-
Matukio Muhimu ya Mwaka Uliopita2012 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
TETEMEKO KUBWA LA NCHI HUKO JAPANI
Habari kutoka sehemu mbalimbali za ulimwengu zimeripoti kuhusu misiba mingi ya asili, kutia ndani matetemeko ya nchi, tsunami, vimbunga, tufani, mafuriko, mioto, na milipuko ya volkano. Hatuwezi kuandika kuhusu misiba yote ya hivi karibuni. Hata hivyo, waabudu wenzetu nchini Japani ni mfano mzuri sana wa jinsi Mashahidi wa Yehova hukabili matatizo kama hayo kwa ujasiri.
Mnamo Ijumaa, Machi 11, 2011, saa 8:46 alasiri, tetemeko la nchi lenye kipimo cha 9.0 liliikumba nchi ya Japani. Tsunami zilizotokea baada ya hapo ziliharibu miji na vijiji vingi katika pwani ya Bahari ya Pasifiki. Watu 20,000 hivi walikufa au hawajawahi kupatikana. Katika maeneo yaliyoathiriwa, Majumba manne ya Ufalme yaliharibiwa na mengine manne hayangeweza kutumiwa. Nyumba 235 za ndugu zetu zilifagiliwa na maji au kuharibiwa sana, na nyingine zaidi ya elfu moja zilihitaji kurekebishwa.
Tetemeko hilo na tsunami hizo ziliharibu mtambo fulani wa nguvu za nyuklia vibaya sana hivi kwamba ulitoa hewani chembe zenye mnururisho. Serikali ilitoa amri ya kuwahamisha wakaaji wa maeneo ya karibu na hivyo majiji mengi yaliachwa ukiwa baada ya usiku mmoja tu. Ndugu walioishi katika maeneo hayo walilazimika kuhama pia, na makutaniko mawili “yakatoweka.”
Kati ya Mashahidi wa Yehova zaidi ya 14,000 wanaoishi katika maeneo yaliyoathiriwa, 12 walikufa, na 5 walijeruhiwa vibaya; 2 bado hawajulikani walipo. Wengi waliookoka tukio hilo lenye kutisha walipoteza makao yao, mali zao, na katika visa vingi, waliwapoteza wapendwa wao.
“Nilifanikiwa kumpandisha mama yangu aliye mlemavu ndani ya gari na nikaanza kuliendesha hadi kwenye makao tuliyoagizwa twende,” asema Kiyoko kutoka Ofunato. “Kulikuwa na harufu ya moshi. Nilipotoka nje ya gari, niliona wimbi kubwa la maji likiisomba nyumba yetu. Wimbi hilo lilikuwa linatukaribia kwa kasi! Nikamsaidia mama kupanda juu ya mwinuko fulani kwenye njia ya gari moshi. Gari letu lilifagiliwa mbali huku tukitazama.”
Baada ya tetemeko hilo, ndugu mmoja kijana anayeitwa Koichi, alijaribu kwenda kwa wazazi wake wanaoishi Ishinomaki, kilomita 5 kutoka baharini. Alipokaribia huko, aliona kuwa eneo lote lilikuwa limezama ndani ya maji. “Singeenda zaidi ya hapo kwa sababu sikuwa na mashua.” Majuma matatu baada ya tetemeko, aliupata mwili wa baba yake katika chumba cha kuhifadhia maiti, na baada ya majuma mengine matatu, akaupata mwili wa mama yake hukohuko.
Tetemeko lilipokoma, Masaaki anayeishi Shichigahama aliegesha gari lake kwenye Jumba la Ufalme, kilomita moja kutoka ufuoni. Masaaki akumbuka: “Nilimwona dada mmoja ambaye pia alikimbilia huko. Nilidhani tsunami hazingefika hapo. Hata hivyo, baada ya muda mfupi maji meusi yaliifunika ardhi! Magari yetu yakaanza kuelea. Nilifungua dirisha, nikapanda juu ya gari langu, lakini gari la dada huyo lilisombwa na maji! Nilimwomba Yehova amsaidie.
“Kulikuwa na theluji, na nilikuwa nimelowa, na kutetemeka kwa sababu ya baridi. Baadaye theluji iliacha kuanguka lakini kulikuwa na baridi kali. Punde si punde, jua lilishuka na giza likaingia. Nyota zilikuwa nyangavu na maridadi. Nilisimama juu ya gari langu, lililokuwa kama kisiwa katika maji baridi kama barafu. Kulikuwa na wengine kama mimi waliokuwa juu ya vifusi au paa za majengo mbalimbali. Sikujua kama ningekuwa hai asubuhi iliyofuata. Ili kujifariji, nilikariri hotuba ambayo nilikuwa nimetoa majuma mawili tu kabla ya wakati huo. Ilikuwa na kichwa chenye kufaa: ‘Unaweza Kupata Wapi Msaada Nyakati za Taabu?’ Baadaye, nikaimba wimbo pekee niliojua kuimba bila kitabu: ‘Baba Yangu, Mungu Wangu, Rafiki Yangu.’ Niliuimba tena na tena. Nilipokuwa nikiimba, nilifikiria jinsi nilivyotumia maisha yangu katika utumishi wa Yehova, na kutokwa na machozi.
“Kisha mtu fulani kutoka nyumba iliyokuwa ule upande mwingine wa barabara akapaaza sauti na kuuliza, ‘Uko sawa? Nitakuja kukusaidia!’” Mwanamume huyo alikuwa ametengeneza chelezo kutokana na mbao zilizokuwa zinaelea juu ya maji na alikuwa akiwaokoa watu waliokuwa karibu. Mwanamume huyo alimsaidia Masaaki kuingia ndani ya nyumba ya mtu fulani katika ghorofa ya pili kupitia dirishani. Baadaye, Masaaki alifurahi kusikia kwamba dada aliyekuwa katika lile gari lingine aliokolewa pia.
Watu walisubiri kwa hamu nyingi arusi ya Kohei na Yuko, iliyopangwa kufanywa katika Jumba la Ufalme la Rikuzentakata siku ya Jumamosi, Machi 12. Baada ya hao wawili kusajili ndoa yao katika ukumbi wa jiji siku ya Ijumaa, tetemeko likatukia. Kohei alisikia tangazo la onyo la tsunami na akakimbilia eneo lililoinuka. Akumbuka, “Sikuamini nilipolitazama jiji. Hakuna chochote kilichobaki isipokuwa majengo machache makubwa. Hadi wakati huo, hangaiko langu kuu lilikuwa mipango ya arusi yetu, lakini nikatambua kwamba jambo kubwa zaidi lilikuwa limetukia.”
Kohei na Yuko walitumia Jumamosi hiyo wakiwasaidia ndugu na dada katika kutaniko. “Tulipokea misaada kutoka kwa makutaniko jirani,” asema Kohei. “Nilifurahi sana kumsikia mke wangu akisema jinsi alivyohisi vizuri kwa kutumia wakati na nguvu zake kuwasaidia akina ndugu. Nilimshukuru Yehova kwa kunipa mke mzuri hivyo. Tsunami ilifagilia mbali nyumba yetu mpya, gari letu, na vitu vyetu vyote. Lakini nathamini sana upendo ambao akina ndugu walituonyesha.”
Kuandaa Msaada wa Kimwili, Kiroho, na Kihisia. Mara moja, ofisi ya tawi ya Japani ilipanga Halmashauri tatu za Kutoa Misaada na wawakilishi wa ofisi ya tawi walitumwa tena na tena katika maeneo yaliyoathiriwa. Waangalizi wa eneo Geoffrey Jackson na Izak Marais kutoka makao makuu walipoitembelea nchi hiyo mwezi wa Mei, vilevile walikutana na ndugu na dada kutoka maeneo yaliyoathiriwa zaidi. Mkutano wa pekee kwa ajili ya makutaniko yaliyoathiriwa ulipangwa, Majumba ya Ufalme 21 yaliunganishwa kwa simu na hivyo ndugu wapatao 2,800 wakahakikishiwa kwamba ndugu zao ulimwenguni pote wanawapenda na wanawahangaikia.
Ndugu wa Halmashauri za Kutoa Misaada na wajitoleaji wengine wamefanya kazi kwa bidii. Vitu vilivyohitajiwa mara moja ni chakula, maji, na fueli. Halmashauri za misaada zilifanya pia mipango ya kutuma nguo za vipimo mbalimbali kwa makutaniko yaliyoathiriwa. Maeneo ya mikutano yalikuwa kama “maduka ya kuuzia nguo” ambapo ndugu wangepata mavazi waliyohitaji.
Ndugu na dada walioathiriwa walifurahi kama nini kuona jinsi Yehova alivyotosheleza mahitaji yao ya kimwili na kihisia! Walitiwa nguvu hasa walipohudhuria mikutano ya Kikristo. Dada mmoja kutoka eneo la msiba aliandika hivi, “Ninapata amani ya akili ninapohudhuria mikutano. Mikutano ndiyo uti wa mgongo wa maisha yangu ya Kikristo.”
Ujumbe wa Tumaini. Ndugu wa Japani hawakupoteza wakati kutumia Neno la Mungu kuwafariji majirani wao waliokuwa wamefadhaika. Kikundi cha wahubiri katika mji fulani ambao haukuathiriwa waliamua kuhubiri barabarani wakiwa na bango kubwa lenye maandishi, “Kwa Nini Msiba Huu Umetukia? Biblia ina jibu.” Watu wengi walipendezwa, na kwa siku moja na nusu tu, ndugu waliwapa watu nakala 177 za kitabu Biblia Inafundisha.
Katika maeneo yaliyoathiriwa, Mashahidi waliwatembelea kwanza wanafunzi wa Biblia, watu waliowarudia, na kisha majirani ili kuwafariji. Akiko asema: “Nilipomsomea mwenye nyumba fulani andiko la Mathayo 6:34, alianza kulia. Inaonekana kulikuwa na mambo mengi yaliyomhangaisha. Nilipomweleza jinsi Biblia inavyotusaidia kudumisha amani ya akili, alikubaliana nami na akanishukuru. Jambo hilo limefanya nithamini upya jinsi Maandiko yalivyo na nguvu za kufikia mioyo ya watu.”
Mwanamume mmoja alisema: “Kuna dini nyingi, lakini ni ninyi tu ambao mmetutembelea, hata katika nyakati hizi mbaya.” Mwingine akasema hivi kwa heshima, “Inashangaza kwamba mnaendelea na utendaji wenu hata wakati wa msiba huu.” Naye mzee mmoja wa kutaniko alisema: “Watu wengi walitukaribisha. Walisema, ‘Ninyi ndio watu wa kwanza kuja kwetu tangu tetemeko litukie. Tafadhali rudini tena.’”
-
-
Matukio Muhimu ya Mwaka Uliopita2012 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Picha katika ukurasa wa 18]
◀ Jumba la Ufalme mjini Rikuzentakata, Japani
[Picha katika ukurasa wa 22]
Juu: Wajitoleaji wakibeba vifusi kutoka nyumba ya ndugu fulani huko Shibata, Miyagi
[Picha katika ukurasa wa 22]
Kushoto: Mshiriki wa Halmashauri ya Tawi akitoa hotuba katika nyumba ya ndugu huko Rikuzentakata
[Picha katika ukurasa wa 22]
Chini: Wajitoleaji wakiwatayarishia wahudhuriaji chakula cha mchana wakati wa kusanyiko la pekee katika eneo lililoathiriwa
-