-
Gideoni na Wanaume Wake 300Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia
-
-
HADITHI YA 52
Gideoni na Wanaume Wake 300
UNAONA yanayofanyika hapa? Wote hao ni wanajeshi wa Israeli. Wanaume hao wanaoinama wanakunywa maji. Mwamuzi Gideoni ndiye anayesimama karibu yao. Anatazama wanavyokunywa maji.
Ebu watazame sana wanaume hao wanavyokunywa kwa namna tofauti. Wengine wanatia uso wao karibu na maji. Lakini mmoja anachota maji kwa mkono wake, ili aone yanayotendeka karibu yake. Hilo ni la maana, kwa kuwa Yehova alimwambia Gideoni achague wanaume wale tu walio macho wanapokunywa. Wengine, Mungu akasema, warudishwe nyumbani. Ebu tuone sababu.
Tena Waisraeli wanapata taabu nyingi. Wamekataa kumtii Yehova. Wamidiani wamewazidi nguvu na wanawaumiza. Basi Waisraeli hao wanamlilia Yehova awasaidie. Yehova asikia vilio vyao.
Yehova anamwambia Gideoni atayarishe jeshi. Basi Gideoni akusanya wanajeshi 32,000. Lakini wanajeshi wanaopigana na Israeli ni 135,000. Hata hivyo Yehova anamwambia Gideoni hivi: ‘Una wanajeshi wengi mno.’ Kwa nini Yehova alisema hivyo?
Kwa sababu Waisraeli wakishinda, labda watadhani wameshinda kwa uwezo wao. Labda watadhani hawakutaka Yehova awasaidie washinde. Basi Yehova anamwambia Gideoni hivi: ‘Waambie wanaume wote ambao ni waoga warudi nyumbani.’ Gideoni anapofanya hivyo, wanajeshi 22,000 wanarudi nyumbani. Wanabaki wanajeshi 10,000 wa kupigana na askari wote 135,000.
Lakini, sikiliza! Yehova anasema: ‘Bado una wanajeshi wengi mno.’ Basi anamwambia Gideoni awanyweshe maji penye mto huu na kuwarudisha wote wale wanaoinamisha uso wao karibu na maji wanywe. ‘Nitakupa ushindi kwa wanaume hawa 300 ambao wamekuwa macho walipokunywa maji,’ asema Yehova.
Wakati wa vita wafika. Gideoni anagawa wanaume wake 300 kuwa vikundi vitatu. Anampa kila mwanamume tarumbeta, na mtungi ulio na mwenge ndani. Kama usiku wa manane hivi, wote wanaizunguka kambi ya askari maadui. Kisha, wakati ule ule, wote wazipiga tarumbeta zao na kuivunja mitungi yao, wakipiga kelele hivi: ‘Upanga wa Yehova na wa Gideoni!’ Askari maadui wanapoamka, wanatatizwa na kuogopa. Wote wanaanza kukimbia, na Waisraeli wanashinda.
-
-
Ahadi ya YefthaKitabu Changu cha Hadithi za Biblia
-
-
HADITHI YA 53
Ahadi ya Yeftha
UMEPATA kutoa zawadi ukaona vigumu kuitimiza? Mwanamume katika picha hii, alitoa ahadi, ndiyo sababu ana huzuni sana. Huyo ni Yeftha, mwamuzi hodari wa Israeli.
Yeftha anakaa wakati Waisraeli hawamwabudu Yehova tena. Wanafanya mabaya tena. Yehova anaruhusu Waamoni wawaumize. Hilo lawafanya Waisraeli wamlilie Yehova hivi: ‘Tumekukosea. Tafadhali, utuokoe!’
Watu wanatubu mabaya waliyofanya. Wanaonyesha kutubu kwao kwa kumwabudu Yehova tena. Yehova anawasaidia tena.
Yeftha anachaguliwa na watu akapigane na Waamoni wabaya. Yeftha anataka sana Yehova amsaidie vitani. Basi anamwahidi Yehova hivi: ‘Ikiwa utanisaidia nishinde Waamoni, mtu wa kwanza kutoka nyumbani mwangu kuja kunilaki nirudipo nitakupa huyo.’
Yehova anasikiliza ahadi ya Yeftha, naye anamsaidia kushinda. Yeftha anaporudi nyumbani, unajua nani wa kwanza kutoka amlaki? Ni binti yake, mtoto wake mmoja tu. ‘O-o, binti yangu!’ Yeftha analia. ‘Unanihuzunisha sana. Lakini nimemwahidi Yehova, siwezi kuvunja ahadi hiyo.’
Binti Yeftha anapojua ahadi ya baba yake, kwanza anahuzunika. Maana ataacha baba na rafiki zake. Lakini atatumia maisha yake akimtumikia Yehova katika hema yake huko Shilo. Basi anamwambia baba yake hivi: ‘Ikiwa umemwahidi Yehova, timiza.’
Basi binti Yeftha aenda Shilo, na anamtumikia Yehova maisha yake yote katika hekalu lake. Kila mwaka wanawake wa Israeli wanamtembelea huko siku nne, na kufurahi pamoja. Watu wanampenda binti Yeftha kwa sababu ni mtumishi mzuri wa Yehova.
-
-
Mwanamume Mwenye Nguvu Kuliko WoteKitabu Changu cha Hadithi za Biblia
-
-
HADITHI YA 54
Mwanamume Mwenye Nguvu Kuliko Wote
UNAJUA jina la mwanamume mwenye nguvu kuliko wote? Ni mwamuzi Samsoni. Yehova anampa Samsoni nguvu hizo. Hata kabla ya Samsoni kuzaliwa, Yehova anamwambia mama yake hivi: ‘Upesi utazaa mwana. Ataongoza kuokoa Israeli kutokana na Wafilisti.’
Wafilisti ni watu wabaya wanaoishi Kanaani. Wana wanajeshi wengi, na wanawaumiza Waisraeli sana. Wakati mmoja, Samsoni anapokwenda kwa Wafilisti, simba mkubwa anatokea akinguruma kukutana naye. Lakini Samsoni anamwua simba huyo kwa mikono yake tu. Pia anaua mamia ya Wafilisti wabaya.
Baadaye Samsoni anapendana na mwanamke, Delila. Viongozi Wafilisti wanaahidi kwamba kila mmoja wao atampa Delila vipande 1,100 vya fedha akiwaambia kinachompa Samsoni nguvu nyingi hivyo. Delila anataka fedha zote hizo. Yeye si rafiki wa kweli wa Samsoni, wala wa watu wa Mungu. Anazidi kumwuliza Samsoni kinachompa nguvu nyingi hivyo.
Mwishowe, Delila amshawishi Samsoni. Naye Samsoni anamwambia siri ya nguvu zake, akisema: ‘Mimi sijanyolewa nywele. Tangu kuzaliwa kwangu, Mungu alinichagua niwe mtumishi wake wa pekee, yaani, Mnadhiri. Nikinyolewa nywele, nitapoteza nguvu.’
Delila anapojua hayo, anamlaza Samsoni katika paja lake. Kisha amwita mtu aje amnyoe nywele. Samsoni anapoamka, anakuta amepoteza nguvu. Ndipo Wafilisti wanakuja kumkamata. Wanamwondoa macho yake mawili, na kumfanya mtumwa wao.
Siku moja Wafilisti wanafanya karamu kubwa ili waabudu Dagoni mungu wao. Wanamtoa Samsoni gerezani ili wamcheke. Wakati huo, nywele za Samsoni zimekua tena. Samsoni anamwambia kijana anayemwongoza kwa mkono: ‘Acha nishike nguzo za jengo hili.’ Kisha Samsoni anamwomba Yehova ampe nguvu, naye anashika nguzo hizo. Anapaza sauti hivi: ‘Acha nife pamoja na Wafilisti.’ Wafilisti wanaokula karamu ni 3,000. Samsoni anapoegemea nguzo hizo, jengo laanguka na kuua watu wote hao wabaya.
-
-
Mvulana Mdogo Anamtumikia MunguKitabu Changu cha Hadithi za Biblia
-
-
HADITHI YA 55
Mvulana Mdogo Anamtumikia Mungu
JE! HUYU si kivulana mzuri? Jina lake ni Samweli. Na mwanamume anayeweka mkono wake juu ya kichwa cha Samweli ni Eli, kuhani mkuu wa Israeli. Yule ni Elkana, baba ya Samweli, Hana mama yake wanaompeleka Samweli kwa Eli.
Samweli ana miaka minne au mitano tu. Lakini atakaa katika hema ya Yehova pamoja na Eli na makuhani wengine. Kwa nini Elkana na Hana wanamtoa Samweli mtoto amtumikie Yehova hemani? Ebu tuone.
Miaka michache kabla ya hayo, Hana huyo alihuzunika sana. Hakuweza kuzaa mtoto, naye alitaka mtoto sana sana. Basi siku moja Hana alipotembelea hema ya Yehova, alisali hivi: ‘Ee Yehova, usinisahau mimi! Ukinipa mwana, nakuahidi kukupa huyo akutumikie maisha yake yote.’
Yehova akajibu sala ya Hana, na baada ya miezi fulani akamzaa Samweli. Hana akampenda kivulana wake, akaanza kumfundisha habari za Yehova akiwa bado mdogo sana. Akamwambia mumewe hivi: ‘Upesi Samweli akiisha kuacha kunyonya, nitampeleka hemani akamtumikie Yehova huko.’
Ndivyo tunavyoona Hana na Elkana wakifanya katika picha hii. Na kwa vile Samweli amefundishwa vizuri na wazazi wake, anafurahia kumtumikia Yehova katika hema ya Yehova. Kila mwaka Hana na Elkana wanakuja kuabudu katika hema hii ya pekee, na kumtembelea kivulana wao mdogo. Na kila mwaka Hana anamletea Samweli vazi jipya ambalo amemshonea.
Miaka inapita, na Samweli anazidi kutumikia katika hema ya Yehova. Yehova na watu wanampenda. Lakini Hofni na Finehasi, wana wa Eli kuhani mkuu si wazuri. Wanafanya mabaya mengi, wanazuia wengine pia kumtii Yehova. Ingempasa Eli awaondoe katika ukuhani, lakini hawaondoi.
Kijana Samweli hakubali kuacha kumtumikia Yehova kwa sababu ya mabaya yanayoendelea hemani. Lakini kwa vile watu wachache sana ndio wanaompenda Yehova, Yehova ameacha kusema na mwanadamu yeyote. Inakuwa hivi wakati Samweli anapokuwa mkubwa kidogo:
Samweli amelala hemani anapoamshwa na sauti. Anajibu hivi: ‘Mimi hapa.’ Anaamka na kumkimbilia Eli, akisema: ‘Uliniita, nimekuja.’
Lakini Eli anajibu: ‘Sikukuita; nenda kalale.’ Samweli anarudi kulala.
Tena anaitwa mara ya pili: ‘Samweli!’ Samweli anaamka na kumkimbilia Eli tena. ‘Uliniita, nimekuja,’ asema. Lakini Eli anamjibu: ‘Sikukuita, mwanangu. Kalale tena.’ Samueli arudi kulala.
‘Samweli!’ sauti yaita mara ya tatu. Samweli amkimbilia Eli. ‘Nimekuja, maana umeniita sasa,’ anasema. Sasa Eli anajua kwamba ni Yehova anayeita. Amwambia Samweli hivi: ‘Nenda kalale tena, na akiita tena, useme: “Sema, Yehova, maana mtumishi wako anasikiliza.”’
Ndivyo Samweli anasema Yehova anapoita tena. Kisha Yehova amwambia Samweli kwamba ataadhibu Eli na wanawe. Baadaye Hofni na Finehasi wanakufa katika kupigana na Wafilisti, Eli anaposikia yaliyotokea anaanguka, anavunja shingo yake na kufa pia. Neno la Yehova latimia.
Samweli anakuwa mkubwa, na kuwa mwamuzi wa mwisho wa Israeli. Anapozeeka, watu wanamwomba hivi: ‘Chagua mfalme wa kututawala sisi.’ Samweli hataki kufanya hivyo, kwa kuwa Yehova ndiye mfalme wao. Lakini Yehova anamwambia asikilize watu hao.
-