Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Ayubu Alilitukuza Jina la Yehova
    Mnara wa Mlinzi—2009 | Aprili 15
    • Ayubu Ajaribiwa na Shetani

      3. Tunajua nini kumhusu Ayubu, na kwa nini alikuwa shabaha ya Shetani?

      3 Ayubu alikuwa tajiri na mtu mashuhuri sana, mzee wa ukoo mwenye sifa nzuri. Alikuwa mshauri mwenye kuheshimiwa sana ambaye aliwasaidia watu wenye uhitaji. Jambo la maana hata zaidi ni kwamba Ayubu alimwogopa Mungu. Ayubu anaelezwa kuwa mtu ambaye ‘hakuwa na lawama na mnyoofu, na aliyemwogopa Mungu na kujiepusha na ubaya.’ Ayubu alikuwa shabaha ya mashambulizi ya Shetani Ibilisi kwa sababu ya kujitoa kwake kwa Mungu, bali si kwa sababu ya mali na umashuhuri wake.—Ayu. 1:1; 29:7-16; 31:1.

      4. Utimilifu ni nini?

      4 Utangulizi wa masimulizi ya kitabu cha Ayubu unaeleza kuhusu mkutano uliokuwa mbinguni ambapo malaika walisimama mbele za Yehova. Shetani pia alikuwepo, na alitoa mashtaka kumhusu Ayubu. (Soma Ayubu 1:6-11.) Ingawa Shetani alitaja mali za Ayubu, shabaha yake ilikuwa hasa kupinga utimilifu wa Ayubu. Neno “utimilifu” linamaanisha kuwa mnyoofu, asiye na lawama, mwadilifu, na bila kosa. Kulingana na Biblia, utimilifu wa wanadamu unamaanisha kujitoa kwa moyo kamili kwa Yehova.

      5. Shetani alidai nini kumhusu Ayubu?

      5 Shetani alidai kwamba Ayubu alimwabudu Mungu kwa sababu ya uchoyo, wala si kwa sababu ya utimilifu. Shetani alidai kwamba Ayubu angekuwa mshikamanifu kwa Yehova ikiwa tu Mungu angeendelea kumthawabisha na kumlinda. Ili kujibu dai la Shetani, Yehova alimruhusu Shetani amshambulie mwanamume huyo mwaminifu. Kwa hiyo, kwa siku moja tu, Ayubu alijulishwa kwamba mifugo yake iliibiwa au kuangamizwa, watumishi wake waliuawa, na watoto wake kumi wakafa. (Ayu. 1:13-19) Je, mashambulizi ya Shetani yalivunja utimilifu wa Ayubu? Maandiko yaliyoongozwa na roho ya Mungu yanaeleza maoni ya Ayubu kuhusu misiba yake: “Yehova ametoa, na Yehova amechukua. Jina la Yehova na liendelee kubarikiwa.”—Ayu. 1:21.

      6. (a) Ni jambo gani lililotukia katika mkutano mwingine huko mbinguni? (b) Shetani alikuwa akimfikiria nani alipotilia shaka utimilifu wa Ayubu kwa Yehova?

      6 Baadaye, kulikuwa na mkutano mwingine mbinguni. Kwa mara nyingine tena Shetani alimshtaki Ayubu, akisema: “Ngozi kwa ngozi, na kila kitu alicho nacho mtu atakitoa kwa ajili ya nafsi yake. Ili kuwe na badiliko, tafadhali nyoosha mkono wako, uguse kufikia mfupa wake na nyama yake, uone kama hatakulaani wewe mbele za uso wako.” Ona kwamba Shetani alihusisha watu wengine katika mashtaka yake. Kwa kusema, “Kila kitu alicho nacho mtu atakitoa kwa ajili ya nafsi yake,” Ibilisi hakutilia shaka utimilifu wa Ayubu tu, bali pia wa “mtu” yeyote yule anayemwabudu Yehova. Baadaye, Mungu alimruhusu Shetani kumpiga Ayubu kwa ugonjwa wenye maumivu makali. (Ayu. 2:1-8) Lakini huo haukuwa mwisho wa majaribu ya Ayubu.

      Mambo Tunayojifunza Kutokana na Msimamo wa Ayubu

      7. Ayubu alisongwa sana katika njia gani na mke wake na pia wageni waliomtembelea?

      7 Mwanzoni, mke wa Ayubu aliumia moyoni kwa sababu ya mapigo yaliyompata mume wake. Bila shaka, alifadhaika kwa sababu ya vifo vya watoto wake na kupoteza mali ya familia yake. Inaonekana, aliumia moyoni kuona mume wake akikabiliana na ugonjwa wenye maumivu makali. Alimwambia Ayubu hivi: “Je, bado unashikilia sana utimilifu wako? Mlaani Mungu, ufe!” Kisha, wanaume watatu wakafika, yaani, Elifazi, Bildadi, na Sofari, inaelekea walikuja kumfariji Ayubu. Hata hivyo, walitumia mawazo ya udanganyifu na hivyo wakathibitika kuwa “wafariji wasumbufu.” Kwa mfano, Bildadi alidai kwamba watoto wa Ayubu walitenda dhambi na hivyo walistahili madhara yaliyowapata. Elifazi alidai kwamba mateso ya Ayubu yalikuwa adhabu kwa sababu ya dhambi alizotenda wakati uliopita. Hata alitilia shaka ikiwa wale wanaoshika utimilifu wana thamani yoyote machoni pa Mungu! (Ayu. 2:9, 11; 4:8; 8:4; 16:2; 22:2, 3) Chini ya hali hizo ngumu sana, Ayubu aliendelea kuwa mtimilifu. Ni kweli kwamba alikosea ‘alipoitangaza nafsi yake mwenyewe kuwa adilifu badala ya Mungu.’ (Ayu. 32:2) Hata hivyo, alibaki mwaminifu mpaka mwisho.

  • Ayubu Alilitukuza Jina la Yehova
    Mnara wa Mlinzi—2009 | Aprili 15
    • Ibilisi alidai kwamba Ayubu, mtumishi mtimilifu wa Yehova, hangeendelea kuwa mshikamanifu ikiwa angepoteza mali yake yote. Ayubu alibaki mshikamanifu katika majaribu. Kisha, Shetani alidai kwamba mwanadamu yeyote angemwacha Mungu ikiwa angeteseka kimwili. Ayubu aliteseka, lakini utimilifu wake haukuvunjwa. Hivyo, Shetani alithibitika kuwa mwongo katika kisa cha mwanamume huyo mwaminifu, lakini asiye mkamilifu.

  • Ayubu Alilitukuza Jina la Yehova
    Mnara wa Mlinzi—2009 | Aprili 15
    • Kipindi cha wakati kisichojulikana kilipita kati ya mkutano wa mbinguni unaotajwa kwenye Ayubu 1:6 na ule unaotajwa kwenye Ayubu 2:1, na wakati huo Ayubu alijaribiwa kikatili. Uaminifu wa Ayubu ulimwezesha Yehova kumwambia Shetani: “Hata sasa bado [Ayubu] anashikilia sana utimilifu wake, ingawa wewe unanichochea juu yake nimmeze bila sababu.” Lakini Shetani hakukubali kwamba madai yake kumhusu Ayubu yalikuwa yamethibitishwa kuwa ya uwongo. Badala yake, aliomba kwamba Ayubu ajaribiwe tena vikali. Hivyo, Ibilisi alimjaribu Ayubu wakati alipokuwa tajiri na wakati ambapo hakuwa na chochote. Kwa wazi, Shetani hawahurumii watu wenye uhitaji au wale wanaopatwa na misiba. Anachukia watu watimilifu. (Ayu. 2:3-5) Hata hivyo, uaminifu wa Ayubu ulionyesha kwamba Shetani ni mwongo.

  • Ayubu Alilitukuza Jina la Yehova
    Mnara wa Mlinzi—2009 | Aprili 15
    • Ayubu Alilitukuza Jina la Yehova

      16. Ayubu alionyesha mtazamo gani kumwelekea Yehova?

      16 Ayubu alilitumia na kulisifu jina la Yehova. Hata alipoumia sana moyoni kwa sababu ya habari za vifo vya watoto wake, Ayubu hakumhesabia Mungu jambo lolote lisilofaa. Ingawa Ayubu alifikiri kimakosa kwamba Mungu ndiye aliyesababisha vifo hivyo, bado alilitukuza jina la Yehova. Baadaye, katika moja ya maneno yake ya kimethali, Ayubu alisema hivi: “Tazama! Kumwogopa Yehova—hiyo ndiyo hekima, na kuacha ubaya ni uelewaji.”—Ayu. 28:28.

      17. Ni nini kilichomsaidia Ayubu kudumisha utimilifu wake?

      17 Ni nini kilichomsaidia Ayubu kudumisha utimilifu wake? Ni wazi kwamba kabla ya kupatwa na misiba hiyo, alikuwa tayari amesitawisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova. Ingawa hatuna uthibitisho wa kwamba alijua kwamba Shetani alikuwa ametoa mashtaka fulani kumhusu Yehova, Ayubu aliazimia kubaki mshikamanifu. Alisema hivi: “Mpaka nitakapokata pumzi, sitajiondolea utimilifu wangu!” (Ayu. 27:5) Ayubu alidumisha jinsi gani uhusiano huo wa karibu pamoja na Mungu? Bila shaka, alithamini yale aliyosikia kuhusu jinsi Mungu alivyoshughulika na Abrahamu, Isaka, na Yakobo, ambao walikuwa watu wake wa ukoo. Na kwa kuchunguza uumbaji, Ayubu angeweza kutambua sifa nyingi za Yehova.—Soma Ayubu 12:7-9, 13, 16.

      18. (a) Ayubu alionyesha jinsi gani kwamba alijitoa kwa Yehova? (b) Tunaiga mfano mzuri wa Ayubu katika njia gani?

      18 Mambo ambayo Ayubu alijifunza yalimchochea kuwa na tamaa ya kumpendeza Yehova. Kwa kuwa huenda washiriki wa familia yake walifanya jambo fulani lisilompendeza Mungu au ‘walimlaani Mungu moyoni mwao,’ Ayubu alitoa dhabihu kwa ukawaida. (Ayu. 1:5) Hata akiwa chini ya majaribu makali, bado Ayubu alisema mambo mazuri kumhusu Yehova. (Ayu. 10:12) Anatuwekea mfano mzuri kama nini! Sisi pia tunapaswa kujifunza kwa ukawaida ili tupate ujuzi sahihi kumhusu Yehova na makusudi yake. Tunapaswa kuwa na mazoea mazuri ya kiroho, kama vile kujifunza, kuhudhuria mikutano, kusali, na kuhubiri habari njema. Zaidi ya hayo, tunafanya yote tunayoweza ili kulitangaza jina la Yehova. Na kama vile utimilifu wa Ayubu ulivyompendeza Yehova, ndivyo utimilifu wa watumishi wa Mungu leo unavyofanya moyo wa Yehova ushangilie.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki