-
Kwa Nini Uhalifu Uliopangwa Unasitawi?Amkeni!—1997 | Machi 8
-
-
Wakati yakuza walipoona jinsi ilivyo rahisi kukopa na kuchuma pesa katika miaka ya 80, wao walianzisha kampuni nyingi na kujitosa katika biashara za nyumba na za kukisia-kisia hisa za biashara. Mashirika ya benki na ya kifedha yalitumia fedha nyingi katika kampuni hizo, bila shaka yakinuia kupata faida. Lakini uchumi ulipozorota, benki hizo zilipata ugumu sana wa kurudisha fedha zao. Akizungumzia uchumi unaozorota katika Japani, aliyekuwa ofisa wa polisi alisema, katika Newsweek: “Sababu yenyewe inayofanya matatizo ya kutolipa mkopo kwa wakati yasisuluhishwe haraka ni kwamba sehemu kubwa ya mikopo hiyo imehusika na uhalifu uliopangwa.”
-
-
Kwa Nini Uhalifu Uliopangwa Unasitawi?Amkeni!—1997 | Machi 8
-
-
Mfumo Bandia wa Familia
Kwa kuongezea mahitaji ya utendaji haramu, kuna mahitaji mengine leo ambayo husitawisha uhalifu uliopangwa. Kiongozi mmoja aliyekufa majuzi wa mojawapo ya magenge makubwa zaidi ya yakuza katika Japani alisisitiza kwamba yeye alikuwa akiwachukua wahalifu na kuwatunza na hivyo akiwafanya wasiwe wabaya zaidi. Alidai kwamba yeye alikuwa baba ya washiriki wa genge hilo. Magenge mengi ya uhalifu, hata yawe ya taifa gani, hujenga magenge yao kwenye uhusiano bandia wa familia.
Chukua mfano wa Chi Sun,a aliyetoka katika familia maskini katika Hong Kong. Mara nyingi baba yake alimpiga sana kwa visababu vidogo-vidogo. Chi Sun mchanga akawa mwasi akajiunga na ule Utatu mashuhuri akiwa na umri wa miaka 12. Katika genge la uhalifu, alipata mahali ambapo alihisi “amestarehe.” Kwa sababu ya ujasiri wake katika mapigano ya silaha, upesi alipandishwa cheo na kusimamia watu kadhaa. Hatimaye alipokuwa na umri wa miaka 17 tu, alifungwa gerezani.
Wengi kama Chi Sun hugeukia magenge ya uhalifu ili kupata upendo wa familia ambao walikosa nyumbani. Washiriki hudai kuwa wanajali, lakini mara nyingi wachanga hutamauka wapatapo kwamba kila mshiriki hasa anajipenda mwenyewe.
Malaika wa Nuru
Wakati genge kubwa zaidi la uhalifu katika Japani lilipotajwa kuwa kikundi chenye jeuri chini ya sheria mpya dhidi ya magenge katika 1992, mmojawapo viongozi walo alidai kwamba kikundi hicho kilijiona kuwa chenye “kuheshimika,” kikipambana na maovu. Lile tetemeko kali la dunia lilipopiga Kobe katika 1995, genge hilohilo liligawanya chakula, maji, na bidhaa nyinginezo za dharura kwa majirani wao. “Ukarimu kama huo,” likaripoti Asahi Evening News, “bila shaka utaimarisha mwonekano wa yakuza kuwa wahalifu wenye kuheshimika.”
-
-
Kwa Nini Uhalifu Uliopangwa Unasitawi?Amkeni!—1997 | Machi 8
-
-
Kwa njia hiyohiyo, katika sehemu za Mashariki yakuza mmoja mchanga ambaye yuko tayari kuwa ngao kwa mkubwa wake asema: “Nyumbani nilikuwa peke yangu pindi zote. Ingawa tulikuwa familia, sikuhisi kamwe kwamba tungeweza kuzungumza kutoka moyoni. . . . Lakini sasa naweza kuzungumza kutoka moyoni na watu hawa.” Vijana wapweke huwashukuru sana washiriki wa genge la uhalifu ambao huwaingiza katika mfumo ulio kama wa familia.
“Watu wa yakuza ni wenye kujali sana, sana,” asema kiongozi wa kikundi cha waendesha-pikipiki wasichana katika Okinawa. “Labda huo ndio ujanja wao; lakini, kwa kuwa hatujapata kutendewa kwa ungwana, jambo hilo hutuvutia.” Mkuu mmoja wa makao ya wasichana wahalifu athibitisha kwamba majambazi “wanajua sana kunasa mioyo ya wasichana.” Wasichana wapweke wawaitapo usiku wa manane, majambazi hao huenda upesi kuwasaidia na kusikiliza yote watakayosema, bila kujaribu kuwatongoza.
-
-
Ulimwengu Usio na Uhalifu Utapatikanaje?Amkeni!—1997 | Machi 8
-
-
Katika Japani serikali ilikaba yakuza ilipoanzisha Sheria Dhidi ya Uhalifu Uliopangwa mnamo Machi 1, 1992. Chini ya sheria hii, mara shirika la majambazi ambalo limetajwa kuwa genge la uhalifu uliopangwa, linazuiwa kufanya matendo 11 ya kulazimisha mambo kijeuri, kutia ndani kudai pesa kwa vitisho, kushiriki katika hila za ulinzi, na mwingilio wa kusuluhisha mizozo kwa kulipwa fedha kiasi fulani. Kwa kutekeleza sheria hii, serikali inanuia kukomesha vyanzo vyote vya mapato ya magenge. Sheria hiyo imepiga vibaya magenge ya uhalifu. Vikundi fulani vimevunjika, na kiongozi mmoja wa uhalifu akajiua—yaonekana kwa sababu ya kutekelezwa sana kwa sheria.
-
-
Ulimwengu Usio na Uhalifu Utapatikanaje?Amkeni!—1997 | Machi 8
-
-
Kwa mhuni kuacha genge la yakuza, anahitajika kulipa pesa nyingi au kidole chake kidogo au sehemu yacho ikatwe.
-
-
Naacha Uhalifu Uliopangwa—“Nilikuwa Yakuza”Amkeni!—1997 | Machi 8
-
-
Naacha Uhalifu Uliopangwa—“Nilikuwa Yakuza”
“BABA, niahidi kwamba ukirudi nyumbani tutaenda mikutano pamoja.” Nilipokea barua hii kutoka kwa binti yangu wa pili nilipokuwa gerezani kwa mara ya tatu. Alikuwa akihudhuria kwa ukawaida mikutano ya Mashahidi wa Yehova pamoja na mke wangu. Kwa kuwa barua kutoka kwa familia yangu ndizo zilizokuwa chanzo cha pekee cha faraja, nilimwahidi kwamba nitafanya atakavyo.
‘Kwa nini ninaishi maisha ya uhalifu yanayonitenganisha na familia yangu?’ Nikawaza. Nikakumbuka siku ambazo nilikuwa mchanga sana. Baba alikufa nikiwa na miezi 18 pekee, kwa hiyo hata sikumbuki sura yake. Mama aliolewa mara mbili baadaye. Hali hizo za familia ziliniathiri kabisa, na nikiwa katika shule ya sekondari, nilianza kushirikiana na wahuni. Nikawa mjeuri na mara nyingi nilihusika katika mapigano nje ya shule. Katika mwaka wangu wa pili wa shule ya sekondari, nilipanga kikundi cha wanafunzi kipigane na kikundi kingine. Tokeo likawa kwamba nilikamatwa na kupelekwa shule ya kurekebisha tabia kwa muda fulani.
Nilikuwa kama mpira unaoteremka bondeni kwenye maisha ya ujeuri. Upesi nikafanyiza kikundi cha vijana wahalifu na tulikuwa tukikaa-kaa karibu na ofisi ya kikundi cha yakuza. Nilipokuwa na umri wa miaka 18, nikawa mshiriki kamili wa kikundi hicho. Nilipokuwa na umri wa miaka 20, nilikamatwa kwa sababu ya vitendo mbalimbali vya jeuri nikahukumiwa kifungo cha miaka mitatu gerezani. Kwanza, nilifungwa katika Gereza la Watoto la Nara, lakini tabia yangu haikuboreka. Basi nikahamishwa hadi gereza jingine, la watu wazima. Lakini nikawa mbaya zaidi na hatimaye nikaishia Kyoto katika gereza la wahalifu sugu.
