-
Yehova Hatawaacha Washikamanifu WakeMnara wa Mlinzi—2008 | Agosti 15
-
-
Wanapotimiza Migawo Ambayo Wamepewa na Mungu
16. Nabii fulani kutoka Yuda alipewa mgawo gani?
16 Yehova alimhukumu Yeroboamu kwa sababu ya uasi-imani. Yehova alimtuma nabii fulani kutoka Yuda aende kaskazini mpaka Betheli ili amwone Yeroboamu alipokuwa akifukiza moshi wa dhabihu kwenye madhabahu. Nabii huyo alipaswa kumpa Yeroboamu ujumbe wa hukumu wenye kushtua. Bila shaka, huo ulikuwa mgawo mgumu.—1 Fal. 13:1-3.
17. Yehova alimlinda mjumbe wake jinsi gani?
17 Yeroboamu alikasirika sana aliposikia hukumu ya Yehova. Akamnyooshea mkono mwakilishi wa Mungu na kuwapaazia sauti wanaume waliokuwa karibu, akisema: “Mkamateni!” Lakini papo hapo, kabla mtu yeyote hajatenda, ‘mkono aliomnyooshea ukapooza, naye hakuweza kuurudisha nyuma kwake. Na ile madhabahu ikapasuka hivi kwamba majivu yenye mafuta yakamwagika kutoka katika madhabahu.’ Yeroboamu alilazimika kumwomba nabii huyo autulize uso wa Yehova na kusali ili mkono huo uliopooza uponywe. Nabii huyo alifanya hivyo, na mkono ukapona. Hivyo, Yehova alimlinda mjumbe wake asipatwe na madhara.—1 Fal. 13:4-6.
-
-
Dumisha Ushikamanifu Ukiwa na Moyo KamiliMnara wa Mlinzi—2008 | Agosti 15
-
-
Tunaweza kujifunza masomo ya maana kutokana na yale yaliyompata nabii fulani kutoka Yuda aliyetumwa na Yehova kwa Mfalme Yeroboamu wa Israeli.
“Nikupe Zawadi”
3. Yeroboamu alitenda jinsi gani aliposikia ujumbe wa hukumu uliotolewa na nabii wa Mungu?
3 Fikiria tamasha hii. Mtu wa Mungu ametoka tu kutoa ujumbe mzito kwa Mfalme Yeroboamu, ambaye alianzisha ibada ya ndama katika ufalme wa kaskazini wa Israeli wa makabila kumi. Mfalme anakasirika. Anaamuru wanaume wake wamkamate mjumbe huyo. Lakini Yehova yuko pamoja na mtumishi wake. Papo hapo, mkono ambao mfalme amenyoosha kwa hasira unapooza kimuujiza, na madhabahu inayotumiwa kwa ajili ya ibada ya uwongo inapasuka katika sehemu mbili. Kwa ghafula, mtazamo wa Yeroboamu unabadilika. Anamsihi hivi mtu wa Mungu: “Tafadhali, utulize uso wa Yehova Mungu wako, na kusali kwa ajili yangu ili nirudishiwe mkono wangu.” Nabii huyo anasali, na mkono wa mfalme unapona.—1 Fal. 13:1-6.
4. (a) Kwa nini mwaliko wa mfalme ulijaribu ushikamanifu wa nabii huyo? (b) Nabii huyo alijibu nini?
4 Kisha Yeroboamu anamwambia hivi huyo mtu wa Mungu wa kweli: “Njoo pamoja nami twende nyumbani ule chakula, nami nikupe zawadi.” (1 Fal. 13:7) Sasa nabii huyo atafanya nini? Je, akubali ukarimu wa mfalme baada ya kumtangazia ujumbe wa hukumu? (Zab. 119:113) Au akatae mwaliko wa mfalme, hata ingawa mfalme anaonekana ametubu? Bila shaka, Yeroboamu ni tajiri na anaweza kuwapa marafiki wake zawadi za bei ghali. Ikiwa nabii huyo wa Mungu ana tamaa yoyote moyoni mwake kuelekea vitu vya kimwili, inaelekea mwaliko huo wa mfalme utakuwa kishawishi kikubwa kwake. Hata hivyo, Yehova amemwamuru nabii huyo hivi: “Usile mkate wala usinywe maji, nawe usirudi kwa njia ile uliyoiendea.” Kwa hiyo, nabii huyo anajibu hivi kwa uthabiti: “Hata ukinipa nusu ya nyumba yako, siwezi kwenda pamoja nawe na kula mkate au kunywa maji mahali hapa.” Kisha nabii huyo anatoka Betheli kupitia njia nyingine. (1 Fal. 13:8-10) Uamuzi wa nabii huyo unatufundisha somo gani kuhusu ushikamanifu unaotoka moyoni?—Rom. 15:4.
‘Uwe Mwenye Kuridhika’
5. Kupenda vitu vya kimwili kunajaribu ushikamanifu wetu jinsi gani?
5 Huenda kupenda vitu vya kimwili kusionekane kuwa jambo linalojaribu ushikamanifu wetu, lakini ni jaribu la ushikamanifu. Je, tunaamini ahadi ya Yehova ya kutuandalia mambo ambayo kwa kweli tunahitaji? (Mt. 6:33; Ebr. 13:5) Badala ya kutumia njia yoyote ile ili kupata vitu fulani vya kimwili vyenye kustarehesha ambavyo hatuna uwezo wa kuvipata kwa sasa, je, inawezekana tuishi bila vitu hivyo? (Soma Wafilipi 4:11-13.) Je, tunashawishiwa kuacha mapendeleo ya kitheokrasi ili tupate vitu tunavyotaka sasa? Je, tunatanguliza utumishi mshikamanifu kwa Yehova katika maisha yetu? Majibu yetu yatategemea sana ikiwa tunamtumikia Mungu kwa moyo wetu wote au hapana. Mtume Paulo aliandika hivi: “Ni njia ya kupata faida kubwa, huu ujitoaji-kimungu pamoja na ujitoshelevu. Kwa maana hatukuleta chochote katika ulimwengu, wala hatuwezi kuchukua chochote nje. Kwa hiyo, tukiwa na chakula na kitu cha kujifunika, tutaridhika na vitu hivyo.”—1 Tim. 6:6-8.
6. Tunaweza kuahidiwa “zawadi” gani, na ni jambo gani litakalotusaidia kuamua ikiwa tutazikubali?
6 Kwa mfano, huenda mwajiri wetu wa kazi anataka kutupandisha cheo kazini, kutuongezea mshahara, na kutupa faida nyingine. Au labda tunaona kwamba tunaweza kupata pesa nyingi zaidi ikiwa tutahamia nchi nyingine au eneo lingine ili kupata kazi. Mwanzoni, nafasi hizo zinaweza kuonekana kuwa baraka kutoka kwa Yehova. Lakini kabla ya kufanya uamuzi, tunapaswa kuchunguza nia yetu. Swali kuu tunalopaswa kujiuliza ni: “Uamuzi wangu utakuwa na matokeo gani kuelekea uhusiano wangu pamoja na Yehova?”
7. Kwa nini ni jambo la maana kung’oa kabisa katika mioyo yetu tamaa ya kupenda vitu vya kimwili?
7 Mfumo wa Shetani unawatia watu moyo sana kupenda vitu vya kimwili. (Soma 1 Yohana 2:15, 16.) Kusudi la Ibilisi ni kuharibu mioyo yetu. Hivyo, tunahitaji kuwa macho ili kutambua na kung’oa kabisa katika mioyo yetu tamaa ya kupenda vitu vya kimwili. (Ufu. 3:15-17) Yesu alikataa kwa uthabiti falme zote za ulimwengu ambazo Shetani alitaka kumpa. (Mt. 4:8-10) Alionya hivi: “Endeleeni kufungua macho yenu na mjilinde na kila namna ya tamaa, kwa sababu hata wakati mtu ana vitu vingi uzima wake hautokani na vitu alivyo navyo.” (Luka 12:15) Ushikamanifu utatusaidia kumtegemea Yehova badala ya kujitegemea wenyewe.
Nabii Fulani Mzee “Alimdanganya”
8. Ushikamanifu wa nabii wa Mungu ulijaribiwa jinsi gani?
8 Mambo yangemwendea vizuri nabii wa Mungu ikiwa angeendelea na safari yake ya kurudi nyumbani. Hata hivyo, punde tu baadaye, alikabili jaribu lingine. Biblia inasema hivi: “Nabii fulani mzee alikuwa akikaa Betheli, na wanawe wakaja na kumsimulia” mambo yote yaliyotendeka mapema siku hiyo. Anaposikia habari hiyo, mwanamume huyo mzee anawaomba wanawe wamtandikie punda ili amfuate nabii wa Mungu. Punde si punde, anamkuta nabii huyo akipumzika chini ya mti mkubwa na kumwambia: “Njoo pamoja nami nyumbani, ule mkate.” Mtu wa Mungu wa kweli anapokataa mwaliko huo, mwanamume huyo mzee anasema: “Mimi pia ni nabii kama wewe, na malaika alisema nami kwa neno la Yehova hivi, ‘Mrudishe pamoja nawe nyumbani kwako ili ale mkate na anywe maji.’” Lakini Maandiko yanasema: “Alimdanganya.”—1 Fal. 13:11-18.
9. Maandiko yanasema nini kuhusu wadanganyifu, nao wanawadhuru nani?
9 Hata ingawa hatujui nia ya nabii huyo mzee, ukweli ni kwamba alidanganya. Labda wakati fulani mwanamume huyo mzee alikuwa nabii mwaminifu wa Yehova. Hata hivyo, wakati huu, alikuwa akidanganya. Maandiko yanashutumu vikali mwenendo kama huo. (Soma Methali 3:32.) Wadanganyifu wanaharibu hali yao wenyewe ya kiroho na mara nyingi wanawadhuru wengine kiroho.
“Akarudi Pamoja” na Yule Mwanamume Mzee
10. Nabii wa Mungu alitenda jinsi gani alipoalikwa na mwanamume mzee, na matokeo yalikuwa nini?
10 Nabii huyo kutoka Yuda alipaswa kutambua ujanja wa nabii huyo mzee. Alipaswa kujiuliza, ‘Kwa nini Yehova anamtuma malaika kwa mtu mwingine akiwa na maagizo tofauti kwa ajili yangu?’ Nabii huyo angemwomba Yehova afafanue mwongozo huo waziwazi, lakini Maandiko hayaonyeshi kwamba alifanya hivyo. Badala yake, ‘alirudi pamoja na yule mwanamume mzee ili ale mkate nyumbani kwake na kunywa maji.’ Yehova hakufurahi. Mwishowe, nabii aliyedanganywa alipokuwa njiani akirudi Yuda, alikutana na simba na simba huyo akamuua. Huo ulikuwa mwisho wenye kusikitisha kama nini kwa kazi yake akiwa nabii!—1 Fal. 13:19-25.a
11. Ahiya aliweka mfano gani mzuri?
11 Kwa upande mwingine, nabii Ahiya, aliyetumwa kumtia mafuta Yeroboamu ili awe mfalme, alibaki mwaminifu hata alipokuwa mzee. Ahiya alipozeeka na kuwa kipofu, Yeroboamu alimtuma mke wake amuulize Ahiya kuhusu hali ya mwana wao aliyekuwa mgonjwa. Kwa ujasiri, Ahiya alitabiri kwamba mwana wa Yeroboamu angekufa. (1 Fal. 14:1-18) Ahiya alipata baraka nyingi kutia ndani pendeleo la kuchangia habari iliyotumiwa kuandika Neno la Mungu lililoongozwa na roho. Jinsi gani? Baadaye, kuhani Ezra alitumia maandishi ya Ahiya kuwa chanzo cha habari yake.—2 Nya. 9:29.
12-14. (a) Tunaweza kujifunza somo gani kutokana na yale yaliyompata yule nabii kijana? (b) Toa mifano inayoonyesha uhitaji wa kusali na kufikiria kwa uzito mashauri yanayotegemea Biblia ambayo yanatolewa na wazee.
12 Biblia haisemi kwa nini nabii huyo kijana hakumuuliza Yehova kabla ya kurudi kula na kunywa pamoja na nabii yule mzee. Je, inawezekana kwamba yule mwanamume mzee alimweleza nabii huyo mambo ambayo alitaka kusikia? Tunapata somo gani hapa? Tunapaswa kusadiki kabisa kwamba matakwa ya Yehova ni ya uadilifu. Na tunapaswa kuazimia kuyafuata kwa vyovyote vile.
13 Wengine wanataka kusikia tu mashauri ambayo yanawapendeza. Kwa mfano, huenda mhubiri akapewa kazi itakayochukua wakati ambao anaweza kutumia pamoja na familia yake na katika utendaji wa kitheokrasi. Huenda akamwomba mzee wa kutaniko mashauri. Pengine mzee huyo anaweza kuanza kwa kumweleza kwamba si daraka lake kumwambia ndugu huyo jinsi anavyopaswa kuitunza familia yake. Kisha huenda mzee huyo akazungumza na ndugu huyo kuhusu hatari za kiroho zinazohusika katika kukubali kazi ambayo amepewa. Je, ndugu huyo atakumbuka tu maelezo ya kwanza yaliyotolewa na mzee huyo, au atafikiria kwa uzito maelezo ya pili? Ni wazi kwamba ndugu huyo anahitaji kuamua jambo litakalomfaidi zaidi kiroho.
14 Fikiria mfano mwingine. Huenda dada fulani akamuuliza mzee wa kutaniko ikiwa anapaswa kutengana na mume wake asiyeamini. Bila shaka, mzee atamweleza kwamba ni juu yake kuamua ikiwa atatengana na mume wake. Kisha mzee huyo anaweza kumwonyesha mashauri ya Biblia kuhusu habari hiyo. (1 Kor. 7:10-16) Je, dada huyo atafikiria kwa uzito yale ambayo mzee huyo anasema? Au tayari ameamua kutengana na mume wake? Dada huyo anapofanya uamuzi, itakuwa vizuri kwake kusali na kufikiria mashauri yanayotegemea Biblia.
Uwe Mwenye Kiasi
15. Tunajifunza nini kutokana na kosa la nabii wa Mungu?
15 Tunaweza kujifunza jambo gani lingine kutokana na kosa lililofanywa na yule nabii kutoka Yuda? Andiko la Methali 3:5 linasema hivi: “Mtegemee Yehova kwa moyo wako wote wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe.” Badala ya kuendelea kumtegemea Yehova kama alivyofanya wakati uliopita, mara hii nabii huyo kutoka Yuda alitegemea akili zake mwenyewe. Kwa sababu ya kosa hilo, alipoteza uhai wake na uhusiano wake mzuri pamoja na Mungu. Mambo yaliyompata yanakazia vizuri sana umuhimu wa kuwa wenye kiasi na washikamanifu tunapomtumikia Yehova!
16, 17. Ni nini kitakachotusaidia kubaki washikamanifu kwa Yehova?
16 Mioyo yetu ina mwelekeo wa kichoyo unaoweza kutupotosha. “Moyo ni wenye hila kuliko kitu kingine chochote nao ni hatari.” (Yer. 17:9) Ili tubaki washikamanifu kwa Yehova, tunapaswa kuendelea kufanya bidii kuvua kabisa utu wa zamani pamoja na mielekeo yake, yaani, kimbelembele na kujitegemea. Na ni lazima tuvae utu mpya, “ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na ushikamanifu.”—Soma Waefeso 4:22-24.
17 Andiko la Methali 11:2 linasema kwamba “wenye kiasi wana hekima.” Kuwa wenye kiasi kwa kumtegemea Yehova kunatusaidia kuepuka kutenda makosa yanayoweza kutuletea hasara kubwa sana. Kwa mfano, kuvunjika moyo kunaweza kutuzuia tusifanye maamuzi mazuri. (Met. 24:10) Tunaweza kuchoshwa na sehemu fulani za utumishi mtakatifu na kuanza kuhisi kwamba tumetumikia vya kutosha kwa miaka mingi, na kufikiri kwamba tunapaswa kuwaachia wengine majukumu hayo. Au tunaweza kutamani kuwa na maisha ya “kawaida.” Hata hivyo, ‘tukijitahidi sana’ na tukiwa ‘sikuzote na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana’ tutailinda mioyo yetu.—Luka 13:24; 1 Kor. 15:58.
18. Tunaweza kufanya nini ikiwa hatujui uamuzi wa kufanya?
18 Nyakati nyingine, huenda tukahitaji kufanya maamuzi mazito, na huenda tusijue njia nzuri ya kufuata. Basi je, tutashawishiwa kufuata njia yetu wenyewe? Tunapojikuta katika hali kama hizo, ni jambo la hekima kumwomba Yehova atusaidie. Andiko la Yakobo 1:5 linasema hivi: “Ikiwa yeyote kati yenu anakosa hekima, na aendelee kumwomba Mungu, kwa maana yeye huwapa wote kwa ukarimu.” Baba yetu wa mbinguni atatupa roho takatifu tunayohitaji ili tuweze kufanya maamuzi mazuri.—Soma Luka 11:9, 13.
-