Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Je, Wakati Ujao Wetu Umeandikwa Kimbele?
    Mnara wa Mlinzi—1998 | Aprili 15
    • Je, Wakati Ujao Wetu Umeandikwa Kimbele?

      MKRISTO, Mwislamu, Myahudi, Mhindu, au mwamini wa dini nyingineyo—watu wa imani zote hupatwa na msiba na kuhuzunika juu yake.

      Kwa mfano, Desemba 6, 1997, msiba mbaya sana ulitokea katika jiji la Siberia la Irkutsk. Ndege kubwa mno aina ya AN-124 ya usafirishaji ilikuwa imetoka tu kuruka wakati ambapo injini zake mbili zilishindwa kufanya kazi. Hiyo ndege, ikiwa imejazwa mafuta, iliangukia majengo ya makazi. Vyumba kadhaa vilifunikwa kwa moto, ukisababisha vifo na majeraha kwa wakaaji wengi wasioweza kujikinga, kutia na watoto wasio na hatia.

      Katika hilo eneo la Siberia ambako aksidenti hiyo ilitokea, yaelekea kuna watu wenye maoni ya kidini yanayotofautiana. Huenda baadhi yao wakaonyesha itikadi katika Ukristo, lakini bado wangeweza kufikiri kwamba huo msiba ulitokana na ajali. Huenda wao na wengine wakahisi, ‘Yalikuwa mapenzi ya Mungu, na ikiwa waliouawa hawangekufa kwa njia hiyo, wangekufa kwa njia nyingine—hawangeiepuka ajali hiyo.’

      Kufikiri kama huko, kuwe ni kwa kusema au kwa kimyakimya, hudhihirisha fikra ambayo ni ya kawaida katika dini nyingi tufeni pote—ajali. Watu wengi huamini kwamba, kwa njia fulani wakati ujao wetu umeandikwa kimbele, tangu siku ya kuzaliwa kwetu hadi siku ya kufa kwetu.

      Itikadi katika ajali hutofautiana, ikifanya iwe vigumu kuwa na ufafanuzi wenye kutia ndani maana zote. Kimsingi ajali hutokeza wazo la kwamba kila kitu kitukiacho, kila tendo, kila tukio—liwe jema au baya—haliepukiki; limekusudiwa kutukia kwa sababu limeamuliwa kimbele na kani ya juu zaidi, ipitayo uwezo wa mwanadamu. Fikra kama hiyo yaweza kupatikana katika unajimu, Uhindu, na karma ya Ubudha, na vilevile katika fundisho la Jumuiya ya Wakristo la kuamuliwa kimbele yatakayompata mtu. Huko nyuma katika Babilonia ya kale, watu waliamini kwamba miungu walidhibiti ajali na wakati ujao kupitia hati iliyoandikwa. Yadhaniwa kwamba, mungu yeyote aliyedhibiti “mabamba [hayo] ya mambo yaliyokusudiwa kimbele” angeweza kuamua ajali ambazo zingepata wanadamu, falme, na hata hiyo miungu yenyewe.

      Waumini wengi huamini kwamba, kupitia agizo la kimungu kabla ya kuzaliwa kwa wanadamu, Mungu huamua yote yatakayowapata watu, kutia na urefu wa maisha yao, iwe watakuwa wanaume au wanawake, tajiri au maskini, wenye furaha au wasio na furaha. Hayo yote husemekana kuwako katika akili ya Mungu au kuandikwa katika kitabu kabla ya tukio kutokea. Kwa hiyo afa litokeapo, ni jambo la kawaida kwa mwamini kusema “mektoub,”—imeandikwa! Yawaziwa kwamba kwa kuwa Mungu ajua kila kitu kimbele, lazima pia aamue ni nani atakayemtii na ni nani atakayekosa kumtii. Hivyo wafuasi wengi huamini kwamba hata kabla mtu hajazaliwa, Mungu tayari ameamua kama amekusudiwa raha idumuyo milele katika Paradiso au kama atapokea hukumu idumuyo milele.

      Huenda ukahisi kwamba hilo lasikika kuwa sawa kabisa na lile fundisho la kuamuliwa kimbele yatakayompata mtu, ambalo hufundishwa katika makanisa fulani ya Jumuiya ya Wakristo. Mtetezi mashuhuri wa fundisho la kuamuliwa kimbele yatakayompata mtu alikuwa Mleta-Mabadiliko Mfaransa, John Calvin, aliyekuwa Mprotestanti. Alifasili fundisho hilo la kuamuliwa kimbele yatakayompata mtu kuwa “agizo la milele la Mungu, ambalo kwalo Mungu aliamua kile alichotaka kufanyia kila mwanadamu. Si wote waumbwao katika hali moja, lakini uhai wa milele umeamuliwa kimbele kwa watu fulani na hukumu ya milele kwa wengine.” Calvin alisisitiza hivi: “Mungu aliona kimbele kutumbukia katika dhambi kwa mwanadamu wa kwanza, na ndani yake akaona kuangamizwa kwa wazao wake; lakini pia kwa kutaka, akapanga iwe hivyo.”

