-
Yerusalemu—“Jiji la Yule Mfalme Mkubwa”Mnara wa Mlinzi—1998 | Oktoba 15
-
-
Yerusalemu—“Jiji la Yule Mfalme Mkubwa”
“Msiape . . . kwa Yerusalemu, kwa sababu ndilo jiji la yule Mfalme mkubwa.”—MATHAYO 5:34, 35.
-
-
Yerusalemu—“Jiji la Yule Mfalme Mkubwa”Mnara wa Mlinzi—1998 | Oktoba 15
-
-
Mahali pa ‘Kiti cha Enzi cha Yehova’
4, 5. Daudi alihusikaje katika kulisaidia Yerusalemu liwe na fungu kubwa katika kutimizwa kwa makusudi ya Mungu?
4 Katika karne ya 11 K.W.K., Yerusalemu lilipata kuwa jiji maarufu la taifa lenye usalama na amani. Yehova Mungu aliamuru kijana Daudi atiwe mafuta kuwa mfalme wa taifa hilo la kale—Israeli. Kwa kuwa makao ya serikali yalikuwa Yerusalemu, Daudi na wazao wake wa kifalme walikuja kukalia ‘kiti cha enzi cha ufalme wa Yehova,’ au ‘kiti cha enzi cha Yehova.’—1 Mambo ya Nyakati 28:5; 29:23.
5 Mwanamume Daudi mwenye kumhofu Mungu—Mwisraeli wa kabila la Yuda—aliteka Yerusalemu kutoka kwa Wayebusi wenye kuabudu sanamu. Wakati huo jiji hilo lilikuwa tu kwenye kilima kiitwacho Zayoni, lakini maana ya jina hilo ilikuja kuwa na maana sawa na jina Yerusalemu lenyewe. Halafu, Daudi akaamuru sanduku la agano la Mungu pamoja na Israeli, lihamishwe hadi Yerusalemu, ambapo liliwekwa katika hema. Miaka kadhaa mapema, Mungu alikuwa amesema na Musa nabii wake kutoka katika wingu juu ya Sanduku hilo takatifu. (Kutoka 25:1, 21, 22; Mambo ya Walawi 16:2; 1 Mambo ya Nyakati 15:1-3) Sanduku hilo lilifananisha kuwapo kwa Mungu, kwa maana Yehova ndiye aliyekuwa Mfalme halisi wa Israeli. Kwa hiyo, kwa usemi wenye maana maradufu, yaweza kusemwa kwamba Yehova Mungu alitawala kutoka jiji la Yerusalemu.
6. Yehova alitoa ahadi gani kuhusu Daudi na Yerusalemu?
6 Yehova alimwahidi Daudi kwamba ufalme wa ukoo wake wa kifalme, uliowakilishwa na Zayoni, au Yerusalemu, haungeisha. Hilo lilimaanisha kwamba mzao wa Daudi angerithi haki ya kutawala milele akiwa Mtiwa-Mafuta wa Mungu—Mesiya, au Kristo.a (Zaburi 132:11-14; Luka 1:31-33) Biblia pia hufunua kwamba mrithi huyo wa kudumu wa ‘kiti cha enzi cha Yehova’ angetawala juu ya mataifa yote, wala si Yerusalemu tu.—Zaburi 2:6-8; Danieli 7:13, 14.
7. Mfalme Daudi aliendelezaje ibada safi?
7 Jitihada za kumwondosha mamlakani Mfalme Daudi aliyekuwa mtiwa-mafuta wa Mungu, hazikufua dafu. Badala yake, mataifa maadui yalitiishwa, na mipaka ya Bara Lililoahidiwa iliyoonyeshwa na Mungu, ikapanuliwa kabisa. Daudi alitumia hali hiyo ili kuendeleza ibada safi. Nazo zaburi nyingi za Daudi humsifu Yehova kuwa ndiye Mfalme halisi wa Zayoni.—2 Samweli 8:1-15; Zaburi 9:1, 11; 24:1, 3, 7-10; 65:1, 2; 68:1, 24, 29; 110:1, 2; 122:1-4.
8, 9. Ibada ya kweli ilipanukaje katika Yerusalemu chini ya utawala wa Mfalme Solomoni?
8 Wakati wa utawala wa Solomoni mwana wa Daudi, ibada ya Yehova ilipanuliwa. Solomoni alipanua Yerusalemu kuelekea upande wa juu ili kutia ndani kilima Moria (eneo ambako siku hizi kuna jengo liitwalo Dome of the Rock). Kwenye eneo hilo lililoinuka zaidi, alipendelewa kujenga hekalu lenye fahari kwa sifa ya Yehova. Sanduku la agano liliwekwa katika Patakatifu Zaidi Sana pa hekalu.—1 Wafalme 6:1-38.
9 Taifa la Israeli lilifurahia amani lilipojitolea kwa moyo wote kwa ajili ya ibada ya Yehova, iliyokuwa na kitovu chake Yerusalemu. Maandiko yanafafanua hali hiyo kwa kutaarifu hivi: “Yuda na Israeli walikuwa wengi kama mchanga wa pwani kwa wingi, wakila, na kunywa, na kufurahi. . . . Naye [Solomoni] alikuwa na amani pande zake zote. Yuda na Israeli wakakaa salama, kila mtu chini ya mzabibu wake na chini ya mtini wake.”—1 Wafalme 4:20, 24, 25.
10, 11. Akiolojia inaungaje mkono yale ambayo Biblia husema juu ya Yerusalemu, Solomoni alipotawala?
10 Uvumbuzi wa kiakiolojia waunga mkono simulizi hilo la utawala wa Solomoni wenye ufanisi. Katika kitabu chake The Archaeology of the Land of Israel, Profesa Yohanan Aharoni ataarifu: “Mali iliyomiminika katika nyumba ya kifalme kutoka pande zote, na biashara yenye kusitawi . . . ilileta ukuzi wa haraka na wenye kuonekana katika kila sehemu ya utamaduni wa vitu vya kimwili. . . . Badiliko katika utamaduni wa vitu vya kimwili . . . laweza kuonekana wazi si katika vitu vya anasa tu bali pia hasa katika vyombo vya ufinyanzi. . . . Ubora wa vyombo hivyo vya ufinyanzi na ukaushaji wake kwa kutumia moto ulifanyiwa maendeleo yasiyo na kifani.”
11 Vivyo hivyo, Jerry M. Landay aliandika: “Chini ya Solomoni, utamaduni wa Israeli wa vitu vya kimwili ulisitawi zaidi kwa muda wa miongo mitatu kuliko vile ulivyokuwa umesitawi katika miaka mia mbili iliyotangulia. Katika tabaka ya ardhi ya nyakati za Solomoni twapata mabaki ya majengo makubwa sana, majiji makubwa yenye kuta kubwa sana, vuvumko la maskani yenye vikundi-vikundi vya makao ya matajiri yaliyojengwa vizuri, usitawi wa ufundi wa mfinyanzi na taratibu zake za utengenezaji. Pia twapata mabaki ya sanaa za bidhaa zilizotengenezewa sehemu za mbali sana, zikiwa ishara za kwamba kulikuwako biashara yenye juhudi ya kimataifa na ubadilishanaji wa bidhaa.”—The House of David.
Kutoka Hali ya Amani Hadi ya Ukiwa
12, 13. Ilikuwaje kwamba ibada ya kweli haikuendelezwa Yerusalemu?
12 Ilifaa kusali kwa ajili ya amani na ufanisi wa jiji la Yerusalemu, ambapo mahali patakatifu pa Yehova palikuwa. Daudi aliandika: “Utakieni Yerusalemu amani; na wafanikiwe wakupendao; amani na ikae ndani ya kuta zako, na kufanikiwa ndani ya majumba yako. Kwa ajili ya ndugu zangu na rafiki zangu niseme sasa, Amani ikae nawe.” (Zaburi 122:6-8) Ingawa Solomoni alipendelewa kujenga hekalu lenye fahari katika jiji hilo lenye amani, hatimaye alioa wake wengi wapagani. Alipokuwa mzee, walimshawishi aendeleze ibada ya miungu ya uwongo ya wakati huo. Uasi-imani huo ulikuwa na uvutano wenye kufisidi juu ya taifa zima, ukilinyima jiji hilo na wakaaji wake amani ya kweli.—1 Wafalme 11:1-8; 14:21-24.
13 Mapema katika utawala wa Rehoboamu mwana wa Solomoni, makabila kumi yaliasi na kufanyiza ufalme wa kaskazini wa Israeli. Kwa sababu ya kuabudu kwao sanamu, Mungu aliuruhusu ufalme huo upinduliwe na Ashuru. (1 Wafalme 12:16-30) Yerusalemu liliendelea kuwa kitovu cha ufalme wa kusini wa Yuda wenye makabila mawili. Lakini baada ya muda, wao pia wakaacha ibada safi, kwa hiyo Mungu akaachilia jiji hilo potovu liharibiwe na Wababiloni mwaka wa 607 K.W.K. Kwa miaka 70 wahamishwa Wayahudi waliteseka wakiwa mateka huko Babiloni. Kisha, kwa rehema ya Mungu, wakaruhusiwa kurudi Yerusalemu na kurudisha ibada ya kweli.—2 Mambo ya Nyakati 36:15-21.
14, 15. Yerusalemu lilipataje tena kuwa na fungu muhimu baada ya uhamisho wa Babiloni, lakini kukiwa na badiliko gani?
14 Baada ya miaka 70 ya ukiwa, ni lazima majengo yaliyoharibiwa yawe yalifunikwa kwa magugu. Ukuta wa Yerusalemu ulibomolewa, kukiwa na mianya mikubwa mahali ambapo wakati mmoja kulikuwa na malango na minara ya kuutegemeza. Hata hivyo, Wayahudi waliorudi hawakuvunjika moyo. Walijenga madhabahu mahali hekalu la kwanza lilipokuwa na kuanza kumtolea Yehova dhabihu kila siku.
15 Huo ulikuwa mwanzo wenye matumaini, lakini Yerusalemu lililojengwa upya halingekuwa tena jiji kuu la ufalme ambao ungetawalwa na mzao wa Mfalme Daudi. Badala yake, Wayahudi walitawalwa na magavana waliowekwa rasmi na walioshinda Babiloni, nao Wayahudi walilazimika kuwalipa kodi mabwana-wakubwa wao, Waajemi. (Nehemia 9:34-37) Ingawa Yerusalemu lilikuwa katika hali ya ‘kukanyagwa-kanyagwa,’ bado lilikuwa jiji la pekee katika dunia nzima lililopendelewa hasa na Yehova Mungu. (Luka 21:24) Likiwa kitovu cha ibada safi, liliwakilisha pia haki ya Mungu ya kudhihirisha enzi kuu yake juu ya dunia kupitia mzao wa Mfalme Daudi.
Kupingwa na Majirani Waliofuata Dini Zisizo za Kweli
16. Kwa nini Wayahudi waliorudi kutoka Babiloni waliacha kujenga upya Yerusalemu?
16 Punde si punde Wayahudi waliokuwa wamerudi Yerusalemu kutoka uhamishoni waliweka msingi wa hekalu jipya. Lakini majirani waliozoea dini isiyo ya kweli walimpelekea Mfalme Artashasta wa Uajemi barua yenye uchongezi, wakidai kwamba Wayahudi wangeasi. Artashasta naye, akapiga marufuku wasiendelee na ujenzi katika Yerusalemu. Waweza kuwazia jinsi ambavyo ungalikuwa na shaka juu ya wakati ujao wa jiji hilo kama ungaliishi humo wakati huo. Kama ilivyothibitika kuwa, Wayahudi waliacha kujenga hekalu, wakajishughulisha sana na utafutaji wao wenyewe wa vitu vya kimwili.—Ezra 4:11-24; Hagai 1:2-6.
17, 18. Yehova alitumia njia gani kuhakikisha kwamba Yerusalemu lilijengwa upya?
17 Miaka 17 baada ya kurudi kwao, Mungu alitokeza manabii Hagai na Zekaria ili wasahihishe kufikiri kwa watu wake. Wakiwa wamesukumwa kutubu, Wayahudi walianza tena kujenga upya hekalu. Wakati huohuo, Dario alikuwa amekuwa mfalme wa Uajemi. Alihakikisha amri ya Mfalme Koreshi kwamba hekalu la Yerusalemu lijengwe upya. Dario aliwapelekea barua majirani wa Wayahudi, akiwaonya ‘wajitenge na mahali pale’ na watoe utegemezo wa kifedha kutoka katika kodi ya mfalme ili kwamba ujenzi uweze kukamilishwa.—Ezra 6:1-13.
18 Wayahudi walikamilisha hekalu miaka 22 baada ya wao kurudi. Waweza kuelewa kwamba wangesherehekea kwa furaha nyingi tukio hilo muhimu. Hata hivyo, sehemu kubwa ya Yerusalemu na kuta zake zilikuwa bado ni magofu. Jiji hilo lilipata uangalifu lililohitaji “siku za Nehemia, liwali, na Ezra, kuhani, mwandishi.” (Nehemia 12:26, 27) Kwa wazi, kufikia mwisho wa karne ya tano K.W.K., Yerusalemu lilijengwa upya kabisa likiwa jiji kuu la ulimwengu wa kale.
Mesiya Atokea!
19. Mesiya alikirije hadhi ya kipekee ya Yerusalemu?
19 Ingawa hivyo, acheni turuke karne kadhaa mbele hadi wakati wa kuzaliwa kwa Yesu Kristo, tukio lililo muhimu kwa wote. Malaika wa Yehova Mungu alikuwa amemwambia mama ya Yesu aliyekuwa bikira hivi: “Yehova Mungu atampa kiti cha ufalme cha Daudi baba yake, . . . na hakutakuwa na mwisho wa ufalme wake.” (Luka 1:32, 33) Miaka kadhaa baadaye, Yesu alitoa Mahubiri yake maarufu ya Mlimani. Katika hayo, alitoa kitia-moyo na ushauri juu ya habari nyingi. Kwa mfano, aliwasihi sana wasikilizaji wake watimize nadhiri zao kwa Mungu lakini wawe waangalifu na wajiepushe kula viapo ovyoovyo. Yesu alisema: “Mlisikia kwamba ilisemwa kwa wale wa nyakati za kale, ‘Lazima usiape bila kutimiza, bali lazima ulipe nadhiri zako kwa Yehova.’ Hata hivyo, mimi nawaambia nyinyi: Msiape hata kidogo, wala kwa mbingu, kwa sababu ni kiti cha ufalme cha Mungu; wala kwa dunia, kwa sababu ndicho kibago cha miguu yake; wala kwa Yerusalemu, kwa sababu ndilo jiji la yule Mfalme mkubwa.” (Mathayo 5:33-35) Inafaa kuangaliwa kwamba Yesu alikiri hadhi ya kipekee ya Yerusalemu—hadhi ambayo jiji hilo lilimiliki kwa karne nyingi. Ndiyo, lilikuwa “jiji la yule Mfalme mkubwa,” Yehova Mungu.
20, 21. Ni badiliko gani lenye kutokeza lililotukia katika mtazamo wa wengi walioishi Yerusalemu?
20 Karibu na mwisho wa uhai wake duniani, Yesu alijitokeza mwenyewe akiwa Mfalme wao aliyetiwa mafuta kwa wakati upasao kwa wakazi wa Yerusalemu. Katika kuitikia pindi hiyo yenye kusisimua, wengi walisema kwa sauti kubwa hivi: “Mbarikiwa ni yeye ajaye katika jina la Yehova! Wenye kubarikiwa ni ufalme unaokuja wa baba yetu Daudi!”—Marko 11:1-10; Yohana 12:12-15.
21 Hata hivyo, katika muda usiozidi juma moja, umati uliacha uchochewe na viongozi wa kidini wa Yerusalemu dhidi ya Yesu. Yesu alionya kwamba jiji la Yerusalemu na taifa zima lingepoteza hadhi yao yenye upendeleo mbele za Mungu. (Mathayo 21:23, 33-45; 22:1-7) Kwa mfano, Yesu alitangaza hivi: “Yerusalemu, Yerusalemu, muuaji wa manabii na mpigaji kwa mawe wale waliotumwa kwake,—ni mara nyingi kadiri gani nilitaka kuwakusanya watoto wako pamoja, kama vile kuku hukusanya vifaranga vyake pamoja chini ya mabawa yake! Lakini nyinyi watu hamkutaka hilo. Tazameni! Nyumba yenu mmeachiwa hali ya ukiwa.” (Mathayo 23:37, 38) Wakati wa Sikukuu ya Kupitwa ya mwaka wa 33 W.K., wapinzani wa Yesu walisababisha kuuawa kwake nje ya Yerusalemu. Hata hivyo, Yehova alimfufua Mtiwa-Mafuta wake na kumtukuza kwa uhai wa roho usioweza kufa katika Zayoni wa kimbingu, utimizo ambao sisi sote twaweza kunufaika kutokana nao.—Matendo 2:32-36.
22. Baada ya kifo cha Yesu, marejezo mengi ya Yerusalemu yamehusu nini?
22 Tangu wakati huo na kuendelea, unabii mwingi mbalimbali ambao haujatimizwa juu ya Zayoni au Yerusalemu, waweza kueleweka kuwa wahusu mipango ya kimbingu au wafuasi wa Yesu watiwa-mafuta. (Zaburi 2:6-8; 110:1-4; Isaya 2:2-4; 65:17, 18; Zekaria 12:3; 14:12, 16, 17) Kwa wazi, marejezo kadhaa ya “Yerusalemu” au “Zayoni” yaliyoandikwa baada ya kifo cha Yesu yana maana ya kitamathali na hayahusiani na jiji au mahali halisi. (Wagalatia 4:26; Waebrania 12:22; 1 Petro 2:6; Ufunuo 3:12; 14:1; 21:2, 10) Ithibati ya mwisho kwamba Yerusalemu halikuwa tena “jiji la yule Mfalme mkubwa” ilitokea mwaka wa 70 W.K wakati ambapo majeshi ya Roma yalilifanya ukiwa, kama ilivyotabiriwa na Danieli na Yesu Kristo. (Danieli 9:26; Luka 19:41-44) Wala waandishi wa Biblia wala Yesu mwenyewe hawakutabiri kurudishwa baadaye kwa Yerusalemu la kidunia kwenye upendeleo wa kipekee wa Yehova Mungu ambao wakati mmoja jiji hilo liliufurahia.—Wagalatia 4:25; Waebrania 13:14.
-
-
Yerusalemu—“Jiji la Yule Mfalme Mkubwa”Mnara wa Mlinzi—1998 | Oktoba 15
-
-
wala kwa dunia, kwa sababu ndicho kibago cha miguu yake; wala kwa Yerusalemu, kwa sababu ndilo jiji la yule Mfalme mkubwa.” (Mathayo 5:33-35) Inafaa kuangaliwa kwamba Yesu alikiri hadhi ya kipekee ya Yerusalemu—hadhi ambayo jiji hilo lilimiliki kwa karne nyingi. Ndiyo, lilikuwa “jiji la yule Mfalme mkubwa,” Yehova Mungu.
-
-
Yerusalemu—“Jiji la Yule Mfalme Mkubwa”Mnara wa Mlinzi—1998 | Oktoba 15
-
-
Ithibati ya mwisho kwamba Yerusalemu halikuwa tena “jiji la yule Mfalme mkubwa” ilitokea mwaka wa 70 W.K wakati ambapo majeshi ya Roma yalilifanya ukiwa, kama ilivyotabiriwa na Danieli na Yesu Kristo. (Danieli 9:26; Luka 19:41-44) Wala waandishi wa Biblia wala Yesu mwenyewe hawakutabiri kurudishwa baadaye kwa Yerusalemu la kidunia kwenye upendeleo wa kipekee wa Yehova Mungu ambao wakati mmoja jiji hilo liliufurahia.—Wagalatia 4:25; Waebrania 13:14.
-