-
Wagibeoni Wenye HekimaKitabu Changu cha Hadithi za Biblia
-
-
HADITHI YA 48
Wagibeoni Wenye Akili
SASA miji mingi katika Kanaani inajitayarisha kupigana na Israeli. Wanadhani wanaweza kushinda. Lakini watu wa mji jirani wa Gibeoni hawadhani hivyo. Wanaamini Mungu anawasaidia Waisraeli, nao hawataki kupigana na Mungu. Basi unajua Wagibeoni hao wanafanya nini?
Wanajifanya kama wanakaa mbali sana. Basi wengine kati yao wanavaa nguo zilizopasuka-pasuka na viatu vilivyokwisha. Wanapakia punda zao mifuko ya zamani, na kuchukua mikate iliyokauka. Kisha wanamwendea Yoshua wakimwambia: ‘Tumetoka mbali sana, kwa kuwa tulisikia habari za Mungu wenu mkuu, Yehova. Tulisikia yote aliyowafanyia huko Misri. Basi viongozi wetu walituambia tutayarishe chakula cha safari tuje tukuambie: “Sisi ni watumishi wako. Utupe ahadi ya kwamba hutapigana na sisi.” Tazama nguo zetu zimekwisha kwa sababu ya safari ndefu na mkate nao umekauka.’
Yoshua na viongozi wengine wanawaamini Wagibeoni hao. Basi wanaahidi wasipigane nao. Lakini baada ya siku tatu wanajua kwamba kumbe Wagibeoni hao wanakaa karibu sana.
‘Mbona mlituambia mmetoka mbali sana?’ Yoshua anawauliza.
Wagibeoni wanajibu hivi: ‘Tulisema hivyo kwa sababu tuliambiwa kwamba Mungu wenu Yehova alikuwa ameahidi kuwapa ninyi nchi yote hii ya Kanaani. Tuliogopa kwamba labda mtatuua.’ Lakini Waisraeli wanafuata ahadi yao, wasiwaue Wagibeoni. Wanawafanya kuwa watumishi wao.
Mfalme wa Yerusalemu anakasirika kwa sababu Wagibeoni wamefanya amani na Israeli. Basi anawaambia wafalme wengine wanne hivi: ‘Njoni mnisaidie kupiga Gibeoni.’ Wafalme hao watano wanafanya hivyo. Je! Wagibeoni walionyesha akili kwa kufanya amani na Israeli? Tutaona.
-
-
Jua Linasimama TuKitabu Changu cha Hadithi za Biblia
-
-
HADITHI YA 49
Jua Linasimama Tu
MTAZAME Yoshua. Anasema: ‘Jua, simama!’ Jua linasimama. Linakaa siku nzima katikati ya anga. Yehova anafanya hivyo! Lakini ebu tuone kwa nini Yoshua anataka jua liendelee kung’aa.
Wale wafalme wabaya watano katika nchi ya Kanaani wanapoanza kupigana na Wagibeoni, hao Wagibeoni wanamtuma mtu aende kumwomba Yoshua msaada. ‘Njoo kwetu upesi!’ asema. ‘Utuokoe! Wafalme wote wa vilimani wamekuja kupigana na watumishi wako.’
Mara hiyo Yoshua na wanajeshi wake wote wanakwenda. Wanasafiri usiku kucha. Wanapofika Gideoni, wale askari wa wafalme watano wanaogopa na kuanza kukimbia. Ndipo Yehova anaangusha mawe makubwa ya mvua kutoka angani. Askari wengi wanakufa kwa mvua ya mawe kuliko wanaouawa na wanajeshi wa Yoshua.
Yoshua anaona kwamba karibu jua litatua. Kutakuwa usiku, na askari wengi wa wafalme watano wabaya watakimbia. Ndiyo sababu Yoshua anamwomba Yehova na kusema: ‘Jua, simama!’ Jua linapoendelea kung’aa, Waisraeli wanashinda vita.
Kuna wafalme wabaya wengi zaidi katika Kanaani wanaochukia watu wa Mungu. Inamchukua Yoshua na jeshi lake karibu miaka sita kushinda wafalme 31 katika nchi hiyo. Kisha, Yoshua anahakikisha kwamba nchi ya Kanaani imegawanywa ili makabila yanayohitaji eneo, yapewe.
Kunapita miaka mingi, mwishowe Yoshua anakufa akiwa mwenye miaka 110. Wakati yeye na rafiki zake bado hai, watu wanamtii Yehova. Lakini watu hao wema wanapokufa, watu wanaanza kutenda mabaya na kutaabika. Huu ndio wakati wanapohitaji msaada wa Mungu.
-