-
Endelea Kumngojea YehovaUnabii wa Isaya I—Nuru kwa Wanadamu Wote
-
-
[Picha katika ukurasa wa 305]
Katika siku ya Musa, Waisraeli waliponyoka kutoka Misri. Katika siku ya Isaya, Yuda yaenda Misri kutafuta msaada
-
-
Endelea Kumngojea YehovaUnabii wa Isaya I—Nuru kwa Wanadamu Wote
-
-
Upumbavu na Kuelekea Msiba
3. Yehova afichua njama gani?
3 Kwa muda fulani, viongozi wa Yuda wamekuwa wakipanga njama kisiri ya kutafuta njia ya kuepuka kuwa chini ya nira ya Ashuru. Hata hivyo, Yehova amekuwa akiwatazama. Sasa aifichua njama yao: “Ole wa watoto waasi; asema BWANA; watakao mashauri lakini hawayataki kwangu mimi; wajifunikao kifuniko lakini si cha roho yangu; wapate kuongeza dhambi juu ya dhambi; waendao kutelemkia Misri.”—Isaya 30:1, 2a.
4. Watu wa Mungu walio waasi wameifanyaje Misri kuwa badala ya Mungu?
4 Viongozi wanaopanga njama washtuka kama nini wasikiapo njama yao ikifichuliwa! Kusafiri hadi Misri ili kufanya mwungano nayo, mbali na kuwa uchokozi dhidi ya Ashuru, ni uasi dhidi ya Yehova Mungu. Wakati wa Mfalme Daudi, taifa hilo lilimtegemea Yehova kama ngome nalo likakimbilia ‘uvuli wa mbawa zake.’ (Zaburi 27:1; 36:7) Sasa ‘wanajitia nguvu kwa nguvu za Farao’ na “kutumainia kivuli cha Misri.” (Isaya 30:2b) Wameifanya Misri kuwa badala ya Mungu! Huo ni uhaini ulioje!—Soma Isaya 30:3-5.
5, 6. (a) Kwa nini kuungana na Misri ni kosa lenye kusababisha kifo? (b) Ni safari gani ya mapema waliyofunga watu wa Mungu ikaziayo upumbavu wa safari hii ya kwenda Misri?
5 Isaya atoa habari zaidi, kana kwamba anajibu wazo lolote la kwamba safari hiyo ya Misri ni ya matembezi tu. “Ufunuo juu ya hayawani wa Negebu. Katikati ya nchi ya taabu na dhiki, ambayo hutoka huko simba jike na simba, nyoka na joka la moto arukaye, huchukua mali zao mabegani mwa punda wachanga, na hazina zao juu ya nundu za ngamia.” (Isaya 30:6a) Ni wazi kwamba safari hiyo imepangwa vema. Wajumbe wapanga msafara wa ngamia na punda, wakiwapakia bidhaa zenye bei ghali na kusafiri hadi Misri kupitia nyika yenye ukiwa iliyojaa simba wanaonguruma na nyoka wenye sumu. Hatimaye, wajumbe wafika waendako na kukabidhi Wamisri hazina zao. Wanadhani kwamba sasa wamejinunulia ulinzi. Hata hivyo, Yehova asema: “Waende kwa watu ambao hawatawafaa kitu. Kwa maana Misri huwasaidia bure, bila faida; kwa hiyo nimemwita, Rahabu aketiye kimya.” (Isaya 30:6b, 7) “Rahabu,” “yule joka,” alifananisha Misri. (Isaya 51:9, 10) Huahidi kila kitu lakini haifanyi lolote. Mwungano kati yake na Yuda ni kosa lenye kusababisha kifo.
6 Isaya afafanuapo safari ya wajumbe hao, huenda watu wanaomsikiliza wakakumbuka safari kama hiyo iliyofanywa siku za Musa. Baba zao wa zamani walitembea katika ‘jangwa hilo kubwa lenye kitisho.’ (Kumbukumbu la Torati 8:14-16) Ingawa hivyo, katika siku ya Musa, Waisraeli walikuwa wakisafiri kutoka Misri na kutoka utumwani. Mara hii wajumbe wanasafiri kwenda Misri na kuingia utumwani hasa. Huo ni upumbavu ulioje! Tusifanye kamwe uamuzi usio wa busara kama huo kwa kubadili uhuru wetu wa kiroho kwa utumwa!—Linganisha Wagalatia 5:1.
Ujumbe wa Nabii Wapingwa
7. Kwa nini Yehova amwambia Isaya aandike onyo Lake kwa Yuda?
7 Yehova amwambia Isaya aandike ujumbe ambao ameutangaza kitambo kidogo ili ‘uwe kwa ajili ya majira yatakayokuja, kwa ushuhuda hata milele.’ (Isaya 30:8) Ni lazima katazo la Yehova dhidi ya kukazia miungano na wanadamu kuliko kumtegemea Yeye lirekodiwe kwa faida ya vizazi vya baadaye—kutia ndani sisi. (2 Petro 3:1-4) Lakini kuna uhitaji wa haraka zaidi wa rekodi iliyoandikwa. “Watu hawa ni watu waasi, watoto wasemao uongo, watoto wasiotaka kuisikia sheria ya BWANA.” (Isaya 30:9) Watu wamekataa shauri la Mungu. Basi, ni lazima iandikwe ili wasikane baadaye kwamba hawakupokea onyo linalofaa.—Mithali 28:9; Isaya 8:1, 2.
8, 9. (a) Viongozi wa Yuda wajaribuje kuwaharibu manabii wa Yehova? (b) Isaya aonyeshaje kwamba hatatishika?
8 Isaya sasa atoa kielelezo cha mtazamo wa uasi wa watu hao. “[Wamewaambia] waonaji, Msione; na manabii, Msitoe unabii wa mambo ya haki, tuambieni maneno laini, hubirini maneno yadanganyayo.” (Isaya 30:10) Kwa kuwaamuru manabii waaminifu wakome kusema mambo ya “haki,” au ya kweli, na badala yake waseme mambo “laini” na “yadanganyayo,” au yasiyo ya kweli, viongozi wa Yuda waonyesha kuwa wanataka masikio yao yatekenywe. Wanataka kusifiwa, wala si kuhukumiwa. Kwa maoni yao, nabii yeyote asiyetaka kutoa unabii unaowapendeza apaswa ‘kutoka katika njia, ageuke kutoka katika mapito.’ (Isaya 30:11a) Aidha, apaswa kusema mambo yanayopendeza masikio au akome kabisa kuhubiri!
9 Wapinzani wa Isaya wasisitiza: “Mkomesheni Mtakatifu wa Israeli mbele yetu.” (Isaya 30:11b) Isaya na akome kusema katika jina la Yehova, “Mtakatifu wa Israeli”! Jina hilo la cheo lawaudhi hasa kwa sababu viwango vya juu vya Yehova hufichua hali yao mbaya. Isaya atendaje? Yeye atangaza: “Mtakatifu wa Israeli asema hivi.” (Isaya 30:12a) Isaya asema pasipo kusita maneno yaleyale ambayo wapinzani wake wachukia kusikia. Hatatishika. Hicho ni kielelezo kizuri kama nini kwetu! Ni sharti Wakristo wasilegeze kamwe msimamo wao kuhusu kutangaza ujumbe wa Mungu. (Matendo 5:27-29) Sawa na Isaya, wao huendelea kutangaza: ‘Yehova amesema hivi’!
Matokeo ya Uasi
10, 11. Uasi wa Yuda utakuwa na matokeo gani?
10 Yuda imekataa neno la Mungu, ikauamini uwongo, na kuutumainia “ukaidi.” (Isaya 30:12b) Matokeo yatakuwa nini? Badala ya Yehova kuachilia hali kama ilivyo, atalikomesha taifa hilo! Hayo yatatendeka ghafula na kwa ukamilifu, kama Isaya anavyokazia kwa kutumia kielezi. Uasi wa taifa hilo ni kama “mahali palipobomoka, palipo tayari kuanguka patokezapo katika ukuta mrefu, ambapo kuvunjika kwake huja ghafula kwa mara moja.” (Isaya 30:13) Kama vile uvimbe unaozidi kutokeza katika ukuta mrefu usababishavyo hatimaye kuanguka kwa ukuta, ndivyo uasi wa watu wa siku ya Isaya unaozidi kuongezeka utakavyosababisha kuanguka kwa taifa hilo.
11 Kwa kutumia kielezi kingine, Isaya aonyesha ukamilifu wa uharibifu unaokuja: “Atapavunja kama chombo cha mfinyanzi kivunjwavyo, akikivunja-vunja asiache kukivunja, hata hakipatikani katika vipande vyake kigae kitoshacho kutwaa moto jikoni, au kuteka maji kisimani.” (Isaya 30:14) Uharibifu wa Yuda utakuwa kamili sana kiasi cha kutobaki kitu chochote chenye faida—hata kigae kikubwa vya kutosha kutwaa majivu-moto jikoni au kuteka maji kisimani hakitabaki. Kikomo hicho chaaibisha kama nini! Vivyo hivyo, uharibifu unaokuja wa watu wanaoasi dhidi ya ibada ya kweli leo utakuwa wa ghafula na kamili.—Waebrania 6:4-8; 2 Petro 2:1.
Msaada wa Yehova Wakataliwa
12. Watu wa Yuda waweza kuepukaje uharibifu?
12 Ijapokuwa hivyo, watu wanaomsikiliza Isaya waweza kuepuka uharibifu huo. Kuna njia ya kuponyokea. Nabii aeleza: “Bwana MUNGU, Mtakatifu wa Israeli, asema hivi, Kwa kurudi na kustarehe mtaokolewa; nguvu zenu zitakuwa katika kutulia na kutumaini.” (Isaya 30:15a) Yehova yuko tayari kuwaokoa watu wake—iwapo waonyesha imani kwa “kustarehe,” au kwa kukoma kujaribu kupata wokovu kupitia miungano ya kibinadamu, na kwa “kutulia,” au kwa kuonyesha tumaini katika nguvu za ulinzi za Mungu kwa kutoogopa. “Lakini,” Isaya awaambia watu hao, “hamkukubali.”—Isaya 30:15b.
13. Viongozi wa Yuda watumaini nini, na je, tumaini hilo lastahili?
13 Kisha Isaya afafanua: “Bali ninyi mlisema, La! maana tutakimbia juu ya farasi; basi, ni kweli, mtakimbia; tena, Sisi tutakimbia juu ya wanyama waendao upesi; basi, wale watakaowafuatia watakuwa wepesi.” (Isaya 30:16) Wayudea wanadhani kwamba farasi wenye mbio, badala ya Yehova, ndio watakaowaokoa. (Kumbukumbu la Torati 17:16; Mithali 21:31) Hata hivyo, nabii ajibu kwamba tumaini lao litakuwa ndoto kwa sababu adui zao watawapita. Hata wingi hautawafaidi kitu. “Elfu moja watakimbia kwa kukemewa na mtu mmoja; kwa kukemewa na watano mtakimbia.” (Isaya 30:17a) Majeshi ya Yuda yatajawa na hofu na kukimbia kwa kukemewa na adui wachache tu.a Mwishowe, ni mabaki tu watakaoachwa, wakiwa peke yao, “kama mlingoti juu ya kilele cha mlima, na kama bendera juu ya kilima.” (Isaya 30:17b) Kupatana na unabii huo, jiji la Yerusalemu linapoharibiwa mwaka wa 607 K.W.K., ni mabaki tu wanaosalia.—Yeremia 25:8-11.
-