-
Hukumu ya Yehova Itakuja Juu ya WaovuMnara wa Mlinzi—2004 | Novemba 15
-
-
11-13. Amosi alitoa unabii hasa juu ya taifa gani, na kulikuwa na ukandamizaji wa aina gani huko?
11 Nabii Amosi alikuwa ametoka tu kutangaza hukumu ya Yehova juu ya mataifa saba. Hata hivyo, yeyote aliyewazia kwamba nabii huyo alikuwa amemaliza kutoa unabii wake, alikuwa amekosea sana. Amosi hakuwa amemaliza! Alikuwa amepewa utume hasa wa kutangaza ujumbe mkali wa hukumu juu ya ufalme wa kaskazini wa Israeli. Taifa la Israeli lilistahili hukumu kali ya Mungu kwa sababu taifa hilo lilikuwa limeharibika sana kiadili na kiroho.
12 Unabii wa Amosi ulifunua ukandamizaji ambao ulikuwa jambo la kawaida katika ufalme wa Israeli. Andiko la Amosi 2:6, 7 linasema hivi kuhusu jambo hilo: “Yehova amesema hivi, ‘Kwa sababu ya maasi matatu ya Israeli, na kwa sababu ya manne, sitaizuia, kwa sababu waliuza mtu mwadilifu kwa sababu tu ya fedha, na maskini kwa bei ya pea moja ya viatu. Wanatamani sana mavumbi ya dunia yaliyo kwenye vichwa vya watu wa hali ya chini; nao huipotosha njia ya watu wapole.’”
13 Waadilifu walikuwa wakiuzwa “kwa sababu tu ya fedha,” labda ikimaanisha kwamba waamuzi ambao walipokea rushwa ya fedha, walikuwa wakiwaadhibu wale wasio na hatia. Wakopeshaji walikuwa wakiwauza maskini utumwani kwa bei ya “pea moja ya viatu,” labda ili kulipa deni fulani dogo tu. Watu wakatili ‘walitamani sana,’ au walitafuta kwa bidii kuwashusha sana “watu wa hali ya chini” hivi kwamba maskini hao walitupa mavumbi juu ya vichwa vyao wenyewe, ambayo ni ishara ya mfadhaiko, maombolezo, au fedheha. Ufisadi ulikuwa umeenea sana hivi kwamba “watu wapole” hawakuwa na tumaini la kutendewa haki yoyote.
14. Ni nani waliokuwa wakitendewa vibaya katika ufalme wa Israeli wa makabila kumi?
14 Ona wale waliokuwa wakitendewa vibaya. Walikuwa waadilifu, maskini, watu wa hali ya chini, na wakaaji wapole wa nchi hiyo. Agano la Sheria ambalo Yehova alifanya kati yake na Israeli lilitaka watu wasio na ulinzi na maskini waonyeshwe huruma. Lakini, badala yake, hali za watu hao katika ufalme wa Israeli wa makabila kumi zilikuwa mbaya sana.
“Jitayarishe Kukutana na Mungu Wako”
15, 16. (a) Kwa nini Waisraeli walionywa: “Jitayarishe kukutana na Mungu wako”? (b) Andiko la Amosi 9:1, 2 linaonyeshaje kwamba waovu hawangeweza kuepuka kutekelezwa kwa hukumu ya Mungu? (c) Ni nini kilichoupata ufalme wa Israeli wa makabila kumi mwaka wa 740 K.W.K.?
15 Kwa kuwa kulikuwa na ukosefu mwingi wa adili na dhambi nyingine huko Israeli, nabii Amosi alikuwa na sababu nzuri ya kulionya hivi taifa hilo lenye kuasi: “Jitayarishe kukutana na Mungu wako.” (Amosi 4:12) Waisraeli waasi hawangeweza kuepuka hukumu ya Mungu iliyokuwa ikikaribia kwa sababu kwa mara ya nane, Yehova alitangaza: “Sitaizuia.” (Amosi 2:6) Mungu alisema hivi kuhusu waovu ambao huenda wangejaribu kujificha: “Hakuna yeyote kati yao anayekimbia atakayefanikiwa kukimbia, na hakuna yeyote kati yao anayeponyoka ambaye atafanikiwa kutoroka. Wakichimba chini kuingia katika Kaburi, toka humo mkono wangu mwenyewe utawachukua; nao wakienda juu mbinguni, toka huko nitawashusha chini.”—Amosi 9:1, 2.
