Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Yerusalemu—“Jiji la Yule Mfalme Mkubwa”
    Mnara wa Mlinzi—1998 | Oktoba 15
    • Yerusalemu—“Jiji la Yule Mfalme Mkubwa”

      “Msiape . . . kwa Yerusalemu, kwa sababu ndilo jiji la yule Mfalme mkubwa.”—MATHAYO 5:34, 35.

      1, 2. Ni nini kiwezacho kutatanisha wengine kuhusu Yerusalemu?

      YERUSALEMU—jina lake tu huamsha hisia zenye nguvu za watu wa dini mbalimbali. Kwa kweli, hakuna yeyote kati yetu awezaye kulipuuza jiji hili la kale, kwa kuwa hutajwa mara nyingi katika habari. Kwa kusikitisha, ripoti nyingi hufunua kwamba Yerusalemu si mahali pa amani sikuzote.

      2 Huenda jambo hilo likatokeza wazo lenye kutatanisha kwa wasomi wa Biblia. Zamani, ufupisho wa jina Yerusalemu ulikuwa Salemu, neno limaanishalo “amani.” (Mwanzo 14:18; Zaburi 76:2; Waebrania 7:1, 2) Kwa hiyo, huenda ukajiuliza, ‘Kwa nini katika nyakati za karibuni jiji lenye jina hilo limekuwa na ukosefu kama huo wa amani?’

      3. Ni wapi tuwezapo kupata habari yenye kutegemeka kuhusu Yerusalemu?

      3 Ili kujibu swali hilo, twahitaji kurudia historia ya zamani na kujifunza juu ya Yerusalemu la nyakati za kale. Lakini huenda wengine wakafikiri, ‘Hatuna wakati wa kujifunza historia ya kale.’ Hata hivyo, ujuzi sahihi wa historia ya mapema ya Yerusalemu ni wenye thamani kwetu sote. Biblia huonyesha sababu kwa kusema: “Mambo yote yaliyoandikwa wakati wa mbele yaliandikwa kwa kufunzwa kwetu, ili kupitia uvumilivu wetu na kupitia faraja kutokana na Maandiko tupate kuwa na tumaini.” (Waroma 15:4) Ujuzi wa Biblia juu ya Yerusalemu waweza kutufariji—ndiyo, na tumaini la amani, si katika jiji hilo tu bali katika dunia yote.

      Mahali pa ‘Kiti cha Enzi cha Yehova’

      4, 5. Daudi alihusikaje katika kulisaidia Yerusalemu liwe na fungu kubwa katika kutimizwa kwa makusudi ya Mungu?

      4 Katika karne ya 11 K.W.K., Yerusalemu lilipata kuwa jiji maarufu la taifa lenye usalama na amani. Yehova Mungu aliamuru kijana Daudi atiwe mafuta kuwa mfalme wa taifa hilo la kale—Israeli. Kwa kuwa makao ya serikali yalikuwa Yerusalemu, Daudi na wazao wake wa kifalme walikuja kukalia ‘kiti cha enzi cha ufalme wa Yehova,’ au ‘kiti cha enzi cha Yehova.’—1 Mambo ya Nyakati 28:5; 29:23.

      5 Mwanamume Daudi mwenye kumhofu Mungu—Mwisraeli wa kabila la Yuda—aliteka Yerusalemu kutoka kwa Wayebusi wenye kuabudu sanamu. Wakati huo jiji hilo lilikuwa tu kwenye kilima kiitwacho Zayoni, lakini maana ya jina hilo ilikuja kuwa na maana sawa na jina Yerusalemu lenyewe. Halafu, Daudi akaamuru sanduku la agano la Mungu pamoja na Israeli, lihamishwe hadi Yerusalemu, ambapo liliwekwa katika hema. Miaka kadhaa mapema, Mungu alikuwa amesema na Musa nabii wake kutoka katika wingu juu ya Sanduku hilo takatifu. (Kutoka 25:1, 21, 22; Mambo ya Walawi 16:2; 1 Mambo ya Nyakati 15:1-3) Sanduku hilo lilifananisha kuwapo kwa Mungu, kwa maana Yehova ndiye aliyekuwa Mfalme halisi wa Israeli. Kwa hiyo, kwa usemi wenye maana maradufu, yaweza kusemwa kwamba Yehova Mungu alitawala kutoka jiji la Yerusalemu.

      6. Yehova alitoa ahadi gani kuhusu Daudi na Yerusalemu?

      6 Yehova alimwahidi Daudi kwamba ufalme wa ukoo wake wa kifalme, uliowakilishwa na Zayoni, au Yerusalemu, haungeisha. Hilo lilimaanisha kwamba mzao wa Daudi angerithi haki ya kutawala milele akiwa Mtiwa-Mafuta wa Mungu—Mesiya, au Kristo.a (Zaburi 132:11-14; Luka 1:31-33) Biblia pia hufunua kwamba mrithi huyo wa kudumu wa ‘kiti cha enzi cha Yehova’ angetawala juu ya mataifa yote, wala si Yerusalemu tu.—Zaburi 2:6-8; Danieli 7:13, 14.

      7. Mfalme Daudi aliendelezaje ibada safi?

      7 Jitihada za kumwondosha mamlakani Mfalme Daudi aliyekuwa mtiwa-mafuta wa Mungu, hazikufua dafu. Badala yake, mataifa maadui yalitiishwa, na mipaka ya Bara Lililoahidiwa iliyoonyeshwa na Mungu, ikapanuliwa kabisa. Daudi alitumia hali hiyo ili kuendeleza ibada safi. Nazo zaburi nyingi za Daudi humsifu Yehova kuwa ndiye Mfalme halisi wa Zayoni.—2 Samweli 8:1-15; Zaburi 9:1, 11; 24:1, 3, 7-10; 65:1, 2; 68:1, 24, 29; 110:1, 2; 122:1-4.

      8, 9. Ibada ya kweli ilipanukaje katika Yerusalemu chini ya utawala wa Mfalme Solomoni?

      8 Wakati wa utawala wa Solomoni mwana wa Daudi, ibada ya Yehova ilipanuliwa. Solomoni alipanua Yerusalemu kuelekea upande wa juu ili kutia ndani kilima Moria (eneo ambako siku hizi kuna jengo liitwalo Dome of the Rock). Kwenye eneo hilo lililoinuka zaidi, alipendelewa kujenga hekalu lenye fahari kwa sifa ya Yehova. Sanduku la agano liliwekwa katika Patakatifu Zaidi Sana pa hekalu.—1 Wafalme 6:1-38.

      9 Taifa la Israeli lilifurahia amani lilipojitolea kwa moyo wote kwa ajili ya ibada ya Yehova, iliyokuwa na kitovu chake Yerusalemu. Maandiko yanafafanua hali hiyo kwa kutaarifu hivi: “Yuda na Israeli walikuwa wengi kama mchanga wa pwani kwa wingi, wakila, na kunywa, na kufurahi. . . . Naye [Solomoni] alikuwa na amani pande zake zote. Yuda na Israeli wakakaa salama, kila mtu chini ya mzabibu wake na chini ya mtini wake.”—1 Wafalme 4:20, 24, 25.

      10, 11. Akiolojia inaungaje mkono yale ambayo Biblia husema juu ya Yerusalemu, Solomoni alipotawala?

      10 Uvumbuzi wa kiakiolojia waunga mkono simulizi hilo la utawala wa Solomoni wenye ufanisi. Katika kitabu chake The Archaeology of the Land of Israel, Profesa Yohanan Aharoni ataarifu: “Mali iliyomiminika katika nyumba ya kifalme kutoka pande zote, na biashara yenye kusitawi . . . ilileta ukuzi wa haraka na wenye kuonekana katika kila sehemu ya utamaduni wa vitu vya kimwili. . . . Badiliko katika utamaduni wa vitu vya kimwili . . . laweza kuonekana wazi si katika vitu vya anasa tu bali pia hasa katika vyombo vya ufinyanzi. . . . Ubora wa vyombo hivyo vya ufinyanzi na ukaushaji wake kwa kutumia moto ulifanyiwa maendeleo yasiyo na kifani.”

      11 Vivyo hivyo, Jerry M. Landay aliandika: “Chini ya Solomoni, utamaduni wa Israeli wa vitu vya kimwili ulisitawi zaidi kwa muda wa miongo mitatu kuliko vile ulivyokuwa umesitawi katika miaka mia mbili iliyotangulia. Katika tabaka ya ardhi ya nyakati za Solomoni twapata mabaki ya majengo makubwa sana, majiji makubwa yenye kuta kubwa sana, vuvumko la maskani yenye vikundi-vikundi vya makao ya matajiri yaliyojengwa vizuri, usitawi wa ufundi wa mfinyanzi na taratibu zake za utengenezaji. Pia twapata mabaki ya sanaa za bidhaa zilizotengenezewa sehemu za mbali sana, zikiwa ishara za kwamba kulikuwako biashara yenye juhudi ya kimataifa na ubadilishanaji wa bidhaa.”—The House of David.

      Kutoka Hali ya Amani Hadi ya Ukiwa

      12, 13. Ilikuwaje kwamba ibada ya kweli haikuendelezwa Yerusalemu?

      12 Ilifaa kusali kwa ajili ya amani na ufanisi wa jiji la Yerusalemu, ambapo mahali patakatifu pa Yehova palikuwa. Daudi aliandika: “Utakieni Yerusalemu amani; na wafanikiwe wakupendao; amani na ikae ndani ya kuta zako, na kufanikiwa ndani ya majumba yako. Kwa ajili ya ndugu zangu na rafiki zangu niseme sasa, Amani ikae nawe.” (Zaburi 122:6-8) Ingawa Solomoni alipendelewa kujenga hekalu lenye fahari katika jiji hilo lenye amani, hatimaye alioa wake wengi wapagani. Alipokuwa mzee, walimshawishi aendeleze ibada ya miungu ya uwongo ya wakati huo. Uasi-imani huo ulikuwa na uvutano wenye kufisidi juu ya taifa zima, ukilinyima jiji hilo na wakaaji wake amani ya kweli.—1 Wafalme 11:1-8; 14:21-24.

      13 Mapema katika utawala wa Rehoboamu mwana wa Solomoni, makabila kumi yaliasi na kufanyiza ufalme wa kaskazini wa Israeli. Kwa sababu ya kuabudu kwao sanamu, Mungu aliuruhusu ufalme huo upinduliwe na Ashuru. (1 Wafalme 12:16-30) Yerusalemu liliendelea kuwa kitovu cha ufalme wa kusini wa Yuda wenye makabila mawili. Lakini baada ya muda, wao pia wakaacha ibada safi, kwa hiyo Mungu akaachilia jiji hilo potovu liharibiwe na Wababiloni mwaka wa 607 K.W.K. Kwa miaka 70 wahamishwa Wayahudi waliteseka wakiwa mateka huko Babiloni. Kisha, kwa rehema ya Mungu, wakaruhusiwa kurudi Yerusalemu na kurudisha ibada ya kweli.—2 Mambo ya Nyakati 36:15-21.

      14, 15. Yerusalemu lilipataje tena kuwa na fungu muhimu baada ya uhamisho wa Babiloni, lakini kukiwa na badiliko gani?

      14 Baada ya miaka 70 ya ukiwa, ni lazima majengo yaliyoharibiwa yawe yalifunikwa kwa magugu. Ukuta wa Yerusalemu ulibomolewa, kukiwa na mianya mikubwa mahali ambapo wakati mmoja kulikuwa na malango na minara ya kuutegemeza. Hata hivyo, Wayahudi waliorudi hawakuvunjika moyo. Walijenga madhabahu mahali hekalu la kwanza lilipokuwa na kuanza kumtolea Yehova dhabihu kila siku.

      15 Huo ulikuwa mwanzo wenye matumaini, lakini Yerusalemu lililojengwa upya halingekuwa tena jiji kuu la ufalme ambao ungetawalwa na mzao wa Mfalme Daudi. Badala yake, Wayahudi walitawalwa na magavana waliowekwa rasmi na walioshinda Babiloni, nao Wayahudi walilazimika kuwalipa kodi mabwana-wakubwa wao, Waajemi. (Nehemia 9:34-37) Ingawa Yerusalemu lilikuwa katika hali ya ‘kukanyagwa-kanyagwa,’ bado lilikuwa jiji la pekee katika dunia nzima lililopendelewa hasa na Yehova Mungu. (Luka 21:24) Likiwa kitovu cha ibada safi, liliwakilisha pia haki ya Mungu ya kudhihirisha enzi kuu yake juu ya dunia kupitia mzao wa Mfalme Daudi.

      Kupingwa na Majirani Waliofuata Dini Zisizo za Kweli

      16. Kwa nini Wayahudi waliorudi kutoka Babiloni waliacha kujenga upya Yerusalemu?

      16 Punde si punde Wayahudi waliokuwa wamerudi Yerusalemu kutoka uhamishoni waliweka msingi wa hekalu jipya. Lakini majirani waliozoea dini isiyo ya kweli walimpelekea Mfalme Artashasta wa Uajemi barua yenye uchongezi, wakidai kwamba Wayahudi wangeasi. Artashasta naye, akapiga marufuku wasiendelee na ujenzi katika Yerusalemu. Waweza kuwazia jinsi ambavyo ungalikuwa na shaka juu ya wakati ujao wa jiji hilo kama ungaliishi humo wakati huo. Kama ilivyothibitika kuwa, Wayahudi waliacha kujenga hekalu, wakajishughulisha sana na utafutaji wao wenyewe wa vitu vya kimwili.—Ezra 4:11-24; Hagai 1:2-6.

      17, 18. Yehova alitumia njia gani kuhakikisha kwamba Yerusalemu lilijengwa upya?

      17 Miaka 17 baada ya kurudi kwao, Mungu alitokeza manabii Hagai na Zekaria ili wasahihishe kufikiri kwa watu wake. Wakiwa wamesukumwa kutubu, Wayahudi walianza tena kujenga upya hekalu. Wakati huohuo, Dario alikuwa amekuwa mfalme wa Uajemi. Alihakikisha amri ya Mfalme Koreshi kwamba hekalu la Yerusalemu lijengwe upya. Dario aliwapelekea barua majirani wa Wayahudi, akiwaonya ‘wajitenge na mahali pale’ na watoe utegemezo wa kifedha kutoka katika kodi ya mfalme ili kwamba ujenzi uweze kukamilishwa.—Ezra 6:1-13.

      18 Wayahudi walikamilisha hekalu miaka 22 baada ya wao kurudi. Waweza kuelewa kwamba wangesherehekea kwa furaha nyingi tukio hilo muhimu. Hata hivyo, sehemu kubwa ya Yerusalemu na kuta zake zilikuwa bado ni magofu. Jiji hilo lilipata uangalifu lililohitaji “siku za Nehemia, liwali, na Ezra, kuhani, mwandishi.” (Nehemia 12:26, 27) Kwa wazi, kufikia mwisho wa karne ya tano K.W.K., Yerusalemu lilijengwa upya kabisa likiwa jiji kuu la ulimwengu wa kale.

      Mesiya Atokea!

      19. Mesiya alikirije hadhi ya kipekee ya Yerusalemu?

      19 Ingawa hivyo, acheni turuke karne kadhaa mbele hadi wakati wa kuzaliwa kwa Yesu Kristo, tukio lililo muhimu kwa wote. Malaika wa Yehova Mungu alikuwa amemwambia mama ya Yesu aliyekuwa bikira hivi: “Yehova Mungu atampa kiti cha ufalme cha Daudi baba yake, . . . na hakutakuwa na mwisho wa ufalme wake.” (Luka 1:32, 33) Miaka kadhaa baadaye, Yesu alitoa Mahubiri yake maarufu ya Mlimani. Katika hayo, alitoa kitia-moyo na ushauri juu ya habari nyingi. Kwa mfano, aliwasihi sana wasikilizaji wake watimize nadhiri zao kwa Mungu lakini wawe waangalifu na wajiepushe kula viapo ovyoovyo. Yesu alisema: “Mlisikia kwamba ilisemwa kwa wale wa nyakati za kale, ‘Lazima usiape bila kutimiza, bali lazima ulipe nadhiri zako kwa Yehova.’ Hata hivyo, mimi nawaambia nyinyi: Msiape hata kidogo, wala kwa mbingu, kwa sababu ni kiti cha ufalme cha Mungu; wala kwa dunia, kwa sababu ndicho kibago cha miguu yake; wala kwa Yerusalemu, kwa sababu ndilo jiji la yule Mfalme mkubwa.” (Mathayo 5:33-35) Inafaa kuangaliwa kwamba Yesu alikiri hadhi ya kipekee ya Yerusalemu—hadhi ambayo jiji hilo lilimiliki kwa karne nyingi. Ndiyo, lilikuwa “jiji la yule Mfalme mkubwa,” Yehova Mungu.

      20, 21. Ni badiliko gani lenye kutokeza lililotukia katika mtazamo wa wengi walioishi Yerusalemu?

      20 Karibu na mwisho wa uhai wake duniani, Yesu alijitokeza mwenyewe akiwa Mfalme wao aliyetiwa mafuta kwa wakati upasao kwa wakazi wa Yerusalemu. Katika kuitikia pindi hiyo yenye kusisimua, wengi walisema kwa sauti kubwa hivi: “Mbarikiwa ni yeye ajaye katika jina la Yehova! Wenye kubarikiwa ni ufalme unaokuja wa baba yetu Daudi!”—Marko 11:1-10; Yohana 12:12-15.

      21 Hata hivyo, katika muda usiozidi juma moja, umati uliacha uchochewe na viongozi wa kidini wa Yerusalemu dhidi ya Yesu. Yesu alionya kwamba jiji la Yerusalemu na taifa zima lingepoteza hadhi yao yenye upendeleo mbele za Mungu. (Mathayo 21:23, 33-45; 22:1-7) Kwa mfano, Yesu alitangaza hivi: “Yerusalemu, Yerusalemu, muuaji wa manabii na mpigaji kwa mawe wale waliotumwa kwake,—ni mara nyingi kadiri gani nilitaka kuwakusanya watoto wako pamoja, kama vile kuku hukusanya vifaranga vyake pamoja chini ya mabawa yake! Lakini nyinyi watu hamkutaka hilo. Tazameni! Nyumba yenu mmeachiwa hali ya ukiwa.” (Mathayo 23:37, 38) Wakati wa Sikukuu ya Kupitwa ya mwaka wa 33 W.K., wapinzani wa Yesu walisababisha kuuawa kwake nje ya Yerusalemu. Hata hivyo, Yehova alimfufua Mtiwa-Mafuta wake na kumtukuza kwa uhai wa roho usioweza kufa katika Zayoni wa kimbingu, utimizo ambao sisi sote twaweza kunufaika kutokana nao.—Matendo 2:32-36.

      22. Baada ya kifo cha Yesu, marejezo mengi ya Yerusalemu yamehusu nini?

      22 Tangu wakati huo na kuendelea, unabii mwingi mbalimbali ambao haujatimizwa juu ya Zayoni au Yerusalemu, waweza kueleweka kuwa wahusu mipango ya kimbingu au wafuasi wa Yesu watiwa-mafuta. (Zaburi 2:6-8; 110:1-4; Isaya 2:2-4; 65:17, 18; Zekaria 12:3; 14:12, 16, 17) Kwa wazi, marejezo kadhaa ya “Yerusalemu” au “Zayoni” yaliyoandikwa baada ya kifo cha Yesu yana maana ya kitamathali na hayahusiani na jiji au mahali halisi. (Wagalatia 4:26; Waebrania 12:22; 1 Petro 2:6; Ufunuo 3:12; 14:1; 21:2, 10) Ithibati ya mwisho kwamba Yerusalemu halikuwa tena “jiji la yule Mfalme mkubwa” ilitokea mwaka wa 70 W.K wakati ambapo majeshi ya Roma yalilifanya ukiwa, kama ilivyotabiriwa na Danieli na Yesu Kristo. (Danieli 9:26; Luka 19:41-44) Wala waandishi wa Biblia wala Yesu mwenyewe hawakutabiri kurudishwa baadaye kwa Yerusalemu la kidunia kwenye upendeleo wa kipekee wa Yehova Mungu ambao wakati mmoja jiji hilo liliufurahia.—Wagalatia 4:25; Waebrania 13:14.

  • Je, ‘Wewe Walikuza Yerusalemu Zaidi ya Furaha Yako Iliyo Kuu’?
    Mnara wa Mlinzi—1998 | Oktoba 15
    • Je, ‘Wewe Walikuza Yerusalemu Zaidi ya Furaha Yako Iliyo Kuu’?

      “Ulimi wangu na ugandamane na kaakaa la kinywa changu, . . . nisipoikuza Yerusalemu zaidi ya furaha yangu iliyo kuu.”—ZABURI 137:6.

      1. Wahamishwa wengi Wayahudi walikuwa na mtazamo gani kuelekea jiji lililochaguliwa na Mungu?

      KARIBU miongo saba ilikuwa imepita tangu wahamishwa Wayahudi warudi Yerusalemu mwaka wa 537 K.W.K. Hekalu la Mungu lilikuwa limejengwa upya, lakini jiji lilikuwa bado ni magofu. Wakati huohuo, kizazi kipya kilikuwa kimekulia uhamishoni. Hapana shaka wengi wao walihisi kama mtunga-zaburi aliyeimba hivi: “Ee Yerusalemu, nikikusahau wewe, mkono wangu wa kuume na usahau.” (Zaburi 137:5) Wengi walifanya mengi zaidi ya kukumbuka tu Yerusalemu; walithibitisha kwa matendo yao kwamba walikuwa wamelikuza ‘zaidi ya furaha yao iliyo kuu.’—Zaburi 137:6.

      2. Ezra alikuwa nani, naye alibarikiwaje?

      2 Kwa kielelezo, fikiria kuhani Ezra. Hata kabla ya kurudi katika nchi yake ya nyumbani, alikuwa ameendeleza kwa bidii masilahi ya ibada safi huko Yerusalemu. (Ezra 7:6, 10) Ezra alibarikiwa sana kwa jambo hilo. Yehova Mungu aligusa moyo wa mfalme wa Uajemi ili ampe Ezra pendeleo la kuongoza kikundi kingine cha wahamishwa wenye kurudi Yerusalemu. Zaidi ya hayo, mfalme aliwapa mchango mkubwa wa dhahabu na fedha ili “kuipamba nyumba ya BWANA iliyoko Yerusalemu.”—Ezra 7:21-27.

      3. Nehemia alithibitishaje kwamba Yerusalemu lilikuwa hangaiko lake kuu?

      3 Miaka 12 baadaye, kulikuwako Myahudi mwingine aliyechukua hatua ya kukata maneno—Nehemia. Alitumikia katika jumba la mfalme wa Uajemi huko Shushani. Alikuwa na cheo chenye fahari akiwa mnyweshaji wa Mfalme Artashasta, lakini cheo hicho hakikuwa ‘furaha ya Nehemia iliyo kuu.’ Badala yake, alitamani sana kwenda na kujenga upya Yerusalemu. Kwa miezi kadhaa Nehemia alisali kuhusu jambo hilo, naye Yehova Mungu akambariki kwa ajili ya kufanya hivyo. Alipojua hangaiko la Nehemia, mfalme wa Uajemi alimwandalia jeshi la kivita na barua zilizomwidhinisha ajenge upya Yerusalemu.—Nehemia 1:1–2:9.

      4. Twaweza kuonyeshaje kwamba ibada ya Yehova ni ya maana zaidi kuliko kitu kingine chochote ambacho tungeweza kufurahia?

      4 Bila shaka, Ezra, Nehemia, na Wayahudi wengi walioshirikiana nao walithibitisha kwamba, ibada ya Yehova iliyokuwa na kitovu chake Yerusalemu, ilikuwa ya maana zaidi kuliko kitu kingine chochote—kwamba ilikuwa ‘zaidi ya furaha yao iliyo kuu,’ yaani ilikuwa ya maana zaidi kuliko kitu kingine chochote ambacho kingeweza kuwafurahisha. Watu kama hao ni kitia-moyo kilichoje leo kwa wote wale ambao wana maoni yaliyo sawa na hayo kuelekea Yehova, ibada yake, na tengenezo lake lenye kuongozwa kwa roho! Je, iko hivyo kwako? Je, wewe huonyesha kwa kuvumilia katika matendo ya kimungu kwamba sababu iliyo kuu zaidi ya furaha yako ni pendeleo la kumwabudu Yehova pamoja na watu wake walio wakfu? (2 Petro 3:11) Ili tutiwe moyo zaidi kuhusiana na hilo, acheni tufikirie matokeo mazuri ya safari ya Ezra kwenda Yerusalemu.

      Baraka na Madaraka

      5. Wakazi wa Yuda walipata baraka zipi nyingi siku za Ezra?

      5 Kikundi cha wahamishwa wapatao 6,000 waliorudi na Ezra kilileta michango ya dhahabu na fedha kwa ajili ya hekalu la Yehova. Michango hiyo ilikuwa yenye thamani iliyo sawa na dola milioni 35 za kisasa. Dhahabu na fedha hiyo ilipita kwa mara zipatazo saba ile ambayo wahamishwa wa kwanza waliweza kuleta. Ni lazima wakazi wa Yerusalemu na Yuda wawe walimshukuru Yehova kama nini kwa kupokea utegemezo huo wa kibinadamu na wa vitu vya kimwili! Lakini kubarikiwa sana na Mungu huleta daraka pia.—Luka 12:48.

      6. Ezra aligundua nini katika nchi yake ya nyumbani, naye alitendaje?

      6 Punde si punde Ezra aligundua kwamba Wayahudi wengi, kutia ndani makuhani na wazee fulani, walikuwa wamekiuka Sheria ya Mungu kwa kuoa wanawake wapagani. (Kumbukumbu la Torati 7:3, 4) Kwa haki, alisononeshwa sana na ukiukaji huo wa agano la Sheria ya Mungu. “Nami niliposikia hayo, nikararua nguo yangu na joho yangu, . . . nikaketi kwa mshangao.” (Ezra 9:3) Kisha, Waisraeli wenye kuhangaika wakiwapo, Ezra akatoa sala yenye hisia kwa Yehova. Huku wote wakisikiliza, Ezra alipitia kutotii kwa Israeli wakati uliopita na onyo la Mungu juu ya kile ambacho kingetukia kama wangeoa wakazi wapagani wa nchi. Alimalizia hivi: “Ee BWANA, Mungu wa Israeli, wewe ndiwe mwenye haki, maana sisi tumesalia, mabaki yaliyookoka, kama hivi leo; tazama sisi tupo hapa wenye hatia mbele zako; maana hapana mtu awezaye kusimama mbele zako kwa sababu ya jambo hili.”—Ezra 9:14, 15.

      7. (a) Ezra alitoa kielelezo gani kizuri cha kushughulikia ukosaji? (b) Wenye hatia walitendaje siku ya Ezra?

      7 Ezra alitumia usemi “sisi.” Ndiyo, alijitia ndani ingawa yeye binafsi hakuwa na hatia. Msononeko mwingi wa Ezra pamoja na sala yake ya unyenyekevu uligusa mioyo ya watu na kuwachochea wafanye kazi zilizofaa toba. Walijitolea kurekebisha mambo katika njia yenye kuwaumiza—wote waliokiuka Sheria ya Mungu wangerudisha wake zao wageni katika nchi zao za nyumbani, pamoja na watoto waliowazaa. Ezra alikubaliana na hatua hiyo na kuwatia moyo waliokuwa na hatia wafanye hivyo. Akiwa na mamlaka aliyokabidhiwa na mfalme wa Uajemi, Ezra alikuwa na haki ya kuwaua wavunja-sheria wote au kuwafukuza Yerusalemu na Yuda. (Ezra 7:12, 26) Lakini yaonekana kwamba hakulazimika kuchukua hatua hiyo. “Mkutano wote” ulisema: “Kama ulivyosema katika habari yetu, ndivyo vitupasavyo kutenda.” Zaidi ya hayo, waliungama hivi: “Tumekosa sana katika jambo hili.” (Ezra 10:11-13) Sura ya 10 ya kitabu cha Ezra huorodhesha majina 111 ya wanaume waliotii uamuzi huo kwa kuwafukuza wake zao wageni na watoto waliowazaa.

      8. Kwa nini hatua kali ya kuwafukuza wake wageni ilikuwa kwa masilahi ya wanadamu wote?

      8 Kitendo hicho kilikuwa kwa masilahi ya Waisraeli na pia wanadamu wote. Kama hawangalifanya lolote kusahihisha mambo, Waisraeli wangaliweza kuwa sehemu ya mataifa yaliyowazunguka. Kwa hiyo, nasaba ya Mbegu Aliyeahidiwa ili kubariki wanadamu wote ingalichafuliwa. (Mwanzo 3:15; 22:18) Ingalikuwa vigumu kuthibitisha kwamba Mbegu Aliyeahidiwa alikuwa uzao wa Mfalme Daudi wa kabila la Yuda. Miaka 12 baadaye, jambo hilo muhimu lilizingatiwa tena ‘wazao wa Israeli walipojitenga na wageni wote.’—Nehemia 9:1, 2; 10:29, 30.

      9. Biblia hutoa shauri gani zuri kwa Wakristo waliooa watu wasioamini?

      9 Watumishi wa Yehova wa siku hizi wanaweza kujifunza nini kutokana na simulizi hilo? Wakristo hawako chini ya agano la Sheria. (2 Wakorintho 3:14) Badala yake, wao hutii “sheria ya Kristo.” (Wagalatia 6:2) Hivyo, Mkristo aliyefunga ndoa na mtu asiyeamini hukubaliana na shauri hili la Paulo: “Ikiwa ndugu yeyote ana mke asiyeamini, na bado ni mwenye kukubali kukaa pamoja naye, asimwache.” (1 Wakorintho 7:12) Zaidi ya hayo, Wakristo waliofunga ndoa na watu wasioamini wana wajibu wa Kimaandiko wa kujitahidi kufanikisha ndoa yao. (1 Petro 3:1, 2) Mara nyingi, kutii shauri hilo zuri kumetokeza baraka kwamba, wenzi wa ndoa wasioamini wamebadili maoni yao kuelekea ibada ya kweli. Wengine hata wamekuwa Wakristo waaminifu waliobatizwa.—1 Wakorintho 7:16.

      10. Wakristo waweza kujifunza nini kutokana na wanaume Waisraeli 111 waliofukuza wake zao?

      10 Hata hivyo, kisa cha Waisraeli waliofukuza wake zao wageni hutoa somo bora kabisa kwa Wakristo waseja. Hawapaswi kuanza kuchumbia watu wa jinsia tofauti wasioamini. Huenda ikawa vigumu kuepuka uhusiano kama huo, hata kuwa jambo lenye kuumiza, lakini huo ndio mwenendo ulio bora zaidi ili mtu aendelee kupata baraka za Mungu. Wakristo wanaamuriwa hivi: “Msiwe wenye kufungwa nira isiyosawazika pamoja na wasio waamini.” (2 Wakorintho 6:14) Yampasa Mkristo yeyote mseja anayetaka kufunga ndoa apange kufanya hivyo na mwamini mwenzi aliye wa kweli.—1 Wakorintho 7:39.

      11. Kama wanaume Waisraeli, twaweza kujaribiwaje kuhusiana na tunachofanya kuwa furaha yetu iliyo kuu?

      11 Katika njia nyingine tofauti pia, Wakristo wamejirekebisha wanapojulishwa kwamba wanafuata mwenendo usio wa Kimaandiko. (Wagalatia 6:1) Mara kwa mara, jarida hili limetambulisha mwenendo usio wa Kimaandiko ambao haungemstahilisha mtu kuendelea kuwa sehemu ya tengenezo la Mungu. Kwa kielelezo, katika 1973, watu wa Yehova walikuja kuelewa kikamili kwamba matumizi mabaya ya madawa ya kulevya na tumbaku ni dhambi nzito. Ili kufuata mwenendo wa kimungu, ni lazima “tujisafishe wenyewe kila unajisi wa mwili na wa roho.” (2 Wakorintho 7:1) Watu wengi waliguswa moyo na shauri hilo la Biblia; walikuwa tayari kupatwa na athari za kwanza za kuacha matumizi hayo ili waendelee kuwa sehemu ya watu safi wa Mungu. Mwelekezo wa Kimaandiko ulio wazi pia umetolewa kuhusu mambo ya kingono, mavazi, kujipamba, na kuchagua kwa hekima kazi ya kuajiriwa, tafrija, na muziki. Hata iwe tutajulishwa kanuni zipi za Kimaandiko, na tuthibitike kuwa tayari “kurekebishwa upya,” kama wale wanaume Waisraeli 111. (2 Wakorintho 13:11) Hilo litaonyesha kwamba pendeleo la kumwabudu Yehova kwa kushirikiana na watu wake watakatifu ‘hukuzwa zaidi ya furaha yetu iliyo kuu.’

      12. Ni nini kilichotukia mwaka wa 455 K.W.K.?

      12 Baada ya kuripoti kisa kilichohusisha wake wageni, Biblia haituambii kilichotukia Yerusalemu kwa miaka 12 iliyofuata. Bila shaka majirani wa Israeli walikuja kuwa wenye uhasama zaidi kwa sababu ya kubatilishwa kwa mapatano mengi ya ndoa. Katika 455 K.W.K., Nehemia aliwasili Yerusalemu akisindikizwa na jeshi. Alikuwa amewekwa rasmi kuwa gavana wa Yuda naye alikuwa ameleta barua kutoka kwa mfalme wa Uajemi zilizomwidhinisha ajenge upya jiji.—Nehemia 2:9, 10; 5:14.

      Upinzani Kutoka kwa Majirani Wenye Wivu

      13. Ni mtazamo gani ulioonyeshwa na majirani wa Wayahudi, ambao walifuata dini zisizo za kweli, naye Nehemia alitendaje?

      13 Majirani waliofuata dini zisizo za kweli walipinga kusudi la kuja kwa Nehemia. Viongozi wao walimtisha kwa kuuliza: “Je! mtaasi ninyi juu ya mfalme?” Akionyesha imani katika Yehova, Nehemia alijibu: “Mungu wa mbinguni, yeye atatufanikisha; kwa hiyo sisi, watumishi wake, tutaondoka na kujenga; lakini ninyi hamna sehemu, wala haki, wala kumbukumbu, katika Yerusalemu.” (Nehemia 2:19, 20) Marekebisho ya ukuta yalipoanza, adui haohao walidhihaki hivi: ‘Wayahudi hawa wanyonge wanafanya nini? Je, watayafua mawe katika chungu hizi za kifusi? Angepanda mbweha, angeubomoa ukuta wao wa mawe.’ Badala ya kujibu dhihaka hizo, Nehemia alisali hivi: “Sikia, Ee Mungu wetu; maana tunadharauliwa; ukawarudishie mashutumu yao juu ya vichwa vyao.” (Nehemia 4:2-4) Kwa kuendelea, Nehemia aliweka kielelezo hicho chema cha kumtegemea Yehova!—Nehemia 6:14; 13:14.

      14, 15. (a) Nehemia alishughulikiaje tisho la jeuri la adui? (b) Mashahidi wa Yehova wameweza kuendeleaje na kazi yao ya ujenzi wa kiroho licha ya upinzani mkali?

      14 Ili kutimiza mgawo wao muhimu wa kuhubiri, leo Mashahidi wa Yehova pia humtegemea Mungu. Wapinzani hujaribu kuzuia kazi hiyo kwa kuwadhihaki. Nyakati fulani, watu wenye kupendezwa na ujumbe wa Ufalme hukata tamaa kwa sababu hawawezi kuvumilia dhihaka hizo. Dhihaka zikishindwa, huenda wapinzani wakakasirika na kutumia vitisho vya jeuri. Wajenzi wa kuta za Yerusalemu walipatwa na jambo kama hilo. Lakini Nehemia alikataa kuogopeshwa. Badala yake, aliwapa wajenzi hao silaha za kujilinda dhidi ya shambulio la adui na kutia imani yao nguvu kwa kusema: “Msiwaogope; mkumbukeni Bwana, aliye mkuu mwenye kuogofya, mkawapiganie ndugu zenu, na wana wenu, na binti zenu, na wake zenu, na nyumba zenu.”—Nehemia 4:13, 14.

      15 Kama ilivyokuwa katika siku za Nehemia, Mashahidi wa Yehova wameandaliwa vifaa ili waendelee na kazi yao ya ujenzi wa kiroho licha ya upinzani mkali. “Mtumwa mwaminifu na mwenye busara” amewaandalia chakula cha kiroho chenye kutia imani nguvu, ambacho huwawezesha watu wa Mungu kuwa na matokeo hata mahali ambapo kazi imepigwa marufuku. (Mathayo 24:45) Tokeo limekuwa kwamba, Yehova ameendelea kuwabariki watu wake kwa ongezeko kotekote duniani.—Isaya 60:22.

      Matatizo ya Ndani

      16. Ni matatizo gani ya ndani yaliyotisha roho ya wajenzi wa ukuta wa Yerusalemu?

      16 Kadiri kujenga upya ukuta wa Yerusalemu kulivyosonga mbele na ukuta kurefuka zaidi, ndivyo kazi ilivyozidi kuwa ngumu. Huo ndio wakati ambapo tatizo fulani lilidhihirika ambalo lilitisha roho ya wajenzi hao wenye juhudi. Kwa sababu ya upungufu wa chakula, Wayahudi wengine waliliona kuwa jambo gumu kulisha familia zao na kulipa kodi kwa serikali ya Uajemi. Wayahudi matajiri zaidi waliwakopesha chakula na fedha. Hata hivyo, kinyume cha Sheria ya Mungu, Waisraeli maskini zaidi walilazimika kuweka mashamba yao na watoto wao kuwa rehani kwamba wangelipa fedha hizo kwa riba. (Kutoka 22:25; Mambo ya Walawi 25:35-37; Nehemia 4:6, 10; 5:1-5) Wenye kudai walikuwa wakitisha kutwaa mashamba yao na kuwalazimisha wauze watoto wao kuwa watumwa. Nehemia alikasirishwa sana na mtazamo huo usio na upendo wa kufuatia vitu vya kimwili. Alichukua hatua upesi ili kuhakikisha kwamba Yehova angeendelea kubariki kazi ya kujenga upya ukuta wa Yerusalemu.

      17. Nehemia alifanya nini kuhakikisha kwamba Yehova angeendelea kubariki kazi ya ujenzi, na kukiwa na matokeo gani?

      17 “Mkutano mkubwa” ulipangwa, naye Nehemia akawaonyesha waziwazi Waisraeli matajiri zaidi kwamba waliyokuwa wamefanya yalimchukiza Yehova. Kisha akawaomba wenye hatia, kutia ndani makuhani kadhaa, warudishe riba yote waliyokuwa wamechukua na kurudisha mashamba waliyokuwa wametwaa isivyo halali kutoka kwa wale ambao hawangeweza kulipa riba. Ni jambo la kustahili pongezi kwamba, wenye hatia walisema hivi: “Tutawarudishia na hatutawadai chochote. Tutafanya kama ulivyosema.” Hayo hayakuwa maneno matupu, kwa maana Biblia yasema kwamba ‘watu walifanya kama walivyokuwa wameahidi Nehemia.’ Nao mkutano wote ukamsifu Yehova.—Nehemia 5:7-13, Biblia Habari Njema.

      18. Mashahidi wa Yehova wamekuja kujulikana kwa mtazamo gani?

      18 Vipi siku yetu? Badala ya kuwa wanyonyaji, Mashahidi wa Yehova wanajulikana sana kwa mtazamo wao wa ukarimu kuelekea waamini wenzao na wengineo ambao wamekumbwa na janga. Kama ilivyokuwa katika siku ya Nehemia, mtazamo huo umetokeza maelezo mengi ya shukrani yenye kumletea Yehova sifa. Hata hivyo, wakati huohuo, “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” amelazimika kutoa shauri la Kimaandiko juu ya mambo ya kibiashara na uhitaji wa kuepuka pupa ya unyonyaji kuelekea wengine. Katika nchi fulani ni jambo la kawaida kudai kiasi kikubwa mno cha mahari, lakini Biblia yaonya waziwazi kwamba watu wenye pupa na wanyang’anyi hawataurithi Ufalme wa Mungu. (1 Wakorintho 6:9, 10) Kuitikia vizuri kwa Wakristo wengi kuhusiana na shauri hilo, hutukumbusha jinsi Wayahudi hao walivyoiona dhambi ya kunyonya ndugu zao maskini zaidi.

      Ukuta wa Yerusalemu Wakamilishwa

      19, 20. (a) Ukamilishaji wa ukuta wa Yerusalemu ulikuwa na matokeo gani kwa wapinzani wa kidini? (b) Mashahidi wa Yehova wamepata ushindi gani katika nchi nyingi?

      19 Licha ya upinzani wote huo, ukuta wa Yerusalemu ulikamilishwa kwa siku 52. Jambo hilo likawa na matokeo gani kwa wapinzani? Nehemia alisema: “Adui zetu wote waliposikia, ndipo makafiri wote waliotuzunguka wakaogopa, nao wakakata tamaa sana machoni pao wenyewe; maana waliitambua kazi hiyo ilivyotendwa na Mungu wetu.”—Nehemia 6:16.

      20 Leo, upinzani wa adui dhidi ya kazi ya Mungu unaendelea katika njia mbalimbali na katika mahali mbalimbali. Hata hivyo, mamilioni ya watu wameona ubatili wa kupinga Mashahidi wa Yehova. Kwa mfano, fikiria majaribio ya wakati uliopita ya kukomesha kazi ya kuhubiri katika Ujerumani ya Nazi, Ulaya Mashariki, na nchi nyingi za Afrika. Majaribio hayo yameshindwa, na watu wengi sasa hukubali kwamba ‘kazi yetu inatendwa na Mungu.’ Jambo hilo limewathawabisha kama nini waaminifu wa zamani ambao ‘walikuza ibada ya Yehova zaidi ya furaha yao iliyo kuu’ katika nchi!

  • Yerusalemu Lililo Kama Vile Jina Lake Limaanishavyo
    Mnara wa Mlinzi—1998 | Oktoba 15
    • 3. Yapita miaka mingapi kabla ya kujulishwa tena shughuli za Ezra, naye twamkuta katika hali zipi?

      3 Biblia haisemi alikokuwa Ezra kipindi cha miaka 12 iliyokuwa katikati ya ziara yake Yerusalemu na kuwasili kwa Nehemia katika jiji hilo. Hali mbaya ya kiroho ya hilo taifa wakati huo, yadokeza kwamba Ezra hakuwepo. Hata hivyo twampata Ezra akitumikia akiwa kuhani wa Yerusalemu baada tu ya ukuta wa jiji kujengwa upya.

      Siku ya Kusanyiko ya Ajabu Sana

      4. Ni nini kilichokuwa cha maana kuhusu siku ya kwanza ya mwezi wa saba wa Israeli?

      4 Ukuta wa Yerusalemu ulikamilishwa wakati uliofaa kabisa kwa ajili ya mwezi muhimu wa msherehekeo Tishri, uliokuwa wa saba katika kalenda ya kidini ya Israeli. Siku ya kwanza ya Tishri ilikuwa ya msherehekeo wa pekee wa mwezi mpya uitwao Msherehekeo wa Kupiga Tarumbeta. Siku hiyo, makuhani walipiga tarumbeta huku dhabihu zikitolewa kwa Yehova. (Hesabu 10:10; 29:1) Siku hiyo iliwatayarisha Waisraeli kwa ajili ya Siku ya Kufunika ya kila mwaka iliyokuwa tarehe 10 mwezi wa Tishri, na vilevile Msherehekeo wa Kukusanya wenye furaha ulioanza tarehe 15 hadi 21 mwezi huohuo.

      5. (a) Ezra na Nehemia walitumiaje vizuri “siku ya kwanza ya mwezi wa saba”? (b) Kwa nini Waisraeli walilia?

      5 “Siku ya kwanza ya mwezi wa saba,” “watu wote” walikusanyika, yaelekea wakitiwa moyo wafanye hivyo na Nehemia na Ezra. Wanaume kwa wanawake, na “wote walioweza kusikia na kufahamu” walitiwa ndani. Hivyo, watoto wadogo walikuwepo na walisikiliza kwa makini wakati Ezra aliposimama juu ya jukwaa na kusoma Sheria “tangu mapambazuko hata adhuhuri.” (Nehemia 8:1-4) Walawi walikuwa wakiwasaidia watu waelewe kilichokuwa kikisomwa baada ya kipindi fulani. Jambo lililowafanya Waisraeli walie walipong’amua jinsi wao na mababa wao wa zamani walivyoshindwa kuitii Sheria ya Mungu.—Nehemia 8:5-9.

      6, 7. Wakristo wanaweza kujifunza nini kutokana na yale aliyofanya Nehemia ili kuzuia Wayahudi wasilie?

      6 Lakini huo haukuwa wakati wa kuomboleza. Ulikuwa msherehekeo, nao watu walikuwa wametoka kumaliza kazi ya kujenga upya ukuta wa Yerusalemu. Kwa hiyo, Nehemia aliwasaidia kuwa na mwelekeo ufaao kwa kusema: “Enendeni zenu, mle kilichonona, na kunywa kilicho kitamu, tena mpelekeeni sehemu yeye asiyewekewa kitu; maana siku hii ni takatifu kwa BWANA wetu; wala msihuzunike; kwa kuwa furaha ya BWANA ni nguvu zenu.” Kwa kutii, “watu wote wakaenda zao kula na kunywa, na kuwapelekea watu sehemu, na kufanya furaha nyingi, kwa sababu walikuwa wameyafahamu maneno yale waliyohubiriwa.”—Nehemia 8:10-12.

      7 Watu wa Mungu leo wanaweza kujifunza mengi kutokana na simulizi hilo. Wanaopendelewa kuwa na migao katika mikutano na makusanyiko wapaswa kukumbuka yaliyotajwa hapo juu. Kwa kuongezea kutoa shauri lenye kusahihisha ambalo nyakati nyingine huhitajika, pindi hizo hukazia manufaa na baraka ambazo hutokana na kutimiza matakwa ya Mungu. Pongezi hutolewa kwa ajili ya kazi njema zilizofanywa na kitia-moyo hutolewa ili kuvumilia. Watu wa Mungu wapaswa kuondoka kwenye mikusanyiko hiyo wakiwa na furaha moyoni kwa sababu ya mafundisho yenye kujenga ambayo wamepokea kutoka katika Neno la Mungu.—Waebrania 10:24, 25.

      Mkusanyiko Mwingine Wenye Furaha

      8, 9. Ni mkusanyiko gani wa pekee ambao ulifanyika siku ya pili ya mwezi wa saba, ukiwa na matokeo gani kwa watu wa Mungu?

      8 Siku ya pili ya mwezi huo wa pekee, “wakuu wa mbari za mababa za watu wote, na makuhani, na Walawi, wakamkusanyikia Ezra, mwandishi, ili wapate kuyasikiliza maneno ya torati.” (Nehemia 8:13) Ezra alistahili sana kuongoza mkusanyiko huo, kwa kuwa “alikuwa ameuelekeza moyo wake kuitafuta sheria ya BWANA, na kuitenda, na kufundisha maagizo na hukumu katika Israeli.” (Ezra 7:10) Bila shaka, mkusanyiko huo ulikazia sehemu ambazo watu wa Mungu walihitaji kujipatanisha zaidi na agano la Sheria. Uhitaji wa kufanya matayarisho yafaayo ya kusherehekea Msherehekeo wa Vibanda uliokuwa ukikaribia ni jambo lililohitaji kushughulikiwa kwa haraka.

      9 Msherehekeo huo wa juma zima ulifanywa kwa njia ifaayo, watu wote wakikaa katika vibanda vya muda vilivyojengwa kwa matawi na majani ya miti mbalimbali. Watu walijenga vibanda hivyo juu ya paa zao bapa, katika nyua zao, katika nyua za hekalu, na katika nyanja za umma za Yerusalemu. (Nehemia 8:15, 16) Ilikuwa fursa nzuri kama nini kukusanya watu na kuwasomea kutoka katika Sheria ya Mungu! (Linganisha Kumbukumbu la Torati 31:10-13.) Walisomewa kila siku, “tangu siku ya kwanza hadi siku ya mwisho” ya msherehekeo huo, jambo ambalo lilitokeza “furaha kubwa sana” kwa upande wa watu wa Mungu.—Nehemia 8:17, 18.

      Hatupaswi Kuachilia Nyumba ya Mungu

      10. Kwa nini mkusanyiko wa pekee ulipangwa siku ya 24 ya mwezi wa saba?

      10 Kuna wakati na mahali pafaapo kusahihisha makosa mazito miongoni mwa watu wa Mungu. Yaonekana kwa kung’amua kwamba huo ndio uliokuwa wakati wa kufanya hivyo, Ezra na Nehemia walipanga tarehe 24 ya mwezi wa Tishri iwe siku ya kufunga. Sheria ya Mungu ilisomwa tena, nao watu wakaungama dhambi zao. Kisha Walawi wakapitia shughuli za Mungu za rehema pamoja na watu wake waliopotoka, wakatumia maneno mazuri ya kumsifu Yehova, na kufanya “agano la hakika” lililotiwa muhuri na wakuu, Walawi na makuhani.—Nehemia 9:1-38.

      11. Ni kuhusiana na ‘agano jipi la hakika’ ambalo Wayahudi walijiweka chini ya wajibu?

      11 Kwa ujumla watu walikula kiapo cha kutimiza ‘agano hilo la hakika.’ Wao ‘wangeiendea torati ya Mungu wa kweli.’ Nao walikubali kutofanya mapatano ya ndoa pamoja na “watu wa nchi.” (Nehemia 10:28-30) Zaidi ya hayo, Wayahudi walijiweka chini ya wajibu wa kushika Sabato, kutoa mchango wa kifedha kila mwaka ili kutegemeza ibada ya kweli, kutoa kuni kwa ajili ya madhabahu ya dhabihu, kutoa wazaliwa wa kwanza wa makundi ya wanyama wao kwa ajili ya dhabihu, na kupeleka mazao ya kwanza ya nchi penye majumba ya kulia ya hekalu. Ni wazi kwamba waliazimia ‘kutoiacha nyumba ya Mungu wao.’—Nehemia 10:32-39.

      12. Kutoachilia nyumba ya Mungu kwahusisha nini leo?

      12 Leo, ni lazima watu wa Yehova wawe waangalifu wasiache pendeleo lao la ‘kutoa utumishi mtakatifu’ katika nyua za hekalu kubwa la kiroho la Yehova. (Ufunuo 7:15) Hilo lahusisha sala za kawaida zenye kuhisiwa moyoni kwa ajili ya kuendeleza ibada ya Yehova. Kuishi kulingana na sala hizo huhitaji kujitayarisha kwa ajili ya mikutano ya Kikristo na kuishiriki, kushiriki katika mipango ya kuhubiri habari njema, na kuwasaidia wenye kupendezwa kwa kurudi, na ikiwezekana, kujifunza Biblia pamoja nao. Wengi wasiotaka kuachilia nyumba ya Mungu hutoa michango ya kifedha kusaidia kazi ya kuhubiri na utunzaji wa mahali pa ibada ya kweli. Sisi pia tunaweza kuunga mkono ujenzi wa mahali pa kukutania penye kuhitajiwa kwa uharaka na vilevile kupaweka pakiwa safi na nadhifu. Njia muhimu ya kuonyesha upendo kwa nyumba ya kiroho ya Mungu ni kuendeleza amani miongoni mwa waamini wenzetu na kuwasaidia wowote wanaohitaji msaada wa kimwili au wa kiroho.—Mathayo 24:14; 28:19, 20; Waebrania 13:15, 16.

      Mzinduo Wenye Furaha

      13. Ni jambo gani lenye uharaka lililohitaji kushughulikiwa kabla ya ukuta wa Yerusalemu kuzinduliwa, na walio wengi waliweka kielelezo gani chema?

      13 “Agano la hakika” lililotiwa muhuri siku ya Nehemia liliwatayarisha watu wa kale wa Mungu kwa ajili ya siku ya mzinduo wa ukuta wa Yerusalemu. Lakini jambo jingine lenye uharaka lilihitaji kushughulikiwa. Likiwa limezungukwa na ukuta mkubwa wenye malango 12, Yerusalemu lilihitaji idadi kubwa zaidi ya watu. Ingawa Waisraeli fulani waliishi humo, “mji ulikuwa na nafasi nyingi, tena mkubwa; lakini watu waliomo walikuwa haba.” (Nehemia 7:4) Ili kutatua tatizo hilo, watu ‘walipiga kura, ili katika watu kumi kumleta mmoja akae ndani ya Yerusalemu mji mtakatifu.’ Itikio lenye utayari kwa mpango huo lilisukuma watu ‘wajitoe kwa hiari ili wakae Yerusalemu.’ (Nehemia 11:1, 2) Ni kielelezo kizuri kama nini kwa waabudu wa kweli leo ambao hali zao zinawaruhusu kuhamia mahali ambapo pana uhitaji mkubwa wa msaada wa Wakristo wakomavu!

      14. Ni nini kilichotukia siku ya kuzinduliwa kwa ukuta wa Yerusalemu?

      14 Punde si punde matayarisho muhimu yalianza kwa ajili ya siku kubwa ya mzinduo wa ukuta wa Yerusalemu. Wanamuziki na waimbaji wakakusanywa kutoka katika majiji yaliyozunguka Yuda. Nao wakafanyizwa kuwa kwaya kubwa mbili za kutoa shukrani, kila moja ikifuatwa na mwandamano. (Nehemia 12:27-31, 36, 38) Kwaya na miandamano hiyo ilianza kwenye sehemu fulani ya ukuta, mbali kabisa na hekalu, labda kwenye Lango la Bondeni, na kutembea kuelekea pande tofauti hadi walipokutana kwenye nyumba ya Mungu. “Wakatoa dhabihu nyingi siku ile, wakafurahi; kwa kuwa Mungu amewafurahisha furaha kuu; na wanawake pia na watoto wakafurahi; hata ikasikiwa mbali sana furaha hiyo ya Yerusalemu.”—Nehemia 12:43.

      15. Kwa nini kuwekwa wakfu kwa ukuta wa Yerusalemu hakukuwa sababu ya furaha ya kudumu?

      15 Biblia haisemi msherehekeo huo ulifanyika tarehe gani. Bila shaka, huo ulikuwa jambo kuu, ikiwa haukuwa upeo wa kujengwa upya Yerusalemu. Bila shaka, kazi nyingi ya kujenga ilihitajika kufanywa ndani ya jiji hilo. Baada ya muda raia wa Yerusalemu walipoteza msimamo wao mzuri wa kiroho. Kwa kielelezo, Nehemia alipozuru jiji hilo kwa mara ya pili, alipata kwamba nyumba ya Mungu ilikuwa imeachwa tena na kwamba Waisraeli walikuwa wakioa tena wanawake wapagani. (Nehemia 13:6-11, 15, 23) Hali zilizo mbaya kama hizo zinathibitishwa katika maandishi ya nabii Malaki. (Malaki 1:6-8; 2:11; 3:8) Kwa hiyo, kuwekwa wakfu kwa ukuta wa Yerusalemu hakukuwa sababu ya furaha ya kudumu.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki