Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Shangilieni Pamoja na Mungu Mwenye Furaha
    Mnara wa Mlinzi—2001 | Mei 1
    • Shangilieni Pamoja na Mungu Mwenye Furaha

      “Mwishowe, akina ndugu, endeleeni kushangilia, . . . na Mungu wa upendo na amani atakuwa pamoja nanyi.”—2 WAKORINTHO 13:11.

      1, 2. (a) Kwa nini watu wengi hawana shangwe maishani? (b) Shangwe ni nini, nasi twaweza kuisitawishaje?

      KATIKA siku hizi zenye kuhuzunisha, watu wengi hawaoni jambo la kuwafurahisha. Watu hao au wapendwa wao wanapopatwa na msiba, huenda wakahisi kama Yobu wa kale, aliyesema hivi: “Mwanadamu aliyezaliwa na mwanamke siku zake za kuishi si nyingi, naye hujaa taabu.” (Ayubu 14:1) Wakristo hupatwa na mikazo ya “nyakati [hizi] za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,” na haishangazi kwamba nyakati nyingine watumishi waaminifu wa Yehova huvunjika moyo.—2 Timotheo 3:1.

      2 Hata hivyo, Wakristo wanaweza kuwa na shangwe, hata wanapopatwa na majaribu. (Matendo 5:40, 41) Ili kuelewa jinsi wanavyoweza kuwa na shangwe, fikiria kwanza maana ya neno shangwe. Shangwe imefafanuliwa kuwa ‘furaha ya kuwa na kitu kizuri au ya kutazamia kitu kizuri.’a Kwa sababu hiyo, tunapofikiria mambo mazuri tuliyo nayo sasa na vilevile kutafakari shangwe tutakayopata katika ulimwengu mpya wa Mungu, twaweza kuwa wenye shangwe.

      3. Ni katika maana gani inaweza kusemwa kwamba kila mtu ana sababu fulani za kushangilia?

      3 Kila mtu amebarikiwa kwa njia fulani ambayo yapasa kumfanya ashukuru. Huenda kichwa cha familia akapoteza kazi yake. Bila shaka, atakuwa na wasiwasi. Anataka kuwaruzuku wapendwa wake. Hata hivyo, ikiwa ana nguvu za kimwili na afya njema, ana sababu za kushukuru. Akipata kazi ataweza kuifanya kwa bidii. Kwa upande mwingine, huenda mwanamke Mkristo akapatwa na ugonjwa wenye kudhoofisha. Hata hivyo, anaweza kushukuru kwa ajili ya msaada kutoka kwa marafiki na washiriki wa familia wenye upendo ambao humsaidia kukabiliana na ugonjwa wake kwa utulivu na ujasiri. Hata hali zao ziweje, Wakristo wote wa kweli wanaweza kushangilia katika pendeleo la kumjua Yehova, “Mungu mwenye furaha,” na Yesu Kristo, ‘Mtawala pekee na mwenye furaha.’ (1 Timotheo 1:11; 6:15) Naam, Yehova Mungu na Yesu Kristo ni wenye furaha kwelikweli. Wamedumisha shangwe yao licha ya uhakika kwamba hali zilizopo duniani zatofautiana kabisa na jinsi Yehova alivyokusudia hapo mwanzoni. Kielelezo chao chaweza kutufundisha mengi kuhusu jinsi tunavyoweza kudumisha shangwe yetu.

      Hawajawahi Kupoteza Shangwe Yao

      4, 5. (a) Yehova alihisije wanadamu wa kwanza walipoasi? (b) Yehova alidumishaje mtazamo mzuri kuelekea wanadamu?

      4 Katika bustani ya Edeni, Adamu na Hawa walikuwa na afya nzuri na akili kamilifu. Waliishi katika mazingira mazuri na walikuwa na kazi yenye kuthawabisha. Zaidi ya yote, walikuwa na pendeleo la kuwasiliana na Yehova kwa ukawaida. Mungu alikusudia wawe na wakati ujao wenye furaha. Lakini wazazi wetu wa kwanza hawakuridhika na zawadi hizo nzuri; waliiba tunda lililokatazwa kutoka katika “mti wa ujuzi wa mema na mabaya.” Tendo hilo la kutotii lilisababisha hali ya huzuni ambayo sisi wazao wao hupatwa nayo leo.—Mwanzo 2:15-17; 3:6; Waroma 5:12.

      5 Hata hivyo, Yehova hakupoteza shangwe yake kwa sababu ya mtazamo wa Adamu na Hawa wa kukosa shukrani. Alikuwa na uhakika kwamba baadhi ya wazao wao wangechochewa na mioyo yao kumtumikia. Alikuwa na uhakika mwingi sana hivi kwamba hata kabla Adamu na Hawa hawajapata mtoto wao wa kwanza, alitangaza kusudi lake la kukomboa wazao wao watiifu! (Mwanzo 1:31; 3:15) Katika karne zilizofuata, wengi walitenda kama Adamu na Hawa, lakini Yehova hakuwakataa wanadamu kwa sababu ya kutotii huko kulikoenea sana. Badala yake, alielekeza fikira zake kwa wanaume na wanawake ‘walioufurahisha moyo wake,’ wale waliojitahidi kwelikweli kumpendeza kwa sababu walimpenda.—Mithali 27:11; Waebrania 6:10.

      6, 7. Ni mambo gani yaliyomsaidia Yesu kudumisha shangwe?

      6 Namna gani Yesu—yeye alidumishaje shangwe yake? Akiwa kiumbe wa roho mwenye nguvu huko mbinguni, Yesu alikuwa na fursa ya kutazama matendo ya wanaume na wanawake duniani. Hali yao ya kutokuwa wakamilifu ilikuwa wazi, hata hivyo Yesu aliwapenda. (Mithali 8:31) Baadaye, alipokuja duniani na “[ku]kaa miongoni” mwa wanadamu, hakubadili maoni yake kuelekea wanadamu. (Yohana 1:14) Ni nini kilichomwezesha Mwana mkamilifu wa Mungu adumishe mtazamo huo mzuri kuelekea wanadamu wenye dhambi?

      7 Kwanza kabisa, Yesu alikuwa na maoni ya kiasi kujihusu na kuhusu wengine. Alijua kwamba hangeweza kugeuza imani ya watu wote ulimwenguni. (Mathayo 10:32-39) Kwa hiyo alishangilia hata kama ni mtu mmoja tu mnyofu aliyekubali ujumbe wa Ufalme. Ingawa wakati fulani mwenendo na mtazamo wa wanafunzi wake haukupendeza, Yesu alijua kwamba walitaka kufanya mapenzi ya Mungu kutoka moyoni, na aliwapenda kwa sababu hiyo. (Luka 9:46; 22:24, 28-32, 60-62) Katika sala aliyomtolea Baba yake wa kimbingu, twaweza kuona kwamba Yesu alitaja jinsi wanafunzi wake walivyojiendesha ifaavyo kufikia wakati huo: “Nao wameshika neno lako.”—Yohana 17:6.

      8. Taja baadhi ya njia ambazo twaweza kumwiga Yehova na Yesu katika kudumisha shangwe yetu.

      8 Bila shaka, sote twaweza kunufaika kwa kuiga mfano uliowekwa na Yehova Mungu na Kristo Yesu kuhusu jinsi ya kudumisha shangwe. Je, twaweza kumwiga Yehova kwa ukamili zaidi labda kwa kutokuwa na wasiwasi kupita kiasi mambo yasipotukia kama tulivyotarajia? Je, twaweza kufuata kwa ukaribu zaidi hatua za Yesu kwa kudumisha mtazamo unaofaa kuelekea hali zetu za sasa, na vilevile kuwa wenye kiasi katika mambo tunayotarajia kutoka kwetu na kwa wengine? Acheni tuone jinsi baadhi ya kanuni hizi zinavyoweza kutumiwa ifaavyo katika huduma ya shambani ambayo inapendwa sana na Wakristo wenye bidii kila mahali.

      Dumisha Mtazamo Unaofaa Kuhusu Huduma

      9. Shangwe ya Yeremia ilichochewaje upya, na kielelezo chake chaweza kutusaidiaje?

      9 Yehova anataka tuwe wenye shangwe katika utumishi wake. Shangwe yetu haipasi kutegemea matokeo tunayopata. (Luka 10:17, 20) Nabii Yeremia alihubiri kwa miaka mingi katika eneo ambalo halikuwa na matokeo. Alipofikiria jinsi watu walivyoitikia vibaya, alipoteza shangwe yake. (Yeremia 20:8) Lakini alipofikiria uzuri wa ujumbe huo, shangwe yake ilichochewa upya. Yeremia alimwambia Yehova hivi: “Maneno yako yalionekana, nami nikayala; na maneno yako yalikuwa ni furaha kwangu, na shangwe ya moyo wangu; maana nimeitwa kwa jina lako, Ee BWANA, Mungu wa majeshi.” (Yeremia 15:16) Naam, Yeremia alifurahia pendeleo lake la kuhubiri neno la Mungu. Sisi pia twaweza kulifurahia.

      10. Tunaweza kudumishaje shangwe yetu katika huduma hata ikiwa eneo letu halina matokeo wakati wa sasa?

      10 Hata wengi wakikataa kukubali habari njema, tuna sababu kubwa sana ya kushangilia tunapokuwa katika huduma ya shambani. Kumbuka kwamba Yehova alikuwa na uhakika kabisa kwamba baadhi ya wanadamu wangechochewa kumtumikia. Kama vile Yehova, hatupaswi kukata tamaa kamwe kwamba huenda hatimaye watu fulani wakatambua suala la enzi kuu na kukubali ujumbe wa Ufalme. Hatupaswi kusahau kwamba hali za watu hubadilika. Mtu anapopatwa na msiba au tatizo fulani ambalo hakutarajia, hata kama alikuwa ameridhika na maisha kadiri gani, huenda akaanza kufikiria kwa uzito kusudi la maisha. Je, utakuwa tayari kusaidia wakati mtu kama huyo atakapoona ‘uhitaji wake wa kiroho’? (Mathayo 5:3) Kwani, huenda mtu fulani katika eneo lenu akakubali kusikiliza habari njema utakapomtembelea wakati ujao!

      11, 12. Ni nini kilichotukia katika mji fulani, nasi twaweza kujifunza nini kutokana na jambo hilo?

      11 Aina ya watu wanaoishi katika eneo letu wanaweza kubadili maoni yao pia. Fikiria kielelezo kimoja. Katika mji mmoja mdogo, paliishi kikundi cha wenzi wa ndoa wachanga waliokuwa na watoto na ambao walikuwa na uhusiano wa karibu. Mashahidi wa Yehova walipowatembelea, walipata jibu lilelile kwenye kila mlango, “Hatupendezwi!” Mtu fulani alipoonyesha upendezi wa kweli katika ujumbe wa Ufalme, majirani walimvunja moyo mara moja asiendelee kuwasiliana na Mashahidi. Bila shaka, ilikuwa vigumu sana kuhubiri eneo hilo. Hata hivyo, Mashahidi hawakukata tamaa; waliendelea kuhubiri. Matokeo yakawaje?

      12 Baada ya muda, watoto wengi katika mji huo walikua, wakafunga ndoa na kuendelea kuishi katika mji huo. Walipotambua kwamba njia yao ya maisha haikuwaletea furaha ya kweli, baadhi ya vijana hao walianza kutafuta kweli. Waliipata kweli walipokubali habari njema zinazotangazwa na Mashahidi. Kwa hiyo baada ya miaka mingi kutaniko dogo likaanza kukua. Hebu wazia jinsi wahubiri wa Ufalme walivyoshangilia kwa sababu hawakukata tamaa! Acheni tupate shangwe vilevile kwa kuhubiri kwa bidii ujumbe wa Ufalme wenye utukufu!

      Waamini Wenzako Watakutegemeza

      13. Tunaweza kuwaendea nani tunapovunjika moyo?

      13 Mikazo inapoongezeka au unapopatwa na msiba, unaweza kutafuta faraja wapi? Watumishi wengi waliojiweka wakfu kwa Yehova, humwendea kwanza katika sala, kisha huwaendea ndugu na dada zao Wakristo. Alipokuwa duniani, Yesu mwenyewe alithamini utegemezo wa wanafunzi wake. Usiku uliotangulia kifo chake, alisema kwamba wao ndio ‘walioshikamana naye katika majaribu yake.’ (Luka 22:28) Bila shaka, wanafunzi hao hawakuwa wakamilifu, lakini uaminifu-mshikamanifu wao ulimfariji Mwana wa Mungu. Sisi pia twaweza kupata faraja kutoka kwa waamini wenzetu.

      14, 15. Ni nini kilichowasaidia wenzi fulani wa ndoa kukabiliana na kifo cha mwana wao, nawe unajifunza nini kutokana na jambo lililowapata?

      14 Wenzi wa ndoa Wakristo, Michel na Diane, walijifunza jinsi utegemezo wa ndugu na dada zao uwezavyo kuwa wenye thamani. Mwana wao mwenye umri wa miaka 20 anayeitwa Jonathan, Mkristo mwenye nguvu na mataraja mema, alipimwa na kupatikana kuwa na uvimbe wa ubongo. Madaktari walijaribu juu chini kumwokoa, lakini hali ya Jonathan ilizorota hadi akafa alasiri moja. Michel na Diane walihuzunika kwelikweli. Walitambua kwamba Mkutano wa Utumishi, uliokuwa unafanywa siku hiyo, ulikuwa unakaribia kwisha. Hata hivyo, kwa kuwa walihitaji kufarijiwa sana, walimwomba mzee aliyekuwa pamoja nao aambatane nao hadi kwenye Jumba la Ufalme. Waliwasili tu wakati ambapo kutaniko lilikuwa likijulishwa habari za kifo cha Jonathan. Baada ya mkutano, wazazi hao waliokuwa wamejaa majonzi walizungukwa na ndugu na dada zao waliowakumbatia na kuwafariji. Diane akumbuka hivi: “Tulikuwa na huzuni nyingi sana tulipofika kwenye jumba, lakini tulipata faraja iliyoje kutoka kwa akina ndugu—walitutia moyo kama nini! Ingawa hawangeweza kutuondolea maumivu, walitusaidia kuvumilia chini ya mkazo!”—Waroma 1:11, 12; 1 Wakorintho 12:21-26.

      15 Msiba huo ulifanya Michel na Diane wawe na uhusiano wa karibu zaidi na ndugu zao. Pia uliwafanya wawe na uhusiano wa karibu zaidi wao kwa wao. Michel asema hivi: “Nimejifunza kumthamini zaidi mke wangu mpendwa. Tunapovunjika moyo, tunazungumza kuhusu kweli ya Biblia na jinsi Yehova anavyotutegemeza.” Diane aongezea hivi: “Tumaini la Ufalme lina maana kubwa hata zaidi kwetu leo.”

      16. Kwa nini ni muhimu kuchukua hatua ya kwanza kuwajulisha ndugu zetu mahitaji yetu?

      16 Naam, ndugu na dada zetu Wakristo wanaweza kuwa “msaada wenye ku[tu]tia nguvu” wakati wenye magumu maishani na hivyo kutusaidia tudumishe shangwe yetu. (Wakolosai 4:11) Bila shaka, hawawezi kujua mambo tunayofikiri. Kwa hiyo, tunapohitaji utegemezo, ni vizuri kuwajulisha mahitaji yetu. Ndipo tutakapoweza kuonyesha uthamini halisi kwa faraja tunayopata kutoka kwa ndugu zetu, na kuiona kuwa inatoka kwa Yehova.—Mithali 12:25; 17:17.

      Angalia Vielelezo Katika Kutaniko Lako

      17. Mama mmoja asiye na mwenzi hukabili magumu gani, nasi twawaonaje watu kama yeye?

      17 Kadiri uangaliavyo vielelezo vya waamini wenzako, ndivyo utakavyojifunza kuwathamini zaidi na kupata shangwe kwa kushirikiana nao. Angalia vielelezo katika kutaniko lako. Unaona nini? Je, kuna mzazi asiye na mwenzi ambaye anajitahidi kulea watoto wake katika njia ya kweli? Je, umewahi kufikiria kwa makini kielelezo kizuri anachoweka? Jaribu kuwazia baadhi ya matatizo anayokabili. Jeanine, ambaye ni mama asiye na mwenzi, ataja baadhi ya matatizo hayo: upweke, kutongozwa na wanaume kazini, kutokuwa na fedha za kutosha. Lakini asema jambo lililo gumu kuliko yote ni kushughulikia mahitaji ya kihisia-moyo ya watoto wake, kwa kuwa kila mtoto ni tofauti na mwingine. Jeanine ataja tatizo jingine: “Inaweza kuwa vigumu sana kukinza mwelekeo wa kutaka mwanao atende kama kichwa cha nyumba yako ili kujazia pengo la kutokuwa na mume. Nina binti, na nyakati nyingine ninasahau na kumlemea kwa kumweleza matatizo yangu ya ndani kabisa.” Sawa na maelfu ya wazazi wasio na wenzi na wanaomhofu Mungu, Jeanine anafanya kazi ya wakati wote na kutunza familia yake. Pia huwafundisha watoto wake Biblia, huwazoeza katika huduma, na kuwapeleka katika mikutano ya kutaniko. (Waefeso 6:4) Lazima Yehova awe anafurahi kama nini aonapo kila siku jitihada ya familia hii ya kudumisha uaminifu-maadili! Je, hatufurahi kuwa na watu kama hao miongoni mwetu? Bila shaka, tunafurahi.

      18, 19. Eleza jinsi tunavyoweza kuwaonyesha uthamini zaidi washiriki wa kutaniko.

      18 Angalia tena vielelezo katika kutaniko lako. Huenda ukaona wajane wanawake au wanaume ambao ‘hawakosi kamwe’ mikutanoni. (Luka 2:37) Je, wao huhisi upweke nyakati nyingine? Bila shaka. Wanatamani sana kuwa na wenzi wao! Lakini wanakuwa na mengi ya kufanya katika utumishi wa Yehova na wanapendezwa kibinafsi na wengine. Mtazamo wao wenye utulivu na unaofaa huongeza shangwe ya kutaniko! Mkristo mmoja ambaye ametumikia katika huduma ya wakati wote kwa miaka zaidi ya 30 alisema hivi: “Jambo moja linalonipa shangwe kubwa zaidi ni kuona ndugu na dada wenye umri mkubwa ambao wamepatwa na majaribu mengi na bado wanamtumikia Yehova kwa uaminifu!” Naam, Wakristo wenye umri mkubwa miongoni mwetu ni kitia-moyo kikubwa kwa wachanga.

      19 Namna gani wapya ambao wameanza tu kushirikiana na kutaniko hivi karibuni? Je, hatuchochewi kuona wakidhihirisha imani yao kwenye mikutano? Fikiria maendeleo ambayo wamefanya tangu waanze kujifunza Biblia. Lazima Yehova awe anapendezwa sana nao. Je, tunapendezwa nao? Je, tunaonyesha kwamba tunawaunga mkono kwa kuwapongeza kwa ajili ya jitihada zao?

      20. Kwa nini tunaweza kusema kwamba kila mshiriki wa kutaniko huchangia fungu muhimu kutanikoni?

      20 Je, umefunga ndoa, u mseja, au mzazi asiye na mwenzi? Je, wewe ni msichana au mvulana asiye na baba (au mama), mjane mwanamke au mwanamume? Je, umeshirikiana na kutaniko kwa miaka mingi au umeanza kushirikiana nalo hivi karibuni tu? Uwe na hakika kwamba kielelezo chako cha uaminifu hututia moyo sote. Na unaposhiriki kuimba wimbo wa Ufalme, unapotoa maelezo au hotuba katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, tunafurahi hata zaidi. Jambo la maana hata zaidi, ni kwamba unaufurahisha moyo wa Yehova.

      21. Tuna sababu nyingi za kufanya nini, lakini ni maswali gani yanayozuka?

      21 Naam, hata katika nyakati hizi zenye matatizo, tunaweza kuwa wenye furaha tunapomwabudu Mungu wetu mwenye furaha. Tuna sababu nyingi za kukubali kitia-moyo cha Paulo: “Endeleeni kushangilia, . . . na Mungu wa upendo na amani atakuwa pamoja nanyi.” (2 Wakorintho 13:11) Ingawa hivyo, vipi tukipatwa na msiba wa asili, mnyanyaso, au magumu ya kiuchumi? Je, tunaweza kudumisha shangwe yetu hata tunapokabiliana na hali kama hizo? Fikiria utakavyofanya uchunguzapo makala ifuatayo.

      [Maelezo ya Chini]

      a Ona kichapo Insight on the Scriptures, Buku la 2, ukurasa wa 119, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

  • Dumisha Shangwe Yako Katika Utumishi wa Yehova
    Mnara wa Mlinzi—2001 | Mei 1
    • Dumisha Shangwe Yako Katika Utumishi wa Yehova

      “Sikuzote shangilieni katika Bwana. Mara moja tena hakika nitasema, Shangilieni!”—WAFILIPI 4:4.

      1, 2. Ndugu mmoja na familia yake waliwezaje kudumisha shangwe yao licha ya kupoteza kila kitu?

      JAMES, Mkristo mwenye umri wa miaka 70 anayeishi Sierra Leone, alikuwa amefanya kazi kwa bidii katika maisha yake yote. Wazia shangwe aliyopata wakati ambapo hatimaye alikusanya pesa za kutosha kununua nyumba ya kiasi yenye vyumba vinne! Hata hivyo, muda mfupi baada ya James na familia yake kuhamia nyumba hiyo, vita vya wenyewe kwa wenyewe vilizuka nchini humo na nyumba yao ikateketezwa kabisa. Walipoteza nyumba yao, lakini hawakupoteza shangwe yao. Kwa nini?

      2 James na familia yake hawakufikiria hasara waliyopata, bali walifikiria mambo ambayo wangepata baadaye. James aeleza hivi: “Hata wakati wa vitisho, tulifanya mikutano, tukasoma Biblia, tukasali pamoja, na kushiriki na wengine vitu vichache tulivyokuwa navyo. Tuliweza kudumisha shangwe yetu kwa sababu tulitafakari juu ya uhusiano wetu mzuri pamoja na Yehova.” Kwa kufikiria mambo mazuri waliyofurahia, jambo kuu zaidi likiwa ni uhusiano wa kibinafsi pamoja na Yehova, Wakristo hao waaminifu waliweza ‘kuendelea kushangilia.’ (2 Wakorintho 13:11) Bila shaka, haikuwa rahisi kuvumilia hali zao zenye taabu. Lakini hawakuacha kushangilia katika Yehova.

      3. Wakristo fulani wa mapema walidumishaje shangwe yao?

      3 Wakristo wa mapema walikabili majaribu kama yale yaliyompata James na familia yake. Hata hivyo, mtume Paulo aliwaandikia Wakristo Waebrania maneno haya: “Kwa shangwe mkakubali kwa uvumilivu kuporwa mali zenu.” Kisha Paulo akaeleza kilichosababisha shangwe yao: “Mkijua nyinyi wenyewe mna miliki bora na yenye kudumu.” (Waebrania 10:34) Naam, Wakristo hao wa karne ya kwanza walikuwa na tumaini lenye nguvu. Walitazamia kwa hamu kupokea kitu wasichoweza kuporwa, kitu kisichoweza kunyauka, ambacho ni “taji la uhai” katika Ufalme wa kimbingu wa Mungu. (Ufunuo 2:10) Leo, tumaini letu la Kikristo—liwe ni la kimbingu au la kidunia—laweza kutusaidia kudumisha shangwe hata wakati wa taabu.

      “Shangilieni Katika Tumaini”

      4, 5. (a) Kwa nini shauri la Paulo “shangilieni katika tumaini” lilikuwa la wakati ufaao kwa Waroma? (b) Ni nini kinachoweza kumfanya Mkristo apoteze tumaini lake?

      4 Mtume Paulo aliwatia moyo waamini wenzake katika Roma ‘washangilie katika tumaini’ la uhai udumuo milele. (Waroma 12:12) Shauri hilo kwa Waroma lilitolewa kwa wakati ufaao. Muda unaopungua mwongo mmoja baada ya Paulo kuwaandikia, walinyanyaswa vikali, na wengine waliteswa hadi kufa kufuatia amri ya Maliki Nero. Bila shaka, walipokuwa wakiteseka walitegemezwa na imani yao kwamba Mungu angewapa taji la uhai alilowaahidi. Namna gani sisi leo?

      5 Tukiwa Wakristo, sisi pia twatarajia kunyanyaswa. (2 Timotheo 3:12) Zaidi ya hilo, twatambua kwamba “wakati na tukio lisilotazamiwa” hutupata sote. (Mhubiri 9:11, NW) Mtu tumpendaye anaweza kufa kwenye aksidenti. Mzazi au rafiki wa karibu aweza kufa kutokana na ugonjwa usiotibika. Tusipozingatia tumaini letu la Ufalme, hali yetu ya kiroho yaweza kuhatarishwa majaribu hayo yatupatapo. Basi yafaa tujiulize, ‘Je “[ninashangilia] katika tumaini”? Mimi hutafakari juu ya tumaini hilo mara nyingi kadiri gani? Je, Paradiso itakayokuja ni halisi kwangu? Je, ninawazia nikiwa katika Paradiso hiyo? Je, ningali na hamu ileile niliyokuwa nayo hapo mwanzo nilipojifunza kweli, kuona mfumo wa sasa wa mambo ukiisha?’ Twapaswa kufikiria sana swali hilo la mwisho. Kwa nini? Kwa sababu ikiwa tuna afya njema, tuna pesa za kutosha, na tunaishi katika nchi isiyo na vita, isiyo na upungufu wa chakula, au misiba ya asili huenda—angalau kwa sasa—tukakosa kutambua uhitaji wa kuja upesi kwa ulimwengu mpya wa Mungu.

      6. (a) Paulo na Sila walipopatwa na dhiki, walifikiria mambo gani? (b) Kielelezo cha Paulo na Sila chaweza kututiaje moyo leo?

      6 Paulo alizidi kuwashauri Waroma ‘wavumilie chini ya dhiki.’ (Waroma 12:12) Paulo alijua dhiki ni nini. Wakati fulani katika maono Paulo aliona mtu aliyemwalika ‘avuke na kuingia Makedonia’ ili kusaidia watu wa hapo wajifunze juu ya Yehova. (Matendo 16:9) Baada ya hapo, Paulo, pamoja na Luka, Sila, na Timotheo walisafiri hadi Ulaya. Mishonari hao wenye bidii wangepatwa na nini? Na dhiki! Baada ya kuhubiri katika jiji la Makedonia la Filipi, Paulo na Sila walipigwa viboko na kutiwa gerezani. Ni wazi kwamba baadhi ya raia wa Filipi hawakuwa na ubaridi tu kuelekea ujumbe wa Ufalme bali waliupinga sana. Je, mishonari hao wenye bidii walipoteza shangwe yao baada ya mambo kubadilika? La. Baada ya kupigwa na kutiwa gerezani, “karibu na katikati ya usiku Paulo na Sila walikuwa wakisali na kumsifu Mungu kwa wimbo.” (Matendo 16:25, 26) Bila shaka, Paulo na Sila hawakufurahia maumivu waliyopata kutokana na kupigwa, hata hivyo, mishonari hao wawili hawakuzingatia mambo hayo. Walifikiri juu ya Yehova na jinsi alivyokuwa akiwabariki. Kwa ‘kuvumilia kwa shangwe chini ya dhiki,’ Paulo na Sila waliweka kielelezo kizuri kwa ndugu zao katika Filipi na kwingineko.

      7. Kwa nini tushukuru pia tunaposali?

      7 Paulo aliandika hivi: “Dumuni katika sala.” (Waroma 12:12) Je, wewe husali unapokuwa na mahangaiko? Wewe husali kuhusu nini? Labda unataja tatizo lako hususa na kumwomba Yehova akusaidie. Lakini pia unaweza kushukuru kwa ajili ya baraka unazofurahia. Kutafakari wema ambao Yehova ametufanyia hutusaidia ‘kushangilia katika tumaini,’ matatizo yanapotokea. Daudi ambaye maisha yake yalijaa matatizo, aliandika hivi: “Ee BWANA, Mungu wangu, umefanya kwa wingi miujiza yako na mawazo yako kwetu; hakuna awezaye kufananishwa nawe; kama ningependa kuyatangaza na kuyahubiri, ni mengi sana hayahesabiki.” (Zaburi 40:5) Bila shaka, tutaendelea kuwa na shangwe ikiwa tutamwiga Daudi kwa kutafakari kwa ukawaida baraka ambazo tumepokea kutoka kwa Yehova.

      Dumisha Mtazamo Unaofaa

      8. Ni nini humsaidia Mkristo aendelee kuwa na furaha anaponyanyaswa?

      8 Yesu anawatia moyo wafuasi wake wadumishe mtazamo unaofaa wanapokabiliana na majaribu mbalimbali. Asema hivi: “Wenye furaha ni nyinyi watu wawashutumupo na kuwanyanyasa nyinyi na kusema kwa uwongo kila namna ya jambo ovu dhidi yenu kwa ajili yangu.” (Mathayo 5:11) Tuna sababu gani ya kufurahi chini ya hali hizo? Uwezo wetu wa kuvumilia upinzani huthibitisha kwamba tuna roho ya Yehova. Mtume Petro aliwaambia hivi Wakristo wenzake katika siku zake: “Ikiwa mnashutumiwa kwa ajili ya jina la Kristo, nyinyi ni wenye furaha, kwa sababu roho ya utukufu, naam, roho ya Mungu, inatulia juu yenu.” (1 Petro 4:13, 14) Kupitia roho yake, Yehova atatusaidia pia kuvumilia na hivyo kudumisha shangwe yetu.

      9. Ni nini kilichowasaidia ndugu fulani wapate shangwe walipokuwa gerezani kwa sababu ya imani yao?

      9 Hata tunapokuwa chini ya hali mbaya sana, twaweza kuwa na sababu za kushangilia. Mkristo aitwaye Adolf alitambua ukweli wa jambo hilo. Anaishi katika nchi ambayo kazi ya Mashahidi wa Yehova ilipigwa marufuku kwa miaka mingi. Adolf na wenzake kadhaa walikamatwa na kufungwa kwa muda mrefu kwa sababu hawakukana imani yao inayotegemea Biblia. Maisha ya gerezani yalikuwa magumu, lakini kama Paulo na Sila, Adolf na wenzake walikuwa na sababu za kumshukuru Mungu. Walisema kwamba mambo waliyokabili gerezani yaliwasaidia kuimarisha imani yao na kusitawisha sifa za Kikristo zinazofaa, kama vile ukarimu, huruma, na shauku ya kidugu. Kwa mfano, mfungwa alipopokea kifurushi kutoka nyumbani, aliwagawia waamini wenzake vitu vilivyokuwamo ndani, nao wakaona vitu hivyo vya ziada kuwa vinatoka kwa Yehova, Mpaji mkuu wa “kila zawadi njema na kila upaji mkamilifu.” Mpaji na wapokeaji walipata shangwe kwa sababu ya matendo hayo ya fadhili. Kwa hiyo ingawa walitiwa gerezani ili kuvunja imani yao, mambo yaliyowapata yalifanya wawe na nguvu zaidi za kiroho.—Yakobo 1:17; Matendo 20:35.

      10, 11. Dada mmoja alitendaje alipohojiwa mfululizo na kufungwa kwa muda mrefu?

      10 Ella, anayeishi pia katika nchi ambayo kazi ya Ufalme ilipigwa marufuku kwa muda mrefu, alikamatwa kwa sababu ya kuwajulisha wengine tumaini lake la Kikristo. Alihojiwa mfululizo kwa muda wa miezi minane. Hatimaye alipopelekwa mahakamani, alihukumiwa kifungo cha miaka kumi katika gereza ambalo halikuwa na mwabudu mwingine wa Yehova. Wakati huo, Ella alikuwa na umri wa miaka 24 tu.

      11 Bila shaka, si kwamba Ella alifurahia kutumia muda mwingi wa ujana wake gerezani. Lakini kwa kuwa hangeweza kubadili hali yake, aliamua kubadili maoni yake. Kwa hiyo alianza kuona gereza hilo kuwa eneo lake la kibinafsi la kutoa ushahidi. “Nilihubiri sana hivi kwamba miaka ilipita upesi sana,” asema. Baada ya miaka zaidi ya mitano, Ella alihojiwa tena. Watu waliokuwa wakimhoji walipotambua kwamba imani yake haikuvunjwa licha ya kufungwa gerezani, walimwambia hivi: “Hatuwezi kukuachilia; hujabadilika.” Ella alijibu hivi kwa uthabiti, “lakini nimebadilika! Sasa nina mtazamo mzuri kuliko wakati nilipotiwa gerezani, na imani yangu ni yenye nguvu kuliko hapo awali!” Kisha akaongezea: “Msipotaka kuniachilia, nitaendelea kukaa hapa hadi Yehova aonapo inafaa kunikomboa.” Ella hakupoteza shangwe yake kwa sababu ya kufungwa gerezani kwa muda wa miaka mitano na nusu! Alijifunza kuridhika na hali zozote zilizompata. Je, unaweza kujifunza jambo fulani kutokana na kielelezo chake?—Waebrania 13:5.

      12. Mkristo anayekabili magumu aweza kupataje amani ya akili?

      12 Usifikiri kwamba Ella ana kipawa fulani kisicho cha kawaida ambacho humwezesha kukabiliana na magumu hayo. Akirejezea kipindi alichohojiwa miezi kadhaa kabla ya kuhukumiwa, Ella akiri hivi: “Nakumbuka meno yangu yakigongana-gongana, na nilihisi kama ndege mdogo aliyeshtuliwa.” Hata hivyo, Ella ana imani yenye nguvu katika Yehova. Amejifunza kumtumaini. (Mithali 3:5-7) Kwa sababu hiyo amemwona Mungu kuwa halisi kwake kuliko hapo awali. Aeleza hivi: “Kila mara nilipoingia katika chumba cha kuhojiwa, nilihisi nikiwa na amani. . . . Kadiri hali ilivyozidi kuwa yenye kutisha, ndivyo nilivyohisi amani nyingi zaidi.” Yehova ndiye aliyekuwa chanzo cha amani hiyo. Mtume Paulo aeleza hivi: “Msihangaikie kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na utoaji-shukrani acheni maombi yenu ya bidii yajulishwe kwa Mungu; na amani ya Mungu izidiyo fikira yote kwa ubora italinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.”—Wafilipi 4:6, 7.

      13. Tuna uhakikisho gani kwamba iwapo tutakabiliana na dhiki, tutakuwa na nguvu za kuvumilia?

      13 Ella, ambaye tayari ameachiliwa, alidumisha shangwe yake licha ya magumu. Alivumilia kwa kutegemea nguvu alizopewa na Yehova wala si kwa kutegemea nguvu zake mwenyewe. Mtume Paulo, ambaye hakutegemea nguvu zake mwenyewe, aliandika hivi: “Kwa hiyo, kwa mteremo zaidi sana afadhali nijisifu kwa habari ya udhaifu wangu, ili nguvu ya Kristo ipate kubaki juu yangu. . . . Kwa maana niwapo dhaifu, ndipo niwapo mwenye nguvu.”—2 Wakorintho 12:9, 10.

      14. Eleza jinsi Mkristo anavyoweza kuwa na maoni yafaayo kuhusu hali fulani yenye kujaribu na matokeo yake yaweza kuwa nini.

      14 Huenda mikazo unayokabili leo ikatofautiana kidogo na ile ambayo tumetaja. Hata hivyo, hata mikazo hiyo iwe ya namna gani, si rahisi kukabiliana nayo. Kwa mfano, huenda mwajiri wako akachambua sana kazi yako kuliko anavyochambua kazi ya wafanyakazi wa dini nyingine. Huenda usiweze kupata kazi nyingine. Unaweza kudumishaje shangwe yako? Kumbuka Adolf na marafiki wake waliositawisha sifa muhimu kwa sababu ya mambo yaliyowapata gerezani. Ukijitahidi kwa unyofu kumpendeza mwajiri wako—hata yule ambaye ni “mgumu kupendeza”—utasitawisha sifa za Kikristo kama vile uvumilivu na ustahimilivu. (1 Petro 2:18) Isitoshe, huenda ukawa mfanyakazi anayefaa zaidi, jambo ambalo laweza kukusaidia kupata kazi yenye kuridhisha zaidi wakati fulani. Acheni sasa tuchunguze njia nyingine zinazoweza kutusaidia kudumisha shangwe yetu katika utumishi wa Yehova.

      Kufanya Maisha Yawe Sahili Huleta Shangwe

      15-17. Wenzi fulani wa ndoa walijifunza nini ambacho kingeweza kupunguza mkazo, hata ingawa kisababishi cha mkazo huo hakingeweza kukomeshwa kabisa?

      15 Huenda usiweze kubadili kazi unayofanya au mahali pako pa kazi, lakini huenda ikawa unaweza kubadili mambo fulani maishani. Fikiria jambo lililoonwa lifuatalo.

      16 Wenzi wa ndoa Wakristo walikaribisha mzee fulani nyumbani kwao kwa chakula. Jioni hiyo, ndugu na mke wake walimwambia mzee huyo kwamba hivi karibuni wamekuwa wakilemewa na mikazo ya maisha. Ingawa wote wawili walikuwa na kazi ya wakati wote iliyowataka watumie muda mwingi na jitihada nyingi, hawangeweza kutafuta kazi nyingine. Hawakujua wangeendelea kukabiliana na hali hiyo mpaka lini.

      17 Alipoulizwa shauri, mzee huyo alijibu, “Fanyeni Maisha Yenu Yawe Sahili.” Jinsi gani? Mume na mke huyo walikuwa wakitumia muda wa saa tatu kila siku kwenda na kurudi kutoka kazini. Mzee huyo ambaye aliwajua vizuri wenzi hao wa ndoa aliwadokezea wahame na kuishi karibu na mahali pao pa kazi ili wapunguze muda wanaotumia kwenda kazini kila siku. Wangeweza kutumia muda huo wa ziada kushughulikia mambo mengine muhimu au kupumzika tu. Ikiwa unapoteza shangwe yako kwa kiasi fulani kwa sababu ya mikazo ya maisha, kwa nini usifikirie kama unaweza kupata kitulizo kwa kufanya marekebisho fulani?

      18. Kwa nini ni muhimu kufikiri kwa makini kabla ya kufanya maamuzi?

      18 Njia nyingine ya kupunguza mkazo ni kufikiria kwa makini kabla ya kufanya maamuzi. Kwa mfano, Mkristo mmoja aliamua kujenga nyumba. Alichagua plani ya jengo lenye vyumba vingi hata ingawa hakuwa amewahi kujenga nyumba hapo awali. Sasa anatambua kwamba angeweza kuepuka matatizo yasiyo ya lazima ikiwa ‘angeangalia sana aendavyo’ kabla ya kuchagua plani ya nyumba yake. (Mithali 14:15) Mkristo mwingine alikubali kuwa mdhamini wa mwamini mwenzake aliyepewa mkopo. Kupatana na makubaliano ya mkopo huo, ikiwa mwenye kukopeshwa angeshindwa kulipa, mdhamini angekuwa na jukumu la kuulipa. Mwanzoni, hakukuwa na matatizo yoyote, lakini baada ya muda mwenye kukopeshwa akashindwa kutimiza ahadi yake. Mkopeshaji alianza kuwa na wasiwasi na kudai mdhamini alipe mkopo wote. Mdhamini alipatwa na mkazo mkubwa sana. Je, angeweza kuepuka mikazo hiyo iwapo angefikiria kwa makini mambo yote yanayohusika kabla ya kukubali jukumu la kulipa mkopo huo?—Mithali 17:18.

      19. Ni baadhi ya njia gani zinazoweza kutusaidia kupunguza mikazo maishani?

      19 Tunapochoka, acheni tusifikiri kamwe kwamba tunaweza kupunguza mkazo na kupata tena shangwe yetu kwa kupunguza muda wa kufanya funzo la Biblia la kibinafsi, utumishi wa shambani, na kuhudhuria mikutano. Hayo ni mambo muhimu kwa kuwa kupitia hayo twaweza kupokea roho takatifu ya Yehova, ambayo hutokeza shangwe. (Wagalatia 5:22) Utendaji wa Kikristo huburudisha wakati wote na hauchoshi mtu kupindukia. (Mathayo 11:28-30) Huenda tunachoshwa na mambo ya kimwili au tafrija, bali si mambo ya kiroho. Kuzoea kulala mapema kwaweza kutusaidia tusichoke kupindukia. Kupumzika kwa muda mrefu zaidi kwaweza kunufaisha sana. N. H. Knorr, aliyetumikia akiwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova hadi alipokufa, alizoea kuwaambia mishonari hivi: “Unapovunjika moyo, jambo la kwanza unalopaswa kufanya ni kupumzika. Utaona jambo ambalo hukuwa umetarajia, yaani itakuwa rahisi kutatua karibu kila tatizo baada ya kulala vizuri!”

      20. (a) Taja kifupi baadhi ya njia zinazoweza kutusaidia tudumishe shangwe yetu. (b) Ni sababu gani zinazoweza kukufanya uwe mwenye shangwe? (Ona sanduku kwenye ukurasa wa 17.)

      20 Wakristo wana pendeleo la kutumikia “Mungu mwenye furaha.” (1 Timotheo 1:11) Kama vile tumeona, tunaweza kudumisha shangwe yetu hata tunapokabiliana na matatizo makubwa. Acheni tuendelee kufikiri juu ya tumaini la Ufalme, turekebishe mtazamo wetu inapokuwa lazima, na tufanye maisha yetu yawe sahili. Kisha, hata tujikute katika hali gani, tutatii maneno haya ya mtume Paulo: “Sikuzote shangilieni katika Bwana. Mara moja tena hakika nitasema, Shangilieni!”—Wafilipi 4:4.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki