Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Sala ya Toba
    Unabii wa Isaya II—Nuru kwa Wanadamu Wote
    • [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 362]

      Sala ya Danieli ya Toba

      Nabii Danieli aliishi Babiloni kipindi chote cha ile miaka 70 ya utekwa wa Wayahudi. Wakati fulani katika mwaka wa 68 wa uhamisho, Danieli alitambua kutokana na unabii wa Yeremia kwamba muda wa Israeli wa kukaa ugenini ulikuwa ukikaribia kwisha. (Yeremia 25:11; 29:10; Danieli 9:1, 2) Danieli alimgeukia Yehova katika sala—sala ya toba kwa niaba ya taifa zima la Kiyahudi. Danieli anasimulia hivi: “Nikamwelekezea Bwana Mungu uso wangu, ili kutaka kwa maombi, na dua, pamoja na kufunga, na kuvaa nguo za magunia na majivu. Nikamwomba BWANA, Mungu wangu, nikaungama.”—Danieli 9:3, 4.

      Danieli alitamka sala yake miaka mia mbili hivi baada ya Isaya kuiandika sala ya kiunabii inayopatikana katika sura ya 63 na ya 64 ya kitabu chake. Bila shaka, Wayahudi wengi wenye moyo mweupe walimtolea Yehova sala wakati wa ile miaka migumu ya uhamisho. Hata hivyo, Biblia inaikazia fikira sala ya Danieli, ambayo inaonekana kuwa iliwakilisha hisia za Wayahudi wengi waaminifu. Hivyo, sala yake inaonyesha kwamba kwa kweli hisia zinazotajwa katika sala ya kiunabii ya Isaya ndizo zilizokuwa hisia za Wayahudi waaminifu katika Babiloni.

      Angalia mifanano fulani kati ya sala ya Danieli na ya Isaya.

      Isaya 63:16 Danieli 9:15

      Isaya 63:18 Danieli 9:17

      Isaya 64:1-3 Danieli 9:15

      Isaya 64:4-7 Danieli 9:4-7

      Isaya 64:6 Danieli 9:9, 10

      Isaya 64:10, 11 Danieli 9:16-18

  • Sala ya Toba
    Unabii wa Isaya II—Nuru kwa Wanadamu Wote
    • Sasa wakiwa mateka Babiloni, Wayahudi wanalia kwa sauti kubwa kwa sababu ya kukosa tumaini: “Laiti ungepasua mbingu, na kushuka, ili milima iteteme mbele zako; kama vile moto uchomapo vichaka, na moto uchemshapo maji; ili kuwajulisha adui zako jina lako, mataifa wakatetemeke mbele zako!” (Isaya 64:1, 2) Kweli Yehova ana uwezo wa kuokoa. Hakika yeye angaliweza kushuka awapiganie watu wake, ararue-rarue mifumo ya serikali zilizo kama mbingu na kuvunja-vunja milki zilizo kama milima. Yehova angaliweza kulijulisha jina lake kwa kuonyesha bidii yake motomoto kwa niaba ya watu wake.

      7 Yehova alikuwa amefanya mambo ya jinsi hiyo zamani. Isaya anasimulia hivi: “Ulipofanya mambo ya kutisha tusiyoyatazamia, ulishuka, milima ikatetema mbele zako.” (Isaya 64:3) Matendo hayo makuu yanaonyesha uwezo wa Yehova na Uungu wake. Hata hivyo, Wayahudi wasio waaminifu wa wakati wa Isaya hawana haki ya kumtazamia Yehova atende hivyo kwa faida yao.

      Ni Yehova Peke Yake Awezaye Kuokoa

      8. (a) Yehova anatofautiana na miungu ya uwongo ya mataifa kwa njia gani moja? (b) Kwa nini Yehova hachukui hatua kuwaokoa ingawa ana uwezo wa kufanya hivyo? (c) Paulo ananukuu na kutumia Isaya 64:4 kwa njia gani? (Ona sanduku katika ukurasa wa 366.)

      8 Miungu ya uwongo haiwafanyii waabudu wake maajabu yoyote ya wokovu. Isaya anaandika hivi: “Tangu zamani za kale watu hawakusikia, wala kufahamu kwa masikio, wala jicho halikuona Mungu, ila wewe, atendaye mambo kwa ajili yake amngojaye. Wewe wamlaki yeye afurahiaye yaliyo haki na kuyatenda, watu wale wakukumbukao katika njia zako.” (Isaya 64:4, 5a) Ni Yehova peke yake aliye “mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.” (Waebrania 11:6) Yeye huchukua hatua kuwalinda wale wanaotenda uadilifu na wale wanaomkumbuka. (Isaya 30:18) Je, Wayahudi wametenda hivyo? Sivyo. Isaya anamwambia Yehova hivi: “Tazama, ulikuwa na hasira, nasi tulitenda dhambi; tumekuwa katika mambo haya muda mwingi; nasi, je! tutaokolewa?” (Isaya 64:5b) Kwa sababu watu wa Mungu wamekuwa wakizidi tu kufanya dhambi kwa muda mrefu, hakuna msingi wa kumfanya Yehova asitesite kuleta ghadhabu yake ya haki na kuwaletea wokovu.

      9. Wayahudi wenye kutubu wanaweza kutumainia nini, nasi tunaweza kujifunza nini kutokana na jambo hili?

      9 Wayahudi hawawezi kufuta kasoro za wakati uliopita, lakini wakitubu na kurudia ibada safi, wanaweza kutumainia kupata msamaha na baraka za wakati ujao. Yehova atawathawabisha wenye kutubu kwa wakati wake kwa kuwafungua kutoka utekwa wa Babiloni. Lakini bado wanahitaji subira. Ingawa wana toba, Yehova hatabadili wakati aliouweka. Hata hivyo, wakiendelea kuwa macho na waitikie mapenzi ya Yehova, wanahakikishiwa kwamba hatimaye watakombolewa. Vivyo hivyo, Wakristo leo wanamtazamia Yehova kwa subira. (2 Petro 3:11, 12) Sisi tunayatia maanani maneno ya mtume Paulo, aliyesema hivi: “Tusife moyo katika kufanya lililo bora, kwa maana katika majira yapasayo tutavuna ikiwa hatuchoki kabisa.”—Wagalatia 6:9.

      10. Sala ya Isaya inaungama wazi kwamba ni jambo gani lisiloweza kufanyika?

      10 Sala ya Isaya ya kiunabii si ungamo la kidesturi tu kuhusu dhambi. Sala hiyo inaonyesha kwamba anatambua kwa moyo mweupe kuwa taifa lao haliwezi kujiokoa lenyewe. Nabii anasema hivi: “Sisi sote tumekuwa kama mtu aliye mchafu, na matendo yetu yote ya haki yamekuwa kama nguo iliyotiwa unajisi [“vazi la vipindi vya hedhi,” “NW”]; sisi sote twanyauka kama jani, na maovu yetu yatuondoa, kama upepo uondoavyo.” (Isaya 64:6) Kufikia mwishoni mwa uhamisho, huenda ikawa Wayahudi wenye kutubu wameacha uasi-imani. Huenda ikawa wamemgeukia Yehova kwa kufanya matendo ya uadilifu. Lakini bado hawajakamilika. Ingawa mema waliyotenda yanastahili sifa, mema hayo ni sawa tu na mavazi yaliyotiwa unajisi, kwani hayawezi kufunika dhambi. Msamaha wa Yehova ni zawadi isiyostahiliwa, naye huitoa kwa sababu ya rehema yake. Msamaha huo si kitu kinachoweza kuchumwa kama mshahara.—Waroma 3:23, 24.

      11. (a) Wengi wa Wayahudi walioko uhamishoni wana hali gani mbaya ya kiroho, na huenda sababu ikawa ni nini? (b) Ni nani waliokuwa mifano bora ya imani wakati wa uhamisho?

      11 Isaya anaona nini anapotazama kule mbele? Nabii huyo anasali hivi: “Hapana aliitiaye jina lako, ajitahidiye akushike; kwa kuwa umetuficha uso wako, nawe umetukomesha kwa njia ya maovu yetu.” (Isaya 64:7) Hali ya kiroho ya taifa hilo imedidimia chini kabisa. Watu wamekuwa hawaiti jina la Mungu katika sala. Ingawa hawana tena hatia ya dhambi nzito ya kuabudu sanamu, ni wazi kwamba wanapuuza ibada yao, na hakuna ‘ajitahidiye kumshika Yehova.’ Ni wazi kwamba hawana uhusiano mzuri na Muumba wao. Labda wengine wanahisi kuwa hawastahili kusema na Yehova katika sala. Huenda wengine wakaendelea na shughuli zao za kila siku bila kumjali. Bila shaka, miongoni mwa wahamishwa mna watu mmoja-mmoja ambao ni mifano mizuri sana ya imani, kama vile Danieli, Hanania, Mishaeli, Azaria, na Ezekieli. (Waebrania 11:33, 34) Huku kile kipindi cha miaka 70 ya utekwa kikikaribia kumalizika, wanaume kama vile Hagai, Zekaria, Zerubabeli, na Kuhani Mkuu Yoshua wako tayari kuongoza kwa kuliitia jina la Yehova. Na bado, inaonekana kwamba sala ya Isaya ya kiunabii inaeleza jinsi hali ya wahamishwa wengi ilivyo.

      “Kutii Ni Bora Kuliko Dhabihu”

      12. Isaya anaonyeshaje kwamba Wayahudi wenye toba wana nia ya kubadili mwenendo wao?

      12 Wayahudi wenye toba wana nia ya kubadilika. Akiwawakilisha, Isaya anamtolea Yehova sala akisema hivi: “Sasa, Ee BWANA, wewe u baba yetu; sisi tu udongo, nawe u mfinyanzi wetu; sisi sote tu kazi ya mikono yako.” (Isaya 64:8) Maneno haya yanakiri tena kwamba Yehova ndiye mwenye mamlaka ya kuwa Baba, au Mpaji wa Uhai. (Ayubu 10:9) Wayahudi wanaotubu wanalinganishwa na udongo unaoweza kufinyangwa uwe na umbo lolote lile. Kwa njia ya mfano, wale wanaoitikia nidhamu ya Yehova wanaweza kupewa umbo au muundo unaopatana na viwango vya Mungu. Lakini inaweza kuwa hivyo iwapo tu Yehova, aliye Mfinyanzi, atawasamehe. Ndiyo maana Isaya anamsihi mara mbili akumbuke kwamba Wayahudi ni watu wake: “Ee BWANA, usione hasira nyingi, wala usiukumbuke uovu siku zote; tazama, angalia, twakusihi, sisi sote tu watu wako.”—Isaya 64:9.

      13. Watu wa Mungu wanapokuwa uhamishoni, nchi ya Israeli ina hali gani?

      13 Wakati wa uhamisho, Wayahudi wanavumilia mengi licha ya kuwa mateka tu katika nchi ya kipagani. Ukiwa wa Yerusalemu na hekalu lake unawaletea suto wao na Mungu wao. Sala ya toba ya Isaya inasimulia baadhi ya mambo yanayosababisha suto hilo: “Miji yako mitakatifu imekuwa jangwa, Sayuni umekuwa jangwa, Yerusalemu umekuwa ukiwa. Nyumba yetu takatifu, nzuri, walimokusifu baba zetu, imeteketea moto; vitu vyetu vyote vyenye kupendeza vimeharibika.”—Isaya 64:10, 11.

      14. (a) Yehova alionyaje kuhusu hali iliyopo sasa? (b) Ingawa Yehova alilifurahia sana hekalu lake na dhabihu zilizotolewa humo, jambo la maana zaidi ni nini?

      14 Bila shaka Yehova anajua sana jinsi mambo yalivyo katika nchi ya babu za Wayahudi hawa. Karibu miaka 420 kabla ya uharibifu wa Yerusalemu, yeye aliwaonya watu wake kwamba wakiziacha amri zake na kutumikia miungu mingine, ‘angewakatilia mbali na uso wa nchi,’ kisha lile hekalu zuri ‘liwe marundo ya magofu.’ (1 Wafalme 9:6-9, NW) Ni kweli kwamba Yehova alifurahia nchi aliyokuwa amewapa watu wake, hekalu tukufu lililojengwa kwa heshima yake, na dhabihu zilizotolewa kwake. Lakini uaminifu-mshikamanifu na utii ni mambo ya maana kuliko vitu vya kimwili, hata kuliko dhabihu. Kwa kufaa, nabii Samweli alimwambia hivi Mfalme Sauli: “Je! BWANA huzipenda sadaka za kuteketezwa na dhabihu sawasawa na kuitii sauti ya BWANA? Angalia, kutii ni bora kuliko dhabihu, na kusikia kuliko mafuta ya beberu.”—1 Samweli 15:22.

      15. (a) Isaya anamsihi Yehova jinsi gani kwa njia ya unabii, na anajibiwaje? (b) Ni matukio gani ambayo hatimaye yalifanya Yehova alikatae taifa zima la Israeli?

      15 Hata hivyo, je! kweli Mungu wa Israeli anaweza kuyatazama mabaya yanayowapata watu wake wenye toba bila kuguswa na huruma? Isaya anamalizia sala yake ya kiunabii kwa swali hilo. Anasihi hivi kwa niaba ya Wayahudi wahamishwa: “Utajizuia usiyaangalie mambo haya, Ee BWANA? utanyamaza, na kututesa sana?” (Isaya 64:12) Mwishowe, kwa kweli Yehova anawasamehe watu wake, na katika mwaka wa 537 K.W.K., anawarudisha kwenye nchi yao waweze kuanza tena ibada safi huko. (Yoeli 2:13) Hata hivyo, jiji la Yerusalemu na hekalu lake liliharibiwa tena karne nyingi baadaye, na hatimaye Mungu akalikataa taifa la agano lake. Kwa nini? Kwa sababu watu wa Yehova walikuwa wamepeperuka wakaziacha amri zake na kumkataa Mesiya. (Yohana 1:11; 3:19, 20) Hilo lilipotukia, Yehova alianzisha taifa jipya lichukue mahali pa Israeli. Hilo lilikuwa taifa la kiroho, yaani, “Israeli wa Mungu.”—Wagalatia 6:16; 1 Petro 2:9.

      Yehova, “Msikiaji wa Sala”

      16. Biblia inafundisha nini kuhusu msamaha wa Yehova?

      16 Kuna masomo muhimu ya kujifunza kutokana na yaliyopata Israeli. Tunaona kwamba Yehova ‘yu mwema na huwa tayari kusamehe.’ (Zaburi 86:5) Sisi hutegemea rehema na msamaha wake ili tuweze kupata wokovu, kwani sisi ni viumbe wasio wakamilifu. Hata tufanye nini, hatuwezi kupata baraka hizo kwa jitihada zetu wenyewe kana kwamba tunachuma mshahara. Ingawa hivyo, Yehova hatoi msamaha kiholela. Wale tu wanaotubu dhambi zao na kugeuka kabisa ndio wanaoweza kutazamia kupata msamaha wa Mungu.—Matendo 3:19.

      17, 18. (a) Tunajuaje kwamba Yehova anapendezwa na mawazo na hisia zetu kwa njia ya kweli? (b) Kwa nini Yehova anatumia subira kuelekea wanadamu wenye dhambi?

      17 Pia tunajifunza kwamba Yehova anapendezwa sana na mawazo na hisia zetu tunapozitaja katika sala. Yeye ndiye “Msikiaji wa sala.” (Zaburi 65:2, 3, NW ) Mtume Petro anatuhakikishia hivi: “Macho ya Yehova yako juu ya waadilifu, na masikio yake yaelekea dua zao.” (1 Petro 3:12) Zaidi ya hilo, tunajifunza kwamba sala ya toba ni lazima iwe pia na ungamo la dhambi lenye unyenyekevu. (Mithali 28:13) Lakini, hiyo haimaanishi kwamba tunaweza kuichezea rehema ya Mungu. Biblia inaonya Wakristo ‘wasiipokee fadhili isiyostahiliwa ya Mungu na kukosa kusudi lake.’—2 Wakorintho 6:1.

      18 Mwisho, tunajifunza kusudi la subira ambayo Mungu aliwaonyesha watu wake wenye dhambi. Mtume Petro alieleza kwamba Yehova ni mwenye subira “kwa sababu hataki yeyote aangamizwe bali hutaka wote wafikie toba.” (2 Petro 3:9) Hata hivyo, wale wanaozidi kuitumia vibaya subira ya Mungu wataadhibiwa hatimaye. Tunasoma hivi kuhusu jambo hilo: “[Yehova] atamlipa kila mmoja kulingana na kazi zake: uhai udumuo milele kwa wale wanaotafuta sana utukufu na heshima na kutofisidika kwa kuvumilia katika kazi iliyo njema; hata hivyo, kwa wale wenye ugomvi na wale wasioitii kweli bali hutii ukosefu wa uadilifu kutakuwa na hasira ya kisasi na hasira.”—Waroma 2:6-8.

      19. Sikuzote Yehova ataonyesha sifa gani zisizobadilika?

      19 Hivyo ndivyo Mungu alivyoshughulika na Israeli wa kale. Uhusiano wetu na Yehova leo unasimamiwa na kanuni hizo hizo kwa sababu yeye si kigeugeu. Ingawa Yehova hasiti-siti kutoa adhabu inayostahiliwa, sikuzote atakuwa “BWANA, Mungu mwingi wa huruma, mwenye fadhili, si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema na kweli; mwenye kuwaonea huruma watu elfu elfu, mwenye kusamehe uovu na makosa na dhambi.”—Kutoka 34:6, 7.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki