-
Mfalme Daudi na MuzikiMnara wa Mlinzi—2009 | Desemba 1
-
-
Muziki Katika Israeli la Kale
Unapotamka maneno ya wimbo fulani, mara moja unakumbuka jinsi muziki huo unavyoimbwa. Biblia ina maneno ya nyimbo mbalimbali, ingawa haijulikani jinsi nyimbo hizo zilivyokuwa zikiimbwa. Lazima ziwe zilikuwa zenye kupendeza, na zenye kuchochea. Ubora wa kishairi ulio kwenye Zaburi unaonyesha kuwa muziki wake ulikuwa maridadi sana.
Biblia inaeleza mambo machache sana kuhusu ala za muziki zilizotumiwa. (Ona sanduku lenye kichwa “Ala za Muziki Zilizotumiwa Nyakati za Biblia.”) Hata haijulikani Daudi alitumia kinubi cha aina gani. Lakini, ni muhimu kutambua kwamba Waisraeli walivumbua ala kadhaa za muziki, kama vile vinubi vya mbao vyenye thamani sana ambavyo havikupatikana kwa urahisi.—2 Mambo ya Nyakati 9:11; Amosi 6:5.
Hata hivyo, jambo moja ni hakika. Muziki ulikuwa na sehemu muhimu katika ya maisha ya Waisraeli, hasa katika ibada yao kwa Mungu. Muziki ulichezwa wakati wa kutawazwa kwa wafalme, katika sherehe za kidini, na pia wakati wa vita. Muziki ulichezwa katika makao ya kifalme, ulifanya sherehe za arusi au mikusanyiko ya kifamilia iwe yenye furaha, na kufanya sherehe za mavuno ya zabibu na nafaka kuwa zenye kuvutia. Kwa kusikitisha, muziki ulihusianishwa pia na maeneo yenye sifa mbaya. Mwishowe, mtu alipokufa muziki uliwaliwaza waliofiwa.
Katika Israeli muziki ulikuwa na fungu lingine. Muziki ulikuwa na uwezo wa kusisimua akili na kuwafanya manabii wapate maono. Elisha aliposikia sauti ya kinanda alipokea maagizo kutoka kwa Yehova. (2 Wafalme 3:15) Muziki ulitumiwa pia kutangaza matukio muhimu. Mwezi mpya na sherehe zote zilitangazwa kwa tarumbeta mbili za fedha. Siku ya Yubile, baragumu ilitangaza kuwekwa huru kwa watumwa na kurudishwa kwa mashamba na nyumba zilizokuwa zimechukuliwa. Lazima maskini wawe walifurahi sana kusikia muziki uliotangaza kurudishwa kwa mali na uhuru wao!—Mambo ya Walawi 25:9; Hesabu 10:10.
Huenda Waisraeli fulani walikuwa wanamuziki wazuri. Kulingana na mchongo wa Kiashuru, Mfalme Senakeribu alimwambia Mfalme Hezekia amlipe wanamuziki wa kiume na wa kike kama ushuru. Inaonekana kuwa walikuwa waimbaji stadi sana. Lakini Daudi alikuwa mmoja kati ya waimbaji wenye ujuzi mwingi sana.
-
-
Mfalme Daudi na MuzikiMnara wa Mlinzi—2009 | Desemba 1
-
-
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 28]
Ala za Muziki Zilizotumiwa Nyakati za Biblia
Vinanda vilivyotengenezwa kwa kutumia nyuzi vilitia ndani udi, kinubi, na kinanda cha nyuzi kumi. (Zaburi 92:3) Vinanda hivi viliundwa ili viweze kutoa sauti inayopatana na Alamothi na Sheminithi, maneno ambayo huenda yalitumiwa kuashiria alama nane za muziki za juu au za chini. (1 Mambo ya Nyakati 15:20, 21) Kati ya vyombo vilivyotengenezwa kwa shaba na pia vyombo vya kupulizwa kulikuwa na zumari, filimbi, baragumu, na pia tarumbeta, ‘zilizopigwa kwa sauti kubwa.’ (2 Mambo ya Nyakati 7:6; 1 Samweli 10:5; Zaburi 150:3, 4) Wakati wa kuwekwa wakfu kwa hekalu, ‘sauti moja ilisikika’ kutoka kwa tarumbeta na waimbaji. (2 Mambo ya Nyakati 5:12, 13) Huenda hili lilimaanisha kuwa waliimba kwa upatano na pia hakukuwa na migongano ya sauti. Ala zinazotoa sauti zinapogongwa zilitia ndani matari na matasa, na pia “namna zote za vyombo vya mbao za mberoshi.” Pia kulikuwa na matoazi—madogo-madogo yanayotoa “sauti tamu” na makubwa yanayoitwa “matoazi ya kugonganishwa.”—2 Samweli 6:5; Zaburi 150:5
[Picha]
Juu: Michoro kwenye Tao la Tito, huko Roma, Italia, ikionyesha tarumbeta zilizotolewa katika hekalu la Yerusalemu mwaka wa 70 W.K. Sarafu za mwaka wa 130 W.K., zikionyesha ala za muziki za Wayahudi
[Hisani]
Coins: © 2007 by David Hendin. All rights reserved.
-