16 Waovu hawangeweza kuepuka hukumu ya Yehova juu yao kwa kuchimba “chini kuingia katika Kaburi,” jambo linaloonyesha kwa njia ya mfano jitihada za kujificha katika sehemu za chini zaidi za dunia. Wala hawangeweza kuepuka hukumu ya Mungu kwa ‘kwenda juu mbinguni,’ yaani, kwa kujaribu kujificha katika milima mirefu. Onyo la Yehova lilikuwa wazi: Hakuna maficho ambayo yeye hawezi kuyafikia. Haki ya Mungu ilidai ufalme wa Israeli utozwe hesabu kwa ajili ya matendo yake maovu. Na wakati huo wa kutoza hesabu ulifika. Katika mwaka wa 740 K.W.K., karibu miaka 60 baada ya Amosi kuandika unabii wake, ufalme wa Israeli ulianguka mikononi mwa Waashuru waliovamia.
Hukumu ya Mungu Huchagua
17, 18. Amosi sura ya 9 hufunua nini kuhusu rehema ya Mungu?
17 Unabii wa Amosi umetusaidia kuona kwamba sikuzote wale wanaohukumiwa na Mungu wanastahili hukumu hiyo, nayo haiepukiki. Pia kitabu cha Amosi kinaonyesha kwamba hukumu ya Yehova huchagua. Mungu anaweza kuwapata waovu popote wanapojificha na kutekeleza hukumu yake juu yao. Anaweza pia kuwapata wale wanaotubu na wanyoofu—wale anaochagua kuwaonyesha rehema. Jambo hilo linakaziwa vizuri sana katika sura ya mwisho ya kitabu cha Amosi.
18 Kulingana na Amosi sura ya 9, mstari wa 8, Yehova alisema: “Sitaiangamiza kabisa nyumba ya Yakobo.” Kama inavyoonyeshwa katika mstari wa 13 hadi 15, Yehova aliahidi kwamba ‘angekusanya na kurudisha mateka’ wa watu wake. Watu hao wangeonyeshwa rehema na kupata usalama na ufanisi. Yehova alitabiri kwamba “anayelima atampita anayevuna.” Hebu wazia jambo hilo—mavuno yangekuwa mengi sana hivi kwamba majira ya kulima na kupanda yangefika kabla ya mavuno mengine kukusanywa ghalani!
19. Ni nini kilichotokea kwa mabaki wa Israeli na Yuda?
19 Tunaweza kusema kwamba hukumu ya Yehova juu ya waovu huko Yuda na Israeli ilikuwa yenye kuchagua kwa kuwa wale waliotubu na wenye mwelekeo unaofaa walionyeshwa rehema. Katika utimizo wa ahadi ya kurudishwa inayotajwa katika Amosi sura ya 9, mabaki wenye kutubu wa Israeli na Yuda walirudi kutoka utekwani Babiloni mwaka wa 537 K.W.K. Walipofika katika nchi yao waliyoipenda, walirudisha tena ibada safi. Pia walijenga upya nyumba zao na kupanda mizabibu na bustani chini ya hali zenye usalama.
Hukumu Kali ya Yehova Itakuja!
20. Tunapaswa kuwa na uhakika gani tunapochunguza ujumbe wa hukumu uliotangazwa na Amosi?
20 Tunapochunguza ujumbe wa hukumu ya Mungu ambao Amosi alitangaza, tunapaswa kuwa na hakika kwamba Yehova atakomesha uovu uliopo siku zetu. Kwa nini tunaweza kuamini hivyo? Kwanza, mifano hiyo ya zamani kuhusu jinsi Yehova alivyowatendea waovu inaonyesha jinsi atakavyofanya katika siku zetu. Pili, kutekelezwa kwa hukumu ya Mungu dhidi ya ufalme ulioasi wa Israeli kunatupa uhakikisho kwamba Mungu ataleta uharibifu juu ya dini zinazojiita za Kikristo ambazo ni sehemu inayolaumika zaidi ya “Babiloni Mkubwa,” milki ya ulimwengu ya dini ya uwongo.—Ufunuo 18:2.