      Hata hivyo, si washiriki wote wa dini ambazo hufundisha juu ya kuamuliwa kimbele yatakayompata mtu au nadhariajali ambao kibinafsi, huamini hayo. Baadhi yao hutoa hoja kwa usahihi kwamba, maandishi ya kidini hutaja hiari ya mwanadamu. Kwa kweli, kumekuwa na ubishi mkubwa juu ya vitendo vya kibinadamu, viwe vyatokana na kuchagua kwa hiari kwa kibinadamu au vimeamuliwa kimbele na Mungu. Kwa mfano, wengine wamebisha kwamba ni lazima mwanadamu awe na hiari ya kuchagua na ya kutenda, kwa kuwa Mungu mwenye haki, humwajibisha mwanadamu kutoa hesabu kwa matendo yake. Wengine wamesema kwamba Mungu hutokeza matendo ya mwanadamu lakini kwa njia fulani mwanadamu “hujipatia” matendo hayo na kuwa mwenye daraka kuyahusu. Hata hivyo, kwa ujumla wengi huamini kwamba kila tukio katika maisha yetu ya kila siku, liwe kubwa au dogo, limeagizwa na Mungu.

      Je, wewe waamini nini? Je, Mungu tayari ameamua wakati ujao wako utakuwaje? Je, wanadamu kwa kweli wana hiari, uwezo wa kuchagua kihalisi juu ya wakati ujao wao? Je, ni kwa kadiri gani mwisho wetu hutegemea matendo yetu? Makala inayofuata itajaribu kutoa majibu kwa maswali hayo.

  • Wakati Ujao Wako Utakuwaje?
    Mnara wa Mlinzi—1998 | Aprili 15
    • Wakati Ujao Wako Utakuwaje?

      IKIWA Mungu Mweza Yote ni mwenye kujua yote, akijua yote yaliyopita, yaliyopo, na yajayo, je, mambo yote hayakusudiwi kutukia sawasawa kabisa na vile ambavyo Mungu ameyaona kimbele? Ikiwa Mungu ameona kimbele na kuagiza kimbele mwendo na mwisho wa kila binadamu, je, yaweza kusemwa kikweli kwamba tuna hiari ya kuchagua mwendo wa maisha yetu, wakati ujao wetu?

      Maswali hayo yamejadiliwa kwa karne nyingi. Huo ubishi bado wagawanya dini zilizo kubwa. Je, uwezo wa Mungu wa kujua kimbele wakati ujao waweza kupatanishwa na hiari ya kibinadamu? Twapaswa kutafuta majibu wapi?

      Mamilioni ya watu tufeni pote wangekubali kwamba Mungu amewasiliana na wanadamu kupitia Neno lake lililoandikwa kama lilivyotolewa kupitia wasemaji wake, manabii. Kwa mfano, Qurani hurejezea mafunuo haya kuwa yalitoka kwa Mungu: Taurāh (Torati, Sheria, au vitabu vitano vya Musa), Zabūr (Zaburi), na Injīl (Gospeli, Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, au “Agano Jipya”), na vilevile yale yaliyofunuliwa kwa manabii wa Israeli.

      Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, twasoma hivi: “Andiko lote limepuliziwa na Mungu na ni lenye manufaa kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo.” (2 Timotheo 3:16) Kwa wazi, mwongozo au mnurusho wowote ambao sisi hupokea wapaswa kimsingi utoke kwa Mungu mwenyewe. Basi je, halingekuwa jambo la hekima kuchunguza maandishi ya manabii wa zamani wa Mungu? Hayo hufunua nini juu ya wakati ujao wetu?

      Wakati Ujao Ulioandikwa Kimbele

      Yeyote ambaye ameyasoma Maandiko Matakatifu ajua kwamba, kihalisi yana mamia ya unabii mbalimbali. Matukio ya kihistoria kama vile kuanguka kwa Babiloni, kujengwa upya kwa Yerusalemu (karne ya sita hadi ya tano K.W.K.), kuinuka na kuanguka kwa wafalme wa kale wa Umedi na Uajemi na wa Ugiriki, kulitabiriwa kinaganaga. (Isaya 13:17-19; 44:24–45:1; Danieli 8:1-7, 20-22) Kutimizwa kwa unabii huo mbalimbali ni mojawapo ya ithibati yenye nguvu zaidi kwamba, Maandiko Matakatifu kwa kweli ni Neno la Mungu, kwa maana Mungu peke yake ndiye aliye na uwezo wa kuona kimbele na kuamua yatakayotukia wakati ujao. Katika maana hiyo Maandiko Matakatifu kwa kweli yamerekodi wakati ujao ulioandikwa kimbele.

      Mungu mwenyewe ajulisha wazi hivi: “Mimi ni Mungu, wala hapana mwingine; mimi ni Mungu, wala hapana aliye kama mimi; nitangazaye mwisho tangu mwanzo, na tangu zamani za kale mambo yasiyotendeka bado; nikisema, Shauri langu litasimama, nami nitatenda mapenzi yangu yote . . . naam, nimenena, nami nitatekeleza; nimekusudia, nami nitafanya.” (Isaya 46:9-11; 55:10, 11) Jina lenyewe ambalo kwalo Mungu alijitambulisha kwa manabii wa kale ni Yehova, ambalo kihalisi lamaanisha “Yeye Husababisha Iwe.”a (Mwanzo 12:7, 8; Kutoka 3:13-15; Zaburi 83:18) Mungu hujifunua mwenyewe kuwa Ndiye ambaye huwa Mtimizaji wa neno lake, Yule ambaye hutimiza makusudi yake.

      Kwa hiyo, Mungu hutumia nguvu yake ya ujuzi wa kimbele katika kutimiza makusudi yake. Mara nyingi ameitumia ili kuwaonya waovu juu ya hukumu yake inayokuja na vilevile kutolea watumishi wake tumaini la wokovu. Lakini je, Mungu hutumia nguvu hiyo katika njia isiyo na mipaka? Je, kuna uthibitisho wowote katika Maandiko Matakatifu wa mambo ambayo Mungu amechagua kutoyajua kimbele?

      Je, Mungu Hujua Kimbele Kila Kitu?

      Majibizano yote ya kuunga mkono fundisho la kuamuliwa kimbele yatakayompata mtu, hutegemea ile dhana kwamba, kwa kuwa kwa wazi Mungu ana nguvu ya kujua kimbele na kuamua matukio ya wakati ujao, ni lazima ajue kila kitu, kutia na matendo ya wakati ujao ya kila mtu. Hata hivyo, je, dhana hiyo ni sahihi? Yale afunuayo Mungu katika Maandiko Matakatifu huonyesha jambo tofauti.

      Kwa mfano, Maandiko husema kwamba ‘Mungu alimjaribu Abrahamu’ kwa kumwamuru amdhabihu mwana wake Isaka akiwa toleo la kuteketezwa. Abrahamu alipokuwa karibu kumdhabihu Isaka, Mungu alimzuia na kusema hivi: ‘Sasa ninajua ya kuwa unamcha Mungu, iwapo hukunizuilia mwanao, mwanao wa pekee.’ (Mwanzo 22:1-12) Je, Mungu angekuwa ametoa taarifa hiyo ikiwa alijua kimbele kwamba Abrahamu angeitii amri hiyo? Je, hilo lingekuwa jaribu la haki?

      Zaidi ya hayo, manabii wa kale huripoti kwamba Mungu alijisema kwa kurudia-rudia kuwa ‘anajutia’ jambo fulani alilokuwa amelifanya au alilokuwa akifikiri kulifanya. Kwa mfano, Mungu alisema kwamba ‘alijuta [neno litokanalo na lile la Kiebrania, na·chamʹ] kwa sababu alimtawaza Sauli awe mfalme juu ya Israeli.’ (1 Samweli 15:11, 35; linganisha Yeremia 18:7-10; Yona 3:10.) Kwa sababu Mungu ni mkamilifu, mistari hiyo haiwezi kumaanisha kwamba Mungu alifanya kosa katika kumchagua Sauli awe mfalme wa kwanza wa Israeli. Badala ya hivyo, ni lazima ionyeshe kwamba Mungu alisikitika kwamba Sauli alikuja kukosa imani na utii. Kutumia kwa Mungu usemi kama huo kujirejezea kungekuwa jambo la upuuzi ikiwa alikuwa amejua kimbele matendo ya Sauli.

      Usemi huohuo waonekana katika Maandiko ya kale zaidi ambako, katika kuzirejezea siku za Noa, yasema hivi: ‘BWANA akajuta kwa kuwa amemfanya mwanadamu duniani, akahuzunika moyo. BWANA akasema hivi, Nitamfutilia mbali mwanadamu niliyemwumba usoni pa nchi; kwa maana najuta ya kwamba nimemwumba.’ (Mwanzo 6:6, 7) Hilo laonyesha kwa mara nyingine tena kwamba, matendo ya mwanadamu hayaamuliwi kimbele na Mungu. Mungu alijuta, akahuzunika, na hata akaumia kwa sababu uovu wa mwanadamu ulipata kuwa mwingi. Muumba alijuta ya kwamba ilikuwa imekuwa lazima awaharibu wanadamu wote ila Noa na familia yake. Mungu hutuhakikishia hivi: ‘Sikufurahii kufa kwake mtu mwovu.’—Ezekieli 33:11; linganisha Kumbukumbu la Torati 32:4, 5.

      Kwa hiyo, je, Mungu alijua kimbele na hata kuagiza kimbele kutumbukia kwa Adamu katika dhambi, na vilevile matokeo yenye maafa ambayo jambo hilo lingeiletea familia ya kibinadamu? Yale ambayo tumechunguza yaonyesha kwamba hilo haliwezi kuwa kweli. Na zaidi, ikiwa Mungu alijua kimbele hayo yote, angalipata kuwa chanzo cha dhambi alipomwumba mwanadamu, na ndiye huwaletea wanadamu uovu kimakusudi na pia kuteseka kwote. Kwa wazi, jambo hilo haliwezi kupatanishwa na yale Mungu hufunua juu yake mwenyewe katika Maandiko. Yeye ni Mungu mwenye upendo na haki, achukiaye uovu.—Zaburi 33:5; Mithali 15:9; 1 Yohana 4:8.

      Miisho Miwili ya Mwanadamu

      Maandiko Matakatifu hayafunui kwamba, wakati ujao wa kila mmoja wetu kwa njia fulani umeamuliwa kimbele na Mungu. Badala yake, yale ambayo Maandiko hufunua ni kwamba, Mungu ametabiri miisho miwili tu ambayo yawezekana kwa mwanadamu. Mungu humpa kila mwanadamu hiari ya kuchagua utakaokuwa mwisho wake. Nabii Musa aliwajulisha Waisraeli wazi hivi: ‘Nimekuwekea mbele yako uhai na kifo basi chagua uhai ili uwe hai, wewe na uzao wako; kumpenda BWANA, Mungu wako, kuitii sauti yake, na kushikamana naye; kwani hiyo ndiyo uhai wako, na wingi wa siku zako.’ (Kumbukumbu la Torati 30:19, 20) Nabii wa Mungu, Yesu, alionya kimbele hivi: “Ingieni kupitia lango jembamba; kwa sababu ni pana na yenye nafasi barabara inayoongoza kuingia katika uharibifu, na wengi ndio wanaoingia kupitia hiyo; lakini lango ni jembamba na barabara ni yenye kufinyana inayoongoza kuingia katika uhai, na wachache ndio wanaoipata.” (Mathayo 7:13, 14) Barabara mbili, miisho miwili. Wakati ujao wetu hutegemea matendo yetu. Kumtii Mungu humaanisha uhai, ilhali kutomtii humaanisha kifo.—Waroma 6:23.

      Mungu “anaambia wanadamu kwamba wapaswa wote kila mahali kutubu. Kwa sababu ameweka siku ambayo katika hiyo akusudia kuihukumu kwa uadilifu dunia inayokaliwa.” (Matendo 17:30, 31) Kama vile walio wengi wa wanadamu katika siku ya Noa walivyochagua kutomtii Mungu, wakaharibiwa, ndivyo walio wengi leo huchagua kutotii amri za Mungu. Hata hivyo, Mungu hajaamua tayari ni nani watakaoharibiwa na ni nani watakaopata wokovu. Kwa kweli, Neno la Mungu husema kwamba “hataki yeyote aangamizwe bali hutaka wote wafikie toba.” (2 Petro 3:9) Hata walio waovu sana waweza kutubu, kuwa watiifu, na kufanya mabadiliko yaliyo ya lazima ili kupata upendeleo wa Mungu.—Isaya 1:18-20; 55:6, 7; Ezekieli 33:14-16; Waroma 2:4-8.

      Kwa wale watiifu, Mungu aahidi uhai udumuo milele katika paradiso yenye amani, dunia ambayo imesafishwa uovu wote, jeuri, na vita, ulimwengu ambako hakutakuwa na njaa, kuteseka, ugonjwa, na kifo. (Zaburi 37:9-11; 46:9; Isaya 2:4; 11:6-9; 25:6-8; 35:5, 6; Ufunuo 21:4) Hata wafu watafufuliwa na kupewa fursa ya kumtumikia Mungu.—Danieli 12:2; Yohana 5:28, 29.

      “Umwangalie sana mtu mkamilifu, umtazame mtu mnyofu,” asema mtunga-zaburi, “maana mwisho wake mtu huyo ni amani. Wakosaji wataangamizwa pamoja, wasio haki mwisho wao wataharibiwa.” (Zaburi 37:37, 38) Je, wakati ujao wako utakuwaje? Ni juu yako kuamua. Wachapishaji wa gazeti hili watafurahia kukutolea habari zaidi ili ikusaidie kujihakikishia wakati ujao wenye furaha na amani.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki