-
Mambo Ambayo Mungu Aliahidi Kupitia ManabiiImani ya Kweli—Siri ya Kuwa na Maisha Yenye Furaha
-
-
Sehemu ya 7
Mambo Ambayo Mungu Aliahidi Kupitia Manabii
MANABII wa kale walimwamini Mungu. Waliamini ahadi zake na kuishi kulingana nazo. Ahadi hizo zilitia ndani nini?
Mara baada ya Adamu na Hawa kuasi katika Edeni, Mungu aliahidi kwamba angemchagua mtu ambaye angeponda kichwa cha “nyoka” anayewakilisha “yule nyoka wa zamani, yeye anayeitwa Ibilisi na Shetani,” na kumharibu milele. (Mwanzo 3:14, 15; Ufunuo 12:9, 12) Mtu huyo angethibitika kuwa nani?
Miaka 2,000 baada ya kutoa unabii huo, Yehova alimwahidi nabii Abrahamu kwamba Yule Anayekuja angetokana na uzao wake. Mungu alimwambia Abrahamu: “Kupitia kwa uzao wako mataifa yote ya dunia hakika yatajibariki kwa sababu wewe umeisikiliza sauti yangu.”—Mwanzo 22:18.
Mnamo 1473 K.W.K., Mungu alimpa nabii Musa habari zaidi kuhusu “uzao” huo. Musa aliwaambia wana wa Israeli: “Nabii kutoka katikati yako mwenyewe, kutoka kwa ndugu zako, kama mimi, ndiye ambaye Yehova Mungu wako atakuinulia—ninyi mnapaswa kumsikiliza yeye.” (Kumbukumbu la Torati 18:15) Kama Musa, nabii huyo anayekuja angetoka miongoni mwa wana wa Abrahamu.
Pia, nabii huyo angekuwa mzao wa Mfalme Daudi naye angekuwa mfalme mkuu. Mungu alimwahidi Mfalme Daudi: ‘Nitainua uzao wako baada yako, ambao utatoka ndani ya viuno vyako; nami kwa kweli nitaufanya imara ufalme wake.’ (2 Samweli 7:12, 13) Mungu pia alifunua kwamba mzao huyo wa Daudi ataitwa “Mkuu wa Amani,” akaongeza: “Hakutakuwa na mwisho kwa habari ya wingi wa huo utawala wa kifalme na kwa amani, juu ya kiti cha ufalme cha Daudi na juu ya ufalme wake ili kuufanya imara na kuutegemeza kwa njia ya haki na kwa njia ya uadilifu, kuanzia sasa na kuendelea mpaka wakati usio na kipimo.” (Isaya 9:6, 7) Ndiyo, Kiongozi huyo mwadilifu atairudisha amani na haki ulimwenguni pote. Lakini angetokea wakati gani?
“Uzao” ulioahidiwa . . . ungetokana na uzao wa Abrahamu, ungekuwa nabii kama Musa, ungetokana na ukoo wa Daudi, ungetokea mwaka wa 29 W. K., ungemponda nyoka, Shetani
Baadaye malaika Gabrieli alimwambia hivi nabii wa Mungu, Danieli: “Nawe ujue na ufahamu kwamba tangu kutolewa kwa lile neno la kurudisha na kujenga upya Yerusalemu mpaka Masihi aliye Kiongozi, kutakuwa na majuma 7, pia majuma 62.” (Danieli 9:25) Hayo yalikuwa majuma 69 ya miaka—kila juma likiwa na miaka 7—ambayo jumla yake ni miaka 483. Ilianza mwaka wa 455 K.W.K. mpaka mwaka wa 29 W.K.a
Je, kweli Masihi, nabii aliye kama Musa na ambaye ni “uzao” uliosubiriwa kwa muda mrefu, alikuja mwaka wa 29 W.K.? Acheni tuone.
-
-
Masihi AtokeaImani ya Kweli—Siri ya Kuwa na Maisha Yenye Furaha
-
-
Sehemu ya 8
Masihi Atokea
MIAKA zaidi ya 500 baada ya Danieli kutoa unabii, malaika wa Mungu, Gabrieli alimtokea msichana bikira aitwaye Maria, mzao wa Mfalme Daudi. Gabrieli akamwambia, “Siku njema, uliyependelewa sana, Yehova yuko pamoja nawe.” (Luka 1:28) Hata hivyo, Maria aliogopa. Salamu ya Gabrieli ilikuwa na maana gani?
Gabrieli alimwambia Maria kwamba atamzaa Masihi
Gabrieli akaeleza: “Usiogope, Maria, kwa maana umepata kibali cha Mungu; na, tazama! utachukua mimba katika tumbo lako la uzazi na kuzaa mwana, nawe utamwita jina lake Yesu, Yehova Mungu atampa kiti cha ufalme cha Daudi baba yake, na . . . ufalme wake hautakuwa na mwisho.” (Luka 1:30-33) Hiyo ilikuwa habari njema kama nini! Maria angemzaa Masihi, “uzao” uliosubiriwa sana!
Mwaka uliofuata, Yesu alizaliwa Bethlehemu. Usiku huo, malaika aliwatangazia hivi wachungaji: “Tazama! ninawatangazia ninyi habari njema ya shangwe kubwa . . . kwa sababu leo katika jiji la Daudi, Mwokozi ambaye ni Kristo Bwana, amezaliwa kwenu.” (Luka 2:10, 11) Baadaye, familia ya Yesu ilihamia Nazareti, ambako alikulia.
Mnamo mwaka wa 29 W.K.—mwaka hususa ambao Masihi alitazamiwa kutokea—Yesu alianza kutumikia akiwa nabii wa Mungu, akiwa “na umri wa karibu miaka 30.” (Luka 3:23) Watu wengi wakaja kutambua kwamba alikuwa ametumwa na Mungu. Wakasema: “Nabii mkuu ameinuliwa katikati yetu.” (Luka 7:16, 17) Hata hivyo, Yesu alifundisha nini?
Yesu aliwafundisha watu kumpenda na kumwabudu Mungu: Alisema: “Yehova Mungu wetu ni Yehova mmoja, nawe lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote na kwa nguvu zako zote.” (Marko 12:29, 30) Pia, alisema: “Yehova Mungu wako ndiye unayepaswa kumwabudu, na yeye peke yake ndiye unayepaswa kumtolea utumishi mtakatifu.”—Luka 4:8.
Yesu aliwahimiza watu wapendane: Alisema: “Mpende jirani yako kama wewe mwenyewe.” (Marko 12:31) Pia alisema: “Mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima mwatendee wao pia vivyo hivyo; hii, kwa kweli, ndiyo maana ya Sheria na Manabii.”—Mathayo 7:12.
Yesu alikuwa na bidii ya kuwatangazia wengine Ufalme wa Mungu: Alisema, “Ni lazima nitangaze habari njema ya ufalme wa Mungu, kwa sababu nilitumwa kufanya hivyo.” (Luka 4:43) Kwa nini Ufalme wa Mungu ni wa maana sana?
Maandiko yanafundisha kwamba Ufalme wa Mungu ni serikali ya mbinguni itakayoitawala dunia. Yesu, yule Masihi, ndiye ambaye Mungu amemteua kuwa Mfalme. Katika maono, nabii Danieli aliona mapema Mungu akimkabidhi Masihi “utawala na heshima na ufalme,” mbinguni. (Danieli 7:14) Ufalme huo utaifanya dunia yote kuwa Paradiso na kuwapa watumishi wa Mungu zawadi ya uzima wa milele. Je, hizo si habari njema?
-
-
Kujifunza Kutoka kwa Masihi KiongoziImani ya Kweli—Siri ya Kuwa na Maisha Yenye Furaha
-
-
Sehemu ya 9
Kujifunza Kutoka kwa Masihi Kiongozi
MUNGU alitabiri kwamba atamweka rasmi Masihi kuwa Kiongozi wa watu wote. Mungu anajua ni kiongozi wa aina gani tunayehitaji naye alimchagua Kiongozi bora zaidi. Masihi alithibitika kuwa Kiongozi wa aina gani? Jenerali mwenye nguvu? Mwanasiasa mwenye ustadi? Mwanafalsafa mwenye hekima? Kulingana na Maandiko Matakatifu, Masihi alikuwa nabii Yesu Kristo aliyekuwa tofauti na wengine wote.—Mathayo 23:10.
Mungu alihakikisha kwamba Yesu alizaliwa akiwa mkamilifu na mtakatifu. Zaidi ya hayo, Yesu alishinda jitihada zote za Shetani za kutaka kumpotosha. Kwa maneno na matendo, Yesu alionyesha kikamilifu jinsi ambavyo Mungu hutumia nguvu zake na vilevile haki, hekima, na upendo. Ona jinsi tunavyoweza kujifunza kutokana na mfano wa Yesu.
Yesu alipenda sana kuwasaidia wengine
Yesu alitumia nguvu alizopewa na Mungu ili kuwasaidia wengine. Yesu aliwajali watu kwelikweli, naye alitumia nguvu zake kwa ukarimu kutosheleza mahitaji yao. Alisema, “Ninausikitikia umati, kwa sababu . . . hawana chakula.” (Marko 8:2) Kisha kimuujiza, Yesu akaulisha umati mkubwa wa watu waliokuja kumsikiliza akifundisha.
Yesu pia alisafiri sana, akifundisha na “kuponya kila namna ya ugonjwa na kila namna ya udhaifu katikati ya watu.” (Mathayo 4:23) Haishangazi kwamba umati wa watu ulimfuata, na “umati wote ulikuwa ukitafuta kumgusa, kwa sababu nguvu zilikuwa zikimtoka na kuwaponya wote.” (Luka 6:19) Bila shaka, Yesu alikuja, “si kuhudumiwa, bali kuhudumu na kutoa nafsi yake kuwa fidia badala ya wengi.” (Mathayo 20:28)a Ni viongozi wangapi wa kibinadamu wanaoonyesha roho hiyo ya kujidhabihu?
Yesu aliwapenda watoto
Yesu alionyesha haki ya Mungu. Yesu alifuata maagizo yote ya sheria ya Mungu na kuishi kulingana na kanuni zinazopatikana katika sheria hiyo. Kama Maandiko yalivyotabiri, ni kana kwamba Yesu alikuwa akisema, “Ee Mungu wangu, nimependezwa na kufanya mapenzi yako, na sheria yako imo ndani yangu.” (Zaburi 40:8) Yesu aliwatendea wote—matajiri kwa maskini, wanaume kwa wanawake, watoto kwa watu wazima—kwa adabu, heshima, na bila ubaguzi, kama afanyavyo Mungu. Wakati fulani wanafunzi wa Yesu waliwakemea wazazi waliokuwa wakiwaleta watoto kwa Yesu. Lakini Yesu akawaambia: “Waacheni watoto wachanga waje kwangu; msijaribu kuwazuia, kwa maana ufalme wa Mungu ni wa wale walio kama hao.”—Marko 10:14.
Yesu alionyesha hekima ya Mungu. Yesu aliwaelewa watu vizuri. “Yeye mwenyewe alijua kile kilichokuwa ndani ya mwanadamu.” (Yohana 2:25) Maadui wa Yesu walipotuma watu wamkamate, watu hao walikiri: “Mtu mwingine hajapata kamwe kusema kama huyu.” Yesu alipata wapi hekima yake? Alieleza hivi: “Yale ninayofundisha si yangu, bali ni yake yeye aliyenituma.”—Yohana 7:16, 46.
Yesu aliwahurumia na kuwaponya wagonjwa
Yesu alionyesha upendo wa Mungu. Pia, Yesu aliwahurumia watu. Mwanamume mmoja aliyekuwa ‘amejaa ukoma’ alimwomba: “Bwana, ikiwa tu unataka, unaweza kunitakasa.” Akimsikitikia, Yesu “akaunyoosha mkono wake, akamgusa, na kusema: ‘Ninataka. Takasika.’ Na mara moja ule ukoma ukamtoka.” (Luka 5:12, 13; Marko 1:41, 42) Kwa kweli Yesu alitaka sana kumwondolea maumivu mtu huyo aliyekuwa akiteseka.
Je, Yesu anakujali wewe pia? Yesu mwenyewe ajibu: “Njooni kwangu, nyote mnaotaabika na kulemewa na mizigo, nami nitawaburudisha ninyi. Chukueni nira yangu na mjifunze kutoka kwangu, kwa maana mimi ni mwenye tabia-pole na mnyenyekevu moyoni, nanyi mtapata burudisho kwa ajili ya nafsi zenu.”—Mathayo 11:28, 29.
Yesu ndiye Kiongozi bora tunayeweza kupata. Hivyo basi anatuhimiza: ‘Jifunzeni kutoka kwangu.’ Je, utaukubali mwaliko wake wenye kugusa moyo? Ukifanya hivyo utakuwa na maisha yenye furaha.
-