‘Kwa nini naendelea kutenda uhalifu?’ Nikajiuliza. Nikikumbuka, natambua kwamba ilikuwa ni kwa sababu ya kusababu kwangu kwa ujinga. Wakati huo, nilidhani kwamba tabia kama hiyo ilikuwa ya kiume, uthibitisho wa kwamba nilikuwa mwanamume. Nilipofunguliwa kutoka gerezani nikiwa na umri wa miaka 25, wahuni wenzangu walinistahi sana. Sasa njia ilikuwa wazi ya kupanda cheo katika ulimwengu wa uhalifu.
Itikio la Familia Yangu
Nilifunga ndoa karibu na wakati huo, na upesi tukapata binti wawili. Lakini maisha yangu hayakubadilika. Nikaendelea kukamatwa-kamatwa na polisi—nilikuwa nikipiga watu na kuwanyang’anya pesa. Kila tukio lilifanya nistahiwe zaidi na majambazi wenzangu na kufanya nitumainiwe na kiongozi. Hatimaye, “ndugu” yangu mkubwa kwa yakuza akawa ndiye kiongozi wa genge. Nikachachawa kwa kupandishwa cheo kuwa naibu wake.
‘Mke wangu na binti zangu wanahisije juu ya njia yangu ya maisha?’ Nikawaza. Ni lazima waliaibika kwamba mume aliye pia baba alikuwa mhalifu. Nilifungwa tena nikiwa na umri wa miaka 30 na tena nikiwa na miaka 32. Wakati huu kifungo changu cha miaka mitatu kilikuwa kigumu kuvumilia. Binti zangu hawakuruhusiwa kunizuru. Nilitamani kusema nao na kuwakumbatia.
Karibu na wakati nilipofungwa mara ya mwisho, mke wangu alianza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Kila siku aliniandikia kuhusu kweli aliyokuwa akijifunza. ‘Hii kweli ambayo mke wangu anazungumzia ni nini?’ Nikajiuliza. Nikasoma Biblia nzima nikiwa gerezani. Nikafikiria yale ambayo mke wangu alikuwa akisema katika barua zake kuhusu tumaini fulani la wakati ujao na kuhusu kusudi la Mungu.
Tumaini la wanadamu kuishi milele katika Paradiso duniani lilinivutia sana kwa sababu nilihofu sana kifo. Sikuzote nimefikiria, ‘Ukifa, umeshindwa.’ Sasa nikikumbuka, natambua kwamba ilikuwa ni hofu ya kifo ambayo ilinisukuma kuwajeruhi wengine kabla hawajanijeruhi. Barua za mke wangu pia zilinifanya nione ubatili wa lengo langu la kutaka kupanda cheo katika genge.
Na bado, sikuchochewa kujifunza kweli. Mke wangu alijiweka wakfu kwa Yehova na kuwa mmoja wa Mashahidi wake waliobatizwa. Ingawa katika barua yangu nilikuwa nimekubali kwenda mikutano yao, sikuwa nimenuia kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Nilihisi kana kwamba mke wangu na binti zangu wameenda mbali, wakiniacha peke yangu.
Naondoka Gerezani
Hatimaye siku ikafika ya kuwa huru. Kwenye malango ya Gereza la Nagoya, majambazi wengi walipiga foleni kunikaribisha. Hata hivyo katikati ya umati mkubwa wa watu nilikuwa nikiwatafuta tu mke wangu na binti zangu. Kuwaona binti zangu, ambao walikuwa wamekua haraka katika miaka mitatu na miezi sita, nikalia machozi.
Siku mbili baada ya kurudi nyumbani, nilitimiza ahadi yangu kwa binti yangu wa pili kwa kuhudhuria mkutano wa Mashahidi wa Yehova. Nilishangaa kuona mtazamo mchangamfu wa wote waliohudhuria. Mashahidi walinikaribisha kwa uchangamfu, lakini nikahisi sifai mahali hapo. Baadaye nilishangaa nilipojua kwamba wale waliokuwa wamenisalimu walijua juu ya historia yangu ya uhalifu. Lakini, nilihisi uchangamfu wao nami nilivutiwa na hotuba yenye kutegemea Biblia iliyotolewa. Ilikuwa juu ya watu kuishi milele katika Paradiso kwenye dunia.
Wazo la kwamba ni mke wangu na binti zangu watakaookoka na kuingia katika Paradiso nami niangamizwe milele lilinihuzunisha sana. Nikatafakari sana juu ya kile nilichohitaji kufanya ili kuishi milele pamoja na familia yangu. Nikaanza kufikiria kuacha maisha ya ujambazi, nikaanza kujifunza Biblia.
Kuacha Maisha Yangu ya Uhalifu
Niliacha kuhudhuria mikutano ya genge na kuacha kushirikiana na yakuza. Haikuwa rahisi kubadili njia yangu ya kufikiri. Niliendesha gari kubwa lililotoka nchi za nje kwa kujifurahisha tu—ilikuwa ni safari ya kujionyesha. Ilinichukua miaka mitatu kubadili gari langu kwa gari la kawaida. Pia nilikuwa na mwelekeo wa kutafuta njia rahisi zaidi ya kufanya mambo. Lakini, nilipokuwa nikijifunza kweli niliweza kuona kwamba ni lazima nibadilike. Lakini kama Yeremia 17:9 lisemavyo, “moyo huwa mdanganyifu kuliko vitu vyote, una ugonjwa wa kufisha.” Nilijua yaliyo sawa lakini nilikuwa napata ugumu wa kutumia niliyokuwa nikijifunza. Matatizo niliyokabili yalionekana kama mlima mkubwa. Nikawa na matatizo, na nyakati nyingi nilifikiria kuacha kujifunza na kuacha kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova.
Ndipo, mwenye kuongoza funzo langu la Biblia alialika mwangalizi asafiriye aliyekuwa na malezi kama yangu aje kutoa hotuba ya watu wote katika kutaniko letu. Akatoka Akita, umbali wa kilometa 600, kuja Suzuka ili kunitia moyo. Baadaye nilipohisi nimechoka na kufikiria kuacha, ningepokea barua yake, akiniuliza kama nilikuwa nikitembea kwa uthabiti katika njia ya Bwana.
Niliendelea kusali kwa Yehova anipe msaada wa kuacha yakuza. Nilikuwa na uhakika kwamba Yehova atajibu sala yangu. Mnamo, Aprili 1987, hatimaye niliweza kuacha genge la yakuza. Kwa kuwa biashara yangu mwenyewe ilikuwa ikinipeleka ng’ambo kila mwezi, mbali na familia, nilibadili kazi yangu ili nifanye kazi ya bawabu. Jambo hilo lilifanya nipate vipindi vya alasiri kwa utendaji wa kiroho. Kwa mara ya kwanza, nilipokea bahasha ya mshahara. Haikuwa na pesa nyingi, lakini nilifurahi sana.
Nilipokuwa mtu wa pili katika genge la yakuza, nilikuwa na pesa nyingi, lakini sasa nina mali za kiroho ambazo hazipotei. Namjua Yehova. Nayajua makusudi yake. Nina kanuni za kufuata. Nina marafiki wa kweli wenye kujali. Katika ulimwengu wa yakuza, majambazi walikuwa wakionekana kijuu-juu kuwa wenye kujali, lakini hakuna yakuza niliyemjua, hata mmoja, ambaye angejidhabihu kwa ajili ya wengine.
Katika Agosti 1988, nilionyesha wakfu wangu kwa Yehova kwa ubatizo wa maji, na mwezi uliofuata, nikaanza kutumia angalau muda wa saa 60 kwa mwezi nikiambia wengine kuhusu habari njema ambazo zilikuwa zimebadili maisha yangu. Nimetumikia nikiwa mhudumu wa wakati wote tangu Machi 1989 na sasa nimepewa pendeleo la kutumikia nikiwa mtumishi wa huduma katika kutaniko.
Niliweza kuondoa alama nyingi za maisha yangu ya yakuza. Lakini kuna moja ambayo inabaki. Ni mchoro ulio mwilini mwangu ambao hunikumbusha, na vilevile familia yangu na wengine, juu ya maisha yangu yaliyopita ya yakuza. Pindi moja, binti yangu mkubwa alikuja nyumbani akilia, akisema kwamba hataenda shuleni tena kwa sababu marafiki wake walimwambia kwamba mimi nilikuwa yakuza na nina mchoro mwilini. Niliweza kuzungumzia jambo hilo kabisa na binti zangu, nao wakaelewa hali hiyo. Natazamia siku ambayo dunia itakuwa paradiso na nyama yangu itakuwa “laini kuliko ya mtoto.” Kisha mchoro wangu na kumbukumbu za maisha yangu ya miaka 20 ya yakuza zitakuwa mambo yaliyopita. (Ayubu 33:25; Ufunuo 21:4)—Kama ilivyosimuliwa na Yasuo Kataoka.
-