-
‘Malaika wa Yehova Anapiga Kambi Pande Zote’Mnara wa Mlinzi—2009 | Machi 15
-
-
Mwaka wa 1956, niliombwa niende kutumika huko Ireland. Nilitumwa pamoja na dada wengine wawili katika mji wa Galway. Siku ya kwanza kabisa, nilimtembelea kasisi fulani. Muda mfupi baadaye, polisi mmoja alifika na kunipeleka mimi na mwenzangu kwenye kituo cha polisi. Tulipomwambia majina yetu na mahali tulipoishi, mara moja alipiga simu. Tulimsikia akisema hivi: “Ndiyo, Kasisi, ninajua vizuri wanakoishi.” Kumbe alikuwa ametumwa na kasisi huyo! Mwenye nyumba tuliyokodi, alishurutishwa atufukuze, kwa hiyo ofisi ya tawi ikapendekeza tutoke katika eneo hilo. Tulifika kwenye kituo cha magari-moshi tukiwa tumechelewa kwa dakika kumi. Lakini bado gari-moshi lilikuwapo, na kulikuwa na mtu fulani aliyekuwa akingoja ili kuhakikisha kwamba tumepanda gari-moshi hilo. Tulikuwa tumekaa Galway kwa majuma matatu tu!
Tulitumwa huko Limerick, mji mwingine ambako Kanisa Katoliki lilikuwa na uvutano mkubwa sana. Kwa kawaida, tulidhihakiwa na umati wa watu. Watu wengi waliogopa kutukaribisha nyumbani mwao. Mwaka uliotangulia ndugu mmoja alikuwa amepigwa katika mji wa karibu wa Cloonlara. Kwa hiyo, tulifurahi kukutana na Christopher, aliyetajwa mwanzoni, ambaye alituomba turudi ili kujibu maswali yake ya Biblia. Tulipokuwa tumemtembelea, kasisi mmoja aliingia na kumwamuru Christopher atufukuze. Alimpinga kasisi huyo kwa kusema hivi: “Niliwaalika wanawake hawa katika nyumba yangu na waligonga mlango kabla ya kuingia. Wewe hukualikwa, wala hukugonga mlango.” Kasisi huyo aliondoka kwa hasira.
Bila sisi kujua, kasisi huyo alikuwa amekusanya kikundi kikubwa cha wanaume, na walikuwa wakitungojea nje ya nyumba ya Christopher. Christopher alijua kwamba walikuwa na hasira sana, hivyo alitenda kama ilivyoelezwa mwanzoni mwa simulizi hili. Alitufanya tukae kwake mpaka walipoondoka. Baadaye tulipata habari kwamba yeye pamoja na familia yake walifukuzwa kutoka katika eneo hilo, kisha wakahamia Uingereza.
-
-
‘Malaika wa Yehova Anapiga Kambi Pande Zote’Mnara wa Mlinzi—2009 | Machi 15
-
-
Ninarudi Ireland
Nilifika Ireland Agosti (Mwezi wa 8) 1959, nikatumwa katika Kutaniko la Dun Laoghaire. Wakati huo, Eric alikuwa amerudi Uingereza na alifurahi sana kwamba nilikuwa karibu naye. Yeye pia alitaka kuwa mmishonari. Aliona kwamba kwa kuwa wamishonari walikuwa wakitumwa Ireland wakati huo, angefanya upainia huko. Alihamia Dun Laoghaire, na tukafunga ndoa mwaka wa 1961.
Miezi sita baadaye, Eric alipata msiba mbaya sana akiendesha pikipiki. Fuvu lake la kichwa lilipasuka, na madaktari hawakuwa na uhakika ikiwa wangeweza kuokoa uhai wake. Baada ya kulazwa hospitalini kwa majuma matatu, nilimtunza akiwa nyumbani kwa miezi mitano mpaka alipopona. Niliendelea na huduma yangu kadiri nilivyoweza.
Mwaka wa 1965, tulitumwa kwenye kutaniko lenye wahubiri wanane huko Sligo, bandari iliyo kwenye pwani ya kaskazini-magharibi. Miaka mitatu baadaye, tulienda kwenye kutaniko lingine dogo huko Londonderry, upande wa juu zaidi wa kaskazini. Siku moja, tulipokuwa tukitoka katika utumishi tulikuta barabara ya kwenda tulikoishi ikiwa imefungwa kwa ua wa seng’enge. Misukosuko ya Ireland Kaskazini ilikuwa imeanza. Magenge ya vijana yalichoma moto magari. Tayari jiji liligawanywa katika maeneo ya Waprotestanti na ya Wakatoliki. Ilikuwa hatari sana kuvuka kutoka eneo moja la jiji kwenda eneo lingine.
Kuishi na Kuhubiri Wakati wa Misukosuko
Hata hivyo, tulihubiri kila mahali. Kwa mara nyingine tena, tulihisi kana kwamba malaika walikuwa wakipiga kambi pande zote kutuzunguka. Tulipojikuta katika maeneo yenye fujo, tuliondoka haraka na kurudi baada ya fujo kutulia. Pindi moja kulipokuwa na fujo karibu na jengo tulimoishi, vitu fulani vililipuka katika duka la karibu la rangi ambalo lilikuwa likichomwa moto, navyo vikaanguka kwenye dirisha letu. Hatukuweza kulala kwa sababu tuliogopa kwamba moto ungeshika jengo tulimoishi. Baada ya kuhamia Belfast mwaka wa 1970, tulipata habari kwamba bomu la petroli lilikuwa limechoma kabisa duka hilo la rangi na jengo tulilokuwa tukiishi ndani yake liliungua kabisa.
Wakati mwingine, nilipokuwa nikihubiri na dada mmoja, tuliona kipande cha bomba cha ajabu-ajabu kwenye kizingiti cha dirisha moja. Tukaendelea kutembea. Punde si punde, kikalipuka. Watu wa mtaa huo walikuja na kufikiri kwamba sisi ndio tuliotega bomu hilo! Dada aliyeishi katika eneo hilo alikuja mara moja na kutuingiza katika nyumba yake. Majirani wake walipoona hilo walitambua kwamba hatukuwa na hatia.
Mwaka wa 1971, tulirudi Londonderry kumtembelea dada mmoja. Tulipokuwa tukimweleza njia tuliyofuata na kizuizi tulichopita njiani, alituuliza, “Hakukuwa na mtu yeyote kwenye kizuizi hicho?” Tuliposema, “Ndiyo walikuwapo, lakini walitupuuza tu,” alishangaa sana. Kwa nini? Kwa sababu siku zilizotangulia gari la polisi na gari la daktari mmoja lilitekwa na kuchomwa moto.
Mwaka wa 1972 tulihamia Cork. Baadaye, tulitumika huko Naas, kisha Arklow. Mwishowe, mwaka wa 1987, tulitumwa Castlebar, ambako tungali mpaka leo. Tukiwa Castlebar tumepata pendeleo kubwa sana la kusaidia kujenga Jumba la Ufalme. Eric alikuwa mgonjwa sana mwaka wa 1999. Hata hivyo, kwa msaada wa Yehova na utegemezo wenye upendo wa kutaniko, nilimtunza tena mpaka alipopona.
Mimi na Eric tumehudhuria Shule ya Utumishi wa Painia mara mbili. Bado anatumika akiwa mzee wa kutaniko. Nina ugonjwa mbaya sana wa baridi yabisi na nyonga zangu na magoti yote mawili yaliondolewa nikawekewa nyonga na magoti bandia. Ingawa nimekabili upinzani mkali wa kidini na nimeishi katika nyakati zenye misukosuko mibaya ya kisiasa na ya kijamii, moja ya matatizo makubwa niliyokabili lilikuwa kuacha kuendesha gari. Hilo lilikuwa jaribu kwa sababu sasa nilikosa uhuru wa kwenda popote pale nilipotaka. Kutaniko limenisaidia sana na kunitegemeza kabisa. Sasa ninaweza kutembea huku na huku kwa fimbo, na ninaenda sehemu za mbali nikitumia pikipiki yenye magurudumu matatu na inayotumia betri.
Mimi na Eric tumetumika tukiwa mapainia wa pekee kwa jumla ya miaka zaidi ya 100, na miaka 98 kati ya miaka hiyo tumetumikia nchini Ireland. Hatutaki kuacha kazi hii eti kwa sababu tumezeeka. Hatutegemei miujiza, lakini tunaamini kwamba malaika wenye nguvu wa Yehova ‘wanapiga kambi pande zote kuwazunguka’ wale wanaomwogopa na kumtumikia kwa uaminifu.
-