Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Philo wa Aleksandria Aeleza Maandiko kwa Kukisia-Kisia
    Mnara wa Mlinzi—2005 | Juni 15
    • Maandishi ya Kale Yapata Maana Mpya

      Kama ilivyokuwa kwa Wayahudi wengi walioishi huko Aleksandria, Kigiriki ndiyo iliyokuwa lugha ya kwanza ya Philo. Hivyo, uchunguzi wake ulitegemea tafsiri ya Septuajinti ya Kigiriki ya Maandiko ya Kiebrania. Alipokuwa akichunguza maandishi ya Septuajinti, alisadikishwa kwamba yalikuwa na mambo ya msingi ya falsafa na kwamba Musa alikuwa “mwanafalsafa stadi.”

      Katika karne za mapema, wasomi Wagiriki hawakuamini hadithi za miungu ya kiume na ya kike, yaani, majitu na mashetani katika hekaya za kale. Walianza kufasiri tena hadithi hizo za kale za Wagiriki. Msomi James Drummond alisema hivi kuhusu njia waliyotumia: “Wanafalsafa walikuwa wakitafuta maana zisizoeleweka za hekaya, na kutokana na mambo ya kuchukiza na ya kipumbavu katika hekaya hizo walikata kauli kwamba waandikaji wake walinuia kuonyesha ukweli fulani wenye kuelimisha kupitia mifano yao yenye kuamsha hisia za kingono.” Philo alijaribu kutumia mbinu hiyo kufasiri Maandiko.

      Kwa mfano, fikiria andiko la Mwanzo 3:22 katika tafsiri ya Bagster ya Septuajinti, ambalo linasema hivi: “Bwana Mungu aliwafanyia Adamu na mke wake mavazi ya ngozi na kuwavika.” Wagiriki walihisi kwamba Mungu Mweza-Yote alijishushia heshima kwa kufanya kazi kama hiyo. Hivyo Philo aliona maana ya mfano katika mstari huo naye akasema: “Mavazi ya ngozi ni usemi wa mfano wa neno ngozi, yaani, mwili wetu; kwa kuwa Mungu aliumba kwanza akili, naye akaiita Adamu; kisha akaumba nguvu zenye msukumo ambazo aliziita Uhai. Mwishowe, alifanya pia mwili ambao aliuita kwa usemi wa mfano, mavazi ya ngozi.” Hivyo Philo akajaribu kufanya tendo la Mungu la kuwavika mavazi Adamu na Hawa kuwa hoja ya kifalsafa iliyopaswa kuchunguzwa.

      Pia fikiria andiko la Mwanzo 2:10-14, ambalo linaeleza kuhusu chanzo cha maji katika bustani ya Edeni. Andiko hilo linataja mito minne ambayo ilibubujika nje ya bustani. Philo alijaribu kutafuta maana ya maneno yanayofafanua bustani ya Edeni. Baada ya kueleza kuhusu nchi yenyewe, alisema hivi: “Huenda masimulizi hayo pia yana maana ya mfano; kwa kuwa mito hiyo minne inawakilisha sifa nne nzuri.” Alikisia kwamba Mto Pishoni unawakilisha busara, Mto Gihoni unamaanisha kuchukua mambo kwa uzito, Mto Tigri unafananisha uvumilivu, nao Mto Efrati unamaanisha haki. Hivyo, kulingana na Philo mito hiyo ni mifano tu (au, sitiari).

      Philo alijaribu kupata maana ya mfano ili kuchanganua masimulizi ya uumbaji, habari kuhusu Kaini kumuua Abeli, Gharika ya siku za Noa, kuvurugwa kwa lugha huko Babeli, na kanuni nyingi za Sheria ya Musa. Kama inavyoonyeshwa na mfano uliotajwa katika fungu lililotangulia, mara nyingi Philo alikubaliana na maana halisi ya andiko la Biblia, kisha akaonyesha jinsi anavyolielewa kwa njia ya mfano kwa kutumia maneno haya: “Labda tunapaswa kufikiria mambo haya kuwa yanazungumzwa kwa njia ya mfano.” Kwa kusikitisha, katika maandishi ya Philo, mifano ndiyo inayokaziwa sana huku maana iliyo wazi ya Maandiko ikipotoshwa.

  • Philo wa Aleksandria Aeleza Maandiko kwa Kukisia-Kisia
    Mnara wa Mlinzi—2005 | Juni 15
    • [Sanduku katika ukurasa wa 12]

      KUFASIRI MIFANO LEO

      Sitiari kwa kawaida ni ‘usemi wa mfano wenye maana ya kuhusianisha kitu kimoja na kingine chenye sifa sawa.’ Inasemekana kwamba maandishi yanayotumia sitiari huwa na mifano inayowakilisha mambo muhimu zaidi ambayo maana yake imefichwa. Kama Philo wa Aleksandria, baadhi ya walimu wa dini wa siku hizi hutumia mifano ili kuifafanua Biblia.

      Fikiria masimulizi ya Mwanzo sura ya 1-11, ambayo yanaeleza historia ya wanadamu tangu uumbaji hadi kutawanywa kwa watu kwenye mnara wa Babeli. Tafsiri ya Kikatoliki ya The New American Bible inasema hivi kuhusu sehemu hiyo ya Biblia: “Ili kufanya ukweli ulio katika sura hizo ueleweke na Waisraeli ambao wangezihifadhi, zilihitaji kuelezwa kwa kutumia mambo yaliyojulikana na watu wa wakati huo. Kwa sababu hiyo, ukweli wenyewe unapaswa kutofautishwa wazi na hadithi zinazoficha maana yake.” Hiyo inamaanisha kwamba maneno ya kitabu cha Mwanzo sura ya 1-11 hayapaswi kuchukuliwa kihalisi. Badala yake, kama vile vazi linavyofunika mwili, ndivyo maneno hayo yanavyofunika maana nzito.

      Hata hivyo, Yesu alifundisha kwamba sura hizo za kwanza za kitabu cha Mwanzo zilikuwa za kweli. (Mathayo 19:4-6; 24:37-39) Mitume Paulo na Petro walifundisha vivyo hivyo. (Matendo 17:24-26; 2 Petro 2:5; 3:6, 7) Wanafunzi wanyoofu wa Biblia wanakataa maelezo ambayo hayapatani na Neno lote la Mungu.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki