-
Mkono wa Yehova WainuliwaUnabii wa Isaya I—Nuru kwa Wanadamu Wote
-
-
26. “Lewiathani” ni nani katika siku ya Isaya na leo pia, na ni nini kinachompata huyu “joka aliye baharini”?
26 Akiutazamia wakati huo, Isaya atabiri: “Katika siku hiyo BWANA, kwa upanga wake ulio mkali, ulio mkubwa, ulio na nguvu, atamwadhibu lewiathani, nyoka yule mwepesi, na lewiathani, nyoka yule mwenye kuzonga-zonga; naye atamwua yule joka aliye baharini.” (Isaya 27:1) Katika utimizo wa kwanza, ‘Lewiathani’ huzirejezea nchi ambako Israeli imetawanyika, kama vile Babiloni, Misri, na Ashuru. Nchi hizo hazitaweza kuzuia kurudi kwa watu wa Yehova kwenye nchi ya kwao wakati ufikapo. Ingawa hivyo, Lewiathani wa leo ni nani? Yaonekana ni Shetani—“nyoka wa awali”—na mfumo wake mwovu wa mambo hapa duniani, ambao ni chombo chake anachotumia kuwapiga Israeli wa kiroho. (Ufunuo 12:9, 10; 13:14, 16, 17; 18:24) “Lewiathani” alipoteza mshiko wake juu ya watu wa Mungu mwaka wa 1919, na hivi karibuni atatoweka kabisa Yehova ‘atakapomwua yule joka aliye baharini.’ Kwa sasa, chochote ambacho huenda ‘Lewiathani’ akajaribu kufanya dhidi ya watu wa Yehova hakitafanikiwa.—Isaya 54:17.
“Shamba la Mizabibu la Mvinyo”
27, 28. (a) Shamba la mizabibu la Yehova limejaza nini duniani kote? (b) Yehova hulilindaje shamba lake la mizabibu?
27 Kwa kutumia wimbo mwingine, Isaya sasa atoa kielezi kizuri kuhusu mazao ya watu wa Yehova walioachiliwa huru: “Katika siku hiyo; Shamba la mizabibu la mvinyo, liimbieni. Mimi, BWANA, nalilinda, nitalitia maji kila dakika, asije mtu akaliharibu; usiku na mchana nitalilinda.” (Isaya 27:2, 3) Mabaki ya Israeli wa kiroho na wenzi wao wanaofanya kazi kwa bidii kwa kweli wameijaza dunia yote kwa mazao ya kiroho. Hiyo ni sababu nzuri kama nini ya kusherehekea na kuimba! Sifa yote yamwendea Yehova, yeye ambaye amelitunza shamba lake la mizabibu kwa upendo.—Linganisha Yohana 15:1-8.
28 Kwa kweli, shangwe imechukua mahali pa hasira ya awali ya Yehova! “Hasira sinayo ndani yangu; kama mibigili na miiba ingekuwa mbele zangu, ningepanga vita juu yake, ningeiteketeza yote pamoja. Au azishike nguvu zangu, afanye amani nami; naam, afanye amani nami.” (Isaya 27:4, 5) Ili kuhakikisha kuwa mizabibu yake yaendelea kuzaa “mvinyo” kwa wingi, Yehova auharibu na kuuteketeza kana kwamba kwa moto, uvutano wowote ulio kama magugu uwezao kuliharibu shamba lake la mizabibu. Kwa hiyo, yeyote asithubutu kuhatarisha hali njema ya kutaniko la Kikristo! Badala yake, wote na ‘wazishike nguvu za Yehova,’ wakitafuta upendeleo na ulinzi wake. Kwa kutenda hivyo, wanafanya amani na Mungu—jambo lililo muhimu sana hivi kwamba Isaya alitaja mara mbili. Matokeo yatakuwaje? “Siku zijazo Yakobo atatia mizizi; Israeli atatoa maua na kuchipuka; nao watajaza uso wa ulimwengu matunda.” (Isaya 27:6)c Kutimizwa kwa mstari huo ni uthibitisho mzuri kama nini wa nguvu za Yehova! Tangu mwaka wa 1919, Wakristo watiwa-mafuta wameijaza dunia kwa “matunda,” yaani, chakula cha kiroho kinachotia nguvu. Matokeo ni kwamba mamilioni ya kondoo wengine wenye uaminifu-mshikamanifu wamejiunga nao, nao kwa pamoja “wanamtolea [Mungu] utumishi mtakatifu mchana na usiku.” (Ufunuo 7:15) Wao hudumisha kwa shangwe viwango vya juu kati ya ulimwengu wenye ufisadi. Yehova naye huendelea kuwabariki kwa kuwapa ongezeko. Na tusilisahau kamwe pendeleo kuu la kuyala “matunda” na kuwagawia wengine kupitia sauti zetu za sifa!
-
-
Mkono wa Yehova WainuliwaUnabii wa Isaya I—Nuru kwa Wanadamu Wote
-
-
[Sanduku katika ukurasa wa 285]
“Tarumbeta Kubwa” Yatangaza Uhuru
Mwaka wa 607 K.W.K., maumivu ya Yuda yaongezeka Yehova alitiapo nidhamu taifa lake lililopotoka kwa kutumia fimbo ya uhamisho. (Soma Isaya 27:7-11.) Dhambi ya taifa hilo ni kubwa sana isiweze kufunikwa kwa dhabihu za wanyama. Basi, kama vile mtu awezavyo kuwatawanya kondoo au mbuzi kwa kutoa ‘sauti ya kushtua’ au awezavyo ‘kuyapepeta’ majani kwa upepo mkali, Yehova afukuza Israeli kutoka katika nchi yao. Baadaye, hata watu walio dhaifu, wafananishwao na wanawake, wanavitumia vitu vibakivyo nchini humo.
Hata hivyo, wakati wa Yehova wa kuwakomboa watu wake kutoka utekwani wafika. Awaweka huru kama vile mkulima awezavyo kuweka huru zeituni zilizofungwa mitini kitamathali. “Itakuwa katika siku hiyo, BWANA atayapiga-piga matunda yake toka gharika ya Mto [Frati] hata kijito cha Misri, nanyi mtakusanywa mmoja mmoja, enyi wana wa Israeli. Tena itakuwa katika siku hiyo, tarumbeta kubwa itapigwa, nao waliokuwa karibu na kuangamia katika nchi ya Ashuru watakuja; na hao waliotupwa katika nchi ya Misri; nao watamsujudu BWANA katika mlima mtakatifu huko Yerusalemu.” (Isaya 27:12, 13) Baada ya ushindi wa Koreshi mwaka wa 539 K.W.K., atoa agizo la kuwekwa huru kwa Wayahudi katika milki yake, inayotia ndani wale walio Ashuru na Misri. (Ezra 1:1-4) Ni kana kwamba “tarumbeta kubwa” ilipigwa, ikitangaza wimbo wa sifa wa uhuru kwa watu wa Mungu.
-