo. Tunaweza kutenda vivyo hivyo.

      Hata hivyo, Yesu Kristo anaweza kufanya zaidi kuliko kumsaidia mtu mmoja-mmoja tu. Kwa kweli, yeye anaweza kuleta mabadiliko, naye atafanya hivyo karibuni sana. Atakapoleta mabadiliko hayo, watu wanaoathiriwa leo na hali za ukosefu wa haki wataweza kuboresha maisha yao, nao watafurahia amani na usalama wa kweli.—Zaburi 4:8; 37:10, 11.

      Tunapoendelea kungojea mabadiliko hayo, tusisite kamwe kufanya yote tuwezayo, kiroho na kimwili, ‘kuwatendea mema’ wote wanaoathiriwa na ulimwengu huu usio na haki.—Wagalatia 6:10.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki