-
Kumtambua Mjumbe wa Aina InayofaaMnara wa Mlinzi—1997 | Mei 1
-
-
7, 8. Isaya alikuwa na ujumbe gani wenye kupuliziwa kwa ajili ya Babiloni, na maneno yake yalimaanisha nini?
7 Yuda na Yerusalemu zilikuwa ziwe ukiwa kabisa, bila mkazi wa kibinadamu, kwa miaka 70. Hata hivyo, Yehova alijulisha kupitia Isaya na Ezekieli kwamba hilo jiji lingejengwa upya na bara hilo kukaliwa kwa wakati barabara aliokuwa ametabiri Yehova! Huo ulikuwa utabiri wenye kushangaza. Kwa nini? Kwa sababu Babiloni lilikuwa na sifa ya kutoachilia kamwe wafungwa walo. (Isaya 14:4, 15-17) Kwa hiyo ni nani ambaye angeweza kwa kweli kuwaweka huru mateka hawa? Ni nani ambaye angeweza kushinda Babiloni lenye uweza, likiwa na kuta zalo kubwa mno na mto ukiwa mfumo wa ulinzi? Yehova Mweza Yote angeweza! Naye aliyesema angefanya hivyo: “Nami [ndiye] . . . niviambiaye vilindi [yaani, maji ya mto yaliyolinda hilo jiji], Kauka, nami nitaikausha mito yako; nimwambiaye Koreshi [“Sairasi,” NW], Mchungaji wangu, naye atayatenda mapenzi yangu; hata ataunena Yerusalemu, Utajengwa; na hilo hekalu, Msingi wako utawekwa.”—Isaya 44:25, 27, 28, linganisha NW.
8 Wazia hilo! Mto Frati, uliokuwa kizuizi kikubwa mno kwa wanadamu, kwa Yehova ulikuwa kama tone la maji juu ya uso wenye moto mwingi sana! Mara moja ungekauka! Babiloni lingeanguka. Ingawa ilikuwa miaka 150 hivi kabla ya kuzaliwa kwa Sairasi Mwajemi, Yehova alimfanya Isaya atabiri kunasa kwa mfalme huyo Babiloni na kuachwa huru kwa Wayahudi walio mateka kwa kutoa kwake amri ya kurudi kwao ili kujenga upya Yerusalemu na hekalu lalo.
9. Yehova alimteua nani kuwa wakili wake ili kuadhibu Babiloni?
9 Twapata unabii huo kwenye Isaya 45:1-3: “Haya ndiyo BWANA amwambiayo Koreshi, masihi [“mtiwa-mafuta,” NW] wake, ambaye nimemshika mkono wake wa kuume, ili kutiisha mataifa mbele yake, nami nitalegeza viuno vya wafalme; ili kufungua milango mbele yake, hata malango hayatafungwa. Nitakwenda mbele yako, na kupasawazisha mahali palipoparuza; nitavunja vipande vipande milango ya shaba, na kukata-kata mapingo ya chuma; nami nitakupa hazina za gizani, na mali zilizofichwa za mahali pa siri, upate kujua ya kuwa mimi ni BWANA, nikuitaye kwa jina lako.”
10. Sairasi alikuwa “mtiwa-mafuta” kwa njia gani, na Yehova angeweza kusemaje naye miaka zaidi ya mia moja kabla ya kuzaliwa kwake?
10 Ona kwamba Yehova anasema na Sairasi kana kwamba tayari yuko hai. Hilo lapatana na taarifa ya Paulo kwamba Yehova “huita mambo yasiyokuwako kama kwamba yamekuwako.” (Waroma 4:17) Pia, Mungu amtambua Sairasi kuwa “mtiwa-mafuta” wake. Kwa nini alifanya hivyo? Kwa vyovyote, kuhani wa Yehova wa cheo cha juu hakutia kamwe mafuta matakatifu kwenye kichwa cha Sairasi. Ni kweli, lakini huku ni kutiwa mafuta kwa kiunabii. Huonyesha kuwekwa rasmi, kuingizwa katika cheo cha pekee. Kwa hiyo Mungu angeweza kusema juu ya tendo lake la kumweka rasmi Sairasi kimbele kuwa kama kutiwa mafuta.—Linganisha 1 Wafalme 19:15-17; 2 Wafalme 8:13.
Mungu Atimiza Maneno ya Wajumbe Wake
11. Kwa nini wakazi wa Babiloni walihisi usalama?
11 Kufikia wakati ambapo Sairasi alipiga hatua dhidi ya Babiloni, wakazi walo walihisi kwamba walikuwa salama salimini. Jiji lao lilizingirwa na handaki la maji lenye kina kirefu na lililo pana, ambalo lilifanyizwa na Mto Frati. Mahali ambapo mto ulipita jijini, kulikuwa na gati lenye kuendelea kandokando ya ukingo wa mashariki wa huo mto. Ili kulitenganisha na jiji, Nebukadreza alijenga kile alichokiita “ukuta mkubwa, ambao kama mlima, hauwezi kusogezwa . . . Kilele chao [alikiinua] juu kama mlima.”a Ukuta huu ulikuwa na malango yenye milango mikubwa mno ya shaba. Ili mtu aingie, ilimbidi akwee mteremko huo kutoka ukingo wa mto. Si ajabu wafungwa wa Babiloni walikata tamaa ya kupata kuwekwa huru!
12, 13. Maneno ya Yehova kupitia mjumbe wake Isaya yalitimiaje wakati Babiloni lilipoanguka mikononi mwa Sairasi?
12 Walakini Wayahudi walio mateka waliokuwa na imani katika Yehova hawakukata tamaa! Walikuwa na tumaini jangavu. Kupitia manabii wake, Mungu alikuwa ameahidi kuwaweka huru. Mungu alitimizaje ahadi yake? Sairasi aliamuru majeshi yake yageuzie mbali mkondo wa Mto Frati mahali fulani, kilometa nyingi kaskazini ya Babiloni. Hivyo, ulinzi mkuu wa hilo jiji ukawa sakafu ya mto iliyokauka kwa kadiri fulani. Usiku huo wa maana, walevi waliokuwa wakinywa humo Babiloni waliacha bila kujali ile milango yenye sehemu mbili kandokando ya sehemu ya jiji iliyokuwa ikikabili Frati. Yehova hakuivunja ile milango ya shaba vipande vipande kihalisi; wala hakuyakata-kata mapingo ya chuma yenye kuifunga, lakini mbinu yake ya kuiacha ikiwa wazi bila kuzuiwa ilikuwa na matokeo hayohayo. Kuta za Babiloni zilikuwa bure. Vikosi vya Sairasi havikuhitaji kuzipanda kuta hizo ili kuingia ndani. Yehova alikwenda mbele ya Sairasi, akipasawazisha “mahali palipoparuza,” ndiyo, vizuizi vyote. Isaya alithibitishwa kuwa mjumbe wa kweli wa Mungu.
13 Sairasi alipokuwa na udhibiti kamili wa hilo jiji, hazina zote zikawa mikononi mwake, hata zile zilizofichwa katika vyumba vyenye giza, vya siri. Kwa nini Yehova Mungu alimfanyia Sairasi hayo? Ili apate kujua kwamba Yehova, ‘amwitaye kwa jina lake,’ ndiye Mungu wa unabii wa kweli na Bwana Mwenye Enzi Kuu wa ulimwengu wote mzima. Angejua kwamba Mungu alikuwa amempangia apate mamlaka ili aweke huru watu Wake, Israeli.
14, 15. Twajuaje kwamba ushindi wa Sairasi dhidi ya Babiloni ulitokana na Yehova?
14 Sikiliza maneno ya Yehova kwa Sairasi: “Kwa ajili ya Yakobo, mtumishi wangu, na Israeli, mteule wangu, nimekuita kwa jina lako; nimekupa jina la sifa; ijapokuwa hukunijua. Mimi ni BWANA, wala hapana mwingine; zaidi yangu mimi hapana Mungu, nitakufunga mshipi ijapokuwa hukunijua; ili wapate kujua toka maawio ya jua, na toka magharibi, ya kuwa hapana mwingine zaidi ya mimi; Mimi ni BWANA, wala hapana mwingine. Mimi naiumba nuru, na kulihuluku giza; mimi nafanya suluhu, na kuhuluku ubaya; Mimi ni BWANA, niyatendaye hayo yote.”—Isaya 45:4-7.
15 Ushindi wa Sairasi dhidi ya Babiloni ulitokana na Yehova, kwa kuwa Yeye ndiye aliyemwimarisha atekeleze alilotaka Yeye dhidi ya jiji hilo ovu na aweke huru watu Wake walio mateka. Kwa kufanya hivyo, Mungu aliitia mbingu zake zinyeshe uvutano au kani zenye uadilifu. Aliitia dunia yake ifunguke na kutokeza matukio yenye uadilifu na wokovu kwa ajili ya watu wake waliohamishwa. Nazo mbingu na dunia zake za ufananisho ziliitikia amri hiyo. (Isaya 45:8) Miaka zaidi ya mia moja baada ya kifo chake, Isaya alionyeshwa kuwa mjumbe wa kweli wa Yehova!
Habari Njema ya Mjumbe kwa Ajili ya Sayuni!
16. Ni habari gani njema ingeweza kupigwa mbiu katika jiji lililofanywa ukiwa la Yerusalemu wakati Babiloni liliposhindwa?
16 Lakini kuna mengi zaidi. Isaya 52:7 hutuambia juu ya habari njema kwa ajili ya Yerusalemu: “Jinsi ilivyo mizuri juu ya milima miguu yake aletaye habari njema, yeye aitangazaye amani, aletaye habari njema ya mambo mema, yeye autangazaye wokovu, auambiaye Sayuni, Mungu wako anamiliki!” Wazia jinsi ilivyofurahisha kumwona mjumbe akikaribia Yerusalemu kutoka milimani! Lazima awe ana habari! Habari gani? Ni habari yenye kusisimua kwa ajili ya Sayuni. Habari ya amani, ndiyo, habari ya nia njema ya Mungu. Yerusalemu na hekalu lalo litajengwa upya! Na huyo mjumbe apiga mbiu akiwa na idili ya ushindi: “Mungu wako anamiliki!”
17, 18. Ushindi wa Sairasi dhidi ya Babiloni uliathirije jina la Yehova mwenyewe?
17 Yehova aliporuhusu Wababiloni kukipindua kiti chake cha ufalme cha kimfano, ambapo wafalme wa ukoo wa Daudi walikaa, huenda ikawa ilionekana kwamba Yeye hakuwa Mfalme tena. Marduki, mungu mkuu wa Babiloni, ndiye aliyeonekana kuwa mfalme badala yake. Lakini, Mungu wa Sayuni alipopindua Babiloni, alionyesha kuwa mwenye enzi kuu ya ulimwengu wote mzima—kwamba alikuwa Mfalme mkuu kupita wote. Na kukazia jambo hili la hakika, Yerusalemu, “mji wa Mfalme mkuu,” lilipasa kusimamishwa tena, pamoja na hekalu lalo. (Mathayo 5:35) Kwa habari ya mjumbe aliyeleta habari hizo njema, ingawa miguu yake ilikuwa na vumbi sana, ilikuwa michafu, na kuchubuka, machoni pa wapenda-Sayuni na Mungu wake, ilionekana, loo, mizuri saana!
18 Katika maana ya kiunabii, kuanguka kwa Babiloni kulimaanisha kwamba ufalme wa Mungu ulisimamishwa naye mchukuaji wa habari njema alikuwa mpiga-mbiu wa jambo hilo la hakika. Na zaidi, mpeleka-habari huyu wa kale, aliyetabiriwa kupitia Isaya, alifananisha mjumbe wa habari njema tukufu zaidi—tukufu zaidi kwa sababu ya yaliyomo yaliyo bora na kichwa chayo cha Ufalme, kukimaanisha mambo mazuri ajabu kwa ajili ya watu wote wa imani.
-
-
Kumtambua Mjumbe wa Aina InayofaaMnara wa Mlinzi—1997 | Mei 1
-
-
20. Isaya alitolea kiunabii Yerusalemu himizo gani lenye furaha?
20 Katika utekwa wa Babiloni, watu wa Mungu walikuwa wakiombolezea Sayuni. (Zaburi 137:1) Sasa wangeweza kushangilia. Isaya alihimiza hivi: “Pigeni kelele za furaha, imbeni pamoja, enyi mahali pa Yerusalemu palipokuwa ukiwa; kwa kuwa BWANA amewafariji watu wake, ameukomboa Yerusalemu. BWANA ameweka wazi mkono wake mtakatifu machoni pa mataifa yote; na ncha zote za dunia zitauona wokovu wa Mungu wetu.”—Isaya 52:9, 10.
21. Maneno ya Isaya 52:9, 10 yalitimizwaje kufuatia ushinde wa Babiloni?
21 Ndiyo, watu wa Yehova waliochaguliwa walikuwa na sababu kubwa ya kushangilia. Sasa walikuwa wakae tena katika sehemu zile zilizokuwa ukiwa wakati mmoja, wakizifanya ziwe kama bustani ya Edeni. Yehova alikuwa “ameweka wazi mkono wake,” kwa ajili yao. Alikunja mkono wa shati lake, kwa kusema kitamathali, ili aweze kufanya kazi ya kurudisha watu wake kwenye bara-pendwa la kwao. Hilo halikuwa tukio dogo, la kisiri katika historia. La, watu wote waliokuwa wakiishi wakati huo waliona ‘mkono wazi’ wa Mungu ukikakamua nguvu katika mambo ya kibinadamu ili kuleta wokovu wa pekee kwa taifa. Walipewa ithibati isiyotilika shaka kwamba Isaya na Ezekieli walikuwa wajumbe wa kweli wa Yehova. Hakuna yeyote angeweza kushuku kwamba Mungu wa Sayuni alikuwa Mungu pekee anayeishi na wa kweli katika dunia yote. Kwenye Isaya 35:2, twasoma juu ya urudisho huo: “Watauona utukufu wa BWANA, ukuu wa Mungu wetu.” Wale waliokubali ithibati hii ya Uungu wa Yehova na walianza kumwabudu.
-