21. Kwa nini dini zinazojiita za Kikristo zinastahili hukumu kali ya Mungu?
21 Bila shaka, dini zinazojiita za Kikristo zinastahili hukumu kali ya Mungu. Ni wazi kwamba kuna upotovu mwingi wa kidini na kiadili katika dini hizo. Dini zinazojiita za Kikristo pamoja na sehemu nyingine ya ulimwengu wa Shetani zinastahili hukumu ya Yehova. Hukumu hiyo pia haiwezi kuepukika, kwa kuwa wakati itakapotekelezwa, maneno haya ya Amosi sura ya 9, mstari wa 1, yatatimia: “Hakuna yeyote kati yao anayekimbia atakayefanikiwa kukimbia, na hakuna yeyote kati yao anayeponyoka ambaye atafanikiwa kutoroka.” Naam, hata waovu wajifiche wapi, Yehova atawapata.
22. Ni mambo gani kuhusu hukumu ya Mungu yanayofafanuliwa kwenye 2 Wathesalonike 1:6-8?
22 Sikuzote hukumu ya Mungu ni yenye kustahili, haiepukiki, nayo huchagua. Tunaweza kuona hilo katika maneno haya ya mtume Paulo: “Ni jambo la uadilifu kwa upande wa Mungu kuwalipa dhiki wale wanaowafanyia ninyi dhiki, lakini, kwenu ninyi mnaopata dhiki, kitulizo pamoja nasi wakati wa ufunuo wa Bwana Yesu kutoka mbinguni pamoja na malaika zake wenye nguvu katika mwali wa moto, anapoleta kisasi juu ya wale wasiomjua Mungu na wale wasiotii habari njema juu ya Bwana wetu Yesu.” (2 Wathesalonike 1:6-8) “Ni jambo la uadilifu kwa upande wa Mungu” kuwalipa wale wanaostahili hukumu kali kwa sababu ya kuwaletea dhiki watiwa-mafuta wake. Hukumu hiyo haitaepukika, kwa kuwa waovu hawataokoka ‘ufunuo wa Yesu pamoja na malaika zake wenye nguvu katika mwali wa moto.’ Pia hukumu ya Mungu itakuwa yenye kuchagua kwa kuwa Yesu ataleta kisasi “juu ya wale wasiomjua Mungu na wale wasiotii habari njema.” Na kutekelezwa kwa hukumu ya Mungu kutawafariji wale wanaopatwa na dhiki.
Tumaini kwa Wanyoofu
23. Tunaweza kupata tumaini na faraja gani katika kitabu cha Amosi?
23 Unabii wa Amosi una ujumbe wa faraja na tumaini kwa watu wenye mwelekeo unaofaa. Kama ilivyotabiriwa katika kitabu cha Amosi, Yehova hakuwaangamiza kabisa watu wake wa nyakati za kale. Mwishowe, aliwakusanya mateka wa Israeli na Yuda, akawarudisha katika nchi yao na kuwapa usalama na ufanisi mwingi. Hilo linamaanisha nini siku zetu? Jambo hilo hufanya tuwe na hakika kwamba wakati hukumu ya Mungu itakapotekelezwa, Yehova atawapata waovu popote pale walipojificha, naye atawapata wale wanaostahili rehema zake, popote pale wanapoishi katika dunia hii.
-
-
Mtafuteni Yehova, Mchunguzaji wa MioyoMnara wa Mlinzi—2004 | Novemba 15
-
-
Mtafuteni Yehova, Mchunguzaji wa Mioyo
“Nitafuteni mimi, mwendelee kuishi.”—AMOSI 5:4.
1, 2. Maandiko humaanisha nini yanaposema kwamba Yehova “huona jinsi moyo ulivyo”?
YEHOVA MUNGU alimwambia nabii Samweli hivi: “Mwanadamu huona kile kinachoonekana kwa macho, lakini Yehova huona jinsi moyo ulivyo.” (1 Samweli 16:7) Yehova ‘huonaje jinsi moyo ulivyo’?
2 Katika Maandiko, mara nyingi moyo hufananisha jinsi mtu alivyo kwa ndani—tamaa, mawazo, hisia, na mapendezi yake. Basi Biblia inaposema kwamba Mungu huuona moyo, inamaanisha kwamba yeye haangalii sura ya nje bali hukaza fikira zake juu ya jinsi mtu alivyo kwa ndani.
Mungu Achunguza Israeli
3, 4. Kulingana na Amosi 6:4-6, kulikuwa na hali gani katika ufalme wa makabila kumi wa Israeli?
3 Mchunguzaji huyo wa mioyo aliona mambo gani alipotazama ule ufalme wa Israeli wa makabila kumi katika siku za Amosi? Andiko la Amosi 6:4-6 linasema kuhusu wanaume waliokuwa ‘wakijilaza katika vitanda vya pembe za tembo na kujitandaza katika vitanda vyao.’ Walikuwa ‘wakila kondoo-dume kati ya kundi na ng’ombe-dume wachanga kutoka kati ya ndama waliononeshwa.’ Wanaume hao walikuwa ‘wamejitengenezea vyombo vya nyimbo’ nao walikuwa ‘wakinywa kwa mabakuli ya divai.’
4 Mtu anapoyatupia jicho, huenda mambo hayo yakaonekana kuwa mema. Matajiri, wakiwa wamestarehe katika makao yao yaliyopambwa vyema, walifurahia vyakula na divai bora zaidi na kuburudishwa kwa vyombo vizuri zaidi vya muziki. Pia walikuwa na “vitanda vya pembe za tembo.” Wachimbaji wa vitu vya kale wamefukua vitu vingi maridadi vilivyochongwa kwa pembe za tembo huko Samaria, mji mkuu wa ufalme wa Israeli. (1 Wafalme 10:22) Huenda vingi vya vitu hivyo vilirembesha vyombo na hata mbao za ukutani.
5. Kwa nini Mungu alichukizwa na Waisraeli wa siku za Amosi?
5 Je, Yehova Mungu aliwakataza Waisraeli wasiishi maisha ya starehe, kula vyakula vitamu, kunywa divai nzuri, na kusikiliza muziki mtamu? Sivyo hata kidogo! Kwa kweli, yeye humpa mwanadamu vitu hivyo kwa wingi ili avifurahie. (1 Timotheo 6:17) Kile kilichomchukiza Yehova ni tamaa mbaya ya watu hao, hali yao mbaya ya moyoni, mtazamo wao wa kutomheshimu Mungu, na kutowapenda Waisraeli wenzao.
6. Hali ya kiroho ya Israeli ilikuwaje wakati wa Amosi?
6 Wale waliokuwa ‘wakijitandaza katika vitanda vyao, wakila kondoo-dume kati ya kundi, kunywa divai, na kujitengenezea vyombo vya nyimbo’ walishangaa. Watu hao waliulizwa: “Je, mnaiondoa akilini mwenu ile siku yenye msiba?” Walipaswa kutaabishwa sana na hali katika Israeli, lakini ‘hawakuwa wagonjwa kutokana na msiba wa Yosefu.’ (Amosi 6:3-6) Licha ya ufanisi wa kiuchumi wa taifa hilo, Mungu aliona kwamba Yosefu—au Israeli—alikuwa katika balaa kubwa ya kiroho. Hata hivyo, watu waliendelea na shughuli zao za kila siku bila kujali. Watu wengi leo wana mtazamo kama huo. Huenda wakakubali kwamba tunaishi katika nyakati ngumu, lakini maadamu magumu hayo hayawapati wao wenyewe, hawajali taabu za wengine wala hawajishughulishi na mambo ya kiroho.
Israeli—Taifa Lililooza
7. Ni nini ambacho kingetokea ikiwa watu wa Israeli hawangetii maonyo ya Mungu?
7 Kitabu cha Amosi kinaeleza juu ya taifa ambalo limeoza, ijapokuwa linaonekana lenye ufanisi. Kwa sababu ya kutotii maonyo ya Mungu na kurekebisha maoni yao, Yehova atawatia mkononi mwa adui zao. Waashuru watakuja na kuwanyakua kutoka katika vitanda vyao vya fahari vya pembe za tembo nao watawapeleka utekwani kwa nguvu. Hawatastarehe tena!
8. Waisraeli walijikuta katika hali mbaya ya kiroho jinsi gani?
8 Waisraeli waliingiaje katika hali hiyo? Hali hiyo ilianza mwaka wa 997 K.W.K., wakati Rehoboamu alipochukua nafasi ya baba yake Mfalme Sulemani, na ufalme wa Israeli wa kabila kumi ukajitenga na makabila ya Yuda na Benyamini. Mfalme wa kwanza wa ufalme wa Israeli wa makabila kumi alikuwa Yeroboamu wa Kwanza, “mwana wa Nebati.” (1 Wafalme 11:26) Yeroboamu aliwasadikisha watu wa utawala wake kwamba ilikuwa vigumu mno kwao kusafiri hadi Yerusalemu ili kumwabudu Yehova. Hata hivyo, hakuhangaikia kikweli hali ya watu. Badala yake, alitaka kuyalinda masilahi yake mwenyewe. (1 Wafalme 12:26) Yeroboamu aliogopa kwamba ikiwa Waisraeli wangeendelea kumiminika kwenye hekalu huko Yerusalemu kwa ajili ya sherehe zilizofanywa kila mwaka ili kumheshimu Yehova, mwishowe wangerudi kuwa waaminifu kwa ufalme wa Yuda. Ili kuzuia jambo hilo lisitendeke, Yeroboamu alisimamisha ndama wawili wa dhahabu, mmoja huko Dani na mwingine huko Betheli. Hivyo, ibada ya ndama ikawa dini rasmi ya ufalme wa Israeli.—2 Mambo ya Nyakati 11:13-15.
9, 10. (a) Ni sherehe gani za kidini zilizopangwa kwa ajili ya Mfalme Yeroboamu wa Kwanza? (b) Mungu alionaje sherehe zilizofanywa Israeli katika siku za Mfalme Yeroboamu wa Pili?
9 Yeroboamu alijaribu kuifanya dini hiyo mpya iheshimike. Alipanga sherehe ambazo zilifanana kwa njia fulani na zile sherehe zilizofanywa huko Yerusalemu. Katika andiko la 1 Wafalme 12:32, tunasoma hivi: “Yeroboamu akafanya sherehe katika mwezi wa nane siku ya kumi na tano ya mwezi huo, kama ile sherehe iliyokuwa katika Yuda, ili atoe matoleo juu ya madhabahu aliyokuwa ameijenga kule Betheli.”
10 Yehova hakuzikubali kamwe sherehe hizo za dini ya uwongo. Kupitia Amosi, Yeye alionyesha waziwazi maoni yake juu ya matendo hayo karne moja baadaye wakati wa utawala wa Yeroboamu wa Pili, ambaye alikuwa mfalme wa ufalme wa Israeli wa makabila kumi yapata mwaka wa 844 K.W.K. (Amosi 1:1) Kulingana na Amosi 5:21-24, Mungu alisema: “Nimechukia, nimezikataa sherehe zenu, wala sitafurahia harufu ya makusanyiko yenu makuu. Lakini ninyi mkinitolea matoleo mazima ya kuteketezwa, hata katika matoleo yenu ya zawadi sitapata furaha, wala sitatazama dhabihu zenu za ushirika za vinono. Ondoeni kutoka kwangu mchafuko wa nyimbo zenu; wala sauti tamu ya vinanda vyenu sitaki kusikia. Na haki itiririke kama maji, na uadilifu kama mto unaotiririka daima.”
Ufanani Uliopo Leo
11, 12. Kuna ufanani gani kati ya ibada ya Waisraeli wa kale na ile ya dini zinazojiita za Kikristo?
11 Kwa wazi basi, Yehova alichunguza mioyo ya wale walioshiriki katika sherehe za Israeli, naye akazikataa sikukuu zao na matoleo mazima ya kuteketezwa. Vivyo hivyo leo, yeye anakataa sikukuu za kipagani kama vile Krismasi na Pasaka za dini zinazojiita za Kikristo. Kwa waabudu wa Yehova, haiwezekani kuwe na urafiki kati ya uadilifu na uvunjaji wa sheria, wala ushirika kati ya nuru na giza.—2 Wakorintho 6:14-16.
12 Ibada ya dini zinazojiita za Kikristo na ile ibada ya Waisraeli walioabudu ndama zinafanana kwa njia nyingine pia. Ingawa watu fulani wanaodai kuwa Wakristo hukubali ukweli wa Neno la Mungu, ibada ya dini zinazojiita za Kikristo haichochewi na upendo wa kweli kwa Mungu. Kama ingekuwa hivyo, dini hizo zingesisitiza kumwabudu Yehova “kwa roho na kweli” kwa sababu hiyo ndiyo ibada inayompendeza. (Yohana 4:24) Isitoshe, dini zinazojiita za Kikristo haziachi “haki itiririke kama maji, na uadilifu kama mto unaotiririka daima.” Badala yake, dini hizo hupuuza daima matakwa ya Mungu ya maadili. Wao huachilia makosa kama vile uasherati na dhambi nyinginezo nzito na hata hukubali ndoa za watu wa jinsia moja!
“Pendeni Yaliyo Mema”
13. Kwa nini tunapaswa kutii maneno ya Amosi 5:15?
13 Yehova anawaambia hivi wote wanaotamani kumwabudu kwa njia inayompendeza: “Chukieni yaliyo mabaya, pendeni yaliyo mema.” (Amosi 5:15) Upendo na chuki ni hisia zenye nguvu ambazo hutoka katika moyo wa mfano. Kwa kuwa moyo ni wenye hila, ni lazima tufanye kila tuwezalo ili kuulinda. (Methali 4:23; Yeremia 17:9) Tukiuacha moyo wetu usitawishe tamaa mbaya, huenda tukajikuta tukipenda mabaya na kuchukia mema. Na ikiwa tutazifuata tamaa hizo kwa kuzoea kutenda dhambi, kuwa na bidii nyingi katika utumishi wa Yehova hakutafanya tupate tena kibali cha Mungu. Kwa hiyo, acheni tuombe msaada wa Mungu ili ‘tuchukie yaliyo mabaya, na kupenda yaliyo mema.’
14, 15. (a) Katika Israeli, ni nani waliokuwa wakifanya yaliyo mema, lakini baadhi yao walitendewaje? (b) Tunawezaje kuwatia moyo wale walio katika utumishi wa wakati wote leo?
14 Si Waisraeli wote waliokuwa wakitenda mabaya machoni pa Yehova. Kwa mfano, Hosea na Amosi ‘walipenda mema’ na kumtumikia Mungu kwa uaminifu wakiwa manabii. Wengine waliweka ahadi za kuwa Wanadhiri. Kwa muda ambao walikuwa Wanadhiri, walijiepusha na chochote kilichotokana na mzabibu, hasa divai. (Hesabu 6:1-4) Waisraeli wengine waliyaonaje maisha ya kujidhabihu ya watu hao wenye kutenda mema? Jibu lenye kushtua kwa swali hilo hufunua kadiri ambavyo taifa hilo lilikuwa limeoza kiroho. Andiko la Amosi 2:12 linasema: “Mliendelea kuwapa Wanadhiri divai wanywe, nanyi mkaweka amri juu ya manabii, mkisema: ‘Msitoe unabii.’”
15 Waisraeli hao walipaswa kuaibika na kubadili njia zao walipoona uaminifu ulioonyeshwa na Wanadhiri na manabii. Badala yake, kwa njia isiyo ya upendo, walijaribu kuwavunja moyo watu hao washikamanifu wasimtukuze Mungu. Hatupaswi kamwe kuwahimiza Wakristo wenzetu ambao ni mapainia, wamishonari, waangalizi wasafirio, au Wanabetheli waache utumishi wao wa wakati wote ili warudie yale yanayoitwa eti maisha ya kawaida. Badala yake, na tuwatie moyo waendelee na kazi yao nzuri!
16. Kwa nini Waisraeli walikuwa katika hali bora kiroho katika siku za Musa kuliko wakati wa Amosi?
16 Ingawa Waisraeli wengi waliishi maisha ya raha mustarehe katika siku za Amosi, hawakuwa ‘matajiri kwa Mungu.’ (Luka 12:13-21) Mababu zao walikula mana tu nyikani kwa miaka 40. Hawakuwa wakila ng’ombe waliononeshwa wala kujilaza kizembe juu ya vitanda vya pembe za tembo. Hata hivyo, Musa aliwaambia hivi kwa kufaa: “Yehova Mungu wako amekubariki wewe katika kila tendo la mkono wako. . . . Miaka hii 40 Yehova Mungu wako amekuwa pamoja nawe. Hukukosa kitu chochote.” (Kumbukumbu la Torati 2:7) Naam, wakiwa nyikani, Waisraeli hawakukosa kamwe vitu ambavyo walihitaji kikweli. Jambo muhimu kuliko yote ni kwamba walikuwa na upendo, ulinzi, na baraka za Mungu!
17. Kwa nini Yehova aliwaongoza Waisraeli wa kale kuingia katika Nchi ya Ahadi?
17 Yehova aliwakumbusha watu walioishi wakati mmoja na Amosi kwamba Yeye aliwaingiza mababu zao katika Nchi ya Ahadi na kuwasaidia kuwaondoa adui zao wote katika nchi hiyo. (Amosi 2:9, 10) Lakini kwa nini Mungu aliwatoa Waisraeli wa kale Misri na kuwapeleka katika Nchi ya Ahadi? Je, alifanya hivyo ili waishi maisha ya anasa, kisha wamkatae Muumba wao? La! Badala yake, alifanya hivyo ili waweze kumwabudu wakiwa watu huru na safi kiroho. Lakini wakaaji wa ufalme wa Israeli wa makabila kumi hawakuchukia mabaya na kupenda mema. Badala ya kumtukuza Yehova Mungu, walikuwa wakizitukuza sanamu za kuchongwa. Hiyo ilikuwa aibu iliyoje!
Yehova Anawatoza Hesabu
18. Kwa nini Yehova ametuweka huru kiroho?
18 Mungu hangevumilia mwenendo huo wa Waisraeli wenye kuaibisha. Alionyesha msimamo wake waziwazi aliposema: “Nitawatoza ninyi hesabu kwa sababu ya makosa yenu yote.” (Amosi 3:2) Maneno hayo yanapaswa kufanya tutafakari jinsi tulivyokombolewa kutoka katika utumwa wa Misri ya leo, yaani, mfumo huu mwovu wa mambo. Yehova hajatuweka huru kiroho ili tufuatilie miradi ya ubinafsi. Badala yake, amefanya hivyo ili tumtukuze kutoka moyoni tukiwa watu huru wanaoshiriki katika ibada safi. Sisi sote tutatoa hesabu kuhusu namna tunavyotumia uhuru wetu tuliopewa na Mungu.—Waroma 14:12.
19. Kulingana na Amosi 4:4, 5, Waisraeli wengi walipenda nini?
19 Kwa kusikitisha, watu wengi katika Israeli hawakutii ujumbe wenye nguvu wa Amosi. Nabii huyo alifunua hali yao mbaya ya kiroho katika maneno haya yanayopatikana kwenye Amosi 4:4, 5: “Njooni Betheli, mfanye makosa. Fanyeni makosa mara nyingi katika Gilgali, . . . kwa maana hivyo ndivyo mmependa, enyi wana wa Israeli.” Waisraeli hawakuwa wamesitawisha tamaa zinazofaa. Hawakuwa wameilinda mioyo yao. Kwa hiyo, wengi wao walianza kupenda mabaya na kuchukia mema. Waabudu-ndama hao wenye shingo ngumu hawakubadilika. Yehova angewatoza hesabu, nao wangekufa katika dhambi zao!
20. Mtu anawezaje kuchukua hatua inayopatana na Amosi 5:4?
20 Haikuwa rahisi kwa yeyote aliyeishi Israeli nyakati hizo kudumu akiwa mwaminifu kwa Yehova. Si jambo rahisi kuwa tofauti na walio wengi, kama vile Wakristo wote leo, vijana kwa wazee, wanavyojua. Lakini upendo kwa Mungu na tamaa ya kutaka kumpendeza iliwachochea Waisraeli fulani wafuate ibada ya kweli. Yehova aliwakaribisha watu hao kwa uchangamfu, kama ilivyoandikwa katika Amosi 5:4: “Nitafuteni mimi, mwendelee kuishi.” Vivyo hivyo leo, Mungu huwaonyesha rehema wale wanaotubu na kumtafuta kwa kutwaa ujuzi sahihi wa Neno lake na kufanya mapenzi yake. Si rahisi kuchukua hatua hiyo, lakini kufanya hivyo huongoza kwenye uzima wa milele.—Yohana 17:3.
Ufanisi Licha ya Njaa ya Kiroho
21. Wale ambao hawafuati ibada ya kweli hupatwa na njaa gani?
21 Ni nini ambacho kingewapata wale ambao hawakuunga mkono ibada ya kweli? Njaa mbaya zaidi—njaa ya kiroho! “Siku zinakuja,” asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, “nami nitaleta njaa katika nchi, wala si njaa ya mkate, nami nitaleta kiu, wala si kiu ya maji, bali ya kuyasikia maneno ya Yehova.” (Amosi 8:11) Dini zinazojiita za Kikristo zinapatwa na njaa hiyo ya kiroho. Hata hivyo, watu walio wanyoofu katika dini hizo wameona ufanisi wa kiroho wa watu wa Mungu, nao wanamiminika katika tengenezo la Yehova. Tofauti iliyopo kati ya dini zinazojiita za Kikristo na Wakristo wa kweli inaonyeshwa ifaavyo na maneno haya ya Yehova: “Tazama! Watumishi wangu watakula, lakini ninyi mtakuwa na njaa. Tazama! Watumishi wangu watakunywa, lakini ninyi mtakuwa na kiu. Tazama! Watumishi wangu watashangilia, lakini ninyi mtaona aibu.”—Isaya 65:13.
22. Kwa nini tuna sababu ya kushangilia?
22 Tukiwa watumishi wa Yehova, je, sisi binafsi huthamini maandalizi yetu ya kiroho na baraka tunazopata? Tunapojifunza Biblia na vichapo vya Kikristo na kuhudhuria mikutano yetu ya kutaniko na makusanyiko, kwa kweli tunahisi kwamba tunataka kupiga vigelegele vya shangwe kwa sababu ya hali nzuri ya moyo. Tunashangilia kwa kuelewa Neno la Mungu waziwazi, kutia ndani unabii wa Amosi ulioongozwa na roho ya Mungu.
23. Wale wanaomtukuza Mungu hupata nini?
23 Unabii wa Amosi una ujumbe wa tumaini kwa wanadamu wote wanaompenda Mungu na wanaotaka kumtukuza. Hata hali yetu ya sasa ya kiuchumi iweje au tukabili majaribu gani katika ulimwengu huu wenye msukosuko, sisi ambao tunampenda Mungu tunapata baraka zake na chakula bora zaidi cha kiroho. (Methali 10:22; Mathayo 24:45-47) Basi utukufu wote unamwendea Mungu, ambaye hutupa sisi vitu vyote kwa wingi ili tuvifurahie. Kwa hiyo, sisi sote na tuazimie kumsifu kutoka moyoni milele. Hilo litakuwa pendeleo lenye shangwe ikiwa tutamtafuta Yehova, Mchunguzaji wa mioyo.
-